Title Devis

Maana ya Mithali 25:25 Kama vile maji ya baridi kwa mtu mwenye kiu 

SWALI: Nini maana ya

Mithali 25:25 Kama vile maji ya baridi kwa mtu mwenye kiu, Ndivyo ilivyo habari njema itokayo katika nchi ya mbali.

JIBU: Biblia inalinganisha burudiko kubwa mtu analolipata pale anaposikia habari fulani njema na mfano wa mtu mwenye kiu halafu ghafla akaletewa kikombe cha maji ya baridi, sasa katika mazingira kama hayo ni wazi kuwa maji yale atayafurahia sana kwasababu yupo katika kiu.

lakini kiini cha mstari huo ni hapo anaposema ni habari njema ITOKAYO KATIKA NCHI YA MBALI.

Tukumbuke kuwa zipo habari njema nyingi..kwamfano habari za kupewa tenda fulani ya kibiashara ni habari njema, habari za kufaulu darasani ni habari njema, habari za kuzaliwa mtoto duniani ni habari njema, habari za kupandishwa cheo ni habari njema n.k…lakini zote hizi hazina jipya kwasababu ni za hapa hapa tu duniani.

Bali zipo habari njema zinazotoka katika nchi ya mbali na huko si kwingine zaidi ya MBINGUNI, hizo ndizo watu wana kiu nazo, wakizisikia tu ni lazima mioyo yao ni lazima iburudike sana.

Na habari zenyewe ni zile zinazomuhusu  Yesu Kristo.

Alisema.

Yohana 6:33-35

[33]Kwa maana chakula cha Mungu ni kile kishukacho kutoka mbinguni na kuupa ulimwengu uzima.

[34]Basi wakamwambia, Bwana, sikuzote utupe chakula hiki. 

[35]Yesu akawaambia, Mimi ndimi chakula cha uzima; yeye ajaye kwangu hataona njaa kabisa, naye aniaminiye hataona kiu kamwe.

Yesu ndio maji yakatao kiu, alileta habari njema iliyotoka mbinguni, alikuja kutuletea ukombozi na msamaha wa dhambi, alikuja kutufungua katika vifungo vyetu, na shida zetu mbalimbali, na kutumwagia karama za rohoni, mambo ambayo mwingine yoyote hawezi kutoa. Lakini zaidi sana alikuja kutuambia habari za ufalme wake, kwa habari ya mambo yanayokuja, kuhusu mbingu mpya na nchi mpya, na Yerusalemu mpya, na umilele, na uzuri na thawabu alizotuandalia sisi tuliomwamini. Mambo ambayo ukisikia kama wewe unapenda kweli maisha…utayafurahia sana.

hivyo yatupasa mimi na wewe tuwe na mwitikio huu, wa habari hizi njema kwa kuwashuhudia pia na wengine maji haya, kwasababu ni wazi kuwa wengi wana kiu, na hivyo wanahaja ya kuzisikia hizi habari njema zimuhusuyo Yesu Kristo.

Sote kwa pamoja tuamke tukahubiri injili. Tukijua kuwa inahitajiwa sana.

shalom

Washirikishe na wengine habari hizi njema kwa kushea

Ikiwa utapenda kupata msaada wa kumpokea Yesu maishani mwako bure, Basi wasiliana nasi kwa namba uzionazo chini ya makala hii.

Pia kwa kupokea mafundisho ya kila siku kwa njia ya WHATSAPP, jiunge na channel yetu kwa kupofya link hii >> https://whatsapp.com/channel/0029VaBVhuA3WHTbKoz8jx1

Kwa mawasiliano: +255789001312 au +255693036618

Bwana akubariki.

Mafundisho mengine:

INJILI NI NINI?

Maana ya Mithali 17:22 Moyo uliochangamka ni dawa nzuri;

KAMA UNAPENDA MAISHA, NA KUTAKA SIKU YAKO IWE NJEMA.

Rudi Nyumbani

Print this post

Je! mtu anaweza kumbariki Mungu au kulibariki jina lake?

Swali: Tumekuwa tukisikia na kuona watu wakisema “Tunalibariki jina la Mungu” na wengine wanasema “tunambariki Mungu”.. Je mtu anaweza kubariki Mungu au jina lake?..au ni Mungu ndiye anayeweza kumbariki mtu na kulibariki jina la mtu?


Jibu: Mungu anaweza kulibariki jina la mtu na vile vile mtu anaweza kulibariki jina la MUNGU. Isipokuwa tafsiri ya neno “baraka” ndiyo inayoleta ukinzani kwetu!.

Neno “Baraka” maana yake ni “kukiongezea kitu au mtu thamani, au heshima au fursa” ambacho hakikuwa nacho au hakuwa nayo!… Na thamani hiyo/heshima hiyo inaweza kuwa ni zawadi, au nafasi, au hadhi.

Mtu anapompa mwingine zawadi, tafsiri yake ni kwamba “amembariki mtu yule” vile vile mtu anapompa mtu mwingine heshima ya juu au fursa ya juu “maana yake amembariki mtu yule”.

Vile vile na sisi Mungu anaweza kutupa fursa, au heshima au zawadi ya jambo Fulani tulitendalo..Na sisi pia tunaweza kumpa heshima Mungu wetu, au fursa au zawadi kwa jambo Fulani atutendealo,…sasa kitendo hicho cha kumheshimu Mungu kwa kumpa kitu Fulani, ndicho kinachoitwa KUMBARIKI BWANA.

Na zawadi kubwa ambayo tunaweza kumpa MUNGU ikawa ni Baraka kwake ni Maisha yetu, pamoja na SIFA za midomo yetu.

Pengine utauliza ni wapi katika maandiko watu walimbariki Bwana…

2Nyakati 20:25 “Nao Yehoshafati na watu wake walipokuja kuchukua nyara zao, wakaona kati yao wingi wa mali, na mavazi, na johari za thamani, walivyojivulia, zaidi kuliko wawezavyo kuchukua; wakawa siku tatu katika kuteka nyara, maana zilikuwa nyingi sana.

26 Hata siku ya nne wakakusanyika katika bonde la baraka; MAANA NDIPO WALIPOMBARIKIA BWANA; kwa hiyo jina lake mahali pale pakaitwa Bonde la Baraka hata leo”.

Umeona hapo mstari wa 26, biblia inasema “MAANA NDIPO WALIPOMBARIKIA BWANA”..Na walimbaki kwa njia gani??… si nyingine Zaidi ya SIFA…

2Nyakati 20:18 “Yehoshafati akainama kichwa, kifulifuli; wakaanguka mbele za Bwana Yuda wote na wakaao Yerusalemu, wakimsujudia Bwana.

