Bwana Yesu alimaanisha nini kusema “yamfaa afungiwe shingoni jiwe kubwa la kusagia, na kutoswa katika kilindi cha bahari?”

Bwana Yesu alimaanisha nini kusema “yamfaa afungiwe shingoni jiwe kubwa la kusagia, na kutoswa katika kilindi cha bahari?”

SWALI : Shalom .. Tukisoma Mathayo 5:43-45 Inazungumzia juu ya mtu ili awe mkamilifu hana budi kumjali mwingine hata kama Anatukosea,kwamba sisi tumeambiwa tuwaombee tuwapende N.K..Sasa tukisoma tena Mathayo 18:6..Inasema Hivi..

“Bali atakayemkosesha mmojawapo wa wadogo hawa waniaminio, yamfaa afungiwe shingoni jiwe kubwa la kusagia, na kutoswa katika kilindi cha bahari.”..Sasa Hapa mtumishi Sjaelewa kwenye Haya maneno aliyoyazungumzia Bwana katika huu mstari, Kwasababu Mathayo 5:43-45 inasema tuwaombee ila hapa Mathayo 18:6 inasema afadhali Afungiwe jiwe ikiwa na maana Aangamizwe..Naona pananitatiza kidogo


JIBU: Bwana Yesu alisema hivi katika Mathayo 5:43-44

“43 Mmesikia kwamba imenenwa, Umpende jirani yako, na, Umchukie adui yako;

44 lakini mimi nawaambia, Wapendeni adui zenu, waombeeni wanaowaudhi,”

Bwana alimaanisha kweli kusema hivyo, kwa namna ya kawaida ukishakuwa  mwanadamu tu, mwenye kitu Fulani kipekee ndani yako, ni lazima utakuwa tu na maadui, wengine watakuwa maadui zao kutokana na wivu, aidha  wa utumishi wako, au ndoa yako, au mafanikio yako, au cheo chako, au kipawa chako, au mwonekano wako, n.k.  Na wivu huo unaweza kufikia hatua hata ya hao watu kutaka kukuua.

Lakini ukijikuta katika hali kama hiyo  wewe kama mkristo unapaswa ufanyaje? Je na wewe uwalipizie kisasi, jibu ni la hapo unapaswa tuwe kama Bwana Yesu alivyokuwa, pale ambapo walimtundika msalabani aliwaombea msamaha, pale ambapo Stefano anauliwa kwa kupigwa mawe mbele ya Paulo aliwaombea na kusema Bwana asiwahesabie kosa lile.

Umeona ni jukumu letu kuwaombea rehema.

Lakini pamoja na hayo kuna wakati mtu anafanya makosa kinyume na Mungu mwenyewe, na hiyo ni hatari zaidi, kwasababu japo Mungu  kasema yeye ni mwingi wa rehema lakini pia ni mwingi wa hasira,  Na ndio maana utasoma hapo, Bwana Yesu akisema..

Mathayo 18:6 “bali atakayemkosesha mmojawapo wa wadogo hawa waniaminio, yamfaa afungiwe shingoni jiwe kubwa la kusagia, na kutoswa katika kilindi cha bahari”

Unapaswa uwe makini sana na Watu waliomwamini Bwana Yesu, hususani wale ambao ni wachanga kiroho, watu waliotubu dhambi zao na kumwelekea Bwana, kwa mioyo yao yote, halafu wewe unakwenda kuwaondoa katika mstari wa wokovu kwa namna moja au nyingine, ukifanya hivyo ujue hukumu yako ni kubwa sana.

Katika biblia utamwona mtu mmoja anaitwa Balaamu, huyu alijua kabisa wana wa Israeli wanaenda sawa na Mungu wao, sasa akatafuta njia ya kuwakosesha kwa makusudi ili wafarakane na Mungu ili waadhibiwe.. Hivyo akabuni njia ya kuwakosesha, kwa kuwaletea wanawake wa kimataifa ili wazini nao, (jambo ambalo Mungu aliwakataza wana wa Israeli)  kisha baada ya hapo Mungu awaadhibu na kuwaacha..Na kweli adhma yake ilifanikiwa, na matatizo yakawakumba kweli wana wa Israeli (Ufunuo 2:14).

