HUDUMA YA (ELIFAZI, SOFARI, NA BILDADI).

HUDUMA YA (ELIFAZI, SOFARI, NA BILDADI).

Habari za Elifazi, Sofari, na Bildadi tunazipata katika kitabu cha Ayubu, kama wewe ni msomaji wa biblia utakumbuka kuwa  walikuwa ni marafiki wa Ayubu  wa karibu sana waliokuja kumlilia pale alipopatwa na yale matatizo ambayo tunayoyasoma kwenye biblia. Lakini kabla ya hao kuja tunasoma pia Ayubu alikuwa ni MWELEKEVU sana aliyemcha Mungu na kuepukana na uovu wa kila namna, na baada ya shetani kuona wivu juu yake,ndipo akaamua kwenda kumshitaki kwa Mungu, ajaribiwe ili aiache Imani yake. Kama tunavyofahamu, baadaye Mungu alimruhusu shetani amjaribu Ayubu.  Na ndipo shetani akaenda kuzimu kuandaa MAJARIBU yake mazito MATATU(3), ambayo katika hayo alipata uhakika kabisa kwamba Ayubu hawezi kunusurika ni lazima amkane Mungu na kuachana na uelekevu wake. Embu tuyapitie kwa ufupi.

Jaribu la kwanza lilikuwa ni la nje ya mwili wake na nafsi yake: 

 Hili lilihusisha  vitu vyote vilivyomzunguka Ayubu, vitu kama mali zake, wanyama wake, biashara zake pamoja na watumwa wake, n.k. Hawa wote shetani aliwapiga kama tunavyosoma habari katika Ayubu sura ya 1,  lakini hakuishia hapo alizidi kupiga kufikia hatua  kuwaua mpaka na watoto wake, na kumfanya Ayubu abaki peke yake, Lakini shetani alipoona hayo majaribu  bado hayamtikisi  Ayubu kwa namna yoyote zaidi ya yote aliishia kulibariki jina la BWANA. ibilishi akakusudia kubadilisha kinyago na kuamia kwenye ngazi ya juu iliyo nzito  zaidi. (lile Neno linatimia mtu hujaribiwa kulingana na Imani yake.)

Jaribu la Pili lilikuwa ni katika mwili wake: 

Tunasoma shetani alianza kumpiga Ayubu kwa magonjwa ya ajabu, majipu yaliyozuka mwili mzima yalimfanya Ayubu kufikia hatua ya kukonda sana na kukaa kwenye majivu muda wote akijikunia vigae. Kumbuka hili ni jaribu baya zaidi kuliko lile la kwanza kwasababu hili lilimuhusu yeye moja kwa moja. Afya yake ilidorora ghafla hivyo aliona kama mlango wa mauti unamwita muda wowote. Lakini pamoja na hayo Ayubu aliushikilia uelekevu wake, hatua hii ndiyo iliyomfanya hata mke wake Ayubu amkufuru Mungu, kwa kuona kuwa huyo Mungu waliyekuwa wanamtumainia kwa hatua hiyo waliofikia sasa hana msaada wowote kwao, kwa mume wake na kwa familia yake, Hivyo hakuna sababu ya kumtumikia tena. Lakini alizidi kuvumilia kwa muda mrefu na shetani alipoona ameshindwa, akaamia kwenye hatua nyingine ya juu zaidi ambayo ndiyo ngumu na ya hatari kuliko zote kiasi kwamba ingekuwa ni rahisi Ayubu kuchukuliwa na shetani kama asingesimama kikamilifu na Mungu wake. Hii ndio silaha ya mwisho shetani anayoitumia kuwamaliza watu wa Mungu. Na hakuna nyingine iliyojuu ya hiyo.

