Category Archive Mafundisho

NI KWA NAMNA GANI KRISTO ALIZIBEBA DHAMBI ZETU?

Ili kuelewa Msamaha wa dhambi jinsi unavyofanya kazi, kwamba ni kwa namna gani Bwana YESU alibeba dhambi zetu, twaweza kuelewa kwa kutafakari mfano huu mrahisi.

Katika sheria za Mahakama inapotokea mfungwa aliyehukumiwa  kifungo, akafariki katikati ya kifungo hiko, na ikathibitishwa na jeshi la magereza pamoja na ripoti za madaktari, na akazikwa basi kile kifungo chake kinakuwa kimefika mwisho, na kesi yake inakuwa haiendelei tena (inafutwa)..

Sasa ikitokea yule mtu akafufuka baada ya siku kadhaa anakuwa hana kesi tena (yupo huru) kwani  kesi yake ilishafutwa, kutokana na ripoti za mahakama na madaktari..

Na zaidi sana mahakama haziamini ufufuo, hivyo itaendelea kuamini kuwa yule mtu alishakufa na taarifa zilithibtishwa na jeshi la magereza pamoja na madaktari.

Sasa ni hivyo hivyo kwa Bwana YESU, yeye alikubali kubeba hatia zetu na makosa yetu yaliyo mengi na akakubali kuhukumiwa kama yeye ndiye aliyeyatenda yale makosa..

Lakini alipokuwa anaanza kukitumikia kile kifungo kwa mateso makali (ambayo kiuhalisia yamgekuwa ya daima)..alikufa katikati..

Na sheria ya hukumu ni kwamba kifo kinahitimisha kifungo cha Mtu, hivyo Kristo alipokufa kifungo chake cha adhabu na mateso kikafikia mwisho, akawa hana hatia tena wala ule mzigo wa dhambi (yupo huru na dhambi sawasawa na maandiko).

Warumi 6:7 “kwa kuwa yeye aliyekufa amehesabiwa haki mbali na dhambi”

Lakini muujiza ni kwamba baada ya siku tatu akaonekana yu hai, na kwasababu hukumu yake ilishafutwa kwa kifo chake, akawa huru na kifungo hiko baada ya kufufuka, ndio maana hatuoni akilia kwa uchungu wa maumivu baadaa kufufuka, bali tunaona ana utukufu mwingi.

Kwahiyo laiti Kristo asingekufa angeendelea kuhesabika laana na mwenye hatia kwaajili ya dhambi zetu nyingi alizozobeba, ingempasa aendelee kukaa katika hali ya adhabu daima, na aendelee kutengwa na MUNGU daima.

Wagalatia 3:13 “Kristo alitukomboa katika laana ya torati, kwa kuwa alifanywa laana kwa ajili yetu; maana imeandikwa, Amelaaniwa kila mtu aangikwaye juu ya mti”

Lakini kifo chake kimehitimisha hukumu yake, ambayo sisi ndio tungepaswa tuitumikie.

Sasa tunapomwamini ndipo tunaingia katika huo mkondo wa kuondolewa dhambi..

Lakini tunapomkataa basi dhambi zetu zinabaki palepale..ni rahisi tu hivyo!.

Je umemwamini Bwana YESU?..Je umebatizwa kwa ubatizo sahihi wa Maji mengi na wa Roho Mtakatifu?.

Kama bado unasubiri nini?…je bado huoni tu gharama kubwa Bwana YESU aliyoingia kwaajili yetu ili tupate ondoleo la dhambi?.

Mpokee YESU leo wala usingoje kesho.

Maran atha!

Washirikishe na wengine habari hizi njema kwa kushea

Ikiwa utapenda kupata msaada wa kumpokea Yesu maishani mwako bure, Basi wasiliana nasi kwa namba uzionazo chini ya makala hii.

Pia kwa kupokea mafundisho ya kila siku kwa njia ya WHATSAPP, jiunge na channel yetu kwa kubofya link hii >> https://whatsapp.com/channel/0029VaBVhuA3WHTbKoz8jx10

Kwa mawasiliano: +255693036618 au +255789001312

Bwana akubariki.

Mafundisho mengine:

Print this post

Fahamu Maana ya Mithali 15:24 Kwa mtu mwenye akili njia ya uhai huenda juu;

SWALI: Nini Maana ya Mithali 15:24?

Kwa mtu mwenye akili njia ya uhai huenda juu; Ili atoke katika kuzimu chini.

JIBU: Hapo yapo mambo matatu,

  1. Mtu mwenye akili.
  2. Njia ya uhai,
  3. Na uelekeo wa njia hiyo.

Mtu mwenye akili ni mtu mwenye uwezo wa kufikiri/kupambanua vema na kufanya maamuzi sahihi katika maeneo mbalimbali ya maisha yake. Hivyo hapo anasema mtu mwenye akili anajua vema kuichagua njia yake ya uhai.

Anasema njia yake hutoka chini kuelekea juu. Kwa lugha ya picha ni barabara iliyopinduliwa na kusimamishwa wima kama ngazi,  na sio mfano wa barabara hizi tulizonazo zilizolala chini, ambazo uelekeo wake ni aidha kaskazini na kusini, au mashariki na magharibi.

Sasa hapa anasema njia yake ya uhai huenda juu, ili atoke kuzimu chini. Akiwa na maana husafiri kutoka kuzimuni kuelekea uzimani juu kwa Mungu.

Hufunua nini?

Safari ya mtu mwenye akili, hufikiri kumtafuta Mungu juu alipo,

Wakolosai 3:1 Basi mkiwa mmefufuliwa pamoja na Kristo, yatafuteni yaliyo juu Kristo aliko, ameketi mkono wa kuume wa Mungu. 2 Yafikirini yaliyo juu, siyo yaliyo katika nchi.

