Haijalishi utaudhiwa na watu kiasi gani, haijalishi utakuwa na maadui wengi kiasi gani, lakini kamwe Mungu hawezi kuwachukia kama unavyowachukia wewe.
Jicho lako linavyowaona wewe ni tofauti na Mungu anavyowaona, wewe unatamani waangamizwe wapotee, lakini Mungu anatamani waokolewe. Wewe unatamani mabaya yawakute lakini Bwana Mungu anatamani watubu ili wasipatwe na mabaya. Ukiifahamu vyema tabia hiyo ya Mungu, utaacha kupoteza muda, kuwatakia shari maadui zako. Badala yake utawaombea Bwana azidi kuwapa neema watubu, na madhara yao yasikupate.
Lakini ukiwaombea kwa Mungu wafe!.utakuwa unapoteza muda, kwasababu kabla hawajawa maadui zako, Mungu alijua kuwa watakuja kuwa maadui zako na akawaumba hivyo hivyo.. angekuwa na hasira nao sana, kama ulizonazo wewe, angewaangamiza kitambo sana, au hata asingewaumba kabisa.
Kwahiyo mpaka unaona wameumbwa fahamu kuwa tayari ni mpango kamili wa Mungu wao wawepo duniani, na tena Mungu kawaumba kwasababu anawapenda.
Ni maneno magumu hayo lakini ndio ukweli.. Kama mtu fulani unamchukia kwasababu kakusengenya, na unatamani Mungu amwue, hayo maombi yako yatafika ukingoni!..kwasababu Mungu hatamwua kama unavyotaka wewe. Lakini ukitaka maombi yako yawe na nguvu ni heri uombe Bwana Mungu ampe roho ya kutubu, hapo utakuwa umeomba sawasawa na mapenzi yake.
Kama kuna mtu amekufanyia jambo baya, au anakufanyia mabaya yanayokuudhi sana. Na wewe ukaenda kuketi kuomba kwa Bwana Mungu kwamba amwue na kumpoteza kabisa, nataka nikuambie hayo maombi yako unapoteza muda. Kwasababu Bwana Mungu hakumuumba ili amwue, bali aifikilie toba na kubadilika… Ndio lengo lake!..kamwe huwezi kumfundisha Mungu ubaya.
Ezekieli 18: 23 “Je! Mimi ninafurahia kufa kwake mtu mwovu? Asema Bwana MUNGU; si afadhali kwamba aghairi, na kuiacha njia yake, akaishi?”
2Petro 3:9b “….bali huvumilia kwenu, maana hapendi mtu ye yote apotee, bali wote wafikilie toba”.
Mtu fulani kakuibia mali yako ambayo ni ya thamani, halafu unapiga magoti ukiomba kwamba Mungu amuue na kumuangamiza huko alipo, hayo maombi hayafiki popote. Maombi yenye tija na yanayompendeza Mungu, ni haya>> “Bwana wasamehe kwa kuwa hawajui watendalo”.
Mtu fulani kakuendea kwa mganga ili upatikane na madhara fulani, na wewe unapiga magoti na kusema “Bwana waangamizwe na kufa kabisa, hata maiti zao zisionekane”..huku ukinukuu mstari huu katika agano la kale Kutoka 22: 18 “Usimwache mwanamke mchawi kuishi”. Mbona unapomfumania mkeo, au mumeo kwenye uzinzi hunukuu huu mstari wa Agano la kale na kuutumia??.
Kumbukumbu 22: 22 “Akifumaniwa mtu mume amelala na mwanamke aliyeolewa na mume, na wafe wote wawili, mtu mume aliyelala na mwanamke, na yule mwanamke naye; ndivyo utakavyoondoa uovu katika Israeli”.
Au sio Mungu mmoja aliyezungumza hayo maneno??… Kama ni Mungu mmoja aliyesema usimwache mwanamke mchawi kuishi, ndio huyo huyo aliyesema mtu akishikwa kwenye uzinzi awe mwanamke au mwanaume sharti auawe, (tena amezungumza hayo kwa kinywa cha Nabii huyo huyo mmoja, Musa)..basi kwanini unachukua mstari mmoja na kuacha mwingine??.
Hivyo ni vyema kufahamu utendaji kazi wa Mungu katika agano la kale ni tofauti na utendaji kazi wake katika agano jipya..Katika agano la kale, kutokana na ugumu wa mioyo ya watu, watu walipewa ruhusa ya kuua wazinzi, kuua waabudu sanamu wote wanaoziabudu nje na kumwabudu Mungu wa Israeli, walipewa pia ruhusa ya kuwapiga kwa mawe wachawi, na watu wote wenye pepo waliokuwa wanaishi katika nchi, walipewa ruhusa ya kuua watu waliomlaani/kumtukana Mungu, walipewa ruhusa ya kuwatenga watu wenye ukoma n.k. Na hiyo yote ni kutokana na ugumu wa mioyo yao, na wala si kwasababu ulikuwa ni mpango kamili wa Mungu. Mpango kamili wa Mungu ulikuja kuletwa na Bwana Yesu pale aliposema..
Mathayo 5:21 “Mmesikia watu wa kale walivyoambiwa, Usiue, na mtu akiua, itampasa hukumu.
22 Bali mimi nawaambieni, Kila amwoneaye ndugu yake hasira itampasa hukumu; na mtu akimfyolea ndugu yake, itampasa baraza; na mtu akimwapiza, itampasa jehanum ya moto”.
Mathayo 5.38 “Mmesikia kwamba imenenwa, Jicho kwa jicho, na jino kwa jino;
39 Lakini mimi nawaambia, Msishindane na mtu mwovu; lakini mtu akupigaye shavu la kuume, mgeuzie na la pili.
40 Na mtu atakaye kukushitaki na kuitwaa kanzu yako, mwachie na joho pia.
41 Na mtu atakayekulazimisha mwendo wa maili moja, nenda naye mbili”.
Mathayo 5:43 “Mmesikia kwamba imenenwa, Umpende jirani yako, na, Umchukie adui yako;
44 lakini mimi nawaambia, Wapendeni adui zenu, waombeeni wanaowaudhi,
45 ili mpate kuwa wana wa Baba yenu aliye mbinguni; maana yeye huwaangazia jua lake waovu na wema, huwanyeshea mvua wenye haki na wasio haki”.
Kwahiyo hakuna jino kwa jino katika Ukristo, wala hakuna kumpiga kwa mawe mtu yeyote anayefumaniwa katika uzinzi, wala hakuna kumuua mchawi yeyote, wala haturuhusiwi kuwachukia maadui zetu. Haja za mioyo yetu kwa Mungu, na sala zetu, ni kwamba Bwana atuepushe na madhara yote yanayoweza kufanywa na wao wanaotuchukia, na Bwana azifedheheshe kazi zao, ili mwisho wanapoona kuwa hazina madhara yoyote kwetu, watubu na kumfuata Mungu wetu sisi, hilo ndio lengo la kwanza la Mungu. Lakini si wafe katika dhambi zao hizo.
Kwahiyo huwezi kumfundisha Mungu uovu, yeye atabaki kuwa mkamilifu siku zote, anawaangazia jua lake waovu na wema, huwezi kumbadilisha yeye kuwa hivyo, hata uombe maombi ya namna gani, isipokuwa anachokitaka kwetu ni sisi kuwa kama yeye, tuwe na huruma kama yeye, tuwe wenye rehema kama yeye, tuwe wenye fadhili kama yeye, tuwe watakatifu kama yeye.
Mathayo 5:46 “Maana mkiwapenda wanaowapenda ninyi mwapata thawabu gani? Hata watoza ushuru, je! Nao hawafanyi yayo hayo?
