SWALI: Je! Kwetu SISI WATAKATIFU mtu akikuambia umuombee anaTATIZO halafu ukimuuliza ni tatizo gani asikuambie tatizo(Anasema hilo ni siri yake moyoni)-Huyo Tumuombee hilo tatizo lake la siri yake moyoni au?? Karibuni wapendwa..
JIBU: Kuna maombi ya kuombeana sisi kwa sisi ambayo hayahitaji mtu kumuhadithia mwingine ili amwombee, kwamfano kumwombea ndugu yako, Mungu amlinde na Yule mwovu, Mungu asimsahau katika ufalme wake, Mungu ampe kuokoa, Mungu ampe afya njema, Mungu amsaidie asimame katika imani asitetereke, Mungu ampe Amani na Upendo, mafanikio n.k..hayo ni maombi ambayo kila siku tunatakiwa tuyatamke kwa ndugu zetu wote wa mwilini na rohoni, Ndio jambo ambalo Mtume Paulo pia alikuwa analifanya:
Wakolosai 1:9 “Kwa sababu hiyo sisi nasi, tangu siku ile tuliposikia, HATUACHI KUFANYA MAOMBI NA DUA KWA AJILI YENU, ili mjazwe maarifa ya mapenzi yake katika hekima yote na ufahamu wa rohoni;
10 mwenende kama ulivyo wajibu wenu kwa Bwana, mkimpendeza kabisa; mkizaa matunda kwa kila kazi njema, na kuzidi katika maarifa ya Mungu;’’
Lakini yapo mahitaji mengine ambayo ni LAZIMA mtu AYANENE kwa faida yake mwenyewe, kama amedhamiria kuhitaji msaada kutoka kwa wengine. Kama mtu anayehitaji kuombewa tatizo Fulani linalomsumbua halafu haweki bayana hitaji hilo, nguvu ya kuombewa itatoka wapi, ni wazi kuwa anajizuilia Baraka zake yeye mwenyewe.
Biblia inaposema tuchukuliane mizigo, inamaanisha kuwa tusaidiane kwa kuitambua mizigo ya wenzetu, ukubwa wake, na uzito wake, ili mtu ajue ni jinsi gani kwa sehemu ya neema aliyopewa atamsaidia kuubeba, lakini kama mzigo kauficha mwenyewe ndani yake, wale wengine hata wakimwombea hawataomba ipasavyo, kwasababu hawatajua ukubwa au uzito wa tatizo lenyewe.
Jaribu kufikiria labda mtu ana ugonjwa ambao unamsumbua kwa muda mrefu, halafu hataki kuwaambia watu wanaomwombea kuwa anaumwa yeye anasema niombeeni tu..wale watu kweli wataomba pamoja naye lakini hiyo itaishia pale pale, lakini kama mfano kama angeweka bayana kuwa anasumbuliwa na ugonjwa Fulani (akautaja jina) na ameshahangaika muda mrefu bila matumaini yoyote, sasa kwa kuzungumza tu vile tayari katika roho anauchukua ule mzigo wake na kuwapa wengine, ndio hapo inatokea wale wenzake wanaguswa sana na shida yake, huruma zinawajaa ndani, wanaamua hata kutenga muda wao kufunga na kuomba kwa ajili ya shida yake, wengine wanampa maneno ya faraja ya kimaandiko, wanakuwa karibu naye kila siku, wengine wanaguswa wanamsaidia katika mahitaji machache ya mwilini kama kuna ulazima, na mwisho wa siku Yule mtu uponyaji wake unamfikia kwa haraka zaidi kwasababu walikuwepo wengine kuuchukua mzigo pamoja naye..
Hivyo ni lazima tujue kuwa kuna aina ya mahitaji ambayo mtu anaweza kukuombea bila hata ya kueleza siri ya moyo wako, lakini kuna mahitaji mengine kwa faida yako mwenyewe, unapaswa uwaambie ndugu wengine waaminifu, kumbuka pia sisemi kuwa kila jambo umweleze mtu, hapana, yapo mengine hayapaswi kuwekwa hadharani bali kwa watu uliowathibitisha kuwa ni waaminifu kwa Mungu. Kuna vitu vitu kama ukimwi, kesi za mauaji, n.k. hizo tafuta tu watumishi waaminifu wa Mungu, lakini vitu vingine kama magonjwa ya kawaida, ndoa, migongano, uzinzi n.k. Zungumza kwa ndugu wengine.
Lakini usikae na tatizo lako moyoni ikiwa unahitaji kweli kuombewa na wengine.
Ubarikiwe.
Mada Nyinginezo:
KWANINI KUNA WATU WANAFANYIWA DELIVERANCE LAKINI BAADA YA MUDA WANARUDIWA TENA NA HALI ILE ILE?
MUNGU NDIYE ANAYEISHAWISHI MIOYO.
KWANINI YESU KRISTO ALIKUJA DUNIANI?
WAISRAELI WENGI SANA WANARUDI KWAO SASA.
SWALI: Katika Biblia tunaona, ni Makuhani tu peke yao ndio walioruhusiwa kuhudumu katika Hema ya Mungu, na ndio walioruhusiwa kuingia ndani ya nyumba ya Mungu,ambao walikuwa ni wa kabila la LAWI mwingine yeyote akiingia kule anakufa, lakini katika biblia hiyo hiyo tunamwona mtoto Samweli ambaye hakuwa Mlawi aliwekwa ndani ya ile hema mbele ya lile sanduku la agano, na hakufa na tunasoma Baba yake aliyeitwa ELKANA alikuwa anatokea katika kabila la EFRAIMU, ukisoma 1 Samweli 1 utaona jambo hilo. Hapo nahitaji ufafanuzi kidogo.
JIBU: Tukisoma
1Samweli 1:1 inasema
“ Palikuwa na mtu mmoja wa Rama, Msufi, wa nchi ya milima milima ya Efraimu, jina lake akiitwa Elkana, mwana wa Yerohamu, mwana wa Elihu, mwana wa Tohu, mwana wa Sufu, MWEFRAIMU”.
Ni kweli kabisa kwa sentensi hiyo inaonyesha dhahiri kuwa Baba yake Samweli alikuwa ni Mwefraimu, lakini ukijifunza maandiko kwa undani! Utagundua kuwa Elkana Baba yake Samweli hakuwa Mwefraimu bali alikuwa Mlawi. Kumbuka wakati wa agano la kale, Kipindi ambacho Yoshua anaigawanya nchi ya Kaanani kwa makabila yote ya Israeli, Kabila la LAWI halikuwa na urithi wowote, Mungu aliwaweka wawe wakfu kwake kwa ajili ya shughuli ya madhabahuni tu, hivyo walipovuka Yordani walitawanywa na kukaa katikati ya makabila yote kuwahudumia watu katika masuala ya Torati na Ibada,..
