NI NANI ALIYEKUPA MAMLAKA HII UYATENDE HAYA?

NI NANI ALIYEKUPA MAMLAKA HII UYATENDE HAYA?

Ulishawahi kujiuliza hoja ya msingi shetani aliyotumia kumshitakia Yesu mpaka kufanikiwa kumpeleka msalabani ilikuwa ni ipi?

Tukilifahamu hilo tutaelewa ni wapi ibilisi anapandaa ili kuwaletea dhiki wakristo katika siku za mwisho.

Ukisoma biblia utaona Wakati ule wayahudi wanatafuta sababu nyingi sana za kumshitaki Bwana Yesu lakini hawakuziona, mpaka dakika za mwisho mwisho wakatokea na hoja nyingine moja, ambayo ilikuwa na mashiko sana kwao..

Na hoja yenyewe ilikuwa ni katika lile HEKALU.

Mathayo 26:59 “Basi wakuu wa makuhani na baraza yote wakatafuta ushuhuda wa uongo juu ya Yesu, wapate kumwua;

60 wasiuone wangawa walitokea mashahidi wa uongo wengi.

61 Hata baadaye wawili wakatokea, wakasema, Huyu alisema, Naweza kulivunja hekalu la Mungu, na kulijenga kwa siku tatu.

Nataka ujifunze jambo moja, kulikuwa na kauli nyingi sana zenye makwazo ambazo wayahudi wangeweza kuzisimamia kumuulia Yesu, kwamfano alipowaita wao ni wa baba yao Ibilisi na sio Ibrahimu(Yohana 8:44). Kwa kauli kama hiyo kwamfano ingetosha tu kumfanya wamuue. Lakini sio hiyo ya  kusema “Bomoeni hili Hekalu nami nitalijenga ndani ya siku tatu…”

Ulishawahi kujiuliza, kwanini kauli hiyo ilipata nguvu?

Hilo ni jambo ambalo shetani alijaribu kulijenga tangu zamani za akina Zerubabeli katika ujenzi wa Hekalu, kama wewe ni msomaji wa biblia, utakumbuka kuwa kipindi wanalijenga Hekalu la pili, maadui zao (ambao hawakuwa wayahudi) waliomba waungane nao ili kulijenga hekalu la Mungu, lakini Zerubabeli na wenzake kwa ufunuo wa Roho, wakawakatalia, kwasababu walijua madhara yake yatakayokuja huko baadaye (Ezra 4:3)..

Lakini muda mrefu ulipopita mamia ya miaka, hekalu hilo lilichakaa, likawa kama limepitwa na wakati, kwa ujenzi wake. Hapo ndipo akatokea mtawala mmoja wa ki-Rumi aliyeitwa HERODE, Akaomba alikarabati hekalu lile,. Sasa wayahudi bila ya Kutaka kumuuliza Mungu, wakakurupuka wakamruhusu, hivyo Herode akaanza kulikarabati tena, akalijenga kwa fedha nyingi sana na kwa muundo wa kisasa.

Muda alioutumia kukarabati ulizidi hata muda uliotumika kujenga Hekalu lile, kwani Herode alitumia miaka 46 kulikarabati, (Soma Yohana 2:20 utaona), wakati wakina Zerubabeli walitumia miaka  isiyozidi 7. Na alifanikiwa kulipamba kweli kweli, mpaka wakati Fulani mitume wakaenda kumuonyesh Bwana uzuri wa jengo hilo jinsi lilivyopambwa vizuri.

Sasa kitendo kile kilikuwa na agenda ya ibilisi nyuma yake. Kwasababu alijua upo wakati Masihi atakuja, na ataingia katika hekalu lile na kuwafundisha watu sheria za Mungu, Hivyo akatumia nguvu zake nyingi sana kutafuta namna ya  kupalimiliki. Ndipo hapo akamwingia Herode, ambaye roho ya mpinga-Kristo ilikuwa nyuma yake, mtu ambaye alikuwa hana hata upendo na Mungu, na ndio maana wakati tu Kristo anazaliwa badala afurahie mwokozi kaja ulimwenguni, kinyume chake akatuma watu kwenda kumuangamiza, lakini cha ajabu ndio mtu huyo huyo aliyelikarabati Hekalu la Mungu.

