Maana ya kanisa ni “walioitwa” kwahiyo watu walioitwa watoke sehemu fulani wanaitwa kanisa…..Hivyo tafsiri ya kanisa sio jengo kama inavyodhaniwa na wengi…
Kwahiyo katika maandiko kanisa la kwanza lilianza siku ile ya PENTEKOSTE. Roho Mtakatifu aliposhuka juu ya watu! Soma Matendo Mlango wa pili yote.
Wale waliomwamini Yesu, na kubatizwa walishukiwa na Roho Mtakatifu, na hivyo Roho huyo huyo aliwaongoza kukusanyika pamoja kwa lengo la kujifunza Neno ambalo Mitume ndio waliokuwa wanalifundisha, pia walidumu katika kushiriki meza ya Bwana, katika kufanya ushirika na katika Kusali. Hayo mambo manne ndiyo yaliyokuwa yanafanyika katika kanisa la kwanza.
Matendo 2:37 “Walipoyasikia haya wakachomwa mioyo yao, wakamwambia Petro na mitume wengine, Tutendeje, ndugu zetu?
38 Petro akawaambia, Tubuni mkabatizwe kila mmoja kwa jina lake Yesu Kristo, mpate ondoleo la dhambi zenu, nanyi mtapokea kipawa cha Roho Mtakatifu
39 Kwa kuwa ahadi hii ni kwa ajili yenu, na kwa watoto wenu, na kwa watu wote walio mbali, na kwa wote watakaoitwa na Bwana Mungu wetu wamjie.
40 Akawashuhudia kwa maneno mengine mengi sana na kuwaonya, akisema, Jiokoeni na kizazi hiki chenye ukaidi.
41 Nao waliolipokea neno lake wakabatizwa; na siku ile wakaongezeka watu wapata elfu tatu.
42 Wakawa wakidumu katika fundisho la mitume, na katika ushirika, na katika kuumega mkate, na katika kusali”.
(Hilo ndilo kanisa la kwanza)
Kanisa katoliki llinalosemekana kama kanisa la kwanza, hilo ilikuja kuzaliwa mwaka wa 325 Baada ya Kristo. Ambalo hilo lilikuwa kinyume na kanisa la kweli la Kwanza la Pentekoste.
Kanisa katoliki, ni kanisa la uongo kwasababu halikudumu katika hayo mambo manne hapo juu… halidumu katika fundisho la Mitume kama kanisa la Kwanza, fundisho la Mitume linasema tusiabudu sanamu na pia linasema mpatanishi kati ya Mungu na mwanadamu ni mmoja tu Yesu Kristo, wakati kanisa katoliki linaamini Mariamu pia ni mpatanishi…..
Pia kanisa katoliki halidumu katika kumega mkate, kwani mwenye ruhusu ya kushiriki ni Padre tu! peke yake jambo ambalo ni kinyume na maandiko, pia halidumu katika kufanya ushirika wala kusali…Sala zinazofanywa ni za desturi za kipagani, kusalia rozari na sanamu jambo ambalo kanisa la kwanza halikufanya. Maombi ya moja kwa moja kwa Mungu hayatiliwi mkazo, na zaidi ya yote maombi ya masafa marefu hayapo kabisa ndani ya kanisa katoliki.
Mada Nyinginezo:
JE! BIKIRA MARIA NI MALKIA WA MBINGUNI?
JE! NI SAHIHI KUMUITA MARIA MAMA WA MUNGU?
Yesu ni nani? Hili ni swali ambalo sio tu linawachanganya watu wengi wa leo, lakini pia limekuwa ni swali lililowasumbua watu wengi tangu enzi na enzi vizazi na vizazi huko nyuma, hata tangu wakati Bwana Yesu mwenyewe akiwa hapa duniani utaona siku moja aliwauliza wanafunzi wake nao swali kama hilo,
Mathayo 16:13 “Basi Yesu akaenda pande za Kaisaria-Filipi, akawauliza wanafunzi wake akasema, Watu hunena Mwana wa Adamu kuwa ni nani?