Hivyo walawi waliokuwa wanakaa Dani, waliitwa wanadani, walawi waliokuwa Rubeni waliitwa warubeni, vivyo hivyo walawi waliokuwa wanakaa Efraimu waliitwa waefraimu.
Kumbukumbu 18:1 “Makuhani Walawi, kabila yote ya Lawi, wasiwe na fungu wala urithi pamoja na Israeli; watakula sadaka za Bwana zifanywazo kwa moto, na urithi wake.
2 Wala wasiwe na urithi kati ya ndugu zao; Bwana ndiye urithi wao, kama alivyowaambia”
Sasa kuthibitisha jambo hilo kuwa Samweli alikuwa ni mlawi, turudi katika kitabu cha Mambo ya Nyakati..Tusome.
1 Nyakati 6:33 “Na hawa ndio waliofanya huduma pamoja na wana wao. Katika wana wa Wakohathi; Hemani mwimbaji, mwana wa Yoeli, MWANA WA SAMWELI;
34 MWANA WA ELKANA, mwana wa Yerohamu, mwana wa Elihu, mwana wa Tohu;
35 mwana wa Sufu, mwana wa Elkana, mwana wa Mahathi, mwana wa Amasai;
36 mwana wa Elkana, mwana wa Shauli, mwana wa Uzia, mwana wa Urieli;
37 mwana wa Tahathi, mwana wa Asiri, mwana wa Ebiasafu, mwana wa Kora;
38 mwana wa Ishari, mwana wa Kohathi, mwana wa Lawi, mwana wa Israeli.
39 Na nduguye Asafu, aliyesimama upande wake wa kuume, huyo Asafu alikuwa mwana wa Berekia, mwana wa Shimea;
40 mwana wa Mikaeli, mwana wa Baaseya, mwana wa Malkiya;
41 mwana wa Yeatherai, mwana wa Zera, mwana wa Ido;
42 mwana wa Yoa, mwana wa Zima, mwana wa Shimei;
43 mwana wa Yahathi, mwana wa Gershoni, mwana wa Lawi.
44 Na upande wa kushoto ndugu zao, wana wa Merari; Ethani, mwana wa Kishi, mwana wa Abdi, mwana wa Maluki;
45 mwana wa Hashabia, mwana wa Amazia, mwana wa Hilkia;
46 mwana wa Amzi, mwana wa Bani, mwana wa Shemeri;
47 mwana wa Mali, mwana wa Mushi, mwana wa Merari, MWANA WA LAWI.
48 Na ndugu zao, Walawi, ndio waliowekwa ili kufanya huduma yote ya maskani ya nyumba ya Mungu”.
Unaona hapo? Ukiufuatilia huo uzao wa Elkana baba yake Samweli utaona unakuja kuishia kwa LAWI. Kwahiyo ni wazi kuwa Baba yake Samweli, Elkana hakuwa Mwefraimu bali Mlawi..Mungu asingeweza kuruhusu mtu yeyote asiyekuwa mlawi kuhudumu katika nyumba yake au hema yake. Kwahiyo Samweli alikuwa ni Mlawi, Mlawi mwenye asili ya Efraimu Ni sawa na leo Mchaga aliyezaliwa Kenya aje kuishi Tanzania, moja kwa moja atajulikana kama ni Mkenya..kwasababu amezaliwa Kenya na si Tanzania, ingawa asili yake na kabila lake ni Tanzania. Kwahiyo hiyo ndio sababu Elkana baba yake Samweli aliitwa Mwefraimu, ni kutokana na mahali alipotokea na sio kutokana na kabila lake.
Ubarikiwe.
Mada Nyinginezo:
MAANDALIZI YA UJENZI WA HEKALU LA TATU YAPO TAYARI.
MAJARIBU MATATU YA YESU KRISTO
JE! ADAMU ALIWASALIANA NA MUNGU KWA LUGHA IPI PALE BUSTANINI?
NITAMJUAJE NABII WA UONGO?
SWALI: 1 Petro 5:14 Biblia inasema …“Salimianeni kwa BUSU LA UPENDO. Amani na iwe kwenu nyote, mlio katika Kristo. ”….Hapo ana maana gani? Mfano Binti mtakatifu akikutana nami anibusu shavuni kisha anisalimu au Mimi nikionana na Mke wako barabarani kwa kuwa ni mtakatifu kama mimi nimbusu kisha nimsalimu SHALOM?..
JIBU: Ukisoma mstari huo kwa makini utaona biblia inasema ‘BUSU LA UPENDO’ Sehemu nyingine biblia inataja kama BUSU TAKATIFU..Unaweza kusoma hiyo katika Warumi..Warumi 16: 16 “Salimianeni kwa busu takatifu. Makanisa yote ya Kristo yawasalimu.”.. Na Pia katika 1Wakorintho16:20 inasema: “Ndugu wote wawasalimu. Salimianeni kwa busu takatifu.”…Na mistari mingine utakayoweza kukutana na hilo neno ni 2 Wakorintho 13:11, na 1 Wathesalonike 5: 24…Mistari yote hiyo inathibitisha kuwa kuna kitu kinaitwa Busu Takatifu. Sasa zamani kipindi cha Bwana wetu Yesu Kristo, na hata kabla ya hapo, kulikuwa na utaratibu wa kubusiana kama ishara ya salamu ya heshima kidogo, salamu ya kubusiana ndio ilikuwa salamu ya msingi kabisa kwa wakati huo, kama sasahivi ilivyo salamu ya kupeana mkono…kwahiyo watu walikuwa wakikutana walikuwa wanabusiana kwa nia ya kuonyesha upendo,shukrani, uthamani wa mtu n.k…Na kumbuka haikuwa busu la mdomo kwa mdomo hapana! Bali busu la mdomo kwa shavu au ubavu wa shavu. Na sasa tukirudi kwenye biblia inasema kuwa tusalimiane kwa BUSU TAKATIFU, ikiwa na maana kuwa sio Busu la mapenzi, wala sio busu la ubaya kama lile Yuda alilomsaliti nalo Bwana katika..
Mathayo 26: 48 “Na yule mwenye kumsaliti alikuwa amewapa ishara, akisema, Nitakayembusu, huyo ndiye; mkamateni.