47 Tena mkiwaamkia ndugu zenu tu, mnatenda tendo gani la ziada? Hata watu wa mataifa, je! Nao hawafanyi kama hayo?
48 Basi ninyi mtakuwa wakamilifu, kama Baba yenu wa mbinguni alivyo mkamilifu”.
Bwana atubariki wote.
Kama hujampokea Yesu, jitafakari mara mbili unasubiri nini?. Injili si habari za kuburudisha kama tunazozisoma katika magazeti, bali ni ushuhuda, maana yake kila unapoisoma mahali au kuisikia mahali, inarekodiwa kuwa ulishawahi kuisikia, kwahiyo kama ukiipuuzia na kuiacha, na yule mwovu akaja kuchukua kile kilichopandwa ndani yako, kuna hatari kubwa sana itakayokukuta baada ya maisha haya.
Hivyo mpokee leo Kristo leo maishani mwako na wala usingoje kesho, kwasababu hujui yatakayozaliwa ndani ya siku moja, biblia inasema hivyo katika Mithali 27:1, na pia katafute ubatizo sahihi wa maji tele (Yohana 3:23) na kwa Jina la Yesu Kristo (Matendo 2:38),kama bado hujabatizwa ubatizo sahihi. Na Roho Mtakatifu atashuka juu yako kukuongoza katika kweli yote.
Maran atha!
Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema,
Kwa maombezi/Ratiba za ibada/ Ushauri/ Maswali.
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312
pia kama utapenda uyapate mafundisho haya kwa njia ya Whatsapp au email basi tutumie ujumbe kwenye namba hizo hizo. jiunge na channel yetu Kwa kubofya hapa >> WHATSAPP
Mada Nyinginezo:
Nakusalimu katika jina lipitalo majina yote la Bwana wetu Yesu Kristo. Karibu tena tujifunze maneno ya uzima..
Wakati ule wanamsulibisha Bwana Yesu, walipoona jua linakaribia kuchwa na waliowasulibisha bado hawajafa, wayahudi walienda kumuomba Pilato awavunje miguu ili waviharakishe vifo vyao, ikumbukwe kuwa kulingana na sheria za wayahudi ilikuwa ni tendo la kinajisi, kuiacha maiti ya mhalifu msalabani mpaka jioni ya sabato,
Hivyo njia waliyoiona inafaa ni kwenda kumuomba Pilato awavunje miguu yao, ili kusaidia wafe haraka, kwani kwa kuvunjwa kule kungewapelekea damu nyingi kuvuja kwa ndani, na vilevile kushindwa kunyanyua miguu juu, ambayo huwa kwa kawaida inarahisisha kupumua. Hivyo kwa kitendo kile cha kuwavunja ingewachukua tu dakika kadhaa mpaka wafe.
Lakini kama ingekuwa sio kwa ajili ya torati yao, kwa kawaida uuaji wa kirumi huwa mtu haondolewi pale msalabani mpaka afe mwenyewe. Na hiyo inaweza kuchukua siku kadhaa, na wanafanya hivyo kwa makusudi kabisa ili mtu huyo afe kifo cha mateso, wahakikishe mpaka wale tai wala mizoga wanashuka juu yake kuila maiti yake ndio wanamtoa.
Sasa kama tunavyojua habari ni kwamba waliwavunja wale wahalifu wote miguu lakini walipofika kwa Bwana Yesu ili wamvunje walimwona tayari ameshakwisha kufa, hivyo hawakumvunja mfupa wake hata mmoja badala yake wakamchoma mkuki ubavuni kuhakikisha kifo chake kama ni kweli.. Tusome..
Yohana 19:31 “Basi Wayahudi, kwa sababu ni Maandalio, miili isikae juu ya misalaba siku ya sabato, (maana sabato ile ilikuwa siku kubwa), walimwomba Pilato miguu yao ivunjwe, wakaondolewe.
32 Basi askari wakaenda, wakamvunja miguu wa kwanza, na wa pili, aliyesulibiwa pamoja naye.
33 Lakini walipomjia Yesu na kuona ya kuwa amekwisha kufa, hawakumvunja miguu;
34 lakini askari mmojawapo alimchoma ubavu kwa mkuki; na mara ikatoka damu na maji.
35 Naye aliyeona ameshuhudia, na ushuhuda wake ni kweli; naye anajua ya kuwa anasema kweli ili ninyi nanyi mpate kusadiki.
36 Kwa maana hayo yalitukia ili andiko litimie, Hapana mfupa wake utakaovunjwa”.
SASA NI KWANINI MIFUPA YAKE HAIKUVUNJWA? KULIKUWA NA ULAZIMA GANI WA JAMBO HILO KUPEWA UZITO KATIKA MAANDIKO?..
Sababu zipo mbili.
Ikumbukwe kuwa wakati ule wana wa Israeli walipokuwa wanatoka Misri, Mungu alipowapa maagizo ya kumchinja yule pasaka(kondoo) na kisha damu yake waipake kwenye miimo ya milango yao ili yule malaika atoaye roho akipita asiingie milangoni mwao, Na tunaona waliambiwa wamuandae pasaka huyo akiwa hana kasoro yoyote, na pia watakapomla asivunjwe mfupa wake wowote.
Kutoka 12:45 “Akaaye kwenu hali ya ugeni, na mtumishi aliyeajiriwa, wasimle pasaka.
46 Na aliwe ndani ya nyumba moja; usiichukue nje ya nyumba nyama yake yo yote; WALA MSIVUNJE MFUPA WAKE UWAO WOTE”.
Unaona, hivyo Kristo kutovunjwa mifupa yake, ilikuwa ni kumthibitisha kuwa yeye ndiye yule pasaka wetu kweli kweli ( yaani mwanakondoo) , atakayechukua dhambi za watu sawasawa na Yohana mbatizaji alivyoonyeshwa katika Yohana 1:29
2) Sababu ya Pili ilikuwa ni kuonyesha kuwa mwili wa Kristo hauvunjwi.
Pamoja na kupitia mateso yote yale msalabani, kuteswa na kupigwa, kudhihakiwa, kugongelewa misumari, lakini bado viungo vyake viliendelea kushimana vilevile, havikuachana hata kimoja. Hiyo inafunua rohoni kuwa sisi kama viungo vya Kristo kama vile biblia inavyotuambia katika..Waefeso 5:30
“Kwa kuwa tu viungo vya mwili wake”.
Kwamba tunapaswa tushikamane kwa umoja na upendo. Hata kama tutapitia shida au dhiki nyingi kiasi gani. Tukumbuke kuwa mwili wa Kristo huwa hauvunjwi, miili mingine ndiyo inayovunjwa lakini wa Kristo huwa hauvunjwi.
ikiwa Imani yetu ni mmoja, ubatizo wetu ni mmoja, Bwana wetu ni mmoja, hatupaswi kutengana kwasababu zisizokuwa na maana, hatupaswi kuwekeana matabaka, au vinyongo, au viburi bali tushikamane kwa umoja ili tuujenge mwili wa Kristo.
Ni wajibu wa kila mmoja wetu kilitimiza hilo agizo kama Bwana Yesu mwenyewe alivyotuambia.
Yohana 17:22 “Nami utukufu ule ulionipa nimewapa wao; ili wawe na umoja kama sisi tulivyo umoja”.
Hivyo tuweke akilini kuwa mtu yeyote anayeuvunja mwili wa Kristo, anakwenda kabisa kinyume na kanuni ya Mungu kwenye kanisa lake..
Shalom
Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema,
Kwa maombezi/Ratiba za ibada/ Ushauri/ Maswali.
