Category Archive Mafundisho

JE UMEJIFUNZA ULE WIMBO MPYA?

Nakusalimu katika jina kuu la Bwana wetu Yesu Kristo, Tukijua kuwa ule mwisho unakaribia, hatuna budi siku baada ya siku tujichunguze je! Tumekamilika vema? ili siku ile tusionekane na mawaa mbele zake. Tulipokee taji timilifu tuliloandaliwa mbinguni na mwokozi wetu Yesu Kristo kwa neema zake.

Leo, napenda tufahamu juu ya wimbo mpya. Kama wewe ni msomaji mzuri wa kitabu cha Ufunuo. Utagundua zimetajwa nyimbo kuu tatu.

  1. Wimbo wa Musa
  2. Wimbo wa Mwanakondoo
  3. Wimbo mpya

Swali ni je! Hizi nyimbo ni zipi na zinatimiaje?

Wimbo wa Musa na wa mwanakondoo tunazisoma, katika Ufunuo 15:2-3

Ufunuo 15:2  Tena nikaona kitu kama mfano wa bahari ya kioo iliyochangamana na moto, na wale wenye kushinda, watokao kwa yule mnyama, na sanamu yake, na kwa hesabu ya jina lake, walikuwa wamesimama kando-kando ya hiyo bahari ya kioo, wenye vinubi vya Mungu.

3  Nao WAUIMBA WIMBO WA MUSA, MTUMWA WA MUNGU, NA WIMBO WA MWANA-KONDOO, wakisema, Ni makuu, na ya ajabu, matendo yako, Ee Bwana Mungu Mwenyezi; Ni za haki, na za kweli, njia zako, Ee Mfalme wa mataifa

Wimbo wa Musa, ni injili ya Musa, ambayo iliwafanya watu wa kale, kutembea katika hiyo ili wamkaribie Mungu, ndiyo ile torati, ambayo wale waliokuwa katika agano la Ibrahimu kwa uzao, walirithi neema hiyo. Hivyo wana wa Israeli wote walikuwa wanauimba wimbo wa Musa. Yoyote ambaye hakuwa hana wimbo huo, basi wokovu au kumkaribia Mungu hakukuwezekana kwake.

Lakini wimbo wa Musa haukuwa na ukamilifu wote kwasababu ulikuwa ni wa mwilini, na wa kutarajia ahadi ya mwokozi mbeleni. Hivyo Mungu akaleta wimbo mwingine mpya kwa wanadamu wote. Ndio huo wimbo wa mwana-kondoo.

Ambayo ni injili ya neema iliyoletwa na Bwana wetu Yesu Kristo na kuhubiriwa na mitume wake. Kwa ufupi sisi wote tuliomwamini Yesu Kristo katika agano hili jipya, kwa pamoja tunauimba wimbo wa mwana-kondoo. Ndio maana kiini cha imani, na wokovu wetu ni Yesu Kristo. Mtu yeyote ambaye hajaoshwa dhambi zake kwa damu ya Yesu, hawezi kumwona Mungu, wala kamwe hataweza kumwelewa, haijalishi ataonyesha bidii zake nyingi kiasi gani. Kwasababu ndio utimilifu wote.

Lakini upo wimbo mwingine wa Tatu ndio huo wimbo mpya.

Wimbo huu, si wote watakaoweza kuuimba, lakini watakaoweza kuuimba watakuwa karibu sana na mwana-kondoo (Yesu Kristo), baada ya maisha haya. Ndio wale washindao, Ndio wale Yesu aliosema atawakiri mbele ya Baba na malaika zake, ndio wale watakaoketi pamoja naye katika viti vya enzi, ndio wale watakaotoka mashariki, magharibi, kaskazini na kusini, kula mkate naye mezani pake. Na vigezo amevianisha pale. Anasema..

Ufunuo 14:1  Kisha nikaona, na tazama, huyo Mwana-Kondoo amesimama juu ya mlima Sayuni, na watu mia na arobaini na nne elfu pamoja naye, wenye jina lake na jina la Baba yake limeandikwa katika vipaji vya nyuso zao.

2  Nami nikasikia sauti kutoka mbinguni, kama sauti ya maji mengi, na kama sauti ya radi kuu. Na hiyo sauti niliyoisikia ilikuwa kama sauti ya wapiga vinubi, wakivipiga vinubi vyao;

3  na KUIMBA WIMBO MPYA mbele ya kile kiti cha enzi, na mbele ya wale wenye uhai wanne, na wale wazee; WALA HAPANA MTU ALIYEWEZA KUJIFUNZA WIMBO ULE, ila wale mia na arobaini na nne elfu, WALIONUNULIWA KATIKA NCHI.

4  HAWA NDIO WASIOTIWA UNAJISI PAMOJA NA WANAWAKE, KWA MAANA NI BIKIRA. Hawa ndio wamfuatao Mwana-Kondoo kila aendako. Hawa wamenunuliwa katika wanadamu, malimbuko kwa Mungu na kwa Mwana-Kondoo.

5  NA KATIKA VINYWA VYAO HAUKUONEKANA UONGO. MAANA HAWANA MAWAA

Kama tunavyoweza kuona hapo tabia za wale walioweza kuuimba wimbo huo ni mbili;

  1. Hawakutiwa unajisi na wanawake.

Hapo hamaanishi kuwa hawakuwa wazinzi, hapana, (ni kweli uzinzi sio jambo lao) bali anamaanisha hasaa uzinzi wa rohoni, yaani Kumwabudu Mungu pamoja na sanamu. Na sanamu kwa wakati wetu si tu vile vinyago vya kuchonga tu, bali pia ni kitu chochote kinachochukua nafasi ya Mungu wako moyoni. Wengine mali, wengine tv,  wengine mipira, wengine elimu, wengine ma-magemu, wengine ushirikina, wengine udhehebu. Hizo ni sanamu, unapozidhibiti wewe kama mkristo hiyo ni hatua mojawapo ya kuweza kuuimba wimbo huo mpya.

Lakini anasema..

  1. Katika vinywa vyao haukuonekana uongo, maana hawana mawaa.

Ni watu walionena kweli yote ya  Mungu (injili ya Kristo), wala hawakuibatilisha kwa ajili ya fedha, au maslahi, au cheo, au unafki au wafuasi. Bali waliitetea kweli yote ya Mungu na kuiishi pia, . Maana yake mimi na wewe tukiinena kweli ya Kristo na kuiishi, basi vinywani mwetu tunakuwa hatuna uongo.

Na matokeo ya mtu wa jinsi hii, ni kwamba anakuwa nafasi maalumu sana mbinguni(Ufunuo 5:8-9), Ni sawa na leo unajisikiaje unapoitwa uishi ikulu na raisi wako? Unajisikiaje kila mahali aendapo na msafara wake wewe upo pamoja naye. Anapopokea heshimu, na wewe unapokea naye.

