USIUZE URITHI WAKO.

USIUZE URITHI WAKO.

Urithi tulioahidiwa sisi wanadamu ni UZIMA WA MILELE. Na tumeahidiwa huo na Mungu wetu pale tu tunapomwamini Yesu Kristo. Mtu aliyemwamini YESU KRISTO, anakuwa ni mrithi wa Ahadi za Mungu zote pamoja na Maisha ya daima.…lakini wakati wa kupokea urithi bado unakuwa haujafika, ila katika roho ameshachaguliwa kuwa mrithi..kama tu vile mtoto anapoweza kuchaguliwa kuwa mrithi kabla hata ya wakati wa kurithishwa kufika..Ndivyo mtu aliyezaliwa mara ya pili anavyokuwa…Wakati utakapofika baada ya maisha haya kupita ndipo tutakapokabidhiwa  vyote mikononi mwetu kama vile Bwana Yesu baada ya kumaliza kazi alivyokabidhiwa vyote na Baba…Mamlaka yote ya mbinguni na duniani alikabidhiwa.

Lakini habari ni kwamba urithi huu mtu anaweza kununua na kadhalika unaweza kuuuza..

Biblia inasema..

Marko 10:17 “Hata alipokuwa akitoka kwenda njiani, mtu mmoja akaja mbio, akampigia magoti, akamwuliza, Mwalimu mwema, nifanye nini nipate kuurithi uzima wa milele?

18 Yesu akamwambia, Kwa nini kuniita mwema? Hakuna aliye mwema ila mmoja, ndiye Mungu.

19 Wazijua amri, Usiue, Usizini, Usiibe, Usishuhudie uongo, Usidanganye, Waheshimu baba yako na mama yako.

20 Akamwambia, Mwalimu, haya yote nimeyashika tangu utoto wangu.

21 Yesu akamkazia macho, akampenda, akamwambia, Umepungukiwa na neno moja. Enenda, ukauze ulivyo navyo vyote, uwape maskini, nawe utakuwa na hazina mbinguni; kisha njoo unifuate”.

Unaona hapo, ili uupate uzima wa milele hauna budi uuze baadhi ya mambo/vitu ulivyonavyo, na maana ya kuuza ni KUUTOA MOYO WAKO katika vitu ambavyo ulikuwa unaona vina maana katika maisha yako..Unatoa moyo wako kwenye fedha, unatoa moyo wako kwenye umaarufu, kwa kumaanisha kabisa sio kwa unafki, unatoa matumaini yako na moyo wako kwenye elimu yako, unatoa moyo wako kwenye anasa unazozifanya na dhambi na mambo yote ya kidunia, unakuwa kama ndio leo umeanza kuishi. Kiasi kwamba hakuna chochote cha nje tena kinachoweza kukusisimua au kilicho na nafasi kubwa katika moyo wako zaidi ya Yesu.

Kama Mtume Paulo alivyofanya…

Wafilipi 3:7 “Lakini mambo yale yaliyokuwa faida kwangu, naliyahesabu kuwa hasara kwa ajili ya Kristo.

8 Naam, zaidi ya hayo, nayahesabu mambo yote kuwa hasara kwa ajili ya uzuri usio na kiasi wa kumjua Kristo Yesu, Bwana wangu; ambaye kwa ajili yake nimepata hasara ya mambo yote nikiyahesabu kuwa kama mavi ili nipate Kristo”

Ukiingia gharama za namna hiyo za kuacha kila kitu kwaajili ya Kristo, hapo ni sawa umeuza kila kitu na kwenda kununua kitu cha thamani..Hivyo ufalme wa mbinguni una gharama, tena sio ndogo..kubwa sana..

Vivyo hivyo ufalme wa mbinguni UNAWEZA KUUZWA…Pamoja na kuwa unanunulika kwa gharama kubwa lakini pia unaweza kuuzwa..na unaweza kuuzwa hata kwa gharama ndogo sana….Hapa ni pale mtu aliyekuwa amepewa neema ya kumjua Kristo anapogeuka na kuidharau Neema ile na kuamua kuiacha na kurudia ulimwengu. Huyo nafasi yake inachukuliwa na mwingine, kama Yuda alivyouza nafasi yake kwa tabia yake ya WIZI, na kusababisha nafasi yake kupewa mwingine alyeitwa Mathiya.

Kadhalika Esau naye alivyouza nafasi yake ya urithi  kwa chakula cha siku moja na kupewa Yakobo ndugu yake.

Waebrania 12:16 “Asiwepo mwasherati wala asiyemcha Mungu, kama Esau, aliyeuuza urithi wake wa mzaliwa wa kwanza kwa ajili ya chakula kimoja.

17 Maana mwajua ya kuwa hata alipotaka baadaye kuirithi baraka, alikataliwa (maana hakuona nafasi ya kutubu), IJAPOKUWA ALIITAFUTA SANA KWA MACHOZI”

Kama tunavyosoma hapo juu..Kuna wakati utafika kwa wale walioidharau Neema waliyopewa , wakati huo utakuwa ni wa majuto, na kilio na uchungu mwingi, watu watatamani kwa machozi warudishwe angalau dakika tano nyuma warekebishe makosa yao, lakini watakosa hiyo nafasi…watakapoona uasherati waliokuwa wanaufanya umewaponza wameikosa mbingu, ulevi waliokuwa wanajifurahisha nao kwa kitambo umewaponza, rushwa walizokuwa  wanakula ziliwapofusha macho n.k..Wakati huo utakuwa ni wakati wa majonzi makubwa na majuto kama ya Yuda na Esau….Yuda baadaye alipokuja kujua makosa yake alilia mpaka kufikia  kujinyonga kuona Maisha hayana maana tena…na Esau naye aliitafuta ile nafasi yake kwa machozi lakini hakuipata tena.

Bwana atusaidie tusiuze urithi wetu kwa vitu vichache vya dunia vinavyopita…badala yake tuutafute na kuununua kwa gharama zote. Ili siku ile tutakapoyaona yale ambayo jicho halijawahi kuona wala sikio kusikia furaha yetu iwe timilifu.

Bwana akubariki.

Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema, na pia kama utapenda tuwe tunakutumia masomo haya kwa njia ya email yako au Whatsapp tutumie ujumbe kwenye box la maoni chini au piga namba hii +255 789001312


Mada Nyinginezo:

Je! kuchora tattoo ni dhambi?

HERI NINYI MLIAO SASA, KWA SABABU MTACHEKA.

LIVUNJENI HEKALU HILI, NAMI KATIKA SIKU TATU NITALISIMAMISHA.

Sabato halisi ni lini, Je! ni Jumapili au Jumamosi?, Ni siku gani itupasayo kuabudu?

MZEITUNI HALISI UTAKAPOPACHIKWA.

KUOTA UMETUMBUKIA SHIMONI.

Rudi Nyumbani:

Print this post

About the author

Admin administrator

Subscribe
Notify of
guest
0 Comments
Inline Feedbacks
View all comments