Title May 2020

KUMBUKUMBU LA DHAMBI.

Wakolosai 3:12 “Basi, kwa kuwa mmekuwa wateule wa Mungu, watakatifu wapendwao, jivikeni moyo wa rehema, utu wema, unyenyekevu, upole, uvumilivu,

13 mkichukuliana, na KUSAMEHEANA, mtu akiwa na sababu ya kumlaumu mwenzake; kama Bwana alivyowasamehe ninyi, vivyo na ninyi”.

Kwanini tunapaswa tuwasamehe wale waliotukosea?…Ni kwasababu na sisi kila siku tunahitaji rehema na msamaha kutoka kwa Mungu wetu..Wengi hatujui nguvu iliyopo katika msamaha…Biblia inasema “achilieni nanyi mtaachiliwa (Luka 6:37)”…Maana yake tusipowaachilia watu na sisi pia hatutaachiliwa…

Na msamaha sio wa masaa machache au siku chache…bali ni wa milele…mtu akikukosea huda budi kumsamehe moja kwa moja…maana yake haitatokea siku ukamwekea kinyongo tena..lakini endapo umemsamehe leo na ikapita mwezi ukayakumbuka makosa yake na kuanza kuyatia tena moyoni…Biblia inasema hapo na wewe dhambi zako ulizozitenda huko nyuma zitakumbukwa na Mungu.

Kwamfano ulishaomba rehema na kutubia wizi ulioufanya huko nyuma kabla hujampa Yesu maisha yako…au kuna siku ulimrusha mtu kiasi Fulani cha pesa, au kuna siku ulimwibia boss wako pesa, au kuna kipindi ulimchomolea mtu simu n.k Na siku moja ukakutana na injili na ukatubu na kulia..na kuacha wizi…na ukaishi hivyo kwa zaidi ya miaka 10 bila kuiba tena…Lakini siku moja ikatokea mtu kakuchomolea simu yako, ambayo ndio hiyo tu ulikuwa nayo na uliinunua kwa gharama…ikakusababishia mpaka ukapoteza mambo yako ya muhimu sana uliyokuwa umeyahifadhi katika simu ile…na moyoni ukaudhika sana, na baadaye ukamgundua yule mtu aliyekuibia, ukamwekea kinyongo moyoni pasipo hata kumwambia..

Sasa katika hali kama hiyo…kama usipomsamehe Yule mtu, ukaendelea kumchukia vile vile moyoni mwako…hata kama huibi sasa, hata kama bado unaendelea kusali na kufanya mambo mengine ya Imani…Tayari Mungu anakuona wewe nawe ni mwizi…ule wizi wote uliokuwa unaiba kule nyuma unakumbukwa wote, kama vile umeufanya jana tu!!…Haijalishi imepita miaka mingapi hujaiba…Mbele zake unarudishwa na kuonekana kama umeufanya masaa machache tu nyuma…na hivyo hata ikitokea umekufa utaenda kuulizwa kwanini uliiba ile simu, kwanini ulimwibia Yule boss wako, kwanini ulimtapeli Yule mtu n.k n.K.

Hebu soma habari hii kwa makini na utaratibu…

Mathayo 18:21 “Kisha Petro akamwendea akamwambia, Bwana, ndugu yangu anikose mara ngapi nami nimsamehe? Hata mara saba?

22 Yesu akamwambia, Sikuambii hata mara saba, bali hata saba mara sabini.

23 Kwa sababu hii ufalme wa mbinguni umefanana na mfalme mmoja aliyetaka kufanya hesabu na watumwa wake.

24 Alipoanza kuifanya, aliletewa mtu mmoja awiwaye talanta elfu kumi.

25 Naye alipokosa cha kulipa, bwana wake akaamuru auzwe, yeye na mkewe na watoto wake, na vitu vyote alivyo navyo, ikalipwe ile deni.

26 Basi yule mtumwa akaanguka, akamsujudia akisema, Bwana, nivumilie, nami nitakulipa yote pia.

27 Bwana wa mtumwa yule akamhurumia, akamfungua, akamsamehe ile deni.

28 Mtumwa yule akatoka, akamwona mmoja wa wajoli wake, aliyemwia dinari mia akamkamata,akamshika koo,akisema Nilipe uwiwacho.

29 Basi mjoli wake akaanguka miguuni pake, akamsihi, akisema, Nivumilie, nami nitakulipa yote pia.

30 Lakini hakutaka, akaenda, akamtupa kifungoni, hata atakapoilipa ile deni.

31 Basi wajoli wake walipoyaona yaliyotendeka, walisikitika sana, wakaenda wakamweleza bwana wao yote yaliyotendeka.

32 Ndipo bwana wake akamwita, akamwambia, Ewe mtumwa mwovu, nalikusamehe wewe deni ile yote, uliponisihi;

33 nawe, je! Haikukupasa kumrehemu mjoli wako, kama mimi nilivyokurehemu wewe?

34 Bwana wake akaghadhibika, akampeleka kwa watesaji, hata atakapoilipa deni ile yote.

35 Ndivyo na Baba yangu wa mbinguni atakavyowatenda ninyi, msiposamehe kwa mioyo yenu kila mtu ndugu yake”.

Ndugu achana na biashara za kupambana pambana na maadui zako, jifunze kusamehe ndivyo na wewe utakavyosamehewa na Mungu Baba…Aliyekufundisha kwamba mlaani anayekukosea…huoni kwamba anataka na wewe ulaaniwe na Mungu?…anayekuzuia kusamehe huoni kama anakutakia mabaya?..huoni anakufungulia mlango wa kwenda jehanamu ya moto??…hebu soma tena mstari wa 35 hapo juu….na wewe binafsi unapojizuia kuwasamehe wanaokukosea hata baada ya kuelewa haya..huoni unajishitaki mwenyewe na kumkumbusha Mungu dhambi zako?.

Bwana atujalie kuyaelewa hayo.

Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema, na pia kama utapenda tuwe tunakutumia masomo haya kwa njia ya email yako au Whatsapp tutumie ujumbe kwenye box la maoni chini au piga namba hii +255 789001312


Mada Nyinginezo:

JE KUNA UISLAMU KATIKA BIBLIA?

Je! kuna maombi yoyote ya kumtoa mtu aliyekufa kwenye mateso ya kuzimu?

Mwaloni ni nini? Na je unafunua nini rohoni?

NAMI NINAZO FUNGUO ZA MAUTI, NA ZA KUZIMU.

Je! Ni sahihi kwa mkristo kuoa/kuolewa na mtu wa imani nyingine?

VITABU VYA BIBLIA: Sehemu ya 4

Rudi Nyumbani:

Print this post

MIGUU ILIYO MYEPESI KUKIMBILIA MAOVU, NI CHUKIO KWA BWANA.

Zipo dhambi za maandalizi, na zipo dhambi zisizo na maandalizi..

Hizi dhambi za maandalizi ni rahisi sana kuzishinda, kwasababu sio za kushtukiza kwani huwa zinaanzia mbali na hivyo mtu ni rahisi kuziona na kuzikwepa, na akizifanya mbele za Mungu adhabu yake inakuwa ni kubwa kuliko zile ambazo zinakuja bila maandalizi,

Mfano wa dhambi zisizo na maandalizi, ni kama vile hasira, hofu, mawazo mabaya, na mara chache sana kuzungumza maneno yasiyofaa..

Lakini Mfano wa dhambi zenye maandalizi, ni kama vile Uzinzi/Uasherati wa aina yoyote ile ikiwepo punyeto, ushoga, usagaji, ulevi, utoaji mimba, utapeli, wizi, n.k.

Hizi ni dhambi ambazo mtu hawezi kuzifanya bila kuwa na maandalizi Fulani, au kupitia hatua Fulani(process). Huwezi kusema nimepitiwa kufanya uzinzi wakati kitendo chenyewe kabla ya kufanya mlikutana mahali Fulani, mkakubaliana, na kabla hujafanya kile kitendo ndani yako kabisa kulikuwa na kipenga chekundu kinalia kikikuambia kuwa hicho kitendo unachokwenda kukifanya sio sawa ni dhambi, lakini wewe unakwenda tu, bila kujali..na mwisho wa siku unakifanya..vile vile na wizi,..n.k.

Fahamu kuwa mbele za Mungu dhambi kama hizo usidhani gharama zake ni ndogo kuziondoa.. kamwe usije ukasema ah, si nitatubu tu?..Fahamu kuwa Toba sio tiba ya dhambi, kama vile Panadol kwamba ukiumwa kichwa unakwenda kumeza kisha unapona, kesho tena ukiumwa unakwenda kumeza nyingine..

