Category Archive Wahubiri (Watumishi)

Jinsi ya kuandaa Somo la kufundisha

Jinsi ya kuandaa mahubiri ya kufundisha kanisani au kwenye semina.

Jinsi ya kuandaa mahubiri ya kufundisha kanisani au katika ibada. Zifuatazo ni dondoo chache zitakazoweza kukusaidia katika kuandaa Somo ambalo litakuwa na uvuvio wa Roho Mtakatifu.

1. Tafuta sehemu ya utulivu.

Hii ni hatua ya kwanza kabisa: Tafuta eneo lisilo na kelele, wala usumbufu, hakikisha husumbuliwi na mtu au simu. Hiyo inaweza kuwa katika chumba cha utulivu au mahali ambao hauwezi kusumbuliwa, Huo ni mlango wa kwanza unaouvuta uwepo wa Mungu karibu nawe, kwasababu maandiko yanasema Mungu wetu si Mungu wa machafuko (1Wakorintho 14:33) na pia ni Mungu anayezungumza katika mazingira tulivu.

1Wafalme 19:12 “na baada ya tetemeko la nchi kukawa na moto; lakini Bwana hakuwamo katika moto ule; na baada ya moto sauti ndogo, ya utulivu”.

Hivyo kabla ya kuanza kufikiri kuandaa somo au hubiri, jitenge na mazingira yote yatakayokuondolea utulivu, kwasababu ukikaa katika hayo mazingira hutamsikia Mungu, Hivyo zima simu kwa muda na pia kaa peke yako kwenye utulivu.

2. Kuwa na Kalamu na Karatasi.

Hii ni hatua ya pili: Andaa kalamu na karatasi kwasababu kabla ya kwenda kuwafundisha wengine, Roho Mtakatifu atakufundisha wewe kwanza.

Warumi 2:21  “basi wewe umfundishaye mwingine, je! Hujifundishi mwenyewe? Wewe uhubiriye kwamba mtu asiibe, waiba mwenyewe”

Kwahiyo wewe ni mwanafunzi wa kwanza wa Roho Mtakatifu kabla ya kwenda kuwafundisha wengine, na Mwanafunzi bora ni sharti awe na kalamu na karatasi kwa lengo la kuyarekodi yale anayojifunza. 

Usipokuwa na sehemu ya kurekodi yale utakayoenda kujifunza itakuwa ni ngumu hata kuyashika..

3. Fungua kwa Maombi.

Omba utakaso kwaajili ya nafsi yako, Omba uwepo wa Mungu ushuke mahali hapo, omba utakaso wa eneo ulilopo, omba roho ya ufunuo ishuke juu yako, kemea nguvu za giza na  zinazoshindana na azimio lako hilo (Tumia muda kidogo kuomba kwa kumaanisha).

4. Anza kusoma biblia na kutafakari

Baada ya maombi, anza kusoma biblia huku ukiruhusu akili yako itafakari. Wengi wakifika hii hatua wanafungua tu biblia na kutafuta mistari wanayoifahamu au watakayokutana nayo kwanza, pasipo kuruhusu tafakari katika fahamu zao.

Siri moja ya Roho Mtakatifu ni kwamba anazungumza na sisi pale tunapotafakari na si pale tunapoziba tafakari zetu. Unapokuwa katika kutafakari ndipo Roho Mtakatifu naye anaungana na tafakari zako pasipo kujua na ghafla unajikuta unafunguka akili na kujikuta unapokea vitu vipya, ambavyo ulikuwa huvijui, vitu hivyo vipya ambavyo ulikuwa huvijui vinavyokubaliana na Neno la Mungu ndio sauti ya Roho Mtakatifu, hivyo andiko hivyo ulivyovipokea kwasababu ndio vitakuwa sehemu ya somo lako ambalo Roho Mtakatifu anataka ujifunze wewe kwanza kisha ukawafundishe na wengine.

5. Omba tena

Hii ni hatua ya mwisho, baada ya kusoma na kutafakari kwa muda mrefu, na kupokea Funuo nyingi. Omba maombi ya mwisho ya kushukuru, kisha funga daftari lako.

Darasa lijalo tutajifunza jinsi ya kusimama na kufundisha kile ulichofundishwa na Roho Mtakatifu. Kwani ni muhimu pia kujua jinsi ya kufundisha ili usije ukajikuta unamzimisha Roho. (Kanuni ya kufundisha kwa matokeo yaliyokusudiwa ni rahisi sana, usikose darasa lijalo).

Maran atha

Tafadhali shea na wengine ujumbe huu;

Pia Kwa maombezi/ Ushauri/ Maswali/ Whatsapp:
Tuandikie katika BOXI la Maoni hapo chini au
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312

Mada Nyinginezo:

JE! UPO KATIKA MAJI YA UTULIVU?

NIFANYE NINI ILI MUNGU AYAJIBU MAOMBI YANGU?

Wanikolai ni watu gani? Katika biblia?

JINSI YA KUSOMA BIBLIA.

Guruguru na Goromoe ni wanyama gani? (Walawi 11:30)

Rudi nyumbani

Print this post

Fahamu maana ya Mithali 29:4 “Mfalme huithibitisha nchi kwa hukumu; Bali yeye apokeaye rushwa huipindua.

Mafundisho maalumu kwa watumishi wa Mungu (Wachungaji, Mitume, manabii, wainjilisti n.k.)

Mithali 29:4 “Mfalme huithibitisha nchi kwa hukumu; Bali yeye apokeaye rushwa huipindua”

Uongozi wa kidunia mara nyingi hutoa picha ya uongozi wa rohoni.

Kama andiko hilo linavyosema, “Mfalme huithibitisha nchi kwa hukumu; Bali yeye apokeaye rushwa huipindua” maana yake ni kuwa kiongozi anayetawala nchi na huku moyo wake ni wa rushwa, kamwe hilo taifa halitakaa liendelee vile ipasavyo.

Kwamfano, mtu anataka kupitisha bidhaa zisizo na ubora bandarini ili ziuzwe ndani ya nchi. Lakini taarifa zinamfikia kiongozi, badala Yule kiongozi azipige marufuku, anapokea pesa kutoka kwa wale wanaotaka kuingiza, hivyo athari inakwenda kwenye jamii kwa tamaa zake za mali.

Au anaingia mikataba ambayo haina manufaa kwa watu wake, kisa tu kaahidiwa atalipwa pesa nyingi kutoka kwao. Hivyo rushwa zipo nyingi sio tu za kipesa, lakini pia za kiuongozi, kisa Yule ni rafiki, au ndugu, anampa nafasi ya utawala, lakini Yule mwenye ujuzi na ueledi ananyimwa. Sasa taifa lake kiongozi huyu, haliwezi kusimama kwa namna yoyote.

Lakini akiwa ni wa haki (Mtoa hukumu za haki), ni lazima tu nchi hiyo itastawi, Kwasababu maandiko yanasema haki huinua taifa.

Mithali 14:34 ‘Haki huinua taifa; Bali dhambi ni aibu ya watu wo wote’.

Uongozi wa Rohoni.

Vivyo hivyo pia na viongozi wanaongoza kanisa la Kristo ambao kuna watu chini yao wanaowaangalia, katika ngazi yoyote iwe ni Maaskofu, Wachungaji, waalimu, wainjilisti, mitume na manabii. Wakiwa na mioyo ya rushwa ndani yao, kamwe kundi hilo halitathibitika.

Kwamfano, mchungaji anapendelea watu Fulani, anawapa nafasi ya uongozi au anawapa viti vya mbele, kisa tu wanachangia huduma kwa sehemu kubwa, hata kama haiwakidhi wanapewa kisa tu wana fedha nyingi, wanaachwa wale wenye uwezo wa Roho nyuma. Sasa Hiyo rohoni ni rushwa na ni mbaya sana kwa maendeleo ya kanisa.

