Birika ni nini?, na yale Matao matano katika birika la Bethzatha ni nini?.

Birika ni nini?, na yale Matao matano katika birika la Bethzatha ni nini?.

Jibu: Kipo kifaa kinachoitwa Birika tulichozoea kukijua, ambacho kinatumika kuhifadhia chai au maji. Lakini pia neno hilo hilo birika lina maana ya “Bwawa” au “Dimbwi dogo”, lilolotengenezwa kwa kazi Fulani mahususi, Na Bwawa hilo linaweza kuwa limetengenezwa kwa utaalamu mkubwa au pasipo utaalamu mkubwa, kufuatia matumizi ya bwawa hilo.

Sasa katika biblia yalikuwepo mabirika mengi, yalikuwepo yaliyotengenezwa kwa kunyweshea wanyama maji mfano hayo ni lile la Yakobo..

Mwanzo 30:38 “Akazisimamisha fito hizo alizozibambua katika mabirika ya kunyweshea maji, pale walipokuja wanyama wanywe; wakachukua mimba walipokuja kunywa.”

Unaweza pia kusoma mfano wa hayo katika 2Nyakati 26:10.

Na pia yalikuwepo mabirika yaliyochimbwa ardhini kwa ajili ya kuhifadhia maji, mfano wa hayo, ni lile Yusufu alilotupwa na ndugu zake..

Mwanzo 37:23 “Ikawa Yusufu alipofika kwa ndugu zake, wakamvua Yusufu kanzu yake, kanzu ile ndefu aliyoivaa,

24 wakamtwaa wakamtupa katika birika; na hiyo birika ilikuwa tupu, hamna maji”.

Unaweza kusoma pia 1Samweli 13:6..

Na pia yalikuwepo mabirika  yaliyotengenezwa kwaajili ya kuogea/kunawia. Mfano wa hayo ni yale yaliyotengenezwa katika hema ya Mungu na katika nyumba ya Mungu, maalumu kwa makuhani kujisafisha kabla ya kuingia ndani ya hema, au nyumba ya Mungu kufanya kazi za kikuhani..

Kutoka 30:17 “Bwana akanena na Musa, na kumwambia

18 Fanya na BIRIKA LA SHABA, na tako lake la shaba, ILI KUOGEA; nawe utaliweka kati ya hema ya kukutania na madhabahu, nawe utalitia maji.

19 Na Haruni na wanawe wataosha mikono yao na miguu yao humo;

 20 hapo waingiapo ndani ya hema ya kukutania; watajiosha majini, ili wasife; au hapo watakapoikaribia madhabahu ili watumike, kumteketezea Bwana sadaka ya moto”

Pia unaweza kusoma juu ya birika hizo katika nyumba ya Mungu katika 1Wafalme 7:38-43 na 2Nyakati 4:6.

Pia yalikuwepo mabirika yaliyotengenezwa kwaajili ya kuogea makahaba..

1Wafalme 22:37 “Hivyo akafa mfalme, akachukuliwa Samaria, wakamzika mfalme huko Samaria.

38 Wakaliosha gari penye BIRIKA LA SAMARIA, na mbwa wakaramba damu yake; (BASI NDIPO WALIPOOGA MAKAHABA); sawasawa na neno la Bwana alilolinena”.

Lakini pia tunasoma katika agano jipya, yakitajwa tena aina nyingine ya mabirika. Na hayo si mengine zaidi ya birika la Siloamu (Yohana 9:7) na Birika la Bethzatha (Yohana 5:2).

Birika ya Bethzatha ilijengwa kwa lengo la kuhifadhi maji yatakayotumika hekaluni. Birika hii ilijengwa kwa kuzungushiwa “Matao matano”. Matao ni nguzo zilizosimamishwa kuzunguka birika hilo, na kulitia uvuli…na nafasi iliyokuwepo kati ya nguzo na nguzo ilikuwa ndio maingilio ya birika hiyo..

Yohana 5:2 “Na huko Yerusalemu penye mlango wa kondoo pana birika, iitwayo kwa Kiebrania Bethzatha, nayo ina matao matano .

3  Ndani ya hayo jamii kubwa ya wagonjwa walikuwa wamelala, vipofu, viwete, nao waliopooza, [wakingoja maji yachemke ”.

Kama tunavyoijua habari, Yule mngonjwa ambaye aliugua kwa miaka 38, na  hakuwa na mtu wa kumwingiza birikani, pindi maji yanapochemka (yaani nguvu za Mungu zinaposhuka ndani ya yale maji), lakini alipokutana na Bwana Yesu, aliponywa siku ile ile pasipo kuingizwa birikani.

