Jina kuu la Mwokozi wetu Yesu Kristo libarikiwe, karibu tujifunze biblia, Neno la Mungu ambalo ndio mwanga wa njia yetu na Taa iongozayo miguu yetu. (Zab.119:135).
Kitabu cha Filemoni ni waraka ulioandikwa na Mtume Paulo wakati akiwa gerezani, Kwa mtu mmoja anayejulikana kama Filemoni. (Ikumbukwe kuwa waraka ni kama barua tu), hivyo Mtume Paulo aliandika waraka huo/barua hiyo kwa Filemoni, na waraka huo kwa uongozo wa Roho, ukawekwa kwenye orodha ya vitabu vya biblia kwasababu una maonyo makubwa na mafunzo makubwa kwa wakristo. Na pia ni mojawapo ya vitabu vifupi katika agano jipya.
Sasa huyu Filemoni alikuwa ni nani?
Filemoni alikuwa ni mmoja wa watu waliompokea Yesu, kupitia injili iliyokuwa inahubiriwa na wakina Paulo katika mji wa Efeso, hivyo huyu Filemoni alikutana na injili hiyo na kumpokea Yesu, na kuanza kumtumikia kwa moyo wake wote, mpaka kufikia hatua ya kuwa askofu wa kanisa, ambalo lilikuwa linakusanyika nyumbani kwake mwenyewe (Filemon 1:2), huko Kolosai.Lakini pamoja na hayo, mtu huyu alikuwa ana uwezo na alikuwa anamiliki watumwa nyumbani kwake (yaani wafanyakazi).
Na mmoja wa watumwa wake aliyekuwa anaitwa Onesimo, siku moja alitoroka kwake na kumwibia baadhi ya mali zake, na kukimbia nazo Rumi. Wakati akiwa njiani kuelekea Rumi, alikutana na Paulo akihubiri injili, na Maneno ya Mungu yakamgusa na kumfanya kutubu kwa dhati kabisa. Na alipotubu ndipo baadaye Paulo akajua alikuwa ni mtumwa wa Filemoni yule wa Efeso, mtenda kazi kazi katika shamba la Mungu. Na kwasababu Paulo amemhakiki Onesimo kuwa ni kweli katubu kwa dhati, na kageuka kuwa mkristo, na kaacha wizi na mambo yote mabaya, na zaidi ya yote alikuwa anataka kufuatana na Paulo katika injili kila anakokwenda na hata katika vifungo vyake.
Lakini Paulo hakuruhusu afuatane naye badala yake kwa kuongozwa na hekima ya Roho akaamua amsafirishe amrudishe kwanza kwa Bwana wake, lakini asimrudishe mikono mitupu bali ampeleke na waraka kutoka kwake, wa ushuhuda wake kwa Onesimo, kwamba kijana wake si yule aliyemwacha, bali amebadilika na kuwa mtu mwingine, (kawa kiumbe kipya), na katika waraka huo pia kulikuwa na mambo machache ya kumshauri Filemoni juu ya Onesimo mtumwa wake….
Kwasababu kwa wakati huo, kulingana na sheria za kirumi, endapo mtumwa akimtoroka bwana wake, na akipatikana, sheria kwake ilikuwa ni kifo. Kwahiyo Paulo alilijua hilo na ndio maana akaazimu kumrudisha Onesimo kwa bwana wake pamoja na waraka.
Na katika waraka huo aligusia vipengele vikuu 3 vifuatavyo.
1. Kwanza aliomba ampokee kwasababu kashatubu na kubadilika..
Filemoni 1:9 “lakini, kwa ajili ya upendo nakusihi, kwa kuwa ni kama nilivyo, Paulo mzee, na sasa mfungwa wa Kristo Yesu pia.
10 Nakusihi kwa ajili ya mtoto wangu niliyemzaa katika vifungo vyangu, yaani, Onesimo;
11 ambaye zamani alikuwa hakufai, bali sasa akufaa sana, wewe na mimi pia;
12 niliyemtuma kwako, yeye mwenyewe, maana ni moyo wangu hasa”
2. Baada ya kumpokea asimfanye tena kama mtumwa, bali kama ndugu katika Kristo.
Filemoni 1:16 “ tokea sasa, si kama mtumwa, bali zaidi ya mtumwa, ndugu mpendwa; kwangu mimi sana, na kwako wewe zaidi sana, katika mwili na katika Bwana.”
3 Na pia kama alimdhulumu, basi Paulo atamrudishia na kulipa pale alipodhulumiwa,
Filemoni 1:17 “Basi kama ukiniona mimi kuwa mshirika nawe, mpokee huyu kama mimi mwenyewe.
18 Na kama amekudhulumu, au unamwia kitu, ukiandike hicho juu yangu.
19 Mimi Paulo nimeandika kwa mkono wangu mwenyewe, mimi nitalipa. Sikuambii kwamba nakuwia hata nafsi yako”
Filemoni 1:20 “Naam, ndugu yangu, nipate faida kwako katika Bwana; uniburudishe moyo wangu katika Kristo.
21 Kwa kuwa nakuamini kutii kwako ndiyo maana nimekuandikia, nikijua ya kuwa utafanya zaidi ya hayo nisemayo”.
Katika waraka huu, biblia inatufundisha jinsi ya kuishi na watumwa wetu, ambao kwasasa tunaweza kusema watu tuliowaajiri. Na pia inatufundisha majukumu ya kila mtumishi wa Mungu (kwamba anapaswa awe mpatanishi).
Unaweza kuwa umeokoka na kumwamini Yesu, na nyumbani unaye mfanya kazi wa ndani, au mlinzi wa geti, au unafanya kazi katika ofisi na chini wako kuna watumishi umewaajiri,…kumbuka huyo mtumishi wako, au mfanyakazi wako anapookoka na kuwa na Imani kama yako, fahamu kuwa huyo kwako ni kama ndugu, hupaswi kumfanya kama mtumwa wako tena…Ndio anaweza kuendelea na kazi yake ya nyumbani, au ya kulinda lakini, mchukulie kama ni ndugu yako..maana yake, kazi anayoifanya iendane sana na mshahara wake, kiasi kwamba ajihisi kama vile analipwa bure, ukilinganisha na kazi anayoifanya…
Pia utu wake uendane sawa na kazi anayoifanya…Maana yake anapofanya kazi yako ajihisi kama na yeye ni sehemu ya ile kazi, kwa kupendwa, kusikilizwa, kupewa muda wa kupumzika, na si ajihisi ni kama mnyama, au mtumwa Fulani anayetumikishwa ili mwisho wa siku tu alipwe mshahara, na pia wewe kama bwana wake unapaswa uwe mvumilivu na mtu wa kusamehe kama Filemoni.
Wakolosai 4:1 “Ninyi akina bwana, wapeni watumwa wenu yaliyo haki na ya adili, mkijua ya kuwa ninyi nanyi mna Bwana mbinguni”.
Na pia kama wewe ni mtumwa huna budi kuwa mnyenyekevu, na kuwa na busara na hekima. Kwasababu biblia inasema pia..
Wakolosai 3:22 “Ninyi watumwa, watiini hao ambao kwa mwili ni bwana zenu, katika mambo yote, si kwa utumwa wa macho, kama wajipendekezao kwa wanadamu, bali kwa unyofu wa moyo, mkimcha Bwana.”
Maana yake ni kwamba, ijapokuwa boss wako ni ndugu yako katika Kristo, hupaswi kumkosea heshima, wala kumdharau. Ukimvunjia heshima, au ukimdharau na kumfanya boss wako ahuzunike tayari umemkosea Mungu.
Pia katika kitabu hichi tunajifunza, majukumu yetu kama watumishi wa Mungu, kwamba tuwe wapatanishi, hapo tunamwona Mtume Paulo, baada ya kumbadilisha Onesimo kwa injili yake, hakumchukua na kuanza ziara za kutembea naye, ingawa Onesimo alikuwa tayari na alitamani sana awe anatembea na Paulo, lakini Paulo aliona si vyema kutembea naye katika utumishi, na ilihali bado ni mtumwa wa mtu mwingine, hivyo ni vizuri kwanza akarudi kwa bwana wake, na kupatana naye, na kama bwana wake kama atampa ruhusa basi ndipo arudi na kuzunguka na wakina Paulo katika kuhubiri. Lakini si hekima kumchukua na ilihali katoroka kwa bwana wake, isingeleta picha nzuri, Filemoni asikie kwamba yule mtu aliyemuibia na kutoroka yupo huko anatembea na Paulo katika kuhubiri.
