Category Archive maswali na majibu

Apitaye cheo ni mtu wa namna gani?

Jibu: Turejee..

2Yohana 1:9 “KILA APITAYE CHEO, wala asidumu katika mafundisho ya Kristo, yeye hana Mungu. Yeye adumuye katika mafundisho hayo, huyo ana Baba na Mwana pia”.

“Cheo” ni neno lenye maana ya “Kipimo”..

> Kwamfano Mtu mwenye kipimo kikubwa cha heshima katika kazi/shughuli fulani maana yake huyo mtu ana cheo kikubwa  katika kazi hiyo…

> Au mtu mwenye kipimo kikubwa che heshima kuliko wenzake katika Serikali/mamlaka, maana yake mtu huyo ana cheo kikubwa..

Marko 6:21 “Hata ilipotokea siku ya kufaa, na Herode, sikukuu ya kuzaliwa kwake, alipowafanyia karamu wakubwa wake, na majemadari, na watu wenye cheo wa Galilaya”

> Vile vile mtu mwenye kipimo kikubwa cha umri, ni sawa na kusema ana cheo kikubwa cha umri..

Mwanzo 43:33 “Wakaketi mbele yake, mzaliwa wa kwanza kwa cheo cha kuzaliwa kwake, na mdogo kwa udogo wake; watu hao wakastaajabu wao kwa wao”.

Sasa tukirudi kwenye swali, mtu apitaye cheo ni mtu wa namna gani?

Mtu “apitaye cheo” kulingana na andiko hilo, ni mtu avukaye kipimo au mipaka ya Mafundisho ya KRISTO.

Maana yake kama neno la Mungu linasema “Usiibe”  au “Usizini” yeye atatafuta namna ya kuhalalisha wizi au uzinzi au ushoga kwa namna yoyote ile (ambapo hapo kwanza tayari alikuwa amekwisha kuamini kuwa wizi na uzinzi ni dhambi) lakini sasa anataka kuhalalisha zinaa au wizi anaoufanya au anaoutamani.

Mtu wa namna hiyo ni mtu aliyevuka cheo cha mafundisho ya Kristo, (maana yake alikuwa katika mafundisho sahihi lakini sasa amevuka mipaka)..na mtu wa hivyo biblia inasema hana Mungu ndani yake.

Hivyo hatuna budi daima kudumu na kusimama katika Neno la Mungu.. Kwasababu biblia inasema limehakikiwa na halina kasoro, na hivyo hatuhitaji sisi kulirekebisha..

Mithali 30:5 “Kila neno la Mungu limehakikishwa; Yeye ni ngao yao wamwaminio.

6 Usiongeze neno katika maneno yake; Asije akakulaumu, ukaonekana u mwongo”.

Tukivuka kipimo (cheo) kwasababu aidha ya kiburi au tamaa ya kuhalalisha mambo mabaya na tukalipindisha Neno la lake (mafundisho yake), basi tutaangukia katika hukumu ile iliyotajwa katika Ufunuo 22:18…

Ufunuo 22:18 “Namshuhudia kila mtu ayasikiaye maneno ya unabii wa kitabu hiki, Mtu ye yote akiyaongeza, Mungu atamwongezea hayo mapigo yaliyoandikwa katika kitabu hiki”.

Bwana atusaidie tufikie cheo na si tuvuke cheo. (Waefeso 4:13).

Maran atha!

Washirikishe na wengine habari hizi njema kwa kushea

Ikiwa utapenda kupata msaada wa kumpokea Yesu maishani mwako bure, Basi wasiliana nasi kwa namba uzionazo chini ya makala hii.

Pia kwa kupokea mafundisho ya kila siku kwa njia ya WHATSAPP, jiunge na channel yetu kwa kupofya link hii >> https://whatsapp.com/channel/0029VaBVhuA3WHTbKoz8jx10

Kwa mawasiliano: +255789001312 au +255693036618

Bwana akubariki.

Mafundisho mengine:

USIKWEPE CHUO CHA UTAKATIFU.

UAMINIFU NI KIGEZO KIKUBWA CHA KUTUMIWA NA MUNGU.

Fahamu Namna ya Kuomba.

Je shetani ana uwezo wa kujua mawazo ya mtu?

MAMBO (2) YATAKAYOKUTENGA NA IMANI SIKU HIZI ZA MWISHO.

Rudi Nyumbani

Print this post

Nyapara/ wanyapara ni watu gani? (Kutoka 5:14)

Jibu: Turejee..

Kutoka 5:14 “Na WANYAPARA wa wana wa Israeli, ambao wasimamizi wa Farao wamewaweka juu yao, wakapigwa, wakiambiwa, Kwa nini hamkutimiza kazi yenu jana na leo; kwa kufanya matofali kama hapo kwanza?

15 Basi WANYAPARA wa wana wa Israeli wakaenda, wakamlilia Farao, wakisema, Mbona umetutendea hivi, sisi watumwa wako?

16 Watumwa wako hawapewi majani, nao wanatuambia, Fanyeni matofali; na tazama, watumwa wako wapigwa; lakini kosa hilo ni la watu wako mwenyewe”.

“Wanyapara” ni wasimamizi wa wafungwa au watumwa.

Katika magereza, wale wafungwa wanaoteuliwa kuwa kama viongozi wa wafungwa wenzao ndio wanaoitwa “wanyapara”. Hivyo yule askari ambaye ni mkuu wa gereza anapotoa agizo basi yule Nyapara ndiye anayelichukua na kuliwasilisha kwa wafungwa wenzake na yeye mwenyewe anakuwa ni msimamizi juu yao, ingawa naye pia ni mfungwa.

Sasa kipindi wana wa Israeli wapo Misri utumwani, wale wasimamizi wa Farao (Maaskari) waliwachagua baadhi ya wafungwa na kuwafanya wanyapara kwa wafungwa wenzao.

Na Wasimamizi hao walipotoa amri ya kazi Fulani, basi waliwaangalia hao wanyapara na hao wanyapara ndio waliowaongoza watumwa wenzao, na ikitokea watumwa (wana wa Israeli) wamekaidi au wanafanya kazi kwa ulegevu basi wanaoathirika wa kwanza ni wanyapara wao, kwani wale wasimamizi wa Farao walikuwa wanashughulika kwanza na hao wanyapara kabla ya watumwa wenyewe.

Kutoka 5:14 “Na wanyapara wa wana wa Israeli, ambao wasimamizi wa Farao wamewaweka juu yao, wakapigwa, wakiambiwa, Kwa nini hamkutimiza kazi yenu jana na leo; kwa kufanya matofali kama hapo kwanza?”

Shetani naye anao wanyapara wake aliowaweka juu ya wote wanaotumikishwa na dhambi!.. kwasababu biblia inasema atendaye dhambi ni mtumwa wa dhambi, na kama ni mtumwa basi ni lazima atakuwa na nyapara wake.

Kama unaishi katika uzinzi na uasherati, yule unayeishi naye kama mume/mke ni nyapara wa ibilisi kwako, ndio maana dhambi inakutesa na huyo naye anakutesa, kwasababu wote mpo katika dhambi na ni hivyo hivyo katika dhambi nyingine zote…ni lazima shetani akupe nyapara juu yako.

Leo hii mkatae shetani na manyapara wake,..mkubali Bwana YESU upate uzima wa milele.

Bwana akubariki.

Washirikishe na wengine habari hizi njema kwa kushea

Ikiwa utapenda kupata msaada wa kumpokea Yesu maishani mwako bure, Basi wasiliana nasi kwa namba uzionazo chini ya makala hii.