Hiyo ni kutufundisha kuwa hakuna matumaini kwenye maji  ya upako, wala visima vya upako. Huyu aliugua miaka 38, na alikuwa anatumainia maji ya upako. Na kama sio Bwana Yesu kumhurumia pengine angekufa bila kupata msaada wowote.

Kristo mponyaji wa mwili na roho yupo, isipokuwa sisi tumemtupa nje, na badala yake tunatafuta miujiza kwa njia zisizo rasmi.

Hebu jifunze kwenye huo mfano… “Hapo inasema ndani ya hayo matao, JAMII KUBWA ya wagonjwa walikuwa wamelala, wakisubiri maji yachemke.”…wamelala!!  wakisubiri!!..na matokeo ya kusubiri ndio hiyo miaka 38 bila matumaini!…Na wakati wakiwa wanasubiri kumbe mponyaji yupo ulimwenguni akitembea huko na huko akiponya na kufungua watu.. lakini hili kundi lingine kubwa huku limelala likisubiri!! Huku likijitumainisha na maji ya upako!…na kisima cha upako!!.

Na si ajabu huyu Bwana peke yake ndio angalau alikuwa na moyo wa kupokea kitu kipya, ndio maana Bwana akamfuata yeye peke yake.. lakini hao wengine wengi waliokuwa wanasubiria, tunaona Bwana hakuwafuata kuwaponya.. kwanini??.. Ni dhahiri kuwa wengi wao walishamsikia huko nje akifundisha na kuponya lakini kwasababu wanaamini zaidi katika maji yale ya upako, wakamdharau, pengine wamesikia Yesu akikuponya anakwambia acha dhambi, acha kisasi, kuwa mtu wa kusamehe, na ili hali wenyewe hawataki kuacha hayo.. Wenyewe wanataka wakishapona waendelee na maisha yao, wasipewe pewe maelekezo ya maisha, ndio maana wakalipenda zaidi lile birika kwasababu ukishaponywa huambiwi chochote…hata kama ulikuwa kahaba na muuaji, ukishaponywa unaweza kuendelea na ukahaba wako.

Ndugu, jihadhari na miujiza BUBU, ambayo unaambiwa njoo ogea maji haya, upone… lakini hugusiwi habari ya dhambi zilizokufunga!.. Unaambiwa njoo ugea maji haya, lakini huambiwi huyo mke/mume unayeishi naye si wako!..huambiwi kwamba unaishi katika uzinzi na ukifa unaenda jehanamu!!.. Na ndio maana unahangaika miaka na miaka kununua maji haya na yale, mafuta haya na yale, kuzunguka katika kisima hiki na kile, kutafuta uponyaji lakini hupati!!..Ni kwanini?.. Ni kwasababu umemtupa Kristo na maneno yake nje!, halafu unatafuta uponyaji kwa njia mbadala..

Ndugu achana na hivyo visima bubu, Kristo kashavilaani!!…achana na hayo mabirika na madimbwi hayana msaada kwa nyakati hizi!!!…haijalishi yanalitaja jina la Mungu kiasi gani!..hili birika la Bethzatha lilikuwepo karibu sana na Hekalu la Mungu, lakini Kristo hakulitukuza!!!….Na wewe ndio maana pengine umekaa muda mrefu, ukitumainia hivyo visima na hakuna chochote!!.. Achana navyo, mtafute yeye..atakuponya na kukupa Maelekezo bora ya maisha ambayo yataiokoa roho yako, na hata kukuponya….

Na pia kama hujampokea Yesu, saa ya wokovu ni sasa, mwamini leo, na ukabatizwe katika ubatizo sahihi wa maji tele na kwa Jina la Yesu. Na utakuwa umemfungulia Roho Mtakatifu njia ya kukuongoza katika kweli yote ya maandiko. Bwana Yesu yupo karibu na hicho kisima akitafuta tafuta ni nani aliye tayari kusikia, na kumkubali.. Uwe wewe leo! Katika Jina la Yesu.

Maran atha!

Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema,

Kwa maombezi/Ratiba za ibada/ Ushauri/ Maswali.
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312

pia kama utapenda uyapate mafundisho haya kwa njia ya Whatsapp au email basi tutumie ujumbe kwenye namba hizo hizo.


Mada Nyinginezo:

BIRIKA LA SILOAMU.

Mruba ni mdudu gani kwenye biblia?(Mithali 30:15)

Neno Bildi linamaanisha nini kwenye biblia(Matendo 27:28) ?

nini maana ya kujikana nafsi na kujitwika msalaba?

JE! UMEPOKEA KWELI ROHO MTAKATIFU?

Rudi nyumbani

Print this post

About the author

Admin administrator

Subscribe
Notify of
guest
0 Comments
Inline Feedbacks
View all comments