19 Na Walawi, wa wana wa Wakohathi na wa wana wa Wakorahi, wakasimama ili wamsifu Bwana, Mungu wa Israeli, KWA SAUTI KUU SANA”.

Na pia katika Zaburi ya 63 tunazidi kulithibitisha hilo…

Zaburi 63:3 “Maana fadhili zako ni njema kuliko uhai; Midomo yangu itakusifu.

4 NDIVYO NITAKAVYOKUBARIKI MAADAMU NI HAI; Kwa jina lako nitaiinua mikono yangu.”

Kwahiyo SIFA, tuimbazo ikiwa tunaziimba katika roho na kweli basi zinalibariki jina lake..utalisoma hilo Zaidi katika Zaburi ile  ya 96 na Ayubu 1:21.

Zaburi 96:1 “Mwimbieni Bwana wimbo mpya, Mwimbieni Bwana, nchi yote.

2 Mwimbieni Bwana, LIBARIKINI JINA LAKE, Tangazeni wokovu wake siku kwa siku”.

Ila kumbuka jambo moja!.. Wewe au Mimi tusipolibariki jina la Mungu kwa kumpa yeye utukufu kwa vinywa vyetu au maisha yetu.. hatumpunguzii chochote, kwani anao mabilioni ya Malaika mbinguni wanaomsifu… Zaidi sana ni kwa hasara yetu wenyewe!!.. YEYE DAIMA ATABAKI KUWA MUNGU, NA WA KUABUDIWA, NA KUPEWA UTUKUFU  HATA PASIPO SISI!!.

2Timotheo 2:12 “Kama tukistahimili, tutamiliki pamoja naye; Kama tukimkana yeye, yeye naye atatukana sisi;

13  KAMA SISI HATUAMINI, YEYE HUDUMU WA KUAMINIWA. Kwa maana hawezi kujikana mwenyewe”.

Bwana atubariki.

Maran atha!

Washirikishe na wengine habari hizi njema kwa kushea

Ikiwa utapenda kupata msaada wa kumpokea Yesu maishani mwako bure, Basi wasiliana nasi kwa namba uzionazo chini ya makala hii.

Pia kwa kupokea mafundisho ya kila siku kwa njia ya WHATSAPP, jiunge na channel yetu kwa kupofya link hii >> https://whatsapp.com/channel/0029VaBVhuA3WHTbKoz8jx1

Kwa mawasiliano: +255789001312 au +255693036618

Bwana akubariki.

Mafundisho mengine:

JINA LAKO NI LA NANI?

Je Mungu anaweza kumdanganya mtu?

Je shetani anaweza kushusha moto kutoka mbinguni?

Tofauti ya kazi ya Damu ya Yesu na Jina la Yesu ni ipi?

JE! UMEBATIZWA UBATIZO SAHIHI?

Rudi Nyumbani

Print this post

Nini maana ya ufalme wa Mungu hauwi katika neno bali katika nguvu?(1Wakorintho 4:20).

Swali: Je, Mtume Paulo alimaanisha Nini kusema Maana ufalme wa Mungu hauwi katika neno Bali katika nguvu?.


Jibu: Turejee mstari huo..

1 Wakorintho 4:20 “Maana ufalme wa Mungu hauwi katika neno, bali katika nguvu”.

Hapo anaposema kuwa Ufalme wa Mungu hauwi katika “neno” hamaanishi “Neno la Mungu”...kwasababu Ufalme wa Mbinguni unajengwa na NENO LA MUNGU kama nguzo ya msingi…na pasipo hilo hakuna ufalme wa Mungu…kinyume chake ni ufalme wa giza unajengwa.

Hivyo biblia inaposema ufalme wa Mungu hauwi katika neno, inamaanisha kuwa hauwi katika “MANENO MATUPU YASIYO NA NGUVU ZA MUNGU”...Bali unakuwa katika maneno yenye nguvu za Mungu.

Maana yake ishara na miujiza inafuatana na Neno la Ufalme…

Mtume Paulo kwa ufunuo wa Roho alizidi kuliweka hilo vizuri katika 1Wathesalonike 1:5.

1 Wathesalonike 1:5 “ya kwamba injili yetu haikuwafikia katika MANENO TU, bali na KATIKA NGUVU, na KATIKA ROHO MTAKATIFU, na uthibitifu mwingi; kama vile mnavyojua jinsi zilivyokuwa tabia zetu kwenu, kwa ajili yenu”.

Vile vile na sisi tunapaswa tuhubiri injili isiyo ya maneno matupu au yenye ushawishi wa maneno ili kuvuta watu… bali yenye dalili na udhihirisho wa Roho.

Maana yake ishara na miujiza vifuatane nasi…Na muujiza wa kwanza ni watu kutubu dhambi kwa kumaanisha kuziacha…

1 Wakorintho 2:4 “Na neno langu na kuhubiri kwangu hakukuwa kwa maneno ya hekima yenye kushawishi akili za watu, bali kwa dalili za Roho na za nguvu”.

Bwana atusaidie.

Washirikishe na wengine habari hizi njema kwa kushea

Ikiwa utapenda kupata msaada wa kumpokea Yesu maishani mwako bure, Basi wasiliana nasi kwa namba uzionazo chini ya makala hii.

Pia kwa kupokea mafundisho ya kila siku kwa njia ya WHATSAPP, jiunge na channel yetu kwa kupofya link hii >https://whatsapp.com/channel/0029VaBVhuA3WHTbKoz8jx10

Kwa mawasiliano: +255789001312 au +255693036618

Bwana akubariki.

Mafundisho mengine:

Rudi Nyumbani

Print this post

AINA TATU ZA IBADA ZA SANAMU.

Jina la Bwana na Mwokozi wetu YESU KRISTO libarikiwe, karibu tujifunze biblia Neno la Mungu wetu, lililo Taa ya njia zetu na Mwanga wa njia yetu (Zab. 119:105).

Zipo aina tatu (3) za sanamu zinazoabudiwa na watu.

1.Sanamu zenye mfano wa Mtu

2.Sanamu-watu

3.Sanamu-vitu

Tutazame moja baada ya nyingine.

      1.SANAMU ZENYE MFANO WA MTU.

Hivi ni vitu vyote visivyo na uhai vyenye mfano wa mtu, ambavyo vinatengenezwa na watu kwa lengo la kuabudiwa.