Pia kwa kupokea mafundisho ya kila siku kwa njia ya WHATSAPP, jiunge na channel yetu kwa kupofya link hii >> https://whatsapp.com/channel/0029VaBVhuA3WHTbKoz8jx10

Kwa mawasiliano: +255789001312 au +255693036618

Bwana akubariki.

Mafundisho mengine:

Ni kosa gani lililowafanya wana wa israeli wawe watumwa miaka 400 Misri?.

VIUNO VYENU VIWE VIMEFUNGWA NA TAA ZENU ZIWE ZINAWAKA

USIMWABUDU SHETANI!

Je Farao alikufa kwenye maji pamoja na jeshi lake au alipona?

Tu uzao wake Ibrahimu, wala hatujawa watumwa wa mtu.

Rudi Nyumbani

Print this post

Amka, Ee upanga, juu ya mchungaji wangu (Zekaria 13:7-9)

SWALI: Nini maana ya hivi vifungu?

Zekaria 13:7-9

[7]Amka, Ee upanga, juu ya mchungaji wangu, na juu ya mtu aliye mwenzangu, asema BWANA wa majeshi; mpige mchungaji, nao kondoo watatawanyika; nami nitaugeuza mkono wangu juu ya wadogo.

[8]Hata itakuwa, ya kwamba katika nchi yote mafungu mawili yatakatiliwa mbali, nao watakufa, asema BWANA; lakini fungu la tatu litabaki humo.

[9]Nami nitalileta fungu lile la tatu na kulipitisha kati ya moto, nami nitawasafisha kama fedha isafishwavyo, nami nitawajaribu kama dhahabu ijaribiwavyo; wataliitia jina langu, nami nitawasikia; mimi nitasema, Watu hawa ndio wangu; nao watasema, BWANA ndiye Mungu wangu.


JIBU: Unabii huu ulimtabiri Yesu, wakati wa kukamatwa kwake na wayahudi ili auawe, ukisoma Mathayo 26:31 utaona Bwana alinukuu yeye mwenyewe maneno hayo kwa kusema..

“Ndipo Yesu akawaambia, Ninyi nyote mtachukizwa kwa ajili yangu usiku huu kwa kuwa imeandikwa, Nitampiga mchungaji, na kondoo wa kundi watatawanyika”.

Na kweli tunaona baada ya Yesu kukamatwa mwanafunzi wake wote wakamkimbia.

Kama mstari wa nane unavyosema mafungu mawili yatakatiliwa mbali, nao watakufa, lakini fungu la tatu litabaki humo.

Ni kuonyesha kwa lugha ya mifano kuwa ni idadi ndogo tu ya wanafunzi ambao hawakumuacha kabisa kabisa, mfano wa “theluthi moja”, lakini theluthi mbili zote zilirejea nyuma moja kwa moja. Na ndio maana utaona siku ile ya pentekoste ni watu 120 tu waliokuwepo pale kuingojea ahadi ya roho. Lakini yale maelfu ya makutano yaliyokuwa yakimfuata yalitawanyika.

Lakini katika mstari wa 9, anasema;

“Nami nitalileta fungu lile la tatu na kulipitisha kati ya moto, nami nitawasafisha kama fedha isafishwavyo, nami nitawajaribu kama dhahabu ijaribiwavyo; wataliitia jina langu, nami nitawasikia; mimi nitasema, Watu hawa ndio wangu; nao watasema, BWANA ndiye Mungu wangu.”

na hao ndio waliopitishwa katika moto, wakabatizwa na Roho, wakawa vyombo vikamilifu vimfaavyo Mungu kwa kazi ya uvuvi.

Lakini adui hakujua ulikuwa ni mpango wa Mungu iwe vile kwamba mchungaji afe, ili wokovu mkuu zaidi ya ule wa kwanza uje kwa kupitia kifo chake.Angelijua hilo hata asingedhubutu kumgusa.

Ndio hapo shetani hakuamini alipoona wale wachache waliojazwa Roho, wakivuta maelfu kwa mamilioni ya watu  kwa kipindi kifupi mpaka dunia nzima ikawa imepinduliwa. Shetani hakujua misheni ya mchungaji ilikuwa ni kuingia ndani ya kondoo, sio kuwachunga tena kwa nje, kama hapo mwanzo.

Je nini tunajifunza?

Je! Wewe ni kundi lipi? Lile la tatu, au yale mawili ya kwanza. Ambayo yanapoona mtikisiko kidogo tu wa kimaisha hurudi nyuma, yanapoona kuyumba kidogo tu kwa kanisa hutoroka, yanapoona kutetereka kidogo kwa kiongozi wao yanarudi Misri? Kumbuka ni kusudi la Kristo wote tupitishwe katika moto, ili tuimarishwe tufae kwa ajili ya kazi njema ya utumishi wake.

Aliwapitisha wana wa Israeli jangwani, ili kuwaimarisha kabla ya kwenda kuwaangusha maadui zao kule Kaanani. Aliwapitishwa mitume wako, kwanini na wewe usipitishwe?

Vivyo hivyo ikiwa wewe ni mwana wa Mungu, ambaye utapenda Bwana akutumie, basi liweke kichwani kwamba kuna mahali fulani utapitishwa ili kuimarishwa, huo ndio ubatizo wa Moto ulio wa Roho Mtakatifu. Wakati huo usimwache Bwana, kuwa fungu la tatu.

Bwana akubariki.

Washirikishe na wengine habari hizi njema kwa kushea

Ikiwa utapenda kupata msaada wa kumpokea Yesu maishani mwako bure, Basi wasiliana nasi kwa namba uzionazo chini ya makala hii.

Pia kwa kupokea mafundisho ya kila siku kwa njia ya WHATSAPP, jiunge na channel yetu kwa kupofya link hii >> https://whatsapp.com/channel/0029VaBVhuA3WHTbKoz8jx10

Kwa mawasiliano: +255789001312 au +255693036618

Bwana akubariki.

Mafundisho mengine:

KWANINI KRISTO AFE?

Tofauti kati ya zaka na sadaka ni ipi?

(Opens in a new browser tab)MWANAMKE ULIYEKOMAA KI-UMRI, ITAMBUE HUDUMA YAKO.(Opens in a new browser tab)

AMELAANIWA AANGIKWAYE MSALABANI.

Rudi Nyumbani

Print this post

Agano la Chumvi ni nini? (2Nyakati 13:5)

Swali: Agano la chumvi kama tunavyolisoma katika 2Nyakati 13:5 ni agano la namna gani?


Jibu: Turejee..

2Nyakati 13:5 “Je! Haikuwapasa kujua ya kwamba Bwana, Mungu wa Israeli, alimpa Daudi ufalme juu ya Israeli milele, yeye na wanawe kwa AGANO LA CHUMVI”

Neno hili “Agano la Chumvi” limeonekana mara tatu (3) katika biblia.. sehemu ya kwanza ni hii tunayoisoma ya 2Nyakati 13:5, na nyingine ni katika Hesabu 18:19, pamoja na Walawi 2:13.

Sasa swali nini maana ya Agano la Chumvi?

Nyakati za zamani na hata sasa katika baadhi ya maeneo na baadhi ya jamii, mbali na matumizi ya chumvi katika kuongeza ladha ya chakula, lakini pia chumvi ilitumika na inatumika kama kiungo cha kuhifadhia chakula ili kiweze kudumu kwa muda mrefu bila kuharibika.

