MADHARA YA KUFUATA MAMBO YAKO TU!

MADHARA YA KUFUATA MAMBO YAKO TU!

Ipo faida  ya kufuata mambo yako na kutojishughulisha na mambo ya wengine!.. Lakini pia ipo hasara kubwa ya kutojishughulisha na mambo ya wengine na kufuata mambo yako tu!. Faida ya kufuata mambo yako ni kwamba utakuwa huru katika mambo yako, na hautaishi kwa wasiwasi wala hofu!…kwasababu utakuwa hufuatilii mambo ya wengine, na wala hushirikiani nao, hivyo hutakuwa na mtu wa kushindana naye wala kujilinganisha naye..Kwahiyo utaishi maisha ya uhuru sana..

Lakini pamoja na hayo kuna hatari kubwa sana ya kuishi maisha ya namna hiyo, Maana yake yanapozidi sana, kiasi kwamba unakuwa umefunga milango yote, umejitenga na hutaki kufuatilia chochote cha nje! Ipo hatari!!

Leo tutajifunza kupitia biblia, mojawapo ya hatari ya maisha ya namna hiyo..

Katika maandiko tunausoma mji mmoja ulioitwa Laisha, mji huu ulikuwepo kaskazini mwa Taifa la Israeli, kabla haujatwaliwa na Israeli, ulikuwa unaitwa hivyo Laisha, lakini mji huu ulikuwa ni wa kipekee sana, kwanza ulikuwa ni mji ambao umejitenga, upo mbali sana na miji mingine, na pili ulikuwa ni mji ambao haukushirikiana na miji mingine, hivyo watu wake walikuwa wanafuata mambo yao tu!, wanafanya kazi kwaajili ya kuuendeleza mji wao, na wala hawakuwa na shughuli na mataifa mengine.. Hiyo ikawafanya wafanikiwe sana, kwasababu mambo yao yote hawakuyaendesha kwa hofu wala kwa mashindano.. Na zaidi ya yote, wakajiwekea utaratibu kuwa watu wote ni sawa katika ile jamii, hakuna wa kumtawala mwenzake wala kunyanyasana..

Lakini biblia inatuambia uharibifu wake ulikuja ghafla bila wao kutegemea..na mji mzima uliangamizwa pasipo msaada, kwasababu walikuwa mbali na miji mingine ambayo pengine ingewasaidia, na vile vile haikuwa na mahusiano na mji wowote ule.. ni wao kama wao..

Tusome habari hiyo kidogo katika maandiko.. (Zingatia vipengele vilivyoainishwa kwa herufi kubwa)

Waamuzi 18:7 “Ndipo hao watu watano wakaenda zao, WAKAFIKA LAISHA, wakawaona wale watu waliokuwamo ndani yake, jinsi walivyokaa salama salimini kwa mfano wa walivyokaa hao Wasidoni, WENYE STAREHE NA HIFADHI, kwa maana hapakuwa na mtu katika nchi hiyo aliyekuwa na amri, aliyeweza kuwatweza katika neno lo lote, nao walikuwa wa mbali na hao Wasidoni, WALA HAWAKUWA NA SHUGHULI NA MTU YE YOTE.

8 Kisha wakawarudia ndugu zao huko Sora na Eshtaoli; ndugu zao wakawauliza; Haya, mna habari gani?

9 Wakasema, Haya, inukeni, twende tukapigane nao; KWA MAANA TUMEIONA HIYO NCHI NAYO NI NCHI NZURI sana; nanyi, je! Mwanyamaa tu? Msiwe wavivu kwenda, na kuingia, ili mpate kuimiliki nchi hiyo.

 10 Hapo mtakapokwenda mtawafikilia WATU WAKAAO SALAMA SALIMINI, na hiyo nchi nayo ni kubwa; kwa kuwa Mungu ameitia mikononi mwenu; ni mahali ambapo hapana kupungukiwa na kitu cho chote kilicho duniani.

 11 Basi wakatoka hapo watu mia sita waliovaa silaha za vita, wa jamaa ya Wadani, kutoka Sora, na kutoka Eshtaoli……………………………………

27 Nao wakakitwaa hicho alichokuwa amekifanya Mika, na kuhani aliyekuwa naye nao wakafikilia Laisha, KWENYE WATU WALIOKUWA WENYE STAREHE NA HIFADHI, wakawapiga kwa makali ya upanga; wakaupiga moto mji wao.

28 WALA HAKUWAKO MWOKOZI, KWA SABABU HUO MJI ULIKUWA NI MBALI SANA NA SIDONI, NAO HAWAKUWA NA SHUGHULI NA MTU AWAYE YOTE; na mji huo ulikuwa katika hilo bonde lililo karibu na Bethrehobu. Nao wakaujenga huo mji na kukaa humo.

29 Wakauita mji jina lake Dani, kwa kuliandama jina la baba yao Dani, aliyezaliwa kwake Israeli; lakini jina la mji huo HAPO KWANZA ULIKUWA UKIITWA LAISHA”.

