NAMWANDAMA BWANA Lyrics~ Swahili?| Trust and Obey
Nyimbo hii iliandwa mwaka 1887, na Mchungaji mmoja aliyeitwa John H Sammis, (Mmarekani), ambaye alifanikiwa pia kuandika nyimbo nyingine Zaidi ya 100 zenye maudhi ya tenzi.
Historia ya wimbo huu ilianza siku moja, katika mkutano wa injili uliofanyika huko Massachusetts Marekani mwaka 1886, katika mkutano huo alisimama kijana mmoja ambaye alitoa ushuhuda wa wokovu wake, Kijana huyu alikuwa hajui mambo mengi kuhusu Mungu, ni mchanga katika wokovu, Lakini katika maneno yake machache alisema..
“Sina uhakika sana, lakini nitakwenda kuamini na kutii”
Maneno hayo yalimgusa sana mwendesha mziki aliyekuwa katika mkutano huo aliyeitwa Danieli Towner, mpaka akaamua kuyaandika maneno yale kwenye kikaratasi, na kisha baadaye akamtumia Rafiki yake ambaye alikuwa mchungaji aliyeitwa John H Sammis, huyo ndiye akauandika wimbo huo, “Namwandama Bwana”. Ambao ndani yake una vina vya maneno ya huyo kijana, nitaamini nitii.
Alipokuwa anauandika, alizingatia vipengele tofauti tofauti ya Maisha yetu tunayopaswa kutii.
NAMWANDAMA BWANA lyrics.
*****
Namwandama Bwana kwa alilonena, | ||||||||||||||||||||||||||||||||
Njia yangu huning’azia; | ||||||||||||||||||||||||||||||||
Nikimridhisha atanidumisha | ||||||||||||||||||||||||||||||||
Taamini nitii pia. | ||||||||||||||||||||||||||||||||
Amini utii, njia pweke ni hii | ||||||||||||||||||||||||||||||||
Ya furaha kwa Yesu: amini ukatii | ||||||||||||||||||||||||||||||||
Giza sina kwangu wala hata wingu, | ||||||||||||||||||||||||||||||||
Yeye mara huviondoa,
|
******
Ni nini tunaweza kujifunza katika historia ya wimbo huu Namwandama Bwana ?
Ushuhuda wako, hata kama utakuwa ni mdogo vipi, unaweza ukawa chanzo cha baraka cha watu wengine wengi duniani na kuwaokoa. Kama kijana huyu angeudharau ushuhuda wake, leo hii tusingekuwa na tenzi yenye faraja ya kipekee kama hii maishani mwetu.
Hivyo nawe pia usigope kushuhudia mambo makuu ya Mungu maishani mwako.
Shalom.
Mada Nyinginezo:
TENZI ZA ROHONI
USINIPITE MWOKOZI Lyrics
BWANA MUNGU NASHANGAA KABISA lyrics
NI SALAMA ROHONI MWANGU Lyrics
KUMTEGEMEA MWOKOZI Lyrics/Swahili.
UNYAKUO.
UFUNUO: Mlango wa 1
NI KITU GANI PETRO NA YOHANA WALIKIGUNDUA KABURINI?
Jina kuu la Bwana wetu Yesu Kristo libarikiwe, Natumai u mzima, karibu tujifunze Maneno ya Uzima kama ilivyo wajibu wetu, maadamu siku ile inakaribia.
Leo tutatazama kwa ufupi juu ya aliyoyatenda mwanamke mmoja aliyeitwa Rispa, mwanamke huyu alikuwa ni suria wa mfalme Sauli. Sasa ilitokea siku moja Israeli ilipitia katika njaa ya mfulilizo wa miaka mitatu, hakuna mvua yoyote juu, mpaka wakajiuliza ni nini hiki? Maandishi ya zamani tofauti na biblia yanasema Daudi akajiuliza pengine kuna watu wanaabudu miungu kwa siri, wakaangalia wakaona mbona sio, wakaangalia kwa kila namna, na wakachunguza kila kitu lakini bado hakuna kilichowapa jibu,
Ndipo Daudi akaona aende moja kwa moja kumuuliza Mungu, pengine labda ni yeye kamkosea, Lakini Mungu akamjibu na kumwambia kuwa kosa lipo katika nyumba ya mfalme Sauli, kwa kuwa yeye alikwenda kuwaua watu ambao walishaingia nao maagano tangu zamani kwamba hawatawaua kwa kinywa cha akina Yoshua (Yoshua 9:15)
Lakini mfalme Sauli hilo hakulijali, akawaua hao watu (wagibeoni), ndipo Mungu akaliona hilo na kuifanya nchi ya Israeli ikae katika njaa kwa miaka mitatu mfufulizo..
Sasa Daudi alichokifanya ni kuwaendea wale wagibeoni, na kuwauliza wawafanyie nini, ili hiyo laana indoke juu yao, ndipo Wagibeoni hawakutaka kitu kingine chochote, bali walitaka tu kumlipizia kisasi Sauli kwa uzao wake, hivyo wakamwomba wapewe wazao wa Sauli waliobaki wawaue kwa kuwatundika kwenye miti milimani. Ndipo Daudi akawajalia haja yao, akawapa wana 7 wa Sauli.
Sasa wawili kati ya hao wana 7 walikuwa wa huyu suria mmoja wa Sauli aliyeitwa Rispa. Tusome.
2Samweli 21:9 “akawatia mikononi mwa Wagibeoni, nao wakawatundika mlimani mbele za Bwana, nao wakaangamia wote saba pamoja; wakauawa siku za mavuno, za kwanza, mwanzo wa mavuno ya shayiri.
10 Naye Rispa, binti Aya, akatwaa nguo ya magunia akajitandikia mwambani, tangu mwanzo wa mavuno hata waliponyeshewa mvua toka mbinguni; wala hakuacha ndege wa angani kukaa juu yao mchana, wala wanyama wa mwitu usiku”.
Unaweza kutengeneza picha mama anayeona watoto wake wakiuliwa kikatili mbele ya macho yake, kwa makosa ya watu wengine, halafu hawazikwi, wameachwa pale msalabani ni uchungu kiasi gani, anausikia..
Lakini kama tunavyosoma hapo huyu Rispa, hakuondoka pale mlimani, bali tangu siku hiyo watoto wake walipotundikwa, alikaa pale pale, kuhakikisha kuwa maiti za wanawe zinaheshimiwa, hakuruhusu ndege aje kula mizoga yao, wala usiku fisi waje kula mifupa.. Na zamani zile ilikuwa mizoga haiondolewi kwenye miti, mpaka hapo Mungu atakapojibu maombi, hivyo kama majibu yakija baada ya wiki moja, ndipo inashushwa pale mtini, yakija baada ya mwezi mmoja ndipo itakaposhushwa, vivyo hivyo hata yakija baada ya mwaka mzigo hiyo itaendelea kubakia pale mtini kwa mwaka mzima.
Na maandiko yanatuambia, mama yule hakuondoka pale mchana wala usiku tangu mwanzo wa mavuno ya shayiri mpaka mvua iliponyesha.. Mwanzo wa mavuno ya yashiri ni mwenzi wa 3-4, na mvua kunyesha ni mwezi 10..Hivyo mwanamke huyu alikaa pale mlimani kwa kipindi kisichopungua miezi 6..
Tengeneza picha, usiku na mchana, unafanya kazi ya kulinda, kuhakikisha maiti za wanao hazivunjiwi heshima kama mizoga ya wanyama, kwa kuliwa na ndege au fisi..alikaa pale mpaka ikawa ni mifupa tu imening’inia lakini hakuruhusu fisi achukue hata kidole cha wanawe.