14 Wakasema, Wengine hunena u Yohana Mbatizaji, wengine Eliya, wengine Yeremia au mmojawapo wa manabii.
15 Akawaambia, Nanyi mwaninena mimi kuwa ni nani?
Unaona, hata leo hii tu angekuwepo duniani angetuuliza na sisi swali hilo hilo, tunamnena yeye kama nani, ni wazi utasikia kila mtu anatoa jibu lake wengine utawasikia watasema, ni mjumbe wa Mungu, wengine watasema ni mmojawapo wa mitume wa Mungu, wangine watasema alikuwa ni nabii wa Mungu, wengine watasema ni mkombozi, wengine watasema ni Mungu…nk. N.k
Lakini Je hiyo inamaanisha mitazamo yao wote haipo sawa?, jibu ni hapana, wanaweza wakawa sawa mahali fulani lakini si sawa kulingana na Mungu anavyotaka watu wamjue Yesu kama nani..Ni sawa tu na leo usimame na boss labda tuseme mbele ya watu 1000 tofauti tofauti, na ukasema kila mmoja aanze kumzungumzia , hutashangaa katikati ya huo mkutano wengine wakimwita, mjomba, wengine wakimwita rafiki, wengine wakimwita baba, wengine wakimwita binamu, wengine wakimwita jirani, wengine wakimwita mwenyekiti, wengine wakimwita shemeji, wengine wakimwita mwenetu n.k…
Hapo utaona akiitwa kila aina ya cheo ambacho hujawahi kutazamia kwamba anaweza akawa nacho boss wako, sasa hapo huwezi kusema hawapo sawa kisa tu kwasababu hukumsikia hata mmoja wao akimwita boss, wao kila mmoja alimwita kulingana na mahusiano aliyonayo naye..ikiwa ni mtoto wake alisimama mbele yake hawezi kumwita shemeji au boss ni lazima atamwita Baba tu..
Lakini hata kama wapo sawa kiasi gani, Bado hawapo sawa kulingana na wewe unavyotaka watu wale wamjue kama boss.
Na vivyo hivyo kwa Bwana Yesu, wengi wanamjua kama mtume wa Mungu, na kweli ndivyo alivyo yeye ndiye mtume mkuu, wengi wanamjua kama nabii, na ni kweli ndivyo ilivyo yeye alikuwa ni nabii mkuu, wengine wanamjua kama kiongozi na kweli ndivyo alivyo, vile vile wengine wanamjua kama Mungu mwenyewe aliyeuchua mwili na kuishi na sisi duniani, na kweli ndivyo ilivyo maandiko mengi yanathibitisha hilo kuwa YESU ndiye Mungu mwenyewe katika mwili wa kibinadamu..lakini swali linakuja pale pale Je! Mungu anataka sisi tumjue YESU kama nani?.
Sasa tukiendelea kusoma pale chini tunaona Petro anamjibu Bwana maneno haya:
15 Akawaambia, Nanyi mwaninena mimi kuwa ni nani?
16 Simoni Petro akajibu akasema, WEWE NDIWE KRISTO, MWANA WA MUNGU ALIYE HAI.
17 Yesu akajibu, akamwambia, Heri wewe Simoni Bar-yona; kwa kuwa mwili na damu havikukufunulia hili, bali Baba yangu aliye mbinguni.
18 Nami nakuambia, Wewe ndiwe Petro, na juu ya mwamba huu nitalijenga kanisa langu; wala milango ya kuzimu haitalishinda.”
Unaona Ufunuo aliopata Petro juu ya YESU kama KRISTO, aliyekuja kama mwana wa Mungu, ndio aliokuwa anauhitaji na ndio kwa kupitia huo huo YESU amelijengea kanisa lake na milango ya kuzimu haiwezi kulishinda.
Hivyo hatupaswi kuhangaika sana, kutafuta kumjua YESU ni nani? Tukianza kumchambua hatutammaliza, lakini biblia imetupa mwongozo mwepesi uliomwelezea yeye kwamba tumjue yeye kama KRISTO, maana ya neno Kristo ni mtiwa mafuta, yaani mtu aliyetiwa mafuta kuwakomboa wanadamu,..hivyo tukishamjua YESU kama mkombozi huo ni ufunguo mkubwa sana uliobeba vyeo vyake vingine vyote vilivyobakia.. Kwamba yeye ndio njia ya kwenda mbinguni, na mtu hawezi kufika kwa Mungu pasipo kupitia yeye.
Hivyo ukiulizwa leo YESU ni nani, jibu tayari lipo yeye ni KRISTO, yaani mkombozi wa ulimwengu, hilo linatosha kumwelezea yeye..Na mtu yeyote akimwelewa kwa namna hiyo hivyo akamruhusu ayakomboe maisha yake basi ajue kuwa shetani atagonga mwamba, tiketi ya kwenda mbinguni ipo mikononi mwake.
