IIGE RATIBA YA MUNGU YA WIKI IKUSAIDIE

IIGE RATIBA YA MUNGU YA WIKI IKUSAIDIE

Nakusalimu katika jina kuu sana la Bwana wetu Yesu Kristo, karibu tujifunze maneno ya uzima.

Tunaposoma kile kitabu cha Mwanzo sura ya kwanza , wengi wetu tunachokiona pale ni tendo la uumbaji tu lakini hatuoni mikakati na ratiba alizojipangia Mungu ili kuukamilisha huo mpango wake mzima wa uumbaji.

Walimwengu wanasema, mtu mwenye akili huwa anajifunza kwa waliofanikiwa.. Sasa sisi wanadamu hatuna aliyefanikiwa Zaidi ya Mungu wetu si ndio?. Tunapoziangalia mbingu na nchi tunachokiona ni kazi stadi iliyobuniwa kwa  umakini  sana isiyokuwa na mapungufu au madhaifu yoyote, hivyo na sisi pia kama tunataka tuwe na mafanikio makubwa hatuna budi kujifunza ratiba ya Mungu jinsi alivyoweza kupangilia mambo yake. Mpaka tukakiona hichi tunachokiona sasa hivi.

Sasa katika zile siku 7 za uumbaji, Mungu alizigawanya shughuli zake katika vipengele vikuu vitatu.

Kipengele cha kwanza: Alijikita katika kufanya kazi ya utenganisho

Kipengele cha pili :Kilikuwa ni uumbaji

Na kipengele cha  tatu: Kupumzika.

Tukianza na kipengele cha Kwanza: Kufanya utenganisho.

Ukisoma Mwanzo 1:2 Utaona utenganisho wa kwanza alioufanya Mungu katika siku ya kwanza ulikuwa ni kati ya Nuru na giza.

Mwanzo 1:3 Mungu akasema, Iwe nuru; ikawa nuru.

4 Mungu akaiona nuru, ya kuwa ni njema; Mungu akatenga nuru na giza.

Siku ya pili tena akaendelea na kazi hiyo hiyo.. akayatenga maji ya juu ya chini, na ya chini ya nchi kwa kuweka kitu kinachoitwa anga katikati..

Mwanzo 1:7 Mungu akalifanya anga, akayatenga yale maji yaliyo juu ya anga na yale maji yaliyo chini ya anga; ikawa hivyo.

8 Mungu akaliita lile anga Mbingu. Ikawa jioni ikawa asubuhi, siku ya pili.

Unaona Kama hiyo haitoshi, bado aliendelea hadi siku ya tatu kufanya matenganisho, kati ya maji na ardhi, ili nchi kavi ionekane

Mwanzo1:9 Mungu akasema, Maji yaliyo chini ya mbingu na yakusanyike mahali pamoja, ili pakavu paonekane; ikawa hivyo.

10 Mungu akapaita pale pakavu Nchi; na makusanyiko ya maji akayaita Bahari; Mungu akaona ya kuwa ni vyema.

Na Siku ya Nne pia, akatenganisha, siku na siku, na mwezi na mwezi, na mwaka na mwaka,..kwa kuumba jua na mwezi na nyota..

Soma Mwanzo 1:16-19 utalithibitisha hilo

Sasa mpaka anafikia siku ya nne, alikuwa bado hajaumba mnyama yoyote, ni kazi tu ya utenganisho tukiachilia mbali mimea ambayo iliumbwa siku ya tatu..

Mungu kuanzana na utenganisho ni kutufundisha nini?

Hii ni kutufundisha kuwa, hatupaswi kukimbilia kufanya jambo lolote,kwanza  kama kuna mambo ambayo bado hayajatenganishwa na sisi rohoni. Tutumie nguvu kubwa kutenganisha nuru na giza kwenye wiki yetu, ..Usianze tu wiki yako hivi hivi, bila kuiambia kwanza iwe nuru kwako,kwa kwenda ibadani nyumbani kwa Bwana usianze wiki bila kuomba, hakikisha unayatenga mambo maovu mbali na wewe kwa kadiri uwezavyo. Ndicho Mungu alichokuwa anakifanya katika siku za mwanzo.

Kama kuna mtu umemdhulumu mlipe..kama una madeni ya watu yasawazishe..kama kuna dhambi ulitenda ziungame mbele za Bwana.

Kipengele cha  Pili: Ni uumbaji,

baada ya pale ndipo utaona Mungu anaanza kuumba, samaki , na wanyama wa kila namna wa mwituni na wa kufungwa pamoja na ndege wote angani..na mwisho kabisa akamwuumba na mwanadamu, katika siku ile ya sita.