Ukadhani pia katika kila aina ya dhambi ya namna hii dawa ni kutubu tubu. Ujue kuwa Zipo dhambi biblia imeziita dhambi za Mauti..Hizi ukitenda na huku unajua hupaswi kuzifanya, hakuna msamaha, ndio unaweza ukasemehewa baada ya kutubu kwa muda mrefu sana lakini adhabu ya kifo bado itabakia pale pale..

(Kwa urefu wa somo hili la dhambi ya mauti,  utalipata chini kabisa mwisho wa somo hili),

Dhambi hii Hata ulieje, hata utubuje, adhabu ya kifo haiondoki..kwasababu uliitenda kwa makusudi,

Inawezekana wewe nawe leo ni mmojawapo wa walio mbioni kukimbilia kutenda maovu hayo..Embu geuka ujiepusha na hatari hiyo iliyopo mbele yako…Na wewe mwingine ambaye umekuwa ukiishi katika kutenda dhambi kama hizo za makusudi ukidhania kuwa utatubu tu, na kwamba neema itakuwepo kila siku kukuokoa..Embu futa mawazo hayo na kwa moyo mmoja leo hii umgeukie muumba wako, utubu leo dhambi zako kwa kumaanisha nawe pia Mungu atakusikia..

Kumbuku miguu ikimbiliayo maovu na machukizo kwake Bwana, ni moja ya mambo sita yanayomuudhi Bwana (Mithali 6:18).

Bwana akubariki.

Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema, na pia kama utapenda tuwe tunakutumia masomo haya kwa njia ya email yako au Whatsapp tutumie ujumbe kwenye box la maoni chini au piga namba hii +255 789001312


Mada Nyinginezo:

DHAMBI YA MAUTI

KUTUBU SIO KUOMBA REHEMA.

MADHABAHU NI NINI?

MUUNGANIKO WA MADHEHEBU NI MPANGO WA MPINGA-KRISTO.

MAOMBI YA VITA

KAMA TUNATAKA KUWA ASKARI WA BWANA, NI LAZIMA TUJUE VIGEZO.

Rudi Nyumbani:

Print this post

USIINGIE MKATABA NA DHAMBI.

Laiti Yuda angefahamu yatakayokwenda kumpata Bwana ni makubwa kiasi kile, asingedhubutu hata kidogo kumsaliti, Yeye alijua tu watakwenda kumchukua na kumkemea asiwafundishe makutano mahubiri yake, na kumtishia kidogo na kisha kumwachia aende…Lakini mambo kule yalienda kuwa makubwa kuliko alivyotegemea…Kwani walikwenda kumpiga, na kumdhihaki, na kufikia hatua mpaka ya kumwua Bwana tena kwa kifo cha aibu na mateso…

Kwasababu ya tamaa ya fedha hakujua tayari ametumika kulitimiza kusudi la shetani…Pasipo kuwa na macho ya kuona mbali alijikuta kawa chombo maalumu cha shetani. Moto mdogo aliouwasha akidhani utateketeza karatasi tu, sasa umeteketeza msitu mkubwa…Ndio maana mwishoni aliishia kujuta kwa aliyoyafanya, alipoona kwamba ni busu lake dogo tu limemfikisha Bwana msalabani, alipoona vipande 30 tu vya fedha vimemwaibisha vile na kumtesa kiasi kile…alipojua atafikishwa salama na kutoka salama lakini mwisho wake anaishia kuvuliwa nguo na kuvishwa taji ya miiba kichwani…ni Dhahiri kuwa ilikuwa ni nje ya mapatano yao..

Marko 14:44 “Na yule anayemsaliti alikuwa amewapa ishara, akisema, Nitakayembusu, huyo ndiye; mkamateni, MKAMCHUKUE SALAMA.

45 Basi alipokuja, mara akamwendea, akasema, Rabi, akambusu.

46 Wakanyosha mikono yao wakamkamata”.

Mstari wa 44 hapo unasema “mkamchukue salama”…Lakini kule alipokwenda walikwenda kumtesa na kumwaibisha na kumuua, kinyume na mapatano yao. Na hiyo yote ni kutokana na kuingia mkataba na dhambi.

Na mwisho Yuda anasema maneno haya…

Mathayo 27: 3 “Kisha Yuda, yule mwenye kumsaliti, alipoona ya kuwa amekwisha kuhukumiwa, alijuta, akawarudishia wakuu wa makuhani na wazee vile vipande thelathini vya fedha, akasema, Nalikosa nilipoisaliti damu isiyo na hatia.

4 Wakasema, Basi, haya yatupasani sisi? Yaangalie haya wewe mwenyewe.

5 Akavitupa vile vipande vya fedha katika hekalu, akaondoka; akaenda, akajinyonga”

Mambo machache tunaweza kujifunza hapo…unaweza kuuza wokovu wako kwa kitu kidogo..lakini mwishoni usijue kama kitakuletea au kitaleta madhara makubwa mbeleni…Umemwamini Yesu tayari, lakini unaingia tamaa ya kufanya zinaa..hivyo unatoka na kumwona mwanamke na kumtamani, na kusema nitatubu tu…siku unakutana naye kumbe kuna mwingine amewaona na kuwafuatilia mpaka nyumba mnayokwenda, na huko mnakuja kufumaniwa..na picha zinapigwa na kuwekwa kwenye mitandao..mtumishi fulani au mpendwa fulani afumaniwa na mke wa mtu…utajisikiaje siku hiyo?..Wewe ulidhani ni moto mdogo tu umewasha kumbe hujui utakwenda kuwa mkubwa wa kushtusha mji mzima, na hivyo hivyo na dhambi nyingine zote, tunaweza kuziona zina madhara madogo hapa tu..lakini baada ya kuzitenda ndio tutaona ukubwa wake..

Kwahiyo tunapaswa kuzidi kuwa makini kwa kila kitu, Mfano wa Yuda ni somo tosha kwetu…Tujichunge yasijikute na sisi, shetani akatudangaya tukajikuta tunamsulubisha Kristo mara ya pili kwa aibu na mateso. Na mwisho wa siku tukashindwa hata kurudi kule tulipokuacha.

Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema, na pia kama utapenda tuwe tunakutumia masomo haya kwa njia ya email yako au Whatsapp tutumie ujumbe kwenye box la maoni chini au piga namba hii +255 789001312


Mada Nyinginezo:

MADHARA YA DHAMBI YA UASHERATI.

Je Mtu anaweza kusema uongo, Na Mungu akambariki?

NAMI NINAZO FUNGUO ZA MAUTI, NA ZA KUZIMU.

JE NI DHAMBI KUWA NA MAHUSIANO KABLA YA NDOA?

Kwanini wanawake wengi huwa wanalipuka mapepo?

MAMBO 5 AMBAYO KILA MKRISTO ANAPASWA KUFAHAMU.

Rudi Nyumbani:

Print this post

JE! TUNAPASWA KUUAMINI UNABII WA SYLVIA BROWNE?

Hivi karibu mwanamke huyu amepata umaarufu mkubwa duniani japo alishafariki mwaka 2013, lakini kitabu chake kilichoitwa “End of days”, ambacho ndani yake kimeandika baadhi ya nabii zitakazotokea siku za mwisho, ndicho kilichomfanya ajulikane kwa haraka, na moja ya nabii hizo ni kuhusiana na mlipuko wa gonjwa ambalo kwasasa linajulikana kama Covid-19, kama wengi wanavyojua alitabiri kwa ufasaha kuwa kipindi cha mwaka wa 2020 kutazuka gonjwa linaloshambulia mapafu, ambalo litaathiri karibu dunia nzima, na akaongezea kusema kuwa hata hivyo gonjwa hilo litatoweka lenyewe kama lilivyokuja, na litarejea tena baada ya miaka 10 ndipo litakapotoweka moja kwa moja.

Lakini unabii mwingine alioutoa ambao ndio kiina cha ujumbe wa leo, ni ule aliosema, mwaka alioutaja kama “3020” Kutazuka viumbe wa ajabu duniani, ambao wataitwa “VAMPIRES” ni watu ambao watafufuka, na watakuwa wanaishi kwa kutegemea kunywa damu za watu, watakuwa hawapatani na mwanga, lakini baadaye watauliwa na hali itarejea kama kawaida. Hivyo watu wengi waliposikia hivyo mitazamo yao ikabadilika kuhusu mambo yajayo..

