Title 26 September 2019

KAZI YA UZURURAJI WA SHETANI.

Biblia inatuambia tabia mojawapo ya shetani ni “kuzunguka zunguka”, na sikuzote tunajua mzungukaji huwa na tabia Fulani ya udadisi na hiyo inafanya mwisho wa siku kuwa na tabia ya kupenda kuteka pia, kwasababu mahali alipo anaona hapamtoshi na hivyo anaamua kutoka na kwenda kuchunguza chunguza maeneo mengine na huko huko akiona upenyo mdogo tu au fursa fulani huwa anaitumia ipasavyo kutimiza matakwa yake mwenyewe..Na ndio maana jina Mzungu, limetokana na Neno mzungukaji, watu waliotoka bara la ulaya zamani walikuwa wakizunguka zunguka nchi mbalimbali na mabara mbalimbali duniani ili kutafuta rasilimali kwa ajili ya nchi zao, Na walipofika maeneo kama Afrika, na kuona kuna kila kitu na vile vitu walivyokuwa wanavitafuta ndipo wakatua hapo, na kufanya yaliyo yao na hata kutumia fursa hiyo kuteka watu na kuwatawala…

Vivyo hivyo na shetani naye, ni mzungukaji kufanikiwa kwake kunategemea kuzunguka zunguka huku na huko duniani, anajua asipofanya hivyo kabisa hawezi kufanikiwa kuuimarisha ufalme wake, Tukisoma kwenye maandiko katika kitabu cha Ayubu tunaona wakati Fulani malaika wa Bwana walipokwenda kujihudhurisha mbele za Mungu, shetani naye alikwenda katikati yao, ndipo Mungu akamuuliza maneno haya..

Ayubu 1:7 “Bwana akamwuliza Shetani, Umetoka wapi wewe? Ndipo Shetani akamjibu Bwana, na kusema, Natoka katika kuzunguka-zunguka duniani, na katika kutembea huku na huku humo”.

Unaona hapo, anasema duniani, ikiwa na maana kila kona ya dunia alikuwa anazunguka zunguka, inamaana hata katika kila taasisi, kila shirika, kila dini, na katika kila nchi, na ndio maana hatushangai kumwona shetani yupo hata katikati ya kanisa la Mungu. Na lengo lake kubwa sio kutalii, hapana bali ni kuchukua mateka, na kuharibu kile kinachoonesha dalili ya kuinuka na kufanikiwa kwa ajili ya Bwana..Ukitaka kujua ukali wa shetani na jinsi anavyomchukia mwanadamu kwa namna isiyokuwa ya kawaida angali tu kitu alichomfanyia Ayubu baada ya Mungu kuuondoa ule ulinzi wake kwake..

Utaona bila kupoteza muda alimletea radi, ikawapiga wale kondoo wake wote, akanusurika Yule mtu mmoja aliyemletea taarifa ambaye alimwambia nimeona moto wa Mungu umeshuka, ilikuwa ni radii ile, sio moto tu kama moto, Hata wewe vile vile anaweza kukutengenezea radi ikiwa tu upo nje ya ulinzi wa Mungu, yaani nje ya wokovu, hiyo ndio kazi inayomfanya azungukezunguke duniani.

Utaona tena Muda huo huo akaandaa majeshi ya maadui, yakawavamia wafugaji wake yakawaua wote, halafu yakaondoka na mifugo, vivyo hivyo hata wewe anaweza akakuundia tu kikundi cha vibaka wakati unakatiza usiku umetoka labda kwenye shughuli zako, wakakuvamia na kukuchoma visu wakaondoka na fedha zako na wewe ukafa saa hiyo hiyo ikiwa tu haupo ndani ya wokovu..

Wakati huo huo tena Shetani akamletea upepo wenye nguvu ukaipiga ile nyumba ikawaangukia watoto wake wote wakafa, hashindwi kukuletea kipunga hapo ulipo umekaa kwa amani, au mafuriko, na kukusababishia tu ajali ambayo chanzo chake hakieleweki, hata gesi tu kukulipukia nyumbani, hashindwi kukufanyia hivyo au shoti kutokea nyumbani au kung’atwa na nyoka tu njiani na habari yako ikawa imeishia hapo,..hashindwi kufanya hivyo vyote kwa mtu ambaye ulinzi wa Mungu haupo juu yake.