Hufikiri ukuaji wa kiroho, atokea hatua moja ya utakatifu kwenda nyingi, kiwango kimoja cha Imani kuelekea kingine kama Kristo (2Petro 1:5-10, Waefeso 4:13). Ni mtu ambaye kila siku anakwenda mbali na njia ya mauti. Mawazo yake yapo juu sikuzote kumjua Kristo na mapenzi yake yote.

Lakini kinyume chake ni ukweli, mtu asiye na akili barabara yake haijasimama wima, bali imelala. Atawaza atoke hatua moja kwenda nyingine lakini hakuna ukuaji wowote au kuongezeka kokote. Huwenda anachowaza tu sikuzote ni kutoka katika umaskini kwenda katika utajiri, kutoka katika kiwango kimoja cha elimu kwenda kingine, kutoka katika cheo kimoja kwenda katika kingine..Hatua zake ni za kidunia tu, akidhani ndio uzima wake upo hapo. Kumbe kapotea njia.

Si kwamba vinapingwa vya dunia hapana, ni vizuri na vinafaa, lakini havina uzima wa milele ndani yake. Ili uwe na akili hakikisha unampokea Kristo, kisha unaanza kukua kiroho, kila siku unafikiri njia ya kuyakimbia machafu ya kidunia. Hapo barabara yako itakuwa umesimama kama ngazi na hivyo utaiponya nafsi yako.

Je! Umeokoka?. Kama ni la! Basi wakati ndio sasa fungua moyo wako mkaribishe Yesu akuokoe hizi ni nyakati za hatari, tubu leo upokee wokovu. Ikiwa upo tayari kumkaribisha Kristo moyoni mwako, basi waweza kubofya hapa kwa mwongozo wa sala ya Toba. Bwana akubariki. >>>> KUONGOZWA SALA YA TOBA

Washirikishe na wengine habari hizi njema kwa kushea

Ikiwa utapenda kupata msaada wa kumpokea Yesu maishani mwako bure, Basi wasiliana nasi kwa namba uzionazo chini ya makala hii.

Pia kwa kupokea mafundisho ya kila siku kwa njia ya WHATSAPP, jiunge na channel yetu kwa kubofya link hii >> https://whatsapp.com/channel/0029VaBVhuA3WHTbKoz8jx10

Kwa mawasiliano: +255693036618 au +255789001312

Bwana akubariki.

Mafundisho mengine:

Maana ya Mithali 29:9 Mwenye hekima akijadiliana na mpumbavu; Akikasirika au akicheka, pia hapana raha. 

Mpumbavu ni nani katika biblia? (Zaburi 14:1, Mithali 10:14)

Biblia inasema nini kuhusu mtu ‘Mwenye kujipendekeza (Mithali 29:5)

Print this post

ELOI ELOI LAMA SABAKTHANI?

Zaburi 22:1 Mungu wangu, Mungu wangu, Mbona umeniacha? Mbona U mbali na wokovu wangu, Na maneno ya kuugua kwangu? 2 Ee Mungu wangu, nalia mchana lakini hujibu Na wakati wa usiku lakini sipati.

Maneno haya ukiyatafakari, utagundua ni ya mtu aliyefikia hatua mbaya sana ya kukaribia kukata tamaa kwasababu ya aidha magumu, au huzuni, au mateso yasiyoelekeza anayoyapitia, akiangalia kulia, haoni  tumaini lolote, akiangalia kushoto haoni mkono wowote wa Mungu ukimsaidia licha ya kuomba na kulia sana, kwa muda mrefu.

Sehemu nyingine anasema, amekataliwa kila kona, amekuwa kama msikwao kwa ndugu zake.

Zaburi 69:10 Nilipolia na kuiadhibu roho yangu kwa kufunga, Ikawa laumu juu yangu.

11 Nilipofanya gunia kuwa nguo zangu, Nikawa mithali kwao. 12 Waketio langoni hunisema, Na nyimbo za walevi hunidhihaki. 13 Nami maombi yangu nakuomba Wewe, Bwana, Wakati ukupendezao; Ee Mungu, Kwa wingi wa fadhili zako unijibu, Katika kweli ya wokovu wako.

14 Uniponye kwa kunitoa matopeni, Wala usiniache nikazama. Na niponywe nao wanaonichukia, Na katika vilindi vya maji. 15 Mkondo usinigharikishe, wala vilindi visinimeze, Wala shimo lisifumbe kinywa chake juu yangu.

16 Ee Bwana, unijibu, maana fadhili zako ni njema, Kwa kadiri ya rehema zako unielekee. 17 Wala usinifiche uso wako, mimi mtumishi wako, Maana mimi nimo taabuni, unijibu upesi.

Mwandishi huyu alikuwa ni  Daudi, alipitia kipindi kirefu sana cha kujiona kama vile Mungu kamtupa, hadi kuna wakati akaona heri aende kuomba hifadhi kwa maadui zake wafilisti ambao hapo mwanzo aliwafukuza na kuwaita makafiri (wasio tahiriwa), lakini safari hii kwa unyenyekevu wote, anaenda kuwa mmoja wa askari wao, ili tu apate hifadhi, asiangamie kabisa. Huyo ni mtu ambaye maji ya shingo yalimfikia kwelikweli.

Sio kwamba alikuwa haombi, au hamlili Mungu?. Au kwamba ana dhambi kuliko wengine, mpaka awe mtu wa bahati mbaya hivyo Hapana, nyakati zote alikuwa mwombaji, lakini akafika mahali katika uhalisia wa kibinadamu aliona kama Mungu amemwacha kabisa.

Lakini kwasababu huruma za Mungu zilikuwa nyingi juu yake alimpa moyo mkuu, wa kuendelea kumngoja Bwana. Ndio maana  sehemu nyingi katika Zaburi anasisitiza sana Neno hili ‘mngojeeni Bwana’ (Zaburi 37:7, 25:3, 31:24,38:15, 40:1).

Sasa moja ya  maneno machache ya Daudi yaliyonikuliwa na Bwana Yesu lilikuwa ni hili.

Mungu wangu, Mungu wangu, Mbona umeniacha?