Lakini ulishawahi kujiuliza juu ya nabii nyingine alizowahi kuzitoa huyu mama? Siko kumkosoa lakini lipo japo nataka ujifunze mwisho wa makala hii ..baadhi ya hizo alisema..

Mwaka 2010 kutatokea Aliens (Viumbe kutoka sayari nyingine) duniani..Jambo ambalo halikutokea, mpaka sasa halipo.

Mwaka 2004, alitabiri Osama ameshakufa,.Lakini Osama alikuja kupatikana mwaka 2011 na kuuawa.

Ndani ya kitabu chake kimoja aliandika, chanjo ya ugonjwa wa HIV, itapatikana mwaka 2005. Lakini chanjo hiyo mpaka leo hii haijapatikana.

Na nyingine nyingi, ambazo hatuwezi kuzichambua moja moja kwasababu sio lengo la ujumbe huu kuwakosoa watu, lakini tufumbuke macho, tusipelekwe na kila aina ya mafunuo yanayokuja duniani siku hizi…

Sasa tukirudi kwenye lile la mwaka 3020 alilolisema kuwa kutatokea viumbe wajulikanao kama Vampires..Na hili limewafanya watu wengi waamini kwa asilimia kubwa kwamba watatokea, kwasababu tu lile la ugonjwa ufananao na nimonia (Corona) lilitokea kisahihi.. na wengine wamekuwa na mtazamo mwingine wa kuishi wakidhani kuwa hii dunia itaendelea kuwepo mpaka huo mwaka wa 3000 yeye alioutaja…

Ni vizuri ukafahamu biblia inatukumbusha kwamba hata kama unabii utatolewa na mtu fulani na ukawa sahihi kabisa, bila kuwa na kasoro kasoro lakini kama unakinzana na maagizo ya Mungu, hatupaswi kupokelewa hata kidogo kwani ni wa uongo, (Soma kumbukumbu 13)

Hivyo usikimbilie kuupokea kila unabii ukasema unatoka kwa Mungu, kisa tu umetokea! bila wewe kukaa chini na kuutathimini katika maandiko..

Hizi ni nyakati za mwisho, kuhusu janga hili la Corona wapo wengine wengi sana wametabiri kiufasaha kuhusu juu ya gonjwa hili kama ulikuwa hujui lakini hawakuwa wakristo fuatilia hata habari ya Novel ya the eyes of the darkness, utaona, wapo wengine wengi sana, watafute internet utawaona,.. Lakini Pia Mungu anaweza kumtuma mtu wake kabisa , atoe unabii na ukaja kutimia, na akatoa maagizo yanayokinzana na Neno lake, Kumbe Ni Mungu ndiye aliyemtuma ili akupime moyo wako kama kweli unalishika Neno lake au la!!.. Na kama ukifuata tu, ndio umekwenda na maji.. Hebu tusome kidogo andiko linalozungumzia mambo hayo…

Kumbukumbu 13: 1 “Kukizuka katikati yako nabii, au mwotaji wa ndoto, akikutolea ishara au ajabu,

2 IKATUKIA HIYO ISHARA AU HIYO AJABU ALIYOKUAMBIA akisema, Na tuifuate miungu mingine usiyoijua, tuitumikie hiyo;

3 wewe usiyasikize maneno ya nabii yule, au yule mwotaji wa ndoto, kwa kuwa Bwana, Mungu wenu, yuawajaribu, apate kujua kwamba mwampenda Bwana, Mungu wenu, kwa mioyo yenu yote na roho zenu zote”.

Sasa tukirudi kwenye maandiko hakuna mahali popote panapotabiri kuhusu ujio wa “Vampires”..Au kutokea kwa viumbe vingine kutoka sayari za mbali (Aliens).. unabii huo ni batili..Hizo ni ndoto za wanasayansi ambazo zinakinzana na Neno la Mungu..

kama hayo yatakuja kutokea basi ungeshayaona kwenye maandiko tangu zamani, kwasababu hakuna jipya chini ya jua..Kwamfano tabiri za kutokea magonjwa ya mlipuko mfano wa tauni, yalitabiriwa hivyo mtu akitabiri kuhusu hilo sio jambo la kushangaza kwasababu biblia ilishaeleza, vile vile matetemeko, au njaa, au vita,manabii wa uongo, wapinga Kristo n.k. yote hayo yapo kwenye maandiko na yalishatabiriwa.. Lakini sio watu wanaofufuka na kunyonya damu za watu, watakaofufuka ni watakatifu tu, na sio kitu kingine chochote..Yesu pekee ndio UFUFUO NA UZIMA(Yohana 11:25), Na yeye peke yake ndiye mwenye funguo za kuzimu na mauti, shetani hana tena hizo funguo, hawezi kumfufua mtu wala kumleta mtu juu kama alishanyang’anywa hayo mamlaka kitambo sana…sasa jiulize atakayewafufua hao mavempire(mazombie) Wanyonye watu damu ni Bwana Yesu?..tafakari..unaona kabisa haingii akilini, ni kinyume na maandiko?…Ufufuo uliotabiriwa ni ufufuo wa wenye haki kwa ajili ya uzima na ufufuo wa waovu kwa ajili ya kuhukumiwa kwa maovu waliyoyafanya, na si kwaajili ya kunywa damu za watu!.

Yohana 5:28 “ Msistaajabie maneno hayo; kwa maana saa yaja, ambayo watu wote waliomo makaburini wataisikia sauti yake.

29 Nao watatoka; wale waliofanya mema kwa ufufuo wa uzima, na wale waliotenda mabaya kwa ufufuo wa hukumu”.

Hivyo jihadhari na udanganyifu wa ndoto za wanasayansi..

Kwa hiyo ndugu kwa maneno mafupi..Ni kwamba tunaishi katika siku za mwisho, na siku yoyote Kristo anarudi kulinyakua kanisa lake.. anayekupa matumaini kuwa kutakuwa na miaka mingine elfu moja ya kuishi mbeleni (1000), anakupoteza, ni agenda za shetani kuwaminisha watu kuwa muda bado sana, Kwamba Kristo bado sana arudi. Ilihali Dalili zote tulizoelezwa na Kristo zimeshatimia..Hivyo ni wakati wa kujiandaa sasa, acha kufuata mafunuo yasiyo dhahiri ya siku hizi za mwisho..Yapo mengi na yataendelea kuwa mengi, kwajinsi siku zinavyozidi kusogea..Ukiyafuata utayumbishwa sana, na kupotezewa mwelekeo wa imani yako kama huna msingi mzuri wa kimaandiko..Hizi ni nyakati za mwisho kweli kweli mpinga-Kristo ameshajiweka tayari kuanza kazi na sio VAMPIRE au ALIENS.

Hivyo Tubu dhambi zako leo, mpokee Kristo, kama hujamwamini, jiweke tayari kwa kurudi kwa pili kwa Kristo duniani.

Shalom.

Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema, na pia kama utapenda tuwe tunakutumia masomo haya kwa njia ya email yako au Whatsapp tutumie ujumbe kwenye box la maoni chini au piga namba hii +255 789001312


Mada Nyinginezo:

KUTAKUWA NA MATETEMEKO YA NCHI, NJAA NA TAUNI.

Kuna ufufuo wa aina ngapi?

BASI TUENDELEE KUMJUA MUNGU,NAYE ATATUJILIA KAMA MVUA YA VULI.

Je! Ni sahihi kuoa/kuolewa na mtu uliyemzidi umri?

MKUMBUKE MKE WA LUTU.

KUZIMU ni mahali pa namna gani, Je! huko wanaishi watu wakifa na kwenda kupata mateso au ni vinginevyo?

Rudi Nyumbani:

Print this post

UWEZO WA KIPEKEE.

Kuna kipindi tuliishi bila kutegemea pua zetu kupumua, kuna kipindi tuliishi bila kutegemea midomo yetu kulia chakula…Na kipindi hicho si kingine zaidi ya kile kipindi ambacho tuliishi tumboni mwa mama zetu, kwa miezi 9 tuliishi maisha ya kimiujiza ujiza.. Hakuna mwanadamu yoyote anayeishi sasa ambaye hajapitia kuishi maisha hayo ya kimiujiza.

Hivyo si ajabu Bwana alisema… “….Imeandikwa, Mtu hataishi kwa mkate tu, ila kwa kila neno litokalo katika kinywa cha Mungu (Mathayo 4:4).

Kama kuna wakati maisha hayo yaliwezekana…hata sasa kuna mambo yanaonekana kama hayawezekani lakini yanawezekana.