Yakobo 2:1  Ndugu zangu, imani ya Bwana wetu Yesu Kristo, Bwana wa utukufu, msiwe nayo kwa kupendelea watu.2  Maana akiingia katika sinagogi lenu mtu mwenye pete ya dhahabu na mavazi mazuri; kisha akiingia na maskini, mwenye mavazi mabovu; 3  nanyi mkimstahi yule aliyevaa mavazi mazuri, na kumwambia, Keti wewe hapa mahali pazuri; na kumwambia yule maskini, Simama wewe pale, au keti miguuni pangu, 4  je! Hamkufanya hitilafu mioyoni mwenu, mkawa waamuzi wenye mawazo mabovu?

Mwingine atauza mafuta, au maji, au chumvi, kisha atasema ni lazima uvinunue ili upokee Baraka zako. Mwingine atasema ili unione mimi nikufanyie maombezi, toa kiwango Fulani, au nikutane na wewe kimwili. Hizo zote ni rushwa za kiroho na zinakuja kwa maumbile mengi sana.

Kunaweza kubuniwa michango ya aina mbalimbali katika kanisa, afadhali lengo lingekuwa ni kwa ajili ya maendeleo ya kazi ya Mungu, lakini unakuta lengo ni ili kiongozi apate fedha ajinufaishe maisha yake.

Mwingine anawachagua viongozi wa kanisani, kindugu, kisa Yule ni mjomba wake, au shemeji yake na kuacha wale walioteuliwa na Mungu.

Yote haya yakiwa ndani ya kiongozi yoyote, ambaye anasimama sio kwa ajili ya kundi bali kwa ajili ya nafsi yake. Kamwe mkusanyiko huo hauwezi kuendelea kiroho. Utazidi kudhoofika, kwasababu umekosa uongozi bora.

Ni vema kujihakiki wewe ambaye umeitwa kulichunga kundi, Maono yako ni nini kwa watu wa Mungu? Je! Ni Uwe tajiri na maarufu kupitia wao? Au ulijenge kanisa la Bwana? Kumbuka utatoa hesabu kwa utumishi wako siku ile ya mwisho, Na kama ukionekana uliwatesa na kuwanyanyasa utakatwa vipande viwili, kisha kutupwa katika ziwa la moto (Mathayo 24:48-51). Na adhabu yako inakuwa kubwa kushinda ya wengine kwasababu ulijua mapenzi ya Bwana wako lakini kwa makusudi hukuyafanya, Hivyo utaadhibiwa sana. Ogopa hukumu ya Mungu. Acha kuiga-iga mifumo ya makristo wa uongo. Tembea katika Neno, kielelezo chako akiwa Kristo ambaye hakuwa na upendeleo wala tamaa ya vitu.

Siku hizi ni siku za mwisho, tubu dhambi zako mgeukie Bwana kwa kumaanisha badili namna ya uongozi wako, simamia haki ya Mungu, uthibitike katika utumishi huo.

Bwana akubariki.

Shalom.

Tafadhali shea na wengine ujumbe huu;

Pia Kwa maombezi/ Ushauri/ Maswali/ Whatsapp:
Tuandikie katika BOXI la Maoni hapo chini au
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312

Mada Nyinginezo:

Vifungu vya biblia kuhusu Uongozi.

Nini maana ya Mhubiri 10:16, inaposema Ole wako, nchi, akiwa mfalme wako ni kijana?

Rushwa inapofushaje macho?

Fanya bidii kuijua hali ya makundi yako (Mithali 27:23)

ROHO YA MPINGA KRISTO IKITENDA KAZI SIKU HIZI ZA MWISHO

Bwana alimaanisha nini kusema “Mwanafunzi hawi mkuu kuliko mwalimu wake”?

Rudi nyumbani

Print this post

Fanya bidii kuijua hali ya makundi yako (Mithali 27:23)

Haya ni Mafundisho maalumu Kwa ajili ya watumishi, ikiwa wewe ni kiongozi, askofu, mwalimu, mchungaji, mtume, mwinjilisti, unayesimama mahali fulani katika kulitazama kundi la Bwana, au jamii ya watu waliookoka, basi mafundisho haya ni maalumu kwako.

Biblia inasema;

Mithali 27:23

[23]Fanya bidii kuijua hali ya makundi yako;  Na kuwaangalia sana ng’ombe zako.

Mchungaji Bora sikuzote anatambua ni wajibu wake kuwa karibu na mifugo yake wakati mwingi. Ili Kuhakikisha Mahali wanapolala ni salama, wanaogeshwa Kila wakati, wanapata chakula Bora, afya zao pia ni njema na wanachungwa Mahali salama.

 Kwamfano kama mchungaji akiwa Hana desturi ya kwenda zizini. Tunajua mifugo Kwa kawaida Huwa Haijui kujisafisha yenyewe, matokeo yake ni kwamba lile zizi litajaa vinyesi na mwisho wa siku watapata magonjwa na kufa, na hasara inaangukia kwa mchungaji?

Vilevile akiiachia mifugo yake ianze kujichunga yenyewe, inaenda popote iwezavyo kujitafutia chakula, bila shaka itapotea, kama sio kuibiwa, au kuliwa na wanyama wakali, au kula vitu visivyostahili.

Hivyo utaona ni sharti Mahali palipo na mifugo, hapapaswi kukosekana mchungaji hata kidogo. Hii inatufundisha sisi tulio watumishi, kuhakikisha tunafahamu Hali mbalimbali za watu wale tunaowaongoza.

Tunawajibu wa kuwapa chakula kizuri kitakachowakuza (yaani Neno la Mungu lisiloghoshiwa), tuna wajibu wa kuwalinda kiroho, dhidi ya mafundisho potofu na mitego ya ibilisi, Kwa kuwaonya na kuwakemea pale inapobidi wavukapo mipaka.

Tuna wajibu wa kuwaombea, tunawajibu wa kuwafariji na kuzijali Hali zao za mwilini katika maisha Yao ya kawaida.

Hivyo wewe kama kiongozi ikitokea upo mbali na kundi lako, usikawie sana, ukaliacha kundi lako ma-miezi na ma-miaka,bila kujua maendeleo yao, ukadhani kwamba litaweza kujichunga lenyewe, hiyo ni hatari..ni heri uwe mtu wa kwenda na kurudi, kwenda na kurudi… lakini pia ukiwa karibu nalo usiwe mlegevu kupeleka jicho lako Kila eneo la maisha Yao ya kiroho na ya kimwili, kuangalia ni wapi Pana mapungufu au  shida..ili kuondoa kasoro hizo, Ili kundi la Bwana listawi kama vile yeye atakavyo.

Ndio maana ya hili andiko Mithali 27:23 “Fanya bidii kuijua hali ya makundi yako;  Na kuwaangalia sana ng’ombe zako”.

Ni wajibu wako kufanya hivyo, kwa hiari yako mwenyewe na sio kama unalazimishwa;

1 Petro 5:2

[2]lichungeni kundi la Mungu lililo kwenu, na kulisimamia, si kwa kulazimishwa, bali kwa hiari kama Mungu atakavyo; si kwa kutaka fedha ya aibu, bali kwa moyo.

Bwana akubariki.

Tafadhali shea na wengine ujumbe huu;

Pia Kwa maombezi/ Ushauri/ Maswali/ Whatsapp:
Tuandikie katika BOXI la Maoni hapo chini au
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312

Mada Nyinginezo:

TEMBEA NDANI YA SUKOTHI YAKO.-Maafundisho maalumu kwa watumishi

LISHA KONDOO WANGU, LISHA WANA-KONDOO WANGU.