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312
pia kama utapenda uyapate mafundisho haya kwa njia ya Whatsapp au email basi tutumie ujumbe kwenye namba hizo hizo.
Mada Nyinginezo:
Maana ya neno “Mintarafu” ni “kuhusiana na”. Kwamfano ukitaka kutamka sentesi hii >> “sifahamu chochote kuhusiana na ujio wa pili wa Kristo” …. unaweza kusema… “Sifahamu chochote mintarafu ujio wa pili wa Kristo”..Hivyo neno mintarafu linasimama kuwakilisha neno “kuhusiana na”.
Katika biblia takatifu yenye vitabu 66, neno hilo limeonekana mara mbili tu. Na mara zote hizo mbili ni ndani ya kitabu kimoja cha Zaburi.
Zaburi 17:4 “Mintarafu matendo ya wanadamu; Kwa neno la midomo yako Nimejiepusha na njia za wenye jeuri.
5 Nyayo zangu zimeshikamana na njia zako, Hatua zangu hazikuondoshwa”.
Na pia tunasoma katika..
Zaburi 87: 5 “Naam, mintarafu Sayuni itasemwa, Huyu na huyu alizaliwa humo. Na Yeye Aliye juu Ataufanya imara. 6 Bwana atahesabu, awaandikapo mataifa, Huyu alizaliwa humo”.
Hivyo ndugu, kama hufahamu chochote kuhusiana na ujio wa pili wa Kristo, basi fahamu kuwa upo hatarini sana, ni vyema ukatafuta kwa bidii kujua saa, nyakati na majira tunayoishi.
Hizi ni siku za mwisho na Kristo yupo mlangoni. Je umejiandaa?
Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema,
Kwa maombezi/Ratiba za ibada/ Ushauri/ Maswali.
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312
pia kama utapenda uyapate mafundisho haya kwa njia ya Whatsapp au email basi tutumie ujumbe kwenye namba hizo hizo.
Mada Nyinginezo:
SWALI: Naomba kufahamu ufunuo wa mstari huu ni upi?
Kutoka 22:6 “Ukiwaka moto, na kushika penye miiba, na ngano zilizofungwa miganda, au ngano ambazo hazijakatwa, au shamba, likateketea; yeye aliyeuwasha huo moto lazima atalipa”.
JIBU: Kama vile biblia inavyotuambia katika kitabu cha Yakobo kuwa, moto ni kitu kidogo sana lakini kinawasha msitu mnene….Ndivyo ndimi zetu zilivyofananishwa na kitu kama hicho..
Yakobo 3:5 “…. Angalieni jinsi moto mdogo uwashavyo msitu mkubwa sana.
6 Nao ulimi ni moto; ule ulimwengu wa uovu, ule ulimi, umewekwa katika viungo vyetu, nao ndio uutiao mwili wote unajisi, huuwasha moto mfulizo wa maumbile, nao huwashwa moto na jehanum.
Hiyo ni kututahadharisha kuwa tunapaswa tuwe makini sana na vinywa vyetu, kwasababu madhara yatakayotokana navyo, Mungu atayadai yote mikononi mwetu, kwa mfano unapopanda mbegu za fitina katikati ya ndugu, (maneno ya uongo au ya chuki) ikapelekea mpaka wakatengana, au wakafikisha mahakamani, au wakapigana, au wakauana, ujue kuwa madhara hayo yote, Na hasara yote iliyotokea Mungu ataidai mikononi mwako.
Kumbuka moja ya mambo sita ambayo Mungu hapendezwi nayo ni pamoja na kupanda mbegu za fitina katikati ya ndugu.(Mithali 6:19).
Unapochonganisha ndoa za watu, ikapelekea mpaka wakaachana, pengine mpaka ndugu za pande zote mbili wakachukiana, watoto wakaishi bila pendo la wazazi wote, ujue kuwa wewe uliyehusika, utachukua makosa yao yote, Hutanusurika. Hata kama hukukusudia hiyo fitina ilete madhara makubwa kiasi kile.
Ukisababisha mpaka ndugu katika Bwana wakatenda dhambi kwa kujengeana chuki na vinyongo kwasababu ya usengenyaji wako, na uzushi wako, ufahamu kuwa wewe uliyehusika, utayachukua makosa yao yote.
Yakobo 3:6 “Nao ulimi ni moto; ule ulimwengu wa uovu, ule ulimi, umewekwa katika viungo vyetu, nao ndio uutiao mwili wote unajisi, huuwasha moto mfulizo wa maumbile, nao huwashwa moto na jehanum”.
Hivyo kabla hatujasema jambo fulani, au kabla hatujatoa taarifa za mtu kwa mwingine, tunapaswa tutafakari kwanza, na pia tuzithibitishe habari zenyewe, na tujiulize je kuna umuhimu wowote wa sisi kuzisema? Au kutoa siri Fulani kwa wengine? Kama upo basi ni vizuri kufanya hivyo. Lakini kama hakuna, ni heri tukazilinda ndimi zetu. Kwasababu madhara yatakayotokana na maneno yetu baadaye Mungu atayadai yote mikononi mwetu.
Hiyo ndio maana ya huo mstari;
Kutoka 22:6 “Ukiwaka moto, na kushika penye miiba, na ngano zilizofungwa miganda, au ngano ambazo hazijakatwa, au shamba, likateketea; yeye aliyeuwasha huo moto lazima atalipa”.
Shalom.
Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema,
Kwa maombezi/Ratiba za ibada/ Ushauri/ Maswali.
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312
pia kama utapenda uyapate mafundisho haya kwa njia ya Whatsapp au email basi tutumie ujumbe kwenye namba hizo hizo.
Mada Nyinginezo:
Kutoka 22:31 “Nanyi mtakuwa watu watakatifu kwangu mimi; kwa hiyo msiile nyama yo yote iliyoraruliwa huko kondeni na mnyama wa mwitu; mtawatupia mbwa nyama hiyo”.
Shalom,
Katika agano la kale Mungu aliwapa wana wa Israeli agizo la kutokula nyama yoyote ambayo hawakuiwinda wao. Hiyo yote ni kwasababu ya usalama wa miili yao. Na alifanya hivyo pia kulifundisha kanisa lake rohoni, jinsi linavyopaswa lienende katika maisha ya utakatifu.
Kwa namna ya kawaida ukikutana na swala aliyekufa porini, huwezi kumla kwasababu hujui kilichompelekea kuuliwa ni nini, pengine aliumwa na nyoka, halafu wewe unakwenda kumla, bila shaka utajikuta unaingia katika matatizo yasiyokuwa ya lazima. Au pengine aliuliwa kweli na simba, lakini baada ya muda mfupi wakatokea fisi, wakaanza kuila ila ile nyama, na wewe baadaye ukaikuta ukaichukua, hujui pengine waliacha bakteria gani wenye madhara, wewe unakula tu.
Na ndio maana Mungu aliwakataza sio tu kula mnyama aliyeraruliwa bali pia wasile kibudu cha aina yoyote.
Walawi 22:8 “Nyamafu au mnyama aliyeraruliwa na wanyama asile, asijitie unajisi kwa hiyo nyama; mimi ndimi Bwana”.
Ni sawa tu na sasahivi, ukienda dukani halafu ukauziwa soda iliyofunguliwa, ni wazi kuwa huwezi kuinywa..Kwasababu hujui aliyeifungua alikuwa na lengo gani, pengine alitia sumu ndani yake, au kama sio sumu, ni dhahiri kubwa hata ubora wake utakuwa umepungua, na imesha expire.. hivyo utakapokunywa utakuwa umejihatarisha wewe mwenyewe.
