Category Archive maswali na majibu

Elewa tafsiri ya Mithali 27:22 Hata ukimtwanga mpumbavu kwa mchi kinuni.

SWALI: Nini tafsiri ya Mithali 27:22

Hata ukimtwanga mpumbavu kwa mchi kinuni pamoja na ngano; Upumbavu wake hautamtoka.


JIBU: Kama tunavyojua mtwangio na kinu ni vyombo vinavyotumika kuponda-ponda nafaka ngumu kuwa unga, au wakati mwingine mimea migumu kuwa milaini. Mfano wa kisamvu ambacho ili kiweze kulika, majani yake huwezi yapika hivyo hivyo huna budi kuyatwanga twanga kidogo, yalainike ndipo upike ule.

Na vivyo hivyo, nafaka kama mahindi, au ngano, ili viweze kulika zamani vilikuwa vinatwangwa kwenye vinu ,tofauti na sasa vinasagwa na mashine.

Sasa katika mithali hiyo, Mungu anatoa, asili ya mtu mpumbavu, kwamba hata akitwangwa, mfano wa ngano kinuni, huo upumbavu hauwezi kumtoka. Yaani njia gani ya lazima itumike bado hawezi kuacha upumbavu.

Sasa ni vizuri kufahamu, mpumbavu ni nani?

Mpumbavu kibiblia sio mtu Fulani mjinga tu hapana, bali ni Neno pana, linalolenga kuanzia

mtu anayesema hakuna Mungu (zaburi 14:1)

Mtu mgomvi (Mithali 9:13),

Mtenda maovu (Mithali 10:23)

Anayejiona njia yake ni sawa machoni pake (Mithali 12:15)

Mwenye kiburi (Mithali 14:3)

Mwenye dharau (Mithali 15:5)

Yaani kwa kifupi mpumbavu ni mtu ambaye hana Mungu ndani yake. Kwasababu dhambi ndani ya mtu ndio chanzo cha Upumbavu wote.

Sasa mtu kama huyu, hakuna kitu kinachoweza kuutoa upumbavu huo ndani yake, waweza kusema elimu, lakini ni watu wangapi wameelimika, lakini walevi, watukanaji, mashoga. Hata atwangwe vipi kinuni hawezi lainika, ikiwa hajui ni kipi sahihi kinachoweza kutoa upumbavu huo.

Kumfunga mwizi, hakumfanyi wizi au tamaa ya kuiba itoke ndani yake, mara ngapi unasikia mwizi katoka jela, karudia wizi wake, au ni kiongozi ambaye anaaminiwa awe kielelezo cha kupambana na ufisadi, lakini yeye ndio anakamatwa katika ufisadi, au teja ametolewa hospitalini karudia, tena madawa la kulevya. Ndio maana jamii ijapojaribu kudhibiti vitendo viovu, bado haviishi, bali hubadilika tu maumbile. Kwasababu mpumbavu hata atwangwe kinuni, hawezi geuka, hakuna nidhamu inayoweza mbadilisha. Huwezi acha mwenendo wake mbovu kwa semina za kijamii, au kuwekewa sheria

Je! Ni kipi kinachoweza kumgeuza?

Ni Yesu Kristo tu. Yeye ndiye aliyetiwa mafuta, na Mungu kuwaokoa watu wa Mungu na kuwafungua. Amwaminiye  na kudhamiria moyoni mwake kumfuata, basi atageuzwa moja kwa moja na kuwa mtu mwingine, huo ni uhakika.

Alisema.

Yohana 1:12  Bali wote waliompokea aliwapa UWEZO wa kufanyika watoto wa Mungu, ndio wale waliaminio jina lake.

Ni ahadi yake kuwa Ukimwamini jambo la kwanza ni kukusamehe dhambi zako, kwasababu ndio jambo lililomfanya aende msalabani kwa ajili yako miaka elfu mbili iliyopita,. Unakuwa huhesabiwi dhambi tena, unahesabiwa haki bure kwa neema yake. Lakini sambamba na hilo anakupa UWEZO wa kuwa kama yeye kwa nguvu za Roho wake Mtakatifu atakayemwachia ndani yako, pindi tu unapoamini.

Na baada ya hapo utashangaa tu unavyoanza kubadilika moyoni mwako.

Zingatia tu toba ya kweli, pamoja na ubatizo sahihi (kuzamishwa katika maji mengi kwa jina la Yesu Kristo). Na kumtii yeye.

Upumbavu utakutoka.

Bwana akubariki.

Washirikishe na wengine habari hizi njema kwa kushea

Ikiwa utapenda kupata msaada wa kumpokea Yesu maishani mwako bure, Basi wasiliana nasi kwa namba uzionazo chini ya makala hii.

Pia kwa kupokea mafundisho ya kila siku kwa njia ya WHATSAPP, jiunge na channel yetu kwa kupofya link hii >>https://whatsapp.com/channel/0029VaBVhuA3WHTbKoz8jx10

Kwa mawasiliano: +255789001312 au +255693036618

Bwana akubariki.

Mafundisho mengine:

Fahamu Maana ya Mithali 18:13 Yeye ajibuye kabla hajasikia, Ni upumbavu na aibu kwake.

HAUWEZI KURUKA MADARASA YA MUNGU!

Nini maana ya Mithali 9:13 Mwanamke mpumbavu hupiga kelele, Ni mjinga, hajui kitu?

Rudi Nyumbani

Print this post

Maana ya Mithali 26:2 Kama shomoro katika kutanga-tanga kwake,

SWALI: Nini maana ya Mithali 26:2

Kama shomoro katika kutanga-tanga kwake, Na kama mbayuwayu katika kuruka kwake; Kadhalika laana isiyo na sababu haimpigi mtu.


JIBU: Mungu anafananisha laana isiyo na sababu na ndege wanaotanga-tanga angani.