USINIPE UMASKINI WALA UTAJIRI. (Mithali 30)

Kwanini Nuhu alimlaani Kaanani badala ya mtoto wake Hamu,

EPUKA MAKUNDI ILI UTAKATIFU WAKO UDUMU!.

FANYA KAMA UONAVYO VEMA.

ZIJUE TABIA ZA AHADI ZA MUNGU KWA MWAMINIO.

Rudi nyumbani

Print this post

TEMBEA NDANI YA SUKOTHI YAKO.-Maafundisho maalumu kwa watumishi

Mafundisho maalumu Kwa ajili ya watumishi wa Mungu.

Huu ni mwendelezo wa mafundisho maalumu Kwa ajili watumishi wa Mungu, ikiwa wewe ni Mchungaji, mwalimu, mtume, askofu,Nabii, au mtu yoyote unayemtumikia Mungu katika nafasi yoyote kanisani au kwenye huduma basi mafundisho haya yatakufaa sana.

Wakati ule Yakobo alipodhamiria kwenda kukutana na ndugu yake Esau baada ya kutengana naye Kwa muda mrefu..maandiko yanasema walifurahi sana walipoonana kule nyikani. Na baada ya mazungumzo Yale kuisha,  sasa ikiwa ni wakati wao wa kuondoka pale nyikani walipokutana waelekee Kaanani.

Na kama tunavyosoma habari tunaona ndugu yake Esau alimshurutisha wasafiri pamoja naye. Ndipo Yakobo akamwambia Esau kuwa jambo hilo ni gumu kwake..kwasababu ya Hali ya makundi mbalimbali na watu na mifugo aliyokuwa nayo..Tusome..

Mwanzo 33:12-17

[12]Kisha Esau akamwambia, Twende zetu, tusafiri, nami nitakutangulia.

[13]Akamjibu, Bwana wangu anajua ya kuwa watoto ni wachanga, tena kondoo na ng’ombe nilio nao wanyonyesha. Hao wanyama wakiharakishwa siku moja, watakufa wote.

[14]Tafadhali bwana wangu na apite mbele ya mtumwa wake; nami nitawaongoza polepole kwa kadiri ya mwendo wa wanyama walio mbele yangu, na kwa kadiri ya mwendo wa watoto, hata nitakapofika kwa bwana wangu huko Seiri.

[15]Esau akasema, Nikuachie, basi, baadhi ya watu walio pamoja nami. Akasema, Pana haja gani? Na nione kibali tu machoni pa bwana wangu.

[16]Basi Esau akarudi siku ile ile akishika njia yake mpaka Seiri.

[17]Yakobo akaendelea mpaka Sukothi. Akajijengea nyumba, akawafanyia makundi yake vibanda. Kwa hiyo jina la mahali pale pakaitwa Sukothi.

Ni nini cha kujifunza hapo?

Yakobo alilitambua kundi analolichunga, alijua kuwa wapo watoto wachanga ndani yake, na mifugo pia michanga, Ambayo haijazoezwa kupelekwa mkiki mkiki, kwani ikilazimishwa kufanywa hivyo itakufa yote njiani. Hivyo akaomba muda wa kusafiri wake uongezwe, kusudi kwamba ayakokote taratibu taratibu mpaka yatakapofika kule Shekemu alipokuwa anapakusudia. Pengine mwendo wa siku moja tu ikamgharimu mwezi.

Tofauti na Esau yeye alikuwa na watu wa vita tu,watu walio hodari, Lakini Yakobo alikuwa na makundi yote. Na hivyo kwenda nayo taratibu taratibu ilimgharimu .

Hii ni kutufundisha asili ya msimamizi wa kweli, kwanza hulijali kundi lake, pia anakuwa tayari kuchukuliana na vile vyombo dhaifu. Kwasababu sio wote katika kanisa watakuwa na mwendo kama wa kwao, SI wote watakuwa wepesi kustahimili vishindo kama baadhi yao. Hivyo wewe kama kiongozi ni lazima ujifunze kuendana na makundi yote kama Musa kule jangwani, ili kisipotee chochote. Maana yake ni kuwa usiwe na haraka ya kufikisha kundi Mahali Fulani Kwa jinsi utakavyo, vinginevyo utawaua wengine.

Yakobo alipaita mahali pale Sukothi, kwasababu ndipo alipowajengea makundi yake vibanda. Na wewe pia jenga Sukothi yako.

Bwana akubariki.

Shalom

Tafadhali shea na wengine ujumbe huu;

Pia Kwa maombezi/ Ushauri/ Maswali/ Whatsapp:
Tuandikie katika BOXI la Maoni hapo chini au
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312

Mada Nyinginezo:

LISHA KONDOO WANGU, LISHA WANA-KONDOO WANGU.

TOFAUTI YA MITUME, MANABII, WAINJILISTI, WACHUNGAJI NA WAALIMU NI IPI?

Mtu asiye na akili ni nani kibiblia?

MAFUNDISHO YA NDOA.

MIGAWANYO MINNE (4), YA HUDUMA YA YESU.

Je! Mwendo wa Sabato ulikuwaje kibiblia?(Matendo 1:12)

Rudi nyumbani

Print this post

NI INJILI GANI UNAHUBIRI?

Masomo maalumu kwa watumishi wa Mungu (Wahubiri).

Je umebeba ushuhuda gani katika injili yako?.

Tujifunze jambo kwa Yohana Mbatizaji..

Yohana 10:40 “Akaenda zake tena ng’ambo ya Yordani, mpaka mahali pale alipokuwapo Yohana akibatiza hapo kwanza, akakaa huko.

41  Na watu wengi wakamwendea, wakasema, yohana kweli hakufanya ishara yo yote, LAKINI YOTE ALIYOYASEMA YOHANA KATIKA HABARI ZAKE HUYU YALIKUWA KWELI.

42  Nao wengi wakamwamini huko”.

Hapo maandiko yanasema Yohana hakufanya ishara yoyote kama alivyofanya Musa katika hatua ya kuwahubiria ukombozi wana wa Israeli, au kama alivyofanya Eliya aliposhusha moto, au kama alivyofanya Eliya na manabii wengine..

Lakini Yohana yeye tunasona alibeba kitu kingine cha ziada.. Na kitu hicho ni “USHUHUDA WA KWELI WA YESU”. Na ndicho kilichomfanya aonekane mbele za Mungu kuwa mkuu kuliko manabii wote waliotangulia..

Mathayo 11:9  “Lakini kwa nini mlitoka? Ni kuona nabii? Naam, nawaambia, na ALIYE MKUU ZAIDI YA NABII.……

11  Amin, nawaambieni, Hajaondokea mtu katika wazao wa WANAWAKE ALIYE MKUU KULIKO YOHANA MBATIZAJI; walakini aliye mdogo katika ufalme wa mbinguni ni mkuu kuliko yeye”.

Kwahiyo kumbe kinachojalisha si miujiza?, si ishara, si maajabu tunayoyatenda.. bali ni kile tunachokihubiri kumhusu Yesu?.. Je kina ukweli?.. na kama kina ukweli, je ni katika kiwango gani?

Yohana alianza kuhubiri habari za Toba na ondoleo la dhambi na kusema Ufalme wa Mungu umekaribia wamwamini yeye ajaye.

Mathayo 3:1 “Siku zile aliondokea Yohana Mbatizaji akihubiri katika nyika ya Uyahudi, na kusema,

Tubuni; kwa maana ufalme wa mbinguni umekaribia”.