49 Mara akamwendea Yesu, akasema, Salamu, Rabi, akambusu”.
Bali busu linalotajwa hapo ni BUSU LA HERI, NA BARAKA na UPENDO..Yaani mtu anambusu ndugu yake katika Kristo kwa nia ya kumtakia heri na Baraka kutoka kwa Mungu, kama mwamini. Lakini huo ulikuwa ni utamaduni wa zamani za wakati huo, ambapo Busu lilikuwa halina tafsiri nyingi tofauti tofauti kama ilivyo leo…Lakini leo hatuna utaratibu huo wa kubusiana..tuna utaratibu wa kupeana mikono…ambao huo unaweza kubeba maana kubwa zaidi au pengine hata sawa na kubusiana…Leo hii mwanamume akikutana na mwanamume mwenzake na kumbusu mbele za jamii haileti hiyo tafsiri Mtume Paulo aliyokuwa anaizungumzia hapo ya BUSU TAKATIFU, bali inaleta tafsiri nyingine…
Ingekuwa ni kwa kipindi cha wakati wake ingeweza kueleweka..Kwa wakati huu Busu takatifu linalokubalika katikati ya kanisa ni Busu kati ya dada na dada, au kati ya mzazi na mtoto na si kati ya kaka na dada ambao si ndugu, au kaka na kaka…Busu kati ya kaka na kaka inaleta tafsiri nyingine na maswali mengi,…
Kwahiyo hapo ni muhimu kutofautisha tu salamu zinazotumika kulingana na nyakati..Mtume Paulo hakusema kuwa hilo ni agizo toka kwa Mungu, kwamba ni lazima kila tukutanapo tusalimiane kwa kubusiana..hapana! kwasababu salamu zinabadilika kulingana na nyakati…angekuwepo katika wakati huu ambao tunapeana mikono au kukumbatiana kama salamu badala ya kubusia, angeshauri tusalimiane kwa kupeana mikono ya Utakatifu, nk. Kwahiyo ukikutana na mwamini mwanamke, msalimie tu kwa kumpa mkono hiyo ni sawa na kumsalimia kwa busu takatifu haileti tofauti yoyote.
Ubarikiwe.
Mada Nyinginezo:
TOFAUTI KATI YA SHERIA YA ROHO WA UZIMA NA SHERIA YA DHAMBI NA MAUTI!
MEZA YA BWANA, NA KUTAWADHANA MIGUU.
FASHION! NI DHAMBI KWA BINTI ZA MUNGU.
JIBU: Kama ukisoma vifungu vya juu katika hiyo habari utaona, ni kuwa kulikuwa na baadhi ya watu wanawashurutisha watu kwa kuwaambia kushika mambo ya mwilini ndio bora na kunafaa kwa uzima wa mtu, kwa mfano kuzingatia aina Fulani ya vyakula, kwamba usile kambale, au usile nguruwe, au ni lazima utahiriwe unapozaliwa, au ni lazima unawe mikono pale unapokula, au kutawadha, au ni lazima mtu afanye mazoezi ya mwili, au mtu ili awe mtakatifu ni lazima mtu asioe,… n.k… Na huku wamesahau au wamepuuzia kabisa mambo ya muhimu ya rohoni yaani kumcha MUNGU na utakatifu wa roho zao….
Na ndio hapa Paulo anamwambia Timotheo Ni kweli kwa namna moja au nyingine vinaweza vikampa mtu uzima wa mwili wake, na afya njema, hapa duniani lakini haviwezi kumpa uzima huko anapokwenda…Vitu kama hivyo haviwezi kumpa mtu daraja la moja kwa moja kwenda mbinguni, haviwezi kuzuia vitu kama tamaa za mwili n.k.
Wakolosai 2:20 “Basi ikiwa mlikufa pamoja na Kristo mkayaacha yale mafundisho ya awali ya ulimwengu, kwa nini kujitia chini ya amri, kama wenye kuishi duniani,
21 Msishike, msionje, msiguse;
22 (mambo hayo yote huharibika wakati wa kutumiwa); hali mkifuata maagizo na mafundisho ya wanadamu?
23 Mambo hayo yanaonekana kana kwamba yana hekima, katika namna ya ibada mliyojitungia wenyewe, na katika kunyenyekea, na katika kuutawala mwili kwa ukali; LAKINI HAYAFAI KITU KWA KUZIZUIA TAMAA ZA MWILI”.
Unaona?. Na ndio maana Paulo anamshauri Timotheo jambo jema la kuchagua…Nalo ni Utauwa, (Utakatifu), kuwa mtu wa rohoni, au kwa namna nyingine ni KUWA NA HOFU YA MUNGU ambalo hilo tu ndio linaweza kuyadhibiti mambo yote ya mwilini na rohoni….Ukiwa na hofu ya Mungu, ukimcha Mungu hata usipozingatia mlo kamili, bado Mungu atakulinda tu na kukupa afya, na bado juu yake utakuwa na ahadi ya uzima wa milele..Tofauti na Yule mtu anayezingatia lishe bora na huku maisha yake ya rohoni yapo chini, anaweza kweli akapata afya njema, na mwonekano mzurimkwa kitambo tu lakini siku akifa atakuwa wapi kama moyo wake ni mchafu..
Unaweza ukawa umehangaika kujipatia mali ili uwe na maisha bora hapa duniani, ni kweli hapo ni sawa na umejipatia nguvu za mwilini, kwani mali ni ulinzi, zinaweza kukulinda kwa sehemu Fulani, lakini roho yako haiwezi kulindwa na mali…lakini ukiwa ni mtu wa rohoni, mtauwa, mtakatifu, unayemcha Mungu, unayeyajua maandiko, anayezijua ahadi za Mungu, analisimama imara katika Imani,..Mali ameahidiwa kuzipata halikadhalika uhakika kwa maisha ya milele upo. Sasa Kwanini na sisi tusichague fungu hilo?
1Timotheo 4:8 “Kwa maana kujizoeza kupata nguvu za mwili kwafaa kidogo, lakini utauwa hufaa kwa mambo yote; yaani, unayo ahadi ya uzima wa sasa, na ya ule utakaokuwapo baadaye.
Hivyo tusipoteze muda mwingi kwa vitu vya muda tu, bali tujishuhulishe zaidi na vile vitakavyotusaidia kwa mambo yote..Hiyo ni hesabu rahisi sana na inayoeleweka.
Ubarikiwe.
Mada Nyinginezo:
NITAONGEZAJE NGUVU ZANGU ZA ROHONI?
MAJARIBU MATATU YA YESU KRISTO
ROHO ZILIZO CHINI YA MADHABAHU:
UTHABITI WA AGANO LA MUNGU KWA MKRISTO.
ALAMA KATIKA VIPAJI VYA NYUSO.