Lakini tukirudi huku upande wa pili, Daudi akashangaa japokuwa tumewatimizia Wagibeoni haja zao, lakini mbona kama mvua inachelewa tena kwa miezi kadhaa?
Ndipo akasikia kuwa kumbe mama wa wale watoto wawili, tangu kipindi kile cha mauaji, hakuondoka pale mlimani akilinda maiti za wanawe.
Hilo likamfikirisha sana Daudi,, akawaza, kama mama huyu anazithamini maiti na mifupa ya wanawe waliotundikwa mitini na wao sio kitu kikubwa sana, Si zaidi mimi kuthamini mifupa ya Mfalme Sauli aliyeuliwa vivyo hivyo kama wao, (1Samweli 31:10-13) isitoshe ni mtiwa mafuta wa Mungu, mfalme wa Israeli na mimi sijui hata mifupa yake ilipo, Ndipo Daudi akatuma watu kwenda kuichukua mifupa ya Sauli iliyokuwa mbali sana, ng’ambo ya mto Yordani, akaileta Israeli, wakaifanyia maombolezo ya kitaifa, akaichanganya akaichukua ni mifupa ya wale watoto 7 waliouliwa, wakaenda kuzikiwa pamoja.
2Samweli 21:11 “Kisha akaambiwa Daudi hayo aliyoyafanya huyo Rispa binti Aya, suria wa Sauli.
12 Akaenda Daudi, akaitwaa mifupa ya Sauli na mifupa ya Yonathani mwanawe mikononi mwa watu wa Yabesh-gileadi; waliyoiiba katika njia ya Bethshani, hapo Wafilisti walipowatungika, katika siku hiyo waliyomwua Sauli huko Gilboa;
13 naye akaileta toka huko hiyo mifupa ya Sauli, na mifupa ya Yonathani mwanawe; nao wakaizoa mifupa yao waliotundikwa.
14 Kisha wakaizika mifupa ya Sauli na ya Yonathani mwanawe katika nchi ya Benyamini, huko Zela, kaburini mwa Kishi babaye; wakafanya yote aliyoyaamuru mfalme. Na baadaye Mungu aliiridhia hiyo nchi”
Na kwa tukio hilo likapelekea Mungu kuileta mvua juu ya nchi.
Ni nini tunajifunza?
Bidii ya mwingine, na kujali kwa mwingine, kunaweza kukawa sababu ya wewe Mungu kukuzuilia baraka zako. Unasema wewe ni mkristo, umeokoka, Lakini Mungu akimtazama mtu mwingine ambaye hamwabudu Mungu mkuu unayemwabudu wewe lakini ana bidii usiku na mchana ya kumtafuta mungu wake, ujue kuwa mbingu itazuliwa juu yako.. Haijilishi utasema umeokoka kiasi gani.
Ikiwa watu wa dini nyingine wanamfanyia mungu wao dua mara 5 mpaka 10 kwa siku, lakini wewe unaambiwa uombe lisaa limoja kwa siku, huwezi unategemea vipi mbingu isifungwe juu yako?, Hata kama utakuwa umetimiza vigezo vingine vyote, yule mwingine atabakia kuwa hukumu tu kwako.
Yatupasa tujirekebishe, ikiwa wao wanafunga siku 30 kila mwaka, sisi tunapaswa tuende zaidi ya hapo, lakini kama inapita mwaka mzima hujawahi kufunga hata wiki moja, mbingu zitafunga tu juu yako.
Ikiwa wanazingatia kushika aya za vitabu vyao vya dini kwa bidii, lakini wewe mkristo hujui hata biblia inavitabu vingapi, hujawahi hata kusoma kitabu kimoja cha biblia ukakimaliza chote, unasubiria tu kuhubiriwa, mbingu zitafungwa juu yako. Mpaka siku utakapojua tatizo ni nini.
Hivyo sote tujitathmini, Na Bwana atusaidie.
Maran Atha.
Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema, na pia kama utapenda tuwe tunakutumia masomo haya kwa njia ya email yako au Whatsapp tutumie ujumbe kwenye box la maoni chini au piga namba hii +255 789001312
Mada Nyinginezo:
Jina la Bwana wetu Yesu Kristo libarikiwe. Karibu tuyatafakari maandiko pamoja.
Katika maisha, hakikisha unarekebisha vitu vinne. 1) Kazi unayoifanya 2) Kabila unalotoka 3) Nchi unayotoka 4) Mahali unapotoka.
Haya ni mambo makuu manne ambayo ni nguzo katika kuyajenga au kuyaharibu maisha. Na kimojawapo kisipokaa sawa mbele za Mungu, basi kitakuletea tufani kubwa katika maisha.
Hebu tuisome kidogo habari ifuatayo..
Yona 1:7 “Wakasemezana kila mtu na mwenzake, Haya, na mpige kura, mpate kujua mabaya haya yametupata kwa sababu ya nani. Basi wakapiga kura, nayo kura ikamwangukia Yona.
8 Ndipo wakamwambia, Tafadhali utuambie, wewe ambaye mabaya haya yametupata kwa sababu yako; kazi yako ni kazi gani? Nawe umetoka wapi? Nchi yako ni nchi ipi? Nawe u mtu wa kabila gani?
9 Akawaambia, Mimi ni Mwebrania; nami namcha Bwana, Mungu wa mbingu, aliyeziumba bahari na nchi kavu.
10 Ndipo watu wale wakaogopa mno, wakamwambia, Ni jambo gani hili ulilolitenda! Kwa maana watu wale walijua ya kuwa amekimbia, ajiepushe na uso wa Bwana, kwa sababu alikuwa amewajulisha.
11 Basi wakamwambia, Tukutende nini, ili bahari itulie? Kwa maana bahari ilikuwa inazidi kuchafuka“
Walipoanza kwenye nchi, aliwaambia yeye ni Mwebrania..hivyo wakajua moja kwa moja ni mtu wa Taifa la Israeli,ametokea katika mojawapo ya miji ya kule, alipoendelea mbele kidogo, kwenye shughuli anayoifanya akasema yeye anamcha Mungu (yaani maana yake ni mtumishi wa Mungu), anayehudumu katika shamba la Mungu, na kwamba ameikimbia kazi ya Mungu, ndipo walipoelewa tatizo lipo hapo, wakaogopa na kutafuta suluhisho kabla mambo hayajazidi kuharibika.
Sasa endapo Yona ingekuwa hajaikimbia kazi ya Mungu na baharini imewachafukia vile, basi tatizo ni lazima lingekuwa aidha kwenye kabila analotokea, na kama sio kwenye kabila basi kungekuwa na tatizo kwenye nchi anayotokea..au mahali anapotokea.
Hivyo Nataka uone leo kwamba kazi yako unayoifanya inaweza kuwa chanzo cha Tufani na misukosuko, hakikisha kazi unayoifanya yoyote ile aidha ya mikono, iwe inampendeza Mungu kwa viwango vyote, uwe mwaminifu katika kazi yako na pia jiepushe na hila na wizi. Vilevile kama unafanya kazi ya Mungu hakikisha hukwepi majukumu yako kama mtumishi, wala huifanyi kwa ulegevu vinginevyo utakumbana na tufani kama iliyokuta Yona.. Na mkristo yoyote ni lazima awe na jukumu katika kazi ya Mungu. Hivyo jihakiki sana.
