KUONGEZEKA KWA MAARIFA.

KUONGEZEKA KWA MAARIFA.

Habari ya uzima wako mtu wa Mungu, katika hizi siku za mwisho na za hatari kama bado upo nje ya wokovu jiulize sana, Na kama bado unaishi kwa kushikilia mapokeo ya kidini jifikirie mara mbili..Kwasababu biblia inatuambia dalili nyingine kubwa inayofungua ukarasa wa siku za mwisho ni Kuongezeka kwa maarifa.. Na maarifa ya kwanza biblia iliyomaanisha ni maarifa ya rohoni, lakini tunajua mambo ya mwilini sikuzote huwa yanafunua yale ya rohoni hivyo tunapoona maarifa yakiongezeka duniani kwa kasi basi tunajua kuwa ule wakati umeshawasili . Sehemu nyingine biblia inatuambia tujifunze katika ‘Maumbile, yaani vitu vya asili (NATURE)’ 1Wakorintho 11:14..

Ni wazi kuwa vitu tunavyoviona karibu vyote ulimwenguni kwa namna moja au nyingine vinatuhubiria injili pengine pasipo hata sisi kujua..Tunamwona Bwana Yesu alitumia mifano mingi ya asili kutufundisha sisi, kwamfano aliposema watafakarini ndege ni mfano wa maumbile ya asili, aliposema tena

“Kila mwonapo wingu likizuka pande za magharibi mara husema, Mvua inakuja; ikawa hivyo.

55 Na kila ivumapo kaskazi, husema, Kutakuwa na joto; na ndivyo ilivyo.

56 Enyi wanafiki, mwajua kuutambua uso wa nchi na mbingu; imekuwaje, basi, kuwa hamjui kutambua majira haya?”(Luka 12:54-56)

Unaona Yote hayo ni maumbile yakituhubiria injili..

Vivyo hivyo biblia pia inaposema Maarifa yataongezeka katika siku za mwisho, inamaanisha tunapaswa tujifunze katika hayo, kwasababu na rohoni ndivyo ilivyo.. tunasoma hilo katika

Danieli 12:4 “Lakini wewe, Ee Danieli, yafunge maneno haya, ukakitie muhuri kitabu, hata wakati wa mwisho; wengi wataenda mbio huko na huko, NA MAARIFA YATAONGEZEKA.”

Hakuna mtu asiyejua ulimwengu wa sasa ni ulimwengu wa ushindani, ili uweze kuishi au kufanikiwa ni lazima uwe na akili timamu vile vile uwe mshapu, na hiyo yote ni kwasababu teknolojia iliyopo sasa ndiyo inayotufanya tuwe watu wa namna hiyo..

Embu jaribu kutafakari, siku hizi unaweza kusoma tangazo kwenye gazeti, au internet, linasema linahitaji wafanyakazi Fulani watakaojaza nafasi za wafanyakazi Fulani walioachishwa kazi,..na linawahitaji ndani ya saa 5-7 wawe wameshafika eneo la shirika kwa ajili ya mahojiano na watakaokidhi vigezo wataanza kazi mara moja Eneo husika ni Daresalaam..

Ukijiangalia wewe upo Kigoma kwa wakati huo, na mwingine yupo Bukoba, na mwingine Afrika ya kusini…. Je! Kwa akili ya harakaharaka unadhani usafiri utakao tumika hapo ni upi ili kufika eneo la kazi?, Je! Ni miguu?, au Baiskeli au gari?..Ni wazi kuwa hapo itahitajika kifaa kinachokwenda kasi zaidi nacho si kingine zaidi ya ndege tu,..Ukitumia usafiri mwingine utachelewa tu..