SWALI: Bwana akubariki ndugu yangu wa thamani . Naomba kujua kwa namna Bwana alivyokujalia kujua juu ya hawa viumbe kutoka katika sayari ya Mars kama sikosei wanaiotwa ALIENS je ni kweli wapo ?au ni elimu ya dunia (sayansi ) inayoidanganya ulimwengu?.
JIBU: Ubarikiwe sana kwa swali zuri ndugu, Ukweli ni kwamba hakuna viumbe vingine vinavyoishi katika ulimwengu (Universe) zaidi ya wanadamu, Biblia haijasema kama kuna viumbe wengine tofauti na wanadamu na wanyama. Hadithi ya huu ulimwengu inamuhusu Mwanadamu na Muumba wake basii!! Inahusu ni jinsi gani Mungu alivyomuumba Mwanadamu na kumpa mamlaka juu ya vitu vyote chini yake, vilivyopo ulimwenguni…
Kwahiyo hakuna kiumbe kingine chochote kilicho na akili zaidi ya mwadamu kinachoishi ulimwenguni wa mbali, kumbuka tunapozungumzia ulimwengu hatuzungumzii tu dunia tunayoishi peke yake hapana bali tunazungumzia sayari zote na magimba yote yaliyopo angani, na kila mahali ambapo upeo wa mwanadamu unaweza kufika kote huko ni ulimwenguni, na hakuna kiumbe kingine chochote kinachoishi katika ulimwengu chenye kumzidi mwanadamu akili…
Zaburi 8: 3 “Nikiziangalia mbingu zako, kazi ya vidole vyako, Mwezi na nyota ulizoziratibisha;
4 Mtu ni kitu gani hata umkumbuke, Na binadamu hata umwangalie?5 Umemfanya mdogo punde kuliko Mungu; Umemvika taji ya utukufu na heshima;
6 Umemtawaza juu ya kazi za mikono yako; Umevitia vitu vyote chini ya miguu yake.
7 Kondoo, na ng’ombe wote pia; Naam, na wanyama wa kondeni;
8 Ndege wa angani, na samaki wa baharini; Na kila kipitacho njia za baharini.
9 Wewe, MUNGU, Bwana wetu, Jinsi lilivyo tukufu jina lako duniani mwote!”
Sasa utauliza kama hakuna viumbe wengine wenye akili kuliko mwanadamu wanaoishi huko angani na kwenye masayari mengine…ni nini basi viumbe hivi wanasayansi wanavyoviona na kuvipiga picha huko angani vinavyofanana na watu?.
Ni ukweli usiopingika kwamba wana-sayansi kuna vitu wanaviona angani, na wakati mwingine wanafanikiwa kuvipiga picha, na wakati mwingine wanaona vinawapa ujumbe Fulani kwa ishara, na wakati mwingine vinatokea tu kwa mfano wa mwanga Fulani na kutoweka, na kuwabakisha katika maswali mengi. Na kwasababu Sayansi kwa sehemu kubwa haiamini kama kuna Mungu hivyo wana-sayansi hawa wanaishia kutafuta kujua ni nini hasa wanavyoviona au kuvipiga picha.
Sasa hivi viumbe (Ambavyo wana-sayansi wanaviiita ALIENS) ni wakina nani?..Jibu la swali hilo tunaweza kulipata katika mstari ufuatao.
Ufunuo 12: 7 “Kulikuwa na vita mbinguni; Mikaeli na malaika zake wakapigana na yule joka, yule joka naye akapigana nao pamoja na malaika zake;
8 nao hawakushinda, wala mahali pao hapakuonekana tena mbinguni.9 Yule joka akatupwa, yule mkubwa, nyoka wa zamani, aitwaye Ibilisi na Shetani, audanganyaye ulimwengu wote; akatupwa hata nchi, na malaika zake wakatupwa pamoja naye”.
Kwahiyo viumbe hawa wanasayansi wanaoviona huko angani ni shetani na majeshi yake (mapepo).Na kwasababu shetani naye ana akili, kama biblia inasema ana uwezo wa kujigeuza na kuwa mfano wa malaika wa Nuru, hivyo anachokifanya yeye na malaika wake walioasi (yaani mapepo) ni kujigeuza na kujifanya kuwa ni viumbe wengine wenye akili sana wanaotokea sayari za mbali, na wanawatokea baadhi ya watu tu! Wale wenye kuamini mambo hayo, na lengo lake Shetani ni lile lile KUDANGANYA WANADAMU. Kuwatoa wanadamu katika kuamini kuwa kuna Mungu na kuwafanya waamini kuna viumbe wengine wanaoishi sayari za mbali wenye akili nyingi zinazowazidi wao…Hivyo wanaweza kuwatumainia wao kuwaletea msaada na utatuzi wa mambo yao ya kiteknolojia na kijamii…
Ni kama vile MASIHI wao wanamngojea. Kumbuka shetani ana vitengo vingi vya kuwapotosha wanadamu, anatumia uchawi kuwapotosha wale watu wanaoamini kuna uchawi, anatumia manabii wa uongo na waalimu wauongo kuwapotosha wale wanaokwenda kanisani wasioamini katika uchawi bali Mungu…na anatumia uongo wa Ma-ALLIENS Kuwadanganya wale watu wasioamini kuwa kuna Mungu, ili waendelee kuamini hivyo hivyo kuwa hakuna Mungu bali kuna viumbe wengine huko angani. Kazi yake ni kuwa akishagundua unapenda nini na upo wapi, anakutafutia upotoshaji katika hicho hicho kitu unachokipenda.
Nimewahi kusoma ushuhuda mmoja, mwanamke mmoja ambaye alikuwa ndio amempa Kristo maisha yake ila hajasimama vizuri, anasema alikuwa anapenda sana kusoma habari za ma-Alliens, na moyoni mwake alikuwa ameshaanza kuamini na kushawishika kuwa kwa namna moja au nyingine ni lazima kutakuwepo na viumbe wengine tofauti na wanadamu wanaoishi mojawapo ya zile sayari kule juu, sasa wakati akiwa katika uchunguzi wake akitamani sana siku moja awaone..maana alisikia shuhuda nyingi mbali mbali kuwa watu wamewaona na wengine wametokewa…anasema siku moja wakati anaendesha gari lake usiku wakati yupo njiani anarejea nyumbani..ghafla mbele ya barabara mbali kidogo akaona kitu kama mwanga Fulani mzuri sana alivyozidi kutazama aliona kile kitu kikakaribia mpaka pale gari lake lilipo na akafunga breki anasema hicho kitu kilikuwa kama ndege Fulani mfano wa kisahani hivi (spaceship).