Vivyo hivyo hata katika wakati huu, wapo watu wamewaibia maboss zao, na wametubu kwa dhati kabisa, lakini hawataki kwenda kupatana na waliowaibia…wanataka watubu tu kimoyo moyo, na zaidi ya yote wanapokelewa makanisani na hata katika huduma na kupewa nafasi ya kuhudumu. Pasipo kujua kuwa huko nje wameacha sifa gani.
Wapo wengine wamekutwa katika udunia, na wameisikia injili na kuamua kutubu, lakini hapo kabla walikuwa wameshawakimbia wake zao, au waume zao, au familia zao…sasa kabla ya kuwapokea watu kama hao katika utumishi, ni vizuri kwanza wakapatane na ndugu zao, na wake zao au waume zao…Huku sisi tuliowahubiria tukiwasaidia, kama Paulo alivyomsaidia Onesimo kurudi kwa bwana wake kwa waraka, ili watakapoingia katika utumishi wasilete picha mbaya kwa walio nje.
Hivyo kama mchungaji, au mtumishi yeyote wa Mungu, tunapaswa tuchunguze kwanza historia ya mtu, kabla ya kuanza naye kazi ya huduma, hata kama ametubu kwa dhati, hiyo pekee haitoshi, anapaswa atengeneze machache ya nyuma, ambayo ameyaharibu, ili isipatikane dosari yoyote katika injili atakayoihubiri, au watakaoihubiri wale waliomhubiria.
Bwana atubariki.
Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema,
Kwa maombezi/Ratiba za ibada/ Ushauri/ Maswali.
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312
pia kama utapenda uyapate mafundisho haya kwa njia ya Whatsapp au email basi tutumie ujumbe kwenye namba hizo hizo.
Mada Nyinginezo:
JINSI MTUME PAULO ALIVYOUTHAMINI WITO WAKE, JUU YA WENYE VYEO.
SWALI: BWANA apewe sifa mtumishi wa Mungu! Nakusalimia katika jina la YESU KIRSTO. naomba unifafanulie Mhubili 5:1 Mtumishi maana huwa sipaelewi vizuri.. Inasema.
Mhubiri 5:1 “Jitunze mguu wako uendapo nyumbani kwa Mungu; Maana ni heri kukaribia ili usikie, Kuliko kutoa kafara ya wapumbavu; Ambao hawajui kuwa wafanya mabaya”.
JIBU: Amen, jina kuu la Bwana wetu Yesu Kristo litukuzwe daima.
Katika vifungu hivyo, biblia inatutahadharisha jinsi ambavyo tunapaswa tuwe pale tunapotaka kwenda nyumbani mwa Mungu (Kanisani) kumfanyia ibada/ huduma. Anasema ni heri ukaribie usikie, kuliko kutoa kafara za wapumbavu. Maana yake ni kuwa si kila jambo tunaweza kulifanya katika kanisa ilimradi tu, kama tunavyoweza kufanya mahali pengine popote. Kumbuka huduma yoyote, au dua yoyote, unayoifanya au unayoipelekea kwa Mungu hiyo ni kafara.
Leo hii utaona, binti au kijana ni mzinzi, halafu bado akifika kanisani, anakuwa wa kwanza kwenda pale mbele kumwimbia Mungu kwaya, hizo ni kafara za wapumbavu. Au mtu hajaitwa na Mungu, haliishi hata Neno la Mungu lakini ni wa kwanza kwenda kufundisha kanisani kisa tu anajiona anakipaji fulani cha kuongea.Sasa hizo ni kafara za wapumbavu ambazo biblia inasema, kuwa wafanyao hayo hawajui kuwa wanatenda mabaya.. Wanafanya mambo ambayo yatawasababishia madhara wao wenyewe.
Vilevile, kuwa na maneno mengi mbele za Bwana, ambayo hayana maana, hizo nazo ni kafara za wapumbavu, kwamfano utamwona mwingine, akifika tu magotini, ni kumnung’unikia Mungu, na kulalamika mbele zake mwanzo mwisho, kama vile wana wa Israeli walivyokuwa wanafanya kule jangwani ambao mwisho wao tunajua ulikuwa ni kuangamizwa tu badala ya kuponywa.. Hizo nazo ni kafara za wapumbavu na ndio maana mistari inayofuata inasema..
Mhubiri 5:1 “Jitunze mguu wako uendapo nyumbani kwa Mungu; Maana ni heri kukaribia ili usikie, Kuliko kutoa kafara ya wapumbavu; Ambao hawajui kuwa wafanya mabaya.
2 Usiseme maneno ya ujinga kwa kinywa chako, wala moyo wako usiwe na haraka kunena mbele za Mungu; kwa maana, Mungu yuko mbinguni, na wewe upo chini, Kwa hiyo maneno yako na yawe machache”.
Unaona? Maneno yako yawe machache..Ni heri utumie muda mwingi kushukuru, na kuomba kuliko kutoa manung’uniko, au kulaani.
Pia, kafara za wapumbavu ni pamoja na kumwekea Mungu nadhiri, bila kutafakari kwanza, kwamfano utakuta mwingine anaahidi, atamfanyia Mungu kitu fulani kwenye kanisa, halafu hatimizi alichokiahidi, angali zipo katika uwezo wa mikono yao, kama walivyofanya Anania na Safira, ambao mwisho wa siku walikufa , Ukiendelea kusoma mstari wa 4 pale unasema..
Mhubiri 5:4 “Wewe ukimwekea Mungu nadhiri, usikawie kuiondoa; kwa kuwa yeye hawi radhi na wapumbavu; basi, uiondoe hiyo uliyoiweka nadhiri.
5 Ni afadhali usiweke nadhiri, Kuliko kuiweka usiiondoe”.
Pia kutoa sadaka, ambayo imetoka katika shughuli haramu, kama za ukahaba au madawa ya kulevya, usizipeleke nyumbani kwa Bwana..
Kumbukumbu 23: 18 “Usilete ujira wa kahaba, wala mshahara wa mbwa, katika nyumba ya Bwana, Mungu wako, kwa ajili ya nadhiri yo yote; kwani haya ni machukizo kwa Bwana, Mungu wako, yote mawili”.
Unaona?.. Hivyo kwa kuhitimisha ni kuwa kama bado hujafahamu ni nini ambacho Mungu anakihitaji kwanza kwako, pale unapofika nyumbani mwake, ni heri usifanye chochote kabisa, ukae usikilize tu, ufundishwe mapenzi ya Mungu kwanza, na ndipo baadaye uanze kumfanyia Mungu huduma kanisani. Kuliko kukurupuka kufanyia Mungu chochote kabla hajafahamu mapenzi yake ni nini kwako.
Tunapaswa tujue Mungu, anahitaji kwanza UTAKATIFU wa maisha yetu, ndipo hayo mengine tutakapoyatoa yawe na Baraka zaidi, hatumdanganyishii Mungu kwa kutumika kwetu wakati maisha yetu yapo mbali na wokovu. Alisema mwenyewe..
1Samweli 15:22 “…Angalia, kutii ni bora kuliko dhabihu, Na kusikia kuliko mafuta ya beberu”.
Hivyo tujitahidi tujue kwanza mapenzi ya Mungu nini.
Shalom.
Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema,
Kwa maombezi/Ratiba za ibada/ Ushauri/ Maswali.
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312
pia kama utapenda uyapate mafundisho haya kwa njia ya Whatsapp au email basi tutumie ujumbe kwenye namba hizo hizo.
Mada Nyinginezo:
Ni kwanini Yesu alisema “Na wakisikia wasikie, wasielewe Wasije wakaongoka?”
SWALI: Katika Marko 4:12, Bwana Yesu anasema.. “ ili wakitazama watazame, wasione; Na wakisikia wasikie, wasielewe; Wasije wakaongoka, na kusamehewa”. Swali ni kwamba, kwanini Yesu alisema hivyo kuwa acha wasisikie na kuelewa ili wasije wakaongoka na kusamehewa…na wakati kusudi lake si anataka watu watubu ili wapate kusamehewa dhambi?.