Tabia ya hizi sanamu kulingana na biblia ni kwamba zina midomo lakini hazisemi, zina macho lakini hazioni, zina masikio lakini hazisikii, zina pua lakini hazinusi..na wanaoziabudu wanafanana na hizo kiroho.

Zaburi 115:4 “Sanamu zao ni fedha na dhahabu, Kazi ya mikono ya wanadamu.

5 Zina vinywa lakini hazisemi, Zina macho lakini hazioni,

6 Zina masikio lakini hazisikii, Zina pua lakini hazisikii harufu,

7 Mikono lakini hazishiki, miguu lakini haziendi, Wala hazitoi sauti kwa koo zake.

8 Wazifanyao watafanana nazo, Kila mmoja anayezitumainia”

Hizi ndio zile zote zinazoabudiwa na wapagani, pamoja na baadhi ya madhehebu yajiitayo ya kikristo. Utakuta sanamu imewekwa ndani ya nyumba ya ibada, na watu wanakwenda kuiangukia na kuisujudia, hata kuitolea sadaka na kuiomba, jambo ambalo ni machukizo makubwa..

Ni dhambi kubwa kusujudia sanamu yoyote ile, Kasome Kutoka 20:1-6.

2. SANAMU-WATU.

Hii ni aina  ya pili ya sanamu ambayo ni tofauti kidogo na ile ya kwanza… ile ya kwanza ina midomo lakini haisemi, ina macho lakini haioni, ina masikio lakini haisikii…. Hii ya pili nayo ni hivyo hivyo, ina macho lakini haioni, ina masikio lakini haisikii, ina macho lakini haioni..tofauti tu ni kwamba ile ya kwanza ile ya kwanza haipumui ila hii ya pili inapumua, ile ya kwanza imetengenezwa kwa miti, udongo, chuma, fedha au dhahabu lakini hii ya pili ni Wanadamu.

Sasa tunaisoma wapi katika biblia…

Ezekieli 12: 1 “Neno la Bwana likanijia tena, kusema,

2 Mwanadamu, wewe unakaa kati ya nyumba iliyoasi, WATU AMBAO WANA MACHO YA KUONA, ILA HAWAONI, WANA MASIKIO YA KUSIKIA, ILA HAWASIKII; kwa maana ni nyumba iliyoasi”.

Umeona? Kumbe sanamu sio tu mawe na udongo vinavyoweza kuwa sanamu bali hata watu..

Kama hujamaanisha kumfuata YESU wewe ni SANAMU.. Kwasababu una macho lakini huoni mambo ya rohoni, una masikio lakini husikii sauti ya MUNGU, Una kinywa lakini hakineni mambo ya Mungu, Hivyo wewe ni sanamu pamoja na viungo vyako vyote.

“KICHWA” chako ni sanamu/mungu wako, ndio maana unakitumikia kwa vitu vya kidunia kama YEZEBELI..

“MASIKIO” yako ni sanamu/mungu wako, ndio maana unayatumikia kwa kubadilisha vipuli kila siku.

“MACHO” yako ni sanamu/mungu wako, ndio maana unayatumikia usiku na mchana kupaka uwanja, na kupadilisha kope pamoja na kuchonga nyusi.

“MDOMO” wako ni sanamu/mungu wako, ndio maana unautumika kwa rangi na kila aina ya lipstick

“MIKONO” yako na “MIGUU” ni sanamu/mungu wako, ndio maana unaitumika kwa bangili na kucha za bandia..

“TUMBO” lako ni mungu wako ndio maana unalitumikia kwa kulinywesha pombe na kuliburudisha kwa kila linachohitaji usiku na mchana… Huna muda wa kufunga na kuomba walau kwa wiki mara moja, kwako kufunga ni adhabu kubwa!!..

Wafilipi 3:19  “mwisho wao ni uharibifu, MUNGU WAO NI TUMBO, utukufu wao u katika fedheha yao, waniao mambo ya duniani”.

Ikiwa hujamaanisha kumfuata YESU kila kiungo katika mwili wako ni sanamu/mungu.. Ndio maana biblia inasema tuvifishe viungo vyetu vilivyo katika nchi, maana kwa hivyo huzaa dhambi na NDIO ibada ya sanamu.

Wakolosai 3:5 “Basi, vifisheni viungo vyenu vilivyo katika nchi, uasherati, uchafu, tamaa mbaya, mawazo mabaya, na kutamani, ndiyo ibada ya sanamu;

6  kwa ajili ya mambo hayo huja ghadhabu ya Mungu”.

     3. SANAMU-VITU.

Hizi ni sanamu zote zisizo na mwonekano au maumbile ya mwanadamu lakni zinaabudiwa.

Mfano wa hizi ni kazi, fedha, umaarufu, Elimu, Mali kama nyumba, magari, ardhi n.k. Mtu akiwa na hivi na hana KRISTO maishani mwake ni mwabudu sanamu tu!

KUMBUKA: Usipomwabudu MUNGU  WA KWELI, basi unaabudu sanamu, na usipoabudu sanamu basi unamwabudu MUNGU WA KWELI, Hakunaga hapo katikati! Ni aidha uwe wa shetani au wa Mungu.

Kama kazi yako inaheshima kuliko Mungu kiasi kwamba unakosa hata siku moja ya wiki kumtolea Mungu wako, hiyo kazi ni sanamu/mungu kwako.

Kama elimu yako, au umaarufu wako au cheo chako kina nguvu kuliko Neno la MUNGU, basi hicho ulichonacho tayari ni mungu wako.

Je umeokoka?…Kumbuka wote wanaoabudu sanamu sehemu yao ni katika lilwe ziwa liwakalo moto na kiberiti kulingana na biblia.

Ufunuo 21:8 “Bali waoga, na wasioamini, na wachukizao, na wauaji, na wazinzi, na wachawi, NA HAO WAABUDUO SANAMU, na waongo wote, sehemu yao ni katika lile ziwa liwakalo moto na kiberiti. Hii ndiyo mauti ya pili”

Bwana akubariki.

Washirikishe na wengine habari hizi njema kwa kushea

Ikiwa utapenda kupata msaada wa kumpokea Yesu maishani mwako bure, Basi wasiliana nasi kwa namba uzionazo chini ya makala hii.

Pia kwa kupokea mafundisho ya kila siku kwa njia ya WHATSAPP, jiunge na channel yetu kwa kupofya link hii >> https://whatsapp.com/channel/0029VaBVhuA3WHTbKoz8jx1

Kwa mawasiliano: +255789001312 au +255693036618

Bwana akubariki.