Sasa kwasababu yeye ndiye aliyelitengeneza upya. Mamlaka yote ikahamia mikononi mwake kutoka kwa wayahudi, wayahudi wakawa hawana la kusema, hapo ndipo akaanzisha biashara kubwa kubwa sana , ndani ya hekalu, akalifanya pia kuwa kama eneo la kitalii, la watu kuja kushangaa uzuri wake.

Vilevile kukawekwa sheria kali, mtu yeyote akitaka kufanya jambo, au kuleta mfumo mpya ni lazima kwanza apokee kibali kutoka kwa HERODE, vinginevyo utaonekana kama ni muhalifu, na msaliti, ambaye anastahili adhabu ya kifo.

Kwahiyo, hakukuwa na mtu aliyeweza kufumbua kinywa chake, kukemea jambo lolote baya lililofanyika katika hekalu la Mungu takatifu, kwa hofu ya Herode na wayahudi. Hivyo hiyo ikaifanya  hali ikaendelea kuwa mbaya kupindukia hadi wakati Kristo anatokea dunia,

Ibilisi alijua kabisa, mwisho wa Siku Bwana Yesu, ni lazima aje aingie katika hekalu lake takatifu. Na kweli wakati ulifika akaingia, ndipo akasambaratisha  biashara zote, na shughuli zote zilizokuwa zinaendelea ndani ya Hekalu.

Wayahudi kuona vile, wakadhani maagizo hayo kapewa na Herode ndipo walipomuuliza…..

Luka 20:2 “wakamwambia, wakisema, Tuambie, unatenda mambo hayo kwa mamlaka gani? Tena, ni nani aliyekupa mamlaka hii?”

Na baada ya kugundua kuwa hakuyapokea Kwa Herode, hapo ndipo wakajua mtu huyu ni msaliti, na gaidi, anataka kutuletea harufu mbaya duniani, ili sisi tuonekane kama waasi, ni lazima tumuue.

Ndipo wakamshitakia kwa kitendo chake kile, na kauli ile.

Nachotaka tuone ni kwamba. Shetani anafahamu kuwa Kristo yupo mlangoni kurudi tena mara pili kulinyakua kanisa lake takatifu. Hivyo alichokifanya tangu kile kipindi cha mitume hadi sasa ni kujiingiza kwa siri , ili kujifanya kama analisaidia kanisa la Mungu..

Lakini lengo lake sio Kristo, na ndio maana utaona sasa, madhehebu mengi ya uongo, yamefanikiwa sana, lakini ukijaribu kuchunguza mifumo yao utaona ipo mbali sana na biblia.

Ukiuliza ibada za sanamu za kumwomba bikira Maria zipo wapi kwenye biblia, au kwenda toharani tunakupata wapi, utaishia kuonekana ni msaliti, na gaidi, msambaza, chuki. Shetani sikuzote hataki mfumo wake mbovu kuhojiwa.. Hataki kwasababu anajua pale sio mahali pake.

Leo hii, bado hajapokea nguvu kamili,za kuleta uharibifu kwa watu, wakati unafika atapokea nguvu ya kuleta mauaji kwa wale wakristo ambao UNYAKUO utakuwa umewapita. Atataka kuwaondosha wote asibakie mtu.

Je! Umeokoka ndugu yangu? Au bado unajisifia dini na madhehebu? Hautanyakuliwa kwa dhehebu lako zuri, utanyakuliwa kwa kukamilishwa katika wokovu, yaani kutubu na kubatizwa na kupokea Roho Mtakatifu, na kuishi katika utakatifu. Tubu leo kama hujatubu, Kumbuka wakati wowote Kristo anarudi.

Maran Atha.

Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema,

Kwa maombezi/Ratiba za ibada/ Ushauri/ Maswali.
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312

pia kama utapenda uyapate mafundisho haya kwa njia ya Whatsapp au email basi tutumie ujumbe kwenye namba hizo hizo.

Mada Nyinginezo:

Kikoto ni nini?(Yohana 2:15)

UFUNUO: Mlango wa 11

TUJIFUNZE JAMBO KWA WANAWAKE HAWA WAWILI:

UNYAKUO.

DHIKI KUU INAKUJA NA UNYAKUO UPO KARIBU.

Rudi nyumbani

Print this post

About the author

Admin administrator

Subscribe
Notify of
guest
0 Comments
Inline Feedbacks
View all comments