Na ndivyo ilivyo leo hii rohoni, Mungu anataka kila mkristo ajue wajibu wake.. Asiwe ni mtu wa kulishwa lishwa tu kila fundisho ambalo linaletwa mbele yake, bila ya yeye mwenyewe kulihakiki kwanza katika maandiko yake matakatifu ubora wake. Mungu anataka tuwe wenye tabia hii kuhakiki.
Ni lazima ulipime kwa Neno la Mungu, na ndio maana kuna umuhimu sana, wa wewe kama mkristo kusoma biblia kila siku, huku ukimwomba Roho Mtakatifu akusaidie kuyaelewa. Vinginevyo utalishwa hata yasiyokupasa. Hata ukiambiwa mti Fulani uliopandwa hapo uwani kwako ni ishara ya mauti, utaamini, na kwenda kuukata kwasababu hujui maandiko, ukiambiwa mjusi sebuleni ni roho ya mkosi, utakwenda kushindana na mijusi yote duniani, kwasababu hujui maandiko yanazungumzia nini kuhusiana na hayo mambo.
Neno la Bwana linatuambia..
1 Yohana 4:1 “Wapenzi, msiiamini kila roho, bali zijaribuni hizo roho, kwamba zimetokana na Mungu; kwa sababu manabii wa uongo wengi wametokea duniani”.
Swali ni Je! wewe umekuwa ni wa kula kila unachokutana nacho njiani?..Je, ulishawahi kujishughulisha mwenyewe kutafuta mawindo yako? Au kuhakiki kuwa hicho unacholishwa ni salama, kimefungashwa vizuri na kwamba unajua chanzo chake ni nini?
Kama sivyo, anza sasa kufanya hivyo, kwasababu katika siku hizi za mwisho biblia inasema manabii wengi wa uongo watawadanganya wengi, hata yamkini wale walio wateule. Kwahiyo thibitisha ubora wa chakula chako kila siku. Mungu ametoa ruhusa kabisa kwa sisi kufanya hivyo. Usiseme tu AMEN! AMEN! Kwa kila fundisho unalolisikia au unalolisoma mitandaoni, lithibitishe kwanza ndipo ulipokee. Kama bado huelewi chanzo chake ni wapi, liache lipite kwa hao wengine, ambao biblia imewataja kama mbwa, kwasababu sikuzote mbwa hawachagui, wala hawajui kama hichi kimechacha, au kimeoza, au kina sumu, maadamu tu kinamwonekano wa kuliwa kwao ni chakula.
Lakini sisi sio mbwa, wa kupokea kila ufunuo au fundisho. Tuyahakiki yote. Tujitaabishe kuwinda mawindo yetu wenyewe. Watu wengi wamedanganywa na hawajui kuwa wamedanganywa kwa njia hii…Na ndio maana wengi wao wanashikilia udhehebu na udini, hata kama wataambiwa hakuna ziwa la moto, kwasababu kasisi wao kalithibitisha hilo wataamini.
Kutoka 22:31 “Nanyi mtakuwa watu watakatifu kwangu mimi; kwa hiyo msiile nyama yo yote iliyoraruliwa huko kondeni na mnyama wa mwitu; mtawatupia mbwa nyama hiyo”.
Bwana akubariki.
Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema,
Kwa maombezi/Ratiba za ibada/ Ushauri/ Maswali.
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312
pia kama utapenda uyapate mafundisho haya kwa njia ya Whatsapp au email basi tutumie ujumbe kwenye namba hizo hizo.
Mada Nyinginezo:
Nini maana ya “saa yaja atakapodhania kila mtu awauaye ya kuwa anamtolea Mungu ibada?”
SWALI: Nini maana ya “saa yaja atakapodhania kila mtu awauaye ya kuwa anamtolea Mungu ibada?”
Jibu: Unabii huo Bwana Yesu aliutoa kwa wanafunzi wake, pamoja na wote ambao watakuja kumwamini baadaye, kwamba utafika wakati kila ambaye atawaua, au kuwatesa atadhani kuwa anamtolea Mungu ibada. Hiyo ni kuonyesha kwamba mateso ya watu wa Mungu, yanaanzia ndani ya dini, au Imani, na si penginepo. Na Bwana Yesu alisema tena, adui za Mtu ni watu wa nyumbani kwake mwenyewe (Mathayo 10:36).
Sasa tukirudi kwenye swali kwanini Bwana Yesu aseme, “saa yaja atakapodhania kila mtu awauaye ya kuwa anamtolea Mungu ibada”. Ni kwasababu dhiki ya wakristo, itaanzia kwa watu wanaojiita wa dini.
Tukianza na Bwana wetu Yesu mwenyewe, watu waliomsulubisha ni Makuhani na wakuu wa dini, Hao ndio waliohusika wa kwanza katika dhiki zote za Bwana, mpaka Golgotha..Hawa makuhani, ndio waliomshawishi Pilato Mrumi, amsulubishe Bwana. Na walipokuwa wanafanya hayo, walidhani wanamfanyia Yehova ibada, (yaani wanampendezesha Mungu) kwasababu Torati ya Musa ilisema..
Kutoka 31:15 “Kazi itafanywa siku sita; lakini siku ya saba ni Sabato ya kustarehe kabisa, takatifu kwa Bwana; kila mtu atakayefanya kazi yo yote katika siku ya Sabato, hakika yake atauawa”.
Kwahiyo walipomwona Bwana Yesu, anatembea huko na huko kuifanya kazi ya Mungu, ikiwemo kuponya wagonjwa na kuwafungua, wakaamini anaivunja torati, hivyo ili kumpendezesha Mungu, ni lazima Bwana Yesu auawe kulingana na hilo andiko la Kutoka 31:15. Hivyo walimuua Yesu mioyoni mwao wakiamini kwamba wamelitimiza Neno la Mungu, kwamba kila mtu atakayefanya kazi yoyote siku ya sabato auawe.. kumbe wamepotea!.
Na sio tu Bwana Yesu, tunaona pia mitume wake na wanafunzi wake waliofuata baada yake, Mfano tunamwona mtu mmoja anayeitwa Stefano. Huyu aliuawa na wale waliomwua walidhani wanaitimiza torati.
Matendo 6:8 “Na Stefano, akijaa neema na uwezo, alikuwa akifanya maajabu na ishara kubwa katika watu.
9 Lakini baadhi ya watu wa sinagogi lililoitwa sinagogi la Mahuru, na la Wakirene, na la Waiskanderia, na la wale wa Kilikia na Asia, wakaondoka na kujadiliana na Stefano;
10 lakini hawakuweza kushindana na hiyo hekima na huyo Roho aliyesema naye.
11 Hata wakashawishi watu waliosema, Tumemsikia mtu huyu akinena maneno ya kumtukana Musa na Mungu.
12 Wakawataharakisha watu na wazee na waandishi, wakamwendea, wakamkamata, wakampeleka mbele ya baraza.
13 Wakasimamisha mashahidi wa uongo waliosema, Mtu huyu haachi kusema maneno ya kufuru juu ya mahali hapa patakatifu na juu ya torati;
14 maana tumemsikia akisema kwamba Yesu huyo Mnazareti atapaharibu mahali hapa, na kuzibadili desturi tulizopewa na Musa.
15 Watu wote walioketi katika ile baraza wakamkazia macho yao, wakamwona uso wake kuwa kama uso wa malaika”.
Sheria ya mtu aliyemtukana/kumlaani Mungu, ilikuwa ni kifo.
Walawi 24:15 “Nawe nena na wana wa Israeli na kuwaambia, Mtu awaye yote atakayemlaani Mungu wake atachukua dhambi yake.
16 Na yeye atakayelikufuru jina la Bwana hakika atauawa; mkutano wote watamwua kwa kumpiga kwa mawe; kama ni mgeni, kama ni mzalia, hapo atakapolikufuru jina la Bwana atauawa”.