Kama tunavyojua ndege hawa aina ya shomoro na mbayuwayu, kila siku tunawaona wanaruka angani, kila siku tunawaona wapo hari-hari, wanaonekana kama wapo buzy, lakini katika kazi zao zote, na juhudi zao zote, na mikakati yao yote, kamwe huwezi ona yanaleta madhara yoyote kwa mwanadamu. Hata kama utawaharibia viota vyao, hata kama watakauwa na hasira na wewe, huwezi ona wanamshambulia mwanadamu, kwasababu uwezo huo hawana. Huwezi wafikiria na kila wanapokuona wanakimbia. Wewe mwenyewe ukiwaona huwezi kuwaogopa, tofauti na ukimwona nyoka, utajidhatiti asikuume. Lakini ndege huvai ‘chapeo’ kichwani kujilinda naye asikuume, kwasababu hana madhara.

Ndivyo Mungu anavyotufundisha, laana zisizo na sababu, haziwezi kukupata ni kama ndege tu angani, zitapita, na kuendelea na shughuli zake, kamwe haziwezi kukupata ikiwa wewe ni mtakatifu, Hii ni kutufundisha kuwa hatupaswi kuwa waoga wa maneno ya watu  (laana) ambayo hayana sababu.

Ukiona laana imekupata basi  ujue kulikuwa na sababu nyuma yake, (lakini sio tu maneno matupu mtu anayoyatoa), mfano wa laana hizi ni ile ya Elisha aliyowalaani wale vijana 42, walioraruliwa na dubu. Kwasababu walimdhihaki. (2Wafalme 2:22-25)

Lakini mfano wa laana zisizo na sababu, ni ile Goliathi aliyomlaani Daudi kwa miungu yake, ambayo  ilikuwa ni kazi bure..

1Samweli 17:42 Hata Mfilisti alipotazama huku na huku, akamwona Daudi akamdharau; kwa kuwa ni kijana tu mwekundu, tena ana sura nzuri.  43 Mfilisti akamwambia Daudi, Je! Mimi ni mbwa hata umenijia kwa fimbo? Mfilisti akamlaani Daudi kwa miungu yake

Ni mfano mwingine ni ile Balaamu mchawi alivyojaribu kuwalaani Israeli ikashindakana, kwasababu huwezi laani vilivyobarikiwa. (Hesabu 23)

Hata leo, ikiwa wewe umeokoka, hupaswi kuogopa, maneno yoyote iwe ya waganga au wanadamu. Kwasababu wewe tayari ni mbarikiwa. Ni ajabu sana kuona mkristo,  analia na kutetemeka, eti! Mchawi kamwambia mwaka huu hautaisha atakuwa watoto wake wote watakuwa wamekufa!!. Mzee wa mila kamwambia atapata ajali kwasababu hakutambika kijijini mwaka huu.

Mwingine anawaza, mzazi kamwambia hatafanikiwa kwasababu kaamua kuokoka. Haa! Unaogopa nini hapo?. Hizo ni laana zisizo na sababu. Ishi kwa amani zione tu kama ndege wa angani ambao hukai kuwafikiria kama watakushambulia siku moja.

Ukiokolewa na Kristo umebarikiwa, wewe sio wa kunenewa maneno ovyo ovyo tu, na yakatokea. Wewe ni uzao wa kifalme usiotetemeshwa, ngome imara isiyoangushwa. Mwamba mgumu usiogharikishwa. Yatambue mamlaka na nguvu ulizopewa ndani ya Kristo. Usiogope!

Washirikishe na wengine habari hizi njema kwa kushea

Ikiwa utapenda kupata msaada wa kumpokea Yesu maishani mwako bure, Basi wasiliana nasi kwa namba uzionazo chini ya makala hii.

Pia kwa kupokea mafundisho ya kila siku kwa njia ya WHATSAPP, jiunge na channel yetu kwa kupofya link hii >>https://whatsapp.com/channel/0029VaBVhuA3WHTbKoz8jx10

Kwa mawasiliano: +255789001312 au +255693036618

Bwana akubariki.

Mafundisho mengine:

Elewa maana ya Mithali 26:2 Kama shomoro katika kutanga-tanga kwake,

Nimekuwa kama mwari nyuni wa jangwani,

Maana yake nini, Mwe na hofu wala msitende dhambi? (Zaburi 4:4)

NUHU WA SASA.

Rudi Nyumbani

Print this post

Daudi alikuwa na wake wangapi, na je ni halali kuwa na wake wengi?

Swali: Napenda kujua Daudi alikuwa na wake wangapi na je na sisi tunaruhusiwa kuwa na wake wengi?


Jibu: Mfalme Daudi alikuwa na wake nane (8), waliotajwa katika biblia, ambao ni..

  1. MIKALI – Aliyekuwa binti sauli (soma 1Samweli 18:20).
  2. ABIGAILI – Aliyekuwa mke wa Nabali (Soma 1Samweli 25:39)
  3. BATH-SHEBA – Aliyekuwa Mke wa Uria ndiye mama yake Sulemani (Soma 2Samweli 12:24).
  4. AHINOAMU – Aliyekuwa mwenyeji wa mji wa Yezreeli (Soma 1Samweli 25:43 na 2Samweli 3:2).
  5. MAAKA- Aliyekuwa binti wa mfalme wa nchi ya Geshuri, aliyeitwa Talmai (Soma 2Samweli 3:3).
  6. HAGITHI- (Soma 2Samweli 3:4 na 1Wafalme 1:5).
  7. ABITALI- (Soma 2Samweli 3:4).
  8. EGLA- (Soma 2Samweli 3:5).

Wake wengine aliokuwa nao hawakutajwa katika biblia, lakini alikuwa nao wengine wengi, pamoja na masuria (nyumba ndogo), aliowatwaa kutoka katika mji wake YERUSALEMU.

2Samweli 5:12 “Akajua Daudi ya kwamba Bwana amemweka imara awe mfalme juu ya Israeli, na ufalme wake ameutukuza kwa ajili ya watu wake, Israeli.

13 Naye Daudi akazidi kujitwalia masuria na wake huko Yerusalemu baada ya kutoka Hebroni; wakazaliwa zaidi kwa Daudi wana na binti. ”

Lakini swali ni je!, kama Daudi alioa wake wengi, basi na sisi ni halali kuoa wake wengi?..