Utaona tena Shetani akimeletea Ayubu mpaka magonjwa ambayo hajawahi kuumwa, Leo hii usijione unayo afya na bado upo nje ya wokovu ukadhani wewe unayo kinga kubwa zaidi ya wengine waliopo mahospitalini ndio maana huugui ugui ovyo, shetani anao uwezo wa kukutupia hapo hata kansa usijue imetokea wapi, au ugonjwa wa ajabu ajabu usiojulikana, na ukafa ndani ya siku tatu tu…

Hayo ndio matunda ya shetani ya kuzunguka zunguka kwake ni ili tu kutafuta mtu wa kummeza basi.. Na kumbuka lengo lake sio kukuangamiza tu halafu basi hapana bali ni anataka ufe haraka katika hiyo hali hiyo hiyo ya dhambi uliyonayo sasa ili uende kuzimu moja kwa moja hilo ndio lengo lake…kwasababu anajua akizidi kuchelewa pengine neema ya Mungu inaweza kukupitia ukatubu siku moja.

Na ndio maana Biblia inazidi kutuhimiza maneno haya..

1Petro 5:8 “Mwe na kiasi na kukesha; kwa kuwa mshitaki wenu Ibilisi, kama simba angurumaye, huzunguka-zunguka, akitafuta mtu ammeze.

9 Nanyi mpingeni huyo, mkiwa thabiti katika imani, mkijua ya kuwa mateso yale yale yanatimizwa kwa ndugu zenu walioko duniani.’’

Unaona ni jinsi gani shetani anavyokuchukia wewe uliye kwenye dhambi, kama sio huruma za Mungu tu kumzuia shetani tayari angeshakuangamiza siku nyingi…

Hivyo kama unahitaji kumruhusu leo Bwana aingie maishani mwako, utakuwa umefanya uamuzi wa busara, hapo ulipo tubu kwa kumaanisha kabisa kuacha dhambi zako zote, na kwamba unamaanisha kutokurudia yale yote maovu uliyokuwa unayafanya huko nyuma, Kisha mwambie Bwana Yesu nisamehe na nakukaribisha uje katika maisha yangu….Na ukishamaliza kumweleza mambo hayo yote kwa kumaanisha kabisa, hatua inayofuata tafuta mahali ukabatizwe ili kukamilisha wokovu wako, kumbuka ubatizo ni muhimu, na ni maagizo ya msingi kwa yeyote aliyempokea Bwana, Usipuuzie, ubatizo sahihi wa kuzamishwa katika maji mengi ni wa kuzingatia na uwe ni kwa jina la BWANA YESU KRISTO sawasawa na maandiko haya (Matendo 2:38, 8:16, 10:48, 19:5).

Hivyo ukikamilisha hayo, Bwana mwenyewe atakupa Roho wake Mtakatifu, naye atakaa na wewe milele kukulinda dhidi ya Yule adui azururaye huko na huko, mpaka ile siku ya mwisho ya kwenda mbinguni itakapofika.

Bwana akubariki.


Mada Nyinginezo:

ANGUKO LA UFALME WA SHETANI:

ZIFAHAMU HUDUMA KUU (10) ZA SHETANI DUNIANI.

VIFUNGO VYA GIZA VYA MILELE.

UNALITUMIA KWA HALALI NENO LA KWELI?.

NJAA ILIYOPO SASA.

CHUKIZO LA UHARIBIFU


Rudi Nyumbani:

Print this post

SIKU YA HUKUMU ITAKUWAJE?

Shalom mtu wa Mungu, karibu tujifunze Maandiko..Biblia inatuasa tuwe tunajikumbusha kila siku yale ambayo tumeshajifunza ( 2 Petro 1:12-13, Yuda 1:5), hiyo itatusaidia kutompa nafasi shetani kuziiba zile mbegu ambazo zilishapandwa ndani yetu tayari…Leo kwa Neema za Bwana tutajikumbusha ni kwa jinsi gani Ulimwengu utahukumiwa na watakatifu.