Injili ya namna hii ndiyo Bwana Yesu aliyoanza kuihubiri pia…

Mathayo 4:17 “Tokea wakati huo Yesu alianza kuhubiri, na kusema, Tubuni; kwa maana ufalme wa mbinguni umekaribia”.

Umeona injili ya Yohana iliyovyofanana na ya Bwana?..Yohana aliuona ushuhuda wa Yesu na akauhubiri kabla hajaja, aliona hizi ni nyakati za kutubu na kumrudia Mungu, kwasababu ufalme wa Mungu umekaribia!!.. .

Vile vile hakuanza kuwaambia watu watubu halafu baadaye waendelee na dhambi zao, bali aliwaambia watubu na baada ya hapo wazae matunda yapatanayo  na toba zao, wala wasijisifie dini, wala madhehebu.. Maana yake baada ya kutubia uzinzi ni lazima waishi maisha ya usafi baada ya hapo, kama umetubia ulevi ni lazima wauache ulevi, kama wametubia ukahaba ni lazima wauache ukahaba na vifaa vyote vya ukahaba, ikiwemo mavazi!..(hiyo ndio maana ya kuzaa matunda yapatanayo na toba).

Luka 3:7 “Basi, aliwaambia makutano ya wale waliomwendea ili awabatize, Enyi wazao wa nyoka, ni nani aliyewaonya ninyi kuikimbia hasira itakayokuja?

8  Basi, TOENI MATUNDA YAPATANAYO NA TOBA; wala msianze kusema mioyoni mwenu, Tunaye baba, ndiye Ibrahimu; kwa maana nawaambia ya kwamba katika mawe haya Mungu aweza kumwinulia Ibrahimu watoto.

9  Na sasa hivi shoka limekwisha kuwekwa penye mashina ya miti; BASI KILA MTI USIOZAA MATUNDA MAZURI HUKATWA NA KUTUPWA MOTONI”.

Injili ya namna hii ndiyo iliyobarikiwa na Bwana Yesu, na ndiyo iliyochaguliwa kuwa NJIA KWAAJILI YA BWANA!, Na ndiyo  iliyomfanya Yohana awe mkuu kuliko manabii wote ingawa hakufanya muujiza wowote.

Je! Na wewe kama mtumishi wa Mungu unahubiri nini? Je unahubiri mambo ya ulimwengu huu au injili ya ufalme wa Mbinguni??..  Injili yako ni ya magari na majumba na pesa?..

Kumbuka Injili ya ufalme wa mbinguni ni ile ile haijabadilika ambayo ni “kutubu na kuzaa matunda yapatanayo na toba kwamaana ufalme wa mbinguni umekaribia” Huo ndio ushuhuda wa Yesu na ndio roho ya unabii.

Ufunuo 19:10b “….. Kwa maana ushuhuda wa Yesu ndio roho ya unabii”.

Vile vile usikimbilia kutafuta au kutengeneza miujiza, usitumie nguvu nyingi kutafuta maajabu… bali tafuta kwanza Ushuhuda wa Yesu, ukiupata huo utakuwa umepata muujiza mkubwa sana katika utumishi wako!.

Bwana akubariki.

Tafadhali shea na wengine ujumbe huu;

Pia Kwa maombezi/ Ushauri/ Maswali/ Whatsapp:
Tuandikie katika BOXI la Maoni hapo chini au
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312

Mada Nyinginezo:

NENO LA MUNGU KATIKA UTIMILIFU WOTE.

TOFAUTI YA UBATIZO WA YOHANA NA UBATIZO WA BWANA YESU

WAKO WATATU WASHUHUDIAO MBINGUNI NA DUNIANI.

IJUE HEKIMA YA MUNGU KATIKA KUKUINUA KIMAISHA.

JE UMEKUFA PAMOJA NA NANI?

Rudi nyumbani

Print this post

LISHA KONDOO WANGU, LISHA WANA-KONDOO WANGU.

Masomo maalumu kwa watumishi wa Mungu,

Je kibiblia ni jukumu la wachungaji peke yao kulichunga kundi? Na mitume na manabii hiyo si kazi yao??….. kama ndio basi huenda Bwana Yesu alikosea alipomwambia Petro ambaye ni Mtume, alichunge kundi lake..

Tusome,

Yohana 21:15  “Basi walipokwisha kula, Yesu akamwambia Simoni Petro, Je! Simoni wa Yohana, wewe wanipenda kuliko hawa? Akamwambia , Naam ,Bwana, wewe wajua kuwa nakupenda. Akamwambia, LISHA WANA-KONDOO WANGU.

16  Akamwambia tena mara ya pili, Simoni wa Yohana, wanipenda? Akamwambia, Ndiyo, Bwana, wewe wajua kuwa nakupenda. Akamwambia, CHUNGA KONDOO ZANGU.

17  Akamwambia mara ya tatu, Simoni wa Yohana, wanipenda? Petro alihuzunika kwa vile alivyomwambia mara ya tatu, Wanipenda? Akamwambia, Bwana, wewe wajua yote; wewe umetambua ya kuwa nakupenda. Yesu akamwambia, LISHA KONDOO ZANGU”.

Kumbe kazi ya kuchunga, na kulisha kondoo si ya mchungaji peke yake, bali hata ya mitume, na waalimu na manabii na wainjilisti… Ikiwa na maana kama Bwana amekupa watu chini yako ni lazima ujue kuwa unawajibu wa kuwachunga na kuwalisha…pasipo kuweka visababu sababu.

Sasa leo hatutazungumzia sana kuhusiana na KUCHUNGA kondoo.. lakini tutalitazama jukumu la KULISHA KONDOO ulilopewa wewe kama mtumishi wa Mungu.

Awali ya yote ni muhimu kujua kondoo ni nani?

Kondoo ni mnyama asiyeweza kujiongoza mwenyewe na Bwana Yesu anao watu ambao siku zote hawataweza kusimama wenyewe (maana yake siku zote watahitaji msaada tu ili waendelee kudumu katika Imani na katika kuifanya kazi ya Mungu). Na kundi hili ni kubwa kuliko lile kundi la watumishi wa Mungu.

Kundi hili lisipochungwa vizuri na kulishwa ipasavyo linaharibika na kupotea kabisa, na shetani ndilo analolitafuta sana….

Sasa Bwana alimpa jukumu Petro, na anakupa jukumu wewe kama mtumishi wa Mungu, pasipo kujali karama yako, kuwa LISHA KONDOO WAKE lakini si tu kondoo bali pia WANA-KONDOO, Haya ni makundi mawili ambayo ni lazima ujifunze kuyatofautisha.

Tofauti ya kondoo na Mwana kondoo, ni hii; Kondoo aliyekomaa anajulikana kwa jina hilo la “Kondoo” na kondoo aliye chini ya umri wa mwaka mmoja anaitwa “mwana-kondoo”. Sasa Bwana alimwambia Petro alishe makundi hayo yote mawili, na anatuambia pia sisi..

Chakula cha kondoo aliyekomaa ni tofauti na cha yule mchanga.. huwezi kuwalisha wote chakula kinachofanana, kwani kundi moja litadhoofika.. ukimpa maziwa kondoo aliyekomaa, atadhoofika, vile vile ukimpa chakula kigumu kondoo mchanga ataathirika.. kwahiyo ni lazima ujifunze kukigawanya chakula kulingana na makundi ya watu walio chini yako.

Ni lazima uwe na chakula cha waongofu wapya, na chakula cha waliokomaa kiimani, na ni  sharti lazima Makundi yote yale chakula cha kushiba..