Umeona?.. Laiti mji huo ungekuwa na mahusiano na miji mingine, labda wangepata mwokozi, na wangeokoka na maangamizi hayo, kwani ingekuwa ni rahisi wao kusaidiwa na majirani zao, lakini maadui zao walipowasoma udhaifu wao kuwa ni watu wanaojiona kuwa hawawezi kuhitaji msaada kutoka kwa mwingine yeyote, ni watu ambao wapo wenyewe wenyewe, ndipo wakapata nguvu!, kwani walitambua hata watakapowavamia hakuna atakayekuja kuwasaidia. Na siku ya maangamizi yao ilipofika, wakaangamia wote!, pamoja na utajiri wao, na fedha zao, na mali zao na kila kitu chao, waliopotea wote.

Hiyo inatufundisha nini?

Umoja ni ulinzi, biblia inasema katika Mhubiri….

Mhubiri 4:12 “ Hata ikiwa  mtu aweza kumshinda yule aliye peke yake, wawili watampinga; wala kamba ya nyuzi tatu haikatiki upesi.”

Wakati mwingine unaweza kufikiri kuwa peke yako ndio afya, lakini kinyume chake ndivyo unavyodhoofisha ulinzi wako! Na usalama wako!.. Ni vizuri kutojishughulisha na mambo ya wengine na kufuata mambo yako!.. lakini isizidi sana, kiasi kwamba hata hutaki kuwa na mahusiano na wengine!, hutaki kujifunza kutoka kwao, hutaki kusaidiwa na wao, hutaki kuwasaidia, hutaki kujinyenyekeza kwao, ni wewe kama wewe tu! n.k

 Kwasababu huo ubinafsi wako ambao unadhani ni ulinzi kumbe ndio nguvu ya adui yako shetani.  Yeye anatamani uendelee kukaa hivyo hivyo bila kuwa na shughuli na mtu mwingine yeyote ili siku atakapokuletea madhara!, ukose msaada. Ni kweli ubinafsi wako utakupa uhuru!, hata unaweza kukupa utajiri, lakini siku ya hautakusaidia siku ya maangamizi..

Hata katika kanisa kitu cha kwanza shetani anachokiua ni Umoja!.. kwasababu anajua ni ngumu kulishambulia kundi kubwa kuliko mtu mmoja mmoja!.. hivyo anachokifanya kwanza ni kuhakikisha analitenganisha kundi, na kutenga mtu mmoja mmoja, hivyo anahakikisha anaweza roho ya kila mtu kufuata mambo yako, na kutojishughulisha na mambo ya wengine.. Na akishafanikiwa hilo, ndipo anaanza kuwamaliza mmoja mmoja.

Ndugu! Usikimbie vikundi vya maombi, na kutafuta kuomba mwenyewe mwenyewe kila mara, ukidhani ndio salama!… Tenga muda wako mwingi wa kusali mwenyewe lakini usiache kukusanyika na wengine katika maombi.

Vile vile usijione kuwa una hekima kwa wewe kutokwenda kanisani kukusanyika na wengine!, kwasababu tu ya vikasoro vidogo vidogo unavyoviona pale!..na huku ukijitumainisha katika kusali mwenyewe ! Bali kinyume chake uogope!… kwasababu upo katika rada ya shetani!!.. Hutadumu muda mrefu, utapotea kabisa..

Yohana 17: 21  “WOTE WAWE NA UMOJA; kama wewe, Baba, ulivyo ndani yangu, nami ndani yako; hao nao wawe ndani yetu; ili ulimwengu upate kusadiki ya kwamba wewe ndiwe uliyenituma.

22  Nami utukufu ule ulionipa nimewapa wao; ILI WAWE NA UMOJA KAMA SISI TULIVYO UMOJA.

23  Mimi ndani yao, nawe ndani yangu, ILI WAWE WAMEKAMILIKA KATIKA UMOJA; ili ulimwengu ujue ya kuwa ndiwe uliyenituma, ukawapenda wao kama ulivyonipenda mimi”.

Bwana atubariki.

Kama hujampokea Yesu, mlango wa neema bado upo wazi!.. ila hautakuwa hivyo siku zote, hivyo mpokee Yesu leo akuoshe dhambi zako na kukupa uzima wa milele.

Maran atha!

Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema,

Kwa maombezi/Ratiba za ibada/ Ushauri/ Maswali.
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312

pia kama utapenda uyapate mafundisho haya kwa njia ya Whatsapp au email basi tutumie ujumbe kwenye namba hizo hizo.


Mada Nyinginezo:

Maashera na Maashtorethi ni nini?

KUWA MAKINI NA MITANDAO, NI SHIMO REFU.

WAOMBEENI WANAOWAUDHI.

Kama wakitenda mambo haya katika mti mbichi, itakuwaje katika mkavu?

Nini maana ya Dirii, Chepeo na Utayari?

Rudi nyumbani

Print this post

About the author

Admin administrator

Subscribe
Notify of
guest
0 Comments
Inline Feedbacks
View all comments