Hivyo bidii ina malipo. Nyakati tulizonazo sio kusema nimeokoka hiyo inatosha!.. Ni nyakati za kujifunza wimbo huu mpya kwa bidii. Kutijahidi kumpendeza Bwana. Na yeye mwenyewe ameahidi neema yake itatusaidia.

Bwana akubariki.

Washirikishe na wengine habari hizi njema kwa kushea

Ikiwa utapenda kupata msaada wa kumpokea Yesu maishani mwako bure, Basi wasiliana nasi kwa namba uzionazo chini ya makala hii.

Pia kwa kupokea mafundisho ya kila siku kwa njia ya WHATSAPP, jiunge na channel yetu kwa kupofya link hii >> https://whatsapp.com/channel/0029VaBVhuA3WHTbKoz8jx10

Kwa mawasiliano: +255789001312 au +255693036618

Bwana akubariki.

Mafundisho mengine:

KARAMU YA MWANA-KONDOO.

JE! NI DHAMBI KUIMBA WIMBO WA TAIFA?

Nanyi mtamweka hata siku ya kumi na nne ya mwezi ule ule(Kutoka 12:4)

Rudi Nyumbani

Print this post

Machela ni nini (Wimbo ulio bora 3:7)

Jibu: Turejee…

Wimbo 3:7 “Tazama, ni MACHELA yake Sulemani; Mashujaa sitini waizunguka, Wa mashujaa wa Israeli”

“Machela” yanayozungumziwa hapo si vile vitanda vinavyotumika zama hizi kwaajili ya kubebea wagonjwa walio mahutihuti!..Bali vilikuwa ni vitanda maalumu vilivyotumika kubebea Wafalme na Mamalkia enzi za zamani, walipotembea kutoka sehemu moja kwenda nyingine (umbali mfupi).

Kutokana na zama kubadilika, matumizi ya Machela kubebea wakuu wa nchi hayapo tena, bali sasa yanatumika magari ya kimakenika, na Machela yamebaki kuwa na matumizi ya kubebea wagonjwa wa dharura walio katika hali ya umahutihuti,..na zaidi sana Machela za zama hizi yana magurudumu na hayabebwi tena kwa mikono kama yale ya zamani.

Kasoro moja ya Machela ya zama za zamani ambayo yaliwabeba wafalme ni kwamba hayakuwa na uimara wa kutosha, kiasi kwamba ikitokea ajali kwa waliombeba bali yule aliyebebwa anaweza kuanguka, na pia kwasababu mwendo wa wanadamu unatofuatiana, hivyo basi hata aliyebebwa wakati wa safari atahisi hali ya kupanda na kushuka, au kurushwa rushwa, na kupepesuka na hivyo yupo hatarini saa yoyote kuanguka..

Na vivyo hivyo, dunia imefananishwa na mfalme aliyebebwa kwenye machela, anawaya-waya, anapepesuka wakati wowote yupo hatarini kuanguka (yupo katika wasiwasi).

Isaya  24:19 “Dunia kuvunjika, inavunjika sana; dunia kupasuka, imepasuka sana; dunia kutikisika, imetikisika sana.

20 Dunia inalewa-lewa kama mlevi, NAYO INAWAYA-WAYA KAMA MACHELA; na mzigo wa dhambi zake utailemea; nayo itaanguka, wala haitainuka tena.

21 Tena itakuwa katika siku hiyo, Bwana ataliadhibu jeshi la mahali palipo juu katika mahali palipo juu, na wafalme wa dunia katika dunia”

Kama dunia inawaya-waya, ya nini kuitumainia??.. Na kwanini inawaya-waya?..ni kwasababu imekaribia mwisho wake, wakati wowote inaisha…na kinachoifanya iwayewaye si kingine Zaidi ya Dhambi, iliyojaa ndani yake.

Kwa urefu zaidi kuhusu kuwaya-waya kwa dunia fungua hapa >>> Dunia inalewa-lewa kama mlevi, nayo inawaya-waya kama machela.

Je umempokea YESU maishani mwako?..au na wewe unawaya-waya na dunia?…anasa zimekutawala, udunia umekushika..ni wakati sasa wa kuikimbia dunia na mambo yake na kumfanya BWANA YESU kuwa msingi wa maisha yako.

Bwana akubariki.

Washirikishe na wengine habari hizi njema kwa kushea

Ikiwa utapenda kupata msaada wa kumpokea Yesu maishani mwako bure, Basi wasiliana nasi kwa namba uzionazo chini ya makala hii.

Pia kwa kupokea mafundisho ya kila siku kwa njia ya WHATSAPP, jiunge na channel yetu kwa kupofya link hii >> https://whatsapp.com/channel/0029VaBVhuA3WHTbKoz8jx10

Kwa mawasiliano: +255789001312 au +255693036618

Bwana akubariki.

Mafundisho mengine:

TOA HUDUMA ILIYO BORA.

Podo ni nini na umuhimu wake ni upi rohoni?

KWA KUWA ROHO BORA ILIKUWA NDANI YAKE.

Kimiami ni nini? (Wimbo ulio bora 2:9).

INGIENI KWA KUPITIA MLANGO ULIO MWEMBAMBA.

Rudi Nyumbani

Print this post

Kusanyiko la makini/ mkutano wa makini ni upi?

Katika agano la kale, Israeli walikuwa na makusanyiko mengi, ambapo walikutanika kumfanyia Mungu ibada, na kuzishika sikukuu. Lakini pia yalichaguliwa makusanyiko mengine yaliyoitwa mikutano/makusanyiko ya makini. Makusanyiko haya yalifanyika  katika siku ya saba ya sikukuu ya Pasaka, na siku ya nane, baada ya sikukuu ya vibanda. Katika siku hiyo hawakuruhusiwa kufanya kazi yoyote. Bali ilitengwa kwa ajili ya kujitakasa, au kujisogeza karibu na Mungu,

Hivi ni vifungu baadhi vinavyoielezea siku hiyo;

Hesabu 29:35 Tena siku ya nane mtakuwa na kusanyiko la makini sana; hamtafanya kazi yo yote ya utumishi;

36 lakini mtasongeza sadaka ya kuteketezwa, sadaka ya kusongezwa kwa moto, harufu ya kupendeza kwa Bwana; ng’ombe mume mmoja, na kondoo mume mmoja, na wana-kondoo waume wa mwaka wa kwanza wakamilifu saba.

Walawi 23:34 Nena na wana wa Israeli, uwaambie, Siku ya kumi na tano ya mwezi huo wa saba ni sikukuu ya vibanda muda wa siku saba kwa Bwana.