Ubarikiwe.
Mada Nyinginezo:
KWANINI YESU KRISTO ALIKUJA DUNIANI?
KWANINI YESU KRISTO NI MWANA WA DAUDI?
KWANINI AWE NI PUNDA NA MWANA-PUNDA?
Ufunuo 14:13 “Nikasikia sauti kutoka mbinguni ikisema, Andika, Heri wafu wafao katika Bwana tangu sasa. Naam, asema Roho, wapate kupumzika baada ya taabu zao; kwa kuwa matendo yao yafuatana nao”.
Biblia inasema “Heri” heri maana yake “amebarikiwa yeye”…na inasema pia heri wafu wafao katika Bwana, ikiwa na maana kuwa sio kufa tu! bali kufa katika Bwana.. Wafu ambao hawajafa katika Bwana ni kinyume chake, kwamba Ole wao…
Sentensi hizo zinamaanisha kuwa kuna kitu kitafuata baada ya kifo, nacho si kingine zaidi ya hukumu! Na watakaokufa katika Kristo wanatumaini la kufufuliwa tena na kupewa uzima wa milele, na kupata raha isiyoisha..ndio maana wanaambiwa wana heri…. ingekuwa hakuna kitu kinachofuata, isingesema heri wafu! bali ingesema heri walio hai!
Je! maisha yako umeyatengeneza kiasi kwamba, una uhakika, hata leo hii ukiondoka ulimwenguni! utakuwa na heri? Utayatengenezaje?..kwa matendo yako! kwasababu Matendo ya kila mtu yanamfuata popote aendapo! Majumba tukifa tutayaacha, magari tutayaacha, mali tutaziacha lakini matendo tunakwenda nayo huko ng’ambo ya pili. Hivyo sio kitu cha kukichukulia kiwepesi!
kumbuka hakutakuwa na nafasi ya pili baada ya kifo.
Waebrania 9:27 “Na kama vile watu wanavyowekewa kufa mara moja, na baada ya kufa hukumu”;
Mgeukie Bwana Yesu kikamilifu. Kimbilio letu na Tumaini letu
Maran atha!
Mada Nyinginezo:
NIFANYE NINI ILI NIIKWEPE HUKUMU.
UMEPATA UHAKIKA WA KUTOKUINGIA HUKUMUNI KATIKA SIKU ILE?
Chanzo cha Baraka zote ni Mungu..Na Mungu anaweza kumbariki mtu moja kwa moja kupitia yeye mwenyewe…na anaweza pia kumbariki mtu kupitia mtu mwingine.
Kwamfano kwenye Biblia Mungu alimbariki Ibrahimu moja kwa moja…akamwambia
Mwanzo 22:15 “Malaika wa Bwana akamwita Ibrahimu mara ya pili kutoka mbinguni
16 akasema, Nimeapa kwa nafsi yangu asema Bwana, kwa kuwa umetenda neno hili, wala hukunizuilia mwanao, mwanao wa pekee,
17 katika kubariki nitakubariki, na katika kuzidisha nitauzidisha uzao wako kama nyota za mbinguni, na kama mchanga ulioko pwani; na uzao wako utamiliki mlango wa adui zao;
18 na katika uzao wako mataifa yote ya dunia watajibarikia; kwa sababu umetii sauti yangu”.
Na pia Mungu anaweza kumbariki mtu kwa kupitia Mtu mwingine, kwa mfano “Mzazi ana uwezo wa kumbariki mwanawe” na baraka hizo zikamfikia vile vile kama alivyombariki. Mfano katika Biblia tunamwona Yakobo Mwana wa Isaka, aliwabariki wanawe 12, na kila mmoja baraka aliyombarikia ilimfikia.
Hivyo Ili tufanikiwe katika maisha yetu, hatuna budi kutafuta Baraka, na Baraka hizo zinakuja kwa kumpendeza Mungu, pamoja na wanadamu…Kuyashika maagizo ya Mungu, na Kuwaheshimu wazazi pamoja na watu wote. Kinyume na hapo ni kujitafutia Laana.
Mada Nyinginezo:
MPENDE JIRANI YAKO KAMA NAFSI YAKO.
NITAONGEZAJE NGUVU ZANGU ZA ROHONI?
KWANINI MUNGU HAKUMUUA NYOKA MPAKA AKARUHUSU AJARIBIWE PALE BUSTANI NA EDENI?