Jaribu la Tatu lilikuwa la rohoni: 

Kule Ayubu alipokuwa anapashikilia ndipo, hapo hapo shetani alipopajia. Kumbuka kitabu cha Ayubu sehemu kubwa kinaeleza juu ya hili jaribu la tatu, ambalo ndio msingi na kila mtu anapaswa afahamu kwasababu hapo ndipo siri hii ilipokaa, (hivyo unaposoma biblia soma kwa kujifunza vinginevyo masomo makuu na ya msingi yaliyo ndani yake yatakupita kama utakuwa unasoma tu kama gazeti). Sasa hapa tunaona ni mapambano ya moja kwa moja kati ya Shetani na Ayubu. Sasa kama tunavyosoma mara baada ya Ayubu kuzidi kushikilia msimamo wake na Mungu wake licha ya kwamba ana magonjwa na kufiwa na watoto wake, lakini bado yupo na Mungu wake. Shetani ndipo sasa akaingia kazini kwa kawatia mafuta watumishi wake wa uongo, ili waende kumgeuza moyo Ayubu kwa mafundisho ya udanganyifu. Na hawa si wengine zaidi ya ELIFAZI, SOFARI, NA BILDADI.

Hawa walikuwa ni marafiki zake na Ayubu wa Karibu, ni watu pia waliomcha Mungu lakini sio kwa kiwango cha Ayubu. walikuwa ni Wazee wenzake, washauri wenzake, ambao pengine kwa wakati wakiwa pamoja waliweza kuwafundisha  hata watu wengine njia za haki, na ukamilifu. Walipata sifa nzuri kwa Ayubu na ndio maana Ayubu aliweza kuwachagua wao tu! kuwa kama marafiki zake na washauri wake wa karibu. Lakini katika hatua kama hii walionekana kama wapo kinyume na Ayubu. Hii inadhihirisha kuwa mtazamo wao juu ya UKAMILIFU ulikuwa ni tofauti na wa AYUBU. Sasa kama tukichunguza habari zao kwa karibu tunaona moja kwa  moja kwa kumtazama Ayubu katika hali aliyokuwa nayo wakaanza kumuhukumu kuwa, hakika kuna mahali amemkosea Mungu. Lakini sababu zao walizozitoa za Ayubu kumkosea Mungu hazikuwa za “rohoni” bali za nje tu, lakini wenyewe waliangalia vya “mwilini” wakilinganisha na vya rohoni (kwamba ndio kigezo cha kukubaliwa na Mungu). Na hii ndio sababu kubwa iliyowafanya wapishane na Ayubu.

Sasa ukitazama moyo wa Ayubu utaona yeye alijua kuwa ushahidi mkubwa wa kukubaliwa na Mungu upo katika moyo wake(uhusiano binafsi alionao na Mungu wake, na si vinginevyo.) pasipo kujali anapitia hali ya namna gani ya nje! iwe ni umaskini, shinda, njaa, uchi, magonjwa n.k. na ndio maana vilipotokea aliweza kustahimili kwasababu alijua ndani ya moyo wake hakijaharibika kitu, hajaona kama amefanya  jambo la kumkosea Mungu. Uwepo wa Mungu ndani yake ulikuwa upo pale pale. Lakini wale marafiki zake watatu ambao wao walitumiwa na shetani kutenda kazi ile, walitazama kwa jicho lingine lisilo la ki-Mungu, na kuhitimisha kwamba kigezo pekee cha Mtu kukubaliwa na Mungu, ni kufanikiwa katika mambo yote, afya, familia, mali,mifugo  umri, n.k.basiii!!! sasa ukiona umepungukiwa na hayo yote basi ni dhahiri kuwa Mungu amekukataa na hayupo na wewe hivyo unapaswa UTUBU.  ndio yalikuwa mahubiri yao kwa Ayubu kuanzia mwanzo mpaka mwisho (Pata muda taratibu mwenyewe upitie kitabu cha Ayubu chote), na kibaya zaidi waliyathibitisha hayo waliyokuwa wanayasema kwa kutumia maandiko matakatifu, na mengine kufunuliwa kupitia maono usiku. Kiasi kwamba unaweza ukadhani ni Mungu kweli anazungumza na wewe kupitia watumishi wake. Embu Tusome baadhi ya maneno yao waliokuwa wanamuhubiria Ayubu..