Mathayo 27: 45 Basi tangu saa sita palikuwa na giza juu ya nchi yote hata saa tisa.

46 Na kama saa tisa, Yesu akapaza sauti yake kwa nguvu akisema, Eloi, Eloi, lama sabakthani? Yaani, Mungu wangu, Mungu wangu, mbona umeniacha?

Je! Unadhani kauli hiyo Yesu aliyoitoa alimaanisha kweli ameachwa?

Hapana, tangu mwanzo alikuwa anajua Mungu yupo pamoja naye, na kwamba saa yake imekaribia, muda si mrefu anakwenda kuinuliwa na kutukuzwa, tena sehemu nyingine anasema alishangalia pale msalabani (Wakolosai 2:15). Lakini kuinukuu kauli ile ni kuonyesha ubinadamu wetu, unavyoweza kutuhubiria tuwapo katikati ya shida, kwamba Mungu ametuacha hususani pale tunapopitia shida, na mateso.

Yesu alinukuu ubinadamu wetu kukumbuka mfano wa yale aliyoyapitia Daudi..

Lakini tunaona dakika chache baada ya pale, pindi tu alipokata roho, makaburi yakapasuka, wafu wakatoka makaburini, pazia la hekalu likapasuka, na baada ya siku tatu akafufuka, ukombozi wetu mkuu ukapatikana, ‘Lakini ni kwa maneno ya kudhaniwa kuwa Mungu amemwacha’.

Mathayo 27:50 Naye Yesu akiisha kupaza sauti tena kwa nguvu, akaitoa roho yake.

51 Na tazama, pazia la hekalu likapasuka vipande viwili toka juu hata chini; nchi ikatetemeka;

miamba ikapasuka; 52 makaburi yakafunuka; ikainuka miili mingi ya watakatifu waliolala; 53 nao wakiisha kutoka makaburini mwao, baada ya kufufuka kwake, wakauingia mji mtakatifu, wakawatokea wengi.

Ndugu, upitiapo hatua hizo ambazo mawazo yako yanakufundisha kuwa Mungu hayupo na wewe tena, amekuacha, kwasababu ya shida unazozipitia muda mrefu, magonjwa yasiyokoma, umeomba mpaka umechoka, umelia hadi ukomo,wewe ona ni kawaida,…. Piga moyo konde Mngojee Bwana. Daudi alistahimili hatimaye akathibitishwa kwenye ufalme ambao ulidumu pamoja na vizazi vyake vingi tofauti na wafalme wengine wa Israeli. Mngojee Bwana, kimaombi, kwasababu baada ya joto huja mvua.

Shalom.

Washirikishe na wengine habari hizi njema kwa kushea

Ikiwa utapenda kupata msaada wa kumpokea Yesu maishani mwako bure, Basi wasiliana nasi kwa namba uzionazo chini ya makala hii.

Pia kwa kupokea mafundisho ya kila siku kwa njia ya WHATSAPP, jiunge na channel yetu kwa kubofya link hii >> https://whatsapp.com/channel/0029VaBVhuA3WHTbKoz8jx10

Kwa mawasiliano: +255693036618 au +255789001312

Bwana akubariki.

Mafundisho mengine:

KWANINI YESU ALIMUITA BABA YAKE “ABA”?

kiaramu ni lugha gani? je ilizungumzwa na Yesu?

Nzi wa Misri, na Nyuki wa Ashuru vilimaanisha nini? (Isaya 7:18-20).

Print this post

Maana ya Mithali 29:9 Mwenye hekima akijadiliana na mpumbavu; Akikasirika au akicheka, pia hapana raha. 

 Mithali 29:9 Mwenye hekima akijadiliana na mpumbavu; Akikasirika au akicheka, pia hapana raha.


Mstari huo kwa lugha rahisi tunaweza kuuweka kwa namna hii. “Mwenye hekima akijadiliana na mpumbavu, akijibu kwa kicheko au kwa hasira, matokeo ni yaleyale tu hakuna amani au suluhisho”

Unafunua sifa za mpumbavu, kwamba sikuzote mwitikio wake wowote hauwezi kuleta mabadiliko. Kwamfano labda hoja imetolewa na ikamuumiza kiasi cha kumfanya ajibu kwa hasira. Sasa wewe waweza tarajia pengine jambo hilo limemgusa kweli moyo, litambadilisha lakini matokeo yake ni kwamba anakuwa vilevile, Halikadhalika waweza kutoa hoja ikamfanya acheke ukitarajia kitaambatana na  badiliko lolote ndani yake lakini hakuna.

Maana yake mpumbavu, haguswi kwa ukali au kwa wepesi wa maneno ya aina yoyote…Na hivyo ni kuachana naye Tu.

Tukiachia wapumbavu wa kawaida tunaowafahamu..Mpumbavu hasaa ni yule mtu anayeikataa kweli ya Mungu mfano wa wale waandishi na mafarisayo wakati wa Bwana Yesu (Mathayo 23:17), mtu wa namna hii unapomuhubiri injili, hata imchomeje au imchekesheje hawezi kufikiri hata chembe kubadilika, kinyume Chake ni mapambano tu.

Bwana Yesu alitufundisha na kutuambia kuwa si kila mtu ni wa kumtupia lulu zetu, maana yake wanaweza kutugeukia na Kuturarua. Ukiona mtu anaishia kwenye ubishi tu na mashindano, ni kuachana naye na kugeukia waliotayari kupokea.

Bwana akubariki.

Washirikishe na wengine habari hizi njema kwa kushea

Ikiwa utapenda kupata msaada wa kumpokea Yesu maishani mwako bure, Basi wasiliana nasi kwa namba uzionazo chini ya makala hii.

Pia kwa kupokea mafundisho ya kila siku kwa njia ya WHATSAPP, jiunge na channel yetu kwa kubofya link hii >> https://whatsapp.com/channel/0029VaBVhuA3WHTbKoz8jx10

Kwa mawasiliano: +255693036618 au +255789001312

Bwana akubariki.