JIBU: Ili tusichanganyikiwe jambo la muhimu tulinalopaswa kujua ni kuwa Katika biblia Neno “mbinguni” limetumika kuwakilisha sehemu tofauti tofauti tatu.
Sehemu ya kwanza ni anga hili ambalo lipo juu yetu: Ambalo ndilo hili tunaloliona lenye nyota, mawingu, mwezi jua na sayari, ambalo ndege wote wa angani wanaruka na kufurahia, biblia imelitaja kama mbingu..Tunasoma..
Isaya 55:10 “Maana kama vile mvua ishukavyo, na theluji, kutoka mbinguni, wala hairudi huko; bali huinywesha ardhi, na kuizalisha na kuichipuza, ikampa mtu apandaye mbegu, na mtu alaye chakula;
11 ndivyo litakavyokuwa neno langu, litokalo katika kinywa changu; halitanirudia bure, bali litatimiza mapenzi yangu, nalo litafanikiwa katika mambo yale niliyolituma.”
Luka 17:24 “kwa kuwa, kama vile umeme umulikavyo toka upande huu chini ya mbingu hata upande huu chini ya mbingu, ndivyo atakavyokuwa Mwana wa Adamu katika siku yake”.
Sehemu ya Pili ya mbingu ni makao ya Mungu yalipo: Na hii ipo katika Roho, sehemu ambayo Mungu na malaika zake wanaishi, hatuwezi kuiona kwa jicho la kibinadamu wala hatuwezi kufika huko kwa kifaa chochote cha kibinadamu, lakini ni mahali halisi kabisa. Tiketi ya pekee ya kufika huko biblia inatuambia ni Yesu Kristo tu, Na hii mbingu ni pana sana ndio imejumuisha ile mbingu mpya na nchi mpya ambayo itakuja kuwa ni makao ya watakatifu baadaye, pamoja na ile paradiso (peponi) kule ambapo wale wote waliokufa zamani na wanaokufa sasa hivi katika Kristo wanahifadhiwa kwa muda wakisubiria ufufuo siku ile ya Unyakuo ili kwa pamoja waingie katika makao ya Mungu mwenyewe yaliyo juu sana na ndio maana utaona mtume Paulo alinyakuliwa mpaka mbingu ya Tatu, mbingu hii ya tatu ni hiyo ya makao ya Mungu mwenyewe, akaonyeshwa sehemu ya maono ya huko, na kusema mambo yaliyo huko hayajuzu hata mwanadamu kuyatamka,(2Wakorintho 12:2-4). na ndiko watakatifu waliokombolewa watakapokwenda siku ile ya Unyakuo itakapofika, ni mahali patakatifu na pasafi ambapo mtu yeyote mchafu hataingia..
1Wafalme 8:27 “Lakini Mungu je? Atakaa kweli kweli juu ya nchi? Tazama, mbingu hazikutoshi, wala mbingu za mbingu; sembuse nyumba hii niliyoijenga!”
1Timotheo 6:16 “ambaye yeye peke yake hapatikani na mauti, amekaa katika nuru isiyoweza kukaribiwa; wala hakuna mwanadamu aliyemwona, wala awezaye kumwona. Heshima na uweza una yeye hata milele. Amina.”
Na sehemu ya tatu biblia inapataja kama mbinguni ni mahali pa juu sana, makao ya juu sana: Mahali ambapo Mungu pekee ndiye anayestahili kuwepo, jambo ambalo hata hapa duniani linaweza kufikiwa,
Watu walio ndani ya Yesu, ambao wameokoka kikamilifu kwa kumwamini Yesu na kubatizwa, katika ulimwengu wa roho, ni sawa na wameketi pamoja na Kristo mbinguni..
Waefeso 2:5 “hata wakati ule tulipokuwa wafu kwa sababu ya makosa yetu; alituhuisha pamoja na Kristo; yaani, tumeokolewa kwa neema.
6 Akatufufua pamoja naye, akatuketisha pamoja naye katika ulimwengu wa roho, katika Kristo Yesu;”
Kadhalika pia, Ufalme wowote au mtu yeyote anayetafuta kuinuliwa ziadi ya vitu vingine vyote huyo katika roho anaonekana anakipandia cheo cha Mungu kilipo, na Mungu yupo mbinguni, hivyo anaonekana kama amefika mbinguni.