Mafundisho mengine:

JIHADHARI NA UONGO WA SHETANI UNAOKARIBIANA NA UKWELI.

Biblia inamaanisha nini kusema Yeye aliye na sikio, na asikie?

USIMWABUDU SHETANI!

MAJARIBU MATANO (5) YA MKRISTO.

DANIELI: Mlango wa 3

Rudi Nyumbani

Print this post

Maana ya Mithali 17:22 Moyo uliochangamka ni dawa nzuri;

SWALI: Nini maana ya

Mithali 17:22 Moyo uliochangamka ni dawa nzuri; Bali roho iliyopondeka huikausha mifupa.


JIBU: Mstari huu unatuonyesha jinsi gani hali ya moyo inavyoweza kuathiri hali za nje za mwili. Si kila wakati dawa itatibu, ikiwa moyo umepondeka afya inaweza kuathiriwa pia. Kwamfano labda mtu yupo katika nyumba au makazi ambayo hana amani, anateswa, anaudhiwa, anaabishwa, muda wote anakuwa mnyonge, utaona pia kwa namna Fulani afya yake itaathirika, labda atasumbuliwa na ugonjwa Fulani ambao hauna sababu wala chanzo.

Lakini moyo ukichangamka, hata kama huyo mtu yupo katika hali/mazingira magumu kiasi gani, mwili wake pia baada ya mda utaitikia hali ya roho yake. Na hivyo atakuwa na afya yake.

Sasa Nitaufanyaje moyo wangu uchangamke?

1)    Kwa kutembea ndani ya ahadi za Mungu katika Neno lake. Mara kadhaa katika maandiko Bwana Yesu alisema” jipeni moyo”. Unapojipa moyo katika ahadi za Mungu ukijua kabisa, ni hakika atatenda,hasemi uongo, Fahamu kuwa utakuwa ni mwanzo wa kuchangamka kwako. Kwamfano ukikumbuka kuwa alisema hatatuacha wala kutupungukia, unakuwa na amani wakati wote, nyakati zote, ukiwa na vingi ukiwa umepungukiwa yote yatakuwa sawa tu, kwasababu sikuzote yupo pamoja na wewe. Furaha inakutawala.

Hata upitiapo magonjwa, ukikumbuka ahadi zake kuwa atakuponya, ukaendelea kuzishika kwa imani, afya yako hurejea.

Yeremia 30:17 Maana nitakurudishia afya, nami nitakuponya jeraha zako, asema Bwana, kwa sababu wamekuita, mwenye kutupwa, wakisema, Ni Sayuni, ambao hapana mtu autakaye. 

18 Bwana asema hivi, Tazama, nitarudisha tena hema za Yakobo zilizohamishwa, na kuyahurumia makao yake; nao mji huo utajengwa juu ya magofu yake wenyewe, nalo jumba litakaliwa, kama ilivyokuwa desturi yake. 

19 Tena kwao itasikiwa shukrani, na sauti yao WACHANGAMKAO; nami nitawazidisha, wala hawatakuwa wachache; tena nitawatukuza, wala hawatakuwa wanyonge.

Hivyo ishi kwa kushikilia ahadi za Mungu kwenye Neno lake, zipo nyingi sana, na zimefika katika kila Nyanja ya maisha yetu. Hakuna sababu ya kutochangamka, wakati Neno la ahadi lipo. Aliyekuahidia ni Mungu wa miungu muumba wa mbingu na nchi hakuna lolote linalomshinda, kwanini uogope?

2) Pili, kwa kupenda ushirika na wengine. Kamwe usiishushe wala kuipuuzia  nguvu iliyopo ndani ya ndugu katika Kristo. Zipo nyakati utahitaji kutiwa nguvu na wenzako, hata kukaa pamoja tu, kutafakari Neno la Mungu na kumwimbia Mungu ni tiba nzuri sana, itakayochangamsha moyo wako, tofauti na kama ungekuwa mwenyewe mwenyewe tu wakati wote.

Ndivyo ilivyokuwa hata kwa Paulo, wakati ule..

Matendo 28:15  Na kutoka huko ndugu, waliposikia habari zetu, wakaja kutulaki mpaka Soko la Apio na Mikahawa Mitatu. Paulo alipowaona alimshukuru Mungu, AKACHANGAMKA.

Chuma hunoa chuma, tuwapo pamoja, tunajengana nafsi, na matokeo ya kufanya hivyo yataonekana mpaka nje.

Bwana akubariki.

Washirikishe na wengine habari hizi njema kwa kushea

Ikiwa utapenda kupata msaada wa kumpokea Yesu maishani mwako bure, Basi wasiliana nasi kwa namba uzionazo chini ya makala hii.

Pia kwa kupokea mafundisho ya kila siku kwa njia ya WHATSAPP, jiunge na channel yetu kwa kupofya link hii >> https://whatsapp.com/channel/0029VaBVhuA3WHTbKoz8jx1

Kwa mawasiliano: +255789001312 au +255693036618

Bwana akubariki.

Mafundisho mengine:

PALE AHADI ZA MUNGU ZINAPOKUJARIBU.

JE! UNAIONA ILE NCHI NZURI YA KUMETA-META MBELE YAKO?

Je sisi wakristo tunaruhusiwa kufanya 40 za marehemu?

Rudi Nyumbani

Print this post

Maana ya Mithali 10:12 Kuchukiana huondokesha fitina

Elewa maana ya mstari huu;

Mithali 10:12 Kuchukiana huondokesha fitina; Bali kupendana husitiri makosa yote.

Mstari huu unalenga kutufundisha sifa za kipekee sana za upendo. Ambazo zinazungumziwa pia sehemu mbalimbali.

Kwamfano hapo anasema kuchukiana hakuzai kingine zaidi ya fitina,( yaani uchongezi, na kudhuriana), lakini upendano husitiri MAKOSA YOTE.  Anaposema yote. Ni kweli yote. Endapo upendo utatoka kwelikweli katika kilele chake. Hiyo ndio sifa ya ajabu ya upendo ambayo kitu kingine chochote chema hakiwezi kutoa, kwamfano imani, nguvu, mamlaka, uweza n.k. haviwezi kusitiri “makosa yote”. Ni upendo tu peke yake.

Neno hilo hilo pia limerudiwa katika agano jipya.