Jibu: Ukianza kusoma kuanzia juu kidogo utaona, Bwana Yesu alikuwa ameutoa ule mfano wa mpanzi mbele ya mkutano mkubwa, na baada ya kuutoa, hakutoa tafsiri yake, kwamba zile mbegu zilimaanisha nini, na lile konde maana yake nini.. Badala yake aliacha tu kama fumbo… Sasa kundi kubwa la watu waliokuwa wanamfuata Yesu, wengi wao walikuwa wanafuata miujiza tu, na si kingine… Lakini ni kundi dogo sana lililokuwa linafuata kwenda kusikia ni nini Yesu anazungumza…Kwa kuelewa zaidi pitia hapa>> Kwa wale walio nje, yote hufanywa kwa mifano.
Kwahiyo hili kundi dogo ambalo lilikuwa linafuatilia kwa makini maneno ya Yesu, ndio lililokuwa linamfuata baadaye Yesu akiwa peke yake na kumuuliza maana ya ile mifano yote aliyokuwa anaitoa. Na ndipo Yesu anawafafanulia mifano ile.
Lakini wengine wengi waliosalia, ambao hawakuwa na haja ya maneno ya uzima ya Yesu, badala yake walikuwa wanafuata miujiza tu, hawakuwa na muda wa kutaka kujua tafsiri ya ile mifano. Kwahiyo ile mifano ilipokuwa inatolewa na Yesu kwao iliishia kuwa kama hadithi tu, na wengine walikuwa wanaishia kuitafsiri wanavyojua wao. Lakini wale wengine wenye hekima walikuwa wanamfuata Yesu baadaye akiwa peke yake na kumuuliza maana ya ile mifano..
Marko 4:8 “Nyingine zikaanguka penye udongo ulio mzuri, zikazaa matunda, zikimea na kukua, na kuzaa, moja thelathini, moja sitini, na moja mia.
9 Akasema, Aliye na masikio ya kusikilia, na asikie.
10 NAYE ALIPOKUWA PEKE YAKE, wale watu waliomzunguka, na wale Thenashara, walimwuliza habari za ile mifano.
11 Akawaambia, Ninyi mmejaliwa kuijua siri ya ufalme wa Mungu, bali kwa wale walio nje yote hufanywa kwa mifano,
12 ili wakitazama watazame, wasione; Na wakisikia wasikie, wasielewe; Wasije wakaongoka, na kusamehewa”.
Sasa kwanini iwe hivyo?..kwanini Yesu asitoe mfano na tafsiri yake palepale??
Ni kwasababu siku zote Mungu hamlazimishi mtu kumfuata, wala hamlazimishi mtu kusikia maneno ya uzima. Bali Yule ambaye amefungua moyo wake kutafuta kumjua ndiye anayemfunulia zaidi.
Luka 19:26 “Nawaambia, Kila aliye na kitu atapewa, bali yule asiye na kitu atanyang’anywa hata alicho nacho”
Kwahiyo lile kundi ambalo halikutaka kutafuta kujua maana ya ile mifano, hiyo ndio kundi lililozibwa macho lisione (maana yake lilinyang’anywa hata kile kidogo lilichokipokea), kwamba lisikie tu mifano lakini lisielewe, kwasababu limekataa kutafuta ukweli.. Kwasababu wametangulia kuyafumba macho yao, na hivyo Mungu akaongeza upofu juu yao….Utaona biblia inalifafanu hilo vizuri katika..
Matendo 28:25 “Na walipokuwa hawapatani wao kwa wao, wakaenda zao, Paulo alipokwisha kusema neno hili moja, ya kwamba, Roho Mtakatifu alinena vema na baba zetu, kwa kinywa cha nabii Isaya,
26 akisema, Enenda kwa watu hawa, ukawaambie, Kusikia, mtasikia wala hamtafahamu; Na kuona, mtaona wala hamtatambua;
27 Kwa maana mioyo ya watu hawa imepumbaa, Na masikio yao ni mazito ya kusikia, Na macho yao WAMEYAFUMBA; Wasije wakaona kwa macho yao, Na kusikia kwa masikio yao, Na kufahamu kwa mioyo yao, Na kubadili nia zao, nikawaponya”
Mstari wa 27, hapo unasema… “na macho yao WAMEYAFUMBA”.. Maana yake hayajafumbwa na mtu, bali wameyafumba wao wenyewe, ili wasisikie… wakati Bwana Yesu anatoa ile mifano, hawakutaka kwenda kutafuta kuuliza maana yake. Hiyo waliyafumba macho yao… Na hiyo sasa Mungu akaitia uzito mioyo yao ili waendelee kukaa katika hali hiyo hiyo…kama neno lake linavyosema katika…
2Wathesalonike 2:10 “…..na katika madanganyo yote ya udhalimu kwa hao wanaopotea; kwa sababu hawakukubali kuipenda ile kweli, wapate kuokolewa.
11 Kwa hiyo Mungu awaletea nguvu ya upotevu, wauamini uongo;
12 ili wahukumiwe wote ambao hawakuiamini kweli, bali walikuwa wakijifurahisha katika udhalimu”.
Kwahiyo kinachotangulia kwanza ni Watu kuikataa kweli ndani ya mioyo yao, ndipo ile nguvu ya upotevu inaachiwa juu yao..
Hiyo ni tahadhari tu hata kwetu.
Kinyume na inavyodhaniwa na wengi kuwa neema ni kitu cha kuchezea, na kwamba unaweza kuchagua muda wowote wa kumgeukia Mungu, pasipo kujua kuwa kumgeukia Mungu ni neema, na kwamba saa ya wokovu ni sasa, na wakati uliokubalika ni sasa, endapo mtu ataisikia injili ikihubiriwa kwake na kuipuuzia pasipo kuzidi kutafuta ukweli, ile neema inaondolewa juu yake na nguvu ya upotevu inakuja juu yake.
Hizi ni siku za mwisho tunazoishi, na muda umekimbia sana, Kristo yupo mlangoni..na atakuja kama mwivi, kulinyakua kanisa lake, je utakuwa wapi siku hiyo? Wewe ambaye hulitilii maanani neno lake leo?..wewe ambaye ukiambiwa mavazi unayovaa ni mavazi yasiyompendeza Mungu, unadhihaki, wewe ambaye unaipuuzia sauti inayokuonya utubu ndani ya moyo wako?..
Bwana anarudi.
Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema,
Kwa maombezi/Ratiba za ibada/ Ushauri/ Maswali.
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312
pia kama utapenda uyapate mafundisho haya kwa njia ya Whatsapp au email basi tutumie ujumbe kwenye namba hizo hizo.
Mada Nyinginezo:
Biblia ina maana gani inaposema akonyezaye kwa jicho huleta masikitiko?
Ukisoma kitabu cha Mwanzo, utaona mara baada ya Adamu na Hawa kuasi, kwa kula yale matunda ya mti wa ujuzi wa mema na mabaya,ambayo Mungu aliwakataza wasiyale, utaona pale kwa tendo lile hawakuona kwanza dhambi ndani yao, bali waliliona tatizo kwenye miili yao. Hawakujiona wamemkosea Mungu, bali walijiona wapo uchi, na ndio maana muda ule ule wakaanza harakati zao za kutafuta namna ya kwenda kujisitiri na sio kwenda kutubu,
Wakaenda kujishonea matawi ya mtini, ili wajirudishe katika hali yao ya mwanzo, wajaribu kuisitiri ile aibu iliyowaingia, sasa unaweza kudhani walikuwa ni wajinga, hapana hawakuwa wajinga, walijua kabisa, nyenzo iliyowafanya wao waweze kumkaribia Mungu na kuzungumza naye ilikuwa ipo katika miili yao. Ndio maana wakakimbilia kwanza kwenda kushona majani,wajisiriti na sio kutubu dhambi zao.