Danieli 4:19 “Ndipo Danieli, aliyeitwa jina lake Belteshaza, akashangaa kwa muda, na fikira zake zikamfadhaisha. Mfalme akajibu akasema, Ee Belteshaza, ndoto ile isikufadhaishe wala tafsiri yake. Belteshaza akajibu, akasema, Bwana wangu, ndoto hii iwapate wao wakuchukiao, na tafsiri yake iwapate adui zako.
20 Ule mti uliouona, uliokua, ukawa na nguvu, urefu wake ukafika mpaka mbinguni, na kuonekana kwake mpaka dunia yote;
21 ambao majani yake yalikuwa mazuri, na matunda yake mengi, na ndani yake chakula cha kuwatosha wote; ambao chini yake wanyama wa kondeni walikaa, na ndege wa angani walikuwa na makao yao katika matawi yake;
22 ni wewe, Ee mfalme, uliyekua, na kupata nguvu; maana ukuu wako umekua na kufika mpaka mbinguni, na mamlaka yako yamefika mpaka mwisho wa dunia.
Mathayo 11:23 “Nawe Kapernaumu, je! Utakuzwa mpaka mbinguni? Utashushwa mpaka kuzimu; kwa kuwa kama miujiza iliyofanyika kwako ingalifanyika katika Sodoma, ungalikuwapo mji huo hata leo.”
Isaya 14:12 “Jinsi ulivyoanguka kutoka mbinguni, Ewe nyota ya alfajiri, mwana wa asubuhi! Jinsi ulivyokatwa kabisa, Ewe uliyewaangusha mataifa!
13 Nawe ulisema moyoni mwako, Nitapanda mpaka mbinguni, Nitakiinua kiti changu juu kuliko nyota za Mungu; Nami nitaketi juu ya mlima wa mkutano, Katika pande za mwisho za kaskazini.
14 Nitapaa kupita vimo vya mawingu, Nitafanana na yeye Aliye juu.
15 Lakini utashushwa mpaka kuzimu; Mpaka pande za mwisho za shimo”.
Hivyo kwa vyovyote vile, tunapaswa tujitahidi ili tufike huko, si kwa kujiinua tukiyatumainia haya Maisha, bali kwa kupitia Yesu Kristo, kwasababu biblia inasema mambo tuliyoandaliwa huko, jicho halijawahi kuona wala sikio kusikia.
Ubarikiwe.
Mada Nyinginezo:
TUMEAMBIWA TUNAPOSALI TUSIPAYUKE-PAYUKE, JE! HUKO KUPAYUKA PAYAUKA NDIO KUPI?
JE! KUNA DHAMBI KUBWA NA NDOGO?
NI NANI ANAYETAWALA DUNIA KATI YA MUNGU NA SHETANI?.
Biblia imeweka wazi kuwa Mariamu, mama yake Yesu alikuwa na watoto wengine..
Mathayo 13:53 “Ikawa Yesu alipoimaliza mifano hiyo, alitoka akaenda zake.
54 Na alipofika nchi yake, akawafundisha katika sinagogi lao, hata wakashangaa, wakasema, Huyu amepata wapi hekima hii na miujiza hii?
55 Huyu si mwana wa seremala? Mamaye si yeye aitwaye Mariamu? Na nduguze si Yakobo, na Yusufu, na Simoni, na Yuda?
56 Na maumbu yake wote hawapo hapa petu? Basi huyu amepata wapi haya yote?
57 Wakachukizwa naye. Yesu akawaambia, Nabii hakosi kupata heshima, isipokuwa katika nchi yake, na nyumbani mwake mwenyewe”.
Maumbu kama inavyosomeka kwenye mstari wa 56, maana yake ni ndugu wa ‘KIKE’ (madada)..Kwahiyo Mariamu alikuwa ana watoto wengine wakiume na wakike.
Mada Nyinginezo:
NI HALALI KUBATIZA WATOTO WADOGO?
SABATO HALISI NI LINI, JE! NI JUMAPILI AU JUMAMOSI?, NI SIKU GANI ITUPASAYO KUABUDU?
MUNGU ALIKUWA ANAONGEA NA NANI ALIPOSEMA NA “TUMFANYE MTU KWA MFANO WETU”,(MWANZO 1:26)?
