KAMA MMOJA TU NDIO HIVI! SI ZAIDI 153?

KAMA MMOJA TU NDIO HIVI! SI ZAIDI 153?

Jina la Bwana wetu Yesu yeye atupendae upeo libarikiwe daima. Nakukaribisha katika kuyatafakari maandiko kama vile tulivyopewa maagizo kwenye biblia kwamba tunapaswa tumjue yeye sana mpaka tufikia kimo cha cheo cha utimilifu wake, ili tusiwe watoto wachanga wa kuchukuliwa na kila aina ya upepo wa elimu (Efeso 4:13-14)

Kuna swali unaweza kujiuliza kwanini Bwana alipowatokea wanafunzi wake siku ile walipokuwa wanavua, tunasoma wanafunzi walivua samaki wengi na wakubwa, ambao jumla yake ilikuwa ni 153. Kwanini idadi itajwe pale? Na kwanini Bwana abakie na samaki mmoja tu kule ufukweni?

Embu tusome ..

Yohana 21:3 “Simoni Petro aliwaambia, Naenda kuvua samaki. Nao wakamwambia, Sisi nasi tutakwenda nawe. Basi wakaondoka, wakapanda chomboni; ila usiku ule hawakupata kitu.

4 Hata asubuhi kulipokucha, Yesu alisimama ufuoni; walakini wanafunzi hawakujua ya kuwa ni Yesu.

5 Basi Yesu akawaambia, Wanangu, mna kitoweo? Wakamjibu, La.

6 Akawaambia, Litupeni jarife upande wa kuume wa chombo, nanyi mtapata. Basi wakatupa; wala sasa hawakuweza kulivuta tena kwa sababu ya wingi wa samaki.

7 Basi yule mwanafunzi ambaye Yesu alimpenda akamwambia Petro, Ndiye Bwana. Naye Simoni Petro, aliposikia ya kwamba ni Bwana, akajifunga vazi lake, (maana alikuwa uchi), akajitupa baharini.

8 Na hao wanafunzi wengine wakaja katika mashua; maana hawakuwa mbali na nchi kavu; ila yapata dhiraa mia mbili; huku wakilikokota lile jarife lenye samaki.

9 Basi waliposhuka pwani, wakaona huko moto wa makaa, na juu yake pametiwa samaki, na mkate.

10 Yesu akawaambia, Leteni hapa baadhi ya samaki mliowavua sasa hivi.

11 Basi Simoni Petro akapanda chomboni, akalivuta jarife pwani, limejaa samaki wakubwa, mia hamsini na watatu; na ijapokuwa ni wengi namna hiyo, jarife halikupasuka.

12 Yesu akawaambia, Njoni mfungue kinywa. Wala hakuna mtu katika wale wanafunzi aliyethubutu kumwuliza, U nani wewe? Wakijua ya kuwa ni Bwana.

13 Yesu akaenda akautwaa mkate, akawapa, na samaki vivyo hivyo”.

Kama tunavyoiona habari, Bwana alipowapa maagizo ya kutupa jarife upande wa pili, na kufanikiwa kutoka na samaki wengi vile, Lakini waliporudi pwani walimkuta Bwana pia akiwa na samaki na mkate lakini cha kushangaza zaidi, alikuwa ni samaki MMOJA TU!.

Unaweza kujiuliza ni kwanini awe mmoja tu na si wengi? Halafu utaona pale samaki huyo huyo ndio Bwana aliyewapa wanafunzi wake, pamoja na mkate, soma pale mstari wa 13 vizuri utaona..

Yesu ambaye aliwapa mbinu wanafunzi wake wa kuvua samaki wengi na wakubwa ambao hata nyavu zao hazikuweza kusapoti kwa uzito wa samaki wale ambao walikuwa 153, Huyo huyo ndiye aliyekuwa na samaki mmoja tu pwani akimwandaa vizuri juu ya makaa, huku akiwangojea wanafunzi wake aliowaagiza wakatupe nyavu.

Ni nini Bwana alikuwa anawafundisha wanafunzi wake?

Alikuwa anataka kuwafundisha samaki mmoja jinsi alivyo na thamani kubwa kuliko wao wanavyoweza kudhani.. Mitume walipomla Yule samaki aliyeandaliwa na Bwana mwenyewe utamu waliouona najua ulikuwa ni wa kipekee sana wa kuwaburudisha wao wote, wa kuwafurahisha wao wote,wa kuwabariki hao wote.. Sasa kama ni hivyo si zaidi wale 153 waliowavua?.

Ni zaidi sana watakuwa furaha kwao mara 153. Hivyo Bwana alikuwa anawaonyesha thawabu watakayoipata katika kuifanya kazi yake siku ile mbinguni, na ndio maana Baada ya pale akaanza kumuuliza Petro ambaye ndiye aliyekuwa kiongozi wao..Petro Je! wanipenda? Petro Akasema ndio nakupenda, Bwana akamwambia, Lisha kondoo zangu..Chunga kondoo zangu..

Hata sasa Bwana Yesu anatufundisha sisi, kuifanya kazi yake aliyotuitia hapa duniani ya kuwavua watu kwake waliopotea katika ulimwengu, kazi hiyo sio ya bure bali inayo malipo makubwa sana katika ufalme wa mbinguni.. Laiti kama Bwana angetuonjesha thawabu aliyotuandalia katika mtu mmoja tunapomvuta kwake, tusingetamani kuacha kufanya hivyo usiku na mchana.

Tunapaswa tujiulize karama zetu tulizopewa na Mungu tunazitumiaje kama wakristo..Je! Zinawavuta watu kwa Kristo au zinawaburudisha tu? Tunapoimba hizo nyimbo za injili Je zinawageuza watu au tunazitumia tu kwa ajili ya kupata kipato, na kutafuta umaarufu..Je! Mahubiri yetu yanawaelekeza watu kwa Bwana, au katika biashara na uchumi?..Je! Uchungaji wetu ni wa kulichunga kundi la Mungu au kulitapanya?..

Bwana na yeye anakuliza wewe, Je! wanipenda?? Kama unampenda Basi fahamu kuwa Kristo anahitaji umvulie samaki wengi kwa kadiri alivyokukirimia karama, kama mitume walivyofanya kwa wale 153..Kwasababu thamani ya kondoo mmoja kwa Kristo, inawafanya malaika waruke ruke kule mbinguni kwa furaha na shangwe.

Bwana atubariki na kutushika mkono.

Maran Atha!

Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema, na pia kama utapenda tuwe tunakutumia masomo haya kwa njia ya email yako au Whatsapp tutumie ujumbe kwenye box la maoni chini au piga namba hii +255 789001312


Mada Nyinginezo:

Mariamu Magdalene ni nani. Na hilo jina amelitolea wapi?

VITA VYA IMANI NI VITA ENDELEVU.

MAHALI UNAPOPASWA USIMVUMILIE SHETANI HATA KIDOGO.

ROHO ZILIZO CHINI YA MADHABAHU:

Rudi Nyumbani:

Print this post

About the author

Admin administrator

Subscribe
Notify of
guest
1 Comment
Newest
Oldest Most Voted
Inline Feedbacks
View all comments
Joseph
Joseph
1 year ago

Amina, Barikiwa kwa somo zuri, lakini neno “samaki halina wingi, kwahiyo tunaweza kusema ni samaki mmoja lakin ikawa si hakika sana.. Au inaweza kuwa kweli maan kam walikuwa ni wengi biblia ingesema “na wale samaki