Lakini tunaona hata baada ya kufanya vile, bado haikusaidia waliendelea kujiona wapo uchi, kuonyesha kuwa aibu ile ilipenya mpaka ndani kabisa ya mioyo yao. waligundua hata wakijisitiri kwa nguo za namna gani, bado miili yao imeshaingiwa na aibu kubwa isiyoneneka.
Mwanzo 3:7 “Wakafumbuliwa macho wote wawili wakajijua kuwa wa uchi, wakashona majani ya mtini, wakajifanyia nguo.
8 Kisha wakasikia sauti ya Bwana Mungu, akitembea bustanini wakati wa jua kupunga; Adamu na mkewe wakajificha kati ya miti ya bustani, Bwana Mungu asiwaone.
9 Bwana Mungu akamwita Adamu, akamwambia, Uko wapi?
10 Akasema, Nalisikia sauti yako bustanini, nikaogopa kwa kuwa mimi ni uchi; nikajificha”.
Ni kama tu wakati wa Samsoni, yeye alijua kabisa asili ya nguvu zake ipo katika nywele zake, lakini siku alipokatwa nywele na Delila, muda ule ule alikuwa dhaifu hata wafilisti walipokuja hakuweza tena kushindana nao,. Ndivyo ilivyokuwa kwa Adamu na Hawa, ujasiri wao wa kuongea na Mungu ulikuwa upo katika miili yao. Lakini walipoasi maagizo ya Mungu, waliona kasoro kubwa sana, ambayo hata majani na ngozi ambazo Mungu alikuja kuwafanyia baadaye ziwasiriti bado hazikufanikiwa kuiondoa ile aibu ya miili yao.
Sasa, aibu hii ya miili ipo hadi sasa, na ndio maana kwa miili yetu hii hatuwezi kumwona Mungu, au kuzungumza na Mungu. Haiwezekani, tatizo sio Mungu, tatizo ni aibu iliyo kwenye miili yetu, haiwezi kustahili utakatifu wa Mungu, sikuzote tutaukimbia tu.
Na ndio maana baada ya Mungu kulijua hilo, akamtuma mwanawe Yesu Kristo duniani, ili afe, kisha afufuke, kisha aende mbinguni kutuandalia VAZI lake mwenyewe ambalo Kila mmoja wetu atakapolivaa hilo, basi aibu hiyo ya mwili ife, na kuanzia hapo amwone Mungu, na azungumze naye Uso kwa Uso kwa ujasiri wote, katika utakatifu hata Zaidi ya kile alichokuwa anakifanya Adamu kwa Mungu pale Edeni.
Na vazi hilo ni MIILI MIPYA itakayoshuka kutoka mbinguni. Hapo ndipo utajua ni kwanini siku tukienda katika unyakuo, hatutaacha miili yetu hapa chini ardhini, bali tutafufuliwa nayo kwanza, kisha tutavikwa hii miili mipya kama vile VAZI,. Na saa hiyo hiyo aibu ya mwili itaondoka..hatutajiona tena tupo uchi, tutapata ujasiri mkubwa sana wa kumwona Mungu wetu, na kuzungumza naye, na kumfurahia milele. Biblia inasema..
2Wakorintho 5:1 “Kwa maana twajua ya kuwa nyumba ya maskani yetu iliyo ya dunia hii ikiharibiwa, tunalo jengo litokalo kwa Mungu, nyumba isiyofanywa kwa mikono, iliyo ya milele mbinguni.
2 Maana katika nyumba hii twaugua, tukitamani sana kuvikwa kao letu litokalo mbinguni;
3 IKIWA TUKIISHA KUVIKWAHATU TAONEKANA TU UCHI.
4 Kwa sababu sisi tulio katika maskani hii twaugua, tukilemewa; si kwamba twataka kuvuliwa, bali kuvikwa, ili kitu kile kipatikanacho na mauti kimezwe na uzima”.
Unaona? Biblia inasema. Tukishavikwa hiyo miili mipya hatutaonekana tena tu Uchi.
Tutamani sana tuifikie hiyo siku, kwasababu itakuwa ni siku ya furaha isiyokuwa na kifani, miili yetu itafanana na ya malaika, haitakuwa na kuumwa, au kufa, au kusinzia, au kuchoka, au kushikwa na udhaifu wowote. Kwasababu itakuwa ni miili ya kimbinguni, vazi la utukufu.
Swali sasa lipo kwako, je wakati huo ukifika utakuwa wapi? Ikiwa leo usiku parapanda italia utakuwa wapi ndugu yangu, kwasababu dalili zote za mwisho wa dunia Bwana Yesu alizozizungumza katika maandiko zimeshatia karibia zote, tunachongoja sasahivi ni UNYAKUO muda wowote. Embu jiulize utakuwa katika majuto makubwa kiasi gani utakaposikia wenzako baadhi wameondoka, wapo mbinguni wakimfurahia Mungu, halafu wewe umebaki hapa duniani, ukijiandaa na dhiki kuu ya mpinga-Kristo na mapigo ya Mungu.
Ndugu yangu, usisubiri, mhubiri Fulani siku moja aje kukubembeleza umgeukie Muumba wako, hizi ni nyakati za wewe mwenyewe kutafakari ulipotoka, ulipo na unapoelekea, na kufanya uamuzi sahihi, kwa hali inavyoendelea sasa hivi duniani, hakuna anayejua kama kesho atakuwa hai. Hivyo tukilijua hilo ni wakati wetu wa kumkaribisha Kristo mioyoni mwetu kwa kumaanisha kabisa.Ili atupe wokovu na uzima wa milele.
Maran Atha.
Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema,
Kwa maombezi/Ratiba za ibada/ Ushauri/ Maswali.
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312
pia kama utapenda uyapate mafundisho haya kwa njia ya Whatsapp au email basi tutumie ujumbe kwenye namba hizo hizo.
Mada Nyinginezo:
SWALI: Samahani mtumishi kuna andiko linatoka kitabu cha Mhubiri 7:29 sijalielewa vizuri linamaanisha nini
Mhubiri 7:29 “Tazama, hili tu nimeliona; Mungu amemfanya mwanadamu mnyofu, lakini wamebuni mavumbuzi mengi”.
JIBU: Mungu alipomuumba mwanadamu alimuumba katika ukamilifu wote, Adamu na Hawa walikuwa ni watu ambao hawakuwa na kasoro yoyote, si ya kimwili, si ya kiroho. Waliumbwa katika ukamilifu wa furaha,amani, upendo, maarifa na kumcha Mungu.
Lakini ilifika wakati, hawakuridhika, na vile ambavyo Mungu alivyowaumba na kuwaweka, wakataka kuwa sawa na Mungu, wakabuni namna yao wenyewe ya kuishi, ya kutaka uhuru wao wenyewe. Na ndio hapo utaona wakashawishika kwenda kula matunda ya mti wa ujuzi wa mema na mabaya, ambayo Mungu aliwaambia wasile, Ili wakipate wanachokitafuta. Lakini matokeo yake ni kuwa mpaka sasa mwanadamu hajakipata alichokitafuta tangu wakati ule, kinyume chake ndio matatizo yalizidi kuongezeka japokuwa anajibunia kila siku njia zake mwenyewe za kuishi.
Mpaka sasa mambo hayo yanaendelea, tunavyoona watu wakijibadilisha maumbile yao, kisa tu hayawavutii machoni pao. Na ndio hapo utaona, wanawake wanachubua ngozi zao, ili waonekane weupe, wengine wanapaka make-up ili waonekane wa kitofauti na wenye mvuto zaidi, wanaweka kucha za bandia, wanavaa wigi za wazungu.. Yote hayo ni mavumbuzi mengi watu wanaojibunia..na kibaya zaidi leo hii wameshafikia mpaka hatua ya kubadilisha maumbile yao kwa kufanyiwa upasuaji na kunyeshwa madawa makali.
Hawataki tena kuwa wao wa asili kama Mungu alivyowaumba ,wanataka wawe kama wanavyotaka wao. Sasa badala mavumbuzi yao yawasaidie, kinyume chake ndio yanawaletea madhara kama sio kuwapoteza kabisa.
Hivyo, tunapaswa tujue kuwa si mpango wa Mungu tujigeuze mionekano yetu, kwasababu Mungu alituumba kwa mfano wake na sura yake, alishatuumbia ukamilifu ndani yetu,.Jukumu letu sisi ni kumcha yeye, na kuisiliza sauti yake basi.