35 Siku ya kwanza kutakuwa na kusanyiko takatifu; msifanye kazi yo yote ya utumishi.

36 Mtamsongezea Bwana sadaka kwa moto siku saba; siku ya nane kutakuwa na kusanyiko takatifu kwenu; nanyi mtamsongezea Bwana sadaka kwa moto; ni mkutano wa makini huu; msifanye kazi yo yote ya utumishi

Kumbukumbu 16:8 Siku sita utakula mikate isiyotiwa chachu; na siku ya saba na uwe mkutano mtukufu kwa Bwana, Mungu wako, usifanye kazi yo yote.

Huo mkutano mtukufu ndio kusanyiko la makini.

Hekalu la kwanza pia lilipomalizika liliwekwa wakfu katika siku hii ya kusanyiko la makini

2Nyakati 7:9 Hata siku ya nane wakaita kusanyiko la makini; kwa maana walishika kuitakasa madhabahu siku saba, na sikukuu siku saba.

Sehemu  nyingine mikusanyiko hii iliitishwa rasmi, kwa lengo la kujimimina kwa Mungu kuomba, kwa ajili ya maovu na majanga ambayo yanaipata nchi. (Yoeli 1:14 – 2:15). Kusanyiko hili liliitwa pia kama kusanyiko  kuu.

Je! Ufunuo wake ni upi leo?

Kama vile tulivyo na mikusanyiko ya aina mbalimbali leo, mfano  ya shule ya jumapili, ya semina, ya injili n.k. Vivyo hivyo hatuna budi kuwa na makusanyiko ya makini. Ambayo ni mikusanyiko ya mifungo na maombi. Ambapo tunapata muda wa kujimimina kwa undani kabisa uweponi mwa Mungu, kumtaka aingilie kati mambo yetu.

Je! unaithamini? Mungu aliyesema tusiache kukusanyika pamoja (Waebrania 10:25). Hakumaanisha tu mikusanyiko ya jumapili, lakini pia ya mifungo na maombi.

Bwana akubariki.

Washirikishe na wengine habari hizi njema kwa kushea

Ikiwa utapenda kupata msaada wa kumpokea Yesu maishani mwako bure, Basi wasiliana nasi kwa namba uzionazo chini ya makala hii.

Pia kwa kupokea mafundisho ya kila siku kwa njia ya WHATSAPP, jiunge na channel yetu kwa kupofya link hii >> https://whatsapp.com/channel/0029VaBVhuA3WHTbKoz8jx10

Kwa mawasiliano: +255789001312 au +255693036618

Bwana akubariki.

Mafundisho mengine:

Rudi Nyumbani

Print this post

NYOSHA MKONO WAKO, UUGUSE MFUPA WAKE NA NYAMA YAKE.

Shetani huwa ana kauli zake, za uongo ambazo hupenda kuwaaminisha watu, kuwa kuna mambo mwanadamu hawezi kuyafanya akiwa hapa duniani hata iweje.

Tukisoma habari ya Ayubu wakati ule shetani alipokwenda kumshitaka kwa Mungu.

Mungu alipomuuliza kuhusu mwenendo wake, majibu ya shetani yalikuwa ni kwamba Mungu amemzungushia wigo, kutunza alivyonavyo, Na kama atapotezewa alivyonavyo, basi atamkufuru Mungu waziwazi. Hivyo Mungu akaruhusu shetani amjaribu Ayubu, amchukulie alivyo navyo vyote, lakini uongo wa kwanza, ukashindwa, alipoona Ayubu anamtukuza Bwana katika misiba yake. Hiyo ni kuonyesha kuwa mwanadamu yoyote anaweza  kuishi bila msukumo wa mali,wala mtu wala kitu chochote katika hii dunia.

Lakini baadaye tena, akaendelea mbele kuzungumza uongo mwingine, alipoona Ayubu bado yupo na Mungu, akamwambia Mungu, yote yanawezekana kwa mwanadamu kuvumilia, lakini hili la kuugusa mfupa wake,kumtesa, kamwe hawezi kuvumilia atakukufuru tu. Mimi ninawajua wanadamu uwezo huo hawana, nilishawafundisha pia huko duniani.

Ayubu 2:4 Shetani akamjibu Bwana, na kusema, Ngozi kwa ngozi, naam, yote aliyo nayo mtu atayatoa kwa ajili ya uhai wake.

5 Lakini sasa nyosha mkono wako, uuguse mfupa wake na nyama yake, naye atakukufuru mbele za uso wako.

6 Bwana akamwambia Shetani, Tazama, yeye yumo mkononi mwako; lakini tunza tu uhai wake.  7 Basi Shetani akatoka mbele za uso wa Bwana, akampiga Ayubu na majipu mabaya tangu wayo wa mguu hata utosi wa kichwa.

8 Naye akashika kigae cha kujikunia; akaketi majivuni.  9 Ndipo mkewe akamwambia, Je! Wewe hata sasa washikamana na utimilifu wako? Umkufuru Mungu, ukafe.

10 Lakini yeye akamwambia, Wewe wanena kama mmoja wa hao wanawake wapumbavu anenavyo. Je! Tupate mema mkononi mwa Mungu, nasi tusipate na mabaya? Katika mambo hayo yote Ayubu hakufanya dhambi kwa midomo yake.

Hilo nalo likashindikana. Kumbe mtu, hata kuupoteza uhai wake kwa ajili ya Kristo, linawezekana.

Ni nini Bwana anatufundisha kwa mawazo ya adui kwetu sisi ?

Leo hii ni rahisi sana kusikia, kauli kama, hakuna mtakatifu duniani! Ni rahisi kuona mtu anaanguka ovyo katika dhambi, na kutumia kisingizio kuwa yeye sio malaika. Utasikia kauli kama haiwezekani mtu kuacha vyote alivyonacho kwa ajili ya Kristo. Ndugu tambua kuwa hizo ni kauli za ibilisi ndani ya moyo wako. Adui anapenda kumshusha thamani mtu, kumweka kama kiumbe ambaye hawezi kujisimamia, hafundishiki, haaminiki.

Ni kweli mwanadamu kuwa na ukamilifu wa Mungu haiwezekani (Ndio sababu Yesu akaja kutukomboa), lakini kuna viwango Fulani Mungu anajua tunaweza kuvifikia, akalithibitisha hilo kwa Ayubu. Kama Ayubu ameweza kwanini wewe ushindwe, usijishushe thamani.

Neema haijaja kutuambia kuwa sisi hatuwezi, bali  imekuja kutuwezesha zaidi kuwa wakamilifu mbele za Mungu, yaani pale Ayubu aliposhindwa sisi tunasaidiwa kwa hiyo, na kutufanya tupokelewe kikamilifu mbele za Mungu, hiyo ndio kazi ya Neema (Soma Tito 2:11-12).