Ni lazima chakula chako kilenge kuwakuza wale kondoo wachanga (maana yake wakue kiroho) na kuwanenepesha wale kondoo waliokomaa (maana yake wajae maarifa). Tukiwa watumishi wa aina hiyo basi mbele zake Bwana tutaonekana tunampenda lakini kama hatuwalishi inavyopaswa na huku tunajivuna kuwa sisi ni watumishi wa Mungu, basi bado hatujalijua pendo la Kristo?.

Hivyo Kama Mtumishi wa Mungu jenga tabia ya kulitazama kundi lako (Sawasawa na Mithali 27:23)..usiseme mimi ni Mtume sina karama hiyo?, na huku unawalisha watu mambo yasiyowajenga, hata Petro alikuwa ni Mtume na si mchungaji lakini alipewa hilo jukumu na Bwana la kulisha vizuri kondoo watakaokuwa chini yake, usiseme mimi ni Nabii sina wito huo na huku unawalisha watu maono ya uongo na mafundisho manyonge…hata Musa alikuwa ni nabii lakini alibeba jukumu hilo la kuwalisha watu amri, na sheria za Mungu.

Maran atha.

Tafadhali shea na wengine ujumbe huu;

Pia Kwa maombezi/ Ushauri/ Maswali/ Whatsapp:
Tuandikie katika BOXI la Maoni hapo chini au
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312mafundisho ya kila siku kwa njia ya WHATSAPP, jiunge na channel yetu kwa kubofya link hii >> https://whatsapp.com/channel/0029VaBVhuA3WHTbKoz8jx10

Mada Nyinginezo:

JE! UNAMPENDA BWANA?

“Nitampiga mchungaji na kondoo wa kundi watatawanyika”,Maana yake nini?

Nitajuaje kuwa nimesamehewa dhambi zangu?

NI LIPI KATI YA MAKUNDI HAYA, WEWE UPO?

USIMLAANI KIZIWI, WALA USITIE KWAZO MBELE YA KIPOFU.

Rudi nyumbani

Print this post

KAMA MTUMISHI WA MUNGU, TAFUTA MAARIFA KWA BIDII.

Huu ni mfululizo wa Masomo maalumu kwa Watumishi wa Mungu (Wahubiri wa Injili, Wachungaji, Wainjilisti, Waalimu, Manabii na Waimbaji wote).

Hosea 4:6 “Watu wangu wanaangamizwa kwa kukosa maarifa; kwa kuwa wewe umeyakataa maarifa, mimi nami nitakukataa wewe, usiwe kuhani kwangu mimi; kwa kuwa umeisahau sheria ya Mungu wako, mimi nami nitawasahau watoto wako”.

Tunaona hapa Bwana anaanza  kama kwa kulaumu!.. sasa anamlaumu nani? Si wana wa Israeli bali anawalaumu  MAKUHANI wake! (Yaani watu waliowekwa kwa lengo la kuwafundisha wana wa Israeli njia ya kumcha Bwana)… ambao kwasasa wanafananishwa na (Wachungaji, Wainjilisti, Waalimu, Mitume, Manabii na wahubiri wote)

Watu hawa Bwana anawalaumu kwa kuwa “wameyakataa maarifa” (maana yake hawataki kujishughulisha kutafuta maarifa yatakayowasaidia wao pamoja na wengine), na hivyo kusababisha Israeli yote kukosa maarifa.. kwasababu laiti wakiyapata maarifa hayo ya kiMungu ya kutosha, basi wangeweza kuwafundisha Israeli nzima na hivyo Israeli yote ingeponyeka..

Lakini kinyume chake, Makuhani hawa hawayataki maarifa!, wanaridhika kukaa katika ujinga, hawataki kusoma maandiko,  na hivyo kusababisha Israeli yote kukosa maarifa na kuangamia, jambo ambalo ni DHAMBI KUBWA SANA MBELE ZA MUNGU!, Kwasababu wao ndio chanzo cha Israeli yote kukosa maarifa..

Na tunaona madhara yake ni nini… Bwana AKAWAKATAA wasiendelee kuwa makuhani, na akawakataa na WATOTO WAO pia.

Ni jambo baya sana, Bwana kukukataa kuwa KUHANI.. kwani unakuwa Umenyang’anywa Neema yote iliyokuwa juu yako.. utalazimisha kuendelea na Mungu, lakini yeye atakuwa yupo mbali na wewe kama ilivyokuwa kwa Sauli..

1Samweli 15:23 “Kwani kuasi ni kama dhambi ya uchawi, Na ukaidi ni kama ukafiri na vinyago; Kwa kuwa umelikataa neno la Bwana, Yeye naye amekukataa wewe usiwe mfalme”

Hili ni jambo baya sana na linaloendelea sasa miongoni mwa watumishi.. Ni heri tukataliwe na wanadamu wote, lakini tusikataliwe na Mungu..

Kama mtumishi wa Mungu tafuta maarifa!!!… kwasababu utumishi wako unapimwa!.. Bwana anategemea kuona watu wake wanajaa maarifa ya kumjua yeye pindi wanapokuja katika kanisa unalohudumu, wanapokuja katika maskani unayo hudumu…. hataki kuona watu wake wanaangamizwa kwa kukosa maarifa, ili hali wewe (unayejiita mtumishi wa Mungu) ndiye ambaye ungepaswa uwape hayo maarifa.!

Bwana akiona watu wake wanaangamia kwa kukosa maarifa, usidhani wewe utabaki salama!.. Bwana atakukataa wewe na pia atawakataa watoto wako..

Usifurahie kuona watu walio chini yako, hawaelewi kanuni ya Imani, wanatanga tanga huku na kule kutafuta  maji, au mafuta au kuufananisha ukristo na uganga wa kienyeji…

Chukua jukumu la kujifunza biblia kwa kina ili ujae maarifa yatakayokusaidia wewe na ukawasaidie na watu wako!!!!!…soma, tafiti, chunguza maandiko kila siku, hakiki mambo yote, acha kutafuta umaarufu na sifa zisizokuwa na maaana kutoka kwa watu wako…. hiyo itathaminisha utumishi wako mbele za Mungu.. wape watu Maarifa ya kiMungu, hayo ndiyo yatakayowalinda wasije wakaangamia!… Kumbuka siku zote kuwa Bwana hataki watu wake waangamizwe kwa kuyakosa hayo!.

Kama unaona uvivu kutafuta maarifa na kuwapa watu hayo, acha hiyo kazi ya kuhubiri, sio wito wako!, nenda katafuta kazi nyingine, kafanye biashara na Mungu atakubariki huko!, lakini usiwaongoze watu katika njia ya upotevu, kwa kuwajaza elimu za mambo ya ulimwengu huu na elimu za kichawi badala ya kuwapa elimu na maarifa ya ufalme wa mbinguni.. utajitafutia laana badala ya Baraka!.

Bwana Yesu na atusaidie sana.

Shalom.

Tafadhali shea na wengine ujumbe huu;

Pia Kwa maombezi/ Ushauri/ Maswali/ Whatsapp:
Tuandikie katika BOXI la Maoni hapo chini au
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312

Mada Nyinginezo:

TAFUTA KWA BIDII KUWA MTAKATIFU.

NJAA ILIYOPO SASA.

Je! Mungu anaupendeleo kwa wanaume zaidi ya wanawake?

UFANYE WEMA WAKO KATIKA MAARIFA.

Tofauti kati ya Hekima, ufahamu na maarifa, ni ipi?

Rudi nyumbani

Print this post

INJILI NI UWEZA WA MUNGU, UULETAO WOKOVU.

Tukiijua nguvu Mungu aliyoiweka katika injili, basi tutakwenda kuihubiri kwa bidii zote.