Mafundisho mengine:

Mpumbavu ni nani katika biblia? (Zaburi 14:1, Mithali 10:14)

Elewa tafsiri ya Mithali 27:22 Hata ukimtwanga mpumbavu kwa mchi kinuni.

KILINDI CHAPIGIA KELELE KILINDI.

Print this post

Theolojia ni nini?. Na je ni sahihi kuisoma?

Theolojia ni elimu ya kujifunza sifa za Mungu na mapenzi yake na jinsi anavyohusiana na wanadamu na ulimwengu  kwa ujumla.

Neno Theolojia limezaliwa kutoka katika maneno mawili ya kigiriki ‘theos’, na ‘logos’

Theos likiwa na maana ya Mungu, na logos ni neno/wazo/elimu/maarifa.

Hivyo tukiunganisha maneno hayo, ni sawa kusema theolojia ni mafundisho au maarifa au elimu kuhusu Mungu.

Ni utafiti kuhusu  Mungu katika mpangilio na mtiririko maalumu. Ukweli ni kwamba theolojia haiwezi kumfafanua Mungu katika ufasaha wote, ikiwa mtu ataitegemea  theolojia tu kumjua Mungu, ukweli ni kwamba amepotea, lakini ikiwa itasomwa vema (si kwa lengo la kitaaluma), bali kwa lengo la kupanua upana wa fikra kuhusu Mungu na maandiko, inafaa sana katika uelewa wa nyanja mbalimbali, hususani kwa wale viongozi na waangalizi kama vile wachungaji, na wahubiri. Si lazima isomwe kwenye vyuo maalumu, mtu yeyote akitia nia kujifunza theolojia anaweza jifunza, kwa kupitia mafundisho mengi, majadiliano na waalimu walio na upeo mpana wa biblia, semina, na kujisomea mwenyewe n.k.

Na Haya ni matawi makuu ya theolojia katika kuichambua biblia.

1) Theolojia ya ki-biblia.

Imejikita katika kutafiti Maudhui au fundisho kuu la biblia, inaangazia jinsi gani vitabu mbalimbali kwenye biblia, vinavyoelezea mpango wa Mungu katika nyakati tofauti tofauti tangu mwanzo hadi mwisho. Mfano kujifunza MAAGANO, katika agano la kale na jipya yalivyotenda kazi na jinsi Yesu alivyoanza kutambulishwa tangu Edeni kama mzao wa mwanamke, hadi nyakati za manabii Isaya 53, hadi wakati wa kutokea kwake duniani Luka 24:27.

Upo umuhimu wa kuijua hii theolojia kwasababu itakupa kujua kiini cha biblia ni nini? Zipo habari nyingi, hadithi nyingi, nyimbo nyingi, mifano mingi, lakini ni vema ujue maudhui zao ni zipi ili usijikute unatoka nje ya shabaha ya imani.

2) Theolojia ya ki-mpangilio/Mada

Inaegemea kujifunza biblia katika migawanyo maalumu ya mada, kwa mfano,

Fundisho la Mungu (theolojia),

Fundisho La Yesu Kristo (Kristolojia),

Fundisho La Roho Mtakatifu (niumatolojia),

Fundisho La wokovu (Soteriolojia),

Fundisho La kanisa,(Ekleziolojia)

La Siku za mwisho.(Esokatolojia)

La mwanadamu (Anthropolojia)

La malaika (Angeolojia)

3) Theolojia ya ki-vitendo

Inajikita kujifunza jinsi maagizo ya kibiblia yanavyoweza kutendewa kazi katika,, huduma kwa mfano kuhubiri na kufundisha , katika uangalizi wa kichungaji, katika umisheni, na katika taratibu za kiibada, na katika kutoa mashauri ya kikristo kama vile kuwaonya wenye matatizo ya kiroho,  kifikra, vifungo n.k.

4) Theolojia ya ki-historia.

Inaangazia jinsi gani imani ya kikristo imekuwa ikipiga hatua katika vipindi mbalimbali vya kihistoria, inaangazia mabaraza mbalimbali ya makanisa yaliyokaa katika kujadili fundisho na misingi ya imani. Kwamfano lile baraza la Nikea (325WK). Mpaka nyakati za matengenezo mfano akina Martin Luther, calvin, na wengine.

Hii inakusaidia kujua historia na chimbuko la imani yetu, na sababu ya ukristo kuonekana katika muundo huu leo.

5) Theolojia ya kimaadili.

Hii inaegemea katika ukristo na jamii, kwamfano mtazamo wa ukristo katika maeneo ya kijamii mfano ndoa, biashara, taratibu za kijamii, haki za kibinadamu, vita,

Zipo theolojia nyingine kama vile theolojia za tafsiri, za kulinganisha, za utetezi, za kifalsafa. n.k. Kwasababu ya upana wa theolojia, haya ni  matawi baadhi tu, kati ya mengi. Hivyo, kama watu wa Mungu, pamoja na kutegemea Bwana kutufunulia mwenyewe maandiko, upo pia wakati ambao hatuna budi kuyamulika maandiko kiundani (Kitheolojia), tukiwa na lengo la kumjua Mungu kwa upana na sio kuwa wasomi, au wanataaluma.

Bwana akubariki.

Washirikishe na wengine habari hizi njema kwa kushea

Ikiwa utapenda kupata msaada wa kumpokea Yesu maishani mwako bure, Basi wasiliana nasi kwa namba uzionazo chini ya makala hii.

Pia kwa kupokea mafundisho ya kila siku kwa njia ya WHATSAPP, jiunge na channel yetu kwa kubofya link hii >> https://whatsapp.com/channel/0029VaBVhuA3WHTbKoz8jx10

Kwa mawasiliano: +255693036618 au +255789001312

Bwana akubariki.

Mafundisho mengine:

Mwanazuoni ni mtu gani kibiblia?

Kwanini kuna tafsiri nyingi za Biblia, na tafsiri ipi ni sahihi?

Yesu anapoitwa mwana wa Azali, maana yake nini?