Zamani hakukuwa na friji kama zilizopo leo, hivyo kitu pekee kilichokuwa kinatumika kuhifadhia vyakula ambavyo bado havijapikwa (kibichi/kikavu) kilikuwa ni CHUMVI.

Kwahiyo Chumvi, tunaweza kusema inalo AGANO BORA la kuhifadhi kitu kwa muda mrefu pasipo kuharibika kuliko kitu kingine chochote (Ni kiungo cha uhakika kinachodumisha kitu kwa muda mrefu).

Ndio maana utaona sadaka zote katika agano la kale, ziwe za Unga, au za wanyama ziliwekwa chumvi, kuwakilisha uthabiti wa agano la Mungu.

Walawi 2:13 “Tena, kila toleo la sadaka yako ya unga UTALITIA CHUMVI; wala usiiache sadaka yako ya unga kupungukiwa na chumvi ya agano la Mungu wako; utatoa chumvi pamoja na matoleo yako yote”.

Ezekieli 43:22 “Na siku ya pili utamtoa beberu mkamilifu awe sadaka ya dhambi; nao wataisafisha madhabahu, kama walivyoisafisha kwa ng’ombe huyo.

23 Utakapokwisha kuitakasa, utatoa ng’ombe mume mchanga mkamilifu, na kondoo mume wa kundini mkamilifu.

24 Nawe utawaleta karibu mbele za Bwana, na MAKUHANI WATAMWAGA CHUMVI JUU YAO, nao watawatoa wawe sadaka za kuteketezwa kwa Bwana”.

Hivyo kitu kilichotiwa Chumvi maana yake kinadumu muda mrefu, na kilichodumu muda mrefu maana yake kimetiwa chumvi nyingi… ndio maana upo usemi unaowatambulisha wakongwe kama “WATU WALIOKULA CHUMVI NYINGI”.. Na usemi huu pia upo katika biblia, kuwakilisha kuwa Wakongwe ni watu wenye chumvi mwilini.

Ezra 4:11 “Hii ndiyo nakili ya waraka waliyompelekea mfalme Artashasta;watumishi wako,watu walio ng`ambo ya mto wakadhalika.

12 Ijulikane kwa mfalme ya kuwa Wayahudi, waliokwea kutoka kwako, wamefika kwetu Yerusalemu; nao wanaujenga ule mji mwasi, mbaya; wamemaliza kuta zake, na kuitengeneza misingi yake.

13 Basi, ijulikane kwa mfalme, ya kuwa mji huu ukijengwa, na kuta zake zikimalizika, hawatatoa kodi, wala ada, wala ushuru, na mwisho wake wafalme watapata hasara.

14 Na sisi, KWA KUWA TUNAKULA CHUMVI YA NYUMBA YA MFALME, wala si wajibu wetu kumwona mfalme akivunjiwa heshima, basi tumetuma watu na kumwarifu mfalme”.

Hivyo tukirudi katika mstari huo wa 2Nyakati 13:5 unaosema “Je! Haikuwapasa kujua ya kwamba Bwana, Mungu wa Israeli, alimpa Daudi ufalme juu ya Israeli milele, yeye na wanawe kwa AGANO LA CHUMVI”..

Maana yake ni kwamba Agano Mungu aliloingia na Daudi la kumpatia Ufalme, basi ni Agano thabiti lenye kudumu muda mrefu (milele) lisilo haribika kama tu vile chumvi itiwavyo katika vyakula na kukidumisha chakula hicho.

Na sisi tunapomwamini Bwana YESU na kutubu dhambi kwa kumaanisha kuziacha, basi TUNATIWA CHUMVI katika roho (ambayo inatufanya tudumu milele katika ahadi za Mungu, na kuwa na uzima wa milele).

Na tunatiwaje Chumvi ili tuweze kupata uzima wa milele?

JIBU, “TUNATIWA CHUMVI KWA MOTO”.

Marko 9:49 “Kwa sababu kila mtu atatiwa chumvi kwa moto”.

Moto unaozungumziwa hapo ni moto wa Roho Mtakatifu (soma Mathayo 3:11 na Matendo 2:3) ambao ukishuka ndani ya mtu unachoma kila kitu cha kidunia, na kusafisha kama vile chuma kisafishwavyo katika moto, (moto huo unamtenga mtu na vile vitu vilivyoshikamana na maisha yake) Ambapo wakati mwingine unaweza kuleta maumivu, kwasababu unaondoa vile viungo vyote vinavyomkosesha mtu.

Ambapo baada ya hapo mtu anakuwa mpya kabisa (kiumbe kipya) na anakuwa ana uzima wa milele ndani yake, kwasababu katika chumvi.. Hilo ndilo Agano la Chumvi kwetu.

Je umetiwa Chumvi?..Kama utamkubali Bwana YESU siku ya leo, basi utatiwa chumvi na Roho Mtakatifu, na utakuwa chumvi ya dunia (Mathayo 5:13) na utakuwa na uhakika wa maisha ya Milele. Hivyo mkaribishe leo maishani mwako kama bado hujafanya hivyo.

Bwana akubariki.

Maran atha!

Washirikishe na wengine habari hizi njema kwa kushea

Ikiwa utapenda kupata msaada wa kumpokea Yesu maishani mwako bure, Basi wasiliana nasi kwa namba uzionazo chini ya makala hii.

Pia kwa kupokea mafundisho ya kila siku kwa njia ya WHATSAPP, jiunge na channel yetu kwa kupofya link hii >> https://whatsapp.com/channel/0029VaBVhuA3WHTbKoz8jx10

Kwa mawasiliano: +255789001312 au +255693036618

Bwana akubariki.

Mafundisho mengine:

Ninyi ni chumvi ya dunia; Andiko hilo lina maana gani?

Bwana alimaanisha nini kusema “kila mtu atatiwa chumvi kwa moto;

TUSIPOUTHAMINI WOKOVU TUTAPATAJE KUPONA?

Siri za Mungu ni zipi? (1Wakorintho 4:1)

JINSI NEEMA YA MUNGU ILIVYOKUWA KUBWA KWA MKE WA LUTU.

Rudi Nyumbani

Print this post

Msikwao ni mtu gani Na nini tunajifunza katika neno hilo? (Zaburi 69:8).

Jibu: Turejee..

Zaburi 69:8 “Nimekuwa mgeni kwa ndugu zangu, Na msikwao kwa wana wa mama yangu”.

Msikwao ni Kiswahili cha “Mgeni aliyetoka nchi nyingine”… Mtu aliyetoka Taifa lingine na kuingia katika Taifa lisilo lake ndio anayeitwa “Msikwao”.

Hivyo katika hilo andiko, aliposema nimekuwa Msikwao kwa wana wa mama yangu, maana yake amekuwa kama mgeni asiye wa nchi ile mbele ya ndugu zake (wana wa mamaye).

Maneno hayo Daudi aliyaandika kumhusu yeye, lakini pia yalikuwa ni unabii wa maisha ya Bwana YESU KRISTO. Ukisoma Zaburi nyingi za Daudi zilikuwa ni unabii wa maisha ya BWANA YESU, Kwa mfano Zaburi ya 22 ule mstari wa kwanza unasema…

Zaburi 22:1 “Mungu wangu, Mungu wangu, Mbona umeniacha? Mbona U mbali na wokovu wangu, Na maneno ya kuugua kwangu?”

Maneno hayo utayaona Bwana YESU anayataja alipokuwa pale msalabani (soma Mathayo 27:46).

