LOLOTE ATAKALOWAAMBIA FANYENI.

LOLOTE ATAKALOWAAMBIA FANYENI.

Jina la Bwana wetu Yesu Kristo, libarikiwe daima. Nakukaribisha katika kuyatafakari maneno mazuri ya Bwana wetu.

Kama tukisoma kitabu cha Yohana, sura ile ya pili tunaona, habari ile ya Yesu kualikwa katika harusi huko kana ya Galilaya, Na mamaye Yesu alikuwa ni mmoja wa wanakamati wa harusi ile..Lakini kwa bahati mbaya kama tunavyosoma habari divai iliwaishia katikati kabla hata ya sherehe kuishi.

Pengine lile lingekuwa ni aibu kwa wana-kamati, kwanini hawakulifikiria hilo kuwa divai inaweza kuwa chache na hivyo wangepaswa wanunue nyingi Zaidi kwa dharura kama hizo, lakini Mariamu, alikumbuka kuwa yupo mtenda miujiza katikati ya watu..Ndipo akamfuata na kumweleza tatizo hilo, lakini Yesu aliposikia akamwambia mama yake ‘wakati wake haujafika’, Mamaye hakukata tamaa kuambiwa vile Zaidi ya yote aliwapa maagizo wale watenda kazi wa kwenye sherehe na kuwaambia…

Yohana 2:5 “…Lolote atakalowaambia, fanyeni…”

Tujiulize ni kwanini aliwaambia vile “Lolote atakalowaambia, fanyeni” au kwa lugha nyepesi alimaanisha kuwaambia “chochote atakachowaelekeza kufanya mtiini bila kushuku shuku”..

Kumbuka Mariamu alikuwa na Bwana Yesu tangu akiwa mtoto, na hivyo alikuwa anajua tabia yake vizuri ni mtu wa namna gani. Pengine wakati fulani huko nyuma kulishawahi kutokea matatizo fulani yanayofanana na haya, Na Yesu akawashauri wafanye kitu fulani wakakipuuzia, na baadaye wanalipopata hasara na kugundua kuwa uamuzi wa YESU wa mwanzoni ndio ulikuwa bora, wakajuta kwanini hawakumskiliza.

Au pengine walitaka kufanya jambo fulani la kimaaendeleo, labda tuchukulie mfano tu, walikuwa wanataka kutanua biashara yao ya useremala, hivyo wakaamua kwenda kutafuta eneo zuri Zaidi la mjini ambapo pana watu wengi na wanunuzi wengi..

lakini Yesu akawashauri na kuwaambia msiende mjini bali rudini nendeni katika kijiji fulani mkanunue shamba kule, na muifanye kazi hiyo pale..Pengine mawazo yake yalionekana kuwa hafifu ya mtu asiyekuwa na tageti, mtu aende kijijini atapata wapi wateja wazuri wa kununua fanicha zao..Lakini pengine baada ya miezi mitatu wakasikia serikali ya Pilato, imeteua makazi mapya, na Kijiji hicho ndicho kimeonekana kuwa ni kizuri kwa makao hayo ya watu na uwekezaji, hivyo amri imetolewa Rumi na kaisari kwamba wale wajenzi wanaoishi maeneo yale yale ndio wapewe tenda ya muda mrefu ya ku-sambazavifaa vyote vya ujenzi pamoja na fanicha za ndani..

Lakini wao sasa wameshakwenda mjini, hawawezi kurudi tena kule,.Na baadaye wanagudua kuwa mawazo ya YESU yalikuwa bora Zaidi kuliko ya kwao, wangemsikiliza tu, japo mwanzoni yalioonekana kama ya kipuuzi.. (Sasa Huo ni mfano tu!).

Sasa matukio kama hayo, au tofauti na hayo lakini yenye maudhui hayo hayo walikutana nayo sana wakina Mariamu mpaka ikafikia wakati wakaamua sasa wawe wanamsikiliza yeye tu ushauri wake na kuufanya hata kama utaonekana unaenda kinyume na hali halisi ya mazingira.. walikuwa wanatii tu. kwasababu walikuwa wanajua Kristo alijaa hekimu ya ki-Mungu ndani yake, na kila alilolifanya lilifanikiwa..