Print this post

Kwanini Mungu alimchagua Musa, na si mtu mwingine?

Mungu hakumchagua Musa kwasababu ya wema, au kipawa, au ujuzi fulani aliokuwa nao tofauti na wengine. Hapana almchagua ili ‘kutumiza kusudi lake la kuchagua’ ambalo tunalisoma kwa urefu katika (Warumi 9:11-17). Linalomaanisha Mungu humchagua mtu na kumfanya awe kama anavyotaka mwenyewe, na sio kwa jinsi Yule mtu atakavyo.  Kwamfano alimchagua Farao, kisha akamwekea moyo mgumu,ili atimize kusudi lake mwenyewe, kujichotea utukufu kwa mapigo yale kumi,aliyoyaachia kwa wamisri, vivyo hivyo na kwa Musa alimchagua na kumpa neema ile kubwa ya hofu ya Ki-Mungu na upole ili atimize kusudi lake la kuwakomboa wana wa Israeli.

Lakini hakuwa na tendo lolote jema alilowahi kutenda lililomshawishi Mungu amchague yeye tofauti na wengine.

Na ndivyo anavyofanya hata sasa kwa wanadamu wote. Tunaokolewa na kutumiwa na Mungu kwa neema tu, na si kwasababu ya matendo Fulani mema tuliyowahi kumtendea Mungu.

Washirikishe na wengine habari hizi njema kwa kushea

Ikiwa utapenda kupata msaada wa kumpokea Yesu maishani mwako bure, Basi wasiliana nasi kwa namba uzionazo chini ya makala hii.

Pia kwa kupokea mafundisho ya kila siku kwa njia ya WHATSAPP, jiunge na channel yetu kwa kubofya link hii >> https://whatsapp.com/channel/0029VaBVhuA3WHTbKoz8jx10

Kwa mawasiliano: +255693036618 au +255789001312

Bwana akubariki.

Mafundisho mengine:

Nini tofauti ya Majira na Wakati?

Tofauti ya kazi ya Damu ya Yesu na Jina la Yesu ni ipi?

NAAM, HATA WABAYA KWA SIKU YA UBAYA. 

Print this post

KILA MTU NA AMCHE BABA YAKE NA MAMA YAKE.

(Mafunzo maalumu kwa watoto na walezi).

Kama wewe ni mtoto basi jifunze haya, na kama ni mzazi basi pia jifunze haya na pia mfunze mwanao…

Mambo ya Walawi 19:3 “Kila mtu na amche mama yake, na baba yake, nanyi mtazitunza Sabato zangu; mimi ndimi BWANA, Mungu wenu”

Biblia imetumia neno “kumcha” kuonyesha msisitizo wa jambo hilo, jinsi lilivyo la msingi.

“Kumcha mzazi” sio “kumwabudu” bali ni kumpa heshima ya hali ya juu sana, ikiwemo kumsikiliza, kumtii na kufanya yale anayosema bila kumsumbua sumbua ikiwa jambo hilo si nje na mapenzi ya MUNGU.

Maana yake kama tunavyomcha MUNGU, kila atuambiacho tunakizingatia, kwasababu tunajua kwake kuna baraka na laana, kadhalika na wazazi hivyp hivyo wanaweza kutubariki na kutulaani.

Sasa wengi wetu inapofika eneo hili la kutafakari mzazi na mtoto akili zetu huwa zinalenga kufikiri wale watoto walio chini ya malezi ya wazazi, pasipo kujua kuwa hata uwe na miaka 70 na kama mzazi wako yupo hai bado hiyo amri inakuhusu hata wewe ya kumcha mzazi wako, kwani wewe bado ni mtoto kwake.

Amri ya watoto kuwatii na kuwaheshimu wazazi inawahusu hata wenye ndevu na hata wazee wenye mvi, haijalishi wewe sasa ni bibi au babu na unao wajukuu…kama mzazi wako yupo hai unayo amri ya kumcha..

Lakini ukimvunjia heshima mzazi kwasababu ni mzee, basi fahamu kuwa bado hujayajua maandiko.

Mithali 23:22 “Msikilize baba yako aliyekuzaa, Wala usimdharau mama yako akiwa mzee”

Jifunze kumcha Mzazi, wapo watu wanapambana na wazazi wakati wote, wanagombana na wazazi, na hata kuwaita wachawi, usiwe jamii ya hao watu waliotabiriwa..

Mithali 30:11,”Kuna kizazi cha watu wamlaanio baba yao; Wala hawambariki mama yao”. 

Yafuatayo ni madhara machache ya kutomcha Mzazi.

    1. Jicho kung’olewa.

Mithali 30:17 “Jicho la mtu amdhihakiye babaye, Na kudharau kumtii mamaye; Kunguru wa bondeni wataling’oa Na vifaranga vya tai watalila”

Mtu aliyetolewa macho ni kipofu, hawezi kuona ya mbele wala ya nyuma katika maisha yake, atabaki anapapasa tu.

  2. Kifo.

Mithali 20:20 “Amlaaniye babaye au mamaye, Taa yake itazimika katika giza kuu”.

Maana ya Taa kuzimika ni “kifo”. (Soma Ayubu 21:17).

Yapo na madhara mengine mengi ikiwemo kukosa Heri mashani..

Je unamcha mzazi wako?..je unameombea?..je umepatana naye?. Kama bado hujafanya hayo yote basi anza leo.

Bwana akubariki na atusaidie.

Washirikishe na wengine habari hizi njema kwa kushea

Ikiwa utapenda kupata msaada wa kumpokea Yesu maishani mwako bure, Basi wasiliana nasi kwa namba uzionazo chini ya makala hii.

Pia kwa kupokea mafundisho ya kila siku kwa njia ya WHATSAPP, jiunge na channel yetu kwa kubofya link hii >> https://whatsapp.com/channel/0029VaBVhuA3WHTbKoz8jx10

Kwa mawasiliano: +255693036618 au +255789001312

Bwana akubariki.