Jibu ni la!, ikiwa ni halali sisi kuoa wake wengi kwa kumwangalia Daudi, basi ni halali pia na sisi kuua kwasababu Daudi pia aliua!..lakini kama si halali kuua basi vile vile si halali kuoa wake wengi, kama Bwana wetu YESU KRISTO alivyotufundisha…

Mathayo 19:4  “Akajibu, akawaambia, Hamkusoma ya kwamba yeye aliyewaumba mwanzo, aliwaumba mtu mume na mtu mke,

5  akasema, Kwa sababu hiyo, mtu atamwacha babaye na mamaye, ataambatana na mkewe; na hao wawili watakuwa mwili mmoja?

6  Hata wamekuwa si wawili tena, bali mwili mmoja. Basi aliowaunganisha Mungu, mwanadamu asiwatenganishe”

Hivyo ndoa ni ya mke mmoja na mume mmoja, kwa urefu Zaidi fungua hapa >>>JE NI HALALI KUOA WAKE WENGI AU KUTOA TALAKA?

Bwana akubariki.

Washirikishe na wengine habari hizi njema kwa kushea

Ikiwa utapenda kupata msaada wa kumpokea Yesu maishani mwako bure, Basi wasiliana nasi kwa namba uzionazo chini ya makala hii.

Pia kwa kupokea mafundisho ya kila siku kwa njia ya WHATSAPP, jiunge na channel yetu kwa kupofya link hii >> https://whatsapp.com/channel/0029VaBVhuA3WHTbKoz8jx10

Kwa mawasiliano: +255789001312 au +255693036618

Bwana akubariki.

Mafundisho mengine:

Swali: Je idadi ya askari waliohesabiwa katika 1Nyakati 21:5 na 2Samweli 24:9 inajichanganya?.

NIFANYE NINI ILI NISILALE NINAPOSOMA BIBLIA.

VIGEZO VYA KUWA KARIBU NA YESU KRISTO KATIKA ULIMWENGU UJAO.

Vyemba ni nini kama tunavyosoma katika 2Samweli 18:14

JE! UNAWEZA KUWA NA GEUKO KAMA LA DAUDI?

Rudi Nyumbani

Print this post

Wakrete ni watu gani na walikuwaje  waongo? (Tito 1:12)

Swali: Biblia inasema wakrete walikuwa ni waongo na walishuhudiwa na nabii wao, je walikuwaje waongo  (walidanganya nini), na huyo nabii wao alikuwa nani?


Jibu: Wakrete ni jamii ya watu waliokuwa wanaishi mahali paitwapo “Krete” na Krete ni kisiwa kilichokuwepo katika nchi ya Ugiriki.

Sasa Mtume Paulo alimwandikia Tito waraka huu kumpa maagizo na maelekezo machache kuhusu kanisa na viongozi (katika uteuzi).. Kwa urefu kuhusiana na kitabu hiki cha Tito na maaelekezo Paulo aliyompa Tito kwa uongozo wa Roho Mtakatifu fungua hapa >>> MAMBO YA KUJIFUNZA KATIKA KITABU CHA TITO.

Lakini kwa ufupi ni kwamba tabia mojawapo waliyokuwanayo watu wa Krete, ni UONGO, Walikuwa wanasifa ya kusema Uongo katika viwango vikubwa, kiasi kwamba mpaka mtu wa kwao, ambaye ni nabii wao wenyewe aliandika kuhusiana na tabia hiyo waliyonayo waKrete ya Uongo, pamoja na ulafi na uvivu.

Biblia haijamtaja huyo Nabii ni nani, na wala haijaandika kuhusu huo waraka, lakini hapa tunaona Mtume Paulo ana unukuu…”

Tito 1:12 “..MTU WA KWAO, NABII WAO WENYEWE, AMESEMA, WAKRETE NI WAONGO SIKU ZOTE, HAYAWANI WABAYA, WALAFI WAVIVU

Sasa tukirudi katika historia, alikuwepo mwana filosofia wa KRETE aliyeitwa “EPIMEDINES”.. Huyu alikuwa ni Nabii wa mungu wa kigiriki aliyeitwa “zeu”..ambaye anatajwa katika Matendo 14:12-13.

Huyu Epimedines pamojana na kuwa alikuwa ni nabii wa mungu huyo wa kigiriki, lakini pia alikuwa ni mwandika mashairi. Moja ya shairi lake aliloliandika (ambalo aliliandika kwa kumtukuza huyo mungu wao wa kigiriki aliyeitwa zeu) lilikuwa linasema hivi..

…“Walikutengenezea kaburi, takatifu, uliye juu (zeu), Wakrete, waongo siku zote, wanyama wabaya, wavivu wa tumbo. Lakini wewe hukufa: unaishi na unakaa milele. Kwa maana ndani yako tunaishi, tunakwenda na kuwa na uhai wetu”…

Ni shari la kumtukuza mungu wao (zeu), lakini lilikuwa maarufu Krete kote kwani huyu Epimedines aliaminika na  wakrete wote kuwa ni nabii. Na Paulo kwasababu ni msomaji, aliujua huu ushairi, na hivyo katika kusisitiza dhambi ya wakrete ya Uongo kuwa ni kweli, ndio ananukuu hayo maneno ya nabii wao aliyewashuhudia kuwa ni waongo.

Lengo la Mtume Paulo si kumthibitisha nabii wao huyo La!.. bali kuthibitisha Uongo wa wakrete ambao watu wote wanauona hata walio wa Imani ya mbali… Hivyo ndio anamwonya Tito aukemee huo!.

Tunachoweza kujifunza ni kuwa UONGO ni mbaya, kwani biblia inashuhudia kuwa ibilisi ndiye baba wa Uongo, hivyo wote wadanganyi wote ni watoto wa ibilisi.

Yohana 8:44 “ Ninyi ni wa baba yenu, Ibilisi, na tamaa za baba yenu ndizo mpendazo kuzitenda. Yeye alikuwa mwuaji tangu mwanzo; wala hakusimama katika kweli, kwa kuwa hamna hiyo kweli ndani yake. Asemapo uongo, husema yaliyo yake mwenyewe; kwa sababu yeye ni mwongo, na baba wa huo”.

Bwana atusaidie tushinde dhambi.

Maran atha!

Washirikishe na wengine habari hizi njema kwa kushea

Ikiwa utapenda kupata msaada wa kumpokea Yesu maishani mwako bure, Basi wasiliana nasi kwa namba uzionazo chini ya makala hii.