Shalom.
Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema,
Kwa maombezi/Ratiba za ibada/ Ushauri/ Maswali.
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312
pia kama utapenda uyapate mafundisho haya kwa njia ya Whatsapp au email basi tutumie ujumbe kwenye namba hizo hizo.
Mada Nyinginezo:
Swali: Yale maelezo ya Ufunuo 12:7-12, yanaeleza vita vya wakati upi?, ile ya kwanza kabisa kabla ya sisi kuumbwa au kuna nyingine iliyotokea tena?
Zipo vita mbili kuu zinazowahusu shetani na Malaika watakatifu.
Vita ya kwanza: Ni ile iliyopiganwa mbinguni, zamani sana kabla ya wanadamu kuumbwa, pale ambapo ibilisi (yaani shetani), alipoasi kwa kutamani kuwa kama Mungu, na hivyo akashindwa vita ile na kutupwa chini, na baada ya kushindwa vita hiyo akawa hana uwezo tena wala mamlaka ya kurudi katika nafasi yake mbinguni. (akaondolewa mbinguni). Lakini hiyo haikumfanya asifike kwenye enzi ya haki ya Mungu iliyopo mbinguni.
Hata katika maisha ya kawaida, mtu anapoasi katika ngazi Fulani kuu ya serikalini mfano Uwaziri, na hata kufikia kufukuzwa, na kuipoteza ile nafasi, hiyo haimfanyi asiwasilishe mashtaka yake mahakamani. Maana yake kama ana haki zake za msingi, anazozidai kule alipoondolewa, au anajambo la kupashitaki kule alipotoka, mahakama ya haki lazima imsikilize na kumpa haki yake kama anastahili. Kwasababu Mahakama ni moja ya muhimili wa serikali ambayo, haina upandeo fulani wa kuegemea wala kupendelea, ina uwezo hata wa kuishtaki serikali nzima ilimradi tu impatie mtu mmoja haki yake, na mtu yeyote anauwezo wa kwenda mahamani kushitaki.
Na pia enzi ya Mungu (yaani mbinguni) pamegawanyika katika sehemu kuu mbili, ipo sehemu ambapo Malaika wapo, ambapo ndio kule shetani alipokuwepo kabla ya kuasi, na pia kuna mahali pa kiti cha Hukumu ya Mungu.
Sasa shetani aliondolewa katika nafasi yake huko mahali malaika walipo, huko hawezi kufika tena wala kurudi, lakini mahali pa hukumu ya Mungu, mbinguni bado ana uwezo wa kufika, na kupeleka hoja zake, na mashtaka yake. Na Mungu siku zote ni wa haki, huwa hana upendeleo, anayestahili kumpatia haki yake anampatia na asiyestahili hampatii.
Sasa vita ya kwanza ilimwondoa shetani katika nafasi yake ya ukuu kule mbinguni, lakini haikuishia hapo, ipo vita nyingine ya pili ambayo ilianza kuendelea tangu alipoondolewa mbinguni mpaka sasa, na hiyo si nyingine zaidi ya vita katika enzi ya hukumu ya Mungu, huko shetani anafika kila siku, kupeleka hoja zake na mashtaka yake dhidi yetu. Na siku zote inajulikana vita vya mtu aliyeshindwa huwa ni vikali mno na vinaumiza kichwa, kwasababu kila siku utasikia yupo mahakamani kushitaki hiki au kile, mara kakata rufaa n.k. Kwahiyo hata baada ya shetani kushindwa mbinguni, bado anaendeleza vita katika enzi ya hukumu ya Mungu, iliyopo mbinguni.
Ndio maana kuna umuhimu mkubwa sana wa kumpokea Yesu, na kuishi maisha ya ukamilifu na uangalifu, kwasababu adui yetu shetani yupo kila siku kuchukua habari zetu na kuzifikisha mbele za Mungu, na kutushitaki.
Lakini tunapookoka na kuishi maisha ya uangalifu katika hii dunia, shetani anakosa hoja za kupeleka mbele za Mungu, na badala yake, malaika watakatifu wanapeleka mambo mazuri tunayoyafanya mbele za Mungu, ili tupewe thawabu. Kwasababu kama vile wanavyotumwa na Mungu kutulinda, vile vile wanachukua mambo yetu mazuri tunayoyafanya na kuyapeleka mbele za haki ya Mungu..
Mathayo 18: 10 “Angalieni msidharau mmojawapo wadogo hawa; kwa maana nawaambia ya kwamba malaika wao mbinguni siku zote huutazama uso wa Baba yangu aliye mbinguni”.
Na kamwe malaika watakatifu hawapeleki mashitaka yetu mabaya mbele za Mungu wetu..ni shetani peke yake ndio anafanya hivyo…
2Petro 2: 11 “Wenye ushupavu, wenye kujikinai, hawatetemeki wakiyatukana matukufu; ijapokuwa malaika ambao ni wakuu zaidi kwa uwezo na nguvu, hawaleti mashitaka mabaya juu yao mbele za Bwana”
Kwahiyo kwasasa kinachoendelea mbinguni, mahali pa haki ya Mungu, wanasimama malaika watakatifu kututetea na wakati huo huo anapita shetani kila mara kutushitaki.. Hiyo ndio vita inayoendelea sasa katika roho, (mapambano kati ya Mikaeli na malaika zake wakishindana na Yule joka na malaika zake), kuhusu mambo yetu sisi tuliomwamini Yesu, Malaika wanatutetea, shetani anatushitaki..(Kwa urefu juu ya hoja hizo fungua hapa >> Huduma ya Malaika watakatifu)
Na vita hivyo vitahitimishwa na unyakuo, wakati watakatifu watakapoondolewa duniani, shetani hatakuwa tena na mtu wa kumshitaki, wala hoja ya kwenda kupeleka mbele za Mungu, kuwashitaki wateule, kwasababu watakuwa wameshashinda na wapo mbinguni wakati huo, na hivyo atatolewa moja kwa moja katika hiyo enzi ya haki ya Mungu, na baada ya kuondolewa na kutupwa chini atakasirika kwasababu hatafika tena kumshtaki mtu yeyote wa Mungu, hivyo atashuka kwa hasira na kuanza kufikiri jambo lingine la kufanya..
Na jambo la kwanza litakalomjia ni kutafuta kufanya vita na vita na Taifa la Israeli, pamoja na wale wakristo vuguvugu walioachwa kwenye unyakuo, ambao watakataa kuipokea chapa yake. Hivyo atashuka chini na kumwingia Yule mwana wa kuasi (Mpinga-Kristo) na kuonyesha rangi zake zote kwa ulimwengu mzima, atawatesa watu kwa miaka mitatu na nusu (Miezi 42). Huo ndio ule wakati wa dhiki kuu.
kama tunavyosoma katika Ufunuo 12..
Ufunuo 12:7 “Kulikuwa na vita mbinguni; Mikaeli na malaika zake wakapigana na yule joka, yule joka naye akapigana nao pamoja na malaika zake;
8 nao hawakushinda, wala mahali pao hapakuonekana tena mbinguni.
9 Yule joka akatupwa, yule mkubwa, nyoka wa zamani, aitwaye Ibilisi na Shetani, audanganyaye ulimwengu wote; akatupwa hata nchi, na malaika zake wakatupwa pamoja naye.
10 NIKASIKIA SAUTI KUU MBINGUNI, IKISEMA, SASA KUMEKUWA WOKOVU, NA NGUVU, NA UFALME WA MUNGU WETU, NA MAMLAKA YA KRISTO WAKE; KWA MAANA AMETUPWA CHINI MSHITAKI WA NDUGU ZETU, YEYE AWASHITAKIYE MBELE ZA MUNGU WETU, MCHANA NA USIKU.