Leo hii wapo watumishi wanaozini na washirika wao, mpaka imepelekea, wale wengine ambao walikuwa wameanza kuamini wameuacha wokovu, kutokana na matendo mabaya ya viongozi wao. Sasa watu kama hawa wanamudhi sana Mungu, hawajui tu. Mpaka kufikia hatua kama hiyo ya Mungu kusema..ingemfaa zaidi mtu kama huyo jiwe la kusagia lifungwe shingoni mwake akatupwe baharini… Ni Kuonyesha kuwa hukumu yake ni kubwa sana…Hata akifungiwa jiwe kubwa na kwenda kutupwa kwenye vilindi vya bahari kwa tendo hilo bado Mungu anaona ni sawa tu, amestahili.

Lakini swali ni je! Kwa ruhusu hiyo, tukawafungue watu mawe shingoni? Jiulize Wewe unaweza kufanya hivyo? Unaweza kudhubutu kumtupa mwanadamu mwenzako baharini? Au ulishawahi kufanya hivyo?. Kuna wakati Mungu alikuwa anamwambia Musa kwa hasira kwamba ajitenge na wana wa  Israeli ili awaangamize kwasababu wamemwacha upesi na kugeukia kuabudu masanamu. Na yeye atamfanya kuwa taifa kubwa.

Lakini Musa alizituliza hasira za Bwana, akawaombea rehema, Sio kwamba angekubali Mungu asingetimiziwa aliyoahidiwa, angetimiza kweli, Mungu angeenda kumfanya kuwa taifa kubwa, na yeye angekuwa mfalme juu yao, lakini bado asingekuwa mkamilifu mbele za Mungu. Na ndio maana mtu kama Musa alipata kibali cha kipekee sana mbele za Mungu.

Kumbukumbu 9:12 “Bwana akaniambia, Ondoka huko, shuka upesi; kwa kuwa watu wako uliowatoa Misri wamejiharibu; wamekengeuka mara katika njia niliyowaamuru; wamejifanyia sanamu ya kusubu.

13 Tena Bwana akasema nami zaidi, akaniambia, Nimeliona taifa hili; na tazama, ni taifa lenye shingo ngumu;

14 niache, nipate kuwaangamiza, na kulifuta jina lao chini ya mbingu; nami nitakufanya wewe uwe taifa kubwa lenye nguvu kuwapita wao”.

Nasi pia, Tunapaswa tuitulize hasira ya Mungu, kwa kuwaombea rehema, na Sio kwa kuitekeleza.

Maombi ya kuwaangamiza maadui zetu, tunapaswa tujue kwa mkristo, hayana nafasi.

Bwana akubariki.

Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema,

Kwa maombezi/Ratiba za ibada/ Ushauri/ Maswali.
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312

pia kama utapenda uyapate mafundisho haya kwa njia ya Whatsapp au email basi tutumie ujumbe kwenye namba hizo hizo.

Mada Nyinginezo:

NITAFANYA YERUSALEMU KUWA JIWE LA KUWALEMEA .

Kongwa ni nini kwenye biblia?(Wagalatia 5:1)

Kwanini wale dubu waliowauwa vijana wa Elisha walikuwa wa kike?

Kwanini Yesu aliwakataza mitume wake kumdhihirisha?

KWASABABU MUDA TULIOBAKIWA NAO SI MWINGI.

NI SAA KUMI NA MBILI (12) TU, ZA KRISTO KWAKO.

Rudi nyumbani

Print this post

About the author

Admin administrator

Subscribe
Notify of
guest
0 Comments
Inline Feedbacks
View all comments