Pia kwa kupokea mafundisho ya kila siku kwa njia ya WHATSAPP, jiunge na channel yetu kwa kupofya link hii >> https://whatsapp.com/channel/0029VaBVhuA3WHTbKoz8jx10

Kwa mawasiliano: +255789001312 au +255693036618

Bwana akubariki.

Mafundisho mengine:

WANNE WALIO WAONGO.

Mzushi ni nani kibiblia? (Tito 3:10).

UJUE UCHAWI WA MANABII WA UONGO?.

Mungu anachukia kuachana (Malaki 2:16)

UNAWAFAHAMU MANABII WA UONGO?

Rudi Nyumbani

Print this post

Kwanini Mungu aliwazuia walemavu wasimtumikie madhabahuni kwake?(Walawi 21:16-24)

SWALI: Kwanini katika agano la kale Mungu aliwazua walemavu wasimtumikie madhabahuni kwake? Ikiwa Mungu hana upendeleo kwanini aliliagiza hili litendeke?


Mambo ya Walawi 21:16-24

[16]Kisha BWANA akanena na Musa, na kumwambia,

[17]Nena na Haruni, umwambie, Mtu awaye yote wa kizazi chako wewe katika vizazi vyao, aliye na kilema, asikaribie kusongeza chakula cha Mungu wake.

[18]Kwa kuwa mtu awaye yote aliye na kilema hatakaribia; mtu kipofu, au kiwete, au mtu aliye na pua iliyoharibika, au aliye na kitu kilichozidi vimpasavyo mwili,

[19]au mtu aliyevunjika mguu, au aliyevunjika mkono,

[20]au aliye na kijongo, au aliye kibeti, au aliye na kilema cha jichoni, au aliye na upele, au mwenye buba, au aliyevunjika mapumbu;

[21]mtu awaye yote wa kizazi cha Haruni kuhani aliye na kilema asikaribie kuzisongeza sadaka za BWANA kwa njia ya moto; ana kilema huyo asikaribie kusongeza chakula cha Mungu wake.

[22]Atakula chakula cha Mungu wake, katika hicho kilicho kitakatifu sana, na hicho kilicho kitakatifu.

[23]Lakini hataingia ndani ya pazia, wala asikaribie madhabahu, kwa sababu ana kilema; ili kwamba asipanajisi patakatifu pangu; kwa kuwa mimi ndimi BWANA niwatakasaye.

[24]Basi Musa akanena na Haruni na wanawe, na wana wa Israeli wote.

JIBU: Agano la kale lilikuwa ni taswira ya agano jipya (la rohoni) jinsi litakavyokuwa baadaye (Wakolosai  2:17).

lile lilikuwa ni agano la mwilini, hivyo mambo mengi yalipaswa yadhihirishwe kwanza ki-mwilini ili kufunua au kufundisha kwa urahisi mambo ya rohoni yatakayokuja baadaye, lakini kiuhalisia haikuwa mpango wa Mungu mkamilifu yachukiliwe vilevile kwa majira yote.

Kwamfano mtoto mdogo anapoanza kujifunza hesabu, huwezi kumwambia  moja jumlisha na tatu ni nne. hatakuelewa. Bali utachukua kitu chenye umbo, (labda vijiti). utampa kimoja, kisha utachukua tena vijiti vingine vitatu utampa. halafu utamwambia avichanganye avihesabu atoe jumla.  atavihesabu vyote..na hapo hapo anakuambia nimepata vinne.

Sasa yeye atadhani hesabu ni vijiti. Lakini anapokuwa mtu mzima anagundua alipewa tu maumbo ili aelewe vizuri. Lakini hesabu ni uelewa wa akilini sio vijiti.

Vivyo hivyo na sisi tulipoanza kuelezwa makusudi makamilifu ya Mungu, tulifananishwa na watoto (Wagalatia 4:1-6). Mungu hakutaka kumleta Kristo moja kwa moja afe, amwage damu yake, ndipo sisi tuondolewe dhambi zetu kwa hiyo damu. Ukweli ni kwamba tusingemwelewa Mungu, vema.

Hivyo alitanguliza agano la kale kwanza, la mwilini, la mambo ya nje. Tuelewe kitaswira jinsi ilivyo sawa na isivyo sawa. ndipo baadaye atumie mifano hiyo kueleza ya rohoni.

kwamfano walikatazwa kula nguruwe, sababu alikuwa hacheui, mnyama asiyecheua ni yule asiyeweza kurejesha chakula akakitafuna na kukimeza tena kama ng’ombe. Sasa lengo la Mungu sio kwasababu nguruwe alikuwa ana magonjwa. kiuhalisia nguruwe ni mboga nzuri tu, lakini ni kwasababu ya ile sifa, ya kutocheua, ambayo rohoni sisi tunafundishwa hatupaswi kuwa nayo. maana yake ukishindwa kutafakari, yale uliyotendewa na Mungu nyuma, au uliyofundishwa na Mungu, wewe ni sawa na kiumbe najisi, mfano wa nguruwe. kwasababu hutaweza kuwa mtu wa shukrani, hutaweza kuwa mtu wa imani. Wana wa Israeli walionyesha tabia hii, wakati wanavuka habari ya shamu. walimnung’unikia Mungu wakisema unatuua, kwasababu hawana chakula. hawakukumbuka miujiza mikubwa aliyowatendea kipindi kifupi nyuma. Lakini Daudi alipokutana na Goliati hakulia wala kuogopa alisema yule Bwana aliyeniokoa na dubu na simba ataniokoa na mfilisti huyu asiyetahiriwa. alicheua akala tena akapata nguvu ya kuendelea mbele, kumshinda adui. Hakutaka kuwa nguruwe.

sasa tukirudi pia katika mambo ya madhabahuni kufuatana na swali letu.  Kumbuka waliopewa nafasi ya kuhudumu hekaluni walikuwa ni jamii ya makuhani tu, wazao wa Lawi. Mtu mwingine yeyote hakuruhusiwa. Vilevile hata yule mlawi ikiwa ni mlemavu wa aina yoyote pia hakuruhusiwa.