Na alipokiona ni kama kilikuwa kimetengenezwa kwa teknolojia ya hali ya juu, ambayo duniani kwasasa haipo. Na vile viumbe vilivyomo mule ndani hakuviona isipokuwa alisikia tu sauti ikizungumza na yeye ndani yake ikimwambia wao ni viumbe kutoka sayari ya mbali wamekuja kuusaidia ulimwengu..Huyo dada anasema ndani ya moyo wake akafurahi sana akahisi kama ndoto yake imetimia ya kuwaona Ma-Aliens…Lakini kipindi kifupi nyuma alisikia injili na kuamua kumfuata Bwana Yesu, lakini alikuwa mguu mmoja nje mwingine ndani..
Hivyo akajikuta tu anawauliza swali hao viumbe..akawauliza “huko mlipo mnamwabudu Yesu?”..havikujibu, alipozidi kuviuliza hilo swali ndipo vikamjibu na kumwambia “sisi hatumwabudu Yesu nyinyi wanadamu ndio mnaomwabudu, sisi sio wanadamu”..wakati anaendelea kuwauliza wao wanamwabudu nani hicho chombo chao kikaondoka mbele yake..Baadaye, anasema kutoka na mwanga ule aliouna ulianza kumletea shida kila alipokuwa anasoma biblia alikuwa anaona mwanga tu, haoni chochote, lakini siku alipokuja kuombewa na hizo roho kumtoka ndipo akaja kufahamu kuwa alichokiona sio ma Aliens kama alivyokuwa anafikiri bali ni mapepo yaliyojigeuza na kujifanya kuwa ni ma aliens. Kwahiyo kwa kuhitimisha, elimu ya ma-ALIENS ni elimu ya shetani kabisa, iliyotengenezwa kuzimu kwa lengo na nia ya kuwapoteza watu wasiamini kuhusu Mungu bali waamini utafiti wa kisayansi juu ya uwepo wa viumbe wengine zaidi ya wanadamu. Na jambo hili limewaathiri sana watu wa Ulaya, huku kwetu ndio nalo linaanza kukita mizizi.
Ubarikiwe.
Mada Nyinginezo:
KUNDI LA MALAIKA WALETAO MABAYA.
ROHO YA MPINGA KRISTO IKITENDA KAZI SIKU HIZI ZA MWISHO.
SWALI: 2 Wafalme2:12; `Naye Elisha akaona,akalia,Baba yangu,baba yangu,GARI LA ISRAELI NA WAPANDA FARASI WAKE! Asimwone tena kabisa;’ ” Hapo anaposema “Gari la Israeli na wapanda farasi wake!-Anamaana gani?”
JIBU: Hilo ni swali la kujiuliza ni kwanini mwisho wa safari ya Eliya linatokea gari kutoka mbinguni na wapanda farasi wake, na si isiwe kitu kingine labda ngazi, au upepo au aishie kutoweka tu asionekane mpaka litokee gari la vita?, Hizi ishara zinazotokea mwisho za washindania Imani, zinakuwa na maana kubwa sana kwetu, ni sawa na Bwana wetu Yesu alivyoondoka tujiulize ni kwanini WINGU lilimpokea na si gari au malaika..lipo jambo Mungu anatuonyesha katika haya matukio.
Lakini tukirudi kwenye tukio la Eliya, Kulitokea gari la Vita, Elisha ndio alivyoliona, hii kuonyesha kuwa Eliya alikuwa vitani Duniani anapigana, na sasa mwisho wa vita vyake umefika, Ushindi ameshaupa, vita kavipiga, mwendo kaumaliza, Umefika wakati wa kuondoka, Hivyo ni wajibu lile jeshi lililokuwa linapigana naye yeye kama Jemedari wao siku zote za maisha yake, lije kumchukua na kumpeleka nyumbani kwa vishindo vikuu vya ushindi. Vivyo hivyo hata leo kwa mtakatifu yoyote atakayemaliza kazi yake duniani kwa ushindi , siku ile anayokufa, katika Ulimwengu wa Roho lile Gari la Israeli [yaani Jeshi la ki-mbinguni] ambalo siku zote za maisha yake amekuwa akitembea nalo kupigana vita litamchukua moja kwa moja mpaka Paradiso kule watakatifu wengine walipo. Lakini hiyo ni mpaka mtu apigane na ashinde, asiposhinda hakuna atakayekuja kumchukua, huyo atabakia kaburini, Na ndio maana Mtume Paulo mwisho wa safari yake aliandika hivi:
2Timotheo 4:6 “Kwa maana, mimi sasa namiminwa, na wakati wa kufariki kwangu umefika.
7 Nimevipiga vita vilivyo vizuri, mwendo nimeumaliza, Imani nimeilinda;8 baada ya hayo nimewekewa taji ya haki, ambayo Bwana, mhukumu mwenye haki, atanipa siku ile; wala si mimi tu, bali na watu wote pia waliopenda kufunuliwa kwake”.
Hivyo na sisi pia tujitahidi tukaze mwendo, siku ile tuondoke na ushindi mnono duniani. Kwasababu yapo mema mazuri Mungu ametuandalia huko tuendako.
Ubarikiwe.
ROHO YA ELIYA KATIKA AGANO JIPYA INATENDAJE KAZI?
NITAONGEZAJE NGUVU ZANGU ZA ROHONI?
JE! MBINGUNI KUTAKUWA NA KULA NA KUNYWA?
JE! NI HALALI KUTOA CHETI KWA WAKRISTO WANAOOA?
SWALI : Pale Bwana Yesu aliposema “Kila mtu amwachaye mkewe, isipokuwa kwa habari ya uasherati, amfanya kuwa mzinzi; na mtu akimwoa yule aliyeachwa, azini.(Mathayo 5:32)” Alimaanisha nini?.
JIBU: Neno usherati kama linavyoonekana kwenye kamusi, tafsiri yake ni “kufanya kitendo cha ngono na mtu ambaye bado haujaoana naye”..hii ikimaanisha kuwa inaweza ikawa mtu yupo ndani ya ndoa au nje ya ndoa, tofauti na Neno UZINZI, ambao huo unakuja pale mtu anapofanya kitendo cha ngono na mtu ambaye si mwanandoa mwenzake (yaani kitendo cha kutoka nje ya ndoa na kwenda kufanya ngono). Hivyo tunaweza kusema Neno Usherati ni Neno la ujumla likimaanisha kitendo chochote cha zinaa kinachofanywa na mtu isivyopaswa yaani nje ya ndoa halali. Kwahiyo Bwana Yesu aliposema pale katika Mathayo 5:32 na Mathayo 19:9, kwamba lakini mimi nawaambia, Kila mtu amwachaye mkewe, isipokuwa kwa habari ya uasherati, amfanya kuwa mzinzi;.. kitendo kile alikilenga hasa kwa wanandoa, kwasababu habari iliyokuwa inazungumziwa pale ni ya watu ambao wapo katika mahusiano ya mke na mume.