Yeremia 48:10 “Na alaaniwe mtu afanyaye kazi ya Bwana kwa ulegevu”
Vile vile kabila unalotoka linaweza kuwa chanzo cha matatizo. Makabila mengi yana mila na desturi zilizo kinyume na Neno la Mungu, makabila mengi yana matambiko na ushirikina, jiepushe na hayo yote baada ya kuokoka. Zipo mila nyingine ambazo ni aibu hata kuzisema hapa..Hizo zote ni rahisi kukusababisha tufani katika maisha yako, na hasira ya Mungu kuwaka juu yako. Jiepushe na hizo mila…Sisemi kwamba ujiepushe na ndugu zako au wazazi wako wanaofanya hizo mila!, na uwachukie na kuwasema Hapana!..endelea kubaki na ndugu zako, waheshimu,wapende, watunze, waombee, na ishi nao kwa furaha zote na kushirikiana nao kwa mambo mengine yote mazuri wanayoyafanya lakini usishiriki mila hizo zilizo kinyume na neno la Mungu.
Pia nchi unayotokea au mahali ulipo panaweza kuwa chanzo cha tufani katika maisha yako..Hivyo ni wajibu wa kushiriki mambo mazuri yanayoendelea katika nchi yako, na kuyakataa yale mabaya yote, Nchi inaweza kuhalalisha ndoa za jinsia moja kisheria kabisa!, nchi inaweza kuhalalisha uvutaji wa bangi, nchi inaweza kuhalalisha utoaji mimba, nchi inaweza kuhalalisha ndoa za wanadamu na wanyama n.k.
Nchi ya namna hiyo tayari ipo chini ya laana na hasira ya Mungu na watu wake ni hivyo hivyo..Hivyo ni wajibu wa wewe uliyeokoka unayeishi ndani ya nchi kama hiyo, kujitenga kwa kutofanya hayo mambo au kukubaliana nayo, ili usiwe miongoni mwa wanaomwudhi Bwana Mungu. Na kujitenga sio kutoongea nao, au kutofanya nao kazi kwenye kampuni moja!..hapana..bali kujiepusha na njia zao, mfano wa Danieli, Meshaki, Shedraka na Abednego jinsi walivyoishi katikati ya taifa la Babeli lakini hawakushiriki matendo ya watu wa Babeli, na walifanikiwa sana katikati ya Taifa lile ovu.
Bwana atusaidie na Bwana atubariki
Na mwisho kabisa kama umejaliwa kupata watoto, au unampango wa kuwa na watoto..kumbuka kuwalea katika njia inayowapasa, angali wakiwa wadogo, kwasababu wakiwa wakubwa hawataiacha biblia inasema hivyo, Na pia wewe mwenyewe kama hujaokoka!. Mlango wa Neema upo wazi, usiidharau injili hata kidogo inayohubiriwa kwako bure! Bila kutozwa chochote… Hata vitu vingi vinavyoishiaga kutolewa bure mara nyingi huwa ni vya gharama sana na vya muhimu sana, kwasababu kama vingeuzwa basi hakuna mtu angeweza kununua..
Hata madawa yanayotolewa bure! Mengi ni ya gharama ya juu sana, yananunuliwa ghali sana aidha na serikali au mashirika binafsi lakini yanakuja kutolewa bure tu kwa watu ili kuokoa maisha!. Na wokovu ni wa gharama sana na wa muhimu kwa kila mtu, ndio maana tunapewa bure!, hivyo usiudharau, Laiti tungetozwa fedha ili kuupata, basi hakuna ambaye angeweza kuununua, hata dunia nzima tungekusanya nguvu zetu zote, tusingeweza kununua wokovu wa mtu mmoja tu! Licha ya watu wa dunia nzima. Mpokee Yesu leo kama hujampokea, na ukabatizwe na kupokea Roho Mtakatifu. Kwa usalama wa maisha yako.
Maran atha!
Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema, na pia kama utapenda tuwe tunakutumia masomo haya kwa njia ya email yako au Whatsapp tutumie ujumbe kwenye box la maoni chini au piga namba hii +255 789001312 Jiunge na magroup yetu ya whatsapp kwa kubofya hapa > WHATSAPP-Group
Mada Nyinginezo:
YONA: Mlango 1
YONA: Mlango wa 2
JINA LA MUNGU NI LIPI?
USIPOKUWA MWAMINIFU, NAFASI YAKO ITACHUKULIWA.
KUMCHA MUNGU NI NINI? NA MTU ANAMCHAJE MUNGU?
JE NI LAZIMA MKRISTO AOE/AOLEWE?
CHUKIZO LA UHARIBIFU
Amin, nawaambia, Kizazi hiki hakitapita..
KAMA ZILIVYOKUWA SIKU ZA NUHU NA ZA LUTU.
SWALI: ‘Siku ya uovu’ inayozungumziwa katika Waefeso 6:13 Ni ipi? Waefeso 6:13 “Kwa sababu hiyo twaeni silaha zote za Mungu, mpate kuweza kushindana siku ya uovu, na mkiisha kuyatimiza yote, kusimama.
JIBU: Ikiwa umedumu katika wokovu kwa muda mrefu utaelewa, si wakati wote mambo yatakwenda sawa kama unavyotaka wewe,
Bwana Yesu aliweka wazi kabisa juu ya suala hilo..akasema..
Mathayo 18:7 “Ole ni wa ulimwengu kwa sababu ya mambo ya kukosesha! Maana hayana budi kuja mambo ya kukosesha…
Unaona anasema, hayana budi kuja..Hiyo haijalishi wewe ni mtakatifu au la!. Si wakati wote shetani atakuwa anakuangalia ukiufurahia wokovu wako kwa kwa amani na utulivu, kuna wakati atapanga mashambulizi ya kukuangamiza, au kukufanya utetereke kwenye imani, au ya kukuudhi, kipindi hicho ukikipitia basi ujue hiyo ndio “siku ya uovu” inayozungumziwa hapo.
Kwahiyo kama siku hiyo ikikukuta halafu ulikuwa hujajiweka tayari, ni ngumu sana kumshinda shetani, ni rahisi kupoa au kuurudia ulimwengu kabisa, katika eneo lolote ulilopo hata katika utumishi wako, anaweza kukuletea vitisho visivyo vya kawaida, anaweza kukuletea majaribu, anaweza kukuletea magonjwa, anaweza kukuletea mashahidi wa uongo, anaweza kukubambikizia hata kesi, anaweza kukujia kwa njia yoyote ile, lengo ni kukuangusha, yalimkuta Yusufu, yalimkuta Danieli, yalimkuta Ayubu, yakamkuta Bwana wetu Yesu Kristo, yakawakuta mitume, mimi na wewe ni nani yasitukute?. Hivyo usipojua namna ya kukabiliana na mitego hiyo inapokuja kwa ghafla, utaanguka mara moja.
Na ndio maana mtume Paulo anatoa suluhisho baada ya mstari huo, anasema;
Waefeso 6:13 “Kwa sababu hiyo twaeni silaha zote za Mungu, mpate kuweza kushindana siku ya uovu, na mkiisha kuyatimiza yote, kusimama
14 Basi simameni, hali mmejifunga kweli viunoni, na kuvaa dirii ya haki kifuani,
15 na kufungiwa miguu utayari tupatao kwa Injili ya amani;
16 zaidi ya yote mkiitwaa ngao ya imani, ambayo kwa hiyo mtaweza kuizima mishale yote yenye moto ya yule mwovu.
17 Tena ipokeeni chapeo ya wokovu, na upanga wa Roho ambao ni neno la Mungu;
18 kwa sala zote na maombi mkisali kila wakati katika Roho, mkikesha kwa jambo hilo na kudumu katika kuwaombea watakatifu wote”
Umeona, vigezo vimeshatolewa hapo juu, ili kumshinda shetani wakati wote, kusema tu umeokoka haitoshi, na huku hujijengei desturi ya kuwa mwombaji wa mara kwa mara, husomi Neno, huifanyi kazi ya Bwana kwa jinsi Mungu alivyokupa karama, Ukiwa ni mkristo wa dizani hiyo ni ngumu kustahimili vishindo vya adui siku ya uovu ikifika, maana ni lazima ije.