Kamwe usiruhusu hayo maneno ya kushushwa thamani na ibilisi, kwamba wewe huwezi mpendeza Mungu, huwezi kuacha vyote kwa ajili yake. Yesu  alisema tutakuwa wakamilifu kama Baba yetu alivyomkamilifu. Tunachopaswa kufanya ni kuamini kuwa hilo linawezekana na kuonyesha bidii katika hilo kumpendeza yeye. Na neema ya Mungu itatusaidia kufikia kilele Hicho cha juu kabisa.

Bwana akubariki.

Washirikishe na wengine habari hizi njema kwa kushea

Ikiwa utapenda kupata msaada wa kumpokea Yesu maishani mwako bure, Basi wasiliana nasi kwa namba uzionazo chini ya makala hii.

Pia kwa kupokea mafundisho ya kila siku kwa njia ya WHATSAPP, jiunge na channel yetu kwa kupofya link hii >>https://whatsapp.com/channel/0029VaBVhuA3WHTbKoz8jx10

Kwa mawasiliano: +255789001312 au +255693036618

Bwana akubariki.

Mafundisho mengine:

VITABU VYA BIBLIA: Sehemu ya 9 (Kitabu cha Ayubu).

ILI TUONEKANE WAKAMILIFU MBELE ZA MUNGU.

Kwanini Labani aseme Yakobo ni Mfupa wake na nyama yake?(Mwanzo 29:14)

Rudi Nyumbani

Print this post

IFAHAMU KANUNI YA KUTAKA NA KUPATA.

Warumi 7:18  “Kwa maana najua ya kuwa ndani yangu, yaani, ndani ya mwili wangu, halikai neno jema; kwa kuwa KUTAKA NATAKA, bali KUTENDA LILILO JEMA SIPATI.

19  Kwa maana lile jema nilipendalo, silitendi; bali lile baya nisilolipenda ndilo nilitendalo”.

Je na wewe ni miongoni mwa watu wanaosumbuliwa na utumwa wa namna hiyo?.. UNATAKA na kutamani lakini unajikuta HUPATI au HUWEZI au HUFANYI au HUPOKEI?.

> Unataka kumtumikia Mungu lakini unajikuta huwezi..

> Unataka kuwa msomaji wa Neno lakini unajikuta hufanikiwi.

> Unataka na kutamani kufanya mema na mazuri kwaajili ya Mungu wako lakini hufanikiwi n.k

Kama UMETAKA mambo mengi na huoni uelekeo wa kulipata, basi huwenda NJIA unayoitumia kutaka na kutafuta hayo mambo ina kasoro..

Hebu jaribu njia hii, ya kutaka mambo halafu uone kama hutapata uyatakayo,

Na njia hii si nyingine Zaidi ya ile aliyoitumia Danieli.

Danieli 9:3 “Nikamwelekezea Bwana Mungu uso wangu, ILI KUTAKA kwa MAOMBI, NA DUA, PAMOJA NA KUFUNGA, NA KUVAA NGUO ZA MAGUNIA NA MAJIVU. 

4 Nikamwomba Bwana, Mungu wangu, nikaungama, nikasema, Ee Bwana, Mungu mkuu, mwenye kutisha, ashikaye maagano na rehema kwao wampendao, na kuzishika amri zake”

Umeona kanuni Danieli aliyoitumia??… HAKUTAKA mambo kwa kupiga ramli, au kwenda kwa waganga wa kienyeji, wala kwa kwenda Kuwadhulumu watu au kukorofishana na watu au kula rushwa, au kujipendekeza kwa watu bali KWA MAOMBI, NA DUA NA KUFUNGA NA KUVAA NGUO ZA MAGUNIA NA MAJIVU, na matokeo yake alipata alichokuwa anakitafuta..

Na sisi tunajifunza mambo hayo hayo…

> Tukitaka Amani nyumbani.. kanuni ni hiyo > Kufunga na Kuomba.

> Tukitaka Amani katika ndoa.. Kanuni ni hiyo > Kufunga na Kuomba.

> Tukitaka Amani kazini.. Kanuni ni hiyo > Kufunga na Kuomba.

> Tukitaka Akili darasani.. Kanuni ni hiyo > Kufunga na Kuomba.

> Tukitaka Ulinzi na afya.. Kanuni ni hiyo > Kufunga na Kuomba.

> Tukitaka Ujazo wa Roho Mtakatifu.. Kanuni ni hiyo > Kufunga na Kuomba.

Luka 11:13 “Basi, ikiwa ninyi mlio waovu mnajua kuwapa watoto wenu vipawa vyema, je! Baba aliye mbinguni hatazidi sana kuwapa Roho Mtakatifu hao wamwombao?”

Kama Bwana YESU alivyosema kuwa “kuna mambo hayawezekaniki, isipokuwa kwa kufunga na kuomba”

Wafilipi 2:13 “Kwa maana ndiye Mungu atendaye kazi ndani yenu, KUTAKA KWENU na kutenda kwenu, kwa kulitimiza kusudi lake jema.

14  Yatendeni mambo yote pasipo manung’uniko wala mashindano”

Bwana atusaidie.

Washirikishe na wengine habari hizi njema kwa kushea

Ikiwa utapenda kupata msaada wa kumpokea Yesu maishani mwako bure, Basi wasiliana nasi kwa namba uzionazo chini ya makala hii.

Pia kwa kupokea mafundisho ya kila siku kwa njia ya WHATSAPP, jiunge na channel yetu kwa kupofya link hii >> https://whatsapp.com/channel/0029VaBVhuA3WHTbKoz8jx10

Kwa mawasiliano: +255789001312 au +255693036618

Bwana akubariki.

Mafundisho mengine:

KANUNI JUU YA KANUNI.

NJIA SAHIHI YA KUFUNGA.

MAMBO MENGINE HAYATOKI ISIPOKUWA KWA KUFUNGA.

Nini maana ya “Heri kuchagua jina jema kuliko mali nyingi”?

HIZI NI NYAKATI ZA KUFUNGA NA KUOMBA.

Rudi Nyumbani

Print this post

MAMBO YA KUZINGATIA WAKATI WA MFUNGO.

Yafuatayo ni mambo saba (7) ya kuzingatia wakati wa Mfungo.

1.MAOMBI

Mfungo wowote ili uwe ni mfungo ni lazima uambatane na Maombi.. Mfungo usiokuwa na maombi ni sawasawa na bunduki isiyo na risasi.

Marko 9:28 “Hata alipoingia nyumbani, wanafunzi wake wakamwuliza kwa faragha, Mbona sisi hatukuweza kumtoa?