Ni jambo la kufurahisha kuona bado kuna watakatifu ulimwenguni, watu wanaojitunza na kumweshimu Mungu, kwa viwango vya juu…kuona bado kuna watu wanamcha Mungu, kuna wanawake na wanaume wanaojiheshimu, kuona kuwa bado kuna watu ni wapole, ni wasomaji na watendaji wa Neno, ni wavumilivu, wasikivu, wenye huruma, wasiolipiza kisasi, wenye mioyo ya Toba, na wenye kuwahurumia wengine n.k Haijalishi watakuwa ni wachache kiasi gani, lakini uwepo wao tayari ni Tiba kubwa kwa ulimwengu.

Jambo lisilojulikana na wengi ni kuwa Uwepo wa Watakatifu duniani leo hii, ndio unaosababisha ulimwengu usiangamizwe…Bwana akitazama katika mji mmoja na kuona maovu yaliyomo ndani ya huo mji, na akaona huko watakatifu watano, basi huo mji wote unaweza ukasalimika kwasababu tu ya hao watakatifu watano waliopo ndani ya Huo mji. Na siku maangamizi ya Huu ulimwengu yatakapokuja Bwana atakuwa ameshawaondoa watakatifu wake kwa kuwanyakua, haiwezekani kuwaangamiza watakatifu wake pamoja na waovu. Ndio maana utaona Bwana alitamani kuuhurumia mji wa Sodoma na Ghomora endapo tu angekuta huko watu kumi tu walio wakamilifu, lakini hawakuwepo hata hao kumi..Na zaidi ya yote, hata Lutu huyo mmoja aliyesalia walimdharau. Na hivyo kujisababishia maangamizi yao….Hiyo ndiyo Neema wanayoibeba watakatifu waliopo katika ulimwengu sasa…

Lakini katika upande wa pili wa shilingi, Uwepo wa Watakatifu mahali fulani pia ni Ishara mbaya kwa ulimwengu…Kwasababu hao hao watakatifu ambao kwa kupitia wao Mungu anairehemu dunia, hao hao siku ya Hukumu watauhukumu Ulimwengu. Biblia inasema hivyo katika

1 Wakorintho 6:2 “Au hamjui ya kwamba watakatifu watauhukumu ulimwengu?……”

Sasa utauliza Watakatifu wataihukumu vipi dunia?..Na nafasi ya Bwana Yesu ya kuhukumu itakuwa ni ipi Kama watakatifu wataihukumu dunia?, Na pia inawezekanikaje siku ile mtu amhukumu ndugu yake ambaye alikuwa anamfahamu?.

Kuelewa Hukumu itakuwaje siku ile, hebu tafakari mfano ufuatao.

Mwalimu alikuwa na darasa lake la wanafunzi 10 la wanafunzi wa Bweni, akawafundisha kwa mwaka mzima, kisha mwisho wa mwaka akawapa mtihani, wawili kati ya hao 10 walipata alama ‘A’ na nane kati yao wakapata alama ya mwisho kabisa ‘F’. Mwalimu akafurahi kuona amepata wanafunzi wawili waliofaulu vizuri, lakini akahuzunika kuona Zaidi ya robo tatu wamefeli na kupata alama ya mwisho kabisa ‘F’…tena miongoni mwa hao waliopata F kuna wengine wamepata sifuri kabisa. Akawapatia zawadi wale wawili, kwa kuwapandisha daraja la juu na wale 8 akawapa barua ya kuwafukuza shule.

Lakini wale waliofukuzwa wakaanza kumlalamikia kwanini tumefukuzwa…Mwalimu akawaambia ni kwasababu mmefeli mtihani, wakaanza kila mmoja kulalamika…oo ni kwasababu Umetoa kitu ambacho hujatufundisha, wengine wakasema oo ni kwasababu mazingira ya shule hayakuwa mazuri, wengine wakasema oo ni kwasababu chakula kilikuwa kibovu kila siku mlo ule ule tu! Ndio maana tukashindwa kula vizuri na kupelekea kufeli, wengine wakasema tunaomba utupe nafasi ya pili.