Ni sawa na mtu anayejisifia nyumba yake kubwa ya kisasa yenye mali nyingi za thamani, lakini ndani amekosa vifaa vya uokozi kama vile zima moto, au waya wa Earth. Anaweza kuifurahia kweli nyumba yake nzuri kaijenga na kuipamba kwa muda mrefu, lakini siku janga kama la moto litakapotokea kwa ghafla na kuteketeza mali zake zote, pamoja na nyumba yake yote, au umeme unapozidi ndani ya nyumba au radi itakapopiga nyumba, ndipo atakapojua kuwa alikosa vifaa muhimu sana ndani ya nyumba yake.
Vivyo hivyo, tukitaka na sisi tuwe wakristo tuliokamilika, ni lazima tuzingatie vigezo tajwa vyote hapo juu. Tuyafanye maombi kuwa sehemu ya maisha yetu kama tahadhari, Neno la Kristo likae kwa wingi ndani yetu kutuongezea imani, na tutumie karama zetu kuwapelekea na wengine habari njema.
Bwana atutie nguvu.
Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema, na pia kama utapenda tuwe tunakutumia masomo haya kwa njia ya email yako au Whatsapp tutumie ujumbe kwenye box la maoni chini au piga namba hii +255 789001312
Mada Nyinginezo:
Yakobo alikuwa na watoto wangapi?
Yakobo, mjukuu wa Ibrahimu, alipewa neema na Mungu ya kuwa na Watoto 13, Kati ya hao 12 ni wa kiume na 1 wa kike aliyejulikana kama Dina.
Yakobo alikuwa na wake wawili, Na hao wake zake kila mmoja alikuwa na kijakazi wake mmoja, ambao baadaye walikuja kufanyikiwa kuwa masuria wa Yakobo.
Mke wa kwanza aliitwa Lea, Na mke wa pili aliitwa Raheli. Kijakazi wa Lea aliitwa Zilpa Na kijakazi wa Raheli aliitwa, Bilha.
Habari yote ya uzao wao utaipata katika kitabu cha Mwanzo, kuanzia sura ya 29 na kuendelea.
Mwanzo 29:31 “Bwana akaona ya kwamba Lea hakupendwa, naye akafungua tumbo lake; bali Raheli alikuwa hazai.
32 Lea akapata mimba akazaa mwana, akampa jina lake, Reubeni, maana alisema, Kwa kuwa Bwana ameona teso langu; sasa mume wangu atanipenda.
33 Akapata mimba tena akazaa mwana, akasema, Kwa kuwa Bwana amesikia ya kwamba mimi sikupendwa, amenipa na huyu; akamwita jina lake Simeoni.
34 Akapata mimba tena, akazaa mwana, akasema, Basi wakati huu mume wangu ataungana nami, kwa sababu nimemzalia wana watatu. Kwa hiyo akamwita jina lake Lawi.
35 Akapata mimba tena, akazaa mwana. Akasema, Mara hii nitamsifu Bwana; kwa hiyo akamwita jina lake Yuda; akaacha kuzaa…………..”
Bwana akubariki.
Angalia Habari za watakatifu wengine wa kale chini.
Pia kama utapenda mafundisho ya biblia yawe yanakufikia kila mara kwa njia ya whatsapp basi utatumie ujumbe kwa namba hii : +255 789001312
Mada Nyinginezo:
Nuhu alikuwa na watoto wangapi?
Israeli ipo bara gani?
Mariamu Magdalene ni nani. Na hilo jina amelitolea wapi?
Bwana aliposema kuwa yeye ni “Mungu wa miungu” alikuwa na maana gani?..je! yeye ni Mungu wa sanamu?
VIFO VYA MITUME WA YESU/ JINSI MITUME WALIVYOKUFA.
Nimrodi ni nani?
Yeshuruni ni nani katika biblia?
Kuota unaolewa/ unaoa kunamaanisha nini?
Zipo ndoto zenye maana katika Maisha yetu, na pia zipo ndoto zisizo na maana yoyote katika Maisha yetu,.
Hizi zisizo na maana ni ndoto ambazo, ubongo wetu unajiundia wakati tunapokuwa tumelala kutoka katika mazingira yetu yanayotuzunguka, au mambo ambayo tulikuwa tunayawaza au tunayafanya mara kwa mara, Na ndio maana biblia inasema;
Mhubiri 5:3 “Kwa maana ndoto huja kwa sababu ya shughuli nyingi..”
Hivyo asilimia kubwa ya ndoto tunazoziota kila siku, zinaangukia katika hili kundi. Kama wewe ni mshonaji, basi tarajia asilimia kubwa ya ndoto utakazokuwa unaota mara kwa mara zitakuwa ni za namna hiyo,..Vilevile ndoto kama Kuota unaolewa/unaoa, wazo hilo pengine si geni katika kichwa chako,kwamba siku moja umekuwa ukifikiria kuwa utakuja kuoa au utaolewa, Hususani pale unapokuwa umefikia umri huo, lakini bado haijawa hivyo kwako.
Au inakuja kutokana na kuwa umekuwa ukihudhuria mazingira ya harusi mara kwa mara, Hivyo ubongo wako ukayachukua hayo matukio na kuyarudia hivyo hivyo au kwa namna nyingine unapokuwa umelala.
Lakini pia ndoto za namna hii zinaweza kuwa ni za rohoni, hivyo kubeba maana Fulani,
Kwa mfano ikiwa ulikuwa katika kumwomba Mungu, akupe mume/mke, ukiota upo katika ndoa, basi ujue jambo hilo lipo mlangoni kwako.
Lakini unachopaswa kufanya ili Mungu akupe sawasawa na chaguo lake.
Lakini ukiwa ni mzinifu, unatanga tanga na kila mwanaume, au mwanamke, au unaishi mtu ambaye hamjaona, sahau Mungu kulitekeleza hilo, na kama likifanikiwa basi ujue huyo utakayempata hujachaguliwa na Mungu.
Ili kufahamu njia sahihi ya kumpa mweza wa Maisha fungua hapa;
>>> NJIA SAHIHI YA KUMPATA MWENZA WA MAISHA KIBIBLIA.
Lakini hayo yote ni lazima uwe katika wokovu, ukimpata Kristo, umepata vyote, Ukimkosa yeye, umepoteza vyote mpaka uzima wako. Hivyo kama leo hii unahitaji kumkaribisha Bwana Yesu maishani mwako, basi uamuzi huo ni mzuri kwako..Ikiwa upo tayari kufanya hivyo sasa, basi fungua link hii, kwa ajili ya kuongozwa sala ya toba. >>> KUONGOZWA SALA YA TOBA
Pia kama utahitaji kujiunga katika magroup yetu ya Whatsapp unaweza ukabofya hapa chini>>
Kwa mgawanyo bora wa masomo download App hapa>> App wingu la mashahidi
Mada Nyinginezo:
Bahari mbalimbali zilizoorodheshwa kwenye biblia.
Shalom, mtu wa Mungu..karibu tujifunze Biblia…
Katika kisiwa cha Patmo, Bwana Yesu alimtokea Yohana alipokuwa ametelekezwa kule na kumwambia maneno mengi sana kama tunavyoyasoma katika kitabu cha Ufunuo. Na moja ya maneno aliyomwambia ni haya.
