MTANGO WA YONA.

MTANGO WA YONA.

Mara nyingi Mungu wetu akitaka kutupa ujumbe, au kumpa mtu ujumbe huwa anazungumza na sisi kwa mifano, au kwa ishara, na mifano hiyo inatusaidia kuzielewa vizuri hisia zake kwetu au kwa kitu fulani..…Kwamfano utaona Daudi alipowaacha wanawake waliokuwa wengi katika nchi yake na kwenda kumchukua mke wa Uria, utaona kabla Bwana hajampa ile adhabu alimpa mfano kwanza ambao ulimsaidia kuelewa kwa undani hisia ya Mungu juu yake kwa kile alichokifanya.

Hebu tusome kidogo,

2 Samweli 12:1 “Ndipo Bwana akamtuma Nathani aende kwa Daudi. Naye akamwendea, akamwambia, Palikuwa na watu wawili katika mji mmoja; mmoja wao alikuwa tajiri, wa pili maskini.

2 Yule tajiri alikuwa na kondoo na ng’ombe wengi sana;

3 bali yule maskini hakuwa na kitu, ila mwana kondoo mmoja, mdogo, ambaye amemnunua na kumlea; naye akakua pamoja naye, na pamoja na wanawe; hula sehemu ya posho lake, na kukinywea kikombe chake, na kulala kifuani mwake, akawa kwake kama binti.

4 Hata msafiri mmoja akamfikilia yule tajiri, naye akaacha kutwaa mmoja wa kondoo zake mwenyewe au mmoja wa ng’ombe zake mwenyewe, ili kumwandalia yule msafiri aliyemfikilia, bali alimnyang’anya yule maskini mwana-kondoo wake, akamwandalia yule mtu aliyemfikilia.

5 Ndipo hasira ya Daudi ikawaka sana juu ya mtu yule; akamwambia Nathani, Aishivyo Bwana, mtu huyo aliyetenda jambo hili, hakika yake astahili kufa;

6 naye atamrudishia yule mwana-kondoo mara nne, kwa sababu ametenda neno hili, na kwa sababu hakuwa na huruma.

7 Basi Nathani akamwambia Daudi, Wewe ndiwe mtu huyo. Bwana, Mungu wa Israeli, asema hivi, Nalikutia mafuta, uwe mfalme juu ya Israeli, nikakuokoa na mkono wa Sauli;

8 nami nikakupa nyumba ya bwana wako, na wake za bwana wako kifuani mwako; nikakupa nyumba ya Israeli na ya Yuda; na kama hayo yangalikuwa machache, ningalikuongezea mambo kadha wa kadha.

9 Kwa nini umelidharau neno la Bwana, na kufanya yaliyo mabaya machoni pake? Umempiga Uria, Mhiti, kwa upanga, nawe umemtwaa mkewe awe mke wako, nawe umemwua huyo kwa upanga wa wana wa Amoni.

10 Basi, sasa upanga hautaondoka nyumbani mwako, kwa sababu umenidharau, ukamtwaa mkewe Uria, Mhiti, kuwa mke wako.

11 Bwana asema hivi, Angalia, nitakuondokeshea uovu katika nyumba yako, nami nitawatwaa wake zako mbele ya macho yako, na kumpa jirani yako, naye atalala na wake zako mbele ya jua hili.

12 Maana wewe ulifanya jambo lile kwa siri; bali mimi nitalifanya jambo hili mbele ya Israeli wote na mbele ya jua”.

Na sehemu nyingine nyingi katika biblia, agano la kale na agano jipya utaona Mungu anazungumza kwa mifano kufikisha ujumbe wake au hisia zake kwa watu wake.

Lakini pia Mungu wetu anatumia mifano kutuonyesha hisia zake pindi tunapotubu na kumgeukia yeye… Wengi wetu hatujui ni jinsi gani Mungu anavyohisi juu yetu, na anavyotuhurumia, hususani pale tunapoghairi maovu yetu na mabaya yetu na kugeukia haki, wengi tunadhani Mungu huwa hasamehi, na anakumbuka kumbuka makosa yetu mara kwa mara…Hebu chukua muda tafakari ule mfano wa mwana mpotevu, Bwana alioutoa katika Luka 15:11-32, utaona jinsi gani Huruma za Mungu jinsi zilivyo kuu kwetu pindi tunapotubu na kuacha maovu.

“Luka 15:20 Akaondoka, akaenda kwa babaye. Alipokuwa angali mbali, baba yake alimwona, akamwonea huruma, akaenda mbio akamwangukia shingoni, akambusu sana.

21 Yule mwana akamwambia, Baba, nimekosa juu ya mbingu na mbele yako; sistahili kuitwa mwana wako tena.

22 Lakini baba aliwaambia watumwa wake, Lileteni upesi vazi lililo bora, mkamvike; mtieni na pete kidoleni, na viatu miguuni;

23 mleteni ndama yule aliyenona mkamchinje; nasi tule na kufurahi;

24 kwa kuwa huyu mwanangu alikuwa amekufa, naye amefufuka; alikuwa amepotea, naye ameonekana. Wakaanza kushangilia.”

