WAKATI AHADI INAPOKARIBIA, HUWA KUNA MAMBO YANATOKEA.

WAKATI AHADI INAPOKARIBIA, HUWA KUNA MAMBO YANATOKEA.

Shalom, nakusalimu katika jina lipitalo majina yote la Bwana wa mabwana na Mfalme wa wafalme YESU KRISTO, Mungu mkuu, Sifa na heshima, na utukufu ni vya kwake milele. Yeye ndiye mwokozi wetu, na huo ndio ukweli pekee uliodumu na utakaodumu duniani kwa wakati wote.

Tukisoma kile kitabu cha Matendo ya mitume 7:17 inasema..

 “17 Basi wakati wa ile ahadi ambayo Mungu alimpa Ibrahimu ulipokuwa unakaribia, wale watu wakazidi na kuongezeka sana huko Misri,

18 hata mfalme mwingine akainuka juu ya Misri, asiyemfahamu Yusufu.

19 Huyo akawafanyia hila kabila yetu, na kuwatenda mabaya baba zetu, akiwaamuru wawatupe watoto wao wachanga, ili wasiishi”.

Lipo jambo moja tunaweza kulitazama leo hii, biblia inatuambia wakati ile ahadi Mungu aliyomuahidia Ibrahimu kuwa siku moja uzao wake, utakwenda kuirithi nchi ya Kaanani aliyomuahidia, ulipokaribia, biblia inasema, kuna tukio lilifuata baada ya pale, na tukio lenyewe ni wana wa Israeli kuongezeka kwa kasi sana kule Misri.

Jambo ambalo liliwashtusha wamisri waseme ni nini kimewapata hawa watu mpaka wanazaliana kwa spidi kasi hivi, yaani pengine ndani ya miaka kumi tu , idadi imejizidisha mara 3 ukilishangisha na miaka mingine yote iliyopita huko nyuma, miaka mitatu tena mingine vivyo hivyo. Hilo liliwashtusha sana wamisri mpaka kuona tunazidiwa sasa tubuni njia mbadala..

Kutoka 1:7 “NA WANA WA ISRAELI WALIKUWA NA UZAZI SANA, NA KUONGEZEKA MNO, NA KUZIDI KUWA WENGI, nao wakaendelea na kuongezeka nguvu; na ile nchi ilikuwa imejawa na wao. 8 Basi akainuka mfalme mpya kutawala Misri, asiyemjua Yusufu.

9 Akawaambia watu wake, Angalieni, watu wa wana wa Israeli ni wengi tena wana nguvu kuliko sisi.

10 Haya! Na tuwatendee kwa akili, wasije wakaongezeka; tena, ikitokea vita, wao nao wasije wakashikamana na adui zetu na kupigana nasi, na kutoka katika nchi hii.

11 Basi wakaweka wasimamizi juu yao wawatese kwa mizigo yao. Nao wakamjengea Farao miji ya kuwekea akiba, Pithomu na Ramesesi.

12 LAKINI KWA KADIRI YA WALIVYOWATESA NDIVYO WALIVYOONGEZEKA NA KUZIDI KUENEA. Nao walichukiwa kwa sababu ya wana wa Israeli”.

Umeona? Lakini biblia inatuambia kuongezeka kwao, hakukuwa bure tu bali kulikuwa na sababu, na sababu yenyewe ni kuwa ILE AHADI YA MUNGU ilikuwa inakaribia kwenda kutimizwa juu yao.

Nachotaka uone ni kuwa, sikuzote, ahadi ya Mungu inapokaribia kutimizwa, Mungu huwa anahimiza mambo fulani fulani yafanyike haraka sana ndani ya kipindi kifupi sana kisichoweza kudhaniwa. Wana wa Israeli pengine walikaa zaidi ya miaka 300, kule Misri na uongezekaji wao ulikuwa wa wastani tu, au wa kawaida sana, lakini walipokaribia karibia miaka 400 hapo, ndipo idadi ya watu ikaongezeka kwa ghafla sana.

Jambo hili linafunua nini  kwa agano jipya?