Ufunuo 1:17 “Nami nilipomwona, nalianguka miguuni pake kama mtu aliyekufa. Akaweka mkono wake wa kuume juu yangu, akisema, Usiogope, Mimi ni wa kwanza na wa mwisho,
18 na aliye hai; nami nalikuwa nimekufa, na tazama, ni hai hata milele na milele. Nami ninazo funguo za mauti, na za kuzimu”
Mtu aliye na funguo maana yake yeye ndie mwenye uwezo wa kuingia na kutoka, au ana uwezo wa kumruhusu mtu mwingine aingie au atoke. Ana uwezo pia wa kumfungia mtu nje au akamfungia ndani. Vilevile huwezi kuzungumzia funguo bila mlango.
Sasa kuna Malango makuu matatu katika maisha 1) Lango la MAUTI na 2) Lango la KUZIMU na 3) Lango la UZIMA WA MILELE
Lango la mauti ni hatua ile ya mwisho kabisa mtu anapouacha mwili na kufa..Anakuwa anaingia katika upeo mwingine, ambao sio wa maisha haya ya duniani. Huko anakwenda kukutana na vitu vipya ambavyo havipo hapa duniani aidha vizuri au vibaya. Katika huu mlango au geti kabla ya agano jipya ilikuwa haiwezekani mtu aliyeenda huko arudie tena huku ulimwenguni. Ukifa hakuna kurudi, wanaoingia mautini wanakuwa wamefungiwa huko huko milele. Lakini baada ya Kristo na kuzitwaa funguo za Mauti, ndipo ukazaliwa uwezekano mpya wa wafu kurudia tena uhai… Na huo ulianza na Yesu mwenyewe kutoka kaburini na kurudia uhai, na siku ile tu alipokufa wapo wengine waliotoka makaburini Pamoja naye, wale waliokufa katika haki wakati wa agano la kwanza.
Lango hili mtu analiingia baada ya kifo, Mtu aliyekufa katika dhambi, pasipo kutubu..anapokufa baada ya kuvuka lango la kwanza la Mauti, anaingia lango la pili la kuzimu. Huko ni sehemu mbaya isiyofaa. Na huko nako kuna malango mengine madogo madogo kumtenganisha mwovu na mwovu..hatutaingia huko sana. Lakini katika lango hili kuu la kuzimu, waliokuwa wamekufa katika uovu katika agano la kale, ilikuwa haiwezekani kutoka huko milele. Lakini Kristo alizitwaa funguo, na siku moja wafu waliopo kuzimu watatolewa huko kwaajili ya hukumu na wakiisha hukumiwa watatupwa katika ziwa la moto.
Yohana 5:27 “Naye akampa amri ya kufanya hukumu kwa sababu ni Mwana wa Adamu.
28 Msistaajabie maneno hayo; kwa maana saa yaja, ambayo watu wote waliomo makaburini wataisikia sauti yake.
29 Nao watatoka; wale waliofanya mema kwa ufufuo wa uzima, na wale waliotenda mabaya kwa ufufuo wa hukumu”.
Hivyo hata wafu waliopo kuzimu siku moja watatolewa huko kwaajili ya hukumu. Ufunuo 20:13 “Bahari ikawatoa wafu waliokuwamo ndani yake; na Mauti na Kuzimu zikawatoa wafu waliokuwamo ndani yake. Wakahukumiwa kila mtu kwa kadiri ya matendo yake”. Ufufuo huu sio mzuri kabisa kwasababu ni wa hukumu.
Na roho ya malango ya kuzimu inafanya kazi hata kabla ya mauti, roho hiyo ndiyo inayowavuta watu wengi waiendee njia iliyopotea, shetani na majeshi yake wanafanya kazi kwa nguvu sana kuhakikisha ni kundi kubwa linataingia kuzimu.
Lango hili ni ndio la lenye maana kwetu wanadamu, kwasababu ndio lango la uzima wa milele. Tofauti na malango hayo mengine ambayo yanahitaji kifo ndipo uyaingie.. Lango hili la uzima wa milele halihitaji mtu ufe, linaanzia hapa hapa duniani..wakati huu huu mtu anapumua na kuishi katika mwili wake. Lango hili ni bure kuingia lakini linahitaji kupambana sana, kwasababu yupo mwingine adui yetu ambaye hatamani hata mmoja wetu aingie.
Lango hili ni lile Bwana Yesu alilolisema katika kitabu cha Luka..
Luka 13:24 “Jitahidini kuingia katika mlango ulio mwembamba, kwa maana nawaambia ya kwamba wengi watataka kuingia, wasiweze.
25 Wakati mwenye nyumba atakaposimama NA KUUFUNGA MLANGO, nanyi mkaanza kusimama nje na kuubisha mlango, mkisema, Ee Bwana, tufungulie; yeye atajibu na kuwaambia, Siwajui mtokako;
26 ndipo mtakapoanza kusema, Tulikula na kunywa mbele yako, nawe ulifundisha katika njia zetu. 27 Naye atasema, Nawaambia, Siwajui mtokako; ondokeni kwangu ninyi nyote mlio wafanyaji wa udhalimu.
28 Ndipo kutakapokuwa na kilio na kusaga meno, mtakapomwona Ibrahimu na Isaka na Yakobo na manabii wote katika ufalme wa Mungu, nanyi wenyewe mmetupwa nje”.
Kama tunapenda uzima wa milele basi lango hili lipo wazi mbele yetu leo, Bado Bwana Yesu hajalifunga na tunaingia ndani ya lango leo hili kwa kuyatii maneno yake yanayohubiriwa katika biblia takatifu na yanayohubiriwa na watumishi wake. Lakini tukiyakataa maneno yake basi mlango huu utafungwa mbele yetu.
Wapo watu wanaoishi hapa duniani ambao tayari wameshafungiwa mlango huu.(kwamfano watu waliomkufuru Roho Mtakatifu tayari wameshafungiwa, hao kamwe hawawezi kusamehewa tena kadhalika na watu baadhi ambao wameisikia injili kwa muda mrefu sana, wamepigiwa kelele sana, injili imerudiwa na kurudiwa masikioni mwao lakini hata kujigusa hawajigusi, wengi wameshafungiwa huu mlango hivyo kamwe hawataweza kusikia tena ile hamu ya kutubu na kuvutwa kwa Mungu).
Yesu ndiye mwenye funguo za hili lango na funguo hizo pia amewapa watumishi wake..Hebu tusome maandiko yafuatayao ili tuelewe Zaidi..
Yohana 20:21 “Basi Yesu akawaambia tena, Amani iwe kwenu; kama Baba alivyonituma mimi, mimi nami nawapeleka ninyi.
22 Naye akiisha kusema hayo, akawavuvia, akawaambia, Pokeeni Roho Mtakatifu.
23 Wo wote mtakaowaondolea dhambi, wameondolewa; na wo wote mtakaowafungia dhambi, wamefungiwa”.
Umeona hapo? Wale waliotumwa na Yesu kuhubiri wamepewa amri ya kuwafungia watu dhambi..Na hawawafungii kwa kutamka mdomoni kwamba “Fulani nakufungia dhambi” hapana hiyo sio tafsiri yake..Tafsiri ya kuwafungia watu dhambi iliyozungumziwa hapo ni hii >>
Mathayo 10:14 “Na mtu asipowakaribisha wala kuyasikiliza maneno yenu, mtokapo katika nyumba ile, au mji ule, kung’uteni mavumbi ya miguuni mwenu.