Inaweza kuonekana haiwezekani kabisa leo kuishi maisha makamilifu yanayompendeza Mungu…lakini nataka nikuambie hilo linawezekana kabisa..kwasababu Bwana mwenyewe alisema tutakuwa wakamilifu kama Baba yetu alivyo mkamilifu…(Mathayo 5:48). Hivyo Mungu asiyeweza kusema uongo, hawezi kuumba kiumbe ambacho anajua atakipa jukumu kubwa zaidi ya uwezo wake…Kwasababu hiyo basi jinsi alivyotuumba sisi, anajua kabisa kuna namna au mazingira ambayo tukijiweka tutakuwa wakamilifu kama yeye anavyotaka sisi tuwe.

Na ukamilifu na utakatifu tunaouzungumzia sio ule wa kujisifu na kujibeza kwamba ni mkamilifu au mtakatifu mbele za Mungu, wala sio ule wa kujihesabia haki kwamba sifanyi hichi wala kile kama mtu Fulani au watu Fulani wanavyofanya…bali ukamilifu na utakatifu unaozungumziwa ni ule wa roho ya unyenyekevu, na ya kumwogopa Mungu, ambao huo unaleta moyo wa toba siku zote mbele za Mungu na hofu ya Mungu…ambapo hofu hiyo itakuzuia wewe kutokufanya mambo yote yasiyompendeza Mungu, hofu hiyo itakufanya usidhubutu kwenda kuzini, mawazo ya uzinzi yanapokujia unayashinda ndani ya sekunde chache sana, pia hofu hiyo inakuzuia kwenda kuiba, kwenda kutoa mimba, kwenda kula rushwa, n.k..Na haikufanyi wewe kujilinganisha na wengine au kufurahia wengine wanapofanya mambo ambayo wewe huyafanyi na kujifanya bora kupita hao…Yaani unapomwona mwingine anajiuza, unapata hisia kama ni dada yako au ndugu yako wa damu ndio yupo vile, lakini sio kufurahia kana kwamba umemzidi utakatifu, na hivyo wewe ni heri kuliko yeye…Huo sio utakatifu bali ni kujibeza, ambako hakumpendezi Mungu.

Hivyo..huo uwezo wa kuwa mkamilifu kwa namna hiyo ya kumpendeza Baba…Tumeahidiwa kwenye Neno la Mungu kwamba “Unaweza ukashuka juu yetu na ni ahadi”..Tunauita ni uwezo kwasababu katika hali ya kawaida, ni ngumu kumpenda Yule mtu anayekuchukia, ni ngumu kumsamehe Yule mtu ambaye amekutendea ubaya mkubwa sana, ni ngumu kurudisha mali ya Yule mtu aliyekuibia, ni ngumu kuacha uasherati au ukahaba unaokuingizia kipato kizuri n.k…Hivyo inahitajika uwezo mwingine kushuka juu yetu. Na huo uwezo ukishuka ndio unatufanya tuishi kimiujiza kama tulivyokuwa tunaishi kipindi Fulani huko nyuma tulivyokuwa tumboni mwa mama zetu…

Tulikuwa na pua lakini tulikuwa huituitumii tumboni, tulikuwa na midomo lakini tulikuwa huutumii kula..lakini bado tulikuwa tunaishi na kukua…Hali kadhalika ukiupokea huu uwezo leo, watu watashangaa unawezaje kuishi bila kufanya uzinzi na hali una uwezo wa kufanya hayo yote, na mazingira yanakuruhusu…wewe mwenyewe utajishangaa umewezaje kuishi bila kulewa tena pombe na ilihali una fedha za kukutosha kufanya hayo yote n.k.

Sasa uwezo huo utashuka juu yako endapo tu, utakubali tu kuviacha hivyo vitu…Kitu kimoja ambacho unahitaji kufahamu wewe ambaye bado hujampokea Yesu, ni kwamba Nguvu ya Roho Mtakatifu haiwezi kuzidi nguvu ya maamuzi yetu…maana yake ni kwamba Mungu hatulazimishi kama ma-robot kufanya mapenzi yake ingawa anao uwezo wa kufanya hivyo, ila hajachagua kufanya hivyo…anachokifanya ni kutuwekea chaguzi mbili mbele yetu…tuchague UZIMA au MAUTI. Tunapochagua uzima basi ndipo anatupa Baraka zote za Uzima ikiwemo UWEZO wa kuwa kama yeye.. Lakini tukichagua mauti hatatulazimisha kutupa uzima…Hivyo uchaguzi ni wetu.

Sasa hatuchagui kwa midomo…bali kwa vitendo..Maana yake ni kwamba kama ulikuwa unafanya kazi ya Bar, unaiacha mara moja, kama ulikuwa ni msikilizaji wa miziki ya kidunia kupitia simu yako unaifuta hiyo miziki na hizo video za kidunia zote pasipo kubakiza hata moja..kama ulikuwa ni mwizi na umeiba, unamrudishia Yule mtu mali yake uliyomuibia kama bado unayo na unakusudia kuacha wizi..kama ulikuwa unajiuza unaiacha hiyo biashara, kama ulikuwa ni mlevi hivyo hivyo unaacha kwenda ile Bar, na vitu vingine vyote visivyompendeza Mungu unajilazimisha kuviacha katika maisha yako Sasa Baba wa mbinguni akiona kwamba kwa vitendo umeacha mambo hayo…Ule uwezo unaushusha juu yako wakati huo huo ulipoamua kuyaweka chini maisha ya kale…

Kwasababu umeingia gharama ya kuyavua maisha yako ya kale, na yeye Baba wa mbinguni anaingia gharama ya kukutuza wewe usirudi tena nyuma..na anakutunza kwa njia gani?..kwa njia hiyo ya kukupa UWEZO wa kushinda Dhambi, na kuwa mkamilifu.

Sasa ndani ya kipindi kifupi baada ya wewe kuamua kuacha maisha ya dhambi kwa vitendo, utaona ile kiu ya pombe inakata ghafla, ile kiu ya kufanya ukahaba inakata ghafla, hupambani vita vikali kuukataa uasherati tofauti na hapo kwanza…mpaka wewe mwenyewe utajishangaa umekuwaje?..zamani ulikuwa ukipitisha siku mbili bila kunywa pombe unasikia kuumwa, lakini utashangaa inapita wiki, mara mwezi, mara mwaka hata ile hamu haipo..ulikuwa haipiti siku bila kujichua lakini utajikuta imepita wiki, mwezi na mwaka bila hata kukikumbuka hicho kitendo…sasa ukishafikia hatua kama hiyo basi ule uwezo umeshamiminwa ndani yako…na uwezo huo utaambatana na mambo mengine ya muhimu kama tuliyoyataja hapo juu..utajikuta unakuwa na hofu ya Mungu, na mtu wa kumpenda Mungu na kuzidi kujitenga na ulimwengu, pamoja na kuwa msaada kwa wengine ambao hawajaingia ndani ya Neema hiyo.

Kwahiyo kama wewe bado hujamwamini Yesu Kristo na bado hujapokea huo uwezo, tambua kwamba bado nafasi unayo…nguvu hiyo ni kutubadilisha ni zawadi kwetu sote kutoka kwa Baba, endapo tu tukimwamini Yesu..Hivyo basi popote pale ulipo tenga muda kadhaa peke yako binafsi, mwombe Mungu rehema..kisha kusudia kuacha yale yote uliomwomba akurehemu…Kumbuka kutubu maana yake ni kugeuka!..Hivyo matendo yako yana maana sana mbele za Mungu Baba zaidi ya maneno yako..

Pia inawezekana umeshamwamini Yesu, lakini umeomba muda mrefu uwezo huu ushuke juu yako, lakini bado huoni chochote, bado unajikuta unafanya punyeto, bado unajikuta unarudi kwenye ulevi, uasherati na ushirikina…kama unapitia hali kama hiyo basi fahamu kuwa hukutubu vizuri…Uliomba tu rehema..kwamba Bwana akusamehe tu hiki na kile..lakini hukukusudia kuviacha vile vitu kwa vitendo..bado ulikuwa ni miziki kwenye simu yako, bado ulikuwa unatembelea zile site za pornograph bado ulikuwa umejiungamanisha na makundi yale ya ulevi na walevi, na ndani kwako kulikuwa na chupa za bia, bado ulikuwa unarudi kwenye kazi yako ya Bar n.k..Hiyo ndio maana ule uwezo haukushuka ndani yako..lakini leo bado unayo nafasi..Tubu tu kwa kuacha hayo mambo na Bwana atakushushia uwezo huo wa kuishi kimiujiza kama aliokupa wakati ule ulipokuwa tumboni mwa mama yako.

Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema, na pia kama utapenda tuwe tunakutumia masomo haya kwa njia ya email yako au Whatsapp tutumie ujumbe kwenye box la maoni chini au piga namba hii +255 789001312

Mada Nyinginezo:

MUUNGANIKO WA MADHEHEBU NI MPANGO WA MPINGA-KRISTO.

NAMI NINAZO FUNGUO ZA MAUTI, NA ZA KUZIMU.

JE MOYO WAKO NI MNYOFU MBELE ZA MUNGU

Je ni sahihi kumtenga mtu anapofanya dhambi kanisani?

Mbona Mungu anaruhusu watu wapate shida, ilhali ana uwezo wa kutuepusha?

Kwanini Mungu alisema hakuna mtu awazaye kuuona uso wake akaishi?

Rudi Nyumbani:

Print this post

JINSI DHAMBI INAVYOMGHARIMU MTU SANA.

Mwanzo 47:9 “Yakobo akamjibu Farao, Siku za miaka ya kusafiri kwangu ni mia na thelathini; siku za miaka ya maisha yangu zimekuwa chache, TENA ZA TAABU, wala hazikufikilia siku za miaka ya maisha ya baba zangu katika siku za kusafiri kwao.”

Hakuna dhambi isiyokuwa na gharama. Unaweza ukajiuliza ni kwanini Yakobo alimwambia Farao siku zake za kusafiri duniani zimekuwa ni za taabu, zisizoweza kufananishwa na za baba zake..?..

Ni kwasababu ya ujanja alioufanya wa kumdanganya baba yake na kuchukua mbaraka wa ndugu yake, Japo ni kweli ndani yake kulikuwa na mpango wa Mungu uliobeba ujumbe uliomhusu Mesia, lakini kitendo alichokifanya bado kilikuwa ni uovu..Na hiyo haikuzuia kutumikia adhabu ya uovu wake.

Na ndio maana utaona Yakobo baada ya kufanya kitendo kile alikimbilia kwa mjomba wake, hata yule mama yake aliyependana naye na kupatana kutenda uovu, ndio ikawa mwisho wa kuonana kwao tena mpaka mwisho wa miaka 20 mbeleni, kuonyesha kuwa upendo wowote wenye makubaliano yasiyo makamilifu huwa haudumu..

Na alipofika kwa mjomba yake Labani, na kukaa huko, akimtumikia kwa ajili ya Raheli mke wake, kwa miaka saba, akidhani sasa ndio anakwenda kumpata Raheli, kumbe mjomba yake Labani akamfanyia hila kama ile ile aliyomfanyia ndugu yake Esau, matokeo yake akapewa dada yake Lea ndio awe mke wake badala ya Raheli, hivyo Labani akamwambia akimtaka na Raheli pia ni lazima amtumie miaka saba mingine..

Akaendelea kuwa mtumishi kwa muda mrefu mingine, mpaka wakati anaondoka, Na kwenda kule Kaanani nchi ya baba yake. Huko nako Watoto wake wawili Simeoni na Lawi, wakamfanyia hila kwa kudanganya, mpaka wakaenda kuwauwa watu wasiokuwa na hatia (Mwanzo 34),

Kama hiyo haitoshi, mwanawe wa kwanza Reubeni, akamzunguka baba yake, naye pia akamfanyia hila akaenda kulala na mke wake.

Tena Zaidi ya hayo, Watoto wake wakamfanyia hila kubwa Zaidi, kumdanganya kuwa mtoto wake Yusufu ampendaye ameliwa na mnyama mkali porini..Ikimfanya alie sana na kuomboleza kwa uchungu mwingi..

Kwahiyo unaweza kuona Maisha ya Yakobo, yalikuwa ni ya kudanganywa danganywa tu, na kufanyiwa hila kila kukicha, tofauti na ilivyokuwa kwa Ibrahimu na Isaka..

Kwasababu biblia inasema…

Mathayo 7:2 “Kwa kuwa hukumu ile mhukumuyo, ndiyo mtakayohukumiwa; na kipimo kile mpimiacho, ndicho mtakachopimiwa”.

Na ndio maana utaona anakiri kabisa Maisha yake yalikuwa ni ya taabu,..Lakini mwishoni kabisa Mungu alikuja kumpa faraja, kupitia mwanawe Yusufu.

Sasa huyo alikuwa ni Yakobo, mtu aliyebarikiwa na Mungu, lakini hakuachwa bila adhabu ya muda mrefu hapa duniani. Tujiulize sisi ambao tunaoendelea kuishi katika Maisha ya dhambi, Maisha yetu sikuzote ni ya dhuluma, tutawezaje kupona tusipouthamini wokovu mkuu namna hii?

Mithali 11:31 “Tazama, mwenye haki atalipwa duniani; Basi mwovu na mkosaji si mara nyingi Zaidi”

Adhabu hizi za mwilini zinafunua zile za rohoni..Wapo wanaodhani ukifa tu, ndio umekufa hakuna adhabu baada ya hapa…Adhabu ipo kwa wakosaji wote. Lakini Neema ya Mungu pia ipo kutukinga na adhabu hizo.

Na neema yenyewe ni kupitia YESU KRISTO. Tukimkabidhi Maisha yetu atatusamehe na kutugeuza na kutufanya kuwa wapya tena. Atafuta hata deni la dhambi na adhabu tulizostahili kuzipokea katika utoaji mimba wetu, katika uuaji wetu, katika rushwa zetu, katika uongo wetu, katika wizi wetu, katika uzinzi wetu, katika utapeli wetu n.k. Na hiyo ndio faida ya agano hili jipya la neema lililo katika damu ya YESU.

Hivyo kimbilia leo msalabani ikiwa bado hujaaokoka, tubu dhambi zako, ukabatizwe, usamehewe dhambi zako kisha upokee Roho Mtakatifu, atakaye kuwa na wewe hadi siku ile ya mwisho ya Unyakuo.

Bwana akubariki sana.

Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema, na pia kama utapenda tuwe tunakutumia masomo haya kwa njia ya email yako au Whatsapp tutumie ujumbe kwenye box la maoni chini au piga namba hii +255 789001312

Mada Nyinginezo:

Amin, nawaambia, Kizazi hiki hakitapita, hata hayo yote yatakapotimia..!!

KWANINI UNAPASWA UJIWEKE TAYARI SASA, KABLA YA ULE WAKATI KUFIKA?.

USIJITAFUTIE KULAMBWA NA MBWA KWA DHAMBI YA KUTAMANI.

MAONO YA NABII AMOSI.

Je Mtu anaweza kusema uongo, Na Mungu akambariki?

MKUMBUKE MKE WA LUTU.

MPINGA-KRISTO

Rudi Nyumbani:

Print this post

Je ni sahihi kumtenga mtu anapofanya dhambi kanisani?

JIBU: Yapo makundi mawili kanisani..kundi la kwanza ni lile ambalo linahusisha washirika, ambalo ndani yake kuna wachungaji, waalimu, wainjilisti, mashemasi na waumini na wengineo…Kundi lote hili linahusisha washirika ambao tayari wameshamwamini Yesu Kristo, na kubatizwa na kupokea Roho Mtakatifu…hali kadhalika wameshajifunza Neno vya kutosha na kukolea katika maarifa ya ki-Mungu…hata kufikia kiasi cha kuweza kuwaelekeza na kuwaelekeza wengine katika njia ya wokovu.

Na kundi la pili ni lile la watu waliookoka karibuni, au walioingia katika Imani kipindi cha hivi karibuni..Wengi wa hawa unakuta ni wachanga kiimani, na mara nyingi wanakuwa ni wageni…Hivyo wanakuwa bado wanahitaji msaada katika kujifunza Imani na uweza wa Mungu..Na kwasababu wametoka katika ulimwengu bado kuna tabia baadhi baadhi wanakuwa hawajaziacha kutokana na kwamba pengine hawajajua Neno la Mungu linasemaje kuhusu mambo hayo wanayoyafanya.

