USHUJAA WA ROHONI HAUANGALII UZOEFU WAKO.

USHUJAA WA ROHONI HAUANGALII UZOEFU WAKO.

Nakusalimu katika jina kuu la Bwana wetu Yesu Kristo. Nakukaribisha tuyatafakari maneno ya uzima ya Bwana wetu.

Leo nataka tujifunze asili ya ushujaa wa rohoni, ambao wakati mwingine tunadhani mpaka tuwe na uzoefu ndio tuweze kufanya makuu kwa Mungu. Wakati Fulani Taifa la Israeli liliingia katika hali mbaya ya njaa isiyokuwa ya kawaida, mpaka kufikia hatua ya baadhi ya watu kuchinja watoto wao na kuwala (2Wafalme 6:28-29),  Na hiyo ilikuwa ni kwasababu ya kuzungukwa na maadui zao wenye nguvu kwa muda mrefu walioitwa washami. Hivyo wakashindwa kuingiza au kutoa chochote ndani ya mji kwa muda usiokuwa mchache.

Hivyo hali ikiwa mbaya sana, mfalme akafunga mji, hawajui cha kufanya, watu wamepaniki, wanakula vita visivyopaswa kulikwa, kiasi kwamba hata ‘mavi ya njiwa’ tu yalikuwa yanauzwa kama chakula. Tengeneza picha taifa kubwa kama hilo, linakumbwa na janga la njaa kali namna hiyo, hadi askari wake wazoefu wa vita, wanatetemeka na kujificha ndani ya mji, kwasababu walijua wakitoka tu ni kifo. Na ndicho maadui zao walichokuwa wanakisubiria kwao, aidha watoke wawaue, au wafe na njaa ndani. Hivyo hali ilikuwa ni ya kutisha sana. Lakini tunaona siku moja Nabii Elisha, akapewa unabii na Mungu, na kuambiwa kuwa chakula kitapatikana na kuuzwa kwa bei ya chini kiasi ambacho hakijawahi kuuzwa hapo kabla siku ya kesho yake, ni sawa ni uambiwe siku ya kesho, gunia la mahidi, linauzwa kwa  Tsh1, wakati unatambua kuwa halipungui wastani wa bei ya Tsh,70,000. Ndivyo ilivyokuwa kwa Israeli, Mungu alipompa Elisha unabii huo akaambiwa siku ya kesho yake, chakula kitauzwa kwa bei ile.

Sasa kulikuwa na wakoma wanne(4), waliokuwa nje ya mji, wakoma hawa walitengwa na taifa, kwasababu ilikuwa ni kuwa watu walioathirika na ugonjwa huu watengwe mbali na makazi ya watu  wao wasije kuleta maafa hayo ndani ya jamii, ni sawa na ugonjwa wa Ebola tunavyouona sasa, ndivyo ilivyokuwa ukoma kwa wakati ule.

Tengeneza picha watu hawa walikuwa ni wagonjwa, hawana wa kuwatazama, na zaidi sana wamekuwa dhaifu kwa njaa kali. Lakini tunaona walishauriana jambo kisha wakafanya maamuzi, ambao ndio ulikuwa ukombozi wa taifa la Israeli; Tusome hapo;

2Wafalme 7:1 Elisha akasema, Lisikieni neno la Bwana; Bwana asema hivi, Kesho panapo saa hii, kipimo cha unga mzuri kitauzwa kwa shekeli, na vipimo viwili vya shayiri kwa shekeli, langoni pa Samaria. 

2 Basi yule akida, ambaye mfalme alikuwa akitegemea mkono wake, akamjibu yule mtu wa Mungu, akasema, Tazama, kama Bwana angefanya madirisha mbinguni, je! Jambo hili lingewezekana? Akamwambia, Angalia, wewe utaliona kwa macho yako, lakini hutakula

3 Basi walikuwapo watu wanne wenye ukoma, penye lango la mji; wakasemezana, Mbona tunakaa hapa hata tufe? 

4 Tukisema, Tutaingia mjini, mjini mna njaa, nasi tutakufa humo; nasi tukikaa hapa, tutakufa vile vile. Haya! Twende tukaliendee jeshi la Washami; wakituhifadhi hai tutaishi; wakituua, tutakufa tu. 

5 Basi wakaondoka kabla ya mapambazuko, ili waende mpaka kituo cha Washami; na walipofika mwanzo wa kimo cha Washami, kumbe! Hapana mtu. 

6 Kwa maana Bwana alikuwa amewasikizisha Washami kishindo cha miendo ya magari, na kishindo cha farasi, kama kishindo cha jeshi kubwa; wakaambiana, Tazama, mfalme wa Israeli amewaajiri wafalme wa Wahiti, na wafalme wa Wamisri, waje wapigane nasi. 