1Petro 4:8  Zaidi ya yote iweni na juhudi nyingi katika kupendana; kwa sababu upendano husitiri wingi wa dhambi

Ndio maana Bwana Yesu alisema Torati yote imelalia hapo, katika kumpenda mwenzako kama nafsi yako, alisema  vile unavyotaka wewe utendewe watendee wenzako. Utashangaa tu, wivu unayeyuka wenyewe, hasira inakufa, vinyongo vinaondoka, mashindano yanapotea, wizi, uzinzi unafutika, kwasababu umegundua kuwa mwenzako ni kama hiyo nafsi yako mwenyewe, kama vile wewe unavyopenda kufanikiwa vivyo hivyo usichukie kuona mwenzako amefanikiwa.

Lakini Jambo hili linaweza kutoka ndani yetu kwa njia tatu. Ya kwanza ni kujazwa Roho Mtakatifu.  Kwasababu tunda mojawapo la Roho Mtakatifu ni upendo (Wagalatia 5:22). Hivyo unapokuwa mwombaji sana, hususani wa “masaa” sio dakika, unajazwa Roho Mtakatifu vema. Na matokeo yake ni kuwa urahisi wa kuudhihirisha upendo unakuja.

Lakini hilo peke yake halitoshi, unapaswa  uambatanishe na usomaji  wa Neno kila siku. Neno ni njia nyingine ya Roho Mtakatifu kukukumbusha, yale unayopaswa kufanya, kwamfano ukidhihirisha hasira ukisoma Neno utajifunza uvumilivu, utajifunza unyenyekevu, kuachia, na madhara ya kutokusamehe. Hivyo litakufanya uweze kurejea  kwenye mstari haraka pale unapokaribia kuteleza. Usipuuzie kusoma Neno kila siku.

Tatu, ni kutendea kazi. Lazima ujiwekee malengo. Kwasababu ukiwa mwombaji tu, na msomaji peke yake bado  haitakusaidia sana , kama huna mikakati ya kukifanyia kazi. Ndio maana hapo anasema iweni na JUHUDI nyingi katika kupendana,.Juhudi ni lazima yaani unaanza kuchukua hatua ya kushindana na vipinga-upendo, na hapo hapo utaanza kuona, wepesi umekuja ndani yako,

Sisi kama watoto wa Mungu, tumeagizwa tukue kila siku kuufikia upendo wa ki-Mungu ndani yetu. Ndio ukomavu wetu na kilele cha imani yetu. Kwasababu hii ndio dawa ya dhambi zote.(2Petro 1:5-11)

Bwana atuongezee neema.

Shalom.

Washirikishe na wengine habari hizi njema kwa kushea

Ikiwa utapenda kupata msaada wa kumpokea Yesu maishani mwako bure, Basi wasiliana nasi kwa namba uzionazo chini ya makala hii.

Pia kwa kupokea mafundisho ya kila siku kwa njia ya WHATSAPP, jiunge na channel yetu kwa kupofya link hii >> https://whatsapp.com/channel/0029VaBVhuA3WHTbKoz8jx1

Kwa mawasiliano: +255789001312 au +255693036618

Bwana akubariki.

Mafundisho mengine:

Kuhubiri injili kwa husuda na fitina ndio kupi?

UMETEKWA NA UPENDO WA KRISTO?

UPENDO NI NINI NA JE! KUNA AINA NGAPI ZA UPENDO?

Rudi Nyumbani

Print this post

MALAIKA NI WALIMU WA SIFA KWETU, TUJIFUNZE KWAO!

Malaika watakatifu waliopo mbinguni, wanaompa Mungu utukufu usiku na mchana, ni WAALIMU wazuri wa SIFA, na KWAYA kwetu!.. Hao wamewekwa ili kutufundisha sisi namna ya kumwimbia Mungu katika viwango vya kimbinguni. Huenda wasitufundishe namna ya kuhubiri, lakini katika kusifa, wanayo mafunzo kwaajili yetu.

> FUNZO LA KWANZA: Wanajisitiri!.

Malaika wa Sifa, (yaani Maserafi na Makerubi) sehemu kubwa ya mbawa walizopewa wanazitumia kujisitiri.. na wanajisitiri kuanzia kichwani mpaka miguuni…wanaposimama mbele za MUNGU KUMPA UTUKUFU..

Isaya 6:1“Katika mwaka ule aliokufa mfalme Uzia nalimwona Bwana ameketi katika kiti cha enzi, kilicho juu sana na kuinuliwa sana, na pindo za vazi lake zikalijaza hekalu.

2 Juu yake walisimama maserafi; kila mmoja alikuwa na mabawa sita; KWA MAWILI ALIFUNIKA USO WAKE, NA KWA MAWILI ALIFUNIKA MIGUU YAKE, NA KWA MAWILI ALIRUKA”

Ikimaanisha kuwa kabla ya kupeleka sifa mbele za MUNGU aliyeziumba mbingu na nchi, kigezo cha kwanza ni KUJISITIRI!!. Lakini leo hii watu watasimama mbele za MUNGU kumwabudu na kumsifu, vifua vikiwa wazi, mgongo ukiwa wazi, mapaja yakiwa wazi, mauongo yakiwa wazi..na wanawake vichwa vikiwa wazi..

Swali la kujiuliza je ni nani amewafundisha hayo????.. kuabudu, na kusifu wakiwa nusu uchi, je wamefundishwa na nani?..na Malaika watakatifu wanaomwimbia Mungu au nani?..jibu rahisi ni kwamba wamefundishwa na shetani, na wanayempa sifa si MUNGU wa Mbinguni bali ni shetani wa duniani na kuzimu!.

> FUNZO LA PILI: Wanahubiri utakatifu.

Malaika wa Sifa mbinguni, (Maserafi na Makerubi) wanaonekana “wakiitana” (maana yake wakiambiana) Mtakatifu…Mtakatifu… Mtakatifu…

Na zingatia hili: si kwamba walikuwa wanamwambia Mungu, kwamba ni Mtakatifu!!.. la! Walikuwa wanaambiana wao!.. maana yake wanakumbushana wao kwa wao!, wanajitangazia na kuwatangazia wengine kuwa Bwana ni mtakatifu, hivyo “kila mmoja adumu katika huo utakatifu”..kwasababu Mungu ni mtakatifu na hakai katika uchafu..

Ufunuo 6:3 “Wakaitana, kila mmoja na mwenzake, wakisema, Mtakatifu, Mtakatifu, Mtakatifu, ni Bwana wa majeshi; dunia yote imejaa utukufu wake”.