Sasa tukirudi kwenye sherehe hii tunaona matatizo kama yaleyale ya nyuma yanajitokeza tena, Kama kawaida Mariamu anamfuata tena Yesu na kumwambia Divai imetuishia tufanye nini?…Lakini Yesu anamwambia Mariamu wakati wangu haujafika..akimaanisha wakati wake wa kuanza kutenda miujiza haujafika..Lakini Mariamu akawaambia wale watumishi..

“watumishi, Lolote atakalowaambia, fanyeni..”

Msipuuzie atakalowaambia, mnaweza kuliona halina maana machoni penu, lakini anajua kitu gani anachokisema…Anaweza akawapa maagizo ya ajabu ajabu tu lakini mtiini fanyeni atakachowaambia ili mfanikiwe..Na kweli walipokwenda kwa Yesu, wakakutana na jambo kama vile la kipuuzi kweli…

waliambiwa wachukue mabalasi wakayajaze maji na kisha wampelekee mkuu wa meza..Kumbuka hayo mabalasi biblia inatuambia yalikuwa yanatumika kwa kutawadhia..Embu fikiria pipa la kutawadhia unaambiwa ukalijaze maji halafu uyachote upeleke mezani kwenye harusi…ni kama uendawazimu hivi..

Yohana 2:6 “Basi kulikuwako huko mabalasi sita ya mawe, nayo yamewekwa huko kwa desturi ya Wayahudi ya kutawadha, kila moja lapata kadiri ya nzio mbili tatu.

7 Yesu akawaambia, Jalizeni mabalasi maji. Nao wakayajaliza hata juu.

8 Akawaambia, Sasa tekeni, mkampelekee mkuu wa meza. Wakapeleka”

Basi wale watu wakafanya hivyo, si rahisi kuyatii maagizo kama hayo, ikiwa hujamjua vizuri mtu anayekuambia ufanye hivyo..

Yohana 2:9 “Naye mkuu wa meza alipoyaonja yale maji yaliyopata kuwa divai, (wala asijue ilikotoka, lakini watumishi walijua, wale walioyateka yale maji), yule mkuu wa meza alimwita bwana arusi,

10 akamwambia, Kila mtu kwanza huandaa divai iliyo njema; hata watu wakiisha kunywa sana ndipo huleta iliyo dhaifu; wewe umeiweka divai iliyo njema hata sasa”.

Unaona mwisho wa siku walipata divai iliyo bora kuliko hata ile ya kwao. Lakini kwa kutii tu maagizo ya Yesu.

Desturi hiyo hiyo Kristo aliendelea kuwa nayo..utakumbuka wakati fulani aliwaambia wayahudi na wale wanafunzi wake waliokuwa wanafuatana naye, kwamba mtu yeyote asipoula mwili wake na kuinywa damu yake hana uzima wowote ndani yake..

Yohana 6:53 “Basi Yesu akawaambia, Amin, amin, nawaambieni, Msipoula mwili wake Mwana wa Adamu na kuinywa damu yake, hamna uzima ndani yenu.

54 Aulaye mwili wangu na kuinywa damu yangu anao uzima wa milele; nami nitamfufua siku ya mwisho.

55 Kwa maana mwili wangu ni chakula cha kweli, na damu yangu ni kinywaji cha kweli.

56 Aulaye mwili wangu na kuinywa damu yangu hukaa ndani yangu, nami hukaa ndani yake”.

Lakini wengi waliposikia maneno yale, jinsi tu yasivyo eleweka-eleweka wengine wakayapuuzia, na wengine kuanzia siku hiyo hiyo wakaacha kufuatana naye, wakamwona kama huyu ni mchawi fulani hivi..anataka kuleta elimu yake ya uchawi..Lakini hawakujua kuwa alikuwa anazungumzia habari za uzima wao.

Hata sisi pamoja na maagizo mengi aliyotuachia ya namna ya kupokea Baraka Fulani.. Bwana alituachia Agizo moja la MUHIMU SANA la kufuata mara tu tunapoamini na kuchukua misalaba yetu na kumfuata. Alisema mtu yeyote akishaamini, hatua inayofuata ni lazima akabatizwe.

Luka 16:16 “Aaminiye na kubatizwa ataokoka; asiyeamini, atahukumiwa..”