Vile vile unabii wa Yuda kumsaliti Bwana YESU, umeandikwa katika Zaburi 41:9..

Zaburi 41:9 “Msiri wangu tena niliyemtumaini, Aliyekula chakula changu, Ameniinulia kisigino chake.”

Na Bwana YESU anakuja kunukuu maneno hayo katika Yohana 13:18…

Yohana 13:18 “Sisemi habari za ninyi nyote; nawajua wale niliowachagua; lakini andiko lipate kutimizwa, Aliyekula chakula changu Ameniinulia kisigino chake”

Sasa tukirejea katika Zaburi hiyo ya 69, ilikuwa inaelezea maisha ya BWANA YESU KRISTO, kwamba kuna wakati ataonekana mbele ya ndugu zake kama mtu aliyetoka nchi ya mbali, maana yake hata ndugu zake watamkataa.. (na ndugu zake wa kwanza ni Taifa la Israeli, na wa pili ni ndugu zake wa damu).

Utauliza ni wakati gani ndugu zake walimwona kama mtu wa ajabu asiye wa kwao (msikwao)?..

Marko 3:21 “Jamaa zake walipopata habari wakatoka kwenda kumkamata; maana walisema, Amerukwa na akili”.

Soma pia Yohana 7:5.

Hivyo Zaburi hiyo ya 69 ni unabii wa maisha ya Bwana YESU asilimia zote… Na tunazidi kulithibitisha hilo katika mstari unaofuata wa 9, ambao tunaona baadaye Bwana YESU anakuja kuurejea..

Zaburi 69:8 “Nimekuwa mgeni kwa ndugu zangu, Na msikwao kwa wana wa mama yangu.

9 MAANA WIVU WA NYUMBA YAKO UMENILA, Na laumu zao wanaokulaumu zimenipata”.

Utaona hapo aliposema “Wivu wa nyumba yako umenila”.. panakuja kujifunua katika Yohana 2:16-17.

Yohana 2:1 “Akawaambia wale waliokuwa wakiuza njiwa, Yaondoeni haya; msiifanye nyumba ya Baba yangu kuwa nyumba ya biashara.

17  Wanafunzi wake wakakumbuka ya kuwa imeandikwa, WIVU WA NYUMBA YAKO UTANILA.”

Ni nini tunajifunza?..

Kikubwa tunachojifunza ni UNABII uliopo katika kitabu cha Zaburi, kwamba kumbe sehemu kubwa ya kitabu hiko ni unabii wa maisha ya BWANA YESU, ili kutumiza yale maneno yake aliyoyasema katika Luka 24:44. 

Luka 24:44  “Kisha akawaambia, Hayo ndiyo maneno yangu niliyowaambia nilipokuwa nikali pamoja nanyi, ya kwamba ni lazima yatimizwe yote niliyoandikiwa katika Torati ya Musa, na katika Manabii NA ZABURI”.

Hivyo tukisoma kitabu hiko kwa uongozo wa ROHO MTAKATIFU, Tutaona mambo mengi sana yamhusuyo YESU.

Lakini pia mambo mengi yaliyoandikwa katika kitabu hiko yanatuhusu pia sisi, kwani Kristo akiwa ndani yetu nasi tunafanana na yeye, na hivyo sehemu ya maandiko hayo pia yanatimia juu ya maisha yetu..

Maana yake ni kwamba kama KRISTO alionekana Msikwao mbele ya ndugu zake kwasababu anafanya mapenzi ya Baba wa mbinguni, hali kadhalika na sisi tutakutana na vipindi kama hivyo tukiwa katika kuyafanya mapenzi ya Mungu, hivyo endapo yakitokea hayo hatuna budi kusimama na kujitia moyo, kwasababu tayari yalishatabiriwa.

Yohana 16:32 “Tazama, saa yaja, naam, imekwisha kuja, ambapo mtatawanyika kila mmoja kwao kwao, na kuniacha mimi peke yangu; walakini mimi si peke yangu, kwa kuwa Baba yupo pamoja nami.

33  Hayo nimewaambieni mpate kuwa na amani ndani yangu. Ulimwenguni mnayo dhiki; LAKINI JIPENI MOYO; MIMI NIMEUSHINDA ULIMWENGU”.

BWANA YESU AKUBARIKI.

KUMBUKA KUSOMA NENO LA MUNGU KILA SIKU!!!!

Washirikishe na wengine habari hizi njema kwa kushea

Ikiwa utapenda kupata msaada wa kumpokea Yesu maishani mwako bure, Basi wasiliana nasi kwa namba uzionazo chini ya makala hii.

Pia kwa kupokea mafundisho ya kila siku kwa njia ya WHATSAPP, jiunge na channel yetu kwa kupofya link hii >> https://whatsapp.com/channel/0029VaBVhuA3WHTbKoz8jx10

Kwa mawasiliano: +255789001312 au +255693036618

Bwana akubariki.

Mafundisho mengine:

KWANINI DAUDI ALIKUWA NI MTU ALIYEUPENDEZA MOYO WA MUNGU?

MWIMBIE BWANA ZABURI KATIKA NYAKATI ZA FURAHA.

Mwandishi wa kitabu cha Zaburi ni nani?

NENO LA MUNGU NI UFUNUO MKAMILIFU.

NGUVU YA UPENDO WA KRISTO.

Rudi Nyumbani

Print this post

Je Adamu na Hawa waliokoka?

Biblia haielezi moja kwa moja kama waliokoka, au hawakuokoka, kwasababu Neno “Kuokoka”, tunalisoma kwenye agano jipya, likimaanisha kukombolewa kutoka katika uharibifu wa hukumu ya Mungu kwasababu ya dhambi kwa kupitia kifo cha Yesu Kristo mwokozi wetu.

Lakini tunaweza kufahamu watu wa agano la kale waliokolewa, kwa kutii kwao ile ahadi ya Mungu aliyoahidi ya kumletea mkombozi duniani baadaye, yaani Yesu Kristo. Hivyo wote waliotembea katika mpango huo wa Mungu, waliokoka. Na mpango wa Mungu wote ulimuakisi Yesu Kristo.

Kwamfano ile safina aliyoijenga Nuhu ilikuwa ni Yesu Kristo, Ule mwamba walionywea wana wa Israeli jangwani ulikuwa ni Kristo, wote waliokataa kuunywea walimkataa Kristo, (1Wakorintho 10:4), Yule nyoka wa shamba alikuwa ni Kristo waliokataa kuitazama, walimkataa Kristo(Yohana 3:14), zile mbao mbili (Amri 10), zilikuwa ni Kristo waliozikataa kuzitii, walimkataa Kristo.  Yule melkizedeki aliyemtokea Ibrahimu alikuwa ni Kristo, wale malaika wawili walioshuka sodoma kuhubiri alikuwa ni Kristo ndani yao, waliowatii walimtii Kristo. Wale wanyama waliochinjwa na damu zao kunyunyizwa katika madhabahu kwa ajili ya upatanisho wa  dhambi za watu walimfunua Kristo, wote waliotii,. Walimtii Kristo ajaye.

Hivyo kila mahali walipotembea, Kristo alijidhirisha kwao kwa lugha ya maumbo na vivuli, na mifano, na maagizo, ili wamwamini yeye. Kwahiyo wote waliomtii katika nyakati zote, waliingizwa katika jopo la watu ambao Kristo atakapofunuliwa basi wataokolewa. Ndio maana baada ya Yesu kufufuka katika wafu miili mingi ya watakatifu ikatoka makaburini, wakahamishiwa peponi, rahani mwa Yesu, kwani hapo kabla watakatifu wote waliokufa walikuwa chini makaburini.