Mafundisho mengine:

Print this post

Uchambuzi wa kitabu cha pili cha Paulo kwa Timotheo (2Timotheo).

Huu ni waraka wa Pili ambao mtume Paulo aliuandika kwa mwanae Timotheo akiwa kama mfungwa kule Rumi (2Timotheo 1:17)

Ni waraka wa Kitume zaidi, akimweleza Timotheo mambo mengi anayopaswa ayafanya, na ayaelewe kuhusiana na kazi ya Mungu.

Maudhui makuu ya Paulo yalikuwa ni haya;.

  1. Kumtaka Timotheo ajithibitishe vema katika huduma, 
  2. Lakini pia kumjuza juu ya tabia za wahudumu mbalimbali atakaokutana nao katika kazi ya Mungu, 
  3. Tabia zitakazoonekana siku za mwisho, jinsi asili ya watu itakavyokuwa na namna ya kukabiliana nazo.

Haya ni maelezo mafupi katika maeneo hayo makuu:

1) Wito kwa Timotheo kuwa kamili Na thabiti Katika huduma.

> Paulo Anaanza kwa kumtaka Timotheo aichochee karama iliyo ndani yake, aliyoipokea kwa kuwekewa mikono na yeye. Akionyesha kuwa huduma ni kama moto ambao ili kuufanya uendelee kuwaka inahitaji wakati wote uchochewe.(2Timotheo 1:6-8)

> Anamsihi kama askari mwema, ajikite katika kazi moja ya injili, Asipeleke fikra zake katika shughuli za kidunia, akimtaka afahamu hilo ili aweze kuvipiga vita vizuri vya imani, bila kuvutwa na mambo mengi.

2 Timotheo 2:3-7

[3]Ushiriki taabu pamoja nami, kama askari mwema wa Kristo Yesu.

[4]Hakuna apigaye vita ajitiaye katika shughuli za dunia, ili ampendeze yeye aliyemwandika awe askari.

[5]Hata mtu akishindana katika machezo hapewi taji, asiposhindana kwa halali.

[6]Yampasa mkulima mwenye taabu ya kazi kuwa wa kwanza wa kupata fungu la matunda.

[7]Yafahamu sana hayo nisemayo, kwa maana Bwana atakupa akili katika mambo yote.

> Anamtaka pia ajionyeshe Kuwa amekubaliwa na Mungu, Mtu awezaye kuligawanya Neno la Mungu vema, (2:15)

> Azikimbie tamaa za ujanani (2:22)

> Awe tayari kuhubiri injili Wakati wote  ufaao na usiofaa.(4:1-2)

> Awe na kiasi katika mambo yote, avumilie mabaya, atimize huduma yake. (4:5)

> Akumbuke pia akikubali kuishi maisha ya utauwa ataudhiwa.(3:12)

2) Tabia mbalimbali za wahudumu wenza.

Paulo anatoa habari za tabia alizokutana nazo kwa baadhi wa wahudumu wenza,

makundi hayo ni kama yafuatayo;

> Walioshirika na yeye nyakati zote kwa uaminifu,  mfano wa hawa ni Onesiforo na watu wa nyumbani mwake, pamoja na Luka(1:16).

> Waliotengana naye  kwasababu njema za mtawanyiko wa kihuduma mfano wa hawa ni Kreste na Tito,(4:9b)

> Lakini wapo ambao walimwacha kwa kupenda dunia mfano wa hawa ni Dema.(4:9)

> Na wengine kwa kujiingiza kwenye mafundisho ya uongo mfano wa hawa ni Himenayo na Fileto.(2:17-18)

> Na wengine walifanyika kabisa wapinzani wake. Mfano wa hawa ni Iskanda mfua shaba.(4:14)

Lengo la Paulo kumjuza juu ya watu hawa ni kumtaka ajifunze kuvumilia, na pia kujiepusha nao hususani wale wapingamizi, na kuweka misingi ya kimafundisho kwa kuwatahadharisha watu wasiyafuatishe mafundisho mengine, kwani makundi hayo atakutana nayo, na yatakuwepo.

3) Nyakati za hatari, katika siku za mwisho.

Paulo anampasha habari Timotheo uhalisia juu ya nyakati za mwisho, ambazo tangu wakati ule zilikuwa tayari zimeshaanza..

2 Timotheo 3:1-5

[1]Lakini ufahamu neno hili, ya kuwa siku za mwisho kutakuwako nyakati za hatari.

[2]Maana watu watakuwa wenye kujipenda wenyewe, wenye kupenda fedha, wenye kujisifu, wenye kiburi, wenye kutukana, wasiotii wazazi wao, wasio na shukrani, wasio safi,

[3]wasiowapenda wa kwao, wasiotaka kufanya suluhu, wasingiziaji, wasiojizuia, wakali, wasiopenda mema,

[4]wasaliti, wakaidi, wenye kujivuna, wapendao anasa kuliko kumpenda Mungu;

[5]wenye mfano wa utauwa, lakini wakikana nguvu zake; hao nao ujiepushe nao.

makusudi yake ni kumtaka avumilie, na kusimama  imara katika huduma, kwasababu nyakati ngumu atakutana nazo za watu wengi kujiepusha na mafundisho ya uzima.

Anasema pia kutazuka wimbi la waalimu wa uongo,  wapinzani wa injili mfano wa Yane na Yambre, ambao watashindana na kweli, (3:8-9).

Hatua za kuchua:

> Adumu katika mafundisho na mwenendo wote alioupokea kwake (3:10, 14)

> Awakabidhi wengine mapokeo hayo. .(2:1)

> Ajiepushe na mashindano ya kidini, na maneno yasiyokuwa na maana (2:16, 23-26)

Mwisho.

Paulo anaeleza mwisho wake, na sababu ya kuvipiga vita vema na kusimama imara katika Imani,  ni kwasababu aliiona ile  taji ya haki aliyowekewa Na Mungu mbinguni. Akitumai na Timotheo atasukumwa kuvipiga vita vema kwa kuiona thawabu hiyo hiyo aliyowekewa mbinguni.