29  Akawaambia, Namna hii haiwezi kutoka kwa neno lo lote, isipokuwa kwa kuomba”.

Mathayo 17:21  [Lakini namna hii haitoki ila kwa kusali na kufunga.]

Kila siku utakayofunga hakikisha unaomba, (tena maombi ya masafa marefu, tofauti na siku nyingine).

 2. KUWA MTULIVU.

Unapofunga usiwe mtu wa kuhangaika na kuzurura huku na kule, bali kuwa mtu wa faragha muda mwingi, wakati wa mfungo si wakati wa kuzurura kwenye makao ya watu, au vijiwe..kuwa mtulivu, tafuta maeno tulivu na omba.

3. ZUIA KINYWA.

Mfungo sio tu kujizuia kula na kunywa, bali pia kujizuia kuzungumza kupita kiasi…. Unapofunga si wakati wa kusema na kila mtu, si wakati wa kujiachia (hususani kwa watu wasio wa kiroho) bali ni wakati wa faragha wewe na Mungu wako (kwa kutafuta sauti ya Mungu kupitia maneno yake)

4. EPUKA MATENDO YA MWILI.

Kama ni mwanandoa jizuie kwa kiwango kikubwa au chote kukutana kimwili na mwenzi wako..Vile vile Kama unafanya shughuli fulani inayohusisha mwili wako, ipunguze kwa kiwango kikubwa..

5. PUNGUZA KIWANGO CHA KULA.

Mfungo sio kuhamisha mlo wa asubuhi na mchana na kuupeleka jioni..La! bali ni  kuunyima mwili ili roho yako ije juu (inufaike).. Maana yake wakati wa kufungua (kufuturu) usile kiwango kikubwa cha chakula, kwa kufidia mlo wa asubuhi na mchana.. Ukifanya hivyo utakuwa hutendi dhambi, lakini mfungo wako unaweza usiwe na matokeo makubwa kama wa yule ajizuiaye kweli kweli.

6.USILE VYAKULA VITAMU-TAMU.

Wakati wa kufungua epuka kula vyakula vitamu tamu, hususani vile unavyovipenda sana, ambavyo vinakuburudisha sana.. “Kumbuka tena mfungo ni kuunyima mwili na si kuupendeza mwili”… Sasa unapoupa vile vitu ambavyo unavipenda sana, hapo bado kuna kaukasoro katika mfungo wako..

Danieli alikuwa ni mtu aliyejinyima vitu vitamu wakati wa mfungo… na hatimaye mfungo wake ukawa na matokeo makubwa.

Danieli 10:2 “Katika siku zile mimi, Danielii, nalikuwa nikiomboleza muda wa majuma matatu kamili.

3 Sikula chakula kitamu, wala nyama wala divai haikuingia kinywani mwangu, wala sikujipaka mafuta kabisa, hata majuma matatu kamili yalipotimia”.

7. USIWE MTU WA KUJITANGAZA.

Mathayo 6:16 “Tena mfungapo, msiwe kama wanafiki wenye uso wa kukunjamana; maana hujiumbua nyuso zao, ili waonekane na watu kuwa wanafunga. Amin, nawaambia, wamekwisha kupata thawabu yao.

17  Bali wewe ufungapo, jipake mafuta kichwani, unawe uso;

18  ili usionekane na watu kuwa unafunga, ila na Baba yako aliye sirini; na Baba yako aonaye sirini atakujazi”.

Mfungo unapaswa uwe siri hususani kwa watu walio wa nje (yaani wasiohusiana na wewe).. Kwa ndugu yako wa karibu sana, au mke au mume au watoto, mfungo wako ni ngumu kuwa siri kwao, kwasababu unaishi nao katika maisha ya kila siku (hata usipowaambia watafahamu tu)..Hivyo unaweza kuwashirikisha ikiwa lengo lako si upokee utukufu kutoka kwao.

Vile vile kiongozi wako wa kiroho, au mpendwa mwenzako (wa Imani moja na wewe) unaweza kumshirikisha mfungo wako (ikiwa lengo lako si kupata utukufu kutoka kwake) bali kupokea hamasa au kumhamasisha (Hilo ni jambo jema).

Lakini kama lengo lako ni wewe uonekane kwao ili utukuzwe, basi mfungo huo unaweza usizae matunda yale mtu anayoyategemea..

Bwana akubariki.

Washirikishe na wengine habari hizi njema kwa kushea

Ikiwa utapenda kupata msaada wa kumpokea Yesu maishani mwako bure, Basi wasiliana nasi kwa namba uzionazo chini ya makala hii.

Pia kwa kupokea mafundisho ya kila siku kwa njia ya WHATSAPP, jiunge na channel yetu kwa kupofya link hii >> https://whatsapp.com/channel/0029VaBVhuA3WHTbKoz8jx10

Kwa mawasiliano: +255789001312 au +255693036618

Bwana akubariki.

Mafundisho mengine:

Je unaruhusiwa kufanya tendo la ndoa ukiwa katika mfungo?

Kwanini tunafunga na kuomba?

KWARESMA IPO KIMAANDIKO?

JUMATANO YA MAJIVU NI TENDO LA KIMAANDIKO?

REKEBISHA YAFUATAYO ILI UCHUMI WAKO UKAE SAWA.

Rudi Nyumbani

Print this post

TUNAPASWA TUWEJE WAKATI WA KUJA KWAKE  BWANA YESU?.

Ipo hali ambayo tunapaswa tukutwe nayo wakati wa kuja kwake Bwana YESU…na endapo akitukuta tupo nje na hiyo hali basi hatutaenda naye, badala yake tutabaki na kukumbana na hukumu ya MUNGU.

Sasa “hali” hiyo ni ipi?..

Hebu tusome maandiko yafuatayo.

1 Wathesalonike 5:23 “Mungu wa amani mwenyewe awatakase kabisa; nanyi nafsi zenu na roho zenu na miili yenu mhifadhiwe mwe kamili, bila lawama, WAKATI WA KUJA KWAKE BWANA WETU YESU KRISTO”.

Kumbe Bwana YESU atarudi tena!!!!….. na wakati atakaporudi anatazamia  tuwe tumetakasika katika maeneo hayo matatu 1) NAFSI 2) ROHO na 3)MWILI.

Vinginevyo mambo hayo matatu yasipokuwa masafi wakati wa kuja kwake Bwana YESU basi kuna hatari kubwa sana.

1.NAFSI.

Ndani ya nafsi kuna maamuzi, hisia na mawazo.. Hivi vinapaswa viwe visafi daima.

Na vinakuwaje visafi?… Kwa kumpokea YESU, kusoma Neno na kuomba.

Usipokuwa mwombaji nafsi yako haiwezi kuwa safi utakuwa mtu wa hasira tu, mtu wa uchungu tu..usipokuwa msomaji wa Neno la Mungu kamwe nafsi yako haiwezi kustahimili majaribu na pia utakuwa mtu usiye na mwongozo n.k.

