PEPETO LA MUNGU.

PEPETO LA MUNGU.

Siku moja nilipokuwa nakula wali na choroko, nilikutana na zile choroko ngumu ambazo tunajua hata ukizipika vipi huwa haziivi, nilishazoea kukutana nazo mara kwa mara, lakini sikuhiyo nilikutana nazo nyingi kiasi cha kushindwa kula chakula, hapo ndipo nilipotamani kujua hasaa huwa zinaondolewaje kwenye choroko nzuri, kwasababu wakati zinachambuliwa huwa hazionekana, ni rahisi kweli kutoa uchafu wote, na makapi yote lakini zile haziondoki zina sura ile ile kama choroko nyingine..

Ndipo nikafuatilia na kuuliza, nikagundua kuwa kumbe choroko hazichambuliwi kama maharage, maharage utatoa uchafu unaouna na kwenda kuosha na kubandika kazi imeisha, lakini choroko huwa inaenda hatua nyingine ya ziada,..Na ndio maana ukila chakula kwenye hoteli nzuri inayothamini huduma zake, chakula kama hichi huwezi kukutana na hizo choroko-mawe mdomoni, niziite hivyo, je! wanafanya nini?.

Wao wakishamaliza kutoa ule uchafu unaoonekana katika hatua ya awali, na kuziosha vizuri choroko zao, hatua inayofuata huwa wanachukua maji ya moto, kisha wanaziweka choroko ndani yake, na kuziacha hapo kwa muda wa kama dakika 5 hivi, kisha warudi kuyamwaga yale maji yote, halafu wanazimwaga kwenye sinia au ungo, wanaanza kuchambua tena, Sasa zile choroko-mawe ambazo hata uzipike na makaa ya mawe haziivi, zinajionyesha zenyewe.Kwasababu katika hatua ya awali zile nyingine zinapoanza kubadilika rangi na kuwa kama jani lililokauka hivi, zenyewe huwa zinabakia na ukijani wake hivyo hivyo kama vile vimetolewa jana shambani,..Hivyo ni rahisi kuziona na kuzitoa moja moja na kuzitupa..baadaye zile zilizobakia nzuri, wanazirudisha jikoni, na kuzipika mpaka mwisho ziive, Na hapo hata ule sufuria nzima la choroko huwezi kukutana na choroko-mawe hata moja mdomoni..

Ndivyo ilivyo hata katika kanisa la Kristo, Mungu naye huwa anachambua watu wake, katika hatua za awali, anawaita wengi sana kwake, na wengi wanamwamini na kusema mimi ni mkristo, nimeokoka, kiasi kwamba ni ngumu kutofautisha mkristo wa kweli ni yupi na Yule feki ni yupi, wote wamebatizwa, wote ni waaminio, wote ni washirika, ni sawa tu na zile choroko zinazooshwa katika maji, haijalishi ndani yao kuna nini..Lakini sasa ili lile andiko litimie linalosema “walioitwa ni wengi, lakini wateule ni wachache”, kutenganisha magugu, na ngano ni lazima kutokee..

Hapo ndipo maji ya moyo ambayo ndio (Neno la Mungu kama upanga linapopita juu ya watu)..kuangalia ni wapi watatii, na ni wapi watakuwa sugu..Hiyo ndio hatua ambayo Kristo anatupima kwa kile tulichokisikia na kufundishwa kutoka katika Neno lake na jinsi tunavyokitendea kazi,..Ikiwa wewe unajiita mkristo halafu umehubiriwa Neno miaka mingi, na ndani yako hakuonekani mabadiliko yoyote, bado ni mzinzi, mtukanaji, mvaaji vibaya, mtazamaji pornography, msengenyaji, mwendaji Disco n.k..na huku nyuma umebatizwa, ni mshirika mzuri wa Kanisani, mwimbaji kwaya,..wewe ni zile choroko-mawe ambazo hazisikii joto la maji, na siku si nyingi utaingia katika pepeteo la pili na la mwisho. Ambalo hilo ni pepeto la milele, hakuna kurudiwa tena. Hili andiko ndipo linapotimia.

1Yohana 2:19 “Walitoka kwetu, lakini hawakuwa wa kwetu. Maana kama wangalikuwa wa kwetu, wangalikaa pamoja nasi. Lakini walitoka ili wafunuliwe kwamba si wote walio wa kwetu.

Wakati wengine Mungu anawavukisha madarasa mengine ya kiroho, wanapikwa vizuri, kwa ajili ya kuurithi ufalme wa mbinguni, wewe kumbe siku nyingi ulishatupwa nje, unakuwa msindikizaji tu pasipo hata wewe kujijua, na dalili mojawapo itakayokuonyesha kuwa siku nyingi Mungu alishakuacha ni wewe kuzidi kuwa vuguvugu wa ajabu, na wenzako maisha yao ya rohoni kuimarika.

Mungu huwa anasema na watu katika viwango tofauti, ikiwa katika hatua awali, mafundisho ya msingi hayakurekebishi, mafundisho gani mengine utafundishwa yakugeuze. Choroko-mawe hata zikiachwa mpaka hatua ya mwisho bado zitabakia vile vile tu.

Ndugu tunaishi katika kanisa la 7 na la mwisho linalojulikana kama LAODIKIA, naamini utakuwa unalifahamu hilo, ni kanisa ambalo linasifika kwa tabia ya kuwa vuguvugu kuliko makanisa yote yaliyotangulia huko nyuma. (soma Ufu3:14). Na kumbuka pia SIRI ya Mungu ipo kwa bibi-arusi wa Kristo tu, na sio pamoja na Masuria..Masuria ndio wale wanawali wapumbavu ambao tunasoma walikuwa wanamngojea Bwana wao, aje lakini hawakuwa na mafuta ya ziada katika TAA ZAO (Mathayo 25)..Mbaya sana na Huo ndio uvuguvugu unaozungumziwa, nusu kwa Bwana, nusu, kwa shetani..nusu choroko, nusu uchafu…na hivyo unakuwa umekidhi vigezo vyote vya kuwa CHOROKO-MAWE. Na kustahili kutapikwa.

Wakati unao sasa wa kutengeneza mambo yako sawa, kabla mlango wa rehema hujafungwa, Mungu ni mwaminifu ukitubu atakupokea na kukuhifadhi kwake..

2Petro 1:10 “Kwa hiyo ndugu, jitahidini zaidi kufanya imara kuitwa kwenu na uteule wenu; maana mkitenda hayo hamtajikwaa kamwe.

11 Maana hivi mtaruzukiwa kwa ukarimu kuingia katika ufalme wa milele wa Bwana wetu, Mwokozi wetu Yesu Kristo”.

Ubarikiwe. Tafadhali “Share” Ujumbe huu na wengine. Na Bwana atakubariki.

Pia kwa Maombezi, Ushauri, Maswali au Ratiba za Ibada Wasiliana nasi kwa namba

+225693036618/ +225789001312

Pia unaweza ukapata mafundisho haya Kwa njia ya Whatsapp yako, jiunge na channel yetu Kwa kubofya hapa >> WHATSAPP


Mada Zinazoendana:

WALIOITWA NI WENGI, ILA WATEULE NI WACHACHE.

TABIA YA KIPEKEE USIYOIJUA KUHUSU NENO LA MUNGU.

HATUA ZA ROHO MTAKATIFU KATIKA KUTUONGOZA.

TUKAZE MWENDO KWA TULIYOANDALIWA.


Rudi Nyumbani

Print this post

About the author

Admin administrator

Subscribe
Notify of
guest
0 Comments
Inline Feedbacks
View all comments