Elifazi alianza kwa kumwambia Ayubu tukisoma Ayubu 4:6-9..

“6 Je! Dini yako siyo mataraja yako, Na matumaini yako si huo uelekevu wa njia zako?

7 Kumbuka, tafadhali, NI NANI ALIYEANGAMIA AKIWA HANA HATIA? Au hao waelekevu, walikatiliwa mbali wapi?
8 Kama mimi nilivyoona, hao walimao maovu, Na kupanda madhara, huvuna yayo hayo.

9 Kwa pumzi za Mungu huangamia. Na kwa kuvuma kwa hasira zake humalizika. “

Akiwa na maana kuwa kwamba Ayubu angekuwa ni mwelekevu kweli asingepatikana na shida zote hizo kwasababu walijua maandiko kwamba mwenye haki hawezi kukatiliwa mbali,(Na ni kweli ndivyo yanavyosema lakini yalitumika mahali pasipoyapasa)na pia  waliongezea “watu wapandao madhara huvuna hayo hayo” hivyo Ayubu kuwa vile ni kwasababu huko nyuma alikuwa ni mkaidi, hivyo kavuna alichokipanda.

Bildadi rafiki yake wa pili naye akaongezea na  kumwambia Ayubu:

Mlango 8

“1 Ndipo Bildadi huyo Mshuhi akajibu, na kusema,
2 Wewe utanena maneno haya hata lini? Maneno ya kinywa chako yatakuwa kama upepo mkuu hata lini?
3 Je! Mungu hupotosha hukumu? Au, huyo Mwenyezi hupotosha yaliyo ya haki?
4 KWAMBA WATOTO WAKO WAMEMFANYIA DHAMBI, NAYE AMEWATIA MKONONI MWA KOSA LAO;
5 Wewe ukimtafuta Mungu kwa bidii, Na kumsihi huyo Mwenyezi;
6 UKIWA WEWE U SAFI NA MWELEKEVU; HAKIKA YEYE SASA ANGEAMKA KWA AJILI YAKO, NA KUYAFANYA MAKAZI YA HAKI YAKO KUFANIKIWA.
7 Tena ujapokuwa huo mwanzo wako ulikuwa ni mdogo, Lakini mwisho wako ungeongezeka sana.
8 Basi, uwaulize, tafadhali, vizazi vya zamani, Ujitie kuyaangalia yale baba zao waliyoyatafuta;
9 (Kwani sisi tu wa jana tu, wala hatujui neno, Kwa kuwa siku zetu duniani ni kivuli tu;)
10 Je! Hawatakufunza wao, na kukueleza, Na kutamka maneno yatokayo mioyoni mwao?
11 Je! Hayo mafunjo yamea pasipo matope Na makangaga kumea pasipo maji?
12 Yakiwa yakali mabichi bado, wala hayakukatwa, Hunyauka mbele ya majani mengine.
13 Ndivyo ulivyo mwisho wa hao wamsahauo Mungu; Na matumaini y
ake huyo mbaya huangamia;
14 Uthabiti wake utavunjika, Na matumaini yake huwa ni nyuzi za buibui.
15 Ataitegemea nyumba yake, isisimame; Atashikamana nayo, isidumu.
16 Yeye huwa mti mbichi mbele ya jua, Nayo machipukizi yake huenea katika bustani yake.
17 Mizizi yake huzonga-zonga chuguu, Huangalia mahali penye mawe.
18 Lakini, aking’olewa mahali pake, Ndipo patamkana, na kusema, Mimi sikukuona.
19 Tazama, furaha ya njia yake ni hii, Na wengine watachipuka kutoka katika nchi.
20 Tazama, Mungu hatamtupa mtu mkamilifu, Wala hatawathibitisha watendao uovu.
21 Bado atakijaza kinywa chako kicheko, Na midomo yako ataijaza shangwe.
22 Hao wakuchukiao watavikwa aibu; Nayo hema yake mwovu haitakuwako tena”.

Unaona hapo tunaona Bildadi anamwambia Ayubu sababu pekee ya watoto wake kuangamizwa ni kwasababu watoto wake walikuwa ni waovu. Lakini tunasoma Ayubu alikuwa kila siku anaamka alfajiri kuwaombea watoto wake rehema na dua kwa Mungu. Yaani kwa ufupi Bildadi alimaanisha kuwa kifo, misiba, wakati wote ni matokeo ya kutokuwa mwelekevu mbele za Mungu. Bildadi aliendelea kumlaumu Ayubu kwamba kama kweli angekuwa ni mkamilifu mbele za Mungu, basi Mungu mwenyewe angenyanyuka amtete, lakini sasa mbona bado anaonekana hali yake iko vile vile tena ndio ikizidi kuwa mbaya zaidi. Kwahiyo matatizo yale ni ushahidi tosha kwamba maisha yake hayapendezi hata kidogo mbele za Mungu.

Na rafiki yake wa mwisho Sofari aliendelea kumvunja moyo Ayubu na kusema..

Mlango 20

“1 Ndipo Sofari, Mnaamathi, akajibu, na kusema,
2 Kwa hiyo mawazo yangu hunipa jawabu, Kwa ajili ya haraka niliyo nayo ndani yangu.
3 Nimesikia maonyo yanayonitahayarisha, Nayo roho ya ufahamu wangu hunijibu.
4 Je! Hujui neno hili tangu zamani za kale, Tangu wanadamu kuwekwa juu ya nchi,
5 YA KUWA SHANGWE YA WAOVU NI KWA MUDA KIDOGO, NA FURAHA YA WAPOTOVU NI YA DAKIKA MOJA TU?.
6 Ujapopanda ukuu wake mpaka mbinguni, Na kichwa chake kufikilia mawinguni;
7 HATA HIVYO ATAANGAMIA MILELE KAMA MAVI YAKE MWENYEWE; HAO WALIOMWONA WATASEMA, YUKO WAPI?
8 Ataruka mfano wa ndoto, asionekane; Naam, atafukuzwa kama maono ya usiku,
9 Jicho lililomwona halitamwona tena; Wala mahali pake hapatamtazama tena.
10 Watoto wake watataka fadhili kwa maskini, Na mikono yake itarudisha mali yake.
11 Mifupa yake imejaa ujana wake, Lakini utalala nchi naye mavumbini.
12 Ingawa uovu una tamu kinywani mwake, Ingawa auficha chini ya ulimi wake;
13 Ingawa auhurumia, asikubali kuuacha uende zake. Lakini akaushika vivyo kinywani mwake;
14 Hata hivyo chakula chake matumboni mwake kinabadilika, Kimekuwa ni nyongo za majoka ndani yake.
15 Amemeza mali, naye atayatapika tena; Mungu atayatoa tumboni mwake.
16 Ataamwa sumu ya majoka; Na ulimi wa fira utamwua.
17 Hataiangalia hiyo mito ya maji, Vile vijito vilivyojaa asali na siagi.
18 Aliyoyataabikia kazi atayarudisha, asiyameze; Kwa mali aliyoyapata, hatafurahi.
19 Kwa maana amewaonea na kuwaacha maskini; Amenyang’anya nyumba kwa jeuri, wala hataijenga.
20 Kwa sababu hakujua utulivu ndani yake, Hataponya cho chote katika hicho alichokifurahia.
21 Hakikusalia kitu asichokula; Kwa hiyo kufanikiwa kwake hakutadumu.
22 Katika kujaa kwa wingi wake atakuwa katika dhiki; Mkono wa kila anayesumbuliwa utamjia.
23 Hapo atakapo kulijaza tumbo lake, Mungu atamtupia ukali wa ghadhabu zake, Na kuunyesha juu yake akiwa anakula.
24 Ataikimbia silaha ya chuma, Na uta wa shaba utamchoma kwa pili.
25 Yeye autoa, nao watoka mwilini mwake; Naam, ncha ing’aayo yatoka katika nyongo yake; Vitisho viko juu yake.
26 Giza lote linawekwa kwa ajili ya hazina zake; Moto ambao haukuvuviwa na mtu utamla; Utayateketeza yaliyosalia hemani mwake.
27 Mbingu zitafunua wazi uovu wake, Nayo nchi itainuka kinyume chake.
28 Maongeo ya nyumba yake yataondoka, Yatamwagika mbali ka
tika siku ya ghadhabu zake.
29 Hii ndiyo sehemu ya mtu mwovu itokayo kwa Mungu, Na urithi aliowekewa na Mungu”.

Kama tunavyosoma hapo, Sofari naye hakuona haya kumwambia Ayubu kwamba yeye alikuwa katika “shangwe za watu waovu ambazo hazidumu ni za muda tu”. Akiwa na maana kuwa Mali Ayubu alizokuwa nazo kwanza zilikuwa ni za muda tu! kwasababu hazikuwa ni za haki, akimaanisha kuwa uthibitisho pekee wa Mungu kuwa na Ayubu ni mali zidumuzo na kama hazidumu basi hizo ni shangwe za waovu. Hivyo hatuwezi kueleza habari zao zote lakini ukiwa na muda pitia kitabu cha Ayubu chote utaona Injili ya hawa watu ilivyokuwa kwa Ayubu na jinsi walivyoweza kutumia maandiko na maono kuthibitisha uongo wao ili tu wamfanye Ayubu auache uelekevu wake mbele za  Mungu. Hawa ndio walimfadhaisha Ayubu mara mia elfu zaidi hata ya kupotelewa na watoto na mali zake, kwasababu walikuwa wanataka kumfanya Ayubu atilie shaka uelekevu wake mbele za Mungu.  walifanyika kama vyombo vya shetani kumjaribu Ayubu.

Mambo hayo yameandikwa ili kutuonya sisi watu wa zamani hizi, Shetani anapomaliza kumjaribu mkristo kwa magonjwa, kwa dhiki, kwa misiba, kwa udhaifu, kwa kupungukiwa na mali, kwa vifungo, kwa mateso, kwa shida, kwa njaa, n.k na kuona kuwa mtu huyo bado kasimama katika imani yake na uelekevu wake kama Ayubu basi huwa  anabadilisha mfumo wake wa majaribu, na kuleta majaribu magumu zaidi, na ya hatari zaidi, anakuletea watu aliowatia yeye mafuta, mfano wa akina ELIFAZI,SOFARI, NA BILDADI ambao watatumia maandiko kukushawishi na kukuhakikishia kwamba njia unayoiendea sio sahihi, na kama hauna Roho wa Mungu ni rahisi sana kuchukuliwa na uongo wa watu hao, watakwambia KIGEZO PEKEE cha Mungu kukukubali ni wewe kuwa na MALI, kigezo pekee cha kuwa Mungu hajakutupa ni kutokupitia shida kabisa, watakwambia ukipitia misiba basi kuna tatizo kwenye imani yako, watakwambia ukipitia magonjwa basi kuna mahali umemuudhi Mungu, ukiwa na ulemavu fulani basi kuna laana fulani inakufuata kwasababu wenye haki lazima wawe na afya, watakuhakikishia kwa maandiko kabisa “Mpenzi naomba ufanikiwe katika mambo yote na kuwa na afya yako, kama vile roho yako ifanikiwavyo. “

watu kama hawa hata siku moja hawataangalia AFYA YA ROHO YAKO, kwamba je! unaishi maisha matakatifu?, au unayo imani? au una upendo? au je! unamzalia Mungu matunda ya haki?? au unamfanyia Mungu ibada ya kweli? wao wataangalia AFYA YA MWILI wako tu! na siku ikitetereka kidogo tu, basi umekwisha chukuliwa nao utaishia kuudharau ukristo na kusema ni ulokole tu,

Ndugu jiepushe nao, wanaipotosha kweli ya Mungu, ni shetani kawainua kuwajaribu watu wa Mungu, na kuwavunja moyo na kuwakatisha tamaa ili waiache imani, kwasababu laana kubwa mbele za Mungu sio kupungukiwa mali, au kukosa afya,au kupitia misiba au dhiki, hapana bali laana kubwa mbele za Mungu ni kutomwamini yeye aliyetumwa na yeye (yaani Yesu Kristo),na  kukosa uhusiano binafsi na Mungu kwasababu biblia inasema..

Warumi 8: 35 “Ni nani atakayetutenga na upendo wa Kristo? Je! Ni dhiki au shida, au adha, au njaa, au uchi, au hatari, au upanga?

36 Kama ilivyoandikwa, ya kwamba, Kwa ajili yako tunauawa mchana kutwa, Tumehesabiwa kuwa kama kondoo wa kuchinjwa.

37 Lakini katika mambo hayo yote tunashinda, na zaidi ya kushinda, kwa yeye aliyetupenda.

38 Kwa maana nimekwisha kujua hakika ya kwamba, wala mauti, wala uzima, wala malaika, wala wenye mamlaka, wala yaliyopo, wala yatakayokuwapo, wala wenye uwezo,

39 wala yaliyo juu, wala yaliyo chini, wala kiumbe kinginecho chote hakitaweza kututenga na upendo wa Mungu ulio katika Kristo Yesu Bwana wetu”.

Hivyo ndugu yatangeneze maisha yako kwa kumpenda Bwana Mungu wako pasipo kupelekwa na upepo huku na huku au  kundi hili la waalimu na manabii wa uongo,(Hao ndio manabii wa uongo wa siku za mwisho) Biblia inasema kila jambo na majira yake wakati wa kupanda na wakati wa kuvuna, wakati wa kulia na wakati wa kucheka, wakati wa kujenga na wakati wa kubomoa, mkumbuke Ayubu baada ya yale majaribu Bwana alimrudishia mara mbili ya vile alivyovipoteza, lakini kama angewasikiliza wale rafiki zake leo hii angekuwa wapi?. Si angeishia kumwangalia Mungu katika kioo cha mafanikio tu??. lakini hakuruhusu imani yake ipotee na zile mali za kwanza alizokuwa nazo, alitunza uhusiano wake binafsi na Mungu katika hali yoyote aliyopo, nasisi vivyo hivyo tuwe matajiri, au maskini, tuwe na vitu au tusiwe na vitu, tuwe wazima au tuwe wagonjwa, uhusiano wetu na Mungu unapaswa uwe pale pale kama Ayubu, usiyumbishwe na mazingira ambayo shetani anayaleta kupitia watumishi wake wa uongo ambao ndio sasahivi wamezagaa kila mahali kuwarubuni watu na mafundisho yao ya kujigamba.

Bwana akubariki sana.

Pia unaweza ukapata mafundisho haya Kwa njia ya Whatsapp yako, jiunge na channel yetu Kwa kubofya hapa >> WHATSAPP


Mada Nyinginezo:

AYUBU 28 : HEKIMA NI NINI? NA UFAHAMU UNAPATIKANA WAPI?

‘’MOTO HUFA KWA KUKOSA KUNI’’..NA NDIVYO ILIVYO KWA UASHERATI

AYUBU ALIJARIBIWA KWA MUDA GANI?.

KITABU CHA YASHARI KINACHOZUNGUMZIWA KATIKA 2SAMWELI 1:17-18, NI KITABU GANI?

KWANINI SAMWELI ALIRUHUSIWA KUHUDUMU HEKALUNI KAMA VILE WALAWI WAKATI YEYE NI MU-EFRAIMU?


Rudi Nyumbani

Print this post

About the author

Admin administrator

Subscribe
Notify of
guest
0 Comments
Inline Feedbacks
View all comments