2.ROHO.

Ndani ya roho ya mtu kuna uzima, na ndio chumba pekee cha ibada ambacho kinaongozwa na Imani. 

Roho ya mtu isipokuwa safi, mtu huyo hawezi kwenda na Bwana siku ya unyakuo…na hata maisha yake ya duniani hawezi kumwona Mungu.

3. MWILI.

Mwili ni vazi la roho ya mtu, na ndilo limejumuisha viungo vyote vya ndani na nje.

Na mwili unapaswa uwe safi (usafi wa kimatendo)..Mwili mchafu kibiblia sio ule wenye jasho au vumbi…mwili mchafu ni ule unaofanya uasherati na zinaa, ni ule unaojichua, ni ule unaotembezwa uchi barabarani, ni ule unaoshika fedha za wizi na utapeli.

Huo ndio mwili mchafu, ambao kama hautatakaswa wakati wa kuja kwake Bwana utampoteza mtu huyo.

Na mtu hautakasi mwili wake kwa kuoga na maji moto, au kwa kumeza vidonge vya matibabu au mitishamba…bali kwa kuacha matendo yote ya mwili yanayotajwa katika Wagalatia 5:19-20.

Wagalatia 5:19 “Basi matendo ya mwili ni dhahiri, ndiyo haya, uasherati, uchafu, ufisadi, 

20 ibada ya sanamu, uchawi, uadui, ugomvi, wivu, hasira, fitina, faraka, uzushi, 

21 husuda, ulevi, ulafi, na mambo yanayofanana na hayo, katika hayo nawaambia mapema, kama nilivyokwisha kuwaambia, ya kwamba watu watendao mambo ya jinsi hiyo hawataurithi ufalme wa Mungu”.

Kwa hitimisho ni kwamba kila mtu lazima ajitakase na kuhifadhi utakaso wake ambao ndio tiketi ya kumwona Bwana siku atakaporudi.

1 Wathesalonike 5:23 “Mungu wa amani mwenyewe awatakase kabisa; nanyi nafsi zenu na roho zenu na miili yenu mhifadhiwe mwe kamili, bila lawama, WAKATI WA KUJA KWAKE BWANA WETU YESU KRISTO”.

Je umempokea Bwana YESU?…Kama bado unasubiri nini??… Na kama tayari umeshampokea je! umetakaswa nafso yako, roho yako na mwili wako?..

Kwa mwongozo wa maombi ya kujijenga kiroho juu ya mambo hayo matatu (nafsi, mwili na roho) basi wasiliana nasi inbox.

Maran atha!.

Washirikishe na wengine habari hizi njema kwa kushea

Ikiwa utapenda kupata msaada wa kumpokea Yesu maishani mwako bure, Basi wasiliana nasi kwa namba uzionazo chini ya makala hii.

Pia kwa kupokea mafundisho ya kila siku kwa njia ya WHATSAPP, jiunge na channel yetu kwa kupofya link hii >> https://whatsapp.com/channel/0029VaBVhuA3WHTbKoz8jx10

Kwa mawasiliano: +255789001312 au +255693036618

Bwana akubariki.

Mafundisho mengine:

MCHE MWORORO.

KWANINI TUNAPASWA KWENDA KUIHUBIRI INJILI KWA UJASIRI WOTE?

Biblia inaposema “Wote tumetenda dhambi” si inamaanisha hakuna mtakatifu duniani?

JITAHIDI KUJA KABLA YA WAKATI WA BARIDI.

Biblia inamaanisha nini kusema Yeye aliye na sikio, na asikie?

Rudi Nyumbani

Print this post

MWOMBENI BWANA WA MAVUNO APELEKE WATENDA KAZI.

(Masomo ya kanuni za kuomba).

Mathayo 9:38 “Basi mwombeni Bwana wa mavuno, apeleke watenda kazi katika mavuno yake”.

Maombi ni jambo kuu na la msingi sana.

Hapa biblia inasema TUOMBE (Bwana apeleke watenda kazi).

Kumbe Maombi ya kuomba uamsho wa watenda kazi ni muhumu!. Kwasababu hiyo basi ni lazima tujiwekee utaratibu wa mara kwa mara kuomba Bwana aongezee watenda kazi.

Na yafuatayo ni baadhi ya maeneno yanayohitaji watenda kazi zaidi.

1.KANISANI.

Hii ni sehemu ya kwanza inayohitaji watenda kazi. Waalimu wa madarasa ya jumapili wanahitajika zaidi ndani ya kanisa, halikadhalika waalimu wa watoto, pia watendakazi katika kuongoza sifa na maombi na wengine wengi.

Hivyo ni muhimu kutenga muda wa kutosha kumwomba BWANA anyanyue watenda kazi yeye anajua yupi anatafaa mahali fulani sisi kazi yetu ni kuzidi kumsihi Bwana awanyanyue wengi.

2. MASHULENI.

Shule kuanzia zile za awali (chekechea) mpaka zile za juu (vyuoni) panahitajika sana watenda kazi, watakaofanya kazi ya mavuno..

Hivyo ni muhimu watu wa Mungu kuomba ili Bwana anyanyue jeshi la watenda kazi (wahubiri) kwenye mashule.

Kwani mbali na mambo mazuri yanayopatikana mashuleni lakini.huko huko pia ndio kitovu cha watoto kujifunza tabia chafu na kupokea maroho ya mapepo.

Na wakati mwingine ni ngumu mtu wa nje kuwafikia na kuwahubiria, hivyo mimi na wewe tukisimama kumwomba Bwana anyanyue watenda kazi katikati yao, basi Bwana atatusikia na kunyanyua vijana miongoni mwao huko huko waliko ambao watawatengeneza wenzao au atawanyanyulia walimu miongoni mwa walimu wanaowafundisha na watawafundisha na kuwakuza kiroho.

3. MAHOSPITALINI.

Hii ni sehemu ya tatu inayohitaji watenda kazi.  Vituo vingi vya afya vinategemea kupokea watumishi kutoka nje kwaajili ya maombi kwa wagonjwa…

Wakati mwingine jambo hili linakuwa ni gumu sana, kutokana ni vizuizi vya kiserikali na uchache wa watenda kazi…na hivyo wagonjwa wengi wanakufa katika dhambi na wengine kuonewa vikali na ibilisi na mapepo yake yachocheayo magonjwa.

Lakini tukisimama kuomba kwamba Bwana anyanyue watenda kazi basi, Bwana atasikia kwasababu ndiye aloyetuambia tuombe.