Kuonyesha kuwa hawakutengwa wao tu, hata watu wa kabila nyingine, haijalishi ni manabii au wanamtumikia Mungu kiasi gani ikiwa wewe si mlawi hukuruhusiwa hata na wanawake wote, hawakuwa tofauti na vilema katika suala la kuhudumu. Kwahiyo hawakutengwa walemavu tu. Bali na makundi mengine yote.

Sasa kwanini Mungu akataze walemavu na wenye madhaifu wasihudumu. Kwasababu Mungu alikuwa.anaonyesha picha ya rohoni ni jinsi gani watumishi wake, wahudumu.wa madhabahuni wanavyopaswa wawe, kwamba wasiwe watu wenye kasoro mbele zake. Yaani wawe watu wakamilifu sio walemavu rohoni.

Huo ndio ulikuwa ujumbe wa Mungu, hakuwa na Neno lolote baya na walemavu. Wala hakuwachukia.

Na ndio maana tunapokuja agano jipya tunaona vipofu, viwete, mabubu wanamjia Mungu, anawaponya. Na isitoshe Yesu alikuwa anakwenda kukaa kwao na kula nao (Marko 14:3).

Mungu hashughulika na ulemavu wa mwilini, bali ule wa rohoni. Ambao ukiwa mdhaifu huko, wewe ni najisi mbele zake. pitia somo hili ufahamu zaidi juu ya ulemavu wa rohoni upoje.

>>> UKOMA NA UJANE ULIO NDANI YAKO, UMEUPATIA TIBA?

wapo walemavu wengi, ambao wengine Mungu mwenyewe ameruhusu wawe vile kwa ushuhuda wake, na wanamtumikia kwa namna isiyo ya kawaida na wanafanya miujiza mikubwa, wanaponya watu na kuwafungua, utauliza kwanini Mungu asiwaponye? mawazo ya Mungu si mawazo yetu, Elisha alikufa na ugonjwa wake, lakini mifupa yake ilifufua wafu.

fuatilia ushuhuda huu ukujenge…. >>> USHUHUDA WA RICKY:

Hii ni kutuonyesha kuwa,  wakati wa sasa mbele za Mungu hakuna mwanamume, au mwanamke, au mlemavu au mtumwa wote ni makuhani wake na tumestahilishwa na Yesu Kristo kuingia patakatifu pa patakatifu kwa damu yake sisi tuliomwamini….

Haleluya. Upendo wake ni wa ajabu kwetu.

Shalom

Washirikishe na wengine habari hizi njema kwa kushea

Ikiwa utapenda kupata msaada wa kumpokea Yesu maishani mwako bure, Basi wasiliana nasi kwa namba uzionazo chini ya makala hii.

Pia kwa kupokea mafundisho ya kila siku kwa njia ya WHATSAPP, jiunge na channel yetu kwa kupofya link hii >> https://whatsapp.com/channel/0029VaBVhuA3WHTbKoz8jx10

Kwa mawasiliano: +255789001312 au +255693036618

Bwana akubariki.

Mafundisho mengine:

Mimbari ni nini? Je tofauti kati ya Mimbari na madhabahu ni ipi?

NITAONGEZAJE NGUVU ZANGU ZA ROHONI?

Ulimwengu wa Roho ni nini? Na mtu anawezaje kuwa wa rohoni?

CHAKULA CHA ROHONI.

Rudi Nyumbani

Print this post

Je mkristo anaruhusiwa kuchangia damu?

Swali: Je mkristo anaruhusiwa kuchangia damu kwa mgonjwa aliye katika uhitaji huo, kwaajili ya kuokoa maisha yake?


Jibu: Biblia inasema maneno yafuatayo…

1Yohana 3:16 “Katika hili tumelifahamu pendo, kwa kuwa yeye aliutoa uhai wake kwa ajili yetu; IMETUPASA NA SISI KUUTOA UHAI WETU KWA AJILI YA HAO NDUGU.

17  Lakini mtu akiwa na riziki ya dunia, kisha akamwona ndugu yake ni mhitaji, akamzuilia huruma zake, je! Upendo wa Mungu wakaaje ndani yake huyo”

Maadamu mtu akiondolewa damu kiasi kidogo mwilini mwake, Hafi!!.. na vile vile mtu anayepokea damu mwilini mwake pia Hafi!, kinyume chake ndio anapata UZIMA! (wa mwilini).. basi ni wazi kuwa si dhambi kuchangia damu kwa mtu mwingine…..Zaidi sana ni jambo la upendo, ikiwa hakuna njia nyingine ya kumsaidia mhitaji huyo zaidi ya hiyo ya kumchangia damu.

Kwanini si dhambi!.. ni kwasababu hata sehemu ya damu tulizonazo tumepokea kutoka kwa wazazi wetu!…HAKUNA MTU ANAYEZALIWA DUNIANI NA DAMU YAKE MAALUM (Special), wote tunazipokea kutoka kwa wazazi wetu ndio maana zinamfanano na hao!, na zinamfanano na ndugu zetu tuliozaliwa nao familia moja.

Kwahiyo kumchangia damu mgonjwa si dhambi!… Maana utamchangia atapona!, na kwa njia hiyo yaweza kuwa sababu ya kumvuta kwa KRISTO, (akiona upendo wako namna hiyo).. lakini kama ukimnyima na akifa katika hali yake ya kutokuamini hakuna faida yoyote wewe unayoipata…

Kwahiyo ni afadhali utafute namna ya kuokoa roho kwa njia hiyo, kwasababu hakuna hasara yoyote unayopata katika mwili wako utoapo kiasi kidogo hiko cha damu na kumpatia mwingine!.. ni lita ngapi za damu umepoteza wakati wa mzunguko wako (wewe mwanamke) na bado unaendelea kuishi.

Ni lita ngapi za damu umepoteza wewe mwanaume ulipopata majeraha au ulipofyozwa na hao mbu kutandani mwako siku zote za maisha yako?.. Kwa kutafakari hayo yote hakuna sababu ya kumnyima damu ndugu yako, ikiwa kuna ulazima huo, na wala hakuna sehemu yoyote kwenye biblia iliyokataza kuchangia damu.

Bwana akubariki.