Huo ndio wimbo wa MALAIKA mbinguni usiku na mchana!!… UTAKATIFU, UTAKATIFU, UTAKATIFU…

Na ndizo zinazopasa kuwa NYIMBO za watakatifu waliopo duniani… Sio kumwambia Mungu MTAKATIFU!!, Kana kwamba tunampa taarifa asiyoijua!!… yeye tayari ni mtakatifu na atabaki kuwa hivyo daima… bali tunapaswa tujikumbushe na kujitangazia sisi kuwa MUNGU NI MTAKATIFU, NA HIVYO TUZIDI KUJITAKASA… SIFA ZA NAMNA HIYO NDIZO ZINAZOMPENDEZA MUNGU!!..

Na sio mtu unaimba huku una mambo mengine ya kando kando!!.. sio unaimba huku unaishi na mke/mume ambaye si wako, sio unaabudu na kuimba kwaya huku ni mzinzi na mwabudu sanamu na unafanya mambo mengine yaliyo machukizo.

Neno la Mungu linasema pasipo huo utakatifu, hakuna mtu atakayemwona MUNGU…

Waebrania 12:14 “Tafuteni kwa bidii kuwa na amani na watu wote, NA HUO UTAKATIFU, ambao hapana mtu atakayemwona Bwana asipokuwa nao”.

Nyimbo au Mahubiri yasiyohubiri utakatifu ni “Ngojera za ibilisi:”.. zinazotoa thawabu za kishetani, haihitaji kuwa mchawi ndio uwe wa shetani… kumwimbia tu ibilisi tayari wewe ni wake!..kuhubiri huku unasifia na kuzitenda dhambi wewe ni wa shetani.

Kama una karama ya uimbaji acha usanii, kazi ya MUNGU lebo!!, si brand! Ni huduma..kwahiyo usijitengeneze na kuwa mfano wa wasanii wa kidunia ambao wamepewa lebo na brandy na shetani ili wafanye mapenzi yake. (Hao wanahitaji kusaidiwa waokoke, na sio kuigwa).

Ukiamua kumwimbia MTAKATIFU aliye juu, VAA NGUO KAMILI!!!, HUBIRI UTAKATIFU, ISHI UTAKATIFU..

BWANA ATUSAIDIE!

Maran atha!

Washirikishe na wengine habari hizi njema kwa kushea

Ikiwa utapenda kupata msaada wa kumpokea Yesu maishani mwako bure, Basi wasiliana nasi kwa namba uzionazo chini ya makala hii.

Pia kwa kupokea mafundisho ya kila siku kwa njia ya WHATSAPP, jiunge na channel yetu kwa kupofya link hii >> https://whatsapp.com/channel/0029VaBVhuA3WHTbKoz8jx1

Kwa mawasiliano: +255789001312 au +255693036618

Bwana akubariki.

Mafundisho mengine:

NIONDOLEENI KELELE ZA NYIMBO ZENU (Amosi 5:23)

MAKABURI YAKAFUNUKA; IKAINUKA MIILI MINGI YA WATAKATIFU WALIOLALA;

NJIA KUU YA KUINGIA KATIKA ULE MJI.

TAFUTA KWA BIDII KUWA MTAKATIFU.

UTUKUFU WA MUNGU NI KITU GANI?

Rudi Nyumbani

Print this post

Nardo ni nini? (Yohana 12:3)

Jibu: Turejee..

Yohana 12:3 “Basi Mariamu akatwaa ratli ya marhamu ya NARDO SAFI yenye thamani nyingi, akampaka Yesu miguu, akamfuta miguu kwa nywele zake. Nayo nyumba pia ikajaa harufu ya marhamu.

4  Basi Yuda Iskariote, mmojawapo wa wanafunzi wake, ambaye ndiye atakaye kumsaliti, akasema,

5  Mbona marhamu hii haikuuzwa kwa DINARI MIA TATU, wakapewa maskini”

“Nardo” ni jamii ya mmea mdogo ujulikanao kama “Nardostachys”. Mmea huu hutoa maua madogo ya rangi ya “Pinki” (Tazama picha juu), na vijimatunda vidogo vyeusi ambavyo ndivyo chanzo cha mafuta aina ya “Nardo” yanayotumika kutengenezea madawa ya asili pamoja na marhamu (yaani Perfumes/pafyumu) iliyo ya gharama kubwa kuliko nyingine nyingi.

marhamu ya Nardo

Pafyumu iliyotengenezwa kwa “Nardo”, ilikuwa ni ya gharama kubwa na hata sasa ni ya gharama kubwa kutokana na upatikanani wa mimea hiyo.

Mimea ya Nardostachy, inapatikana katika safu za milima ya Himalaya, iliyopo nchini Nepali, na sehemu chache za “nchi ya India” pamoja na “Uchina”.  Na inamea kuanzia kwenye kimo cha Mita 3,000 mpaka mita 5,000 kutoka katika usawa wa bahari (Mita 5,000 ni karibia na kimo cha Mlima Kilimanjaro).. Hivyo upatikanaji wake ni mgumu sana, kutokana na sehemu chache unazomea na kimo unapopatikana!.

Kutokana na sababu hizo, ndizo zinazoifanya Marhamu ya Nardo kuwa ya gharama. Mpaka hapo tutakuwa tumeshafahamu kuwa ile Marhamu yule mwanamke aliyompaka Bwana iliagizwa kutoka mbali sana (maana yake nje ya Israeli) na ilikuwa ya gharama sana… Dinari 300 ni sawa na shilingi Milioni 6 za kitanzania.

Mistari mingine inayozungumzia Marhamu ya Nardo ni pamoja na Wimbo ulio bora 1:12, na 4:13-14

Sasa kufahamu kwa urefu ni nini tunajifunza kupitia tukio la mwanamke yule kukivunja kile kibweta fungua hapa >>AKAKIVUNJA KIBWETA AKAIMIMINA KICHWANI PAKE.

Bwana akubariki.

Washirikishe na wengine habari hizi njema kwa kushea

Ikiwa utapenda kupata msaada wa kumpokea Yesu maishani mwako bure, Basi wasiliana nasi kwa namba uzionazo chini ya makala hii.

Pia kwa kupokea mafundisho ya kila siku kwa njia ya WHATSAPP, jiunge na channel yetu kwa kupofya link hii >> https://whatsapp.com/channel/0029VaBVhuA3WHTbKoz8jx1

Kwa mawasiliano: +255789001312 au +255693036618

Bwana akubariki.

Mafundisho mengine:

AKAZIDI KUENDELEA KATIKA HEKIMA NA KIMO.

Marhamu ni nini? Na Manukato ni nini?

Biblia inamaana gani iliposema “Dhambi ilipozidi, Neema ilizidi kuwa nyingi Zaidi”.