Na matokeo ya kuomba ni madaktari wengi kuokoka na manesi na wahudumu wa vituo hivyo vya afya na hivyo wagonjwa wengi wataombewa na kufunguliwa na kumpokea BWANA YESU, pasipo kusubiri watumishi kutoka nje.

4. SERIKALINI.

Hii ni sehemu ya nne inayohitaji watenda kazi wengi…kwani huko serikalini ikiwemo katika mabunge, wizara na mahakama, adui anadhulumu wengi na kuwapoteza wengi, na hiyo ni kutokana na upungufu wa watenda kazi.

Lakini tukisimama kuomba, Bwana YESU atasikia na kunyanyua watenda kazi ndani ya serikali..Watanyanyuka watu mfano wa akina Danieli na Yusufu ambao watahubiri na kufundisha na kukemea kazi za ibilisi katika mahakama, bunge na katika asasi zote za serikali.

5. MITAANI.

Hili ni eneo la tano linalohitaji watenda kazi wengi…Kwani katika mitaa ndiko watu wanakofanyia kazi, wanakokusanyika katika vigenge vya mizaha, au wanakofanyia mabaya.

Hivyo kunahitajika injili sana, ili watu waokolewe… na wakati mwingine inakuwa ni ngumu kufika kila mtaa kuhibiri, au watumishi wa Mungu kuzunguka kila mahali kuhubiri na kuombea watu.

Lakini kama tukisimama kumwomba BWANA anyanyue watenda huko basi kazi (katikati ya hao hao wahuni, au hao hao wanaofanya kazi haramu, au wanaoketi katika vijiwe vya mizaha) basi kazi ya injil itakuwa nyepesi sana na yenye matunda mengi.

Tutashangaa kuona wale waliokuwa walevi namba moja ndio wahubiri namba moja, wale waliokuwa makahaba namba moja ndio wainjilisti namba moja n.k

6. MITANDAONI

Hii ni sehemu ya sita na muhimu sana inayohitaji watenda kazi.

Kwani katika mitandao ndiko watu wanakojifunzia mambo yote maovu, ndani ya mitandao watu wanajifunza  mauaji, kiburi, uasherati, uchawi, utapeli, wizi na mambo yote mabaya ambayo biblia inayataja kama malango ya kuzimu.

Na wanaotumia mitandao hiyo kuhubiri habari njema ni wachache ukikinganisha na wale wanaoitumia kusambaza maovu.

Lakini tukisimama na kumwomba Bwana awageuze watu na kuwafanya watenda kazi shambani mwake, tutaona mageuzi makubwa.

Kwani wale waliokuwa wanahamasisha wizi, uasherati, utapeli na uhuni ndio watakaokuwa vipaumbele kuitumia mitandao hiyo hiyo kumhubiri YESU na kusaidia wengi,..

Wale waliokuwa watangazaji watageuzwa na kutangaza habari njema, wale waliokuwa waigizaji wa tamthilia za mapenzi ya kishetani sasa wanatengeneza mafundisha ya kuwajenga watu kiroho n.k

Lakini ikiwa tutaomba kwa bidii sana.

Hayo ni meneo sita yanayohitaji watenda kazi, yapo na maeneo mengine mengi lakini haya sita ndio yenye vipaumbele zaidi.

Hivyo kama mtu uliyeokoka usiishie tu kuombea familia yako, au kazi zako au ndugu zako au kanisa lako..

Piga hatua zaidi kuombea ongezeko la watenda kazi katika shamba la Mungu, kwani maombi hayo ni ya muhimu na yenye thawabu nyingi.

Mathayo 9:38 “Basi mwombeni Bwana wa mavuno, apeleke watenda kazi katika mavuno yake”.

Maran atha.

Washirikishe na wengine habari hizi njema kwa kushea

Ikiwa utapenda kupata msaada wa kumpokea Yesu maishani mwako bure, Basi wasiliana nasi kwa namba uzionazo chini ya makala hii.

Pia kwa kupokea mafundisho ya kila siku kwa njia ya WHATSAPP, jiunge na channel yetu kwa kupofya link hii >> https://whatsapp.com/channel/0029VaBVhuA3WHTbKoz8jx10

Kwa mawasiliano: +255789001312 au +255693036618

Bwana akubariki.

Mafundisho mengine:

 MAVUNO NI MENGI

MWISHO WA MAVUNO, NI MWISHO WA DUNIA.

Kuomba katika roho ni kupi? na je nifanye nini ili niweze kuomba hivyo?

Fahamu Namna ya Kuomba.

VIACHENI VYOTE VIKUE HATA WAKATI WA MAVUNO.

Rudi Nyumbani

Print this post

Je ni malaika wawili au mmoja?

Je ni malaika wawili au mmoja

Swali: Katika Luka 24:4-6, biblia inasema ni malaika wawili..lakini tukirudi katika Marko 16:5-6 tunasoma ni malaika mmoja. Je biblia inajichanganya, au mwandishi yupi yupo sahihi?.


Jibu: Turejee..

Marko 16:5 “Wakaingia kaburini wakaona kijana ameketi upande wa kuume, amevaa vazi jeupe; wakastaajabu”.

Ni kweli hapa biblia inasema ni malaika mmoja, tena ni kijana.

Lakini hebu twende kwenye Luka, tuanzie ule mstari wa 4 hadi wa 6.

Luka 24:4“Ikawa walipokuwa wakifadhaika kwa ajili ya neno hilo, tazama, watu wawili walisimama karibu nao, wamevaa nguo za kumeta-meta; 

5 nao walipoingiwa na hofu na kuinama kifudifudi hata nchi, HAO WALIWAAMBIA, Kwa nini mnamtafuta aliye hai katika wafu? 

6 Hayupo hapa, amefufuka. Kumbukeni alivyosema nanyi alipokuwa akaliko Galilaya”

Je ni kwamba biblia inajichanganya? Au kuna mwandishi ambaye hayupo sahihi?.

Jibu ni la! Biblia haijichanganyi na wala haijawahi kujichanganya kabisa isipokuwa tafakari zetu ndio zinajichanganya.

Sasa katika maandiko hayo hakuna mwandishi aliyekosea wala anayempiga mwenzake.

Waandishi wote wapo sahihi na malaika waliowatokea ni wanawake wale walikuwa ni wawili na si mmoja.

Isipokuwa malaika aliyesema na wanawake wale ni mmoja kati ya wale wawili na ndiye huyo aliyetajwa na Marko.

Tunajuaje kuwa ni malaika mmoja ndiye aliyekuwa anazungumza na mwingine amenyamaza?.

Tunafahamu kupitia mwandishi wa kitabu cha Luka ule mstari wa 5 unaosema…. “nao walipoingiwa na hofu na kuinama kifudifudi hata nchi, HAO WALIWAAMBIA, Kwa nini mnamtafuta aliye hai katika wafu?….