Mwalimu akawauliza swali moja wote! Je! Hao waliopata alama ‘A’ hawakuwa kwenye mazingira kama hayo hayo ya kwenu? Ndio mwalimu akaamua kumuita mmoja wa hao waliopata alama ‘A’ mbele yao na kuanza kumhoji na kumwuliza…

Je! Wewe ulikuwa unakula chakula kizuri sana tofuati na hawa ndio ikakusababishia kufaulu, yule akajibu hapana mwalimu, nilikula chakula kimoja na hao, isipokuwa mimi nilikuwa sio mnung’unikaji kama wao nilijua tu hapa shuleni napita hivyo nilivumilia tu shida za kitambo hizi na nikaweka jitihada yangu yote kwenye masomo…akaulizwa tena je! Ulikuwa unalala kwenye kitanda kizuri Zaidi ya wengine, akasema hapana!..akaulizwa na swali la mwisho je! Katika mtihani uliofanya ulikutana na swali ambalo mimi sikuwahi kuwafundisha darasani?…akasema hapana! Maswali yote uliyoyatoa uliyafundisha darasani ndio maana mimi nimeweza kuyajibu mengi ya hayo kifasaha..

Baada ya mwalimu kumwuliza hayo maswali, akawageukia wale wanafunzi 8 waliofeli akawaambia..mnasikia anachosema mwenzenu?..Huyo ndiye anayewahukumu sio mimi…mlilala wote pamoja, mlikula wote chakula kimoja, wote mlikuwa darasa moja…lakini tofauti yenu ni kwamba ninyi hamkuwa makini na shule, na pia hamkujua kilichowapeleka shuleni ndio maana mkafeli kwahiyo ni haki yenu kufukuzwa shule. Kwasababu mlipitia mazingira sawasawa na ya wenzenu waliofaulu lakini nyinyi hamkuzingatia, mlipaswa mvumilie na kujituma kama wenzenu hata kama chakula kilikuwa ni mlo mmoja kila siku. Wale wanafunzi walikosa cha kujitetea na wakaondoshwa shuleni.

Ndugu yangu ndivyo itakavyokuwa siku ile ya Hukumu, Bwana atawahukumu wenye dhambi wote kulingana na matendo yao mbele ya kile kiti cheupe! Atawaambia wamefeli mtihani wa haya Maisha, na hivyo watashushwa daraja la chini (ambalo ni ziwa la Moto), Majina yao hayataonekana katika Kitabu cha uzima hivyo wataondolewa mbele yake, Kwasababu kila mtu sasahivi anafanya mtihani wake na kuandika kitabu chake…Na wengi watakaosikia hiyo hukumu wataanza kulalamika kuwa wanaonewa, wengine watasema Ulimwengu ulikuwa umejaa vishawishi tungewezaje kushinda! Wakubwa kwa wadogo, matajiri kwa maskini, kila mtu ataanza kutoa malalamiko yake..Ndipo yule aliyeketi katika kile kiti cha hukumu, atawaita watakatifu walioshinda ulimwenguni na kuwahoji mbele yao. Na hao waliohukumiwa watakosa cha kujitetea mbele yao, Kwahiyo wataenda kwenye lile ziwa la moto kwa huzuni na majuto makubwa, wakijua kuwa ni kweli wamestahili.

Ndugu wakati leo hii unaona wapo watakatifu wanaojituma kweli katika Mungu, hao sio ishara nzuri kwako, siku ile ya Hukumu watakuhukumu…Utasema Bwana mbona ilikuwa ni ngumu sana mimi kuacha uasherati kwenye kizazi changu ambacho kila kona ya barabara nilipishana na wanawake wapo nusu uchi? Nikifungua tv, internet, radio nakutana na mambo yavishawishi vya uasherati? Bwana atamleta mmoja ambaye alikuwepo kwenye hicho hicho kizazi chako, ambaye naye pia alikuwa anapitia majaribu kama ya kwako na hata pengine Zaidi hata na hayo yako kama vile Yusufu na akashinda uasherati na wewe utakosa cha kujitetea siku hiyo..

Utasema mbona mimi nilikuwa mzuri sana ningewezaje kushinda vishawishi mahali ambapo kila kona watu walikuwa wananitaka?..simalizi hatua mbili kila mwanamume ananijaribu? Siku ile watasimamishwa waliokuwa wazuri kuliko wewe mfano wa Sara katika kizazi chako, na pamoja na kwamba walikuwa ni wazuri sana, lakini walishinda vishawishi, na kujihadhari na ulimwengu, utakosa cha kujitetea siku ile.