Hivyo kwa msingi huo, tutachunguza kama Adamu na Hawa walimtii Kristo au la, baada ya anguko. Biblia inatuonyesha walipojiona wapo uchi, hawakuendelea kufurahia anguko lile, bali walijificha, kuonyesha majuto ya dhambi zao, ndipo Mungu akamchinja mnyama Yule, akawavika vazi lake. Sasa Mnyama Yule alimfunua Kristo,(Mwanzo 3:21) lakini kama wangekataa basi wasingeweza kuokoka, ndio maana Yesu alisema..pia maneno haya haya kwetu sisi wa siku za mwisho, tuvikwe vazi lake, ili aibu yetu iondoke.

Ufunuo 3:18  Nakupa shauri, ununue kwangu dhahabu iliyosafishwa kwa moto, upate kuwa tajiri, na MAVAZI MEUPE UPATE KUVAA, AIBU YA UCHI WAKO ISIONEKANE, na dawa ya macho ya kujipaka macho yako, upate kuona

Halikadhali, biblia inataja uzao wa mwanamke kwamba utauponda kichwa uzao wa nyoka. Kuashiria kuwa Hawa hakuwa mwana wa Adui (Mwanzo 3:15). Bali ni zao mbili tofauti kabisa.

Lakini pia watoto wao, mpaka sethi, tunaona walifundishwa njia ya kumtolea Bwana sadaka, na sadaka zile zilikuwa ni Kristo katika maumbo. Ni wazi kuwa wasingeweza kufanya vile kama hawakupokea au kuona kwa wazazi wao.

Na sababu nyingine ya mwisho, Kristo anatajwa kama mwana wa Adamu, hata katika vizazi vile vilivyoorodheshwa anatajwa kama “wa Adamu” (Luka 3:23-38). Asingeitwa hivyo wa Adamu  kama angekuwa ni wa ibilisi,. Mungu hawezi anza na mguu usio sahihi. Atashinda mwanzo, vilevile atashinda mwisho.

Kwa hitimisho ni kwamba Adamu na Hawa hawakupotea, bali walimwamini Kristo, baada ya anguko.

Bwana akubariki.

Washirikishe na wengine habari hizi njema kwa kushea

Ikiwa utapenda kupata msaada wa kumpokea Yesu maishani mwako bure, Basi wasiliana nasi kwa namba uzionazo chini ya makala hii.

Pia kwa kupokea mafundisho ya kila siku kwa njia ya WHATSAPP, jiunge na channel yetu kwa kupofya link hii >> https://whatsapp.com/channel/0029VaBVhuA3WHTbKoz8jx10

Kwa mawasiliano: +255789001312 au +255693036618

Bwana akubariki.

Mafundisho mengine:

KWANINI YESU NI ADAMU WA PILI?(Opens in a new browser tab)

Biblia inaposema “Wote tumetenda dhambi” si inamaanisha hakuna mtakatifu duniani?(Opens in a new browser tab)

Nini Maana ya Adamu?

Kwanini Yesu Kristo ni mwana wa Adamu?(Opens in a new browser tab)(Opens in a new browser tab)

Rudi Nyumbani

Print this post

MAMBO SITA, AMBAYO MUNGU HUTUMIA KUONDOA UOVU NDANI YA MTU.

Nakusalimu katika jina kuu la mwokozi wetu Yesu Kristo, karibu katika kujifunza Neno la Mungu. Leo tutaona mambo Makuu sita (6), ambayo Mungu anatumia kuondoa uovu ndani ya mtu, na kumfanya awe mtakatifu kabisa kama yeye alivyo. Ikiwa wewe umemfuata Kristo basi tarajia mambo haya matano atayatumia katika maisha yako, kukukamilisha.

  1. Damu
  2. Maji
  3. Moto
  4. Fimbo
  5. Pepeto
  6. Dawa

Tukianza na

DAMU:

Kumbuka sisi sote tulizaliwa na deni la dhambi. Hivyo tulistahili hukumu ya mauti, (Warumi 6:23), Lakini deni hilo lilikuja kulipwa na Bwana wetu Yesu kwa kifo chake pale msalabani (Warumi 5:8). Kumwagika kwa damu yake, sote tumepokea “msamaha wa dhambi” bure kwa neema. Hakuna mwanadamu yoyote anayeweza kukubaliwa na Mungu, kwa uweza wake mwenyewe. Kwahiyo damu ya Yesu imekuwa hatua ya kwanza ya sisi kukubaliwa na Mungu.

Sasa tunaweza kupokea msamaha kweli, tukasemehewa, lakini dhambi bado ikawepo ndani yetu. Na hilo sio kusudu la Mungu atusemehe tu, halafu atuache tuendelee kuwa watumwa wa dhambi ndani kwa ndani. Si lengo la Mungu, hata mtu mwenye upendo wa dhati wa Yule aliyekosewa naye, anapoona amemsamehe, huwa hamwachi tena kesho arudie kosa lile lile ili, amsamehe, hapana, bali humwonyesha njia ya kuepuka makosa ili yeye mwenyewe aweze kusimama kwa ujasiri mbele zake. Na ndivyo ilivyo kwa Mungu mara baada ya kupokea msamaha wa dhambi, huyo mtu anaanza hatua ya utakaso wa Mungu ambao sasa hufanywa na Roho Mtakatifu aliyeingia ndani yake, Ndio hapo inakuja hatua ya pili,

NENO:

Biblia inasema Neno ni kama maji, ambayo yanasafisha.

Waefeso 5:26  ili makusudi alitakase na kulisafisha kwa maji katika neno; 27  apate kujiletea Kanisa tukufu, lisilo na ila wala kunyanzi wala lo lote kama hayo; bali liwe takatifu lisilo na mawaa.

Umeona, Kristo hulisafisha kanisa lake, kwa Neno, ndio maana wewe kama mtu uliyempokea Yesu, Ni lazima uwe na juhudu nyingi sana za kusoma Neno la Mungu kila siku, usikie maonyo, fundisho, agizo,  njia, (2Timotheo 3:16), Na kwa jinsi unavyojifunza sana, ndivyo unavyosafishwa moyo wako na roho yako, hatimaye unaanza kujiona mtu ambaye huna hatia ndani yako. Na hapo ndipo unapojikuta unaacha baadhi ya mambo uliyokuwa unafanya huko nyuma. Kumbuka biblia uliyonayo sio kitambulisho cha mkristo au pambo la mkoba, bali ni maji hayo ya kukusafisha, hivyo oga kila siku, uwe msafi. Kwasababu usipofanya hivyo utakuwa mchafu tu sikuzote.

MOTO:

Kwa kawaida sio kila uchafu hutoka kwa maji, mwingine huitaji moto ili kuundoa. Kwamfano ukiupata mwamba wenye dhahabu ndani yake ukipitisha maji huwezi toa uchafu uliogandamana nao,hivyo wale wafuaji, wanaupitisha kwenye moto, kisha unayeyuka na baada ya hapo uchafu na dhahabu hujitenga kisha wanaikusanya dhahabu. Ndivyo ilivyo na Mungu kwa watoto wake. Upo moto ambao wewe kama mwana wa Mungu ni lazima tu utapitishwa hata iweje, kuondoa mambo sugu yaliyogandamana na wewe yasiyoweza kutoka kwa Neno tu bali kwa hatua ya kimaisha, ndio huo unaoitwa “ubatizo wa moto”. Mfano wa huu ndio ule uliompata mfalme Nebukadreza (Danieli 4), kukaa miaka saba maporini kula majani ili tu aondolewe kiburi ndani yake. Ni aina Fulani ya maisha ambayo kwako yatakuwa kama moto, lakini mwisho wake hukuletea faida ya roho yako.