Hapo anasema “Hao waliwaambia”…sasa kwa kauli hiyo isingewezekana wote waseme kwa pamoja maneno hayo kama maroboti…Ni wazi kuwa ni malaika mmoja ndiye aliyetoa hiyo kauli na hivyo ikawa ni sawa wote wamesema.

Na huyo mmoja aliyetoa hiyo kauli ndiye anayetajwa na Marko…lakini Luka anataja uwepo wa wote wawili.

Ili tuelewe vizuri tutafakari mfano huu… wanahabari wawili wanaripoti hotuba ya Raisi na wa kwanza akasema hivi…. “Raisi wa nchi ya Tanzania amezuia matumizi ya vifungashio vya plastiki”…

Na mwandishi mwingine wa nje aripoti hivi..”Watanzania wazuia matumizi ya vifungashio vya plastiki”.

Je waandishi hawa watakuwa waongo?…au je kuna mmoja atakuwa anampinga mwenzake?..

Jibu ni la! Wote watakuwa sahihi kwani kauli na Raisi ni kauli ya watazania wote…atakalosema Raisi ni sawa na watanzania wote wamesema.

Sawa sawa kabisa na hiyo mwandishi wa Luka…alitaja kauli ya ujumla ya malaika wote wawili na Marko akataja ya mmoja tu (yule aliyetoa kauli).

Je umempokea Bwana YESU KRISTO?.

Kama bado unasubiri nini?..ule mwisho umekaribia sana na Bwana YESU amekaribia kurudi sana.

Ikiwa utahitaji msaada wa kumpokea Bwana YESU basi waweza wasiliana nasi na tutakuongoza sala ya kumkiri Bwana YESU baada ya wewe kumwamini.

Bwana akubariki.

Washirikishe na wengine habari hizi njema kwa kushea

Ikiwa utapenda kupata msaada wa kumpokea Yesu maishani mwako bure, Basi wasiliana nasi kwa namba uzionazo chini ya makala hii.

Pia kwa kupokea mafundisho ya kila siku kwa njia ya WHATSAPP, jiunge na channel yetu kwa kupofya link hii >> https://whatsapp.com/channel/0029VaBVhuA3WHTbKoz8jx10

Kwa mawasiliano: +255789001312 au +255693036618

Bwana akubariki.

Mafundisho mengine:

Je kauli ya Bwana Yesu inajichanganya? Katika Yohana 8:14 na Yohana 5:31?

WAZAZI WA YOHANA NA YAKOBO

Forodhani ni mahali gani?

Biblia inaposema Yesu ameketi mkono wa kuume inamaana gani?

DANIELI: Mlango wa 11

Rudi Nyumbani

Print this post

TIA MIZIZI CHINI, ILI UZAE MATUNDA JUU.

Nakusalimu katika jina la Bwana Yesu Kristo, Karibu tujifunze habari njema za uzima wa roho zetu.

  Neno la Mungu linatuambia..

2 Wafalme 19:30

[30]Na mabaki yaliyookoka ya nyumba ya Yuda yatatia mizizi chini, na kuzaa matunda juu. 

Unaelewa maana ya mstari huu? Anazungumzia kustawi kwa nyumba ya Yuda (ambao ndio sisi kanisa)..

Lakini kustawi kwake hakuji hivi hivi, matunda yake kutokea kule juu, anasema kanuni yake ni lazima pia mizizi yake ikite chini.

Haiwezekani mti ukazaa kama hauna mzizi, jiulize je wewe una mizizi imara ya rohoni, ya kukufanya uweze kuzaa matunda yampendezayo Bwana?

Kumbuka kuthamini kwako wokovu, ndivyo hueleza urefu wa mizizi yako yenye nguvu, itakayokuwezesha kustawisha matunda juu.

Jani haliihitaji mizizi yoyote ya maana, kwasababu halina matunda ya kutoa. 

Ukiona huwezi kuzama ndani katika wokovu, hauwi siriazi na maisha yako ya rohoni ujue pia hautakuwa na matunda yoyote kwa Mungu wako.

Katika ule mfano wa mpanzi Bwana Yesu alieleza kitu kilichofanya ile mbegu ya nne kustawi mpaka kuzaa matunda..anasema ilizaa kwa kuvumilia.(Luka 8:15)

kuvumilia nini?

Kuvumilia hatua zote 3 za mwanzo. yaani alihakikisha adui haibi mbegu iliyopandwa ndani yake, ni mtu ambaye aliweza kuvumilia dhiki, na majaribu yaliyozuka kinyume na lile neno lililopandwa moyoni mwake, alijiepusha na anasa, na kutoruhusu masumbufu ya ulimwengu huu kumsonga akashindwa kuivisha chochote. Hayo ndio mambo aliyovumilia.

Huyu ni mtu ambaye yupo makini na wokovu alioupokea.

Swali la kujiuliza je tunayo matunda hayo? kumbuka Hayaji kwa kutamani au kusubiri yanakuja kwa urefu wa mizizi yetu yenye uwezo wa kufikia vyanzo vya chini kabisa vyenye virutubisho vyote vya kustawisha matunda.

Ndio maana biblia inasema

Zaburi 1:1-3

[1]Heri mtu yule asiyekwenda Katika shauri la wasio haki; Wala hakusimama katika njia ya wakosaji; Wala hakuketi barazani pa wenye mizaha.

[2]Bali sheria ya BWANA ndiyo impendezayo, Na sheria yake huitafakari mchana na usiku.

[3]Naye atakuwa kama mti uliopandwa Kandokando ya vijito vya maji, Uzaao matunda yake kwa majira yake, Wala jani lake halinyauki; Na kila alitendalo litafanikiwa. 

Anza sasa kushughulika na mizizi yako, mpaka ifikie kwa hakika mito hiyo ya maji.

Usipoe kimaombi, kimifungo, kiibada, kiuinjilisti, na kiusomaji Neno.

2 Wafalme 19:30

[30]Na mabaki yaliyookoka ya nyumba ya Yuda yatatia mizizi chini, na kuzaa matunda juu. 

Bwana akubariki.

Washirikishe na wengine habari hizi njema kwa kushea

Ikiwa utapenda kupata msaada wa kumpokea Yesu maishani mwako bure, Basi wasiliana nasi kwa namba uzionazo chini ya makala hii.

Pia kwa kupokea mafundisho ya kila siku kwa njia ya WHATSAPP, jiunge na channel yetu kwa kupofya link hii >> https://whatsapp.com/channel/0029VaBVhuA3WHTbKoz8jx10

Kwa mawasiliano: +255789001312 au +255693036618

Bwana akubariki.

Mafundisho mengine:

KWA KUVUMILIA AKAIPATA ILE AHADI.

Rudi Nyumbani

Print this post