15 Amin, nawaambia, itakuwa rahisi nchi ya Sodoma na Gomora kustahimili adhabu ya siku ya hukumu, kuliko mji ule”.
Kwahiyo mtu anaposikia injili na kuidharau tena kuikejeli..Yule mtumishi wa Mungu Roho Mtakatifu anapomwongoza aondoke mahali pale..hao waliosalia hapo nyuma, ndio Habari yao imeisha!..hawatapata tena neema kamwe, wataendelea katika njia hiyo hiyo! Mlango umefungwa tayari. Hali kadhalika wanapoikubali na kuitii, basi wanafunguliwa mlango ambao malango ya kuzimu hayataiweza..maana yake hao watu watakaoitii injili inayohubiriwa na mtu yule aliyetumwa na Mungu..basi ni ngumu sana kupotea…Watakuwa wana ulinzi Fulani wa daima ambao hata wakirudi nyuma kidogo nguvu ya Mungu itawarudisha kwenye mstari kwasababu tu! Waliitii injili ya Kristo. Bwana Yesu alimwambia maneno haya Petro.
Mathayo 16:18 “Nami nakuambia, Wewe ndiwe Petro, na juu ya mwamba huu nitalijenga kanisa langu; wala milango ya kuzimu haitalishinda.
19 Nami nitakupa wewe funguo za ufalme wa mbinguni; na lo lote utakalolifunga duniani, litakuwa limefungwa mbinguni; na lo lote utakalolifungua duniani, litakuwa limefunguliwa mbinguni”
Petro ni mfano wa watu wote waliothibitishwa na Mungu na kuwekwa wakfu kwa ajili ya kazi yake.
Hivyo dada/kaka unayesikia maneno haya. Kama unapenda kuishi Maisha yasiyo na mwisho…miaka milioni kwa mamilioni yasiyo na shida wala taabu, wala uchungu…Njia ni moja tu, nayo ni Yesu. Yeye ndiye mwenye funguo za Uzima wa Milele, na funguo hizo amewapa watumishi wake pia..Ukitaka kuishi, ukitaka uzima..Mkubali Yesu. Ukimkubali Yesu malango ya kuzimu yatakukwepa..kuna nguvu fulani itaachiliwa juu yako ambayo atakuweka katika mstari uliyoonyooka..Lakini kama hutaki kuishi milele, basi malango ya Mauti na kuzimu yanakungoja, hivyo chagua chaguo jema, Yesu ndiye lango na anakupenda!
Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema, na pia kama utapenda tuwe tunakutumia masomo haya kwa njia ya email yako au Whatsapp tutumie ujumbe kwenye box la maoni chini au piga namba hii +255 789001312
Mada Nyinginezo:
KUZIMU ni mahali pa namna gani, Je! huko wanaishi watu wakifa na kwenda kupata mateso au ni vinginevyo?
USIUZE URITHI WAKO.
HASIRA YA MUNGU KUKUWAKIA, KWA KUTOMZUNGUZIA TU MUNGU IPASAVYO.
FAHAMU MAJIRA ULIYOPO NA NINI UNAPASWA UWE NACHO.
MWANAMKE ULIYEKOMAA KI-UMRI, ITAMBUE HUDUMA YAKO.
NI KITU GANI PETRO NA YOHANA WALIKIGUNDUA KABURINI?
UHARIBIFU HAUNA KIFUNIKO.
Kuna ufufuo wa aina ngapi?
Mwezi wa Abibu ni upi?
Huu ni mwezi wa kwanza kwa kalenda ya Kiyahudi. Ambao kwa kalenda yetu hii ya ki-gregory unaangukia katikati ya mwezi Machi, na Aprili, kutegemeana na mwaka wenyewe jinsi ulivyokuja.
Upo mwaka ambao mwezi huu wa Abibu unaanza katikati ya mwezi wa tatu, na upo mwaka, unaanza mwanzoni mwa mwezi wa nne.
Mwezi huu ni mwezi muhimu sana kwa wayahudi, kwasababu ndio mwezi wa kumbukizi yao ya kutoka katika nchi ya Misri(Nchi ya Utumwa).
Kutoka 13:4 “Ninyi mwatoka leo katika mwezi wa Abibu”.
Ndani ya mwezi huu, Siku ya 14 walikuwa wanasheherekea sikukuu iliyojulikana kama sikukuu ya pasaka, Na kuanzia tarehe 15-21, walisheherekea sikukuu ya mikate isiyotiwa chachu.
Kumbukumbu 16:1 “Utunze mwezi wa Abibu, ukamfanyie pasaka Bwana, Mungu wako, kwa kuwa ilikuwa ni mwezi wa Abibu alipokutoa Misri usiku Bwana; Mungu wako.
2 Nawe umchinjie pasaka Bwana, Mungu wako, katika kundi la kondoo na la ng’ombe, mahali atakapochagua Bwana apakalishe jina lake”.
Mwenzi wa Abibu ulijulikana kwa jina lingine kama mwezi Nisani.
Esta 3:7 “Basi mwezi wa kwanza, ndio mwezi wa Nisani, mwaka wa kumi na mbili wa mfalme Ahasuero, wakapiga Puri, yaani kura, mbele yake Hamani; siku kwa siku, na mwezi kwa mwezi, hata mwezi wa kumi na mbili, ndio mwezi wa Adari”.
Soma pia. Nehemia 2:1
Sasa wayahudi kila wanapoiungia huu mwezi wa Abibu/Nisani, huwa wanakumbuka siku ya kutolewa kwao utumwani..
Lakini swali linakuja kwako wewe mkristo, Siku yako ya Nisani ni ipi?
Abibu/Nisani yetu ni pale tunapookoka, siku tunapoamua kuacha dhambi na kumfuata Kristo, na kwenda kubatizwa, basi kuanzia siku hiyo nasi pia tunakuwa tumejumuishwa katika kalenda ya ki-Mungu. Hivyo rohoni tunaonekana kuwa tumeshauanza mwezi wa Abibu/Nisani.
Na faida yake ni kuwa, kuanzia huo wakati unakuwa unaanza kutembea katika mpango wa Mungu wa kimbinguni, wewe unakuwa sio mwana-haramu tena, Mungu anaanza kutenda kazi zake ndani ya maisha yako, kipindi kwa kipindi, Na hilo utalishuhudia mwenyewe, kwa jinsi siku zitakavyokuwa zinakwenda. Utaona tofauti yako ya mwezi uliopita na mwezi huu, utaona tofauti yako ya mwaka ule uliookoka, na ile mingine iliyopita nyuma.
Lakini kama upo katika dhambi, wewe bado kalenda ya ki-Mungu haijaanza kuhesabiwa kwako. Na hivyo Mungu anakuwa hana mpango wowote na wewe, unakuwa ni kama mwana haramu tu. Shetani atajiamulia kufanya lolote atakalo katika maisha yako, atakuharibia maono yako, atafanya chochote ajisikiacho na mwisho wa siku utapotea na kwenda kuzimu. Na kuishia katika majuto ya milele
Lakini ukitubu dhambi zako, leo na ukawa tayari kuanza maisha mpya na Kristo, basi ni uhakika kuwa utaanza kutembea katika huo mpango wa Mungu. Hivyo bila kupoteza muda Ikiwa upo tayari kufanya hivyo leo, basi fungua hapa kwa ajili ya kuongozwa sala ya Toba >>>> KUONGOZWA SALA YA TOBA
Bwana akubariki,
pia fungua vichwa vingine vya masomo chini, upate mafundisho mengine ya rohoni.
Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema, na pia kama utapenda tuwe tunakutumia masomo haya kwa njia ya email yako au Whatsapp tutumie ujumbe kwenye box la maoni chini au piga namba hii +255 789001312
Mada Nyinginezo:
SIKUKUU 7 ZA KIYAHUDI ZINAFUNUA NINI KWETU?
Israeli ipo bara gani?