Wengi wetu hatuijui vizuri historia ya ulimwengu, tunadhani mambo yalivyo sasahivi ndivyo yalivyokuwa miaka ya nyuma. Ndugu,fahamu karne ya 20 na ya 21, ndizo karne pekee ambazo zinawashangaza watu wengi sana ulimwenguni hususani wale wanaofuatilia habari za historia, tukisema karne ya 20 tunamanisha kuanzia mwaka wa 1901.

Mambo mengi sana yametimia yaliyokuwa yanazungumziwa na Bwana Yesu, pengine yalionekana kama ni uongo kwasababu hayakuwahi kutimia kwenye miaka yote ya huko nyuma. Lakini ilipotimia karne ya 20 yakaanza kuonekana, Jambo mojawapo ni kuchipuka tena kwa taifa la Israeli, ambalo linafananishwa na mtini. Pili, kutokea kwa vita vya dunia viwili, kulipuka kwa magonjwa yasiyohesabika, na yasiyotibika, hata mafua unayofahamu wewe, hayakuwepo miaka ya 1800,  zote hizo zilizungumziwa katika Mathayo 24, Marko 13 na Luka 21

Na mbaya zaidi, kulipuka kwa wimbi la manabii wengi wa uongo duniani. Hili tumelishuhudia sana sana kwenye hii karne yetu ya 21, kote huko nyuma hakukuwahi kuwa hata na mtu aliyejiita nabii, lakini leo hii ni kitu cha kawaida sana..

Mambo mengine ni Kuongezeka kwa maasi, watu kupenda anasa kuliko kumpenda Mungu, kuongezeka kwa teknolojia, smartphones, n..k ambapo kunatimiza ule unabii wa Danieli unaosema maarifa yataongezea(Danieli 12:4)…

Hayo yote ni kwasababu ile ahadi ya Mungu ya kulinyakuwa kanisa lake inakaribia kutokea hivi karibuni, kwahiyo Mungu anazidisha spidi ya mambo yote yatokee haraka haraka. Na mambo yote yakishatimia ghafla, atatokea Kristo na kulinyakua kanisa lake.

Ni kitendo cha kufumba na kufumbua, hutaona mtu. Tupo ukingoni mwa wakati, Mungu anahimiza mambo yake haraka haraka sasa hivi, Si wakati wa kuwa kama mke wa Lutu, mguu mmoja nje, mwingine ndani, ni wakati wa kumfuata Yesu wewe, kama wewe.

Luka 17:32 “Mkumbukeni mkewe Lutu.

33 Mtu ye yote atakaye kuiponya nafsi yake, ataiangamiza; na ye yote atakayeiangamiza ataiponya.

34 Nawaambia, usiku huo watu wawili watakuwa katika kitanda kimoja; mmoja atatwaliwa, mmoja ataachwa.

35 Wanawake wawili watakuwa wakisaga pamoja; mmoja atatwaliwa, mmoja ataachwa.

36 Watu wawili watakuwa shambani, mmoja atatwaliwa, mmoja ataachwa.]”

Swali ni Je, umezaliwa mara ya pili, Je, wewe bado ni rafiki wa dunia? Je bado unaishi maisha ya kuwapendeza marafiki na wazazi? Mkumbuke mke wa Lutu.

Maran Atha.

Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema, na pia kama utapenda tuwe tunakutumia mafundisho ya Neno la Mungu ya mara kwa mara kwa njia ya email yako au Whatsapp basi tutumie ujumbe kwenye namba hii +255693036618 au +255789001312

Mada Nyinginezo:

Ni vitu vipi hivyo viwili visivyoweza kubadilika? (Ebr 6:18)

Je ni wanyang’anyi wawili waliomtukana Bwana Yesu au mmoja?

Bwana Yesu alikufa akiwa na umri gani?

VIKAANGUKA MACHONI PAKE VITU KAMA MAGAMBA.

Rudi nyumbani

Print this post

About the author

Admin administrator

Subscribe
Notify of
guest
0 Comments
Inline Feedbacks
View all comments