Vilevile Sio mifano tu, hata katika ishara Mungu anazungumza na watu wake, kasome kitabu cha Ezekieli mlango wa 4 na wa 5 na Isaya 20:3.

Sasa hebu tuitazame ishara ya mwisho ambao tutazidi kufahamu hisia ya Mungu juu yetu pindi tunapogeuka na kutubu.

Kama wewe ni msomi wa biblia utakuwa unaijua vizuri habari ile ya Nabii Yona, jinsi alivyoikimbia sauti ya Mungu na mwishowe kujikuta yupo katika tumbo la nyangumi siku tatu, na baadaye kulazimika kuitii sauti ya Mungu na kwenda kuwahubiria watu wa Ninawi..Na alipowahubiria biblia inasema walitubu na kuacha njia zao mbaya..Na kwa tendo lile Mungu aliwasamehe na kughairi kuwaangamiza…Lakini kitendo kile cha Mungu kuwasamehe hakikumpendeza Nabii Yona, kwani alitafakari mateso aliyoyapitia yote na shida zote zile mpaka za kukaa tumboni mwa samaki siku tatu, na mwishowe Mungu hafanyi chochote?..yeye alitamani watu wauawe…Lakini hisia za Mungu hazikuwa hizo..yeye aliwahurumia watu wake, lakini Yona hakujua ukubwa wa huruma na hisia za Mungu juu ya watu wa Ninawi mpaka Mungu alipozungumza naye tena kwa ishara nyingine ya Mtango.

Kwani alipokuwa amekaa kwa mbali autazame mji ukiangamizwa, Mungu aliuotesha mtango ambao uliota ndani ya siku moja, ukawa na matawi yenye uvuli, na kwasababu jua lilikuwa kali na Yona alikuwa na hasira na uchungu.. alipouona ule mtango akaenda kukaa chini yake, apate kivuli, na pengine pia ale matango mawili matatu asahahu shida zake, na alipozidiwa na burudani za mtango ule siku nzima, akasahau habari za Ninawi na kuangamizwa kwake.

Lakini biblia inasema siku ya pili yake alivyoamka mambo yalibadilika, ule mtango uliliwa na buu na jua ukaupiga ukakauka, Yona kuona vile akakasirika tena..Hasira yake ikarudi kama mwanzo..kwanini mtango umekauka ambao ndio uliokuwa unamfanya asahau shida zake na apunguze hasira zake.

Kwa tukio hilo Mungu akampa somo Yona…kama vile ule mtango ulivyomfanya asahau shida zake na hasira zake kwa uvuli tu wa matawi yake, pengine na kwa matunda yake yaliyouzaa ndani ya siku moja, na ukamfanya pia auhurumie ule mtango..(Yona 4)

Ni hivyo hivyo watu wa Ninawi kwa kutubu kwao ni kama mtango ulioota juu ya kichwa cha Mungu, ambapo hapo kwanza Mungu aliwakasirikia watu wa Ninawi kwa maovu yao, lakini walipotubu na kuacha njia zao mbaya ni kama mtango ulioota juu ya kichwa cha Mungu, ukampa utulivu ndani ya moyo wake, na kumfanya asahau na kughairi mabaya aliyopanga kuwaletea watu wa Ninawi.

Hivyo kila siku tunapoghairi mabaya yetu, ndipo matawi yetu mbele za Mungu wetu yanavyoongezeka, na tunapozidi na kuzidi kuwa wasafi na hata kufikia hatua ya kuzaa matunda ndipo tunapomfanya Mungu wetu aburudike na kusahau mabaya yetu yote…Lakini tunapozidisha uovu, ni tunayapunguza wenyewe matawi yetu na hivyo dhambi zetu zinafika kwake na kumghadhibisha…

Hivyo Mungu wetu anatupenda na kutuhurumia…kuna uhusiano mkubwa sana wa matendo yetu na hisia za Mungu wetu..hivyo tujitahidi kuupendeza moyo wake ndipo tutakapata mema…kila siku tujisafishe, kama tulikuwa tumeacha matusi lakini bado vitabia vidogo vidogo vya ugomvi, vinatutawala tuvisafishe na hivyo..ndivyo tunavyozidi kujiepusha na hasira ya Mungu.

Mungu wetu anatupenda, Mungu wetu anatuhurumia na bado tunayo nafasi kubwa kwake.

Bwana akubariki.

Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema, na pia kama utapenda tuwe tunakutumia masomo haya kwa njia ya email yako au Whatsapp tutumie ujumbe kwenye box la maoni chini au piga namba hii +255 789001312


Mada Nyinginezo:

KUTUBU SIO KUOMBA REHEMA.

TAHADHARI YA NEEMA YA MUNGU.

USITUPE LULU ZAKO MBELE YA NGURUWE.

BASI TUENDELEE KUMJUA MUNGU,NAYE ATATUJILIA KAMA MVUA YA VULI.

TUMTOLEE MUNGU VILE VINAVYOTUGHARIMU ZAIDI.

Zile mbao mbili za mawe Musa alizoambiwa achonge zilikuwaje?

Rudi Nyumbani:

Print this post

About the author

Admin administrator

Subscribe
Notify of
guest
0 Comments
Inline Feedbacks
View all comments