Wengi wetu tunasubiri tufikie kimo Fulani cha maarifa ndipo tukahubiri, wengine tunasubiri tupate upako Fulani au uweza Fulani ushukao juu ndipo tukahubiri.. wengine tunangoja unabii na maono au sauti utuambie tukahubiri ndipo tukaianze kazi hiyo… Wengine tunasubiri tupitia kwanza madarasa fulani ya theolojia ndipo tukaitangaze habari njema.. Kuanzia leo anza kufikiri tofauti!..

Hebu tusome maandiko yafuatayo…

Warumi 1:15  “Kwa hiyo, kwa upande wangu, mimi ni tayari kuihubiri Injili hata na kwenu ninyi mnaokaa Rumi.

16  Kwa maana siionei haya Injili; kwa sababu ni UWEZA WA MUNGU UULETAO WOKOVU, kwa kila aaminiye, kwa Myahudi kwanza, na kwa Myunani pia”.

Hapo mstari wa 16, maandiko yanasema “INJILI NI UWEZA WA MUNGU UULETAO WOKOVU”.. Kumbe injili ni “UWEZA” yaani nguvu au maajabu… na Zaidi sana si wa mwanadamu bali wa Mungu. Ikiwa na maana kuwa NGUVU ILIYOPO KATIKA INJILI, inatoka kwa Mungu..na wala si kwetu!.

Tukilijua hili tutapata ujasiri wa kwenda kuhubiri bila hofu, bila mashaka yoyote… bila woga wowote, kwasababu katika kuhubiri ndipo Mungu atashughulika katika kuuingiza wokovu katika watu, na wala si kazi yangu mimi kuwageuza watu!.. kwasababu Injili yake NI UWEZA WAKE, ambao unaleta wokovu ndani ya mtu.

Ndugu baada ya kumwamini Bwana Yesu kama Mwokozi wa maisha yako, na kutubu kwa kumaanisha kuziacha dhambi na kubatizwa fahamu kuwa tayari umekidhi vigezo vya kwenda kuwahubiria wengine habari njema… usingoje ufikie ukamilifu Fulani!.. usingoje uanze kunena kwa lugha, usingoje uanze kuona maono!.. wewe nenda kahubiri hayo ambayo tayari umeshayajua.. na utaona uweza wa Mungu kwa hicho utakachokwenda kukihubiri.. utaona Mungu akiwaokoa watu na kuwafungua katika hicho hicho kidogo ulichonacho, kwasababu Injili ni UWEZA WA MUNGU!, na si uweza wa mwanadamu!.

Utasema tunazidi kulithibitisha vipi hili kimaandiko.

Rejea wakati Bwana Yesu anawatuma wanafunzi wake wawili wawili kwenda kuhubiri, utagundua kuwa Bwana Yesu alianza kuwatuma wanafunzi wake hata kabla ya Pentekoste…na waliporudi walirudi kwa kushangilia jinsi watu walivyokuwa wakifunguliwa…

Petro alianza kuhubiri hata kabla ya kupokea Roho Mtakatifu, wewe leo unasubiri nini?.. Petro na mitume wote wa Bwana Yesu waalianza kuwaeleza watu habari toba na msamaha wa dhambi hata kabla ya kunena kwa lugha!, je wewe uliyemwamini Yesu leo unasubiri nini?.

Luka 10:17  “Ndipo wale sabini waliporudi kwa furaha, wakisema, Bwana, hata pepo wanatutii kwa jina lako”

Hicho kidogo ulichonacho kinaweza kuleta mabadiliko makubwa sana ndani ya watu, endapo ukiamua! Kwasababu injili NI UWEZA WA MUNGU wa kuwaokoa watu na si uweza wako wewe au mwanadamu mwingine yoyote.

Amka hapo ofisini kwako, anza kuhubiri habari za Yesu, usijiangalie kama unaweza kuongea au la!.. wewe hubiri Bwana atakuwa na wewe katika kuzungumza…kwasababu kuna UWEZA wa kiMungu katika maneno ya injili.. Wakati unahubiri watu hawataangalia kasoro zako bali watalisikiliza lile Neno la litawageuza.. na baada ya pale utashangaa jinsi Bwana anavyofanya kazi.

Bwana akubariki.

Group la whatsapp Kwa mgawanyo bora wa masomo download App hapa>> App wingu la mashahidi

Tafadhali shea na wengine ujumbe huu;

Pia Kwa maombezi/ Ushauri/ Maswali/ Whatsapp:
Tuandikie katika BOXI la Maoni hapo chini au
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312

Mada Nyinginezo:

KUMBE MUNGU ANAWEZA KUKULIPA KWA USICHOSTAHILI!

JE! HAMPOTEI KWA SABABU HII?

USIMPE NGUVU SHETANI.

Nini tofauti ya Uwezo na Uweza kibiblia?

MWIMBIE BWANA ZABURI KATIKA NYAKATI ZA FURAHA.

Rudi nyumbani

Print this post

KWANINI TUNAPASWA KWENDA KUIHUBIRI INJILI KWA UJASIRI WOTE?

Karibu tujifunze biblia, Neno la Mungu wetu, lililo taa na mwanga wa njia zetu.

Je unajua ni kwanini tunapaswa kwenda kuihubiri injili kwa ujasiri wote, tena pasipo woga wowote?.. na tena sio kwa watu baadhi tu, bali kwa watu wote wa dunia yote na katika kila mtaa, na wilaya, na mkoa, na Taifa, na kila bara?.. Ni lazima tukijue kitu kinachotupa ujasiri wa sisi kufanya hivyo!, tusipokujua hicho tutakuwa waoga wa kuhubiri.

Sasa hebu tusome maandiko yafuatayo..

Mathayo 28:18  “Yesu akaja kwao, akasema nao, akawaambia, NIMEPEWA MAMLAKA YOTE MBINGUNI NA DUNIANI.

19  Basi, enendeni, mkawafanye mataifa yote kuwa wanafunzi, mkiwabatiza kwa jina la Baba, na Mwana, na Roho Mtakatifu;

20  na kuwafundisha kuyashika yote niliyowaamuru ninyi; na tazama, mimi nipo pamoja nanyi siku zote, hata ukamilifu wa dahari”

Hicho ni kipindi ambacho Bwana Yesu aliwatokea wanafunzi wake baada ya kufufuka kwake.. Na siku hiyo alipowatokea alikuja na agizo maalumu kwao!.. Na agizo lenyewe ni hilo la “KWENDA KUHUBIRI INJILI DUNIANI KOTE”.

Lakini agizo hilo ni gumu na zito!.. Yaani kwenda ulimwenguni kote kusema habari za Masihi, kwenda katika jamii za watu wabaya, na wakatili na wauaji, kwenda katika jamii za wasomi na watawala, na tena ulimwenguni kote?, hilo jambo si jepesi hata kidogo!.

Sasa Bwana Yesu alijua hilo jambo sio dogo wala sio lepesi, hivyo akatanguliza kwanza SABABU za kwanini awaagize kwenda duniani kote, katika mitaa yote, na miji yote na vijiji vyote na kwa watu wote wakawahubirie watu..

Na sababu yenyewe ndio tunayoisoma katika mwanzoni mwa mistari hiyo.. hebu tusome tena mstari wa 18..

Mathayo 28:18  “Yesu akaja kwao, akasema nao, akawaambia, NIMEPEWA MAMLAKA YOTE MBINGUNI NA DUNIANI.

19  Basi, enendeni, mkawafanye mataifa yote kuwa wanafunzi, mkiwabatiza kwa jina la Baba, na Mwana, na Roho Mtakatifu”

Hiyo sentensi ya kwanza kwamba “amekabidhiwa mamlaka yote mbinguni na duniani” ndio iliyowapa ujasiri Mitume wake kwenda kuhubiri injili kila mahali.