Kwahiyo kulingana na hilo andiko Stefano alistahili kupigwa mawe, kwasababu tayari walikuwa wamemwambia kuwa amemtukana Mungu (Ingawa alisingiziwa), hivyo wote walioshiriki kumuua waliamini kuwa wanalitimiza hilo andiko kwamba “yeyote atakayemlaani Bwana Mungu wake, sharti mkutano wote wampige kwa mawe mpaka afe”. Hivyo hao kwa kumuua Stefano walidhani wanamtolea Mungu ibada.
Kadhalika na vifo vya mitume karibia wote, ni hivyo hivyo, wote walioshiriki kuwaua walidhani kuwa wanamtolea Mungu ibada, na yote hayo yametokea ili litimie hilo Neno Bwana Yesu alilolisema. “saa yaja atakapodhania kila mtu awauaye ya kuwa anamtolea Mungu ibada”.
Lakini pamoja na hayo, unabii huo wa Bwana haukuishia tu kwa mitume au wakristo wa kanisa la kwanza, bali pia unaendelea mpaka leo. Leo watu wa kwanza wanaotumika na shetani bila kujua kuwaletea wakristo wa ukweli dhiki ni watu wanaojiita watu wa imani, hao ndio shetani anaowavaa kuwaletea wakristo wa kweli dhiki, na hata kuwaua.
Leo hii akitokea mtu wa Mungu kajikana nafsi, na kaenda kasimama mahali Fulani anahubiri, kwa adabu yote, labda kwenye gari, au mahali Fulani penye watu, utaona watakaotokeza wa kwanza kwenda kumshitaki kwa wenye mamlaka, na hata kumweka ndani, kwamba anawapigia kelele na hana kibali ni watu Fulani wanaojiita wakristo, tena wanaoyajua maandiko au hata pengine ni kiongozi Fulani mkubwa wa kanisa. Na anafanya hivyo akitumia andiko linalosema…
Warumi 13: 1 “Kila mtu na aitii mamlaka iliyo kuu; kwa maana hakuna mamlaka isiyotoka kwa Mungu; na ile iliyopo umeamriwa na Mungu”
Na tena anafurahi kuona au hata akisikia Yule mtu kapotea kabisa, huku moyoni akiamini kwamba “anamfanyia Mungu ibada”, kumbe anamfanyia ibada shetani. Wakati yeye anafurahia Yule mtu kutiwa ndani, upande wa pili kuna mtu yale maneno yamemgusa na anakwenda kutubu..
Wakati Fulani Petro na Yohana walisimama hekaluni kuhubiri, wakakamatwa na wakuu wa dini, na kutiwa gerezani, wakiwa kule gerezani malaika akaja kuwatoa, na huyo huyo malaika akawaambia warudi kuhubiri kule kule hekaluni walikokamatiwa. Sasa huyo malaika hakujua kwamba wanapaswa watii mamlaka iliyo kuu, na wawe na vibali?? Kasome Matendo 5:17-21.
Bwana Yesu alisema katika Mathayo 28:18 “Yesu akaja kwao, akasema nao, akawaambia, Nimepewa mamlaka yote mbinguni na duniani.
19 Basi, enendeni, mkawafanye mataifa yote kuwa wanafunzi…”
Hivyo ni lazima tujihakiki kila siku, na tuwe makini tusije tukajikuta tunafanya mambo tukidhani kuwa tunampendezesha Mungu kumbe ndio tunakwenda mbali naye, na kumuudhi. Ukikuta mahali popote jina la Yesu linatajwa ni vyema ukafunga mdomo wako na kutulia, kwasababu hujui ni nini Mungu anafanya kwa wakati huo.
Bwana atusaidie.
Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema,
Kwa maombezi/Ratiba za ibada/ Ushauri/ Maswali.
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312
Jiunge na kundi letu la mafundisho ya Biblia whatsapp kwa kubofya hapa > Group-whatsapp
Mada Nyinginezo:
Shalom, Jina la Bwana wetu Yesu Kristo libarikiwe daima.
Siku ya leo, dunia inaadhimisha tukio kuu lililotokea takribani miaka 2000 iliyopita, Na tukio lenyewe ni lile la kufufuka kwa Bwana wetu Yesu Kristo kaburini.
Lakini lipo jambo nataka tujifunze, juu ya mazingira yaliyokuwa yanaendelea siku ile. Lakini kabla ya kuingia katika kiini cha somo letu, nikurudishe nyuma kidogo ili tuweke msingi. Naomba ufuatilie mpaka mwisho lipo jambo kubwa utajifunza leo.
Siku mbili kabla ya Kristo kusulibiwa alikuwa ameketi katika nyumba ya mtu mmoja aliyeitwa Simoni mkoma, kama tunavyojua habari akiwa anawafundisha alitokea mwanamke mmoja, akiwa amebeba kibweta cha Marhamu ya Nardo, akakifungua, akamwagia Yesu kichwani, lakini wale watu waliokuwa karibu walipoona tukio lile walianza kumnung’unikia yule mwanamke sana, kwanini anapoteza fedha nyingi katika mambo yasiyo ya msingi. Sasa mpaka unaona watu wanakinung’unikia kitendo kile ujue kuwa marhamu ile ilikuwa si ya bei ya kawaida.
Kwani kama ingeuzwa wenyewe wanasema wangepata dinari 300, na dinari moja kwa enzi za kibiblia ni mshahara wa kibarua wa siku nzima, (Soma Mathayo 20:1-15), hivyo tukijaribu kubadilisha kwa wakati wetu huu, mshahara wa kibarua kwa siku nzima tunajua ni kama sh. Elfu 20 hivi, ukiizidisha kwa 300, hiyo ni sawa na milioni 6.
Hivyo marhamu hiyo kwasasa ingeuzwa sh. Milioni 6. Kwahiyo unaweza kuona hapo mwanamke yule alijitoa kimasomaso kweli kuinunua, pengine aliuza kila kitu alichokuwa nacho ili tu, amnunulie Kristo marashi yale mazuri ya kupendeza. Na matokeo yake ni kuwa Bwana Yesu akampa thawabu kubwa sana, ya kumbukumbu lisilofutika daima..
Tusome.
Marko 14:3 “Naye alipokuwapo Bethania, nyumbani mwa Simoni mkoma, ameketi chakulani, alikuja mwanamke mwenye kibweta cha marhamu ya nardo safi ya thamani nyingi; akakivunja kibweta akaimimina kichwani pake.
4 Palikuwa na watu waliochukizwa katika nafsi zao wakisema, Kwani kupoteza marhamu namna hii?
5 Maana marhamu hii ingaliweza kuuzwa kwa dinari mia tatu na kuzidi, wakapewa maskini. Wakamnung’unikia sana yule mwanamke.
6 Yesu akasema, Mwacheni; mbona mnamtaabisha? Amenitendea kazi njema;
7 maana sikuzote mnao maskini pamoja nanyi, na kila mpendapo mwaweza kuwatendea mema; lakini mimi hamnami sikuzote.
8 Ametenda alivyoweza; ametangulia kuupaka mwili wangu marhamu kwa ajili ya maziko
9 Amin, nawaambia, Kila ihubiriwapo Injili katika ulimwengu wote, na hili alilotenda huyu litatajwa kwa kumbukumbu lake”.
Sasa mpaka hapo tutakuwa tumeshajenga msingi wa somo letu la leo, Sasa tuzidi kusonga mbele.
Wakati Bwana Yesu anashushwa pale msalabani baada ya kufa kwake, biblia inatuambia kulikuwa na wanawake waliotoka naye Galilaya wakifuatilia kwa karibu, kujua ni wapi watakapokwenda kuulaza mwili wa Bwana (Soma Luka 23:55-56 ).