Sasa katika lile kundi la kwanza ambalo linahusisha washirika ambao tayari wameshaijua kweli ya Mungu kwa utimilifu mkubwa…wameshajua na kufundishwa uasherati ni dhambi, wizi ni dhambi, ulevi ni dhambi n.k…Wakakengeuka na kurudia matapishi na kufanya mojawapo ya dhambi hizo ambazo tayari walishajifunza kuwa ni machukizo kwa Mungu…Mtu wa Namna hiyo kimaandiko ANAPASWA ATENGWE!!…Na endapo asipotengwa wale ambao wanapaswa wamtenge watakuwa WANAFANYA DHAMBI MBELE ZA MUNGU!!…Hivyo ni agizo la Mungu kwamba ni lazima atengwe…

Na kutengwa huko kunahusisha, yeye kutoonekana maeneo au mazingira ya kanisa kwa kipindi kirefu…Na washirika wengine hawatakiwi hata kumsalimia wala kushirikiana naye kwa lolote lile, hata hata kama atatubu…atakaa mwenyewe kwa kipindi chote hicho…mpaka wakati ambao Kanisa litasikia amani ya Roho kumrudisha…na wakati huo wa kutengwa huku akiwa katika hali ya toba na maombolezo, Mungu atakuwa anamrudi kwa aliyoyafanya. Hivyo hakuna raha yoyote katika kutengwa, kama kweli ni mtoto wa Mungu. Kwasababu asipotolewa katika kanisa, watu wote wataiga na hawatamwogopa Mungu..Hivyo ili kuzuia hilo, biblia imeruhusu kumwondoa mtu huyo ili kanisa zima lisiharibike…

Utauliza ni wapi maandiko yanasema hivyo?

1Wakorintho 5:1 “Yakini habari imeenea ya kuwa kwenu kuna zinaa, na zinaa ya namna isiyokuwako hata katika Mataifa, kwamba mtu awe na mke wa babaye.

2 Nanyi mwajivuna, wala hamkusikitika, ili kwamba aondolewe miongoni mwenu huyo aliyetenda jambo hilo.

3 Kwa maana kweli, nisipokuwapo kwa mwili, lakini nikiwapo kwa roho, mimi mwenyewe nimekwisha kumhukumu yeye aliyetenda jambo hilo, kana kwamba nikiwapo.

4 Katika jina la Bwana wetu Yesu, ninyi mkiwa mmekusanyika pamoja na roho yangu, pamoja na uweza wa Bwana wetu Yesu;

5 kumtolea Shetani mtu huyo, ili mwili uadhibiwe, ili na roho iokolewe katika siku ya Bwana Yesu.

6 Kujisifu kwenu si kuzuri. Hamjui kwamba chachu kidogo hulichachusha donge zima

9 Naliwaandikia katika waraka wangu, kwamba msichangamane na wazinzi.

10 Sisemi msichangamane kabisa na wazinzi wa dunia hii, au na wenye kutamani, au na wanyang’anyi, au na wenye kuabudu sanamu; maana hapo ingewalazimu kutoka katika dunia.

11 Lakini, mambo yalivyo, naliwaandikia kwamba msichangamane na mtu aitwaye ndugu, akiwa ni mzinzi au mwenye kutamani au mwenye kuabudu sanamu au mtukanaji au mlevi au mnyang’anyi; mtu wa namna hii msikubali hata kula naye.

12 Maana yanihusu nini kuwahukumu wale walio nje? Ninyi hamwahukumu hao walio ndani?

13 Lakini hao walio nje Mungu atawahukumu. Ninyi mwondoeni yule mbaya miongoni mwenu.”

Soma pia..

2Wathesalonike 3:14 “Na ikiwa mtu awaye yote halishiki neno letu la waraka huu, jihadharini na mtu huyo, wala msizungumze naye, apate kutahayari; 15 lakini msimhesabu kuwa adui, bali mwonyeni kama ndugu”.

Hivyo kuna hatari sana ya kufanya dhambi za makusudi baada ya kuujua ukweli..Tunakuwa tunakabidhiwa shetani ashughulike na sisi, Hivyo tujihakiki na Bwana atuepushe na hayo yote.

Maran atha!

Mada Nyinginezo:

Je! mtu aliyeokoka anaruhusiwa kumiliki Lodge ambayo ina Bar ndani yake?

Mahuru ndio nini?

Kwanini Mungu alisema hakuna mtu awazaye kuuona uso wake akaishi?

Je Mtu anaweza kusema uongo, Na Mungu akambariki?

Nini maana ya mstari huu: (Mtu ambarikiye mwenzake kwa sauti kuu asubuhi na mapema; Itahesabiwa kuwa ni laana kwake.Mithali 27:14 )?

Maana ya huu mstari ni ipi? Mithali 14:4 ‘Zizi ni safi ambapo hapana ngombe;bali nguvu za ngombe zaleta faida nyingi’.

Rudi Nyumbani:

Print this post

NAMI NINAZO FUNGUO ZA MAUTI, NA ZA KUZIMU.

Ufunuo 1: 17 “…Usiogope, Mimi ni wa kwanza na wa mwisho,

18 na aliye hai; nami nalikuwa nimekufa, na tazama, ni hai hata milele na milele. Nami ninazo funguo za mauti, na za kuzimu”.

Hayo ni Maneno ya Bwana wetu Yesu Kristo, akiliambia kanisa.. Sasa ukiona mpaka Bwana Yesu anasema anazo funguo za mauti, na kuzimu, ni dhahiri kuwa hapo mwanzo hakuwa nazo, zilikuwa kwa mwingine..Na huyo si mwingine zaidi ya Ibilisi.

Kumbuka Tahadhari ya kwanza Mungu aliyowapa Adamu na Hawa pale Edeni, kuhusu kula Tunda, haikuwa kwamba matokeo yake watakuwa uchi, au watajua mema na mabaya au watakula kwa jasho, au watazaa kuwa uchungu . Hapana, bali tahadhari aliyowapa ya kwanza na ya mwisho ilikuwa ni kuwa WATAKUFA(‘KIFO’)..Siku watakapokula matunda ya mti ule watakufa..akimaanisha watakufa kweli kweli..sio kwamba watakufa halafu siku moja watafufuka hapana, bali watakufa moja kwa moja..

Kwasababu Mungu alimwona muhasisi wa kifo hicho pale Edeni, Lakini wazazi wetu hawakuzingatia hilo badala yake wakala, Na matokeo yake ndio yale tuliyoyaona yalifuata baada ya pale..watu wakawa na makao mengine, baada ya pale yaliyoitwa KUZIMU. Chini ya mungu wao mpya aliyeitwa Ibilisi.

Na ndio maana katika agano la kale, hakukuwa na mtu aliyekuwa na uhakika wa maisha baada ya kifo, ni waisraeli tu ndio walifahamu hilo, nao si wote, isipokuwa wale tu waliokuwa wanafuatailia masuala ya Mesiya, ambaye alitabiriwa kuwa huko mbele atakuja kuwafufua wafu, lakini wengine waliosalia hawakujua hilo…

Na ndio maana tena utaona kulikuwa na mapambano makali kati ya mafarisayo na masadukayo, wengine waliamini kuna ufufuo wa wafu, na wengine hawakuamini hicho kitu (Soma, Matendo 4;1-2,23:7-8, Marko 12:18)..Ni kwasababu gani? Ni kwasababu suala la wafu kufufuliwa lilikuwa si jambo lililoandikwa kwa uwazi sana katika maandiko kama wengi wanavyodhani.. isipokuwa tu waliotambua jambo hilo ni wale waliokuwa wanafuatilia habari za Mesiya kuwa atakuja kufanya jambo hilo.

Kwahiyo wakati wote huo watu walikuwa wametawaliwa na roho ya mauti ya ibilisi.

Warumi 5:14 “walakini mauti ilitawala tangu Adamu mpaka Musa, nayo iliwatawala hata wao wasiofanya dhambi ifananayo na kosa la Adamu, aliye mfano wake yeye atakayekuja”.

Unaona wakati huo wote shetani alikuwa na funguo hizo, alikuwa wakati mwingine anao uwezo hata wa kuwaendea wafu walio watakatifu na kuzungumza nao, soma habari za samweli(1Samweli 28)..

Lakini sasa Kristo alipokuja alipindua kila kitu,(majira yakageuka), kwanza aliiondoa hofu ya mauti ambayo ilikuwa imewatawala wanadamu kwa muda mrefu tangu zamani..

Waebrania 2:14 “Basi, kwa kuwa watoto wameshiriki damu na mwili, yeye naye vivyo hivyo alishiriki yayo hayo, ili kwa njia ya mauti amharibu yeye aliyekuwa na nguvu za mauti, yaani, Ibilisi,

15 awaache huru wale ambao kwamba maisha yao yote kwa hofu ya mauti walikuwa katika hali ya utumwa”.