ESTA: Mlango wa 8, 9 & 10. (SIKU KUU YA PURIMU)
MAVUNO NI MENGI
KRISIMASI (CHRISTMAS) NI NINI? JE IPO KATIKA BIBLIA?
Amin, nawaambia, Kizazi hiki hakitapita, hata hayo yote yatakapotimia..!!
CHUKIZO LA UHARIBIFU
UNYAKUO.
SWALI: Nimrodi ni nani? Na je! Alikuwa ni mtumishi wa Mungu?
Nimrodi ni kitukuu cha Nuhu kwa kupitia uzao wa Hamu,
Biblia inatuambia alianza kuwa mtu Hodari, na sio Hodari tu, bali alikuwa ni Hodari wa kuwinda mbele za Bwana, Mpaka enzi hizo ukatungwa msemo maarufu kwa jina lake (Soma Mwanzo 10:9),
Hivyo aliendelea na huo uhodari wake mpaka akafikia hatua ya kuwa na nguvu nyingi za kuanza kujenga miji mikubwa, ikiwemo Babeli na Ninawi.
Mwanzo 10:8 “Kushi akamzaa Nimrodi, akaanza kuwa mtu hodari katika nchi.
9 Alikuwa hodari kuwinda wanyama mbele za Bwana. Kwa hiyo watu hunena, Kama Nimrodi, hodari wa kuwinda wanyama mbele za Bwana.
10 Mwanzo wa ufalme wake ulikuwa Babeli na Ereku, na Akadi, na Kalne, katika nchi ya Shinari.
11 Akatoka katika nchi ile akaenda mpaka Ashuru, akajenga Ninawi, na Rehoboth-iri, na Kala;
12 na Reseni, kati ya Ninawi na Kala, nao ni mji mkubwa”
Lakini japokuwa alikuwa ni Hodari, alikuwa ni mwovu katika fikra zake na matendo yake, nakala nyingi za kale zinaonyesha, hata nia yake ya kutaka kuujenga mnara wa Babeli ilikuwa ni kumlipizia Mungu kisasi, kwamba kwanini aliwaua mababu zake, hivyo akaunyanyua mnara ule juu sana kuelekea mbinguni kiasi kwamba hata Mungu akileta tena mafurukio mengine asiweze kuwaangamiza.
Lakini jitihada zake hazikufika mbali, tunajua kilichotokea ni nini baada ya pale, ni kwamba walichafuliwa lugha zao na semi, ndoto zao zote zikayeyukia palepale, Kwasababu Mungu hadhihakiwi.
Lakini Pamoja na hayo bado tunakuja kuona Babeli iliendelea kuwepo kwa miaka mingi mbeleni, mpaka ikaja kuwa kitovu cha machafuko yote duniani, Na ndio hawa wababiloni baadaye wakaja kulichukua taifa la Israeli utumwani tena. Kama ulikuwa hujui ni kwamba chimbuko la ibada zote za sanamu na miungu, ilianzia huko, Hii miungu ya Rumi ya kuabudu mungu mke na katoto chake (ambayo kwa sasa wameipachika majina ya watakatifu kama Mariamu ) chimbuko lake lilikuwa ni huko,
Na ndio maana Babeli hiyo mpaka siku hizi za mwisho bado inaonekana kuishi, isipokuwa safari hii inatenda kazi rohoni. Katika kivuli cha dini.
Sasa muhasisi wa hayo yote alikuwa huyu Nimrodi.
Biblia inasema..
Mithali 1:32 “Maana kurudi nyuma kwao wajinga kutawaua, Na kufanikiwa kwao wapumbavu kutawaangamiza”
Usifurahie mafanikio ya kipumbavu hata kama utasifiwa na ulimwengu mzima, shetani naye alikuwa ni Hodari hivyo hivyo kabla ya kuasi, lakini ulikuwa ni uhodari unaokwenda kinyume na mapenzi ya Mungu.
Ezekieli 28:14 “Wewe ulikuwa kerubi mwenye kutiwa mafuta afunikaye; nami nalikuweka hata ukawa juu ya mlima mtakatifu wa Mungu, umetembea huko na huko kati ya mawe ya moto.
15 Ulikuwa mkamilifu katika njia zako tangu siku ile ulipoumbwa, hata uovu ulipoonekana ndani yako.
16 Kwa wingi wa uchuuzi wako watu walikujaza udhalimu ndani yako, nawe umetenda dhambi; kwa sababu hiyo nimekutoa kwa nguvu katika mlima wa Mungu, kama kitu kilicho najisi; nami nimekuangamiza, Ewe kerubi ufunikaye, utoke katika mawe hayo ya moto.
17 Moyo wako uliinuka kwa sababu ya uzuri wako; umeiharibu hekima yako kwa sababu ya mwangaza wako; nimekutupa chini, nimekulaza mbele ya wafalme, wapate kukutazama.
18 Kwa wingi wa maovu yako, katika uovu wa uchuuzi wako, umepatia unajisi patakatifu pako; basi nimetokeza moto kutoka ndani yako, nao umekuteketeza, nami nimekufanya kuwa majivu juu ya nchi, machoni pa watu wote wakutazamao.
19 Wote wakujuao kati ya kabila za watu watakustaajabia; umekuwa kitu cha kutisha, wala hutakuwapo tena hata milele”.
Nasi pia tusiige mifano hiyo, tuwe wanyenyekevu kwa Mungu, tuishi kwa kuyafanya mapenzi yake, Hilo tu linatosha Sio kila jambo linalofanywa na watu Hodari wa mataifa yaliyoendelea na sisi tuigee, Ni heri tubakie na ushamba wetu kuliko tuige utukanaji, ushoga, au upagani, au uvaaji wa mavazi yasiyo na heshima mbele za Mungu na wanadamu.
Imemfaidia nini Nimrodi kuupata ulimwengu mzima, halafu amepata hasara ya roho yake?
Bwana atusaidie.
Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema, na pia kama utapenda tuwe tunakutumia masomo haya kwa njia ya email yako au Whatsapp tutumie ujumbe kwenye box la maoni chini au piga namba hii +255 789001312
Mada Nyinginezo:
Je! Unazijua faida za kufunga na kuomba?
Embu isome Habari ifuatayo kwa makini;
Mathayo 17:18 “Yesu akamkemea pepo, naye akamtoka; yule kijana akapona tangu saa ile.
19 Kisha wale wanafunzi wakamwendea Yesu kwa faragha wakasema Mbona sisi hatukuweza kumtoa?
20 Yesu akawaambia, Kwa sababu ya upungufu wa imani yenu. Kwa maana, amin, nawaambia, Mkiwa na imani kiasi cha punje ya haradali mtauambia mlima huu, Ondoka hapa uende kule; nao utaondoka; wala halitakuwako neno lisilowezekana kwenu.
21 [Lakini namna hii haitoki ila kwa kusali na kufunga”.
Mstari wa 21 unasema.. “Lakini namna hii haitoki ila kwa kusali na kufunga”
Hii ikiwa na maana kuwa yapo mambo ambayo mtu atashindwa kuyafanya, haijalishi yeye ni mkristo au la, haijalishi yeye ni mtakatifu au la! kama hafungi na kuomba, basi atashindwa kufanya mambo mengi sana.
Embu tuzitazame faida za kufunga na kuomba..
1) Pale mtu unapofunga, ina maana kuwa hali chakula, au hanywi maji, kwa wakati Fulani, Na hiyo inampelekea mtu kuwa katika uhitaji mkubwa, Sasa uhitaji huo ndio unaoutesa mwili na kufanya mates ohayo yapenye mpaka kwenye nafsi ya mtu. Nafsi ya mtu ikishapokea mabadiliko hayo inaifanya roho ya mtu kuwa na mwitikio wa tofauti sana katika mambo ya rohoni. Tofauti na mtu ambaye hajafunga kabisa.
