Nini maana ya mbingu na nchi zitapita lakini maneno yangu hayatapita kamwe? (Mathayo 24:35).

Nini maana ya mbingu na nchi zitapita lakini maneno yangu hayatapita kamwe? (Mathayo 24:35).

Jibu: Turejee,

Mathayo 24:35  “Mbingu na nchi zitapita; lakini maneno yangu hayatapita kamwe”

Ili tuelewe vizuri, tutafakari kwanza mstari ufuatao…

Waebrania 13:8 “Yesu Kristo ni yeye yule, jana na leo na hata milele”.

Mpaka maandiko yaseme kuwa “Yesu Kristo ni yeye yule, jana na leo na hata milele”… Maana yake kuna watu, au vitu ambavyo haviwezi kuwa vile vile jana, leo na hata milele.

Kwa mfano mtu hawezi kuwa na tabia ile ile, au msimamo ule ule jana na leo na hata milele,..ni lazima tu utafika wakati tabia yake itabadilika, mtazamo wake utabadilika, utendaji wake utabadilika au hata msimamo wake!…. lakini KRISTO YESU yeye ni yule yule, kitabia, na kiutendaji, hajawahi kusema jambo halafu akajikosoa.. ni yeye yule na ataendelea kuwa vile vile Milele.

Hali kadhalika, vitu tunavyoviona katika mbingu kama jua, mwezi  na nyota, ijapokuwa tunaona vimedumu kuwa vilevile kwa maelfu ya miaka, lakini biblia inatabiri kuwa siku moja vitatoweshwa vyote…

Ufunuo 6:12 “Nami nikaona, alipoifungua muhuri ya sita, palikuwa na tetemeko kuu la nchi; jua likawa jeusi kama gunia la singa, mwezi wote ukawa kama damu,

13  na NYOTA ZIKAANGUKA juu ya nchi kama vile mtini upukutishavyo mapooza yake, utikiswapo na upepo mwingi.

14  MBINGU ZIKAONDOLEWA KAMA UKURASA ulivyokunjwa, na kila mlima na kisiwa kikahamishwa kutoka mahali pake”.

Vile vile vitu tunavyoviona katika “NCHI” kama vile milima, na habari ambavyo tunaviona kama zimedumu kwa maelfu ya miaka, lakini bado biblia inatabiri kuwa siku moja vitafutika..

Ufunuo 16:20  “Kila kisiwa kikakimbia, wala milima haikuonekana tena”

Soma pia Ufunuo 21:1..

Lakini wakati ambapo vitu vyote hivi vinaondolewa (maana yake VINAPITA) Bado Kristo atabaki kuwa yeye yule, na maneno yake yatabaki kuwa yale yale, na yana nguvu ile ile katika umilele wote.

Kwamfano maneno ya Yesu anayosema yeye ni ALFA na OMEGA, yaani Mwanzo na Mwisho (katika Ufunuo 21:6 na Ufunuo 22:13) yataendelea kuwa hivyo hivyo Milele, hakuna wakati utafika Kristo ataacha kuwa Alfa na Omega…jua na mwezi na nyota na wanadamu watapita, lakini maneno hayo yataeendelea kuwa halisi hivyo hivyo milele na milele.

>Vile vile maneno yake aliyosema kuwa “Yeye ndio Njia, Kweli na Uzima (Yohana 14:6)” yataendelea kuwa hivyo milele na milele, hakuna wakati utafika ambao Kristo ataacha kuwa Njia, au ataacha kuwa  Kweli au ataacha kuwa Uzima..Kristo YESU sasa ni Uzima, na ataendelea kuwa UZIMA hivyo hivyo milele na milele.

>Vile vile aliposema kuwa yeye ni “Nuru ya Ulimwengu (Yohana 8:12)”…Maneno hayo hautafika wakati ambao yata-expire… Jua na mwezi kuna wakati vitaisha muda wake wa matumizi, jua litaondolewa halitamulika tena, na mwezi utaondolewa hautaangaza tena.. lakini Kristo ataendelea kuwa NURU hata kipindi ambacho jua na mwezi havipo..

Ufunuo 21:23  “Na mji ule hauhitaji jua wala mwezi kuuangaza, KWA MAANA UTUKUFU WA MUNGU HUUTIA NURU, NA TAA YAKE NI MWANA-KONDOO”.

> Vile vile maneno yake mengine yanamtaja yeye kama “Mwaminifu na wa Kweli (katika Ufunuo 3:14, na Ufunuo 19:11)”. Yeye atabaki kuwa hivyo Milele na milele, hakuna wakati ambao atabadilika na kukosa uaminifu!… Sisi wanadamu tunaoishi chini ya jua na juu ya nchi, tutakuwa waaminifu tu kwa kitambo Fulani lakini si milele. Lakini yeye ataendelea kuwa mwaminifu milele na milele hata wakati ambao mbingu zitafutwa, na kuletwa mbingu mpya na nchi mpya, bado ataendelea kuwa mwaminifu.

> Pia alisema wote wamwaminio yeye watakuwa na uzima wa milele, hakuna wakati hilo Neno litabadilika, kwamba awanyime uzima wa milele wale wote waliomwamini na kuishi kwa kuzifuata amri zake.. Majira yatabadilika, vipindi vitabadilika lakini milele na milele hawezi kujisahihisha maneno yake hayo. AKIAHIDI AMEAHIDI!!.. Na milele habadiliki.

Na maneno mengine yote yaliyosalia aliyoyasema BWANA YESU hakuna hata moja litapita!!! , yote yatabaki kuwa vile vile

Je umemwamini huyu Mkuu wa UZIMA asiyeweza KUBADILIKA?, Au Unawatumainia wanadamu ambao leo wapo na kesho hawapo, leo wanaahidi na kesho wamebadilika, leo wanakupenda kesho wanakuchukia.. Ni heri ukaanza kumtumainia yeye asiyeweza kubadilika, YESU KRISTO, MFALME WA WAFALME, na BWANA WA MABWANA.

Mungu akubariki.

Mafundisho Mengine

Mbinguni ni sehemu gani?

Kuna Mbingu ngapi?

MBINGU MPYA NA NCHI MPYA. (Sehemu ya 1)

INJILI YA MILELE NI IPI KATIKA BIBLIA?

Je! Sulemani alienda mbinguni?

Rudi Nyumbani:

 

 

Print this post

About the author

Admin administrator

Subscribe
Notify of
guest
0 Comments
Inline Feedbacks
View all comments