Hakuna mahali popote Biblia imerekodi kifo cha Mariamu, wala hakuna mahali popote Biblia imerekodi kifo cha Mtume Petro, wala Yusufu mume wake Mariamu, wala Mtume Paulo, wala Mtume Adrea wala Tomaso, Nathanieli, n.k…manabii wengi sana na mitume vifo vyao havijarekodiwa kwenye Biblia takatifu..
Na ni kwanini biblia havijarekodi vifo vya hawa watu, ni kwasababu sio vitu vya muhimu sana kuvijua kwetu sisi…Inatusaidia nini sisi kujua Petro alikufa mwaka gani? au mwezi gani?.. unaona haitusaidii chochote! Lakini tunajua kuwa Petro alikufa, Paulo alikufa, Yusufu alikufa…kadhalika na Bikira Mariamu alikufa vile vile.
Mariamu hakuwa mtu wa tofauti sana na watu wengine…Eliya ambaye hakufa bali alipaa, Biblia inamtaja kuwa mtu wa mwenye tabia sawa na sisi, (soma Yakobo 5:17) itakuwaje Mariamu ambaye hakupaa?..Ni mmoja tu ndiye aliyekuwa wa kipekee ambaye biblia inasema alikufa na kufufuka na akapaa mbinguni, na huyo ni Yesu Pekee yake, ndio maana wokovu upo kwake. Kulikuwa hakuna haja ya kuja Bwana Yesu kama Mariamu alikuwa na wokovu .
Hivyo kwa hitimisho ni kwamba Mariamu alikufa kama watu wengine.
Mada Nyinginezo:
JE! NI SAHIHI KUMUITA MARIA MAMA WA MUNGU?
JE! BIKIRA MARIA NI MALKIA WA MBINGUNI?
KWANINI MUNGU AWACHOME WATU KWENYE ZIWA LA MOTO NA HALI YEYE NDIYE ALIYEWAUMBA?
Jambo moja linalowachanga watu wengi wa Mungu, ni kutokujua Ujio wa Yesu utakuwaje.
Ujio wa Bwana Yesu umegawanyika katika sehemu kuu 3. nazo ni UJIO WA KWANZA, UJIO WA PILI na UJIO WA TATU.
UJIO WA KWANZA: Ni wakati Bwana Yesu alipozaliwa na Bikira Mariamu, na kuifanya kazi yake kwa miaka mitatu na nusu, na kufa, na kufufuka, kisha kurudi mbinguni alikotoka. Huo ulikuwa ni ujio wa kwanza.
UJIO WA PILI: Utakuwa ni wakati wa unyakuo…Ujio huu hautahusisha Bwana kushuka kabisa duniani, bali Bwana atakuja na ataishia mawinguni, sisi tulio hai tutaungana pamoja na wale waliokufa katika Kristo, kwa pamoja tutanyakuliwa kwenda kumlaki mawinguni, na kwenda mbinguni kwenye karamu yake aliyotuandalia, (1 Wathesalonike 4) ambapo huko tutakaa kwa muda wa miaka 7…
UJIO WA TATU: Utahusisha Bwana kurudi tena na watakatifu wake duniani walionyakuliwa, atakuja duniani kwa ajili ya Hukumu ya Mataifa, Vita ya Harmagedon, pamoja na kuanzisha utawala mpya duniani wa Amani utakaodumu kwa miaka 1000. Ujio huu ndio kila jicho litamwona akija wa majeshi ya mbinguni..Na atashukia Israeli. Hapo ndio yatakuwa makao yake makuu kipindi cha utawala wake duniani.
Kwa urefu wa ujio huo pitia somo hapa chini linalosema UTAWALA WA MIAKA 1000.
Mada Nyinginezo:
NAMNA YA KUITAMBUA SAUTI YA MUNGU INAPOZUNGUMZA NA WEWE
Jehanamu au Jehanum ni Neno lenye chimbuko la kiyunani Gehenna, ambalo limetafsiriwa kutoka katika lugha ya kiyahudi ge-hinnom Ikiwa na maana bonde la mwana wa Hinomu.. Hili ni eneo lililokuwa kusini mwa mji wa Yerusalemu, lililojulikana kama Tofethi ambao watu wasiokuwa wanamcha Bwana walikuwa wanalitumia kuwatolea watoto wao kafara kwa kuwapitisha motoni kwa miungu waliyoikuta huko Kaanani. Jambo ambalo lilikuwa ni chukizo kubwa sana kwa Mungu, ambalo nalo pia lilikuwa ni mojawapo ya mambo yaliyowafanya wachukuliwe utumwani Babeli.