Washirikishe na wengine habari hizi njema kwa kushea

Ikiwa utapenda kupata msaada wa kumpokea Yesu maishani mwako bure, Basi wasiliana nasi kwa namba uzionazo chini ya makala hii.

Pia kwa kupokea mafundisho ya kila siku kwa njia ya WHATSAPP, jiunge na channel yetu kwa kupofya link hii >> https://whatsapp.com/channel/0029VaBVhuA3WHTbKoz8jx10

Kwa mawasiliano: +255789001312 au +255693036618

Bwana akubariki.

Mafundisho mengine:

Je!Sisi kama wakristo Tunaruhusiwa kuchangia ujenzi wa Imani nyingine?

Je mama mjamzito anaruhusiwa kufunga?

Tofauti ya kazi ya Damu ya Yesu na Jina la Yesu ni ipi?

Nini maana ya Mithali 27:21  inaposema “mtu hujaribiwa kwa sifa zake?”

JE UMEUFIKIA ULE UTUKUFU HALISI WA MANA? 

Rudi Nyumbani

Print this post

Kwanini kuna mrudio wa uumbaji kwenye Mwanzo sura ya pili?

Swali: Tukisoma Mwanzo sura ya kwanza tunaona Mungu akimaliza kazi yote ya uumbaji kwa zile siku saba, lakini tukirudi kwenye Sura ya pili tuona ni kama tena Mungu anarudia uumbaji anamuumba mwanadamu,  na pia mimea, je kulikuwa na uumbaji wa aina mbili ulitokea pale. Na ni nini tunajifunza pale?


JIBU: Jibu ni hapana, uumbaji wa Mungu ulikuwa ni ule ule mmoja, tofauti na baadhi ya watu wanavyodhani. isipokuwa Sura ya kwanza Mungu anaeleza ‘kwa taswira ya ujumla’, lakini katika sura ya pili anaeleza jinsi ‘utaratibu wa uumbaji wake ulivyokuja kutokea’, mpaka kuileta hiyo picha ya ujumla.

Kwamfano katika Sura ya kwanza anasema Mungu alimuumba mwanamke na mwanaume..

Mwanzo 1:27 Mungu akaumba mtu kwa mfano wake, kwa mfano wa Mungu alimwumba, mwanamume na mwanamke aliwaumba.

28 Mungu akawabarikia, Mungu akawaambia, Zaeni, mkaongezeke, mkaijaze nchi, na kuitiisha; mkatawale samaki wa baharini, na ndege wa angani, na kila kiumbe chenye uhai kiendacho juu ya nchi.

Lakini katika sura ya pili anaonyesha jinsi alivyoanza kumuumba  kwa kumtoa ardhini mpaka alivyompulizia pumzi ya uhai, hadi utaratibu wake wa kutawala.

Mwanzo 2:4 Hivyo ndivyo vizazi vya mbingu na nchi zilipoumbwa. Siku ile Bwana Mungu alipoziumba mbingu na nchi

5 hapakuwa na mche wa kondeni bado, wala mboga ya kondeni haijachipuka bado, kwa maana Bwana Mungu hajainyeshea nchi mvua, wala hapana mtu wa kuilima ardhi;

6 ukungu ukapanda katika nchi, ukatia maji juu ya uso wote wa ardhi.  7 Bwana Mungu akamfanya mtu kwa mavumbi ya ardhi, akampulizia puani pumzi ya uhai; mtu akawa nafsi hai.

8 Bwana Mungu akapanda bustani upande wa mashariki wa Edeni, akamweka ndani yake huyo mtu aliyemfanya.

Umeona,? Vilevile ukisoma Mwanzo 1:11&12, utaona Mungu anaumba mimea yote . Lakini hapo kwenye sura ya pili anaonyesha  jinsi mime hiyo inavyokuja kutokea, anaeleza kwanza inaanza  katika mbegu, kisha inyeshewe mvua, ikue baadaye ndio iwe mche kamili wenye matunda.

Hivyo, Kulikuwa na umuhimu wa kuwekwa sura zote mbili, ili tuelewe  kanuni za Mungu za utekelezaji wa mipango yake. Maana kama tungeishia tu sura ya kwanza tusingeelewa ni kwa namna gani mambo yanaendelea kama yalivyo leo.

Ni fundisho gani lipo hapo?

Hata sasa Mungu anasema jambo. Lakini pia huna budi kuelewa mpango wake wa utekelezaji wa hilo jambo! Ili usiudhike, au usikate tamaa, au usijikwae, au usiwe na mashaka. Unatafakari ni kweli Mungu alimuumba mwanamke tangu awali, lakini kutokea kwake kulikuja baadaye sana, tena sio ardhini bali ubavuni mwa Adamu. Kama hilo tusingelifahamu, tusingeelewa kwanini tunaambiwa sisi wote ni mwili mmoja.

Kama tusingejua kuwa  ili mti ufikie matunda, kama Mungu alivyoukusudia, ni lazima uanze kwanza kama mbegu, ioze ardhini, kisha ipate mvua, imee, itoke katika jani, hadi shina, hadi mti. Tungesema hii si sawa, kuna shida, mbegu kuoza ardhini, hakuna mmea hapo?.

Halikadhalika hata sasa Mungu amekuahidi pengine, atakupa jambo Fulani. Sasa usitarajie lije ghafla tu, pengine litapitia hatua Fulani, huwenda likaonekana kama limetoweka kabisa,kama vile mbegu inayooza ardhini, lakini mwishowe itakuja kutokea tu, kama tu Yusufu alivyoonyeshwa kuwa ndugu zake watamwinamia, Au Ibrahimu kuonyeshwa atakuwa  baba wa mataifa mengi, lakini mapito yao unayajua, Yusufu kuuzwa utumwani, kutupwa gerezani, Ibrahimu kuwa tasa. Lakini mwisho utaona yale waliyoahidiwa yalikuja kutokea vilevile.

Tunapaswa tumwelewe sana Mungu ili tuwe na amani, Neno la Mungu linaposema, kwa kupigwa kwake sisi tumepona, amini kuwa umepona kwa kifo cha Yesu, hata kama utahisi maumivu mengi kiasi gani leo, daktari atakuambia huwezi kupona ugonjwa wako hautibiki. Wewe amini, tu hilo jambo litatokea, haijalishi litachukua wakati gani, utapitia mateso mengi kiasi gani leo, mwisho wa siku utakuwa tu mzima.