11 Nao wakamshinda kwa damu ya Mwana-Kondoo, na kwa neno la ushuhuda wao; ambao hawakupenda maisha yao hata kufa.
12 Kwa hiyo shangilieni, enyi mbingu, nanyi mkaao humo. Ole wa nchi na bahari! Kwa maana yule Ibilisi ameshuka kwenu mwenye ghadhabu nyingi, akijua ya kuwa ana wakati mchache tu”
Hapo katika mstari wa 10, utaona Malaika mmoja anatangaza kwamba…“Sasa kumekuwa wokovu, na nguvu, na ufalme wa Mungu wetu, na mamlaka ya Kristo wake; kwa maana ametupwa chini mshitaki wa ndugu zetu, yeye awashitakiye mbele za Mungu wetu, mchana na usiku”..Maana yake Yule anayewashitaki watakatifu hawezi tena kupanda kwenda kuwashitaki…kashashindwa, kwasababu wateule wameshamshinda kwa damu ya mwanakondoo, na wameenda kwenye unyakuo mbinguni..huko hawezi kuwashitaki tena awatoe huko..
Lakini “ole wa nchi na bahari”..maana yake ole wa waliobakia ambao hawakwenda mbinguni. Ibilisi anashuka kwao mwenye ghadhabu nyingi, na pia ole kwa Taifa la Israeli, ambalo ndio “Yule mwanamke mwenye mimba (Ufu.12:1)”.
Hivyo hiyo biblia inatutahadharisha, juu ya mambo yanayokuja. Ndugu sasa hivi unafahamika kama ni mkristo lakini unazini kwa siri, unaiba, unaua, unacheza kamari, unavaa vibaya, unatukana, n.k..kumbuka shetani anayefikisha hayo kila siku mbele za haki ya Mungu, na kukushitaki. Na lengo lake ni ufe katika hizo dhambi ili uwe wake milele, au kama unyakuo utapita leo wewe ubaki, uingie katika dhiki kuu.
Dhiki kuu sio sehemu ya kutamani kuwepo, kama umeshindwa leo kumkiri Yesu wakati neema ya Mungu bado ipo, hutaweza siku ile katika dhiki kuu. Kama umeshindwa kuvumilia njaa ya siku moja katika kufunga ili uutafute uso wa Mungu hutaweza kuvumilia njaa ya miaka mitatu na nusu ya dhiki kuu. Kama leo hii kipindi cha amani unashindwa kujikana nafsi na kuchukua msalaba wako umfuate Yesu, kamwe hutaweza kufanya hivyo wakati wa dhiki kuu.
Hapo Yule malaika anasema… “Nao wakamshinda kwa damu ya Mwana-Kondoo, na kwa neno la ushuhuda wao; AMBAO HAWAKUPENDA MAISHA YAO HATA KUFA”.
Je leo hii unayapenda maisha yako kiasi kwamba, wokovu kwako ni jambo lililopitwa na wakati?, fashion za dunia,umaarufu, kusifiwa, kutukuzwa, kupendwa na kila mtu ndio mambo ya heshima kwako?…Hapo biblia inasema “ambao hawakupenda maisha yao hata kufa!!!”, ndio waliomshinda shetani!!.
Bwana Yesu pia alisema.. Yohana 12:25 “Yeye aipendaye nafsi yake ataiangamiza; naye aichukiaye nafsi yake katika ulimwengu huu ataisalimisha hata uzima wa milele”.
Kama bado hujampokea Kristo maishani, ni vizuri ukampokea leo, kwa kumwamini kwamba alikuja duniani akafa kwaajili ya dhambi zako, na akafufuka na kupaa mbinguni, na pia atarudi tena. Na kwa kutubu dhambi zako kwa kumaanisha kutozifanya tena, Na pia kwa kubatizwa katika ubatizo sahihi wa maji tele (Yohana 3:23), na kwa jina la Yesu Kristo (Matendo 2:38, 8:16), naye atakupa kipawa cha Roho wake mtakatifu, atakayekuongoza na kukutia katika kweli yote ya kuyaelewa maandiko.
Bwana akubariki.
Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema,
Kwa maombezi/Ratiba za ibada/ Ushauri/ Maswali.
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312
pia kama utapenda uyapate mafundisho haya kwa njia ya Whatsapp au email basi tutumie ujumbe kwenye namba hizo hizo.
Mada Nyinginezo:
2Wathesalonike 3:13 inasema..
“Lakini ninyi, ndugu, msikate tamaa katika kutenda mema”.
Unajua mpaka biblia inakuambia usikate tamaa, inamaanisha kuwa si kitu chepesi kukishikilia wakati wote. Si kitu ambacho unaweza ukaona faida yake moja kwa moja pale unapokifanya.. Lakini katika yote hayo bado inakuambia usikate tamaa.
Ili jambo lolote liwe wema, ni lazima malipo yake yasilingane na huduma iliyotolewa. Kwamfano mtu anapokwenda kuwasaidia yatima au maskini, huo ni wema, kwasababu hawana cha kumlipa hata baada ya kuwapa mahitaji yao, au pale anapowasomesha ndugu, huo nao ni wema, kwasababu pesa hizo ungeweza kuzitumia katika mambo yake mengine lakini ameona vema, ujinyime yeye uwape wengine maarifa.. Au unapowapa wengine chakula au mavazi bila kuwachaji pesa au kuwadai kitu chochote huo ni wema.. Au unapowapa wengine maarifa ya ufalme wa mbinguni bila malipo yoyote huo nao ni wema mkuu sana n.k.
Lakini katika hayo, kuna wakati akili inaweza kukujia, ukajisikia kuchoka na kusema nimeshasaidia watu sana mbona sioni faida yoyote ya kufanya hivyo? Au mbona sioni nikirudishiwa fadhila yoyote kutoka kwao? Wacha nipunguze wema wangu, nianze kujijali mimi mwenyewe. Au nitafute mambo yangu mwenyewe.
Katika mazingira kama hayo, biblia inasema.. usichoke kutenda wema..Kwasababu ni mbegu nzuri sana ambayo unaipanda leo, lakini siku moja utavuna matunda yake ukiwa mvumilivu.
Wagalatia 6:9 “Tena tusichoke katika kutenda mema; maana tutavuna kwa wakati wake, tusipozimia roho”.
Hata kama utaona wale uliowatendea mema wamekutangulia,wewe umekuwa daraja kwao la kufika juu, au wengine wamekudharau kwa ukarimu wako, bado usichoke katika kutenda kwako, kwasababu hicho unachokipanda thamani yake ni kubwa kuliko fedha au dhahabu. Utakuja kujua vizuri utakapovuka kule ng’ambo.
Katika biblia, tunamwona, mtu mmoja aliyeitwa Mordekai, yeye alikuwa ni mlinda mlango wa mfalme, lakini siku moja baadhi ya watumishi walipanga njama ili wamuue mfalme. Mordekai alipopata habari, kwasababu alikuwa ni mtu mwema, hakukaa kimya bali alikwenda kutoa taarifa ya njama hizo, na hatimaye mfalme akanusurika kifo, lakini biblia inatuonyesha akasahaulika, muda mrefu ukapita, wala hakuna aliyekumbuka wala kujali wema wake.
Siku moja akiwa katika hatihati ya kuuliwa na adui yake aliyeitwa Hamani, biblia inatuambia usiku huo huo mfalme alikosa uzingizi kabisa, ndipo akaanza kupitia vitabu vya kumbukumbu za taarifa za kifalme, ndipo akakutana na tukio la wema alilofanyiwa na Mordekai, mfalme akauliza je mtu huyu alitendewa fadhila gani?, wakasema, hakutendewa lolote. Ndipo akatoa maagizo kwamba avikwe mavazi yake ya kifalme anayoyavaa yeye, kisha apandishwe kwenye farasi ambaye yeye mwenyewe ndiye anayempanda, kisha wamzungushwe mji mzima, huku akipigiwa mbiu, ili atukuzwe mbele ya watu wote, kwasababu mfalme AMEMUHESHIMU biblia inasema hivyo;. Soma Esta 6
Sasa mambo hayo yanafunua na ya rohoni pia. Ukiwa ni mtenda wema, ipo Heshima ya kipekee sana, itokayo kwa Mungu mwenyewe, italetwa juu yako, siku ile ikifika. Atakugawia ule utukufu wake mwenyewe,.. Biblia inasema..