Pia kwa kuongezea hapo, ukisoma sehemu nyingi katika maandiko kwenye agano la kale na jipya, utaona Mungu alilitumia hilo neno Uasherati, kumaanisha uzinzi ambao watu wake walikuwa wanafanya katika roho, soma 〈2 Nyakati 21:10-14,〉 〈Ezekieli 16:27, 43, 58,〉 Ezekieli 22:11, 〈Ufunuo 17:1-5, 19:2 〉n.k. vipo vifungu vingi sana na vyote hivyo vinautaja uzinzi kama uasherati, ambao watu wa Mungu wameufanya na sanamu na machukizo yao…Uasherati ni Neno la Ujumla, ukitaka kushikilia tu Uasherati katika biblia unamaanisha kitendo cha ngono nje ya ndoa takatifu, basi biblia itakuwa haina maana sehemu nyingi, ikiwemo katika hivyo vifungu nilivyovitoa hapo juu.
Hivyo biblia inaposema Ndoa na iheshimiwe na watu wote, ilimaanisha kweli kweli. huwezi kuingia tu kwenye ndoa halafu ukajifanyia tu mambo unayotaka ukaamua kwenda kuzini ukijifariji kuwa hiyo ndoa tayari imeshafungwa haiwezi kuvunjika..Ndugu nataka nikuambie Inaweza kuvunjika kwa kitendo hicho na isiwe makosa mbele za Mungu kwenda kuoa/kuolewa na mwingine.
Lakini ifahamikie pia hilo halikuwa agizo kwamba kila kitendo cha kukosa uaminifu katika ndoa iwe sababu ya mtu kumwacha mkewe na kwenda kuoa mwingine hapana.. Mungu hapendi kuachana biblia imesisitiza hilo, na zaidi ya yote tumefundishwa kusamehe, kwani hata na sisi tunamkosea Mungu kwa mengi. Hivyo kusamehe ni msingi mkubwa sana wa ndoa kusimama. Na zaidi ya yote ni uaminifu na kuwa na hofu kwa Mungu, tukijua kuwa ndiye Mungu aliyeiunganisha, tusigeuke kuwa VIFO katikati yetu. mwanandoa aliweke hilo kichwani kuwa akienda kuzini amestahili kuachwa kibiblia na kusiwe na hatia zozote mbele za Mungu.
Shalom.
Pia unaweza ukapata mafundisho haya Kwa njia ya Whatsapp yako, jiunge na channel yetu Kwa kubofya hapa >> WHATSAPP
Mada Nyinginezo:
MADHARA YA DHAMBI YA UASHERATI.
‘’MOTO HUFA KWA KUKOSA KUNI’’..NA NDIVYO ILIVYO KWA UASHERATI
USIWE SABABU YA WATU KUMKUFURU MUNGU.
JIBU: Tusome..
Luka 19:12 “Basi akasema, Mtu mmoja, kabaila, alisafiri kwenda nchi ya mbali, ili ajipatie ufalme na kurudi.
13 Akaita watu kumi katika watumwa wake, akawapa mafungu kumi ya fedha, akawaambia, Fanyeni biashara hata nitakapokuja.
14 Lakini watu wa mji wake walimchukia, wakatuma wajumbe kumfuata na kusema, Hatumtaki huyu atutawale.
15 Ikawa aliporudi, ameupata ufalme wake, aliamuru waitwe wale watumwa aliowapa fedha, ili ajue faida aliyopata kila mtu kwa biashara yake.
16 Akaja wa kwanza, akasema, Bwana, fungu lako limeleta faida ya mafungu kumi zaidi.
17 Akamwambia, Vema, mtumwa mwema; kwa vile ulivyokuwa mwaminifu katika neno lililo dogo, uwe na mamlaka juu ya miji kumi.
18 Akaja wa pili, akasema, Bwana, fungu lako limeleta mafungu matano faida.
19 Akamwambia huyu naye, Wewe uwe juu ya miji mitano.
20 Akaja mwingine akasema, Bwana, hili ndilo fungu lako, ambalo nililiweka akiba katika leso.
21 Kwa maana nilikuogopa kwa kuwa u mtu mgumu; waondoa usichoweka, wavuna usichopanda.
22 Akamwambia, Nitakuhukumu kwa kinywa chako, mtumwa mwovu wewe. Ulinijua kuwa ni mtu mgumu, niondoaye nisichoweka, na kuvuna nisichopanda;23 basi, mbona hukuiweka fedha yangu kwa watoao riba, ili nijapo niipate pamoja na faida yake?
24 Akawaambia waliosimama karibu, Mnyang’anyeni hilo fungu, mkampe yule mwenye mafungu kumi.
25 Wakamwambia, Bwana, anayo mafungu kumi.
26 Nawaambia, Kila aliye na kitu atapewa, bali yule asiye na kitu atanyang’anywa hata alicho nacho.
27 Tena, wale adui zangu, wasiotaka niwatawale, waleteni hapa mwachinje mbele yangu”.
Shalom!
Mfano huo Bwana aliutoa alikuwa anajizungumzia yeye na kanisa lake.
Huyo Mtu Kabaila aliyesafiri kwenda nchi ya mbali ni BWANA wetu YESU mwenyewe, (KABAILA maana yake ni MTU ALIYEZALIWA KATIKA FAMILIA YA JUU ZAIDI KATIKA JAMII inaweza kuwa familia ya kifalme au kichifu,nk) kama tunavyojua, Bwana Yesu asili yake ni Mbinguni ametoka katika familia ya kimbinguni, na ndio maana hapa anajifananisha na huyu Kabaila, tunaona na baada ya kumaliza tu kazi yake alipaa kwenda mbingu za mbingu..sasa hiyo ndiyo nchi ya mbali inayozungumiwa pale kwenye huo mfano, Na amekwenda kule kwa makusudi kabisa ili kutuandalia sisi makao ili arudi tena kuja kutuchukua. Na kama mfano unavyosema “akawaita watumwa wake kumi akawapa mafungu 10 ya fedha” maana yake ni kwamba Bwana wakati anaondoka duniani siku ile alituachia sisi Roho wake Mtakatifu..kisha akatugawia majukumu kama agizo kuu, akatuambia tukahubiri injili kwa kila kiumbe ili kuleta faida katika ufalme wa mbinguni, aaminiye na kubatizwa ataokoka, kwahiyo Roho Mtakatifu aliachiliwa juu ya kila mwamini kila mmoja kwa kiwango chake cha neema alichopewa, hilo ndio fungu la fedha kwenye huo mfano (Matendo 2:38)..