Sasa ndivyo itakavyokuwa kwa habari ya unyakuo. Kipindi kifupi kabla ya Unyakuo, Bwana atawaita watu wake kwa sauti nyingine kuu..Na sauti hiyo inajulikana kama Sauti ya Malaika mkuu ukisoma (Ufuno 10:3) utaliona hilo, Hicho ndicho kipindi ambacho watu wote waliovuguvugu na walio moto wataisikia hiyo sauti kwa mahubiri ya kipekee yatakayokuwa yanafundishwa na watumishi wa Mungu waaminifu duniani kote..Na wito huu utakuwa ndani ya Muda mchache sana, Bwana Yesu alitumia mfano wa wale wanawali 10, kueleza tukio hilo litakavyokuwa ambapo tunasoma 5 walikuwa werevu na 5 wapumbavu, pindi wote waliposikia sauti ya Bwana harusi tokea mbali, wote walinyanyuka kuzitengeneza taa zao, lakini wale wapumbavu walipoona wameishiwa mafuta walijaribu kuwaomba wale werevu wawapunguzie walau hata kidogo, lakini wale werevu waliwaambia hayatutoshi sisi na nyie, ni heri mkanunue ya kwenu ndani ya hichi kipindi kifupi kabla Bwana harusi hajatokea..

Lakini kwa bahati mbaya walikuwa wameshachelewa waliporudi walikuta mlango umeshafungwa.

Sasa ndivyo itakavyokuwa ndani ya hicho kipindi kifupi, Sauti kuu italia karibia ulimwengu mzima, tunapozungumza inaweza ikawa siku yoyote kuanzia sasa, Na watu watafahamu kabisa kuwa Bwana siku yoyote anawanyakuwa watu wake, lakini kwa bahati mbaya wakati huo wapo watu ambao watakuwa tayari wapo nyuma ya teknolojia ya kimbinguni,..Wakati wenzao wanatumia kifaa cha ndege kumfikia Mungu wengine watakuwa bado wapo kwenye miguu wengine bado kwenye baiskeli, wengine kwenye gari…

Na hiyo itawachelewesha kufikia malengo yao katika hicho kipindi kifupi sana..Na siku ya kuitwa juu mbinguni itakapofika Mlango utakuwa umeshafungwa, hakutakuwa na udahili tena..Hapo ndipo kutakapokuwa na kilio na kusaga meno kama biblia inavyosema utakapoona mbona Fulani niliyemjua hayupo, mbona huyu nilikuwa ninakwenda naye kanisani hayupo, wewe ndiye utakayeumia zaidi kuliko Yule mlevi wa Bar..kwasababu mlevi wa Bar hataamini chochote.

Na ndio maana ni muhimu tuyajue hayo kwamba suala la kwenda mbinguni sio jambo la kuotea tu, bali ni jambo la kimkakati, na mkakati huo ulishaanza tangu zamani na bado hata sasa unaendelea. Leo hii unaambiwa tafuta Roho Mtakatifu maana huyo ndio muhuri wa Mungu na ndiye atakayekuongoza na kukufanya kuwa mkamilifu unasema dhehebu langu linanitosha..Unapohubiriwa juu ya mambo ya ufalme wa mbinguni, unasema sisi tupo duniani, hatuishi mbinguni, injili unazozipenda ni za kuambiwa njoo pokea, unapoambiwa tengeneza mambo yako sasa hizi ni nyakati za hatari, unasema mbona hakuna dalili yoyote ya mwisho wa dunia, lakini biblia inasema siku hiyo itakuja katika siku ambazo zinaonekana kuwa za amani ndipo uharibifu unapokuja kwa ghafla.(1Wathesalonike 5:3).

Hivyo kama ikitokea leo hii Injili hiyo ya ajabu inahubiriwa duniani kote, na bado upo vuguvugu, basi hesabu kuwa utaachwa siku ile, na utabaki tu hapa duniani kwa ajili ya dhiki kuu…Tubu leo, ili saa ile itakapokaribia uwe mfano wa wale wanawali werevu waliokuwa na mafuta ya ziada katika taa zao. Na maarifa ya kutosha kwa ajili ya kumlaki BWANA MAWINGUNI..

Ubarikiwe.

Tafadhali “Share” Ujumbe huu na kwa wengine. Na Bwana atakubariki.


Mada Nyinginezo:

DANIELI: MLANGO WA 12.

INJILI KULINGANA NA TEKNOLOJIA

SAUTI NYUMA YA ISHARA.

AMIN! NAWAAMBIA KIZAZI HIKI HAKITAPITA.

CHUKIZO LA UHARIBIFU.

MIHURI SABA.

TAZAMA, NASIMAMA MLANGONI.


Rudi Nyumbani:

 

Print this post

About the author

Admin administrator

Subscribe
Notify of
guest
0 Comments
Inline Feedbacks
View all comments