1Petro 1:6  Mnafurahi sana wakati huo, ijapokuwa sasa kwa kitambo kidogo, ikiwa ni lazima, mmehuzunishwa kwa majaribu ya namna mbalimbali;7  ili kwamba kujaribiwa kwa imani yenu, ambayo ina thamani kuu kuliko dhahabu ipoteayo, ijapokuwa hiyo hujaribiwa kwa moto, kuonekane kuwa kwenye sifa na utukufu na heshima, katika kufunuliwa kwake Yesu Kristo.

FIMBO:

Zipo tabia nyingine ambazo Mungu anaona mwanawe anakuwa nazo kwa ujinga tu, hivyo, ili kuundoa ujinga huo, haihitaji maji wala moto, bali kiboko. Anapoona unafanya jambo Fulani kwa makusudi na alishakukataza hapo awali fahamu pia kiboko kitapita juu yako.

Waebrania 12:6  Maana yeye ambaye Bwana ampenda, humrudi, Naye humpiga kila mwana amkubaliye.

7  Ni kwa ajili ya kurudiwa mwastahimili; Mungu awatendea kama wana; maana ni mwana yupi asiyerudiwa na babaye?

8  Basi kama mkiwa hamna kurudiwa, ambako ni fungu la wote, ndipo mmekuwa wana wa haramu ninyi, wala si wana wa halali. 9  Na pamoja na hayo tulikuwa na baba zetu wa mwili walioturudi, nasi tukawastahi; basi si afadhali sana kujitia chini ya Baba wa roho zetu na kuishi?

10  Maana ni hakika, hao kwa siku chache waliturudi kama walivyoona vema wenyewe; bali yeye kwa faida yetu, ili tuushiriki utakatifu wake.

Biblia inasema pia..

Mithali 22:15 Ujinga umefungwa ndani ya moyo wa mtoto; Lakini fimbo ya adhabu itaufukuzia mbali.

PEPETO:

Yohana mbatizaji kwa uvuvio wa Roho aliandika maneno haya kuhusu  Bwana Yesu..

Mathayo 3:11  Kweli mimi nawabatiza kwa maji kwa ajili ya toba; bali yeye ajaye nyuma yangu ana nguvu kuliko mimi, wala sistahili hata kuvichukua viatu vyake; yeye atawabatiza kwa Roho Mtakatifu na kwa moto.

12  Ambaye pepeto lake li mkononi mwake, naye atausafisha sana uwanda wake; na kuikusanya ngano yake ghalani, bali makapi atayateketeza kwa moto usiozimika.

Yesu akija kwako, fahamu kuwa mkononi ameshika pepeto pia, na wewe utawekwa juu yake, Anajua kabisa ulipo wewe makapi pia yapo, uliyotoka nayo huko shambani (ulimwenguni), hivyo ili kukutenga nayo, ataanza kukupepeta, kama vile ngano, utarushwa juu, utashushwa chini, utarushwa juu utashushwa chini, huwezi kuachwa utulie, lengo ni kuhakikisha makapi yote yanapeperushwa na upepo, iwe ni watu, vitu, utaona tu unapelekwa mbele, unarudishwa nyuma..baadaye akishaona ni ngano tu imebakia chini, hapo ndipo anapokuacha, unaanza kuona ushwari. Hii ilimkuta Ibrahimu, Bwana anamtoa Uru, anampeleka kaanani, mara anakimbilia Misri, mara anarudisha, lakini baadaye Mungu alimpa pumziko, baada ya kuona wote waliokuwa wameshikamana naye hawapo naye.

Usishangae kutokuwa na utulivu katika nyakati fulani za maisha yako wokovu, wakati Fulani unafanikiwa, halafu unarudi chini, wakati Fulani unapata amani kotekote, gafla inaondoka, unapata, ghafla tena unapoteza, tulia tu, kuwa na amani ndani ya Kristo, utakuwa tu, imara, wala hiyo misukosuko haitakuwepo tena, ni kwanini iwe hivyo? Ni kwasababu makapi yanapeperushwa na upepo.

DAWA:

Kaa ukifahamu Yesu anajulikana pia kama tabibu,(Marko 2:17) na anajua maovu mengine unayoyafanya yanatokana na magonjwa na majeraha ya rohoni, anajua hali yako ilivyo hivyo anachokifanya ni kukutibu yeye mwenyewe, ndio hapo unashangaa tu mwingine anatokwa na mapepo yaliyokuwa yanamsumbua na kumpelekea kutenda dhambi mwingine anapona udhaifu fulani, uliokuwa unamfanya amkosee Mungu, mwingine anapokea faraja, amani, utulivu usio wa kawaida, anashangaa kuona tofauti kubwa  ya sasa na hapo kabla. Hili nalo mtu aliyempokea Kristo ataliona kwenye maisha yake. Na atimaye anakuwa mwema yeye tu mwenyewe, asukumwi tena na presha ya dhambi fulani. Kwasababu tabibu mkuu ameshamponya, ambaye akikuweka huru, unakuwa huru kwelikweli.

Ufunuo 3:18

Nakupa shauri, ununue kwangu dhahabu iliyosafishwa kwa moto, upate kuwa tajiri, na mavazi meupe upate kuvaa, aibu ya uchi wako isionekane, na DAWA ya macho ya kujipaka macho yako, upate kuona.

Hivyo, wewe kama mwana wa Mungu, tambua yote hayo yatapita katika sehemu Fulani ya maisha yako. Usidhani kusafishwa tu na damu ya Yesu ndio basi, utatakaswa na hiyo ni katika maisha yako yote. Haiwezekani mtu aliyeokoka ambaye amepokea Roho maisha yake yote awe Yule Yule wa zamani, hizo sio kanuni za wokovu, wala sio kusudi la Mungu. Ukubali utakaso, au usiwe mkristo kabisa. Kwasababu hivi viwili huenda sambamba wala haviwezi kutenganishwa. Huo ndio upendo wa Mungu.

Utukufu na heshima ni vyake  milele na milele.

Bwana akubariki.

Shalom.

Washirikishe na wengine habari hizi njema kwa kushea

Ikiwa utapenda kupata msaada wa kumpokea Yesu maishani mwako bure, Basi wasiliana nasi kwa namba uzionazo chini ya makala hii.

Pia kwa kupokea mafundisho ya kila siku kwa njia ya WHATSAPP, jiunge na channel yetu kwa kupofya link hii >> hhttps://whatsapp.com/channel/0029VaBVhuA3WHTbKoz8jx10

Kwa mawasiliano: +255789001312 au +255693036618

Bwana akubariki.

Mafundisho mengine:

MADHARA YA KUKOSA MAJI YA UZIMA BAADA YA KIFO.

(Opens in a new browser tab)UTAKASO NI SEHEMU YA MAISHA YA MKRISTO YA KILA SIKU.

Ipi tofuati kati ya UTAKATIFU na UKAMILIFU?

Rudi Nyumbani

Print this post

Maana ya Mithali 21:30 Hapana hekima, wala ufahamu, Wala shauri,  juu ya Bwana.