Kufungu kunakwenda sambamba na magonjwa, kwamfano mtu aliye katika hali nzito ya kuumwa au kuugua mwilini, mateso yale huwa yanashuka mpaka kwenye nafsi ya mtu, na ndio hapo utaona wagonjwa wengi wapo karibu na Mungu kuliko watu walio na afya zao,
Sasa turudi katika kufunga, pale unapofunga hata maombi yako yanakuwa na uzito wa tofauti ukilinganisha na siku nyingine ambazo ulikuwa hufungi, (jaribu hilo utalithibitisha) kama ulikuwa katika kuyatafakari maandiko, uelewa wako unakuwa wa ndani Zaidi tofauti na siku nyingine ambazo ulikuwa hufanyi hivyo .
Na kwa jinsi atakavyozidi kuenendelea kufunga kwa siku nyingi, ndivyo utakavyozidi kuwa mwepesi katika mambo ya rohoni.
Musa alifanikiwa kufunga siku 40 asiku na mchana bila kula, na sote tunajua ni nini alipata kule mlimani..Mungu alizungumza naye uso kwa uso, na kumpa zile Amri 10, Vivyo hivyo hata kwa Eliya naye alipofunga siku 40, Mungu alisema naye kwenye ule ule mlima wa Musa..
Halikadhalika na kwa Bwana wetu Yesu Kristo, yeye pia alifunga siku 40 usiku na mchana bila kula chochote, mpaka ibilisi akatokea kumjaribu na kushindwa na aliposhuka kule mlimani alishuka na nguvu nyingi za Roho Mtakatifu ndipo akaanza kuhubiri injili na kuponya wangojwa katika Israeli yote.
Hivyo mifungo ya muda mrefu inafaa sana.
2) Faida nyingine ya kufunga inakusaidia kushusha chini matamanio ya mwili. Kwa kuwa chakula kinakuwa hakina sehemu kubwa katika mwili kwa wakati huo, hivyo hata kazi za uzalishaji wa homoni, zinapungua na hivyo inamfanya yule mfungaji awe katika hali ya utulivu Zaidi katika kumtafuta Mungu.
Biblia inatuambia pia, ukifunga, Mungu anakupa thawabu, Hiyo ni kuonyesha kuwa Mungu anathamini kujitesa kwetu kwa ajili yake.
Mathayo 6:16 “Tena mfungapo, msiwe kama wanafiki wenye uso wa kukunjamana; maana hujiumbua nyuso zao, ili waonekane na watu kuwa wanafunga. Amin, nawaambia, wamekwisha kupata thawabu yao.
17 Bali wewe ufungapo, jipake mafuta kichwani, unawe uso;
18 ili usionekane na watu kuwa unafunga, ila na Baba yako aliye sirini; na Baba yako aonaye sirini atakujazi”.
Lakini pia unapaswa kujua kuwa kufunga kokote ni lazima kuambatane na kuomba..hivi ni vitu viwili vinavyokwenda sambamba, ni sawa na chai na sukari, unapobandika chai jikoni, inamaanisha kuwa sukari ni lazima iwepo chini pale inaongojea chai iepuliwe, vinginevyo haitaitwa chai.
Vivyo hivyo na Katika kufunga, hupaswi kufunga tu, unaamka asubuhi, unarudi jioni, halafu hufanyi lolote, unarudia tena hivyo kesho, na kesho kutwa,..hapo ni sawa na kufanya “diet” tu , Lakini unapofunga ni lazima uwe na malengo ya rohoni kwanini unafanya hivyo.
Hapo ndipo hapo sasa suala la kuomba lazima lijitokeze; Danieli alipofunga alikuwa mwombaji, vivyo hivyo na watu wote katika biblia..
Danieli 9:3 “Nikamwelekezea Bwana Mungu uso wangu, ili kutaka kwa maombi, na dua, pamoja na kufunga, na kuvaa nguo za magunia na majivu.
4 Nikamwomba Bwana, Mungu wangu, nikaungama, nikasema, Ee Bwana, Mungu mkuu, mwenye kutisha, ashikaye maagano na rehema kwao wampendao, na kuzishika amri zake;
5 tumefanya dhambi, tumefanya ukaidi, tumetenda maovu, tumeasi, naam, hata kwa kuyaacha maagizo yako na hukumu zako”;
Ukizingatia vigezo hivyo basi faida za kuomba ni kama zifuatazo;
Mathayo 26:40 “ Akawajia wale wanafunzi, akawakuta wamelala, akamwambia Petro, Je! Hamkuweza kukesha pamoja nami hata saa moja?
41 Kesheni, mwombe, msije mkaingia majaribuni; roho i radhi, lakini mwili ni dhaifu”
Mathayo 6:5 “Tena msalipo, msiwe kama wanafiki; kwa maana wao wapenda kusali hali wamesimama katika masinagogi na katika pembe za njia, ili waonekane na watu. Amin, nawaambia, Wamekwisha kupata thawabu yao
6 Bali wewe usalipo, ingia katika chumba chako cha ndani, na ukiisha kufunga mlango wako, usali mbele za Baba yako aliye sirini; na Baba yako aonaye sirini atakujazi”.
Kama tulivyoona katika mistari ya mwanzoni juu, Bwana aliwaambia wanafunzi wake, pale waliposhindwa kutoa mapepo, kuwa namna ile haitoki isipokuwa kwa kufunga na kusali. Hata wewe unapojijengea ustaarabu wa kuwa mwombaji mzuri, basi unapokea mamlaka kubwa Zaidi ya kuamrisha nguvu za giza ziwatoke watu.
Siri nyingine ya maombi ni kuwa, kwa jinsi unavyodumu kwenye kuomba ndivyo unavyoukaribisha uwepo wa Mungu ndani yako..Na matokeo yake ni kuwa ile furaha ya wokovu inajengeka ndani yako.
Usipokuwa mwombaji, ni ngumu sana kuufurahia wokovu wako, utaona kama Mungu yupo mbali na wewe kila siku, utakosa ujasiri wa Imani yako, lakini ukiwa mwombaji amani Fulani utaipata na ujasiri.
Hivyo kama wewe, ulikuwa unalega lega, au ulikuwa hujua faida za kufunga, basi anza leo kufanya hivyo, pia hakikisha unajijengea utaratibu wa kuomba, saa moja kila siku, hicho ndio kiwango cha chini tulichopewa na Bwana Yesu.Kama ukifanya hivyo hakika utaona matokeo makubwa katika Maisha yako..
Utaona tofauti yako ya leo na jana.
Bwana akubariki.
Ikiwa utatamani kujua Zaidi juu ya faida za kufunga, basi tazama masomo mengine yaliyoorodheshwa chini hapa.
Lakini Kama hujaokoka, na unatamani kuokoka leo, Basi uamuzi huo ni mzuri sana, hivyo fungua hapa kwa ajili ya kuongozwa sala ya Toba >>>>>
Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema, na pia kama utapenda tuwe tunakutumia masomo haya kwa njia ya email yako au Whatsapp tutumie ujumbe kwenye box la maoni chini au piga namba hii +255 789001312
Mada Nyinginezo:
NJIA SAHIHI YA KUFUNGA.
Namna ya kuomba
KAMA UNAPENDA MAISHA, NA KUTAKA SIKU YAKO IWE NJEMA.
KIAMA KINATISHA.
NA NENO LA BWANA LILIKUWA ADIMU SIKU ZILE.
SABATO TATU NI NINI?