MWAMUZI WA KWELI:

MWAMUZI WA KWELI:

Shalom mtu wa Mungu, ni siku nyingine tumepewa neema ya kuishi, Hivyo karibu kwa pamoja tushiriki kujifunza maneno ya uzima, ambayo ndio msingi hasaa wa sisi kuwa hapa duniani.

Tukisoma biblia tunaona jinsi Mungu alivyowanyanyua waamuzi wengi tofauti tofauti kwa udhihirisho tofauti tofauti katika vipindi vya awali kabisa baada ya wana wa Israeli kutoka katika nchi ya Misri,Na Mungu aliwanyanyua kwa lengo lile lile moja la kuwarejesha watoto wake katika njia sahihi, kuwarejesha mahali ambapo walipaswa wawepo.Hivyo kitu alichokifanya Mungu kwa wakati ule ni kumtia “mafuta ya kipekee” mtu mmoja ili aende kushughulika ipasavyo na yule adui yao mtekeaji, na mwisho wa siku wanapata ukombozi wao kuwa yule mtu Mungu aliyemtia mafuta..

Kwa mfano tunaweza kumwona Musa, Mafuta yaliyokuwa juu ya Musa ni ISHARA NA MIUJIZA na yale MAPIGO. Hivyo kwa kupitia huduma hiyo aliweza kukishusha kiburi cha Farao na Misri nzima na hivyo wakaweza kuwaacha wana wa Israeli waende katika nchi yao Mungu aliyokusudia wafike ili wakamtumikie Mungu. Lakini japo ishara zile kubwa zilionekana kwa mkono wa Musa bado watu wale hawakupata ukombozi mkamilifu ambao ungewafanya wawe huru kabisa kabisa mbali na maadui zao wote.

Tunaona pia wakati mwingine Mungu aliwanyanyanyulia mwamuzi mwingine baada ya kutumikishwa na maadui zao kwa muda mrefu kutokana na dhambi zao wenyewe ndipo Mungu akawaletea Gidioni kwa Roho(Mafuta) ya ushujaa ili kuwaamua kwa upanga,(Waamuzi 6)..Ni kweli mwisho wa siku walipata ukombozi, lakini ukombozi ule ulikuwa ni wa kitambo tu, baada ya muda kidogo watu walirejea katika dhambi zao za kumwasi Mungu.

Hali kadhalika tunaona wakati mwingine Mungu alimtia mafuta Samsoni katika upako wa “Nguvu za kibinadamu”…Hivyo kwa nguvu zile za kimwili aliweza kuwashida wafilisti mpaka kuwafanya wawaache huru kabisa wana wa Israeli. Lakini ukombozi ule ulidumu kwa muda tu, haukuweza kutoa ulinzi wa kudumu kwa wana wa Israeli,kwa wakati ujao.Ndivyo ilivyokuwa siku zote waamuzi zaidi ya waamuzi 12 walipita juu ya Israeli.

Hali kadhalika wakati ulipofika walipohitaji kiongozi, Mungu aliwanyanyulia mtu mwenye Hekima atakayeweza kuwaamua katika mambo yote. Na hivyo akatokea Sulemani, wakamfurahia kwa muda lakini alipokengeuka kwa muda nchi ilitetereka kwa kasi sana, na kusababisha watu kurejea katika hali zao za zamani.

Vivyo hivyo tunaona kwa manabii kama Samweli, Eliya, Elisha, Samweli, Yehu, Yohana mbatizaji ambaye Yesu alisema watu waliifurahia nuru yake kwa kitambo tu (Yohana 5:35) na baadaye ikazima..wote hao Mungu aliwatia mafuta kwa namna tofauti tofauti ili kuwaokoa au kuwarejesha wana wa Israeli katika mstari waliopaswa wawe, lakini hakukuwa na hata mmoja aliyefanikiwa kuleta ukombozi mkamilifu wa kudumu kwa watoto wa Mungu, licha ya kuwa walikuwa hodari na mashujaa.

Lakini tunasoma katika biblia wakati ulipofika wa Mungu kumleta KRISTO duniani, hakuja na kauli mbiu ya mapanga au nguvu za misuli kama Samsoni, hapana badala yake alikuja kutumbua JIPU ambalo lilikuwa limekaa kwa muda mrefu kwa SIRI tangu zamani ambalo ndio lilokuwa linawafanya watoto wa Mungu wajione ni wananafuu kwa kipindi kifupi tu pale wanapookolewa na waamuzi lakini kumbe ugonjwa bado upo ndani yao, na ndio maana mwisho wa siku wanaishi kurudia kumuudhi Mungu..

Waamuzi wote waliotangulia walikuwa wanatoa tu dawa za kutuliza maumivu (Pain-killer), lakini YESU alipokuja kuutibu ugonjwa wote,kutoa mpaka mzizi wa mwisho na kisiki, wala hakikusalia chochote si hata kovu la alama.

Na ugonjwa huo si mwingine zaidi ya DHAMBI ambayo chimbuko lake ni SHETANI.

Na ndio maana ukisoma agano la kale utaona Shetani akitajwa mara chache sana, utaona shetani akijidhihirisha mara chache sana, tofauti na ilivyo katika agano jipya…Hivyo BWANA alivyokuja ilikuwa ni kwa lengo la kumweka huru mwana yoyote wa Mungu, tena kuwa huru kweli kweli, na sio nusu nusu kesho utumwa unajirudia… na ndio maana baada yake yeye hakuna mkombozi mwingine yeyote anayehubiriwa, hata hapa hatumuhubiri mtu mwingine zaidi ya YESU yule aliyesulibiwa miaka 2000 iliyopita na aliyeandikwa kwenye biblia takatifu kwamba yeye ndiye anayeweza Kumwokoa mtu na kumfanya kuwa huru kweli kweli, hana mshirika na yeye ndiye mwanzo na mwisho, hakuna mwingine.

Yeye mwenyewe anasema.. Yohana 8:36 “Basi Mwana akiwaweka huru, mtakuwa huru kweli kweli”.

YESU anakomesha dhambi kwa mtu yeyote anayemwamini, kumbuka dhambi ndio chimbuko la kila kitu; dhambi, ndio chimbuko la magonjwa, ndio chimbuko la mateso, ndio chimbuko la tabu, ndio chimbuko la kuteswa na mapepo, ndio chimbuko la kukosa raha, na kukata tamaa ya kuishi ndio chimbuko la masumbufu ya kila namna unayoyofahamu wewe huku duniani, ndio chimbuko la mauaji na vitendo vyote viovu vinavyoendelea huku duniani…n.k.

Dhambi ndio “control tower” ya shetani, ndio dira yake hiyo kukumaliza wewe na mimi..Wana wa Israeli walikuwa wanapata ukombozi wa miili yao kutoka kwa maadui zao, lakini hawakujua kuwa bado hajawekwa huru kweli kweli kwani yao dhambi bado zilikuwa zinawatawala, na shetani ametulia kimya asiwafunulie siri hiyo..na ndio maana baadaye waliendelea kurudi katika mateso yao ya siku zote, lakini mtu anayemwamini YESU KRISTO leo hii, hatarejea tena katika mateso yake ya kwanza.

Kumbuka wale waamuzi walipoondoka habari zao ziliishia pale pale lakini YESU wakati alipokuwa duniani alitujali na kutuombea kwa Baba tulindwe na yule mwovu, halikadhalika na alipopaa juu kwa Baba amesimama mpaka sasa kama kuhani mkuu akituombea kwa Mungu..Hivyo unaweza kuona hapo mtu aliye ndani ya Kristo kweli kweli sio wale mguu mmoja nje mwingine ndani hapana bali yule aliyekusudia kutembea na Kristo anayo faida nyingi kiasi gani!…Shetani anafahamu kabisa mtu wa namna hiyo hawezi kumpata tena milele, kwasababu mwamuzi wake, mkombozi wake anasimama mbele yake daima masaa 24, kumuamua na kumlinda.

Leo hii watu watashangaa inawezekanikaje mtu kuishi bila kuzini, mtu kuishi bila kutazama pornography, kuishi bila pombe, kuishi bila sigara, kuishi bila kuongoa matusi, inawezekanikaje mtu kuishi maisha ya furaha wakati huna pesa, inawezekanikaje unapitia shida zote hizo lakini bado tumaini lako lote lipo kwa Kristo, inawezekanikaje katika kizazi hiki cha Sodoma na Gomora, kutokuvaa suruali kwa mwanamke, na kuweka mawigi na ma-lipstick na marangi usoni, wala kupaka uwanja kama Yezebeli, inawezekanikaje unadumu katika imani bila kutetereka…

Hawajui kuwa nguvu hizo si zake bali ni za yule mwamuzi wake YESU KRISTO aliyemchagua maishani mwake, laiti zingekuwa ni zake asingekuwa vile alivyo leo…..

Maneno ya YESU yana nguvu ndugu, hilo tunalithibitisha kwa maombi yake aliyomwomba Baba akiwa hapa hapa duniani akisema..

Yohana 17: 9 “Mimi nawaombea hao; siuombei ulimwengu; bali hao ulionipa, kwa kuwa hao ni wako;

10 na wote walio wangu ni wako, na walio wako ni wangu; nami nimetukuzwa ndani yao.

11 Wala mimi simo tena ulimwenguni, lakini hawa wamo ulimwenguni, nami naja kwako. Baba mtakatifu, KWA JINA LAKO ULILONIPA UWALINDE HAWA, ili wawe na umoja kama sisi tulivyo.

12 Nilipokuwapo pamoja nao, mimi naliwalinda kwa jina lako ulilonipa, nikawatunza; wala hapana mmojawapo wao aliyepotea, ila yule mwana wa upotevu, ili andiko litimie.

13 Na sasa naja kwako; na maneno haya nayasema ulimwenguni, ili wawe na furaha yangu imetimizwa ndani yao.

14 Mimi nimewapa neno lako; na ulimwengu umewachukia; kwa kuwa wao si wa ulimwengu, kama mimi nisivyowa ulimwengu.

15 Mimi siombi kwamba uwatoe katika ulimwengu; BALI UWALINDE NA YULE MWOVU.

16 Wao si wa ulimwengu, kama mimi nisivyo wa ulimwengu.

17 Uwatakase kwa ile kweli; neno lako ndiyo kweli”.

Unaona hapo?, YESU aliwaombea wale waliomwini kuwa Baba awalinde na yule mwovu,na si watu wote..Sasa kama Kristo amekataa kukuombea mtu mwingine akikuombea ina faida gani?? ni sawa na bure tu!….hivyo mtu yeyote anayemwamini Kristo sasa kwa kumaanisha kabisa kumfuata na kujikana nafsi yake kama mitume na sio kwa maneno tu , hapo hapo bila kupoteza muda Neno hilo linakuwa linaanza kufanya kazi ndani yake, na ndio hapo anajikuta anao uwezo wa kuvishinda vishawishi vyote vya shetani vile ambavyo hapo mwanzo alikuwa hawezi kuvishinda kwasababu nguvu za shetani zinakuwa hazijakaa juu yake kumtawala.

Vile vile, hiyo haiishii hapo tu bali mtu huyo hata akihitaji lolote kutoka kwa Mungu, mwamuzi wake wakati wote yupo kumtetea huko juu mbinguni..Ni faida juu ya faida.

Warumi 8:33 “Ni nani atakayewashitaki wateule wa Mungu? Mungu ndiye mwenye kuwahesabia haki.

34 Ni nani atakayewahukumia adhabu? Kristo Yesu ndiye aliyekufa; naam, na zaidi ya hayo, amefufuka katika wafu, naye yuko mkono wa kuume wa Mungu; TENA NDIYE ANAYETUOMBEA”.

Sasa kama Mungu hapokei mashtaka yako…mtu mwingine akikushtaki yadhuru nini?

Unaona Faida zote hizo ni kwa mtu yule aliyemwamini Kristo,lakini ikiwa upo nje ya wokovu, au upo vuguvugu leo huku kesho kule, usijidanganye fahamu kuwa hutakaa uishinde dhambi milele, itaendelea kukusumbua na huku shetani akiichochoa zaidi na zaidi, utaendelea tu kutazama pornography, kufanya mustarbation na kuwa mzinzi, na kuvaa mavazi machafu ya kikahaba na kwako mambo hayo yataendelea kuwa magumu kuyaacha hata kama utatamani kuyaacha hutaweza kwasababu Kristo hajakamilika ndani yako..Na mwisho utakufa katika hali hiyo hiyo ya dhambi na kujikuta kuzimu. Kwasababu biblia hiyo hiyo inasema mshahara wa dhambi ni MAUTI!

Ni maombi yangu sote tutamtazama huyu MWAMUZI mkuu, aponyaye roho zetu na miili yetu kuanzia sasa, kwake kuna raha, kwake kuna amani, kwake kuna tumaini, kwake kuna utulivu…

Kwa kumalizia yatafakari maneno yake haya..

Mathayo 11: 28 “Njoni kwangu, ninyi nyote msumbukao na wenye kulemewa na mizigo, nami nitawapumzisha.

29 Jitieni nira yangu, mjifunze kwangu; kwa kuwa mimi ni mpole na mnyenyekevu wa moyo; NANYI MTAPATA RAHA NAFSINI MWENU;

30 kwa maana nira yangu ni laini, na mzigo wangu ni mwepesi”.

Ubarikiwe sana. Tafadhali “SHARE” ujumbe huu na wengine. Pia unaweza ukapata mafundisho haya Kwa njia ya Whatsapp yako, jiunge na channel yetu Kwa kubofya hapa >> WHATSAPP


Mada Zinazoendana:

TUNAYE MWOMBEZI.

HUDUMU YA MALAIKA WATAKATIFU.

NI KWASABABU YA YESU KRISTO.

DHAMBI YA ULIMWENGU.


Rudi Nyumbani

Print this post

About the author

Admin administrator

Subscribe
Notify of
guest
0 Comments
Inline Feedbacks
View all comments