7 Kwa hiyo wakaondoka, wakakimbia kungali giza bado, wakaziacha hema zao, na farasi zao, na punda zao, na kimo chao vile vile kama kilivyokuwa, wakakimbia wapate kujiponya nafsi zao. 

8 Basi wale wenye ukoma walipofika mwisho wa kituo, waliingia katika hema moja, wakala, na kunywa, wakachukua fedha, na dhahabu, na mavazi, wakaenda wakavificha; wakarudi, wakaingia katika hema ya pili, vile vile wakachukua vitu, wakaenda, wakavificha. 

9 Ndipo wakaambiana, Mambo haya tufanyayo si mema; leo ni siku ya habari njema, na sisi tunanyamaza; mkingoja hata kutakapopambazuka, madhara yatatupata; basi twende tukawaambie watu wa nyumba ya mfalme. 

10 Basi wakaenda, wakawaita mabawabu wa mji; wakawaambia, Tulifika kituo cha Washami, na tazama, hapana mtu ye yote huko, wala sauti ya mtu, ila farasi wamefungwa, na punda wamefungwa, na hema zao kama walivyoziacha. 

11 Na mabawabu wakaita wakawaambia watu wa nyumba ya mfalme.

Ni nini kimejificha hapa?

Siri nayotaka uone ambayo imejificha nyuma ya hawa wakoma wanne, ni kwamba, pindi tu walipoamua kufanya uamuzi, wa kujitoa muhanga kwa ajili ya maisha yao, na kuanza mwendo, kuelekea kambi ya maadui, kumbe kule kwenye kambi ya washami, wanasikia kama JESHI kubwa sana la maaskari linawafuata. Hivyo wakakimbia kwa kasi sana, na kuacha kila kitu nyuma. Lakini wale maaskari wa kiisraeli waliokuwa wazoefu wakati huo wamejifungua ndani ya mji hawadhubutu kuchukua hatua..

Watu waliokuwa dhaifu na wagonjwa, ndio waliowafukuza washami na kuleta ukombozi Israeli. Watu wanne tu, waligeuka kuwa jeshi la maaskari elfu rohoni.

Hiyo ni kutufundisha nini?

Na sisi pia pale tunapoamua kufanya jambo kwa ajili ya Mungu, bila kujali hali zetu au udhaifu wetu, tufahamu kuwa jeshi la shetani linaogopa na kutetemeka kushinda hata sisi tunavyoweza kudhani. Daudi alijijua kuwa yeye si mtu wa vita, hajazoea vita, hawezi kutumia upanga wala mkuki, lakini yeye ndiye aliyesimama, kinyume na Goliathi, na kulifuka jeshi lake lote.

Hivyo, hupaswi kujidharau, ikiwa umeokoka leo, au jana, usiseme mimi sina uzoefu, au sijui biblia vizuri, kama kushuhudia watu wenye dhambi ambao wengine wameshindwa, wewe nenda, usisubiri mpaka mchungaji wako afanye hivyo, hujui kuwa wakati huo ndio Mungu kakuchagua kuwa sababu ya ukombozi kwa wengine.

Hivyo, popote unapojiona hukidhi vigezo, fahamu kuwa rohoni ndio unakidhi. Unajiona hustahili, jua tu kwa Mungu unastahili, kuwa na imani, chukua hatua, usingoje ngoje. Tumia karama uliyopewa ndani yako kuujenga ufalme wa Mungu. Popote pale unapojiona unafaa, basi tumia nafasi hiyo kumtangaza Kristo kwa wengine. Na hakika rohoni shetani atatoweka kama jeshi la washami.

Bwana akubariki.

Shalom.

Je, umeokoka? Kama bado basi fungua hapa kwa ajili ya mwongozo huo wa kumwalika Yesu maishani mwako.

Tafadhali shea na wengine ujumbe huu;

Pia Kwa maombezi/ Ushauri/ Maswali/ Whatsapp:
Tuandikie katika BOXI la Maoni hapo chini au
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312

Mada Nyinginezo:

Hazina za gizani ni zipi? (Isaya 45:3).

MAHANAIMU (Jeshi la Mungu)!

Yerusalemu ni nini?

BWANA AWEZA KUKUPA ZAIDI SANA KULIKO HIZO.

YANAYOENDELEA SASA KATIKA MADHABAHU YA MUNGU ROHONI.

JINSI YA KUPIGANA MAOMBI YA VITA.

MAGONJWA YAKUPATAYO MARA KWA MARA.

Rudi nyumbani

Print this post

About the author

Admin administrator

Subscribe
Notify of
guest
2 Comments
Newest
Oldest Most Voted
Inline Feedbacks
View all comments
Micchael Paul
Micchael Paul
1 year ago

Amina somo zuri.Barikiwa sana