Nawiwa na Wayunani na wasio Wayunani.

Nawiwa na Wayunani na wasio Wayunani.

SWALI: Ni kwa jinsi gani Paulo aliwiwa na Wayunani na wasio Wayunani, wenye hekima na wasio na hekima? (Warumi 1:14).


JIBU: Labda tuanze kusoma kuanzia juu kidogo mstari wa 13.

Warumi 1:13 “Lakini, ndugu zangu, sipendi msiwe na habari, ya kuwa mara nyingi nalikusudia kuja kwenu, nikazuiliwa hata sasa, ili nipate kuwa na matunda kwenu ninyi pia kama nilivyo nayo katika Mataifa wengine.

14 Nawiwa na Wayunani na wasio Wayunani, nawiwa na wenye hekima na wasio na hekima.

15 Kwa hiyo, kwa upande wangu, mimi ni tayari kuihubiri Injili hata na kwenu ninyi mnaokaa Rumi”.

Awali ya yote ni vizuri kujua maan a ya neno kuwiwa.. Neno kuwiwa maana yake “kudaiwa”

Kwahiyo Mtume Paulo alikuwa anajaribu kueleza ni kwa jinsi gani, ana deni kubwa la kuhubiri injili kwa makundi ya watu mbalimbali.

Na baadhi ya makundi hayo ndio hayo aliyoyataja..ambayo ni Wayunani na Wasio wayunani.

Sasa wayunani kwa lugha nyingine Ndio Wagiriki.

Wagiriki ndio kundi la watu lililokuwa linajulikana kuwa na akili nyingi enzi za kale.

Hekima nyingi ziligunduliwa huko Ugiriki, watu kama Plato, na Alexander ambao tunawajua sana leo kama wana filosofia wakubwa, walitokea huko Ugiriki.

Kwahiyo ni watu waliokuwa na hekima na elimu kubwa sana, nyakati hizo.

Hiyo ikawafanya mambo mengi wanayoyasikia kutoyabeba bila kuyafanyia uchunguzi wa kutosha..Maana yake ni kwamba walikuwa wanashawishika sana na hoja zinazotumia akili na hekima nyingi..kuliko hata zinazotumia ishara..

Kwa maana ishara kama miujiza mtu anaweza kuitengeneza na kudanganya, lakini jambo lolote ambalo limechambuliwa kwa hoja nyingi zenye akili na mashiko ni ngumu kupotosha..Hivyo walikuwa ni watu wasioshawishika kwa miujiza..

Kwamfano ukiwafuata na kufanya muujiza na kisha kuwaambia Yesu ni mwana wa Mungu, pasipo kuwaelezea kwa kina na elimu ya kutosha, si rahisi kukuamini ijapokuwa umeitenda ishara mbele yao.

Lakini ukafika na kuwaeleza ni kwa kina, na kwa elimu ya kiMungu, ambayo ina mantiki ndani yake..na ina hekima kuliko wanachokijua na kukiamini..basi ni rahisi wao kukuamini hata bila kufanya muujiza wowote…

Wapo watu ambao wanahitaji kuona miujiza ili waamini kama Wayahudi ambao Bwana aliwasema katika….

Yohana 4:48 “Basi Yesu akamwambia, Msipoona ishara na maajabu hamtaamini kabisa?”

Na wapo watu ambao hawahitaji kuona muujiza ndipo waamini, bali wanachotaka ni kupata hekima kwa kile unachowapelekea ndipo waamini mfano wa hao ndio hawa Wayunani (Wagiriki).

1 Wakorintho 1:22 “Kwa sababu Wayahudi wanataka ishara, na Wayunani wanatafuta hekima”

Kwahiyo tukirudi kwenye swali letu, ni kwa namna gani Mtume Paulo alikuwa anawiwa na Wayunani na wasio wayunani.

Jibu ni katika kuipeleka injili. Alikuwa na deni kubwa sana la kuwafikishia injili, na mara nyingi alipojaribu kwenda alikuwa anapitia vipingamizi vingi.

Na Paulo alikuwa anatumia akili nyingi ili kuwavuta watu kwa Kristo, alipofika kwa Wayahudi waliokuwa wanata ishara, alizitumia hizo ili kuwavuta kwa Kristo..

Kadhalika alipofika kwa Wayunani ambao walikuwa wanataka hekima, hakuitumia miujiza kuwavuta, bali alitumia elimu sana ili kuwavuta..

Hivyo alikuwa anageuka kulingana na aina ya watu aliokutana nao..

1 Wakorintho 9:19 “Maana, ingawa nimekuwa huru kwa watu wote, nalijifanya mtumwa wa wote, ili nipate watu wengi zaidi.

20 Nalikuwa kama Myahudi kwa Wayahudi, ili niwapate Wayahudi; kwa wale walio chini ya sheria, nalikuwa kama chini ya sheria, (ingawa mimi mwenyewe si chini ya sheria), ili niwapate walio chini ya sheria.

21 Kwa wale wasio na sheria nalikuwa kama sina sheria, (si kwamba sina sheria mbele za Mungu, bali mwenye sheria mbele za Kristo), ili niwapate hao wasio na sheria.

22 Kwa wanyonge nalikuwa mnyonge, ili niwapate wanyonge. Nimekuwa hali zote kwa watu wote, ili kwa njia zote nipate kuwaokoa watu.

23 Nami nafanya mambo yote kwa ajili ya Injili ili kuishiriki pamoja na wengine.

24 Je! Hamjui, ya kuwa wale washindanao kwa kupiga mbio, hupiga mbio wote, lakini apokeaye tuzo ni mmoja? Pigeni mbio namna hiyo, ili mpate”.