Hebu tafakari leo hii umetumwa kupeleka ujumbe kwa watu Fulani katika mkoa Fulani, halafu aliyekupa huo ujumbe ni mtu tu wakawaida..bila shaka itakuwa ni ngumu kwako kupeleka ujumbe kwa jamii ya hao watu kwasababu kwanza huenda wana nguvu kuliko wewe, hivyo ukiwapelekea vitu tofauti na itikadi zao au jamii zao ni rahisi kujitafutia madhara.. lakini hebu tengeneza picha ni Raisi ndio anakupa ujumbe uwapelekee watu Fulani, ni dhahiri kuwa mashaka yatapungua na ujasiri utaongezeka…kwanini?.. Kwasababu unajua kuwa Raisi amepewa mamlaka yote juu ya hii nchi!..

Vivyo hivyo na kwa mitume…waliposikia tu hayo maneno ya kwanza ya Bwana Yesu kwamba “amepewa mamlaka yote ya mbinguni na duniani” ikawa ni sababu tosha ya wao kuwa na ujasiri wa kwenda kila mahali, kwasababu wanajua kila mahali waendapo tayari ni milki ya Kristo, kwamba Kristo ana nguvu juu ya hilo eneo… na maana akawaambia waende kwasababu yeye atakuwa pamoja nao hata mwisho wa Dahari (yaani mwisho wa Nyakati). Na sasa tupo karibia na Mwisho wa Nyakati, Kwahiyo Kristo yupo na sisi pale tunapokwenda kuieneza injili.

Ndugu usisubiri Bwana Yesu akutokee na kukuambia nenda kahubiri!.. Tayari agizo lilishatoka miaka zaidi ya elfu 2 iliyopita… kwamba nenda kahubiri injili.

Wengi leo hii wanaogopa kwenda kuhubiri injili, kwasababu hawana vitu vya kuhubiri.. Bwana Yesu hakuwaambia wanafunzi wake wakanunue vyombo vya miziki kwanza, au spika au wapate nguo nzuri ndipo wakahubiri injili..hapana! kinyume chake aliwaambia wasibebe chochote kwasababu huko waendako watavipata vyote.

Na wewe unasubiri nini usiende kuhubiri injili? Ni wito gani unaoungoja?, ni sauti gani unayoingoja?.. na upako gani unaoungoja?…ni ujuzi gani unaousubiri?.. ukisubiri ufikie ujuzi Fulani au maarifa Fulani hutayafikia kwasababu kila siku tunakua kutoka utukufu hadi utukufu, hakuna siku tutasema tumeshajua!!.. kila siku tunajifunza..hivyo usiseme ngoja nifikia levo Fulani ndipo nikahubiri, hizo ni akili za kichanga!.. Nenda kahubiri injili..

Sasa unaanzia wapi kuhubiri injili?

Kabla ya kwenda mbali anza kuhubiri injili hapo hapo ulipo, kabla ya kufikiri kwenda nje ya mtaa anza katika mtaa wako, anza katika nyumba yako, anza katika ofisi yako, anza katika shule yako.. hakikisha hapo umemaliza kwanza na watu wameitii injili ndipo uende nje!.. na katika hatua hiyo ya awali kumbuka kuwa Kristo yupo na wewe, na kumbuka kuwa yeye amekabidhiwa mamlaka yote ya mbinguni na duniani, kwahiyo hakuna nguvu zozote wala mamlaka yoyote unayoweza kushindana na hilo agizo la Bwana Yesu.

Bwana Yesu akubariki.

Tafadhali shea na wengine ujumbe huu;

Pia Kwa maombezi/ Ushauri/ Maswali/ Whatsapp:
Tuandikie katika BOXI la Maoni hapo chini au
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312

Mada Nyinginezo:

ENZI NA MAMLAKA AMEZIFANYA KUWA MKOGO

NI KWA NAMNA GANI SHETANI ANAIZUIA INJILI?

Ni kweli Paulo alipuuzia maonyo aliyopewa ya kwenda Yerusalemu?

Ni sahihi kusema sikuitiwa kuhubiri ubatizo kama Paulo alivyosema (1Wakorintho 1:17)?.

TUNALINDWA NA NGUVU ZA MUNGU.

Rudi nyumbani

Print this post

MAUMIVU  NYUMA-YA-HUDUMA.

Mtu yeyote aliyeokoka (Kwa kumaanisha kabisa), ni lazima Bwana ataweka huduma ndani yake, anaweza akawa mchungaji, au mwinjilisti, au mwalimu, au mwimbaji, shemasi, lakini pia anaweza akawa  mwandishi, mtunza bustani, mratibu wa vipindi, mwasibu wa kanisa,  n.k. maadamu tu zinafanya kazi ya kulihudumia kanisa  la Mungu, na si vinginevyo.

Licha ya kuwa utaifurahia kazi yako na kupata thawabu, lakini uhalisia wake ni kwamba, huduma yoyote Mungu anayokupa haitakuwa nyepesi kama wewe unavyoweza kudhani, yaliyowakuta mitume wakati fulani, yatakukuta na wewe, lakini yatamkuta hata na Yule ambaye atakuja kutumika baadaye.

Haya ni baadhi ya maumivu utakayokutana nayo;

KUACHWA:

2Timotheo 4:10  “Maana Dema aliniacha, akiupenda ulimwengu huu wa sasa, akasafiri kwenda Thesalonike; Kreske amekwenda Galatia; Tito amekwenda Dalmatia”

Tengeneza picha, Wakati ambapo mtume Paulo yupo katika kilele cha utumishi, halafu mtendakazi mwenzake mpendwa, anageuka ghafla, na kumwachwa alijisikiaje. Ni heri angemwacha na kwenda kutumika mahali pengine, lakini anamwacha na kuurudia ulimwengu. Ni maumivu makali  kiasi gani? Ni kuvunjwa moyo kiasi gani?

Mwaka 2016-2018, tulikuwa na rafiki yetu mmoja, hatukudhani kama siku moja tungekaa tutengane, kwasababu tulikuwa tumeshajiwekea malengo mengi makubwa ya kumtumikia Mungu, tuliishi kama Daudi na Yonathani, lakini tulipoanza kupiga hatua tu ya kutekeleza malengo yetu, ghafla alikatisha mawasiliano na sisi, akawa hapokei simu zetu, na baadaye kutu-block kabisa, akaurudia ulimwengu, hadi leo.

Tuyahifadhi haya ili yatakapotokea tusivunjike moyo tukaacha utumishi. Wakina Dema unaweza kupishana nao katika huduma Mungu aliyoweka ndani yako, ila usivunjike moyo.

UPWEKE:

Pale pale Mtume Paulo anamsihi Timotheo asikawie kumfuata, kwasababu Kreske, amekwenda Galatia, Tito, Dalmatia..

2Timotheo 4:9  “Jitahidi kuja kwangu upesi. 10  Maana Dema aliniacha, akiupenda ulimwengu huu wa sasa, akasafiri kwenda Thesalonike; Kreske amekwenda Galatia; Tito amekwenda Dalmatia. 11  Luka peke yake yupo hapa pamoja nami. Umtwae Marko, umlete pamoja nawe, maana anifaa kwa utumishi. 12  Lakini Tikiko nalimpeleka Efeso.

Kundi hili halikuondoka, kwasababu ya kuupenda ulimwengu kama Dema, hapana bali kwasababu ya huduma, hivyo mtume Paulo akabaki peke yake. Kuna wakati alikuwa na kundi kubwa la watenda kazi pamoja naye, lakini upo wakati alibaki peke na Luka tu.. Anamhizi Timotheo afike  pamoja na Marko, ili afarijike katika huduma, hali ya upweke imwache.