Usiishi tu na mwanzo sura ya kwanza, ishi pia na sura ya pili. Utamwelewa Mungu.

Bwana akubariki.

Washirikishe na wengine habari hizi njema kwa kushea

Ikiwa utapenda kupata msaada wa kumpokea Yesu maishani mwako bure, Basi wasiliana nasi kwa namba uzionazo chini ya makala hii.

Pia kwa kupokea mafundisho ya kila siku kwa njia ya WHATSAPP, jiunge na channel yetu kwa kupofya link hii >> https://whatsapp.com/channel/0029VaBVhuA3WHTbKoz8jx10

Kwa mawasiliano: +255789001312 au +255693036618

Bwana akubariki.

Mafundisho mengine:

NGUVU YA MUNGU YA UUMBAJI

Kwanini Bwana achukizwe na mtumwa yule aliyeficha talanta yake ardhini? (Mathayo 25:26-30)

Ni maneno gani Bwana Yesu aliyokuwa anayaandika ardhini? (Yohana 8:7).

Rudi Nyumbani

Print this post

Nyota ya bahati yangu ni ipi?

Je ni kweli kuna watu wenye nyota ya bahati? Na je nitaipate nyota hiyo maishani mwangu?


JIBU: Nyota ya bahati inasadikika ni pale mtu anapobahatika kupata kitu kwa haraka au kwa wepesi, au bila matarajio yake,au nguvu zake nyingi katika kukipata tofauti na wengine. Kwamfano labda mtu ni mchimba madini, mara ghafla anatapa dhahabu nyingi tofauti na wachimbaji wengine. Au mwingine amehitimu chuo, mara anapata kazi nzuri, yenye cheo, zaidi hata ya wengine wengi waliomtangulia. Au ni mfanya-biashara mara anapata tenda kubwa ambayo inainua biashara yake kwa kasi zaidi ya wengine. N.k.

Sasa mtu kama huyu wengi husema ana nyota ya bahati. Lakini je ni kweli?

Ukweli ni kwamba twaweza kusema ana-bahati –tu, lakini hana nyota-ya-bahati. Kwavipi.

Kwasababu mafanikio hayo, yanaweza kuondoka tena kwake, na kama yakibaki, bado bahati hiyo hainunui tunu za rohoni. Mfano amani, upendo, utu wema,  imani, adili, unyenyekevu, na uzima baada ya kifo. N.k., Ni mafanikio ambayo hata mashetani huyatoa.

Lakini ni lazima ujue nyota halisi ya bahati ni ipi? Ambayo katika hiyo unaweza kupata vyote, Kisha uifuate.

Hiyo si nyingine zaidi ya YESU KRISTO. Vitabu vitakatifu vinasema hivyo, Vilevile Watu wote wanalijua hilo, ikiwemo wachawi wote, wanajimu wote, malaika wote, na mashetani yote.

Soma hapa;

Mathayo 2:1  Yesu alipozaliwa katika Bethlehemu ya Uyahudi zamani za mfalme Herode, tazama, MAMAJUSI WA MASHARIKI walifika Yerusalemu, wakisema,

2  Yuko wapi yeye aliyezaliwa mfalme wa Wayahudi? Kwa maana TULIIONA NYOTA YAKE MASHARIKI, nasi tumekuja kumsujudia.

3  Basi mfalme Herode aliposikia hayo, alifadhaika, na Yerusalemu pia pamoja naye. 4  Akakusanya wakuu wa makuhani wote na waandishi wa watu, akatafuta habari kwao, Kristo azaliwa wapi?

5  Nao wakamwambia, Katika Bethlehemu ya Uyahudi; kwa maana ndivyo ilivyoandikwa na nabii,

6  Nawe Bethlehemu, katika nchi ya Yuda, Hu mdogo kamwe katika majumbe wa Yuda; Kwa kuwa kwako atatoka mtawala Atakayewachunga watu wangu Israeli.

7  Kisha Herode akawaita wale mamajusi faraghani, akapata kwao hakika ya muda tangu ilipoonekana ile nyota.

8  Akawapeleka Bethlehemu, akasema, Shikeni njia, mkaulize sana mambo ya mtoto; na mkiisha kumwona, nileteeni habari, ili mimi nami niende nimsujudie.

9  Nao waliposikia maneno ya mfalme, walishika njia; na tazama, ile nyota waliyoiona mashariki ikawatangulia, hata ikaenda ikasimama juu ya mahali alipokuwapo mtoto.

10  NAO WALIPOIONA ILE NYOTA, WALIFURAHI FURAHA KUBWA MNO.

11  Wakaingia nyumbani, wakamwona mtoto pamoja na Mariamu mamaye, wakaanguka wakamsujudia; nao walipokwisha kufungua hazina zao, wakamtolea tunu; dhahabu na uvumba na manemane.

Ikiwa Yesu yupo moyoni mwako. Ikiwa umemwamini, kisha ukamfanya Bwana na kiongozi wa maisha yako. Jambo la kwanza analolifanya ndani yako ni kuondoa laana yote ya dhambi, ambayo humfanya mwanadamu aende kuzimu, ambayo kila mwanadamu anayo. Na wakati huo huo huyo mtu anaitwa mbarikiwa, anaitwa mtakatifu, makosa yake yote yanakuwa yamefutwa, hahesabiwi dhambi tena.

Na moja kwa moja anapewa, Roho Mtakatifu. Sasa Kazi ya huyu Roho Mtakatifu, ni kumtengeneza roho yake,kumsafisha kutoka katika ubaya kumweka katika wema, na kumfanya aweze kushinda dhambi na maovu yote.

Ndio hapo kama alikuwa mlevi, kiu hiyo inaondolewa, alikuwa mzinzi, hamu ya mambo hayo yanakufa ndani yake, alikuwa ana uchungu, furaha inaanza kujengeka, alikuwa ni mwenye hasira, upendo wa ki-Mungu unaumbika sana moyoni mwake, anaanza kupenda watu wote.