SWALI: Nini maana ya Mithali 21:30 Hapana hekima, wala ufahamu, Wala shauri,  juu ya Bwana ?


JIBU: Mstari huo unaweza ukasemwa hivi; “Hapana hekima, wala ufahamu, wala shauri linaloweza kufanikiwa/kusimama kinyume na Mungu”.

Ikiwa na maana iwe ni mwanadamu au malaika, atumie uwezo wake wote, kufanya jambo la hila kinyume na yeye haliwezi kufichika kwasababu yeye ni mkuu zaidi ya vyote. Mpango wa shetani kuliharibu kanisa huawezi kufanikiwa hata azidishe kufanya kazi mara elfu zaidi ya mwanzo hilo haliwezekani kama lilivyoshindikana mbinguni.

Mambo yote yanayotokea hayafiki kwake ghafla tu bila hodi, kama ilivyo kwetu sisi wanadamu. Elimu ya darasani haiwezi pindua ukweli wake wa uungu, wajaposema mwanadamu ametokana na nyani, mwishoni wanarudia kule kule kwenye ukweli wa uumbaji wa kiungu, kwasababu atabakia kusimama kuwa Mungu wa daima, na ataabudiwa vizazi vyote haijalishi dunia itaelimika kiasi gani.

Mungu Anajua mawazo yetu yote tokea mbali, wewe kama mwanadamu huwezi mficha dhambi zako, ukajifanya  mbele zake umesahau, au ulikuwa hujui, hata utumie hekima nyingi kiasi gani kuficha ukweli bado anatambua nia ya mioyo yetu.

Anasema;

Zaburi 50:17 Maana wewe umechukia maonyo, Na kuyatupa maneno yangu nyuma yako.  18 Ulipomwona mwivi ulikuwa radhi naye, Ukashirikiana na wazinzi.

19 Umekiachia kinywa chako kinene mabaya, Na ulimi wako watunga hila.  20 Umekaa na kumsengenya ndugu yako, Na mwana wa mama yako umemsingizia.

21 NDIVYO ULIVYOFANYA, NAMI NIKANYAMAZA; UKADHANI YA KUWA MIMI NI KAMA WEWE. Walakini nitakukemea; Nitayapanga hayo mbele ya macho yako.

22 Yafahamuni hayo, Ninyi mnaomsahau Mungu, Nisije nikawararueni, Asipatikane mwenye kuwaponya.

Pale tunapomwona Mungu ni kama sisi ndio unakuwa mwanzo wa kuto-mhofu  yeye. Unapokuwa na udhuru wa kuifanya kazi yake halafu unasingizia sina muda, lakini una muda wa kufanya mambo yako, ukidhani yeye hajui nia yako ya ndani, unajidanganya mwenyewe. Unapoepuka maombi, kwa kisingizio umechoka, na bado unataka Mungu akuhudumie, fahamu Mungu anakuelewa vizuri sana, atakuonyesha ambao wanachoka zaidi yako, lakini hawana udhuru. Jambo lolote tulifanyalo, tutambue kwanza kwa Mungu halifichiki.

Kwasababu Hapana hekima, wala ufahamu, wala shauri litakalosimama kinyume cha Mungu

Shalom.

Washirikishe na wengine habari hizi njema kwa kushea

Ikiwa utapenda kupata msaada wa kumpokea Yesu maishani mwako bure, Basi wasiliana nasi kwa namba uzionazo chini ya makala hii.

Pia kwa kupokea mafundisho ya kila siku kwa njia ya WHATSAPP, jiunge na channel yetu kwa kupofya link hii >> https://whatsapp.com/channel/0029VaBVhuA3WHTbKoz8jx10

Kwa mawasiliano: +255789001312 au +255693036618

Bwana akubariki.

Mafundisho mengine:

Nini maana ya Mithali 19:21Mna hila nyingi moyoni mwa mtu; Lakini shauri la Bwana ndilo litakalosimama.(Opens in a new browser tab)

Je shauri la kuipepeleza Kanaani lilitoka kwa wana wa Israeli au kwa BWANA?(Opens in a new browser tab)

Tofauti kati ya Hekima, ufahamu na maarifa, ni ipi?

(Opens in a new browser tab)Maana ya Mithali 11:17 Mwenye rehema huitendea mema nafsi yake(Opens in a new browser tab)

Rudi Nyumbani

Print this post

Maana ya Mithali 21:17 Mtu apendaye anasa atakuwa maskini;

SWALI: Nini maana ya  Mithali 21:17 Mtu apendaye anasa atakuwa maskini; Apendaye mvinyo na mafuta hatakuwa tajiri.


JIBU: Mstari huo unamaana mbili.

Maana ya kwanza ni ya mwilini, ni ukweli watu wanaopenda maisha ya anasa, mwisho wao huwa ni kutofanikiwa. Kwasababu kile wanachokipata ambacho kingepaswa kiwekwe akiba kwa wakati wa baadaye au kiwekezwe kizalishe zaidi, wao hutumia chote katika starehe mfano wa pombe, uasherati, na kununua vitu vya gharama kubwa, lengo tu asionekane amepitwa na wakati, au aonekane wa kisasa.

Hapo anaposema apendaye mvinyo na mafuta, hayo mafuta yanayozungumziwa hapo ni marashi ya gharama ambayo zamani waliokuwa wananunua ni matajiri. Ni sawa na leo labda mwajiriwa analipwa mshahara wa laki tatu (3) kwa mwezi, halafu anakwenda kununua perfume (marashi), ya  laki 2, ili tu aonekane wa kisasa, hiyo ni anasa, na mwisho wake ni umaskini.

Anasa ni tunda la majivuno, na kukosa adabu. Hivyo biblia inamfundisha mwanadamu yoyote kuwa, anasa ni kinyume cha mafanikio.

Lakini pia rohoni, anasa ni zao la ufukara wa ki-Mungu. Mtu wa anasa, hutumia muda wake vibaya, kwasababu nyakati zake za ziada huishia kwenye starehe za kimwili na sio kwenye mambo ki-Mungu.

Bwana alisema;

Luka 8:14  Na zilizoanguka penye miiba ni wale waliosikia, na katika kuenenda kwao husongwa na shughuli na mali, na anasa za maisha haya, wasiivishe lo lote.

Umeona? Anasa husonga mbegu ya Mungu ndani yako.

Katika kizazi cha sasa anasa ni pamoja na kushinda kwenye tv kutazama muvi kila kukicha, ni pamoja na kushinda mitandaoni kufuatilia vipindi vinavyokupa raha za kimwili na kihisia lakini havikujengi rohoni,  ni kuwekeza muda wako katika matanuzi ya mijini na kwenye sherehe-sherehe za kila mara ambazo hazina mpangalio. Muda wote akili yako ipo katika kile kitu wanachosema “ku-party weekend” na marafiki. Ushikapo simu yako, usiku wote ni kuchat, na wale wanaowaita ma-boyfriend na ma-girlfriend. Muda ambao ungepaswa kusoma Neno na kuomba.

Sasa ikiwa wewe umeokoka, na una mwenendo huo wa maisha, usitazamie hapo utazalisha kitu. Utabakia kuwa Yule Yule milele. Biblia inasema ni heri kuona kwa macho kuliko kutangatanga kwa tamaa(Mhubiri 6:9). Sio kila taarifa uifuatilie, sio kila kitu ukitende, viache vingine vikupite, ili upate nafasi ya kuwa karibu na Mungu wako, uwe mtu wa matunda. Komboa wakati.