Utasema nitawezaje kutubu na kumgeukia Kristo ninaposikia injili, si kila mtu atanicheka na kuniona mwendawazimu, nitawezaje kuacha Imani yangu na dini yangu, na dhehebu langu nililolizoea? Na kutubu na kumgeukia Kristo kikamilifu?…Biblia inasema katika Mathayo 12: 41 “Watu wa Ninawi watasimama siku ya hukumu pamoja na watu wa kizazi hiki, nao watawahukumu kuwa wamekosa; kwa sababu wao walitubu kwa mahubiri ya Yona; na hapa yupo aliye mkuu kuliko Yona”

Utasema tena Bwana mimi nilikuwa ni Tajiri sana, nilikuwa ni Mkuu wa Wilaya, ningewezaje kupata muda wa kukutafuta wewe?..Siku ile watasimamishwa waliokuwa matajiri kuliko wewe katika wakati wako na katika utajiri wao wote walimtafuta Mungu na kujiepusha na ulimwengu. Biblia inasema katika..

Mathayo 12: 42 “Malkia wa kusini atasimama siku ya hukumu pamoja na watu wa kizazi hiki, naye atawahukumu kuwa wamekosa; kwa sababu yeye alikuja kutoka pande za mwisho za dunia ili asikie hekima ya Sulemani, na hapa yupo aliye mkuu kuliko Sulemani”

..Malkia anasafiri maelfu ya Maili…kwenda kuitafuta Hekima ya Mungu, wewe Balozi wa nyumba kumi huna muda! Siku ile hutakuwa na la kujibu.

Kwahiyo uonapo! Mtu mwema anafanya wema katika mazingira yasiyostahili wema..usiishie kufurahia tu! Bali pia Ujiulize nawe pia unafanya wema kama yeye katika mazingira kama yake?..Kwasababu kama hufanyi hivyo siku ile hutakuwa na cha kujitetea, na wala hutapata mtetezi…Dada uonapo kuna mwanamke mzuri kuliko wewe anavaa kwa kujisitiri pamoja na uzuri wake wote..usifikiri utakuwa na cha kujitetea siku ile ya hukumu mbele za Mungu, utaelekea kwenye Ziwa la Moto, na utasema ni kweli umestahili.

Unapoona kuna watu wanamtafuta Mungu katika kizazi chako cha uovu..Usiishie kufurahia tu! Na kusema nakushukuru Mungu!…Tambua kuwa kitendo wafanyacho huko mbeleni kitakuja kugeuka kuwa mashitaka kwa wasiomtafuta Mungu katika kizazi hicho hicho kigumu.

Bwana akubariki sana. Ni matumaini yangu kuwa umepata kitu, kama hujampa Kristo Maisha yako, mlango wa Neema haujafungwa, lakini siku si nyingi utafungwa, watakatifu wataondolewa duniani na kunyakuliwa juu mbinguni, na dhiki kuu kuanza duniani. Je! Bado ni vuguvugu?..bado unaupenda ulimwengu na anasa zake! Shetani anakudanganya kuwa hakuna watu wanaomcha Mungu duniani leo?…usidanganyike Mungu ana watu wake kila mahali, shetani anachotaka ni wewe uendelee kufikiri hivyo ili siku ile ya hukumu, uhukumiwe vizuri na Maisha ya watakatifu waliopo leo duniani.

Baada ya kutubu kama ulikuwa hujatubu, ni Ubatizo, ubatizo sahihi ni ule wa kuzama mwili wote katika maji mengi na kwa jina la Bwana Yesu.


 

Mada Nyinginezo:

KUNA HUKUMU ZA AINA NGAPI?

KUNA UFUFUO WA AINA NGAPI?

UTAWALA WA MIAKA 1000.

KARAMU YA MWANA-KONDOO.

WAFALME WATOKAO MAWIO YA JUA.

NYOTA ZIPOTEAZO.


Rudi Nyumbani:

Print this post

NYOTA ZIPOTEAZO.

Kila mtu anayemwongoza mwenzake katika kutenda haki biblia inamfananisha na nyota..
 
Danieli 12:3 “Na walio na hekima watang’aa kama mwangaza wa anga; na hao waongozao wengi kutenda haki watang’aa kama nyota milele na milele.”
 