Na walipoona na kupamaki, wakaondoka kwenda nyumbani, kuandaa, Manukato na Marhamu. Lengo lao lilikuwa ni kwenda kuipaka maiti ya Bwana marhamu hiyo. Lakini kwasababu siku hiyo ilikuwa ni maandalio ya sabato hawakuweza, ikawabidi, wayaweke tayari wasubiri mpaka siku ya jumapili asubuhi ambapo sabato itakuwa imeshakwisha, waende kuupaka mwili wake manukato hayo.
Marko 16:1-3
“1 Hata sabato ilipokwisha kupita, Mariamu Magdalene na Mariamu mamaye Yakobo, na Salome walinunua manukato wapate kwenda kumpaka.
2 Hata alfajiri mapema, siku ya kwanza ya juma, wakaenda kaburini, jua lilipoanza kuchomoza;
3 wakasemezana wao kwa wao, Ni nani atakayetuvingirishia lile jiwe mlangoni pa kaburi”?
Lakini tunapaswa tujifunze, katika habari hiyo, kulikuwa hakuna umuhimu wowote wa kwenda kuupamba na manukato mwili ambao tayari upo kaburini, tena umeshakaa siku 3 mule, uzingatia tena kaburi lenyewe limetiwa muhuri na walinzi, kiashirio kuwa hakuna mtu yoyote aliyeruhusiwa kusogelea mahali pale.
Kwa namna ya kawaida Marhamu ile ilistahili kumwagiwa Yesu akiwa hai, kama alivyofanya yule Mwanamke wa kwanza nyumbani kwa Simoni mkoma, au kama alivyofanya Miriamu nduguye Martha siku ile Yesu alipokwenda kwao (Yohana 12:3)..
Au wangemwagia, wakati bado hajazikwa, yaani mwili ukiwa bado haujaenda kaburini ili kuufanya usiotoe harufu, kama alivyofanya Nikodemo wakati ule walipomshusha msalabani ili kwenda kumzika
Yohana 19:39 “Akaenda Nikodemo naye, (yule aliyemwendea usiku hapo kwanza), akaleta machanganyiko ya manemane na uudi, yapata ratli mia.
40 Basi wakautwaa mwili wake Yesu, wakaufunga sanda ya kitani pamoja na yale manukato, kama ilivyo desturi ya Wayahudi katika kuzika”.
Lakini tunaona hawa wanawake, hawakujali upotevu wowote, waliindaa kwa ajili ya maiti iliyokwisha kuzikwa tayari,..Hilo ni tendo kuu sana la Upendo kwa Bwana wao.
Japokuwa walijua kuwa watakumbana na kikwazo cha Jiwe kubwa pale kaburini, japokuwa walijua kwa namna ya kawaida zoezi lao wanalojaribu kulifanya haliwezi kufanikiwa lakini walijitoa ufahamu, wakaanza safari yao hivyo hivyo, ya kwenda kupoteza marhamu zao za thamani nyingi, kwa ajili ya maiti iliyokwisha kuzikwa siku chache nyuma..
Lakini kwa tukio lao lile la upendo usio wa kawaida, walipofika tu pale kaburini, biblia inatuambia waliona kaburi limeshakuwa wazi tayari, malaika wa Bwana alitangulia kuwafungulia, tena akiwa mule ndani ya kaburi tayari anawangojea,… Embu Tuendelee kusoma..
Marko 16:3-8
“3 wakasemezana wao kwa wao, Ni nani atakayetuvingirishia lile jiwe mlangoni pa kaburi”?
4 Hata walipotazama, waliona ya kuwa lile jiwe limekwisha kuvingirishwa; nalo lilikuwa kubwa mno.
5 Wakaingia kaburini wakaona kijana ameketi upande wa kuume, amevaa vazi jeupe; wakastaajabu.
6 Naye akawaambia, Msistaajabu; mnamtafuta Yesu Mnazareti, aliyesulibiwa; amefufuka; hayupo hapa; patazameni mahali walipomweka.
7 Lakini enendeni zenu, mkawaambie wanafunzi wake, na Petro, ya kwamba awatangulia kwenda Galilaya; huko mtamwona, kama alivyowaambia.
8 Wakatoka nje, wakakimbia kutoka kaburini; kwa maana wameingia tetemeko na ushangao; wala hawakumwambia mtu neno, maana waliogopa”.
Unaona? Na baadaye wakati wanarudi walitokewa na Bwana Yesu mwenyewe, wakamsujudia, na kupewa maagizo ya kwenda kuwaambia mitume wake yawapasayo kufanya (Soma Mathayo 28:1-10)
NI UJUMBE GANI TUNAFUNDISHWA?
Kuna wakati Yesu atakuwa hai anatambea, na pia kuna wakati Yesu atajifanya kama amekufa..Tunapaswa tuonyesha upendo wetu dhati, na wa hali na mali kwake nyakati zote, kwasababu zote zina thawabu zake kubwa.
Wapo wale wanawake walimtia Yesu marhamu wakati akiwa hai, na Kristo akawapa thawabu zao, lakini tunaona wanawake hawa wengine watatu nao walikuwa radhi hata kwenda kufukua kaburi la Yesu ili tu wautie mwili wake mafuta ya thamani, japokuwa walijua kuwa hakuna matumaini yoyote, masaa machache baadaye yatageuka kuwa harufu mbaya, kutokana na kuwa Bwana alikaribia kwenda kutoa harufu, lakini hawakujali, kutoa walichokuwa nacho maadamu ni kwa ajili ya Bwana wao waliyempenda walifanya hivyo kwa furaha tele, na matokeo yake walipofanya hivyo, walikuwa wa kwanza kabisa kutokewa na Bwana, na kupewa maagizo ya kuwapelekea wale wengine, ambao hawakujishughulisha na chochote.
Na sisi pia, kuna wakati tunaweza kuona kazi ya Mungu imekufa, au inakaribia kufa, au haina thamani sana machoni petu, pengine unaweza kuona hata kama ukiisaidia au kutoa msaada wako ni kama unapoteza nguvu zako tu, au mali zako tu.. Lakini katika mazingira kama hayo, wewe jitoe kwenye kazi ya Mungu, kama ni fedha peleka, kama ni nguvu zako zipeleke, kama ni utumishi wako uachie hapo, hata kama kutakuwa hakuna matumaini yoyote ya kazi hiyo kufanikiwa kwasasa.. Wewe mfanyie Kristo kwa moyo wako wote..
Na matokeo yake ni kuwa utakuwa wa kwanza kumwona Kristo aliyefufuka, katika kanisa lake. Na yeye ndiye atakayekupa ujumbe wa kuwapelekea wengine..Hiyo yote ni kwasababu ulimthamini hata angali akiwa maiti inayokaribia kuoza na kunuka.. Hivyo na yeye atakuthamini na kukujalia kumuona katika utukufu wa kufufuka kwake.
Hivyo ujumbe wa leo ni kuwa tunapoadhimisha, kufufuka kwa Kristo, tukumbuke kuwa waliomwona wa kwanza walikuwa ni wale wanawake watatu, Na kilichowafanya wamwone Yesu ni moyo wao ule wa kumtendea jambo bila kujali, kupotea kwa tumaini lao.
Injili kama hizi, zinazohubiriwa na wanawake wacha Mungu kama hawa, zinamatokeo makubwa sana rohoni, kama tutazizingatia katika maisha yetu ya ukristo.
Bwana akubariki sana.
Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema,
Kwa maombezi/Ratiba za ibada/ Ushauri/ Maswali.