GHARAMA YA UFALME WA MBINGUNI.

SI KILA KILICHO HALALI KINAFAA.

Rudi Nyumbani

Print this post

Kimiami ni nini? (Wimbo ulio bora 2:9).

Jibu: Turejee,

Wimbo 2:9 “Mpendwa wangu ni kama paa, au ayala. Tazama, asimama nyuma ya ukuta wetu, Achungulia dirishani, atazama kimiani”.

“Kimiami” ni dirisha kubwa lililo katika “ghorofa”..

Madirisha makubwa yaliyo katika maghorofa tofauti na yale yaliyo katika nyumba za chini ndiyo yaliyoitwa “kimiami”.

Mfano wa dirisha la Kimiami ni lile ambalo mfalme Ahazia aliloanguka na kuugua..

2Wafalme 1:2 “Na Ahazia AKAANGUKA KATIKA DIRISHA la chumba chake orofani, katika Samaria, akaugua; akatuma wajumbe, akawaambia, Enendeni mkaulize kwa Baal-zebubu, mungu wa Ekroni, kwamba nitapona ugonjwa huu”.

Na lile ambalo Yezebeli alianguka, baada ya kuangushwa na wale matowashi..

2Wafalme 9:30 “Hata Yehu alipofika Yezreeli, Yezebeli akapata habari; akatia uwanja machoni mwake, akapamba kichwa chake, akachungulia dirishani.

31 Hata Yehu alipoingia lango la mji, alisema, Je! Ni amani, Ewe Zimri, mwenye kumwua bwana wako?  32 AKAINUA USO WAKE KULIELEKEA DIRISHA, akasema, Aliye upande wangu ni nani? Matowashi wawili watatu wakachungulia.

33 Akasema, Mtupeni chini. Basi wakamtupa chini; na damu yake ikamwagika nyingine juu ya ukuta, na nyingine juu ya farasi, naye akamkanyaga-kanyaga”.

Tazama pia shubaka hapa >>>Shubaka ni nini kibiblia? (Mithali 7:6) 

Bwana akubariki.

Washirikishe na wengine habari hizi njema kwa kushea

Ikiwa utapenda kupata msaada wa kumpokea Yesu maishani mwako bure, Basi wasiliana nasi kwa namba uzionazo chini ya makala hii.

Pia kwa kupokea mafundisho ya kila siku kwa njia ya WHATSAPP, jiunge na channel yetu kwa kupofya link hii >> https://whatsapp.com/channel/0029VaBVhuA3WHTbKoz8jx1

Kwa mawasiliano: +255789001312 au +255693036618

Bwana akubariki.

Mafundisho mengine:

TOA HUDUMA ILIYO BORA.

INGIENI KWA KUPITIA MLANGO ULIO MWEMBAMBA.

KUTII NI BORA KULIKO DHABIHU.

VITABU VYA BIBLIA: Sehemu ya 11 (Mithali, Wimbo ulio bora, Mhubiri)

MUNGU HAJARIBIWI NA MAOVU BALI MEMA.

Rudi Nyumbani

Print this post

MAMBO YA KUJIFUNZA KATIKA KITABU CHA MATHAYO.

(Hotuba za Yesu)

Kitabu cha Mathayo ni moja ya vitabu vinne (4), vya injili. Yapo mambo mengi ya kujifunza ndani yake, lakini katika makala hii, tutaona mambo muhimu ya kufahamu ambayo yatakusaidia katika usomaji wako.

Tukiachia mbali matukio, na huduma mbalimbali ikiwemo za uponyaji alizozifanya Yesu. Tunafahamu kuwa Bwana “ALIFUNDISHA” pia. Na hapa ndipo kiini cha kujifunza kwetu.

Hivyo katika kufundisha kwake, kuligawanyika mara mbili. Kuna taarifa ambazo alizotoa bila kutolea maelezo mengi, lakini pia kuna taarifa alizitoa kama hotuba.

Sasa tutaangazia hizo HOTUBA, ambazo zimerekodiwa kwenye kitabu hichi.

Zipo tano (5), Nazo ni

  1. Hotuba ya Mlimani. (Mathayo 5-7)
  2. Hotuba ya utume (Mathayo 10)
  3. Hotuba ya ufalme wa mbinguni (Mathayo 13)
  4. Hotuba ya kanisa (Mathayo 18)
  5. Hotuba ya siku za mwisho (Mathayo 24)

Kabla ya kuziangalia kwa upana kidogo. Tufahamu kwanza hapo tusemapo “hotuba” tunamaanisha nini.

Hotuba ni mahubiri/mafundisho aliyoyasema Yesu kwa upana, yaliyolenga mada Fulani maalumu.

Ni mazungumzo marefu ya Bwana Yesu. kukazia jambo lile lile moja. Sasa embu Tuangalie kiini cha kila hotuba.

1) Hotuba ya mlimani. (Mwenendo wa Mkristo)

Hii tunaisoma katika sura ile ya 5,6,7. Ni wakati ambapo Bwana Yesu alipanda mlimani, kisha wanafunzi wake wakamfuata, akaanza kuwafundisha mambo mengi. Sasa kiini cha hotuba hii, kilikuwa ni kuwafundisha mwenendo sahihi wa Mkristo, unaokubaliwa na Mungu.

Anaanza kwa kusema HERI, HERI, HERI, maskini wa roho, wapole, wenye rehema, wapatanishi, wenye moyo safi, wenye kiu na njaa ya haki, n.k. anaendelea jinsi tunapavyopaswa tuwapende maadui, tusamehe, tusilipize kisasi, akafundisha usahihi wa kuomba, kufunga, kutoa sadaka, usafi wa moyo, na upendo, na mambo mengine kadha wa kadha.

Ni maneno ambayo kama wewe ni mwamini basi unapaswa uyasome na kuyatafakari kila inapoitwa leo. Kwasababu Huu ndio uliokuwa mwenendo wa Yesu duniani. Akahesabiwa kumpendeza Mungu kabla hata hajaanza huduma yake ya kuhubiri, kwasababu aliishi aliyokuwa anayasema. Hivyo siri iliyopo hapa ni kwamba alikuwa anasema mwenendo wa maisha yake yalivyokuwa.

Na sisi pia tukitaka tufanane, na Kristo kimwenendo na tabia, basi tuzingatie sana, kuyaaishi haya tunayoyasoma katika sura hizi tatu yaani 5,6,7, Ni muhimu sana, sio kuimba “natamani kufanana na wewe”, lakini hatujui tunafananaje na yeye.