2 Timotheo 4:6-8

[6]Kwa maana, mimi sasa namiminwa, na wakati wa kufariki kwangu umefika.

[7]Nimevipiga vita vilivyo vizuri, mwendo nimeumaliza, Imani nimeilinda;

[8]baada ya hayo nimewekewa taji ya haki, ambayo Bwana, mhukumu mwenye haki, atanipa siku ile; wala si mimi tu, bali na watu wote pia waliopenda kufunuliwa kwake.

Shalom.

Washirikishe na wengine habari hizi njema kwa kushea

Ikiwa utapenda kupata msaada wa kumpokea Yesu maishani mwako bure, Basi wasiliana nasi kwa namba uzionazo chini ya makala hii.

Pia kwa kupokea mafundisho ya kila siku kwa njia ya WHATSAPP, jiunge na channel yetu kwa kubofya link hii >> https://whatsapp.com/channel/0029VaBVhuA3WHTbKoz8jx10

Kwa mawasiliano: +255693036618 au +255789001312

Bwana akubariki.

Mafundisho mengine:

Uchambuzi wa kitabu cha kwanza cha Paulo kwa Timotheo (1Timotheo)

MAMBO NANE (8), AMBAYO WEWE KAMA KIONGOZI UTAIGWA.

UNALITUMIA KWA HALALI NENO LA KWELI?.

Print this post

Fahamu maana ya Mithali 27:19 Kama uso katika maji ndivyo mtu na mwenzake

Mithali 27:19 Kama uso ufananavyo na uso katika maji; Kadhalika moyo wa mtu na mwenzake.


JIBU: Anaanza kwa kutoa mfano halisi, ili kueleza vema jambo la kitabia. Anasema kama vile maji yanavyoweza kuwa kioo kiakisicho, vivyo hivyo mioyo ya watu walio pamoja.

Kama tunavyojua ukiyatazama maji, utauona uso wako vilevile kama ulivyoyatazama, wala hayawezi kudanganya, ukiyaangalia umekunja sura, utaonekana hivyo hivyo, ukiyaangalia umevaa kofia, utajiona hivyo hivyo.

Ndivyo Mungu anavyowaona watu wawili waliojiungamanisha katika kitu kimmoja,(urafiki),  tabia ya mmoja itamwakisi mwingine, mwisho wa siku watafanana tu na kuwa na mwenendo sawa. Akiwa mmoja ni mwizi, Yule mwingine atakuwa kama yeye tu, akiwa mmoja ni mwamini mwombaji Yule mwenzake atakuwa naye mwombaji, akiwa ni mkarimu, mwenzake naye atakuwa hivyo hivyo.

Ndio sababu biblia inasema wawili hawawezi kukaa pamoja isipokuwa wamepatana (Amosi 3:3). Hivyo vifungu hivi vinatukumbusha umuhimu wa kuchagua watu sahihi wa kuambatana nao, imesisitiza tusifungwe nira ya watu wasioamini, kwa jinsi isivyo sawasawa, kwasababu kwa njia hiyo watatuambukiza tabia zao.

Hata katika kuoa/kuolewa, ikiwa umeokoka, tafuta wa kufanana na wewe, au mbadilishe kwanza awe kama wewe ndio umwoe/uolewe naye vinginevyo, unajiandaa kugeuzwa tabia kama ilivyokuwa kwa Sulemani kuoa wake wa kimataifa.

Shalom.

Washirikishe na wengine habari hizi njema kwa kushea

Ikiwa utapenda kupata msaada wa kumpokea Yesu maishani mwako bure, Basi wasiliana nasi kwa namba uzionazo chini ya makala hii.

Pia unaweza ukapata mafundisho haya Kwa njia ya Whatsapp yako, jiunge na channel yetu Kwa kubofya hapa >> WHATSAPP

Kwa mawasiliano: +255693036618 au +255789001312

Bwana akubariki.

Mafundisho mengine:

NI UTUKUFU WA MUNGU KUFICHA JAMBO.

Na alaaniwe ampigaye mwenzake kwa siri.

Amali, na kila kazi ya ustadi, inatokana na mtu kupingana na mwenzake.

Print this post

NI NANI TUNAPASWA TUMWONE ZAIDI KILA TUSOMAPO BIBLIA?

Je ni nani unayemwona zaidi usomapo biblia?..Je ni Musa?, au Eliya? au Elisha au nabii gani mwingine?..


Je ni habari za nani unapenda kuzihubiri zaidi katika biblia?…

Kama ni taswira za wanadamu ndizo zinazokujia zaidi basi kuna uwezekano macho yako bado hayajafunguka vizuri..

Leo nataka tuangalie ni nani tunayepaswa kumwona zaidi na kumhubiri zaidi kila tusomapo biblia…

Tuyarejee maneno yafuatayo ya Bwana YESU..

Luka 24:25 “Akawaambia, Enyi msiofahamu, wenye mioyo mizito ya kuamini yote waliyoyasema manabii!

26 Je! Haikumpasa Kristo kupata mateso haya na kuingia katika utukufu wake?

27 AKAANZA KUTOKA MUSA NA MANABII WOTE, akawaeleza katika maandiko yote mambo yaliyomhusu yeye mwenyewe”.

Hapa Bwana YESU hakuanza kuwafunulia maandiko kwa kuanza kumtukuza Musa au Eliya na uhodari wao…La! Bali alianza kuelezea habari zinazomhusu yeye mwenyewe..

Wala kumsifu Samson na ushujaa wake, bali kupitia habari za Samson alijionyesha nafasi yake..

Vile vile hakuanza kumsifia na kumtukuza Sulemani na wake zake na mke wake, bali kupitia maisha ya Sulemani alielezea habari zake zaidi..na hivyo hivyo kwa manabii wengine wote, kupitia maisha yao na nyaraka zao alijielezea yeye mwenyewe…

Tuangalie maandiko machache ya manabii yaliyomhusu yeye

》  Nabii Musa aliandika habari za Bwana YESU!!..