Lakini wengi wanayapuuzia maagizo haya, na kusema aah! Hakuna jambo kama hilo ubatizo sio muhimu, kinachookoa ni damu ya Yesu na sio maji..Lakini nataka nikuambia ubatizo unaweza usiwe na maana sana kwako lakini unamaana sana kwa Yesu aliyekuagiza ufanye hivyo.

“Lolote atakalowaambia, fanyeni..” Maji ndani ya vyombo vya kutawadhia, yaligeuka divai juu ya meza za harusi…Maji unayoyakataa leo kwa ubatizo wako ndio Bwana anayoyaagiza kwa ajili ya ondoleo la dhambi zako.

Unayakiuka maagizo ya Mungu, halafu bado unatazamia dhambi zako ziondolewe, utakuwa unajidanganya!..Hata daktari akikupa dawa halafu ukaacha kuzitumia hadi mwisho kwa kisingizio kuwa umeshaanza kujisikia nafuu, siku itafika ugonjwa utakurudia na hali yako itakuwa ni mbaya ziadi kuliko ilivyokuwa pale mwanzo…Vivyo hivyo ubatizo kwa mtu anayeamini ni jambo lisiloweza kuepukika, Na ubatizo Yesu aliouagiza ni ule wa kuzamishwa katika maji tele (Yohana 3:23) kwa jina la YESU KRISTO. Sawasawa na (Matendo 2:38)..Ubatizo mwingine tofauti na huo ni batili!.

Vilevile Bwana aliagiza tushiri meza yake. Hivyo Kama wakristo ni muhimu kufanya hivyo, tusipofanya hivyo kama yeye alivyosema “hatuna uzima ndani yetu”..Ni kweli tutakuwa hatuna uzima ndani yetu..Kwani kitendo kile cha kushiriki divai na mkate, tunakuwa tunaitangaza mauti yake mpaka ajapo.

Vilevile alitoa maagizo mengine ya mwisho ambayo ni muhimu sana..Nayo ni kutawadhani miguu watakatifu..Hili linapuuziwa lakini ukweli usiopingika watakatifu ni sharti tulitimize agizo hili nalo..Alisema..

Yohana 13:12 “Basi alipokwisha kuwatawadha miguu, na kuyatwaa mavazi yake, na kuketi tena, akawaambia, Je! Mmeelewa na hayo niliyowatendea?

13 Ninyi mwaniita, Mwalimu, na, Bwana; nanyi mwanena vema, maana ndivyo nilivyo.

14 Basi ikiwa mimi, niliye Bwana na Mwalimu, nimewatawadha miguu, imewapasa vivyo kutawadhana miguu ninyi kwa ninyi.

15 Kwa kuwa nimewapa kielelezo; ili kama mimi nilivyowatendea, nanyi mtende vivyo.

16 Amin, amin, nawaambia ninyi, Mtumwa si mkuu kuliko bwana wake; wala mtume si mkuu kuliko yeye aliyempeleka.

17 Mkiyajua hayo, heri ninyi mkiyatenda”.

Hivyo kama ulikuwa hujafanya mojawapo ya hayo matatu yaani (KUBATIZWA, KUSHIRIKI MEZA YA BWANA, na KUTAWAZANA MIGUU )..ni vizuri ukaanza kufanya hivyo sasa.

Wengi waliyapuuzia maagizo ya Yesu lakini baadaye walikuja kuona umuhimu wake, wakati ambao wameshachelewa. Na wewe usije ukaukosa uzima kwa kuzembea maagizo ya Bwana wetu YESU KRISTO, mshauri wa ajabu.

“Lolote atakalowaambia, fanyeni..”

Ubarikiwe sana.

Mada Nyinginezo:

MTUMAINIE YESU ASIYEISHA MATUKIO.

BASI MUNGU AKAMUADHIMISHA SANA..

UMUHIMU WA YESU KWETU.

KAMA MHUBIRI NI WOKOVU UPI UNAUPELEKA KWA WATU?

KRISIMASI (CHRISTMAS) NI NINI? JE IPO KATIKA BIBLIA?

JIEPUSHE NA MASHINDANO YA DINI.

KWANINI YESU ALIMUITA BABA YAKE “ABA”?

Rudi Nyumbani:

Print this post

About the author

Admin administrator

Subscribe
Notify of
guest
0 Comments
Inline Feedbacks
View all comments