Tunasoma hayo katika..
Jeremia 7:30 “Maana wana wa Yuda wametenda yaliyo maovu machoni pangu, asema Bwana; wameweka machukizo yao ndani ya nyumba hiyo, iitwayo kwa jina langu, hata kuitia unajisi.
31 Nao wamepajenga mahali palipoinuka pa Tofethi, palipo katika bonde la mwana wa Hinomu, ili kuwateketeza wana wao na binti zao motoni; jambo ambalo mimi sikuliagiza, wala halikuingia moyoni mwangu.”
Yeremia 19:1 “Bwana akasema hivi, Enenda ukanunue gudulia la mfinyanzi, ukachukue pamoja nawe baadhi ya wazee wa watu, na baadhi ya wazee wa makuhani;
2 ukatoke uende mpaka bonde la mwana wa Hinomu lililo karibu na mahali pa kuingia kwa lango la vigae, ukahubiri huko maneno nitakayokuambia,
3 ukisema, Lisikieni neno la Bwana, enyi wafalme wa Yuda, na wenyeji wa Yerusalemu; Bwana wa majeshi, Mungu wa Israeli asema hivi, Angalieni, nitaleta mabaya juu ya mahali hapa, ambayo mtu ye yote akisikia habari yake, masikio yake yatawaka.
4 Kwa sababu wameniacha mimi, nao wamepafanya mahali hapa kuwa mahali pageni, nao hapa wamewafukizia uvumba miungu mingine wasiowajua, wala wao, wala baba zao, wala wafalme wa Yuda; nao wamepajaza mahali hapa damu ya wasio na hatia;
5 nao wamemjengea Baali mahali pake palipo juu, ili kuwachoma moto wana wao, wawe sadaka za kuteketezwa kwa Baali; tendo nisiloliamuru mimi, wala kulinena, wala halikuingia moyoni mwangu;
6 basi, angalieni, siku zinakuja, asema Bwana, ambazo katika siku hizo mahali hapa hapataitwa tena Tofethi, wala Bonde la mwana wa Hinomu, bali, Bonde la Machinjo.”
2Wafalme 23:10 “Naye akainajisi Tofethi, iliyomo katika bonde la wana wa Hinomu, ili mtu asipitishe mwana wake au binti yake motoni kwa Moleki.”
likabakia kutumika kama dampo la jiji, na bonde la kutupia miili ya watu waovu, pamoja na wanyama waliokufa pamoja na kuchoma takataka na kila aina ya uchafu wote uliotoka mjini..Na hiyo ilipelekea bonde hilo kuwa la kinyaa sana na wakati wote kuwa linawaka moto, na moshi mkubwa unaopanda juu pamoja na harufu kali sana, kutokana na kwamba kila wakati uchafu ulikuwa unaingia..
Sasa zile sehemu ambazo moto ulikuwa haufiki vizuri, kulikuwa na funza wengi sana, ambao walipita katikati ya mizoga ile iliyokuwa imetupwa, ni eneo ambalo hakuna mtu angeweza kukaa hata dakika mbili au kusogea karibu na akawa sawa. Kama ulishawahi kuona jalala kuu la manispaa au jiji basi fahamu kuwa huo ni mfano mdogo sana ukilinganisha na GEHENA ilivyokuwa..bonde hilo lilikuwa linatisha sana. Funza wa jehanamu walikuwa ni wagumu kufa kwasababu walikuwa ni tofauti na funza wengine.
Na ndio maana Bwana YESU alitumia mfano huo, kueleza picha halisi ya kuzimu ilivyo kwa wale ambao watakufa katika dhambi zao. Alisema..
Marko 9:43 “Na mkono wako ukikukosesha, ukate; ni afadhali kuingia katika uzima u kigutu, kuliko kuwa na mikono miwili, na kwenda zako jehanum, kwenye moto usiozimika;
44 ambamo humo funza wao hafi, wala moto hauzimiki.] 9.45 Na mguu wako ukikukosesha, ukate; ni afadhali kuingia katika uzima, u kiwete, kuliko kuwa na miguu miwili, na kutupwa katika jehanum; [
46 ambamo humo funza wao hafi, wala moto hauzimiki.]
47 Na jicho lako likikukosesha, ling’oe, ulitupe; ni afadhali kuingia katika ufalme wa Mungu, una chongo, kuliko kuwa na macho mawili, na kutupwa katika jehanum;
48 ambamo humo funza wao hafi, wala moto hauzimiki.”