Kumbukumbu 18:15 “BWANA, Mungu wako, atakuondokeshea nabii miongoni mwa ndugu zako kama nilivyo mimi; msikilizeni yeye”.

》 Nabii Samweli naye aliandika naye habari za Bwana YESU!!..

1Samweli 2:1 “Nami nitajiinulia kuhani mwaminifu, atakayefanya sawasawa na mambo yote niliyo nayo katika moyo wangu, na katika nia yangu; nami nitamjengea nyumba iliyo imara; naye atakwenda mbele ya masihi wangu milele”.

》 Na Nabii Isaya naye aliandika habari za mkuu wa uzima YESU, 

Isaya 9:6 “Maana kwa ajili yetu mtoto amezaliwa, Tumepewa mtoto mwanamume; Na uweza wa kifalme utakuwa begani mwake; Naye ataitwa jina lake, Mshauri wa ajabu, Mungu mwenye nguvu, Baba wa milele, Mfalme wa amani”

Soma pia Isaya 7:14.

》 Pia Nabii Mika aliandika habari za YESU..

Mika 5:2 “Bali wewe, Bethlehemu Efrata, uliye mdogo kuwa miongoni mwa elfu za Yuda; kutoka kwako wewe atanitokea mmoja atakayekuwa mtawala katika Israeli; ambaye matokeo yake yamekuwa tangu zamani za kale, tangu milele”

》 Bila kumsahau na Daudi naye aliandika habari za YESU.

Zaburi 22:18 “Wanagawanya nguo zangu, Na vazi langu wanalipigia kura”.

Linganisha na Mathayo 27:35..

》 Nabii Hosea naye hakuacha kumtaja YESU..

Hosea 11:1 “Israeli alipokuwa mtoto, nalikuwa nikimpenda, nikamwita mwanangu atoke Misri”.

Linganisha na Mathayo 2:14-15.

》 Na Yeremia naye alimzungumzia YESU KRISTO.

Yeremia 31:15 “BWANA asema hivi, Sauti imesikiwa Rama, kilio, na maombolezo mengi, Raheli akiwalilia watoto wake; asikubali kufarijiwa kwa watoto wake, kwa kuwa hawako”

Linganisha na Mathayo 2:18.

》Na nabii Zekaria ni hivyo hivyo..

Zekaria 9:9 “Furahi sana, Ee binti Sayuni; Piga kelele, Ee binti Yerusalemu; Tazama, mfalme wako anakuja kwako; Ni mwenye haki, naye ana wokovu; Ni mnyenyekevu, amepanda punda, Naam, mwana-punda, mtoto wa punda”.

Linganisha na Mathayo 21:5.

》 Bila kumsahau Danieli naye alimwona YESU

Danieli 7:13 “Nikaona katika njozi za usiku, na tazama, mmoja aliye mfano wa mwanadamu akaja pamoja na mawingu ya mbingu akamkaribia huyo mzee wa siku, wakamleta karibu naye.

14 Naye akapewa mamlaka, na utukufu, na ufalme, ili watu wa kabila zote, na taifa zote, na lugha zote, wamtumikie; mamlaka yake ni mamlaka ya milele, ambayo hayatapita kamwe, na ufalme wake ni ufalme usioweza kuangamizwa”.

》 Na malaki alimwona pia..

Malaki 3:1 “Angalieni, namtuma mjumbe wangu, naye ataitengeneza njia mbele yangu; naye Bwana mnayemtafuta atalijilia hekalu lake ghafula; naam, yule mjumbe wa agano mnayemfurahia, angalieni, anakuja, asema BWANA wa majeshi”

》 Nabii Yona naye ni hivyo hivyo aliandika habari za YESU..Soma Mathayo 12:40.

》 Nabii Ezekieli alieleza habari zake YESU…Soma Ezekieli 36:26-27 linganisha na Yohana 15:26.

》  Nabii Amos aliandika mahubiri ya yake YESU…Soma  Amosi 8:9 linganisha na Mathayo 24:29.

》 Nabii Yoeli naye alizigusia kazi zake..

Soma Yoeli 2:28-32

》 Ayubu naye alimwona Soma Ayubu 19:25.

Na manabii wengine wote walimwona YESU kabla ya wakati na kuandika habari zake.

Hiyo ni kuonyesha jinsi YESU KRISTO alivyo kiini cha Imani, na kiini cha mafundisho..

Tukiweza kufikia kiwango cha kumwona Bwana YESU zaidi katika biblia zaidi ya mtu mwingine yeyote sisi ni watu wengine na wenye akili, na hapo ndipo tunapoweza kusema kuwa tunaijua biblia..

Luka 24:44 “Kisha akawaambia, Hayo ndiyo maneno yangu niliyowaambia nilipokuwa nikali pamoja nanyi, ya kwamba ni lazima yatimizwe yote niliyoandikiwa katika Torati ya Musa, na katika Manabii na Zaburi.

45 Ndipo akawafunulia akili zao wapate kuelewa na maandiko”.

Bwana atufune akili zetu tumjue sana Mwana wa Mungu.

Waefeso 4:13 “hata na sisi sote tutakapoufikia umoja wa imani na kumfahamu sana Mwana wa Mungu, hata kuwa mtu mkamilifu, hata kufika kwenye cheo cha kimo cha utimilifu wa Kristo”.

Maran atha.

Washirikishe na wengine habari hizi njema kwa kushea

Ikiwa utapenda kupata msaada wa kumpokea Yesu maishani mwako bure, Basi wasiliana nasi kwa namba uzionazo chini ya makala hii.

Pia kwa kupokea mafundisho ya kila siku kwa njia ya WHATSAPP, jiunge na channel yetu kwa kubofya link hii >> https://whatsapp.com/channel/0029VaBVhuA3WHTbKoz8jx10

Kwa mawasiliano: +255693036618 au +255789001312

Bwana akubariki.

Mafundisho mengine:

Print this post