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312
pia kama utapenda uyapate mafundisho haya kwa njia ya Whatsapp au email basi tutumie ujumbe kwenye namba hizo hizo.
Mada Nyinginezo:
Jina la Bwana wetu Yesu Kristo libarikiwe, nakukaribisha katika kuyatafakari maandiko. Leo tutajifunza mbinu nyingine ambayo adui shetani anaitumia kuwapunguzia watu kasi ya kumtafuta Mungu.
Ni wazi kuwa kila mtu ana kiu ya kusikia sauti ya Mungu katika maisha yake, na ana kiu ya kujua ni nini kinamzunguka, ni hatari gani iliyopo sasa na iliyopo mbele yake. Na kutokana na wengi kukosa kufahamu ni namna gani wanaweza kuisikia sauti ya Mungu, wameishia kujikita kuishi kwa ndoto wanazoota, wakiamini kuwa kila ndoto wanayoota ni Mungu anazungumza nao.
Leo nataka nikuambie ndugu, ambaye pengine una kiu ya kutafuta kuisikia sauti ya Mungu katika maisha yako, nataka nikuambie sauti ya Mungu haipo katika ndoto unazoota kila siku, njia pekee ya kuisikia sauti ya Mungu si ndoto unazoota bali ni NENO LA MUNGU linalokaa ndani yako. Sauti ya Mungu ni Neno lake katika biblia na si ndoto!.
Si kila ndoto ni sauti ya Mungu kwako. Nyingi zinakuja kutokana na shughuli zako za kila siku na mambo yaliyoujaza moyo wako.
Kwa mfano kama maisha yako yamejaa kutazama filamu za kidunia, na kusikiliza miziki, basi ndoto zako zitajaa hayo mambo, kama moyo wako umeujaza kutukana na maisha ya anasa, na ndoto zako pia zitakuwa hivyo hivyo, kama maisha yako yamejaa kufanya shughuli nyingi kutwa kuchwa, basi na ndoto zako zitakuwa zinahusiana na hizo hizo shughuli unazozifanya..
Mhubiri 5:3 “Kwa maana ndoto huja kwa sababu ya shughuli nyingi;….”.
Sasa inapotokea mtu anaacha kulisoma Neno, na kuishi kwa ndoto zake, na kwamba kila anachoota anatafsiri kwamba ni ujumbe kutoka kwa Mungu, mtu namna hiyo ni rahisi sana kupotezwa na uongo wa shetani. Kwasababu ameacha kujua njia sahihi ya kuisikia sauti ya Mungu, na amekijita kwenye ndoto anazoota kila siku.
Sauti ya Mungu, ni Neno lake ndani ya biblia takatifu. Ukitaka kujua Mungu anataka kuzungumza nawe nini kwa wakati huu, au kwa wakati ujao, nenda kasome biblia, na utaisikia sauti ya Mungu kwa wakati huo..inakuambia nini, (Ni kweli Mungu anaweza kuzungumza na mtu kwa ndoto, lakini hiyo ni mara chache sana..ukilinganisha na jinsi anavyoweza kuzungumza na sisi kwa kupitia Neno lake).
Yusufu japokuwa alikuwa na kipawa hicho cha Mungu kuzungumza naye kwa ndoto, lakini biblia inarekodi mara tatu tu, katika maisha yake yote. Lakini leo utaona mtu kila ndoto anayoota kwake ni ujumbe kutoka kwa Mungu!!. Na huku kaisahau kabisa biblia, hafahamu chochote kuhusu maneno ya Mungu.
Ndugu, Kama unaishi kwa ndoto, (Na kwamba kila asubuhi unapoamka wewe ni kutafuta tafsiri ya ndoto yako kwa watumishi), fahamu kuwa upo mbali sana na sauti ya Mungu, na ndoto unazoota umepofushwa macho ukidhani kuwa Mungu anazungumza na wewe kila siku huko kwenye ndoto zako. Mifano wa sauti ya Mungu kwako na kwangu ni hii >>
Mathayo 5:21 “Mmesikia watu wa kale walivyoambiwa, Usiue, na mtu akiua, itampasa hukumu.
22 Bali mimi nawaambieni, Kila amwoneaye ndugu yake hasira itampasa hukumu; na mtu akimfyolea ndugu yake, itampasa baraza; na mtu akimwapiza, itampasa jehanum ya moto”.
Mathayo 5:38 “Mmesikia kwamba imenenwa, Jicho kwa jicho, na jino kwa jino;
Lakini mimi nawaambia, Msishindane na mtu mwovu; lakini mtu akupigaye shavu la kuume, mgeuzie na la pili”.
Na..
Mathayo 5:43 “Mmesikia kwamba imenenwa, Umpende jirani yako, na, Umchukie adui yako;
44 lakini mimi nawaambia, Wapendeni adui zenu, waombeeni wanaowaudhi,
45 ili mpate kuwa wana wa Baba yenu aliye mbinguni; maana yeye huwaangazia jua lake waovu na wema, huwanyeshea mvua wenye haki na wasio haki”.
Hiyo ndio mifano ya sauti na maonyo ya Mungu kwetu, ambayo ipo moja kwa moja isiyo na mafumbo yoyote. Lakini tukizutumainia ndoto tunazoota kila siku, na kufikiri huo ndio mlango wa kwanza wa Mungu kuzungumza na sisi, tutakuwa tumepotea njia pakubwa sana.
Hivyo tusiishi kwa ndoto, bali kwa Neno la Mungu!
Maran atha!
Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema,
Kwa maombezi/Ratiba za ibada/ Ushauri/ Maswali.
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312
pia kama utapenda uyapate mafundisho haya kwa njia ya Whatsapp au email basi tutumie ujumbe kwenye namba hizo hizo.
Jiunge na magroup yetu ya whatsapp kwa kubofya hapa > Group-whatsapp
Mada Nyinginezo:
Nini maana ya “Tumejengwa juu ya msingi wa mitume na manabii”?
Nakusalimu katika jina kuu la Bwana wetu Yesu Kristo, karibu tuyatafakari maneno ya uzima, ambayo ndio chakula cha kweli kutupacho afya roho zetu.
Lipo jambo moja nataka tujifunze leo linalohusiana na utendaji kazi wa shetani pale anapopata nafasi ya kumwingia mtu. Katika biblia tunaona Yuda ndiye mtu wa kwanza aliyerekodiwa kwa uwazi kabisa kuingiliwa na shetani. Tunalisoma hilo katika
Luka 22:3 “Shetani akamwingia Yuda, aitwaye Iskariote, naye ni mmoja wa wale Thenashara.
4 Akaondoka, akaenda akasema na wakuu wa makuhani na majemadari, jinsi atakavyoweza kumtia mikononi mwao”.
Na matokeo ya yeye kuingiliwa kule na shetani ilipelekea kutiwa moyo mwingine na ibilisi ambao yeye mwenyewe hakuwa nao kabisa.. Na moyo wenyewe ulikuwa ni moyo wa kusaliti.
Yohana 13:1 “Basi, kabla ya sikukuu ya Pasaka, Yesu, hali akijua ya kuwa saa yake imefika, atakayotoka katika ulimwengu kwenda kwa Baba, naye ali amewapenda watu wake katika ulimwengu, aliwapenda upeo.
2 Hata wakati wa chakula cha jioni; naye Ibilisi amekwisha kumtia Yuda, mwana wa Simoni Iskariote, moyo wa kumsaliti;”
Sasa moyo kama huu ukishaingia ndani yako, huwa haujali kitu kingine chochote, huwa haufikirii kwamba huyu ni ndugu yangu, au huyu ni mama yangu, au huyu ni jirani yangu, au huyu ni mwenye haki,au nani n.k. wenyewe kazi yake ni kuvuruga, kuharibu, kusaliti, kuchinja kama sio kuua kabisa. Kwasababu si moyo wa mwanadamu tena unaofanya kazi ndani ya mtu bali ni moyo wa ibilisi mwenyewe ule wa kuasi.