Hii ni kutufundisha kuwa, mara baada ya kutenganisha mambo yasiyofaa mbali nasi ndipo hapo sasa tuwe na uhakika kuwa kila tunachotia mkono kukifanya, kitakuwa ni chema sana.. Kisichokuwa na mapungufu au kasoro..Kama Mungu alivyoona jinsi uumbaji wake ulivyokuwa vema sana usio na mapungufu yoyote.

Mwanzo 1:31 Mungu akaona kila kitu alichokifanya, na tazama, ni chema sana. Ikawa jioni ikawa asubuhi, siku ya sita.

Kipengele cha Tatu: Kupumzika.

Sasa alipomaliza kazi yake yote, kwa siku 6, akaona ni vema atenge siku moja apumzike. Akatenga muda wa saa 24 wa kutofanya kazi yoyote.

Hii ni kutufundisha pia, kuwa sisi tusijifanye tupo buzy sana kuliko Mungu, ikiwa yeye alipumzika, wewe ni nani usipumzike? Kama unatenda kazi kama mashine wiki nzima, usiku na mchana huna muda wa kupumzika, wiki nenda wiki rudi, miaka nenda miaka rudi.. Tambua kuwa hata hicho unachokifanya hakiwezi kuwa na ubora wowote. Hivyo na wewe ukienenda kwa ratiba kama hii ya Mungu katika wiki yako, jiandae kukutana na matokeo chanya katika mambo yako yote unayoyasumbukia. Uwe ni mtumishi wa Mungu katika huduma yako, au mwanafunzi, au mfanyakazi, au kiongozi, ijaribu ratiba hii ya Mungu uone.Lakini kama wewe  ibada si kitu cha muhimu kwako, unachowaza siku zote ni kazi tu, hujitenganishi, na kazi haramu, au marafiki wabaya, au mazungumzo mabaya, hujitengi na dhambi, huna muda na kuomba, au kujifunza Neno la Mungu, au kujirekebisha, unachowaza ni pesa tu ujue kuwa wiki yako, na masumbuko yako ni hasara tu. Kwasababu unapanda katika giza..unaumba katika maji..mahangaiko yako uwe na uhakika yatakuwa ni bure tu..

Kumbuka tunapoizungumzika ratiba hii ya Mungu, haimaanisha na wewe uifuate hivyo hivyo kwamba siku ya 1-4 ufanye hivi au vile, hapana, bali, walau katika wiki yako nzima, uhakikishe kila kipengele umekigusua, kwa muda unaolingana na huo Mungu alioutumia. Kama ni kupumzika, unaweza usiwe na saa 24 mfululizo, lakini hakikisha walau kwa wiki hukosi hizo saa 24 za kupumzika, vivyo hivyo na hayo mengine yote.

Bwana akubariki.

Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema,

Kwa maombezi/Ratiba za ibada/ Ushauri/ Maswali.
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312

pia kama utapenda uyapate mafundisho haya kwa njia ya Whatsapp au email basi tutumie ujumbe kwenye namba hizo hizo.

Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema,

Kwa maombezi/Ratiba za ibada/ Ushauri/ Maswali.
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312

pia kama utapenda uyapate mafundisho haya kwa njia ya Whatsapp au email basi tutumie ujumbe kwenye namba hizo hizo.

Mada Nyinginezo:

MWANZO WA INJILI YA YESU KRISTO.

NAMNA YA KUITAMBUA SAUTI YA MUNGU INAPOZUNGUMZA NA WEWE

AHADI YA ROHO ILIYOSALIA SASA KWA KIPINDI CHETU.

JE UNAIFANYA KAZI YA MUNGU?

VITABU VYA BIBLIA: Sehemu ya 1

Rudi nyumbani

Print this post

About the author

Admin administrator

Subscribe
Notify of
guest
1 Comment
Newest
Oldest Most Voted
Inline Feedbacks
View all comments
Friedrich@son of JESUS%
Friedrich@son of JESUS%
2 years ago

Amina mtumishi wa BWANA{YESU}
Nimejifunza kitu kikubwa hapo, ndio maana wakati mwingine naweza kujipanga wiki hii nifanye hvi na hvyo, lakini inapita bila mafanikio yeyote!

>>> Jina la MUNGU wetu {YESU} lihimidiwe&kusifiwa milele yote, NA UZIDI KUPOKEA UFUNUO WA ROHO MTAKATIFU SIKUZOTE.
Maran atha!