2) Hotuba ya Utume (Mathayo 10)

Katika mahubiri haya, Bwana Yesu aliwaita wanafunzi wake na kuanza, kuwapa maelezo ya namna ya kuhubiri kule atakapowatuma. Akawaeleza kwa upana jinsi mazingira ya kuhubiri yalivyo, kwamba kuna mahali pia hawatakubalika, akawafundisha pia jinsi ya kuhubiri, akawaondoa hofu ya wanadamu, na hofu ya kusumbukia mahitaji kwamba huko huko mbele ya safari Bwana atakuwa nao, akawafundisha pia mahali pa kuanzia kuhubiri, akawafundisha hekima ya kuhubiri, na kuponya watu. Na mambo mengine kadha wa kadha.

Kiasi kwamba, wewe kama mtendakazi katika shamba la Bwana ukisoma habari hizi, zitakusaidia katika ustahimilivu wako shambani mwa Bwana, tukikumbuka kuwa kila mmoja wetu ameitwa na Bwana kwenda kuwafanya wengine kuwa wanafunzi. Hivyo, Usomapo habari hii ya kitume, itakusaidia kunoa vema utumishi wako, katika eneo la upelekaji kazi ya Mungu mbali. Pata nafasi pitia wewe mwenyewe kwa utulivu sura yote ya kumi. Bwana atakupa kuelewa mengi ndani yake. Na hivyo utakuwa mtume, kama mitume wako walivyokuwa.

3) Hotuba ya ufalme wa mbinguni (Mathayo 13)

Hii ni hotuba, iliyohusu siri za ufalme wa Mbingu. Ambapo Bwana Yesu alitumia mifano (mafumbo), kuulezea. Biblia inaposema ufalme wa mbinguni, inamlenga YESU mwenyewe, na kazi yake aliyokuja kuifanya duniani (Luka 4:18-19).

Katika sura hii ya 13, alieleza mifano mikuu saba (7), japokuwa kulikuwa na mengine aliyokuwa iliyohusu ufalme wa mbinguni isipokuwa haijarekodiwa katika kitabu hichi. Mfano wa kwanza ulikuwa ni wa mpanzi, kisha magugu na ngano, kisha chembe ya haradali, kisha chachu katika unga, kisha hazina iliyositirika katika shamba, kisha mfano wa mfanyabiashara na lulu, na juya lililotupwa baharini.

Katika mifano hii yote, maudhui ni kuonyesha ukubwa ulio ndani ya Kristo Yesu, pale mtu anapomwamini na kustahimili kumfuata ukweli ni kwamba ataanza kama chenye ya haradali, lakini ataishia mti mkubwa, ni kama aliyepata hazina na lulu kubwa sana, akaenda kuuza akawa tajiri,.

Hivyo usomapo kwa makini mifano hii, utakuwa na kila sababu ya kuutafuta sana ufalme wa Mungu (yaani Kumuhufadhi Kristo sana moyoni mwako). Kwasababu unajua ulichokitapata ni zaidi ya vitu vyote duniani. Ambavyo utakuja kuvifurahia vema uendapo kule ng’ambo mbinguni.

4) Hotuba ya kanisa (Mathayo 18)

Hotuba hii inalenga, namna ya kuchukuliana sisi kwa sisi (Kanisa), tuliomwamini Yesu katika eneo la kujishusha na kunyenyekeana, kutokwazana, kutokupuuziana, lakini pia kuwa tayari kuwatafuta wale waliopotea na kuwarudisha kundini, ni muhimu sana, akatoa mfano wa mtu aliyeacha kondoo wake tisini na tisa, na kwenda kumtafuta Yule mmoja aliyepotea. Na sisi yatupaswa tuwe na moyo huo wa kichungaji.

Vilevile kusameheana sisi kwa sisi hata saba mara sabini akatoa mfano wa Yule mtu aliyesamehewa talanta elfu kumi, lakini yeye hakuwa tayari kumsamehe aliyemdai dinari mia, pia alifundisha njia nzuri ya kuonyana kingazi kufatana na utaratibu kwa kikanisa.

Hivyo usomapo hotuba hii, utafahamu namna ambavyo Bwana anataka sisi tuishi kama ndugu tuwapo pamoja kama kanisa lake.

5) Hotuba ya siku za mwisho (Mathayo 24)

Hii ni hotuba inayohusu, matukio yote ya siku za mwisho wa dunia, na kurudi kwa Yesu kutakavyokuwa, anaeleza kwa urefu dalili zake, mabadiliko ya kimwenendo ya watu, yatakavyokuwa, majanga ya asili, na vita vitakavyofuata baadaye, anatoa tahadhari ya manabii wa uongo, unyakuo wa kanisa, dhiki kuu na mapigo ya Mungu, Na mwisho anatoa angalizo ni nini tunapaswa tufanye. Kwamba “Tukeshe”, kwasababu hatujui siku wala saa.

Hotuba hii ni vizuri ukaisoma kwa urefu, na kuelewa kwa undani, kwasababu nyakati tulizopo sasa, tupo katika “mwisho wa siku za mwisho.” Dalili nyingi zilizotabiriwa zilishatimia. Jiulize umejiandaaje kwa yaliyo mbele yetu?

Hivyo kwa hitimisho ni kuwa, ufahamupo Mahubiri hayo (Hotuba), utapata uelewa wa undani kimaudhui ndani ya kitabu cha Mathayo, Jifunze kusoma sana, na kurudia rudia, hotuba hizi, kulikuwa na sababu kwanini Bwana atoe habari zake kwa urefu, kwasababu ndio “Fundisho” la mwamini. Zingatia hayo na Bwana akubariki.

Tutakuwa na uchambuzi wa vitabu vingine..

Washirikishe na wengine habari hizi njema kwa kushea

Ikiwa utapenda kupata msaada wa kumpokea Yesu maishani mwako bure, Basi wasiliana nasi kwa namba uzionazo chini ya makala hii.

Pia kwa kupokea mafundisho ya kila siku kwa njia ya WHATSAPP, jiunge na channel yetu kwa kupofya link hii >> https://whatsapp.com/channel/0029VaBVhuA3WHTbKoz8jx1

Kwa mawasiliano: +255789001312 au +255693036618

Bwana akubariki.

Mafundisho mengine:

VITABU VYA BIBLIA: Sehemu ya 2

UFALME WA MUNGU HAUPATIKANI KIRAHISI.

NENO LA MUNGU KATIKA UTIMILIFU WOTE.

ANGUKO LA UFALME WA SHETANI:

Rudi Nyumbani

Print this post