Na pili akaiteka ile Kuzimu iliyokuwa chini ya shetani, ambayo ndio ilikuwa makao ya wafu wote…

Na ndio maana siku ile alipokufa tu, utasoma makaburi yalipasuka na watakatifu wengi wakatoka makaburini

Mathayo 27:51 “Na tazama, pazia la hekalu likapasuka vipande viwili toka juu hata chini; nchi ikatetemeka; miamba ikapasuka;

52 makaburi yakafunuka; ikainuka miili mingi ya watakatifu waliolala;

53 nao wakiisha kutoka makaburini mwao, baada ya kufufuka kwake, wakauingia mji mtakatifu, wakawatokea wengi”.

Tangu huo wakati hadi leo ibilisi hajui wafu wapo wapi na wanafanya nini saa hii, anachojua tu, ni kuwa wale watakatifu wapo upande wa PEPO(Paradiso) na wale waovu wapo sehemu ya mateso (Jehanum)..Hana uwezo wa kuleta mzimu wa mtu yeyote aliyekufa kwasababu sasahivi Kristo ndiye anayewamiliki walio hai na waliokufa soma Warumi 14:9. Kwahiyo hivyo vinavyoonekana na watu vyenye sura kama za wapendwa waliokufa..kiuhalisia sio wale watu wenyewe, bali ni roho tu za mapepo zilizovaa sura za watu waliokufa…

Kristo sasa ameshashikilia mamlaka yote, ya mbinguni, ya duniani na ya kuzimu..Haleluya.

Hivyo ikiwa wewe ni mtakatifu, kama utakufa leo basi ujue roho yako na nafsi yako itakwenda sehemu salama, yenye raha na pumziko la kweli, mahali pasipoelezeka panapoitwa Pepo, lakini wewe ambaye ni mwenye dhambi, ukifa leo, shetani hakuchukui bali utakayekuchuwa na Mungu mwenyewe na kwenda kukutupa katika jehanamu ya moto ukingoja hukumu ya siku ile ya mwisho..

Unatanga tanga nini kwa waganga wa kienyeji? Hao hawatakusaidia chochote, unawatafuta wanadamu, hao nao hawawezi kukuondolea hofu ya mauti na mashaka uliyonayo sasa, kwamba ukifa utakwenda wapi..Anayeweza kufanya hivyo ni Kristo tu peke yake, mwenye funguo za mauti na kuzimu.Yeye ndiye atakayeweza kukufanya uwe huru na hofu ya kifo, kiasi kwamba hata ikitokea unakufa leo, utakuwa na uhakika kuwa roho yako imekwenda sehemu salama. Ukingojea siku ile kuu ya kwenda mbinguni kwa Baba.

Hivyo leo mpe Kristo maisha yako kama bado hujampa, vivyo hivyo kama ni vuguvugu huu ni wakati wa kuwa moto!.. Tubu dhambi zao kwa kumaanisha kuziacha, hizi ni nyakati za mwisho, parapanda italia wakati wowote, na Yesu atawafufua kwanza wale waliokufa katika haki nao kwa pamoja na sisi tulio hai tutakwenda kumlaki mawinguni,..lakini jiulize wewe mwenye dhambi utakuwa wapi siku hiyo?..Au ukifa leo hii ni nani atayekusaidia huko uendako? Shetani anaivizia roho yako kwasababu anajua ukifa katika dhambi ni umepotea kwelikweli hata yeye mwenyewe hata kuona milele…Hivyo acha leo ulevi, wizi, rushwa, anasa, uasherati, vipodozi unavyopaka, vimini unavyovaa, matusi unayotukana na mambo yote yanayofanana na hayo..Na upokee Roho Mtakatifu ambaye ni ahadi kwetu tutakaomwamini Yesu.

Uamuzi ni wako, tafakari tena kisha chagua uzima. Wokovu ni bure kwa wote wanaouhitaji..Kristo anaokoa kweli.

Shalom.

Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema, na pia kama utapenda tuwe tunakutumia masomo haya kwa njia ya email yako au Whatsapp tutumie ujumbe kwenye box la maoni chini au piga namba hii +255 789001312

Mada Nyinginezo:

TOFAUTI KATI YA HEKALU, SINAGOGI NA KANISA NI IPI?

Nifanye nini ili niondokane na Hofu maishani mwangu?

SI KWA FAIDA YA MWENYEZI, BALI KWA FAIDA YETU.

MWAKA WA BWANA ULIOKUBALIWA.

NAO WAKADHANI YA KUWA YUMO KATIKA MSAFARA;

Nini maana ya maneno haya ya Bwana? “Nami nikiinuliwa juu ya nchi,NITAWAVUTA WOTE KWANGU”(Yohana12:32).

Rudi Nyumbani:

Print this post

MAOMBI YA VITA

Maombi ya vita yakoje?..Je! ni lazima kuomba maombi ya vita?

Maombi yamegawanyika katika sehemu kuu 3

  1. Maombi ya shukrani
  2. Maombi ya kuwasilisha haja mbele za Mungu.
  3. Na Maombi ya KUTANGAZA.

Katika aina aina ya kwanza ya maombi ni ile ya KUSHUKURU, Ambapo mwamini atapiga magoti au atasimama na kumshukuru Mungu kwa mema yote anayomtendea yeye binafsi, na familia yake, na jamaa zake, na Taifa lake…hali kadhalika na kwa kila kitu ambacho anastahili kukishukuru mbele za Mungu. Na maombi haya ndio maombi ya muhimu kuliko yote, na yanayopaswa kuchukua muda mrefu kuliko maombi mengine yoyote.

Aina ya pili ya maombi ni ya kuwasilisha haja mbele za Mungu…Haya ni yale ambayo mtu atapiga magoti na kumwomba Mungu hitaji fulani amtimizie, hilo linaweza kuwa hitaji lake binafsi au la mtu mwingine au la kanisa au la Taifa.

Na Aina ya tatu na ya mwisho ya maombi ni maombi ya KUTANGAZA…Katika aina hii ya mwisho ya maombi ndipo panapopatikana maombi ya vita kama yanavyotajwa na wengi, yanaangukia katika kundi hili.

Katika maombi ya kutangaza..hapa ndipo mtu atatumia kinywa chake na mamlaka aliyopewa kuamuru na kuamrisha kila nguvu zote za giza, zilizo kinyume na nguvu za Mungu zipate kuanguka chini kwa jina la Yesu..

Mfano wa maombi ya kutangaza ni maombi ya kutoa pepo. Tunapoamuru pepo amtoke Mtu au kitu kwa jina la Yesu hapo tumetangaza kile kitu kifunguliwe kwa mamlaka ya kimbinguni, na hivyo ni lazima kitii.

Hali kadhalika kama kuna maneno maovu, au mitego ya adui, au kuna mipango na mikakati iliyopangwa na wanadamu au watumishi wa shetani dhidi yako au ndugu,au jamaa au kanisa au Taifa, kwa kutumia vinywa vyetu na kwa jina la YESU, tunaweza kuifuta mipango hiyo, na ratiba hizo na mikakati hiyo, na ikafutika sawasawa na tulivyotamka/kutangaza.

Sasa maombi haya ndio yanayojulikana na wengi kama MAOMBI YA VITA..Mwamini anaweza kutumia muda wa kutosha kutamka baraka juu yake na kwa ndugu zake na kwa kanisa la Kristo kwa jina la Yesu, hali kadhalika anaweza kutangaza kufuta kila mipango ya ibilisi iliyopangwa juu yake, juu ya familia yake, ndugu zake, kazi zake, afya yake, kanisa lake, nchi yake na kila kitu kinachohusiana na yeye. Maombi haya yanaweza kuchukua masaa kadhaa kwa kadiri mtu alivyojaliwa kuomba, na yanaweza kufanyika kila siku. Na pia ni maombi ya muhimu sana. Na maombi haya yanahusisha kutoa au kupaza sauti kwa nguvu…Huwezi kukemea pepo lililopo ndani ya mtu kimoyomoyo…Katika biblia Bwana wetu Yesu, pamoja na Mitume walitamka kwa nguvu na pepo wakawatoka watu…Bwana alipoulaani ule mtini, alitoa sauti kutoka katika kinywa chake..Hali kadhalika tunapozilaani kazi za Adui shetani, ni lazima sauti zitoke katika vinywa vyetu. Sio lazima itoke sauti kama kilio, lakini angalau sauti isikike..Na ndivyo shetani na mapepo yake tutakavyoyaangusha chini..