Ukichunguza pia utaona hawakuambiwa wakafanye biashara moja, hapana kila mmoja alikuwa na uhuru wa kufanya biashara yake, hii ikiwa na maana kila mmoja anayo karama yake Mungu kampa. Na kwa kupitia hiyo utaulizwa uliitumiaje katika mambo yahusuyo ufalme wa mbinguni.
Uwe ni mwinjilisti uwe ni mwalimu uwe ni mchungaji n.k. Na kama huo mfano unavyosema kwamba kuna siku moja yule kabaila alirudi, na kuanza kuwauliza wale watu aliowapa yake mafungu kila mmoja ameleta faida kiasi gani katika biashara, Ndivyo itakavyokuwa kwetu kila mmoja ataenda kutoa hesabu mbele ya Bwana wetu YESU siku ile. kaitumiaje neema aliyopewa duniani Ndipo atakapowakusanya watumishi wake wote, na kuanza kumlipa mmoja baada ya mwingine kulingana na jinsi alivyotumika katika huduma, katika nafasi yake ya kuhubiri injili..waliotumika kwa uaminifu watalipwa thawabu kubwa zaidi, lakini waliozembea au waliokuwa wanafanya kazi ya Mungu kwa ulegevu na uvivu, au kinyume cha Neno Bwana anasema atawanyang’anya na thawabu yao na kupewa watu wengine.
Kwahiyo hiyo ndio maana ya mfano huo, unatufundisha kuwa makini sana na Neema Mungu aliyotupa ya Roho wake Mtakatifu, na karama alizotupa, kwamba siku moja tutakwenda kuulizwa, kama umepewa karama ya kuhubiri, au kufundisha halafu haufundishi inavyopaswa au kulingana na Neno, au unakuwa mvivu na kuendelea na mambo yako mengine na kuidharau kazi ya Mungu…Basi siku za mwisho utakwenda kuulizwa..Kama ulipewa karama ya kuhubiri kwa njia ya uimbaji na uimbaji wako hauna tofauti na waimbaji wa miziki ya kidunia, kila mtu akutazamapo anaona kitu tofauti na unachoimba, utakwenda kuulizwa siku ile. Ndio maana Bwana anasema..
Ufunuo 22:12 “Tazama, naja UPESI, na ujira wangu u pamoja nami, kumlipa kila mtu kama kazi yake ilivyo.
13 Mimi ni Alfa na Omega, mwanzo na mwisho, wa kwanza na wa mwisho”.
Ubarikiwe.
Mada Nyinginezo:
JIFANYIE RAFIKI KWA MALI YA UDHALIMU.
ACHENI MJUE YA KUWA MIMI NI MUNGU.
NINI MAANA YA HILI ANDIKO “USHUHUDA WA YESU NDIO ROHO YA UNABII” (UFUNUO 19:10)?
MTEGEMEE MUNGU, NA SI MWANADAMU.
JIBU: Biblia haijatueleza muda Ayubu aliokaa katika majaribu, Lakini tukisoma baadhi ya vipengele inatupa picha kukisia muda aliodumu, kwa mfano tukisoma ile sura ya Ayubu 7:2-6 Ayubu anasema..
“2 Kama mtumishi atamaniye sana kile kivuli, Kama mwajiriwa anayetazamia mshahara wake;
3 Ni vivyo nami NIMEPEWA MIEZI YA UBATILI iwe fungu langu, NAMI NIMEANDIKIWA MASIKU YENYE KUCHOKESHA.
4 Hapo nilalapo chini, nasema, Nitaondoka lini? Lakini usiku huwa mrefu; Nami nimejawa na kujitupa huku na huku hata kupambazuke.
5 Mwili wangu unavikwa mabuu na madongoa ya udongo; Ngozi yangu hufumba, kisha ikatumbuka tena.
6 Siku zangu hupita upesi kuliko chombo cha kufumia, Nazo zapita pasipokuwa na matumaini.”
Unaona hapo Ayubu anajaribu kujifananisha na mtu aliyeajiriwa ambaye kwa uvumilivu mwingi anasubiri mshahara wake kila mwisho wa kipindi Fulani labda tuseme wiki, au mwezi au mwaka,.apate faraja ya taabu yake, vivyo hivyo Ayubu naye anaonyesha amekaa katika hali hiyo ya kusononeka na kutaabika kwa MIEZI na masiku mengi, kama ya mwajiriwa vile, akisubiria faraja yake kutoka kwa Mungu ni lini atamrehemu na kumtoa katika mateso yale na majonzi yale.. Tunaona hapo Ayubu katamka neno MIEZI na sio MWEZI, hiyo ikiwa na maana ni zaidi ya mmoja, inaweza ikawa ni miwili au mitatu, au mitano au 12, au 20, au 100 hatujui kwasababu biblia haijaeleza jambo lingine la ziada.
Halikadhalika Pia hatujui ni muda gani ilimchukua Ayubu kukaa na wale marafiki zake, ambao tunasoma pia waliwasili kwake na kukaa siku 7 bila kuzungumza naye chochote, hivyo tukijumulisha na siku ambazo ziliwagharimu kufika kwa Ayubu kutoka majumbani kwao baada ya kupata taarifa za msiba wake, pamoja na siku ambazo walikuwa wanazungumza naye.. tukijumuisha na wakati ambapo Mungu anamwagiza Ayubu awaombee rehema wale marafiki zake kwa kwenda kuchukua ng’ombe 7 na kondoo 7 kwa ajili ya sadaka ya kuteketezwa, tunaweza kukisia ni muda unaoweza kuchukua zaidi ya mwezi.. Lakini pia hatujui, kipindi Mungu alichotumia kumrejeshea Ayubu vitu vyote na mali zote alizozipoteza, je ilikuwa ni mara moja au kidogo kidogo, kama ni kidogo kidogo basi ni muda mrefu ulipita, lakini tunachofahamu ni kuwa Mungu alimburudisha Ayubu mara mbili ya alivyokuwa navyo pale mwanzo. Lakini hiyo ilikuwa ni kwa kusubiri na kwa kustahilimili na kwa kuvumilia.
Yakobo 5.10 “Ndugu, watwaeni manabii walionena kwa jina la Bwana, wawe mfano wa kustahimili mabaya, na wa uvumilivu.