Hiyo inatufundisha nini sisi wakristo?.
Na sisi pia tunawiwa injili na makundi yote ya watu, tunawiwa injili na maskini na Matajiri, wenye elimu na wasio na Elimu, watu wakuu na watu wanyonge.

Wapo wengi wanaohubiri kwa masikini tu, wakiamini kuwa matajiri hawawezi kuwasikia…

Wapo wanaohubiri kwa kwa watu watu wanyonge tu, wakiamini kuwa watu wakuu hawawezi kuwasikia.

Kumbe kiuhalisia ni wao ndio wamekosa hekima ya kuwaendea…sio kila mtu ataamini kwa kuona ishara ya pepo kutoka. Wengine huna kuanzia huko walipo, hicho wanachokiamini..ukaanza kukifafanua kwa hekima za Roho, ndipo aamini.

Lazima tumwombe Roho Mtakatifu hekima ya jinsi ya kuipeleka injili ili tuyapate makundi yote.

Kwa kumalizia hebu, tuangalie jinsi Paulo alivyowapata baadhi ya watu wa Athene, ambao ni Wayunani..wakati fulani alipokwenda katika nchi yao..

Matendo 17:16 “Paulo alipokuwa akiwangojea huko Athene na kuona jinsi mji ule ulivyojaa sanamu, roho yake ilichukizwa sana ndani yake.

17 Basi katika sinagogi akahojiana na Wayahudi na waliomcha Mungu, na wale waliokutana naye sokoni kila siku.

18 Na baadhi ya Waepikureo na Wastoiko, wenye ujuzi, wakakutana naye. Wengine wakasema, Mpuzi huyu anataka kusema nini? Wengine walisema,Anaonekana kuwa mtangaza habari za miungu migeni, kwa maana alikuwa akihubiri habari za Yesu na ufufuo.

19 Wakamshika, wakamchukua Areopago, wakisema, Je! Twaweza kujua maana ya elimu hii mpya unayoinena?

20 Kwa maana unaleta mambo mageni masikioni mwetu, tutapenda kujua, basi, maana ya mambo haya.

21 Kwa maana Waathene na wageni waliokaa huko walikuwa hawana nafasi kwa neno lo lote ila kutoa habari na kusikiliza habari za jambo jipya.

22 Paulo akasimama katikati ya Areopago, akasema, Enyi watu wa Athene, katika mambo yote naona ya kuwa ninyi ni watu wa kutafakari sana mambo ya dini.

23 Kwa sababu nilipokuwa nikipita huko na huko na kuyaona mambo ya ibada yenu, naliona madhabahu iliyoandikwa maneno haya, KWA MUNGU ASIYEJULIKANA. Basi mimi nawahubirini habari zake yeye ambaye ninyi mnamwabudu bila kumjua.

24 Mungu aliyeufanya ulimwengu na vitu vyote vilivyomo, yeye, kwa kuwa ni Bwana wa mbingu na nchi, hakai katika hekalu zilizojengwa kwa mikono;
[25]wala hatumikiwi kwa mikono ya wanadamu kana kwamba anahitaji kitu cho chote; kwa maana ndiye anayewapa wote uzima na pumzi na vitu vyote.

26 Naye alifanya kila taifa la wanadamu kutoka katika mmoja, wakae juu ya uso wa nchi yote, akiisha kuwawekea nyakati alizoziamuru tangu zamani, na mipaka ya makazi yao;

27 ili wamtafute Mungu, ingawa ni kwa kupapasa-papasa, wakamwone, ijapokuwa hawi mbali na kila mmoja wetu.

28 Kwa maana ndani yake yeye tunaishi, tunakwenda, na kuwa na uhai wetu. Kama vile mmoja wenu, mtunga mashairi alivyosema, Maana sisi sote tu wazao wake.

29 Basi, kwa kuwa sisi tu wazao wa Mungu, haitupasi kudhani ya kuwa Uungu ni mfano wa dhahabu au fedha au jiwe, vitu vilivyochongwa kwa ustadi na akili za wanadamu.

30 Basi, zamani zile za ujinga Mungu alijifanya kama hazioni; bali sasa anawaagiza watu wote wa kila mahali watubu.

31 Kwa maana ameweka siku atakayowahukumu walimwengu kwa haki, kwa mtu yule aliyemchagua; naye amewapa watu wote uthabiti wa mambo haya kwa kumfufua katika wafu.

32 Basi waliposikia habari za ufufuo wa wafu wengine walifanya dhihaka; wengine wakasema, Tutakusikiliza tena katika habari hiyo.

33 Basi hivi Paulo akaondoka akawaacha.

34 Baadhi ya watu wakashikamana naye, wakaamini; katika hao alikuwamo Dionisio, Mwareopago, na mwanamke mmoja jina lake Damari, na watu wengine pamoja na hao.

Maran atha!

Tafadhali washirikishe na wengine habarihizi njema,

Kwa maombezi/Ratiba za ibada/ Ushauri/ Maswali.
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312

pia kama utapenda uyapate mafundisho haya kwa njia ya Whatsapp au email basi tutumie ujumbe kwenye namba hizo hizo.


Mada Nyinginezo:

Mataifa ni nini katika Biblia?

KWANINI TUNAOMBA KWA JINA LA YESU?

Tofauti kati ya kuungama na kutubu ni ipi?

JINA LAKE KWA KIEBRANIA NI ABADONI, NA KWA KIYUNANI NI APOLIONI.

Tofauti kati ya Myunani, Farisayo na Sadukayo ni ipi?

Rudi nyumbani

Print this post

About the author

Admin administrator

Subscribe
Notify of
guest
0 Comments
Inline Feedbacks
View all comments