JE UNAYAFANYA MAPENZI YA MUNGU?

JE UNAYAFANYA MAPENZI YA MUNGU?

Wewe kama mtumishi wa Mungu, je! unayafanya mapenzi ya Bwana Yesu?.

Ni muhimu kuyafahamu mapenzi ya Bwana Yesu na kuyatenda hayo ili umpendeze Mungu.

Sasa Mapenzi ya Bwana Yesu ni yapi?.

Tusome,

Yohana 6:37 “Wote anipao Baba watakuja kwangu; wala ye yote ajaye kwangu sitamtupa nje kamwe.

38 Kwa kuwa mimi sikushuka kutoka mbinguni ili niyafanye mapenzi yangu, bali mapenzi yake aliyenipeleka.

39 Na mapenzi yake aliyenipeleka ni haya, YA KWAMBA KATIKA WOTE ALIONIPA NISIMPOTEZE HATA MMOJA, BALI NIMFUFUE SIKU YA MWISHO.

40 Kwa kuwa mapenzi yake Baba yangu ni haya, ya kwamba KILA AMTAZAMAYE MWANA NA KUMWAMINI YEYE, AWE NA UZIMA WA MILELE; NAMI NITAMFUFUA SIKU YA MWISHO”

Hayo ndio mapenzi ya Mungu, kwamba “wote waliokuja kwa Yesu wasipotee hata mmoja” na pia “kila atakayemtazama Yesu na kumwamini apate uzima wa milele”..

Maana yake ni kwamba, mtumishi yeyote wa Mungu ili kuyatenda mapenzi kamili ya Mungu, hana budi KUISHI KATIKA HAYO MAONO MAWILI ;

1) kuhakikisha kwamba “anawafanya watu wamtazame Yesu, na kumwamini ili wapate uzima wa milele” na

2) kuhakikisha kwamba “wote waliomfuata Yesu, hapotei hata mmoja”.

Hayo ndio maono makuu mawili Bwana Yesu aliyotembea nayo, hata akashuhudiwa na Baba kuwa amempendeza yeye.

Ukitaka kumpendeza Yesu kikamilifu, hakikisha unawafanya watu wamtazame Yesu na kumwamini. Biblia inasema kuna furaha mbinguni, mtu mmoja atubupo, malaika wanashangilia na kuruka ruka. Hivyo ili tuifurahishe mbingu hatuna budi kuwafanya wengi wamwamini Yesu, kwa kadri tuwezavyo.

Na haishii hapo tu!, kuwageuza wamwache Yesu na kisha kuwaacha!.. Ili kuyakamilisha mapenzi ya Mungu, hatuna budi kuhakikisha kwamba Wote waliomfuata Yesu (yaani waliomwamini), hapotei hata mmoja. Maana yake kuwachunga! Na kuwalea na kuhakikisha sisi hatuwi sababu ya wao kurudi nyuma au kuanguka..(Kwa ufupi, tunakuwa tunawafanya wazidi kudumu katika wokovu).

Yohana 15:16 “Si ninyi mlionichagua mimi, bali ni mimi niliyewachagua ninyi; nami nikawaweka mwende mkazae matunda; NA MATUNDA YENU YAPATE KUKAA; ili kwamba lo lote mmwombalo Baba kwa jina langu awapeni”.

Hapo anasema “amesema ametuweka tukazae matunda” na “matunda hayo yapate kukaa”…Umeona hajaishia kusema tu!, mkazae matunda halafu basi!…hapana!..bali pia matunda hayo tutakayoyazaa yapate kukaa! Yaani yadumu kwa muda mrefu. Sio la leo na kesho, bali lidumu muda mrefu.

Bwana Yesu kuna wakati alimwuliza Petro kama anampenda..akamwambia..

Yohana 21:15 “Basi walipokwisha kula, Yesu akamwambia Simoni Petro, Je! Simoni wa Yohana, wewe wanipenda kuliko hawa? Akamwambia , Naam ,Bwana, wewe wajua kuwa nakupenda. Akamwambia, LISHA WANA-KONDOO WANGU.

16 Akamwambia tena mara ya pili, Simoni wa Yohana, wanipenda? Akamwambia, Ndiyo, Bwana, wewe wajua kuwa nakupenda. Akamwambia, CHUNGA KONDOO ZANGU.

17 Akamwambia mara ya tatu, Simoni wa Yohana, wanipenda? Petro alihuzunika kwa vile alivyomwambia mara ya tatu, Wanipenda? Akamwambia, Bwana, wewe wajua yote; wewe umetambua ya kuwa nakupenda. Yesu akamwambia, LISHA KONDOO ZANGU”.

Umeona hapo Bwana anamwambia vitu viwili LISHA, na CHUNGA. Hajamwambia tu alishe, bali pia achunge.. Na sisi tuna wajibu sio tu wa kulisha, bali pia kuchunga!. Tunachunga watu wasirudi nyuma, (hapo tutayafanya matunda yetu yakae), na ndio tutayafanya mapenzi ya Mungu.

Matendo 15:36 “Baada ya siku kadha wa kadha Paulo akamwambia Barnaba, Haya! Mrejee sasa tukawaangalie hao ndugu katika kila mji tulipolihubiri neno la Bwana, wa hali gani………………..

40 Lakini Paulo akamchagua Sila, akaondoka, akiombewa na wale ndugu apewe neema ya Bwana.

41 AKAPITA KATIKA SHAMU NA KILIKIA AKIYATHIBITISHA MAKANISA”.

Je na wewe unayatenda mapenzi ya Mungu?..Unawavuta watu kwa Yesu?, je unawafanya wadumu katika Imani?. Kama unafanya hayo, basi jua unafanya jambo jema sana na kuu.

Yohana 4:34 “Yesu akawaambia, Chakula changu ndicho hiki, niyatende mapenzi yake aliyenipeleka, nikaimalize kazi yake.

35 Hamsemi ninyi, Bado miezi minne, ndipo yaja mavuno? Tazama, mimi nawaambieni, Inueni macho yenu myatazame mashamba, ya kuwa yamekwisha kuwa meupe, tayari kwa mavuno”.

Bwana atusaidie tuyafanye mapenzi yake.

Maran atha!

Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema,

Kwa maombezi/Ratiba za ibada/ Ushauri/ Maswali.
Piga namba hizi:+255693036618/ +255789001312

pia kama utapenda uyapate mafundisho haya kwa njia ya Whatsapp au email basi tutumie ujumbe kwenye namba hizo hizo.


Mada Nyinginezo:

SI KWA UWEZA WALA KWA NGUVU BALI KWA ROHO YANGU, ASEMA BWANA.

USIPOTEZWE NA MANENO YA MANABII WA UONGO.

UFUNUO: Mlango wa 22

TUMAINI NI NINI?

HATARI YA KUTOKUITAFAKARI BIBLIA VIZURI?

Rudi nyumbani

Print this post

About the author

Admin administrator

Subscribe
Notify of
guest
1 Comment
Newest
Oldest Most Voted
Inline Feedbacks
View all comments
Anonymous
Anonymous
1 year ago

Leave your messagenaomba somo la mapenzi ya Mungu