11Angalieni, twawaita heri wao waliosubiri. Mmesikia habari ya subira yake Ayubu, mmeuona mwisho wa Bwana ya kwamba Bwana ni mwingi wa rehema, mwenye huruma.”
Hivyo na sisi tunafundishwa tujifunze kuwa wavumilivu maadamu tunajiona bado tupo katika njia sahihi ya wokovu,hatuna budi kuwa hivyo kama Ayubu, tabu, shida, misiba, dhiki, mateso, kupungukiwa, n.k. visituzimishe roho tukamkufuru Mungu kama mke wa Ayubu, hata kama itachukua mwezi, au miezi, au miaka, au miongo, hilo lisituzuie kuangalia ahadi za Mungu, sisi tunachofahamu tu ni kuwa mwisho wa siku tutamwona Mungu jinsi alivyo mwingi wa rehema na huruma…kama alivyokuwa kwa Ayubu.
Ubarikiwe.
Mada Nyinginezo:
HUDUMA YA (ELIFAZI, BILDADI, NA SOFARI).
MAJARIBU MATATU YA YESU KRISTO
AYUBU 28 : HEKIMA NI NINI? NA UFAHAMU UNAPATIKANA WAPI?
TUTAWEZAJE KUMZALIA MUNGU MATUNDA?
SWALI: Shalom!
Luka 23:27 “Mkutano mkubwa wa watu wakamfuata,na wanawake waliokuwa wakijipiga vifua vyao na kumwombolezea.Yesu akawageukia,akasema,Enyi binti za Yerus’alemu,msinililie mimi,bali jililieni nafsi zenu na watoto wenu.29″KWA MAANA TAZAMA SIKU ZINAKUJA mtakaposema,HERI WALIOTASA,na MATUMBO YASIYOZAA,na MAZIWA YASIYONYONYESHA. Naomba kufahamu Siku hizo Kwanini hao walisema “Heri waliotasa..heri matumbo yasiyozaa..heri maziwa yasiyonyonyesha??
JIBU: Shalom! Hayo maneno a Bwana Yesu aliyazungumza kabla ya kupandishwa msalabani, Tunaona wale wanawake waliokuwa wanamfuata walimwonea huruma sana na kusikia uchungu mkubwa kwa mateso aliyokuwa anayapitia…lakini Bwana Yesu akawaambia msinililie mimi bali jililieni ninyi nafsi zenu na watoto wenu.. Kwanini alisema vile…
Kwasababu aliona kipindi kifupi sana kinachokuja mbeleni…kwamba mambo yaliyompata yeye yatakwenda kuwapata na wao pia, pamoja na watoto wao tena makubwa zaidi ya hayo…ambapo na wao pia watakatwa katwa na wanawake watachichwa kama kuku. Na kama unafuatilia unabii vizuri wa Biblia utakuja kuona kuwa kipindi kifupi tu baadaye AD 70 (yaani miaka 37 baada ya kusulibiwa kwa Bwana)..Jeshi la Rumi lilikuja na kuuzingira mji wa Yerusalemu na kuuchoma moto na kuwaaua watu wengi sana wakiwemo wanawake na watoto …historia inasema zaidi ya watu milioni moja na laki moja waliuawa…Mpaka ikaonekana kuwa ni heri mwanamke aliyetasa ambaye hakuzaa mtoto kuliko Yule aliyezaa na kuona mtoto wake anachichwa kama kuku mbele yake,Yerusalemu kulikuwa na maombolezo makubwa sana, hiyo ni kutimiza unabii alioutoa Bwana juu ya Mji huo katika..
Luka 19: 41 “Alipofika karibu aliuona mji, akaulilia, 42 akisema, Laiti ungalijua, hata wewe katika siku hii, yapasayo amani! Lakini sasa yamefichwa machoni pako. 43 Kwa kuwa siku zitakuja, adui zako watakapokujengea boma, likuzunguke; watakuzingira na kukuhusuru pande zote; 44 watakuangusha chini wewe na watoto wako ndani yako, wasikuachie jiwe juu ya jiwe, kwa sababu hukutambua majira ya kujiliwa kwako”.
Mathayo 23.37 “Ee Yerusalemu, Yerusalemu, uwauaye manabii, na kuwapiga kwa mawe wale waliotumwa kwako! Ni mara ngapi nimetaka kuwakusanya pamoja watoto wako, kama vile kuku avikusanyavyo pamoja vifaranga vyake chini ya mabawa yake, lakini hamkutaka! 38 Angalieni, nyumba yenu mmeachiwa hali ya ukiwa”.
Unaona hapo? Sababu ya Mji kuharibiwa na kufanywa ukiwa?..Ni kwasababu hawakujua saa ya kujiliwa kwao, ni kwasababu Masihi alikuja kwao na wao wakamkataa wakasema anapepo, anakufuru n.k hawakujua kuwa yeye ni mwokozi na ndiye aliyeteuliwa na MUNGU kuwa ukombozi kwa mwanadamu…Na kwasababu hiyo, Bwana akawaambia ule ulinzi na amani vimeondoka kwao siku zinakuja siku watakapoteketezwa na kuangamizwa na kutolewa kutoka katika nchi yao..Ndio maana Bwana akawaambia msinililie mimi, bali jililieni nyinyi na watoto wenu..kwasababu yatakayokuja kutokea mbeleni ni makubwa kuliko haya yangu.
Hiyo ilikuwa ni dhiki au adhabu kwa wayahudi (yaani waisraeli) kwa kumkataa Masihi, na kadhalika itakuja dhiki nyingine iliyo kubwa na isiyo na mfano kwa watu wa dunia nzima, kwa wale wote ambao wanamkataa Kristo sasa na kumsulibisha katika akili zao..Dhiki hiyo itakuwa ni kubwa isiyokuwa na mfano kuliko hiyo iliyowapata wayahudi..Biblia inaeleza hivyo. Kwahiyo tukiyajua hayo, sio wakati wa kuchezea hatima yetu ya milele, kabla dhiki kuu haijamiminwa duniani tunapaswa wakati huo tuwe tumekwenda na Bwana katika unyakuo. Je! Na wewe una uhakika utakuwepo miongoni mwao watakaomlaki Bwana mawinguni?
Bwana akubariki.Pia unaweza ukapata mafundisho haya Kwa njia ya Whatsapp yako, jiunge na channel yetu Kwa kubofya hapa >> WHATSAPP
NGURUMO SABA
JIFANYIE RAFIKI KWA MALI YA UDHALIMU.
WAISRAELI WENGI SANA WANARUDI KWAO SASA.
TUNAPOSEMA TUISHI KWA NENO, INAMAANISHA TUISHI MAISHA YA NAMNA GANI?