Maombi haya hayana muda maalumu wa kuomba…Ni vizuri zaidi kuomba kwa pamoja kama kikundi, au peke yako binafsi wakati wa utulivu.

Kwa kina kuhusu Aina tatu hizi za maombi Mwishoni kabisa mwa somo hili chini kuna somo lenye kichwa cha FAIDA ZA MAOMBI. Lifungue hilo ulisome kwa msaada wa Roho Mtakatifu naamini utapata kuongeza kitu juu ya vile unavyovijua.

Bwana akubariki.

Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema, na pia kama utapenda tuwe tunakutumia masomo haya kwa njia ya email yako au Whatsapp tutumie ujumbe kwenye box la maoni chini au piga namba hii +255 789001312


Mada Nyinginezo:

FAIDA ZA MAOMBI.

JE MOYO WAKO NI MNYOFU MBELE ZA MUNGU

Je kuzalishwa na mkunga wa kiume ni dhambi?

KIJITO CHA UTAKASO.

MKARIBIE BWANA ZAIDI ILI UFANYIKE NGUZO.

KUTUBU SIO KUOMBA REHEMA.

Rudi Nyumbani:

Print this post

Hamtaimaliza miji ya Israeli hata ajapo mwana wa Adamu?

Bwana alimaanisha nini kusema “Hamtaimaliza miji ya Israeli hata ajapo mwana wa Adamu”


Tusome;

Mathayo 10:23 “Lakini watakapowafukuza katika mji huu, kimbilieni mwingine; kwa maana ni kweli nawaambia HAMTAIMALIZA MIJI YA ISRAELI HATA AJAPO MWANA WA ADAMU”

JIBU: Ukiusoma mstari huo kuanzia juu kabisa, yaani kuanzia mstari wa kwanza…Utaona ni Habari inayohusu tendo la Bwana Yesu kuwatuma wanafunzi wake kwenda kuhubiri injili katika miji ya Israeli…Na utaona alipowaagiza wakahubiri aliwapa na baadhi ya maagizo au masharti, kwamba wasichukue chochote na pia wawe wavumilivu kwa watakayoyapitia huko..Lakini mwishoni kabisa mwa maagizo tunaona Bwana anawaambia…“hamtaimaliza miji ya Israeli hata ajapo mwana wa Adamu”..

Sasa swali linalojitengeneza kwenye vichwa vyetu hapo ni kwamba…mbona Bwana Mitume walikuwa wameshaimaliza hiyo miji na Yesu bado alikuwa hajarudi?..ina maana mpaka leo injili haijasambaa kwenye miji yote ya Israeli ndio maana Bwana hajarudi mpaka leo?.

Jibu rahisi la swali hili tunaweza kulipata kwenye Habari kama hii hii katika kitabu cha Luka…Tusome,

Luka 10:1 “Basi, baada ya hayo Bwana aliweka na wengine, sabini, akawatuma wawili wawili wamtangulie kwenda kila mji na kila mahali alipokusudia kwenda mwenyewe.

2 Akawaambia, Mavuno ni mengi, lakini watenda kazi ni wachache; basi mwombeni Bwana wa mavuno apeleke watenda kazi katika mavuno yake.

3 Enendeni, angalieni, nawatuma kama wana kondoo kati ya mbwa-mwitu.

4 Msichukue mfuko, wala mkoba, wala viatu; wala msimwamkie mtu njia”

Tuvichunguze baadhi ya vipengele katika mstari huo wa kwanza ambavyo ndivyo vitakavyotupa dira ya kuelewa Habari nzima….katika mstari wa kwanza biblia inasema… “Bwana aliweka na wengine, sabini, AKAWATUMA WAWILI WAWILI WAMTANGULIE kwenda kila mji na kila mahali alipokusudia kwenda mwenyewe”…Zingatia hilo neno “WAMTANGULIE”..Kama wewe ni mswahili mzuri utaelewa maana ya neno “kutangulia” ni nini…kutangulia maana yake ni mtu anakwenda mahali kisha wewe unafuata baadaye…yaani anawahi kufika kule kabla wewe kufika…hiyo ndiyo maana ya kutangulia…

Hivyo mstari huo una maana kuwa “hao wanafunzi sabini na wale 12 Bwana aliokuwa anawatuma kwenda huko katika miji ya Israeli hakuwatuma tu…huko wenyewe…bali Bwana aliwaahidi kwamba atawafuata, hivyo aliwatuma tu kama wamtangulie.”

Ili kuelewa vizuri tafakari tena kamfano haka… “Umemwagiza mfanyakazi wako atangulie asubuhi na mapema sehemu ya kazi kuendelea na kazi, na ukamwambia hatamaliza kazi zote kabla ya wewe kufika hapo ofisini, maana yake utafika kabla hata hajamaliza kazi zote”.. Ndicho Bwana alichowaambia wanafunzi wake, kwamba huko wanakwenda naye pia atakuja kabla hawajaimaliza miji yote ya Israeli (Hilo ni neno la Faraja)…Na kweli aliiungana nao baadaye hakuwaacha yatima…

Sasa kuna jambo moja la kujifunza hapo…Kwamba Desturi ya Bwana ilikuwa hafiki mahali kabla ya kutuma kwanza wajumbe wake wakamtengenezee njia…Maana yake kabla ya yeye kuja mahali anatuma kwanza watumishi wake wakahubiri injili..Ndivyo alivyofanya kwa Yohana Mbatizaji…yeye alitumwa kumtengenezea Bwana njia na kuiandaa mioyo ya watu kabla Bwana mwenyewe hajaanza kuhubiri..ili atakapoanza kuhubiri vile Bwana atakavyohubiri visiwe ni vitu vigeni sana kwa watu wake.(kasome Yohana 10:41-42, na Luka 1:17).

Utaona sehemu zote kabla Bwana hajaenda mahali huwa anatuma wanafunzi wake kwanza na baadaye anaungana nao.. (kasome Luka 9:52-54, Marko 14:12-18, Marko 11:1-4)..

Ndugu Mpendwa hata sasa, Bwana bado anatuma watu wake kuitengeneza njia yake…Umesikia injili mara ngapi?, kila mahali upitapo, mtaani, kwenye magari, mashuleni, unapofanyia kazi?..lakini unadharau kwasababu labda anayekuhubiria umemzidi kipato, au umemzidi elimu, au umri?..Lakini lisikie hili neno ambalo Bwana Yesu alilisema..

Marko 9:37 “Mtu akimpokea mtoto mmoja wa namna hii kwa jina langu, anipokea mimi; na mtu akinipokea mimi, humpokea, si mimi, bali yeye aliyenituma”

Hako katoto unakokadharau sasa, huyo uliyemzidi elimu, pengine na kipato…huyo ambaye hata maandiko hawezi kuyatamka vizuri na anakuhubiria utubu umgeukie Mungu lakini unamchukulia unavyojua wewe…Bwana Yesu ambaye sasa hivi yupo mbingu za mbingu anamheshimu, siku ile tutaonyeshwa tumemkataa yeye Dhahiri.

Bwana atusaidie.

Kama bado hujampa Yesu Kristo Maisha yako, tupo ukingoni sana mwa siku za mwisho, ambapo ghafla tu unyakuo utapita na watakatifu watatoweka….waliobaki hawatasikia tena usumbufu wa mahubiri wanayohubiriwa sasa..watakuwa wamefungua jalada lingine la maisha..na watakatifu vivyo hivyo..Kwahiyo sio wakati wa kukaa nje..Mlango wa Safina unakaribia kufungwa, waasherati,walevi, wezi, watukanaji, watazamaji picha chafu mitandaoni, wanaokula rushwa, na wanaofanya kila aina ya machafuko biblia inasema sehemu yao itakuwa ni katika lile ziwa la moto. Ingia leo ndani ya Safina ya Yesu, wokovu unapatikana bure.

Maran atha!

Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema, na pia kama utapenda tuwe tunakutumia masomo haya kwa njia ya email yako au Whatsapp tutumie ujumbe kwenye box la maoni chini au piga namba hii +255 789001312

Mada Nyinginezo:

Wewe u nabii yule akajibu la!..swali huyu ‘nabii yule’ ni nani?

JE! WEWE NI MWAKILISHI MWEMA?

Kwanini Bwana alisema Hakuna aliye mwema ila mmoja?

Kwanini Bwana alisema Hakuna aliye mwema ila mmoja?

Habari ile ya Pilato kuchanganya zile damu za wayahudi na pamoja na dhabihu zao,(Luka 13) ilihusu nini?

Rudi Nyumbani:

Print this post