Shalom..

Washirikishe na wengine habari hizi njema kwa kushea

Ikiwa utapenda kupata msaada wa kumpokea Yesu maishani mwako bure, Basi wasiliana nasi kwa namba uzionazo chini ya makala hii.

Pia kwa kupokea mafundisho ya kila siku kwa njia ya WHATSAPP, jiunge na channel yetu kwa kupofya link hii >> https://whatsapp.com/channel/0029VaBVhuA3WHTbKoz8jx10

Kwa mawasiliano: +255789001312 au +255693036618

Bwana akubariki.

Mafundisho mengine:

Wakidhania kuwa ulevi wakati wa mchana ni anasa.

(Opens in a new browser tab)APENDAYE FEDHA HASHIBI FEDHA.

Heri walio maskini wa roho; Maana ufalme wa mbinguni ni wao.

JINSI MUNGU ATAKAVYOTOA THAWABU ZAKE, NA VIGEZO ATAKAVYOTUMIA. (Sehemu ya 4)(Opens in a new browser tab)(Opens in a new browser tab)(Opens in a new browser tab)

Rudi Nyumbani

Print this post

Ipi tofuati kati ya UTAKATIFU na UKAMILIFU?

Swali: Ipi tofuati kati ya kuwa MTAKATIFU (1Petro 1:15-16) na kuwa MKAMILIFU (Mathayo 5:48)?

Jibu: MTAKATIFU ni Mtu aliyetakaswa, aliye safi, asiye na mawaa na anayefanya matendo mema.. Na biblia inatufundisha tuwe watakatifu kama Baba wa mbinguni alivyo mtakatifu…

1Petro 1:15  “bali kama yeye aliyewaita ALIVYO MTAKATIFU, ninyi nanyi iweni watakatifu katika mwenendo wenu wote;

16  kwa maana imeandikwa, MTAKUWA WATAKATIFU KWA KUWA MIMI NI MTAKATIFU”.

Na tena Mambo ya Walawi 19:2  inarudia jambo hilo hilo..

Walawi 19:2 “Nena na mkutano wote wa wana wa Israeli, uwaambie, Mtakuwa watakatifu; kwa kuwa mimi Bwana, Mungu wenu, ni mtakatifu”.

Lakini MKAMILIFU ni Mtakatifu aliye kamilika….. Wapo Watakatifu waliokamilika na ambao hawajakamilika.

Mtakatifu aliye kamilika ni yule ni anayefanya JAMBO LA ZIADA katika UTAKATIFU WAKE linalomtofautisha na wengine na kufanya afanane na MUNGU … Mfano wa mambo hayo ni kama yale yote Bwana YESU aliyoyataja katika Mathayo 5.

Mathayo 5:43 “Mmesikia kwamba imenenwa, Umpende jirani yako, na, Umchukie adui yako;

44  lakini mimi nawaambia, Wapendeni adui zenu, waombeeni wanaowaudhi,

45  ili mpate kuwa wana wa Baba yenu aliye mbinguni; maana yeye huwaangazia jua lake waovu na wema, huwanyeshea mvua wenye haki na wasio haki.

46  Maana mkiwapenda wanaowapenda ninyi mwapata thawabu gani? Hata watoza ushuru, je! Nao hawafanyi yayo hayo?

47  Tena mkiwaamkia ndugu zenu tu, MNATENDA TENDO GANI LA ZIADA? Hata watu wa mataifa, je! Nao hawafanyi kama hayo?

48  Basi ninyi MTAKUWA WAKAMILIFU, KAMA BABA YENU WA MBINGUNI ALIVYO MKAMILIFU

Kwahiyo na sisi ni Lazima tuutafute UKAMILIFU na si UTAKATIFU TU!.

> “Mtakatifu” anafunga na kuomba kwaajili yake peke yake, lakini “Mkamilifu” anafunga na kuomba kwaajili yake na kwaajili ya wengine,

> “Mtakatifu”  anasoma neno na kuomba basi!…Lakini “Mkamilifu”  anasoma Neno na kuomba na kuwafundisha wengine mambo aliyojifunza, ili nao wabarikiwe kama yeye.

> “Mtakatifu”  anafanya kazi ya Mungu kwa moyo ili akapate thawabu mbinguni, lakini “Mkamilifu”  pamoja na kufikiri thawabu mbinguni lililo kubwa zaidi analolifikiri ni ndugu zake wasiangamie katika moto wa milele (moyo wake unaugua juu ya roho za wengine kupotea).

> “Mtakatifu”  atampa Mungu siku moja katika wiki ya kukusanyika nyumbani kwa Mungu, lakini “Mkamilifu”  atafikiri Zaidi ya siku moja.

> Mtakatifu” atazishika AMRI ZOTE ZA MUNGU, lakini Moyo wake utakuwa pia katika mali…. Lakini “Mkamilifu” Atazishika Amri zote na Moyo wake hautakuwa katika mali kama yule kijana aliyekutana na Bwana YESU.

Mathayo 19:16 “Na tazama, mtu mmoja akamwendea akamwambia, Mwalimu, nitende jambo gani jema, ili nipate uzima wa milele?

17  Akamwambia Kwani kuniuliza habari ya wema? Aliye mwema ni mmoja. Lakini ukitaka kuingia katika uzima, zishike amri.

18  Akamwambia, Zipi? Yesu akasema, Ni hizi, Usiue, Usizini, Usiibe, Usishuhudie uongo,

19  Waheshimu baba yako na mama yako, na, Mpende jirani yako kama nafsi yako.

20  Yule kijana akamwambia, Haya yote nimeyashika; nimepungukiwa na nini tena?

21  Yesu akamwambia, UKITAKA KUWA MKAMILIFU, enenda ukauze ulivyo navyo, uwape maskini, nawe utakuwa na hazina mbinguni; kisha njoo unifuate.

22  Yule kijana alipolisikia neno lile, akaenda zake kwa huzuni; kwa sababu alikuwa na mali nyingi”.

Hivyo hatuna budi kuutafuta UKAMILIFU na sio UTAKATIFU tu peke yake!!.

Biblia inasema Nuhu alikuwa mtu Mkamilifu katika vizazi vyake ndio maana akapona katika ile gharika (Mwanzo 6:9),  Daudi alikuwa mkamilifu ndio maana alipendwa na Mungu zaidi ya wafalme wote (2Samweli 22:24), Ayubu alikuwa mkamilifu ndio maana alimwona Mungu katikati ya majaribu (Ayubu 1:1).

Na hata sisi tukiwa WAKAMILIFU tutamwona Mungu.

Bwana akubariki.

Washirikishe na wengine habari hizi njema kwa kushea

Ikiwa utapenda kupata msaada wa kumpokea Yesu maishani mwako bure, Basi wasiliana nasi kwa namba uzionazo chini ya makala hii.

Pia kwa kupokea mafundisho ya kila siku kwa njia ya WHATSAPP, jiunge na channel yetu kwa kupofya link hii >> https://whatsapp.com/channel/0029VaBVhuA3WHTbKoz8jx10

Kwa mawasiliano: +255789001312 au +255693036618

Bwana akubariki.

Mafundisho mengine:

MADARAKA YA WAKATI MKAMILIFU.

BABA UWASAMEHE

NJIA KUU YA KUINGIA KATIKA ULE MJI.

Nini maana ya Mungu amemfanya mwanadamu mnyofu?

NENO LA MUNGU NI UFUNUO MKAMILIFU.

Rudi Nyumbani

Print this post