Ni wazi kuwa hakuna mtu anayependa kuwepo sehemu yeyote chafu, basi hiyo inatupa chachu pia tujiepushe na kuzimu kwasababu kuzimu ipo kweli na si mahali pazuri hata kidogo huko hakuna raha, ukishajikuta kule, utakuwa katika mateso siku zote ukisubiria hukumu ya siku za mwisho kabla ya kutupwa katika lile ziwa la moto..
Kama upo nje ya Kristo, wakati ndio huu, tubu sasa, mpe Bwana maisha yako naye atakupokea..Na kukusamehe kabisa, kwasababu mbingu amekuandalia wewe, hivyo daima hataki nafasi yako ipotee.
Ubarikiwe.
Mada Nyinginezo:
BWANA ALIMAANISHA NINI KUSEMA “WAACHE WAFU WAZIKE WAFU WAO?.
MADHARA YA KUKOSA MAJI YA UZIMA BAADA YA KIFO.
Kanisa ni nini?..kanisa la Mungu ni kitu gani?
hili ni swali linalowachanganya watu wengi ikidhaniwa kuwa Kanisa ni jengo. Lakini hiyo sio maana halisi ya kanisa. Neno kanisa limetokana na Neno la kiyunani EKKLESIA, ikimaanisha “walioitwa”, Enzi za Agano jipya kasanyiko lolote la wakristo(yaani hao walioitwa) lilijulikana kama kanisa..Na kusanyiko hilo liliweza kuanzia watu wawili au watu, kufuatana na maneno ya Yesu Kristo mwenyewe aliyosema katika..
Mathayo 18:20 “Kwa kuwa walipo wawili watatu wamekusanyika kwa jina langu, nami nipo papo hapo katikati yao.”
Hivyo ilifahamika kuwa mahali popote walipokusanyika watu waliomwamini Kristo iwe ni nyumbani, au hekaluni, au kwenye sinagogi, au popote pale kwa jina lake kutokujali mazingira yazungukayo basi hilo tayari ni kanisa.
Wagalatia 1:13 “Maana mmesikia habari za mwenendo wangu zamani katika dini ya Kiyahudi, kwamba naliliudhi kanisa la Mungu kupita kiasi, nikaliharibu”
Umeona?..Sentensi hiyo haioneshi kanisa kama jengo bali “wakristo” Paulo ndio aliowaudhi na kuwaharibu..Kwahiyo kanisa ni nini? Ni mkusanyiko wa watu walioitwa (au kwa lugha rahisi wakristo)
Hivyo kwa ufupi, mkusanyiko wowote usio wa kikristo, yaani usio usiomtambua Kristo kama kichwa cha kusanyiko hilo haijalishi ni mkubwa kiasi gani, haijalishi upo kwenye jengo lenye misalaba mingi kiasi gani, haijalishi linafuata utaratibu mzuri kiasi gani, hilo sio kanisa kibiblia. Ni sawa na mwili ambao hauna kichwa, ni mfu, vivyo hivyo na mkusanyiko wowote usio na Kristo hauwezi kuwa ni Kanisa.
Waefeso1:20 “aliotenda katika Kristo alipomfufua katika wafu, akamweka mkono wake wa kuume katika ulimwengu wa roho;
21 juu sana kuliko ufalme wote, na mamlaka, na nguvu, na usultani, na kila jina litajwalo, wala si ulimwenguni humu tu, bali katika ule ujao pia;
22 akavitia vitu vyote chini ya miguu yake, akamweka awe kichwa juu ya vitu vyote kwa ajili ya kanisa; ambalo
23 ndilo mwili wake, ukamilifu wake anayekamilika kwa vyote katika vyote.”
AMEN.
Kwa Maswali, Maombezi, Ushauri, au Ratiba za Ibada Wasiliana nasi kwa namba hizi
+225693036618/ +225789001312
Mada Nyinginezo:
WALIPO WAWILI AU WATATU KWA JINA LANGU.
NYAKATI SABA ZA KANISA NA WAJUMBE WAKE.
AGENDA KUBWA YA SHETANI KWA KANISA HILI LA LAODIKIA.
SIRI YA KUASI KATIKA KANISA LA MUNGU.
MADHARA YA KUKOSA MAJI YA UZIMA BAADA YA KIFO.
JE KUJIUA NI DHAMBI?