Unaona? Na ndio maana mtume Paulo aliandika kuna tofauti ya fahari kati ya nyota na nyota. (1Wakorintho 15:41), akiwa na maana kuwa zipo nyota zinazong’aa sana, vile vile zipo zisizong’aa sana, vile vile zipo zinazoonekana kubwa kuliko nyingine na zipo zinazoonekana ndogo..Na tunajua kuwa Bwana wetu Yesu Kristo ndio ile nyota ing’aayo sana kuliko zote, Iliyoonekana na mamajusi, tokea mbali, sio kana kwamba kulikuwa hakuna nyota nyingine hapana , bali ile ndio iliyoonekana yenye fahari na utukufu mkubwa kuliko zote, iliyozidi zote, yeye ndio nyota yenye nguvu kuliko zote, ile nyota ya Asubuhi (Ufunuo 22:16)wakati Jua linakaribia kuchomoza nyingine zote zitazama lakini yenyewe bado itaendelea kuangaza, na nyota hii hata mchana huwa inaonekana kama anga lisipokuwa na mawingu.
 
Lakini bado biblia inatuambia pia katikati ya hizo nyota zipo pia nyota zipoteazo na leo tutaziangazia hizi nyota ni zipi tunalisoma hilo katika
 
Yuda 1:12 “Watu hawa ni miamba yenye hatari katika karamu zenu za upendo walapo karamu pamoja nanyi, wakijilisha pasipo hofu; ni mawingu yasiyo na maji, yachukuliwayo na upepo; ni miti iliyopukutika, isiyo na matunda, iliyokufa mara mbili, na kung’olewa kabisa;
 
13 ni mawimbi ya bahari yasiyozuilika, yakitoa aibu yao wenyewe kama povu; NI NYOTA ZIPOTEAZO, AMBAO WEUSI WA GIZA NDIO AKIBA YAO WALIOWEKEWA MILELE”.
 
Hizi nyota ni zipi katika anga?.
 
Zamani nyota zote ambazo zilikuwa hazitulii au hazina mzunguko maalumu zilijulikana kama nyota zipoteazo, ni nyota ambazo hazikutegemewa na mabaharia katika safari zao za majini, na kuonyesha dira..Ni nyota ambazo unaweza ukaziona leo, na usikae uzione tena mpaka mwisho wa dunia, Kwa mfano hata leo hii ukitazama angani utaona kuna nyota zinakatiza anga kwa mwendo kasi, dakika mbili tatu huzioni tena..huo ni mfano wa nyota zipoteazo, tofauti na baadhi ya nyota ambazo unaweza kuziona mara kwa mara kwamfano mimi tangu nilipokuwa mdogo kuna nyota nilikuwa ninazionaga angani wakati wa usiku, na kama wewe pia nimtazamaji juu, utangundua kuna nyota ambazo zinakuwa zimejikusanya nyingi nyingi ndogo kama kifungu, sasa hizo kwa lugha ya kisayansi zinaitwa KILIMIA, na nyingine utaziona zipo tatu tu kwenye mstari mnyoofu nazo kwa lugha ya kisayansi zinaitwa ORIONI, kama huzijui unaweza ukatoka nje usiku mmoja wenye nyota ukatazama juu hazihitaji elimu au hadubini kuziona, zipo angani na zinaonekana wazi kabisa..Sasa hizi ni nyota sio tu utaziona leo, bali zilikuwa zikionekana tangu vizazi na vizazi huko nyuma, hadi kwenye maandiko zimeandikwa soma..
 
Amosi 5: 8 “mtafuteni YEYE AFANYAYE KILIMIA NA ORIONI, NA KUKIGEUZA KIVULI CHA MAUTI KUWA ASUBUHI, NA KUUFANYA MCHANA KUWA giza kwa usiku; yeye ayaitaye maji ya bahari, na kuyamwaga juu ya uso wa nchi; Bwana, ndilo jina lake;”
 
Ayubu 9:7 “Aliamuruye jua, nalo halichomozi; Nazo nyota huzipiga muhuri.
8 Ambaye peke yake ni mwenye kuzitandika mbingu, Na kuyakanyaga mawimbi ya bahari.
9 Yeye afanyaye hizo NYOTA ZA DUBU, na ORIONI, na hicho KILIMIA, Na makundi ya nyota ya kusini”.
 
Ayubu 38: 31 “Je! Waweza kuufunga mnyororo wa KILIMIA, Au kuvilegeza vifungo vya ORIONI?
32 Je! Waweza kuziongoza Sayari kwa wakati wake?….”
 
