KWANINI TUNAOMBA KWA JINA LA YESU?

KWANINI TUNAOMBA KWA JINA LA YESU?

Ili kujua vizuri ni kwanini tunaomba kwa jina la Yesu. Tafakari kidogo mfano huu.

Jaribu kuwaza, mfano wewe ni mwekezaji halafu umeona shamba zuri mahali Fulani na unataka kwenda kuekeza kwa ukulima wa kisasa, Ukaanza kufuata taratibu zote za kupata eneo hilo, kuanzia ngazi ya kijiji mpaka almashauri, lakini ‘process’ imekuwa ngumu, mara unaambiwa kinahitajika hiki, mara kinahitajika kile, mara bado hujakidhi vigezo, n.k. Na umeendelea  kusubiria hivyo kwa miaka 2 sasa lakini bado hujapewa eneo hilo.

Lakini kwa bahati nzuri siku moja raisi, akiwa anapita, kuzungumza na wajasirimali, ukapata fursa, ya kumweleza shida zako, na raisi akatoa agizo saa hiyo hiyo na kusema ‘Mimi ninaagiza mtu huyu apewe shamba hilo’ Unadhani, itakuwa ni ngumu kama ulivyokuwa unahangaika wewe mwenyewe?

Kwa agizo tu hilo la raisi unakuwa na mamlaka hata ya kuwaharakisha wale wahusika wafanye haraka, nao watatii na kutimizi ndani ya ule wakati walioambiwa.

Ndivyo ilivyo kwa Yesu, utauliza ni kwanini tunaomba kwa jina la Yesu,. Ni kwasababu jina hili ndilo jina lililo kuu kuliko majina yote hapa Duniani, ni zaidi ya jina la raisi yeyote unayemjua, au mfalme yeyote, au Sultani yeyote aliyewahi kuishi hapa duniani. Hivyo unapolitumia jina hili agizo halitoki kama ombi, bali kama amri..

Biblia inasema..

Wafilipi 2:9 “Kwa hiyo tena Mungu alimwadhimisha mno, akamkirimia Jina lile lipitalo kila jina;

10 ili kwa jina la Yesu kila goti lipigwe, la vitu vya mbinguni, na vya duniani, na vya chini ya nchi;

11 na kila ulimi ukiri ya kuwa YESU KRISTO NI Bwana, kwa utukufu wa Mungu Baba”.

Hivyo popote pale unapopeleka maombi yako mbele za Mungu, ni lazima uende wa jina hilo la YESU KRISTO..Vinginevyo huwezi kukubaliwa na mbingu, kwa lolote lile unaloliaomba.

Unaposhindana na nguvu za giza, ni lazima uziamrishe kwa jina hili la YESU KRISTO, Vinginevyo, utaumia wewe mwenyewe..

Na ndio maana biblia imetuambia jambo lolote liwe tulifanyalo kwa Neno au kwa tendo tufanye katika jina hili, kwa faida yetu wenyewe na kwa usalama wetu.

Wakolosai 3:17 “Na kila mfanyalo, kwa neno au kwa tendo, fanyeni yote katika jina la Bwana Yesu, mkimshukuru Mungu Baba kwa yeye”.

Vilevile unapookoka, ni sharti ulikiri hili jina kuwa ndio jina pekee linalookoa, Maana ndio tafsiri ya jina lake (YESU-YEHOVA ANAOKOA)

Vivyo hivyo tunapokwenda kubatizwa baada ya kumpokea kwetu Kristo, ni lazima tubatizwe kwa jina hili na sio lingine.

Matendo 2:37 “Walipoyasikia haya wakachomwa mioyo yao, wakamwambia Petro na mitume wengine, Tutendeje, ndugu zetu?

38 Petro akawaambia, Tubuni mkabatizwe kila mmoja kwa jina lake Yesu Kristo, mpate ondoleo la dhambi zenu, nanyi mtapokea kipawa cha Roho Mtakatifu”.

Soma tena (Matendo 8:16, 10:48, 19:5)

Ukizingatia yote hayo, basi rohoni unaonekana umepigwa chapa zake, kiasi kwamba laana yoyote haiwezi kukupata, wala nguvu za giza kukushinda….

Wagalatia 6:17 “Tangu sasa mtu asinitaabishe; kwa maana ninachukua mwilini mwangu chapa zake Yesu”.

Na wewe je! jina hili lina nguvu yoyote ndani yako?. Usidhani ni kulitamka tu, halafu basi, shetani ndio atakuogopa, hilo wazo liondoe, wapo watu waliojaribu kufanya hivyo katika biblia na huku maisha yao yapo mbali na wokovu, kilichowakuta hadi leo habari yao tunaisoma..

Matendo 19:13 “Baadhi ya Wayahudi wenye kutanga-tanga, nao ni wapunga pepo, wakajaribu kutaja jina la Bwana Yesu juu yao waliopagawa na pepo wachafu, wakisema, Nawaapisha kwa Yesu, yule anayehubiriwa na Paulo.

14 Walikuwako wana saba wa mtu mmoja Skewa, Myahudi, kuhani mkuu, waliofanya hivyo.

15 Yule pepo mchafu akawajibu, akawaambia, Yesu namjua na Paulo namfahamu, lakini ninyi ni nani?

16 Na yule mtu aliyepagawa na pepo mchafu akawarukia wawili, akawaweza, akawashinda, hata wakatoka mbio katika nyumba ile hali wa uchi na kujeruhiwa.

17 Habari hii ikajulikana na Wayahudi wote na Wayunani waliokaa Efeso, hofu ikawaingia wote, na jina la Bwana Yesu likatukuzwa”.

Unaona hapo ili jina la YESU liwe na nguvu ni sharti umpokee yeye kwanza, na ukishampokea ndipo unapokuwa na mamlaka ya kulitumia jina hilo kuwasilisha mahitaji yako kwa Mungu, vilevile kuziamrisha nguvu za giza, na kufungua kifungo vyote vya laana vilivyokufunga katika maisha yako.

Hivyo kama upo tayari leo kumruhusu Yesu Kristo aingie maishani wako, basi, fungua hapa kwa ajili ya kuongozwa sala ya toba.>>>> KUONGOZWA SALA YA TOBA

Ikiwa umefuatisha sala hiyo kwa imani, basi kuanzia sasa ni vizuri ukaanza kujifunza mafundisho mengine ya rohoni kukusaidia kukua kiroho..Pakua tovuti hii, kwani yapo masomo zaidi ya 1000, na majibu ya maswali mengi yaliyojibiwa, ambayo ukiyasoma maisha yako ya rohoni hayatabaki kama yalivyokuwa.

Au yakufikie kwa njia ya Whatasapp: +255789001312

Lakini kwasasa anzana na haya tuliyoyaorodhesha chini hapa..

Mada Nyinginezo:

BASI MUNGU AKAMUADHIMISHA SANA..

JINA LA MUNGU NI LIPI?

WEWE U MWALIMU WA ISRAELI,NA MAMBO HAYA HUYAFAHAMU?

UMUHIMU WA KUZALIWA MARA YA PILI.

KWA KUPIGWA KWAKE SISI TUMEPONA.

JINSI MUNGU ANAVYOIPIGA NA KUIPONYA AFRIKA.

Rudi Nyumbani:

Print this post

About the author

Admin administrator

Subscribe
Notify of
guest
2 Comments
Newest
Oldest Most Voted
Inline Feedbacks
View all comments
Madgalena...
Madgalena...
2 years ago

Mnapatikana wapi watumishi