Warumi 2:6 “atakayemlipa kila mtu kwa kadiri ya matendo yake; 7 wale ambao KWA SABURI KATIKA KUTENDA MEMA WANATAFUTA UTUKUFU NA HESHIMA NA KUTOKUHARIBIKA, watapewa uzima wa milele; 8 na wale wenye fitina, wasioitii kweli, bali wakubalio dhuluma, watapata hasira na ghadhabu; 9 dhiki na shida juu ya kila nafsi ya mwanadamu atendaye uovu, Myahudi kwanza na Myunani pia; 10 BALI UTUKUFU NA HESHIMA NA AMANI KWA KILA MTU ATENDAYE MEMA, Myahudi kwanza na Myunani pia”;
Unaona? hivyo, usichoke kutenda mema, kumbuka wema mkuu ni pamoja na kuwakumbuka walio katika dhambi na kuwavuta kwa Bwana. Pia kuwafariji na kuwaombea wale waliowadhaifu katika Imani. Swali ni je! Katika maisha yako, ni mema mangapi, ulishawahi kufanya kwa ajili ya Mungu?
Bwana atusaidie, tuyatimilize yote.
Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema,
Kwa maombezi/Ratiba za ibada/ Ushauri/ Maswali.
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312
pia kama utapenda uyapate mafundisho haya kwa njia ya Whatsapp au email basi tutumie ujumbe kwenye namba hizo hizo.
Mada Nyinginezo:
NGAZI 7 AMBAZO MKRISTO NI LAZIMA AZIPANDE KUUFIKIA UKAMILIFU.
Nini maana ya mhubiri 9:11? si wenye mbio washindao katika michezo?
SWALI: a) Naomba kujua tofauti Kati ya Hekima , Ufahamu na Maarifa kwenye biblia
b) jinsi gani vitu hivyo vinavyohusiana?
Mithali 2:6 “Kwa kuwa BWANA huwapa watu hekima; Kinywani mwake hutoka maarifa na ufahamu”;
2 Mambo ya Nyakati 1:10 “Basi sasa nipe hekima na maarifa, nijue kutoka na kuingia mbele ya watu hawa; kwa kuwa ni nani awezaye kuwahukumu watu wako hawa walio wengi”?
JIBU:
Maarifa ni uwezo wa kujua mambo mengi, na hiyo inakuja kwa kusoma sana, au kujifunza Neno la Mungu kwa bidii, au kusikiliza, au kupitia mazingira Fulani ambayo yatakupa uzoefu husika.
Mungu anatutaka sana watu wake tuwe na maarifa ya kutosha kuhusu yeye ili tusiangamie. Kwani biblia inasema,
Watu wangu wanaangamizwa kwa kukosa maarifa; (Hosea 4 :6)
Na ndio maana moja ya zile ngazi 7 zinazozumngumziwa katika kitabu cha 2Petro ambazo kila mkristo anapaswa azipitie, ni maarifa.
2Petro 1:5 “Naam, na kwa sababu iyo hiyo mkijitahidi sana kwa upande wenu, katika imani yenu tieni na wema, na katika wema wenu maarifa”
Tukikosa maarifa hata kama sisi tutasema ni wakristo tutashindwa kuwa na ujasiri na Mungu kwasababu hatujui tabia zake, tutashindwa hata kumwamini Mungu ipasavyo kwasababu hatuujui uweza wake, vilevile tutaishi maisha ya uvuguvugu kwasababu tu,hatuna maarifa ya kutosha ya kujua nyakati na majira tunayoishi. Hivyo maarifa ni nyenzo muhimu sana kwa mkristo yeyote.
Na hayo yanakuja kwanza kwa kuonyesha bidii kusoma Neno lake ‘kwa kujifunza’ na sio kama gazeti. Pia kwa kuonyesha kiu ya kutafuta kuijua kweli yake kwa kusikiliza mafundisho sahihi yatakayokusaidia kumjua yeye kupitia watumishi wake.
Hekima. Ni uwezo wa kupambanua, kuhukumu, na kufanya maamuzi sahihi. Sulemani alimwomba Mungu hekima na Mungu akampa, na ndio maana utaona mwanzoni kabisa,mwa hekima yake kujidhihirisha ilikuwa ni siku ile wale wanawake wawili walipomfuata, awamue kwa habari ya watoto wao, sasa kwa tukio lile kama asingekuwa na hekima ya ki-Mungu ndani yake asingeweza kupambanua lolote..(Soma 1Wafalme 3:16-18 )
Utaona tena wakati ule yule malkia wa Sheba alipokuja kumjaribu kwa mafumbo yake ya ndani, aliweza kuyafichua yote, kwa usahihi, mpaka yule malkia akashangaa sana (1Wafalme 10)
Vivyo hivyo katika siku hizi za mwisho, Mungu anasema walio na hekima, ndio watakaoelewa siri za Mungu na mafumbo ya yule mnyama(mpinga-Kristo) na kazi zake, inahitaji hekima ya Mungu ya kutosha iwepo ndani yetu ili tuelewe, vinginevyo, zipo habari katika haya maandiko kamwe hatutakaa tuzielewe, hususani zile zinazozuhusu nyakati za mwisho. Soma
Danieli 12:10 “Wengi watajitakasa, na kujifanya weupe, na kusafika; bali wabaya watatenda mabaya; wala hataelewa mtu mbaya awaye yote; BALI WAO WALIO NA HEKIMA NDIO WATAKAOELEWA.
Ufunuo 3:17 “tena kwamba mtu awaye yote asiweze kununua wala kuuza, isipokuwa ana chapa ile, yaani, jina la mnyama yule, au hesabu ya jina lake.
18 HAPA NDIPO PENYE HEKIMA. Yeye aliye na akili, na aihesabu hesabu ya mnyama huyo; maana ni hesabu ya kibinadamu. Na hesabu yake ni mia sita, sitini na sita”.
Ufahamu ni uelewa. Ukikosa uelewa huwezi kutafuta maarifa, wala kuomba hekima. Wanyama hawana ufahamu, na ndio maana hawajui kumtafuta Mungu, halikadhalika, wanadamu pia tumepishana viwango vya ufahamu, na ndio maana wengine hawamtafuti Mungu kwasababu wamekosa ufahamu wa kujua umuhimu wa Mungu maishani mwao ni upi.
Kwa mfano mtu anayepata ufahamu wa kujua madhara ya zinaa, kamwe hawezi kwenda kuzini ovyo, kwasababu anajua mwisho wake utakuwa ni ukimwi, au mimba zisizotarajiwa. Au kijana anayepata ufahamu wa kujua elimu ina umuhimu gani kwake ,kamwe hawezi kuchezea shule.
Vivyo hivyo kibiblia mtu anayeikimbia dhambi huyo amepata ufahamu.
Ayubu 28:27 “Ndipo alipoiona na kuitangaza; Aliithibitisha, naam, na kuichunguza.
28 Kisha akamwambia mwanadamu, Tazama, kumcha Bwana ndiyo hekima, NA KUJITENGA NA UOVU NDIO UFAHAMU”.
b) Hivyo vyote hivi vitatu ni nguzo kwa mtu yeyote kuwa navyo katika maisha yake, Ufahamu, maarifa na Hekima. Na vyote hivi Mungu anataka kuviona ndani yetu.
Hivyo tumche Bwana, pia tuonyeshe kumpenda na kumtafuta ndipo atakapotugawia.
Shalom.
Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema,
Kwa maombezi/Ratiba za ibada/ Ushauri/ Maswali.
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312
Jiunge na kundi letu la mafundisho ya Biblia whatsapp kwa kubofya hapa > Group-whatsapp
Mada Nyinginezo:
Nakusalimu katika jina kuu lipitalo majina yote la Bwana wetu Yesu Kristo. Karibu tuyatafakari maneno yake pamoja, Tukisoma kitabu cha Mathayo ile sura ya saba inatuambia..
Mathayo 7:28 “Ikawa, Yesu alipoyamaliza maneno hayo, makutano walishangaa mno kwa mafundisho yake;
29 kwa maana alikuwa akiwafundisha kama mtu mwenye amri, wala si kama waandishi wao”.