Unaona, na nyingine nyingi, nyota ya asubuhi unaifahamu ni moja ya nyota zilizo rasmi, wakati wote ipo, lakini embu fikiria juu ya kitu kinachoitwa KIMONDO kama unakifahamu, chenyewe hata hakipiti angani bali utaona sekunde mbili au tatu kina’ngaa sana angani hata kuliko nyota zote halafu baada ya hapo ukioni tena milele hujui kimepotelea wapi..
Ndivyo ilivyo kwa wahubiri wengi wa siku hizi za mwisho, kigezo cha wao kushika biblia au kuwa viongozi wa makundi ya watu, hakiwafanyi kuwa nyota bora, ni kweli anaweza akawa amekidhi vigezo vya kuwa nyota lakini ni nyota ipoteayo..Nyota isiyodumu, ambayo Mtume Yuda ameandika weusi wa giza ndio akiba yao waliowekewa milele…ukisoma mistari michache ya juu utaona anawafananisha na maji, yachukuliwayo na upepo; ni miti iliyopukutika, isiyo na matunda, iliyokufa mara mbili, na kung’olewa kabisa;…
 
Hawa ni viongozi wasiotoa matunda ambayo Mungu anataka ayaone wakiyatoa yaani kuwafanya watu waokolewe na wamjue yeye, hawa ni viongozi wasiodumu katika mzunguko waliowekewa wa injili, yaani hawadumu katika mafundisho ya msingi ya Neno la Mungu, na dalili kubwa inayowatambulisha utaona watu wanaowafuata hawaoni dira yoyote ya kuwafanya wafikie hatma njema ya maisha yao ya milele, wanaangaza kidogo tu, halafu muda mfupi hawapo, wanatafuta mambo yao wenyewe, na katika kipindi hichi cha mwisho wapo wengi.
 
Ndugu, wakati tuliopo sasa, si wakati wa kukaa bila ufahamu, kwasababu upotevu ni mwingi, na njia ni nyembamba sana ielekeayo uzimani…Hivi unajua kuwa kuongezeka kwa waalimu wa Uongo na wahubiri wa uongo ndivyo inavyozidi kuifanya ile njie izidi kuwa nyembamba zaidi?..Njia ya uzima kila siku inazidi kuwa nyembamba….soma biblia jifunze Neno la Mungu tafuta kwanza kuweka uhusiano wako na Mungu sawa, Nyota kweli ni NYINGI, Lakini zipoteazo pia ni NYINGI ZAIDI, hivyo kuwa makini na ile nyota inayokuongoza. Bwana Yupo mlangoni kurudi.
 
Je! Unahabari kuwa hili ndio kanisa la mwisho la saba tuishilo lijulikanalo kama Laodikia na hakutakuwa na kanisa lingine zaidi ya hili?. Je! Unahabari kuwa taifa la Israeli sasa linazidi kupata nguvu, na moja ya hizi siku neema itahamia kwao na kwa wakati huo UNYAKUO utakuwa umeshapita?, Na je unahabari kuwa kama huna Roho Mtakatifu huwezi kunyakuliwa?.
 
Unasubiri nini, Ulimwengu ukutese na bado mbingu uikose?..Tafakari tena ufanye maamuzi yenye akili, Kristo anakuita alikufa kwa ajili yako, ukimaanisha kumgeukia atakupokea na kukufanya uwe wake, hivyo TUBU TU, kisha tafuta mahali ukabatizwe ubatizo sahihi wa kuzamishwa katika maji mengi kwa jina la YESU KRISTO kama hujafanya hivyo, upate ondoleo la dhambi zako, kisha Bwana atakupa kipawa chake cha Roho Mtakatifu bure.
 
Ubarikiwe sana.
 

Mada Nyinginezo:

KITABU CHA YUDA: SEHEMU YA 1

UNAWAFAHAMU MANABII WA UONGO?

INJILI KULINGANA NA TEKNOLOJIA.

HUDUMA YA (ELIFAZI, BILDADI, NA SOFARI).

UTEKA ULIOGEUZWA.

MAMBO (2) YATAKAYOKUTENGA NA IMANI SIKU HIZI ZA MWISHO.

SIRI YA KUASI KATIKA KANISA LA MUNGU.


Rudi Nyumbani:

Print this post