Ndicho kilichomtokea Yuda, alipoingiwa na moyo huo, hakujali kuwa Yesu alimpenda Upeo kama tulivyosoma hapo juu, mpaka akamfanya kuwa msiri wake, na kumpa tonge lake alilolipenda yeye peke yake.. Lakini kinyume chake ni kuwa alimwinulia kisigino chake, akaenda kumsaliti kwa maadui zake, tena mbele ya macho yake kwa kumbusu. Usifikiri ule ulikuwa ni moyo wa Yuda.. Haukuwa moyo wake hata kidogo, na ndio maana baadaye shetani alipomwacha, alijuta sana na mwisho wa siku akaenda kujinyonga.
Zaburi 41:9 “Msiri wangu tena niliyemtumaini, Aliyekula chakula changu, Ameniinulia kisigino chake”
Moyo huu huu ndio utakaomwingia mpinga-Kristo siku ile ya mwisho, ambaye kazi yake itakuwa ni kuchinja tu wale wote ambao hawana ile chapa ya mnyama. Na baadaye itamtoka na kuyaendea mataifa ili kuleta vita duniani.
Ufunuo 16:13 “Nikaona roho tatu za uchafu zilizofanana na vyura, zikitoka katika kinywa cha yule joka, na katika kinywa cha yule mnyama, na katika kinywa cha yule nabii wa uongo.
14 Hizo ndizo roho za mashetani, zifanyazo ishara, zitokazo na kuwaendea wafalme wa ulimwengu wote kuwakusanya kwa vita ya siku ile kuu ya Mungu Mwenyezi.
Leo hii unaona watu wanafanya mauaji makubwa ya kinyama, na kuchinja watu, au kuwatoa ndugu zao kafara usidhani ni mioyo yao inafanya hivyo. Hao ni watu ambao tayari walishamfungulia milango shetani tangu zamani ya kuwaingia, na matokeo yake shetani naye akawawekea mioyo mingine ndani yao, ambayo haijali utu tena, au haithamini kitu chochote, haijalishi itaonyeshwa upendo mkubwa kiasi gani.
Na kwa kawaida mwisho wa siku watu hawa huwa wanaishia katika majuto makubwa sana, pale ambapo wanajiona wameishia katika dhiki, au vifungo, au kukaribia kuuliwa, kutokana na makosa yao, wakati huo shetani ameshawaacha..ndipo wanaposhangaa ilikuwaje walijihusisha katika mambo kama hayo.
Mpaka mtu anafikia hatua ya kuzini zini ovyo hajali chochote, hajali huyu ni mke wa mtu, au mume wa mtu, hajali maradhi, hajali kuwa ni machukizo kwa Mungu, hata wakati mwingine anafanya hivyo na wanyama, au watu wa jinsia moja na yeye, huo ni moyo mwingine wa ibilisi umeshakwisha kuingia ndani yake. Na mwisho wa siku itakuwa ni majuto tu kwake.
Tukumbuke kuwa Yuda alikuwa ni mtume aliyechaguliwa na Yesu mwenyewe, lakini kwa uzembe wake, yalimkuta mambo kama yale, hiyo ni kutufundisha kuwa hata sisi tunaosema tumeokoka yanaweza kutukuta endapo tutakuwa ni watu wa kumpa ibilisi nafasi au upenyo ndani ya maisha yetu.
Tusidhani kuwa tukishafikia hatua hiyo itakuwa ni rahisi kumshinda ibilisi, hilo haliwezekani. Hivyo tuwe makini sana. Tukisema tumeokoka tumaanishe kweli kweli, Yuda alianza na tabia ndogo sana ya wizi, ambayo hakuna mtu aliyejua ingempelekea hata kusaliti na mwisho wa siku kujinyonga. Na sisi mambo madogo madogo tunayoyakumbatia hayo ndiyo yatakuwa upenyo wa ibilisi kutuingia na kuweka mioyo mingine ndani yetu.
Bwana atutie nguvu sote katika safari yetu hii ya wokovu.
Swali ni je, umemwamini Yesu? Je amekusafisha dhambi zako kwa damu yake?. Kama sivyo, unasubiri nini? Una habari kuwa hizi ni nyakati za mwisho? Na shetani naye analijua hilo na ndio maana anafanya kazi zake kwa bidii kukuingia mtu kama wewe mwenye mawazo mawili, kukutia moyo mwingine ndani yako, kwasababu anajua wakati alionao ni mchache?.
Ufunuo 12:12 “..Ole wa nchi na bahari! Kwa maana yule Ibilisi ameshuka kwenu mwenye ghadhabu nyingi, akijua ya kuwa ana wakati mchache tu”.
Huu ni wakati wa kuamka katika usingizi wa mauti, na kumgeukia Kristo, na kumaanisha kweli kumfuata yeye, hivyo tubu dhambi zako kwa kumaanisha kabisa kuziacha, kisha kuwa tayari kwenda kubatizwa katika ubatizo sahihi wa kuzamishwa katika maji mengi na kwa jina la Yesu Kristo ikiwa hukubatizwa hapo kabla. Na baada ya hapo Bwana mwenyewe atakupa kipawa cha Roho wake Mtakatifu, atakayekulinda na kukuongoza katika kweli yote.
Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema,
Kwa maombezi/Ratiba za ibada/ Ushauri/ Maswali.
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312
pia kama utapenda uyapate mafundisho haya kwa njia ya Whatsapp au email basi tutumie ujumbe kwenye namba hizo hizo.
Mada Nyinginezo:
SWALI: Biblia ina maana gani inaposema “Mwenye hekima huvuta roho za watu”?
JIBU: Tusome.
Mthali 11:30 “Mazao ya mwenye haki ni mti wa uzima; Na mwenye hekima huvuta roho za watu”
Zipo hekima nyingi, lakini hekima inayozungumziwa katika biblia ni hekima ya rohoni, ambayo ndiyo kuu kuliko hekima zote, ndio hekima aliyonayo Mungu mwenyewe. Sasa hapo aliposema mwenye hekima huvuta roho za watu, anamaanisha kuwa yeye anayewavuta watu kwa Mungu au watu wamjue Mungu, huyo anatambulika kama mtu mwenye hekima sana.
Hekima hii ilianza kuonekana kwa Bwana wetu Yesu Kristo, Kama tunavyojua yeye aliacha enzi na nguvu na mamlaka huko mbinguni akashuka hapa duniani kwa lengo moja tu, na kuturejeshea sisi ule uhusiano tuliokuwa tumeupoteza na Mungu, na ndio maana akawa radhi kuhubiri injili na kama hiyo haitoshi kuutoa uhai wake kwa ajili yetu.
Vivyo hivyo na sisi pia, tukisema tumeokoka, ni lazima tuwavute na wengine kwa Mungu, ili na wao pia waokoke kama sisi, Hapo ndipo tutatambulika na mbingu kuwa tuna hekima, lakini kama hatuonyesha bidii ya namna hiyo, haijalishi tutasema sisi ni wa rohoni kiasi gani, bado tutakuwa hatuna hekima, kwa mujibu wa maandiko.
Bwana akubariki.
Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema,
Kwa maombezi/Ratiba za ibada/ Ushauri/ Maswali.
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312
Jiunge na kundi letu la mafundisho ya Biblia whatsapp kwa kubofya hapa > Group-whatsapp
Mada Nyinginezo: