NI NINI TUNAJIFUNZA KWA YOANA NA MANAENI?

NI NINI TUNAJIFUNZA KWA YOANA NA MANAENI?

Kama unadhani mazingira ni sababu ya wewe kutokuwa Mwanafunzi wa Yesu, basi tafakari mara mbili!.

Unaweza kusema labda Nimezaliwa katika dini inayompinga Kristo, nawezaje kuwa Mkristo tena yule wa kujikana nafsi?..nimeolewa na mtu ambaye anampinga Bwana Yesu? Na familia yangu yote haimwamini Yesu wala haiamini Ukristo..je inawezekana mimi kuwa mkristo na kuanza kwenda kanisani na hata kumtumikia yeye?

Jibu ni Ndio! Yote yanawezekana endapo utaamua kujikana nafsi kwa kumaanisha kumfuata Yesu..

Inawezekana kabisa kuwa mwanafunzi wa Yesu, na hata kuifanya kazi yake. Wewe sio wa kwanza kukutana na  mazingira kama hayo, hata katika biblia walikuwepo watu wa namna kama yako, ambao walikutana na mazingira magumu kuliko yako, lakini walishinda…lakini pia walikuwepo  walioshindwa..

Hebu tujifunze katika makundi yote mawili, ya walioshindwa na walioshinda.

1 . WALIOSHINDWA.

Tusome,

Yohana 12:42 “Walakini hata katika wakuu walikuwamo wengi waliomwamini; lakini kwa sababu ya Mafarisayo hawakumkiri, wasije wakatengwa na sinagogi”.

Hawa ni Wayahudi, ambao walimwamini Kweli Yesu lakini, walihofia kutengwa na ndugu zao na zaidi sana masinagogi yao, yaani watu wa dini yao!. Hivyo wakaishia tu kumwamini Yesu lakini hakuna chochote walichozalisha.

2 . WALIOSHINDA.

Lilikuwepo ambalo lilikuwepo katika mazingira magumu, lakini lilishinda.

Mfano wa hao ni YOANA MKEWE KUZA, wakili wa Herode. Na MANIELI ndugu wa Herode.

YOANA, MKEWE KUZA.

Huyu Yoana, alikuwa ni mke wa mtu aliyeitwa Kuza, ambaye alikuwa ni wakili wa mfalme Herode. Sasa ili kujua vizuri familia ya Herode ilikuwa ni ya watu wa namna gani, tusome mistari ifuatayo..

Mathayo 2:16 “Ndipo Herode, alipoona ya kuwa amedhihakiwa na wale mamajusi, alighadhabika sana, akatuma watu akawaua watoto wote wanaume waliokuwako huko Bethlehemu na viungani mwake mwote, tangu wenye miaka miwili na waliopungua, kwa muda ule aliouhakikisha kwa wale mamajusi”.

Herode alimtafuta kumwua Bwana Yesu katika uchanga wake, na hata kipindi amekuwa mkubwa mwanae alimkata kichwa Yohana mbatizaji.(Mathayo 14:1-10), na Zaidi sana baadaye alikuja kumwua Yakobo, mtume wa Bwana Yesu (Matendo 12:1-2) na alitafuta kumwua na Petro pia, lakini Bwana alimwepusha na mauti yake hiyo..

Kwahiyo kwa ufupi ni kwamba Herode alikuwa ni mpinga Kristo kwa wakati huo, na endapo angesikia yeyote katika watu wake kajishikamanisha na Bwana Yesu, wazo lake ni lile lile la kuua.. lakini tunaona huyu mke wa Wakili wake, aliyajua hayo yote, na Pamoja na hayo, akaamua kumfuata Yesu na kuwa mwanafunzi wake, pasipo kujali atapitia nini mbeleni.

Na tena sio yule mwanafunzi wa siri siri, bali yule wa wazi kabisa..ambaye anaambatana na Bwana Yesu kila mahali, na tena anamhudumia..

Luka 8:1 “Ikawa baada ya hayo alikuwa akizunguka-zunguka katika miji na vijiji akihubiri na kuitangaza habari njema ya ufalme wa Mungu; na wale Thenashara walikuwa pamoja naye,

2 na wanawake kadha wa kadha ambao walikuwa na pepo wabaya na magonjwa wakaponywa; nao ni Mariamu aitwaye Magdalene aliyetokwa na pepo saba,

3 NA YOANA MKEWE KUZA, WAKILI WAKE HERODE, na Susana, na wengine wengi, waliokuwa wakimhudumia kwa mali zao”.

Umeona?..Yoana alijua kuna kifo kinamgoja wakati wowote, lakini alijikana nafsi na akawa moja ya wanawake wa mbele kabisa walioheshimiwa na Bwana Yesu.

MANAENI

Sio huyo tu! Kulikuwepo na mwanaume mwingine anayeitwa Manaeni..Huyu maandiko yanasema alikuwa ni NDUGU WA KUNYONYA wa Mfalme Herode…maana yake wametoka katika familia moja na Herode, wanajuana ndani na nje!.. lakini pamoja na kwamba anajua ndugu yake ni mfalme tena Mpinga-Kristo, yeye hakumwogopa.. bali aliacha vyote akachukua msalaba wake, akamfuata Yesu, na hatimaye Bwana akamfanya kuwa NABII wake.

Matendo 13:1” Na huko Antiokia katika kanisa lililokuwako palikuwa na MANABII NA WAALIMU, nao ni Barnaba, na Simeoni aitwaye Nigeri, na Lukio Mkirene, na MANAENI ALIYEKUWA NDUGU WA KUNYONYA WA MFALME HERODE, na Sauli.

2 Basi hawa walipokuwa wakimfanyia Bwana ibada na kufunga, Roho Mtakatifu akasema, Nitengeeni Barnaba na Sauli kwa kazi ile niliyowaitia”.

Kupitia watu hawa wawili YOANA Pamoja na MANAENI, itoshe kutupa kila sababu ya sisi kujikana nafsi!.

Watu hawa watasimama siku  ya hukumu Pamoja na sisi, ambao tunasema tupo katika mazingira magumu ya kumfuata Yesu, watatuhukumu.

Hivyo ndugu kama wewe umeolewa na mtu asiye mkristo, na sasa umemwamini Yesu, usione aibu wala usiogope, mkiri Kristo hadharani…kama wewe unaishi na wapagani ambao hawamwamini Yesu au wanampinga!.. bali usiwaogope.. wewe mfuate Yesu, kuwa mwanafunzi wake, jikane nafsi kama Yoana na Manaeni. Na Bwana Yesu atakuheshimu kuliko kawaida, atakutukuza kama alivyowatukuza Yoana na Manaeni.

Maran atha!

Tafadhali shea na wengine ujumbe huu;

Pia Kwa maombezi/ Ushauri/ Maswali/ Whatsapp:
Tuandikie katika BOXI la Maoni hapo chini au
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312

Mada Nyinginezo:

TUJIFUNZE JAMBO KWA WANAWAKE HAWA WAWILI.

Maherodi walikuwa ni akina nani, Na kazi yao ilikuwa ni ipi?

NI NANI ALIYEKUPA MAMLAKA HII UYATENDE HAYA?

Wanafunzi wa Yesu, walimaanisha nini kusema kama “Mambo ya mtu na mkewe yakiwa hivyo, haifai kuoa”?

Kwanini Herode aliwakasirikia watu wa Tiro na Sidoni? (Matendo 12:20)

Rudi nyumbani

Print this post

About the author

Admin administrator

Subscribe
Notify of
guest
0 Comments
Inline Feedbacks
View all comments