Kama mhudumu wa Kristo, zipo nyakati utakuwa peke yako, Hivyo usife moyo, ni vipindi tu vya Muda.

KUACHANA:

Moja ya ziara za mtume Paulo iliyokuwa na mafanikio makubwa sana, basi ni ile ziara ya kwanza. Ni kwasababu gani? Ni kwasababu alikuwa na Barnaba. Wote wawili walikuwa na nia ya Kristo, hawakuwa na fikra za kiulimwengu au kimaisha. Lakini cha kusikitisha hilo halikuendelea sana.. Walipishana kauli, kutokana na kwamba kila mmoja aliona uchaguzi wake ni bora kuliko wa mwingine.. Paulo alitaka kwenda Sila, lakini Barnaba kwenda na Marko. Lakini kama wangetoa tofauti zao, na kuwachukua wote, naamini huduma ingekuwa na mafanikio makubwa zaidi, lakini hilo lilikuwa halina budi kutokea.

Matendo 15:36 “ Baada ya siku kadha wa kadha Paulo akamwambia Barnaba, Haya! Mrejee sasa tukawaangalie hao ndugu katika kila mji tulipolihubiri neno la Bwana, wa hali gani.

37  Barnaba akaazimu kumchukua Yohana aliyeitwa Marko pamoja nao.

38  Bali Paulo hakuona vema kumchukua huyo aliyewaacha huko Pamfilia, asiende nao kazini.

39  Basi palitokea mashindano baina yao hata wakatengana. Barnaba akamchukua Marko akatweka kwenda Kipro”.

Nyakati za kupoteza kiungo chako muhimu katika huduma utapishana nacho.

KUFANYIWA UBAYA:

2Timotheo 4:13  “Lile joho nililoliacha kwa Karpo huko Troa, ujapo ulilete, na vile vitabu, hasa vile vya ngozi. 14  Iskanda, mfua shaba, alionyesha ubaya mwingi kwangu; Bwana atamlipa sawasawa na matendo yake. 15  Nawe ujihadhari na huyo, kwa sababu aliyapinga sana maneno yetu”.

Haijalishi, utampendeza mtu kiasi gani, utafanya wema mwingi namna gani, bado wapo watakaokupinga tu utumishi wako, na zaidi watakuwa ni kama maadui zako. Ni jambo ambalo mtume Paulo hakulitarajia lakini alikumbana nalo baadaye, kutoka kwa Iskanda.. Yaliyomkuta Kristo Bwana wetu kutoka kwa mafarisayo yakamakuta na yeye. Na huwenda yatakukuta na wewe wakati Fulani mbele. Usirudi nyuma.

KUDHANIWA VINGINE:

Watu wengi wanaweza kuchukizwa na wewe kwasababu matarajio yao kwako ni tofauti na walivyokutegemea, hili lilianza tangu wakati wa Bwana alipokuwa duniani. Watu wengi waliosikia habari zake, ikiwemo Yohana mbatizaji, walimtazamia Bwana angekuja kama mfalme Daudi, akipambana na utawala sugu wa kirumi, akivaa nguo za kifalme, akiogopwa na kila mtu. Lakini aliposikia analala kwenye milima ya mizeituni, anaongozana na wavuvi, anakaa na wenye dhambi..Imani ya Yohana ikatetereka kidogo na kutuma watu ili kuulizia kama yeye kweli ndiye, au wamtazamie mwingine..Lakini maneno ya Bwana Yesu yalikuwa ni haya;

“Naye heri awaye yote asiyechukizwa nami” (Mathayo 11:6).

Vivyo hivyo na mtume Paulo, alitarajiwa na wengi kuwa atakuwa ni mtu mkuu kimwonekano, mwenye mavazi ya kikuhani kama waandishi, kutoka na sifa zake, na nyaraka zake, kuvuma duniani kote..lakini walipokutana naye walimwona kama kituko Fulani hivi;

2Wakorintho 10:10  “Maana wasema, Nyaraka zake ni nzito, hodari; bali akiwapo mwenyewe mwilini ni dhaifu, na maneno yake si kitu.

11  Mtu kama huyo na afikiri hivi, ya kwamba jinsi tulivyo kwa maneno katika nyaraka tusipokuwapo, ndivyo tulivyo kwa matendo tukiwapo”

Hivyo si kila mtu atapendezwa na jinsi atakavyokukuta, wengine watakuacha au hawatakuamini kwasababu umekuja nje ya matarajio yao.

KUPUNGUKIWA:

Japokuwa vipo vipindi vyingi vya mafanikio, lakini pia vipo vipindi vya kupungukiwa kabisa. Paulo anamwagiza Timotheo pindi amfuatapo makedonia ambebe joho(Koti) lake, kwa ajili ya ule wakati wa baridi. Kama angekuwa na fedha ya kutosha wakati huo, kulikuwa hakuna haja ya kumwagiza, angenunua lingine tu alipokuwepo.

Mungu hawezi kukuacha, wala kukupungukia kabisa, atakupa, na kukufanikisha, lakini pia vipindi kama hivi utapishana navyo mara kwa mara na ni Mungu mwenyewe anaruhusu. Hivyo usitetereke.

Wafilipi 4:11  “Si kwamba nasema haya kwa kuwa nina mahitaji; maana nimejifunza kuwa radhi na hali yo yote niliyo nayo.

12  Najua kudhiliwa, tena najua kufanikiwa; katika hali yo yote, na katika mambo yo yote, nimefundishwa kushiba na kuona njaa, kuwa na vingi na kupungukiwa. 13  Nayaweza mambo yote katika yeye anitiaye nguvu”

KUUGUA:

Ukiwa mtumishi, haimaanishi wewe ni malaika, umejitenga na mateso ya hii dunia, Kazi hii itakufanya uumwe wakati mwingine, Timotheo alikuwa anaumwa mara kwa mara tumbo, kwasababu ya mifungo, kuhubiri sana, hivyo akashauriwa na Paulo atumie mvinyo kidogo kwa ajili ya kuweka tumbo lake sawa. Alikuwepo Epafrodito mtume, naye kwasababu ya injili, aliumwa sana, karibu na kufa lakini baadaye Bwana akamponya( Wafilipi 2:25). Elisha alikufa na ugonjwa wake.

Upitiapo vipindi vya magonjwa, usitetereke ukaacha utumishi bali jifariji kwa kupitia mashujaa hawa.

Hivyo, tukiyahifadhi haya moyoni, basi utumishi wetu hautakuwa wa manung’uniko au wa kuvunjika moyo, mara kwa mara. Kwasababu ndio njia ya wote. Hivyo tukaze mwendo katika kumtumikia Bwana, kwasababu malipo yake ni makubwa kuliko mateso tunayopishana nayo. Thawabu za utumishi ni nyingi sana,

Ufunuo 3:11  “Naja upesi. Shika sana ulicho nacho, asije mtu akaitwaa taji yako”.

Bwana akubariki.

Shalom.

Tafadhali shea na wengine ujumbe huu;

Pia Kwa maombezi/ Ushauri/ Maswali/ Whatsapp:
Tuandikie katika BOXI la Maoni hapo chini au
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312

Mada Nyinginezo:

GHARAMA YA UFALME WA MBINGUNI.

Je Musa yupo anawashitaki watu..kulingana na Yohana 5:45?

Tofauti kati ya mtume na mwanafunzi ni ipi kibiblia?

Naye atawachunga kwa fimbo ya chuma.

Je mbinguni itakuwa ni kuimba tu wakati wote?

MAFUNDISHO MAALUMU KWA WAONGOFU WAPYA.

KAMA MHUBIRI USIWE MFANO WA DIOTREFE.

Rudi nyumbani

Print this post