Maandiko hayo yanatuonyesha, mafundisho ya Yesu yalikuwa ni ya tofauti sana na jinsi yalivyotegemewa na watu wengi wakati ule, na hata yanavyochukuliwa na watu wengi leo hii, hapo anasema alipoanza kufundisha makutano walishangaa “MNO”.. Ikiwa na maana maneno yake yalikuwa ni tofauti sana na walichokuwa wanakitarajia kwake, na sababu ya kushangaa kwao ni kwasababu alikuwa akifundisha kama mtu mwenye AMRI, na sio kama waandishi wao.
Mtu mwenye amri sikuzote huwa ni mtu mwenye mamlaka, na mtu wa namna hiyo maneno yake huwa sio ya kupinda pinda, au ya kupamba pamba, bali maneno yake yananyooka, na ya wazi sana, kwamfano raisi akisimama mbele ya watumishi wake, huwa hawambelezi bembelezi, bali anapotoa maagizo, labda akisema, nataka huu mradi uishe ndani ya wiki mbili, hapo ni hakuna cha majadiliano, yule mtumishi ni lazima afanye ili uishe, asipofanya hivyo ni kazi hana, kamwe haji kumwambia naomba unisaidie kama ikikupendeza huu mradi uishe ndani ya wiki 2, Huwezi kusikia mwenye mamlaka yoyote kuzungumza maneno ya kusihi sihi namna hiyo.
Ndivyo Bwana Yesu alivyokuja kuhubiri ulimwenguni, ukisoma mistari iliyotangulia ya juu na mengine iliyofuata utaona maneno yake yalikuwa yamenyooka sana, bila maficho ficho tofauti na ya waandishi, ambao wenyewe walikuwa ni kufundisha desturi za kiyahudi tu kwa watu, na kuwapembeleza, hawawaambii watu wajibu wao kwa Mungu, au madhara yatokanayo na dhambi, au kumpenda Mungu kwa mioyo yao yote.
Lakini Bwana Yesu aliwaambia, mmesikia imenenewa, ‘Lakini mimi nawaambia hivi’ kuonyesha kuwa anayo mamlaka “YEYE”..Unaona, kuna mahali akasema kiungo chako kimoja kikikukosea king’oe ukitupe mbali na wewe, kuliko mwili wako wote kutupwa jehanum, mahali ambapo funza wa kule hawafi wala moto wake hauzimiki..Maneno ambayo usingekaa uyasikie yakitoka kwenye vinywa vya waandishi hata siku moja, kumwambia mtu apoteze kiungo chake kimoja kwa ajili ya kunusuru maisha yake ya milele, hakuna jambo kama hilo. Kuipoteza biashara yakoe haramu, au kuwapoteza marafiki zake waovu, au kupoteza hata kiungo cha mwili wake mwenyewe kinachomkosesha, huwezi sikia wakifundisha hivyo.
Aliwaambia, mtu asiyeuchukua msalaba wake, na kumfuata hawezi kuwa mwanafunzi wake, ampendaye Baba au mama kuliko yeye hamstahili, aipataye nafsi yake ataipoteza, na aipotezaye kwa ajili yake ataipata…
Wengi watakuja wakati ule wakisema, Bwana hatukutoa pepo, na kufanya miujiza mingi kwa jina lako? Lakini mimi nitawaambia Dhahiri, siwajui ninyi ondokeni kwangu mtendao maovu.
Jitahidini kuingia kupitia mlango uliomwembamba, kwasababu njia ni pana iendayo upotevuni. .
Unaona maneno hayo ni maneno yaliyonyooka, yanakueleza madhara ya kitu Fulani,kama usipochukua tahadhari.
Hata sasa kinywa cha Bwana ni kilekile, kwasababu anasema yeye ni yule yule jana na leo na hata milele. Bado anazungumza kama mtu mwenye amri, lakini watu wa leo, wanayatafsiri maneno ya namna hiyo kama KUHUKUMU au KUTISHA WATU. Watu wanataka kusikia maneno kama ya waandishi. ‘Yesu anakupenda’, wewe kuwa tu mtu mwema inatosha, utabarikiwa, utafanikiwa, waandishi hawataki kukueleza uvuuaji wako mbovu, kuwa hautakupeleka mbinguni, hawawezi kukueleza hivyo, kwasababu wanaogopa wasimpoteze mshirika wao.
Waandishi hawawezi kukueleza habari za siku za mwisho, wanahisi watakuogopesha, na hivyo utawakimbia.
Ndugu Ukiona upo mahali unahubiriwa maneno laini laini tu, wakati wote ujue kuwa Yesu hayupo hapo, bali ni waandishi ndio wanaokufundisha. Yesu sikuzote anazungumza kwa amri, ndivyo alivyo anasema..
Ufunuo 3:19 “Wote niwapendao mimi nawakemea, na kuwarudi; basi uwe na bidii, ukatubu”.
Usidanganywe na mtu anayesema kufundishwa maneno laini ndio ishara ya upendo. Bwana Yesu hakufanya hivyo, lakini ni mtu aliyetupenda kuliko mtu yeyote aliyewahi kuishi hapa duniani.
Hii ni moja ya njia ambayo utayatambua mafundisho ya kweli ya Bwana..
Maran atha.
Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema,
Kwa maombezi/Ratiba za ibada/ Ushauri/ Maswali.
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312
pia kama utapenda uyapate mafundisho haya kwa njia ya Whatsapp au email basi tutumie ujumbe kwenye namba hizo hizo.
Mada Nyinginezo:
Nini maana ya mhubiri 9:11? si wenye mbio washindao katika michezo?
SWALI: Shalom wana wa Mungu Naomba msaada kuelewa andiko hili;
Mhubiri 9:11 “Nikarudi, na kuona chini ya jua, ya kwamba si wenye mbio washindao katika michezo, wala si walio hodari washindao vitani, wala si wenye hekima wapatao chakula, wala si watu wa ufahamu wapatao mali, wala wenye ustadi wapatao upendeleo; lakini wakati na bahati huwapata wote”.
JIBU: Ukisoma utaona Sulemani anasema, nikarudi na kuona chini ya jua, ikiwa na maana kuwa ni jambo ambalo amekuwa akiliona likitokea mara kwa mara duniani, hivyo akaona aandike, pengine na sisi tukilichunguza tunaweza kuliona, au pengine tulishawahi kuliona sehemu fulani.
Kwamba si wote wenye mbio, au ujuzi, au maarifa, au nguvu, ustadi au hekima mara zote zinawasaidia kupata mafanikio makubwa kuliko wale wengine wasiokuwa navyo. Na ndio maana hapo mwishoni mhubiri anamalizia kusema “lakini wakati na bahati huwapata wote”..Ikiwa na maana majira hubadilika, leo elimu yako inaweza ikawa na faida ikakuletea mfanikio mengin lakini kesho, isiwe na maana sana, lakini yule mwingine ambaye hakuwa na elimu mambo yakambadilikia pengine kwa ujuzi wake tu wa kuzaliwa aliokuwa nao ukamfanya apate fursa nyingi kuliko wewe, na matokeo yake akawa juu yako.
Na ndio maana tunapaswa tujue majira hayo yanayobadilika yapo mikononi mwa Mungu, Bahati hizo anazitoa Mungu mwenyewe na sio mwanadamu.. Paulo alisema..
Warumi 9:16 “Basi, kama ni hivyo, si katika uwezo wa yule atakaye, wala wa yule apigaye mbio; bali wa yule arehemuye, yaani, Mungu”.
Vivyo hivyo na sisi, kwa kuwa hatujui ni majira gani yapo mbele yetu, basi tujifunze kuwa wanyenyekevu chini ya Mungu atoaye mema yote, bila kuwadharau wengine, haijalishi tutakuwa na maarifa mengi kiasi gani kuwazidi wao, au elimu kubwa kiasi gani, au nguvu hatupaswi kujiona tumefika, vinginevyo, neno hili linaweza kutimia mbele ya macho yetu kwa wale tunaowadharau.
1Petro 5:6 “Basi nyenyekeeni chini ya mkono wa Mungu ulio hodari, ili awakweze kwa wakati wake”;
Bwana akubariki.
Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema,
Kwa maombezi/Ratiba za ibada/ Ushauri/ Maswali.
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312
Jiunge na kundi letu la mafundisho ya Biblia whatsapp kwa kubofya hapa > Group-whatsapp
Mada Nyinginezo: