UTEKA ULIOGEUZWA.

UTEKA ULIOGEUZWA.

Ukisoma kitabu cha Ayubu utagundua kuwa jaribu kubwa shetani alilomshambulia Ayubu halikuwa Kufiwa na wanawe au kupoteza mali zake zote ndani ya siku moja! Hayo kweli yalimuumiza sana…lakini utaona Ayubu hakuongea lolote kuhusu hayo…Alisema tu BWANA ALITOA na BWANA AMETWAA…Jina la Bwana libarikiwe. Basi akaishia hapo! Ndio maana unaona mpaka sura ya Pili habari ya Ayubu inakuwa imeshaisha…

Lakini kuanzia sura ya 3 hadi ya 42…utaona ni habari nyingine zinaanza kuzungumziwa hapo…utaona ni mazungumzo kati ya watu watatu mpaka wane…Ayubu, Sofari, Bildadi na Elifazi…akitoka huyu anaongea huyu, akitoka huyo sofari anaongea bildadi, akitoka bildadi anaongea Ayubu hivyo hivyo mpaka mpaka sura ya 40.

Sasa wengi wetu tunapenda kusoma tu ile sura ya kwanza na ya Pili tukidhani kuwa ndio lengo la kile kitabu cha Ayubu, lakini hiyo sio kweli..Ufunuo mkubwa wa kitabu cha Ayubu upo kuanzia ile sura ya 3 na kuendelea…kuanzia ile sura ya 3 na kuendelea ndio utaona jinsi gani shetani alivyokuwa anampepete Ayubu kwa kupitia vinywa vya wale marafiki zake watatu.

Utaona jinsi gani wale marafiki zake Ayubu, walivyokuwa wanatumia maandiko kuivunja imani ya Ayubu. Nakushauri ndugu kama hujakipitia kitabu cha Ayubu kuanzia hii sura ya 3 na kuendelea kafanya hivyo leo..Kuna mambo mengi sana Bwana atakuonyesha ambayo ulikuwa huyajui.

Shetani anakawaida ya kuwa..akishindwa kumjaribu mtu kwa njia ya kawaida ya nje! Huwa anabadilisha mbinu na kuja kwa njia nyingine ya kutumia maandiko, atawaingia hata wapendwa au hata wachungaji kukuhakikishia jambo Fulani ambalo sio sahihi, nia na madhumuni ni kukuangusha tu!. Ili kulielewa hili vizuri chukua mfano ufuatao.

Tuseme shetani anataka kumwangusha mtu anayeitwa Amelia aanguke kwenye dhambi ya uasherati. Atakachokifanya kama kawaida atatafuta kwanza kibali kutoka kwa Mungu, akishakipata ataanza kutikisa kwanza uchumi wake..ili amweke katika mazingira ya uhitaji wa fedha, wakati yupo katika hayo mazingira ya kuhitaji fedha anatokea mtu mwenye fedha nyingi kidogo na kumshawishi. Na atakaposhinda vile vishawishi na kumkataa Yule mtu…Shetani atamjaribu kwa njia nyingine, atamletea mpaka magonjwa ilimradi tu! Atafute njia mbadala ya kupata fedha kwa kuutoa mwili wake….Na endapo akimwona bado huyo mwanamke kasimama…atamjaribu kwa njia nyingine mbalimbali..Na mwishowe ataacha na kuingia kwenye mbinu yake ya mwisho na kuu kuliko zote ya kumwangusha.

Katika hiyo mbinu yake ya mwisho hatatumia tena watu wa nje kumshawishi, kwasababu anajua huyu dada Amelia amesimama hawezi kutikiswa na watu wasiomjua Mungu, atakachokifanya atamfuata kule kule kanisani kwasababu imani yake yote ipo katika nyumba ya Mungu na anawaamini watu wa Mungu.

Kwahiyo siku moja ataingia kanisani na kusikia mahubiri yafuatayo…. “kuna watu humu ndani wanachezea bahati, utakuta mtu anashida, Mungu anamfungulia mlango wa fedha anakataa, unakuta mtu ni mgonjwa, hana hela anakuja mtu anataka kumsaidia anakataa, kwa njia hiyo hata kuolewa hutaolewa..dada! na watu wote kanisani wanajibu Ameen!” Na huyo mtumishi atasoma mistari kadha kadhaa kwenye biblia kuthibitisha mahubiri yake.

Sasa kwa mahubiri kama hayo..huyu dada atatoka kanisani huku kuna kitu kinamuhukumu ndani,…anaanza kujitathimini pengine lile Neno lilikuwa linamhusu yeye…Ni watu wangapi wamekuja kumjaribu akawakataa…pengine kweli anachezea bahati! Akijiangalia ni kweli ana matatizo ya fedha, sasa Kidogo kidogo anaanza kushawishika na kuhisi alikuwa anafanya makosa kujiepusha na wale watu waliokuwa wanakuja kumjaribu, anaanza kufikiri pengine hata alikuwa anamkosea Mungu, hivyo baada ya siku kadhaa akitokea mwingine anaanza kumsikiliza na mwishowe kuanguka kwenye dhambi ya uasherati na kushindwa na shetani.

Hizo ndizo njia shetani anazozitumia kuwaangusha wengi waliosimama…Na ndio Ayubu naye yalimkuta hayo hayo…shetani alipoona hatetereki hata kwa msiba wa wanawe..akawaingia marafiki zake Ayubu watatu ambao nao pia walikuwa tunaweza kusema ni watumishi kama Ayubu, walikuwa wanamtafuta Mungu pamoja naye na kusali pamoja naye. Wakaanza kumwambia Ayubu, tatizo haliko kwa Mungu, tatizo lipo kwako, haiwezekani yakupate haya yote wewe tu na si mtu mwingine, lazima utakuwa umetenda dhambi kwahiyo nenda katubu! Ubadilishe na njia zako. Na walitumia maaandiko kumshawishi Ayubu ageuke aiache njia yake. Lakini tunaona Ayubu alisimama thabiti mpaka Mwisho na hatimaye Bwana akageuza uteka wake..

Sasa leo kwa Neema za Bwana hatutazungumzia sana juu ya huduma za hawa rafiki zake watatu Ayubu, kama utahitahi somo kwa urefu kuhusu huduma zao unaweza ukawasiliana na mimi inbox nikutumie somo hilo.

Lakini leo tutazungumzia ni kwa namna gani Bwana alimrejeshea Ayubu mali zake zote maradufu na familia yake. Kwa namna hiyo hiyo na sisi tunaweza kuzipata Baraka zetu maradufu endapo tukifanya kama Ayubu alivyofanya.

Ukisoma Mwishoni mwa kitabu cha Ayubu ile sura ya 42 tunasoma..

Ayubu 42: 7 “Basi ikawa, baada ya Bwana kumwambia Ayubu maneno hayo, Bwana akamwambia huyo Elifazi Mtemani, Hasira zangu zinawaka juu yako, na juu ya hao rafiki zako wawili; kwa kuwa ninyi hamkunena yaliyo sawa katika habari zangu, kama alivyonena mtumishi wangu Ayubu.

8 Basi sasa, jitwalieni ng’ombe waume saba, na kondoo waume saba, mkamwendee mtumishi wangu Ayubu, mjisongezee sadaka ya kuteketezwa; na huyo mtumishi wangu Ayubu atawaombea ninyi; kwa kuwa nitamridhia yeye, nisiwatende sawasawa na upumbavu wenu; kwani ninyi hamkunena maneno yaliyonyoka katika habari zangu, kama alivyonena mtumishi wangu Ayubu.

9 Basi Elifazi, Mtemani, na Bildadi, Mshuhi, na Sofari, Mnaamathi, wakaenda, wakafanya kama vile Bwana alivyowaamuru; naye Bwana akamridhia Ayubu.

10 KISHA BWANA AKAUGEUZA UTEKA WA AYUBU, HAPO ALIPOWAOMBEA RAFIKI ZAKE; BWANA NAYE AKAMPA AYUBU MARA MBILI KULIKO HAYO ALIYOKUWA NAYO KWANZA.

11 Ndipo wakamwendea nduguze wote, waume kwa wake, nao wote waliojuana naye hapo zamani, wakala chakula pamoja naye katika nyumba yake; nao wakamlilia na kumtuza moyo katika habari za huo uovu wote Bwana aliouleta juu yake; kila mtu akampa kipande cha fedha, na pete ya dhahabu kila mmoja.

12 Basi hivyo Bwana akaubarikia huo mwisho wa Ayubu zaidi ya mwanzo wake; naye alikuwa na kondoo kumi na nne elfu, na ngamia elfu sita, na jozi za ng’ombe elfu, na punda wake elfu.

13 Tena alikuwa na wana waume saba, na binti watatu.

14 Akamwita huyo wa kwanza jina lake Yemima; na wa pili akamwita jina lake Kesia; na wa tatu akamwita jina lake Keren-hapuhu.

15 Katika nchi hiyo yote hawakuwapo wanawake waliokuwa wazuri kama hao wana wa Ayubu; na baba yao akawapa urithi kati ya ndugu zao wana waume.

16 Kisha baada ya mambo hayo Ayubu akaishi miaka mia na arobaini, naye akawaona wanawe, na wana wa wanawe, hata vizazi vinne.

17 Basi Ayubu akafa, mzee sana mwenye kujawa na siku”.

Nataka uuone huo mstari wa 10 unaosema.. “ kisha bwana akaugeuza uteka wa ayubu, HAPO ALIPOWAOMBEA RAFIKI ZAKE; Bwana naye akampa ayubu mara mbili kuliko hayo aliyokuwa nayo kwanza”.

HAPO ALIPOWAOMBEA RAFIKI ZAKE”…hilo ndilo Neno la Msingi la leo. Pamoja na kwamba shetani aliwatumia rafiki zake kumjaribu yeye, pamoja na kwamba rafiki zake walimchukiza sana Mungu, mpaka hasira za Bwana zikawaka juu yao, akataka kuwaua…Lakini Ayubu hakuwahukumu wala kuwachukia aliwahurumia…akaenda akapiga magoti akawaombea toba! Na msamaha! Akatubu kwa ajili yao kwa dhabihu na machozi…Akawaombea rafiki zake Baraka badala ya Laana, heri badala ya shari..Na Mungu akawasamehe.. Na Bwana akapendezwa sana na AYUBU kwasababu hiyo ya kuwaombea rafiki zake…ndipo UTEKA WAKE UKAGEUZWA.. Akapewa vile vitu mara mbili..Bwana akamrudishia vyote alivyopoteza HALELUYA!!

Tunajifunza nini hapo?…kuna watu watatumiwa na shetani kutujaribu, hususani wanaotumia biblia..pengine ni marafiki zetu au ndugu zetu, na kwasababu Neno la Mungu linakaa ndani yetu, tunazitambua fikra za shetani ndani yao..Na mambo wanayofanya ukaona kabisa yanamchukiza Mungu na Mungu kawakasirikia, sasa huo sio wakati wa kupiga maadui yako!! Sio wakati kusema walaaniwe maadui zangu, wafe maadui zangu, waanguke!! Hapana! Biblia haitufundishi hivyo hata kidogo…inatufundisha kwenda kwenye magoti kutubu kwa ajili yao, kuwaombea msamaha, kulia hata ikiwezekana kutoa sadaka kwa ajili yao…hivyo ndivyo Bwana naye atakavyogeuza UTEKA WETU! Ndugu jitenge na injili za kupiga maadui si za kimaandiko hata kidogo…ukifanya hivyo Mungu hatageuza uteka wako hata kidogo. Tujifunze kwa Ayubu hakuna mtu aliyeumizwa moyo kama Ayubu, kapata msiba na wakati huo huo rafiki zake wanamwambia ana dhambi nyingi…inaumiza kiasi gani, lakini hakuwalaani bali aliwaombea..

Biblia inasema katika Mithali 24: 17 “Usifurahi, adui yako aangukapo; Wala moyo wako usishangilie ajikwaapo;

18 Bwana asije akaliona hilo, likamkasirisha; Akageuzia mbali naye hasira yake”.

Unaona! Ndio maana Bwana alisema “ombea adui yako”..kwasababu unavyomwombea ndivyo Bwana anavyogeuza uteka wako.

Bwana akubariki sana.

Pia unaweza ukapata mafundisho haya Kwa njia ya Whatsapp yako, jiunge na channel yetu Kwa kubofya hapa >> WHATSAPP

Kwa Maombezi, Ushauri au Ratiba za Ibada, Wasiliana nasi kwa namba

+225693036618/ +225789001312


Mada Zinazoendana:

HUDUMA YA (ELIFAZI, BILDADI, NA SOFARI).

MNGOJEE BWANA

AYUBU ALITESEKA KATIKA MAJARIBU KWA MIAKA MINGAPI?.

NINAJUA MAWAZO NIKUWAZIAYO:

AYUBU 28 : HEKIMA NI NINI? NA UFAHAMU UNAPATIKANA WAPI?


Rudi Nyumbani

Print this post

About the author

Admin administrator

Subscribe
Notify of
guest
0 Comments
Inline Feedbacks
View all comments