Na zaidi sana, anapokea uzima wa milele, hata akifa ghafla, haendi kuzimu, hapotei, bali anakuwa amelala tu, anasubiri siku ya ufufuo, aamshwe aende mbinguni.

Pamoja na hilo, hata yale mengine ambayo alikuwa anayatafuta au anayapata kwa shida, Yesu anampa mafanikio pia  kiwepesi kwasababu aliahidi hivyo. Zile bahati ambazo anatamani azipate, Yesu anamletea mara mia (100), katika maisha yake.

Mathayo 19:28  Yesu akawaambia, Amin, nawaambia ya kwamba ninyi mlionifuata mimi, katika ulimwengu mpya, atakapoketi Mwana wa Adamu katika kiti cha utukufu wake, ninyi nanyi mtaketi katika viti kumi na viwili, mkiwahukumu kabila kumi na mbili za Israeli.

29  NA KILA MTU ALIYEACHA NYUMBA, AU NDUGU WA KIUME AU WA KIKE, AU BABA, AU MAMA, AU WATOTO, AU MASHAMBA, KWA AJILI YA JINA LANGU, ATAPOKEA MARA MIA, NA KUURITHI UZIMA WA MILELE.

Umeona, mwisho wa siku unakuwa umepata vyote, kwasababu kwa Yesu vipo vyote.

Huoni kuwa hiyo ni NYOTA nzuri sana ya bahati? Kwanini uende wa waganga wa kienyeji, kutafuta laana, huko? Kwasababu wale wanakurushia mapepo, ambayo mafanikio yao ni batili, ni kitanzi, mwisho wa siku ni kukuangamiza, sasa unakuwa umepata faida gani? Wakati mafanikio ya Yesu Kristo, hutajirisha wala hayana huzuni ndani yake, biblia inasema hivyo;

Mithali 10:22 Baraka ya Bwana hutajirisha, Wala hachanganyi huzuni nayo

Ungoja nini usimpokee Yesu leo? Ikiwa umedhamiria kwa dhati kufanya hivyo, basi fungua hapa kwa mwongozo wa namna ya kuokoka leo >>>>> KUONGOZWA SALA YA TOBA

Washirikishe na wengine habari hizi njema kwa kushea

Ikiwa utapenda kupata msaada wa kumpokea Yesu maishani mwako bure, Basi wasiliana nasi kwa namba uzionazo chini ya makala hii.

Pia kwa kupokea mafundisho ya kila siku kwa njia ya WHATSAPP, jiunge na channel yetu kwa kupofya link hii >>https://whatsapp.com/channel/0029VaBVhuA3WHTbKoz8jx10

Kwa mawasiliano: +255789001312 au +255693036618

Bwana akubariki.

Mafundisho mengine:

Falaki ni elimu gani? (Isaya 47:13).

NYOTA YA ASUBUHI.(Opens in a new browser tab)

JINSI WATU WANAVYOZAMA KATIKA USHIRIKINA NA UCHAWI.

Rudi Nyumbani

Print this post

Nuhu akaanza kuwa mkulima, akapanda mizabibu.

Ni nini tunajifunza katika maisha ya Nuhu, ambaye Mungu alimshuhudia kuwa mwenye haki katika kizazi chake? Lakini baadaye akaja kunaswa katika ulevi uliomletea aibu kubwa nyumbani mwake?

Mwanzo 9:20 Nuhu akaanza kuwa mkulima, akapanda mizabibu;  21 akanywa divai, akalewa; akawa uchi katika hema yake.

Ulishawahi kujiuliza kama Nuhu asingekuwa mkulima wa mizabibu, angekuwa na wazo la kutengeneza divai? Na hatimaye kuanguka kwenye makosa?

Jibu ni la! Kwasababu bila shaka Nuhu alikuwa mkulima, ili ajipatie rizki, na sio ili atengeneze divai. Lakini hakujua kuwa nyuma ya kazi yake ya halali upo mtego wa dhambi. Na hivyo akauridhia na ndio ikamshawishi mpaka kutoa bidhaa isiyopasa katika maisha yake kwa kazi hiyo.

Hata sasa watoto wengi wa Mungu wanashindwa kujua kuwa “shughuli za ulimwenguni zilizo za halali kabisa” zina udanganyifu Fulani nyuma yake, unaolewesha ambao unaweza mpelekea mtu anguko kubwa sana, kama asipokuwa makini.

Bwana Yesu alisema..

Marko 4:18  Na hawa ndio wale wapandwao penye miiba; ni watu walisikiao lile neno, 19  na SHUGHULI ZA DUNIA, NA UDANGANYIFU WA MALI, na tamaa za mambo mengine zikiingia, hulisonga lile neno, likawa halizai.

Kwamfano labda ni kijana, ameokoka, hapo mwanzo alikuwa amesimama vizuri tu, katika Bwana, anapata muda wa kuomba, kushuhudia, kujisomea Neno n.k. lakini akapata kazi nzuri, na ile kazi ikawa inamlazimu, awe bize wiki nzima, isipokuwa jumamosi na jumapili. Sasa katika miezi ya mwanzo, alikuwa anatimiza majukumu yake ya ushuhudiaji/ kuhudhuria mikusanyiko ya nyumbani na maombi, bila shida siku ya jumamosi, na jumapili anahudhuria ibadani , kama kawaida. Lakini baada ya miezi kadhaa, alivyozidi kufanikiwa, uvivu na udanganyifu wa mali ukaanza kumuingia, akasema, huu muda wangu wa jumamosi, nifanye kitu kingine cha kuniingizia kipato, (jambo  ambalo si baya), lakini hajui kuwa analisogeza mahali ambapo sio sahihi. Na kweli akajiongezea kitu cha kufanya, matokeo yake jumamosi yake yote ikawa ni kazi zake za miradi. Hakuna ushuhudiaji tena, hakuna ibada za jumuiya tena, hakuna maombi.

Na inapofika jumapili, anaamka amechoka, anasema, aa wiki hii napumzika, wiki ijayo nitaenda..anaanza kuwa mdokoaji-dokoaji wa ibada,  hivyo baada ya miezi miwili, anapokea mialiko ya marafiki zake, kwenda kwenye party, picnic, vikao vya kirafiki, sinema, n.k. vyote hivyo vinapaswa vifanyike siku ya jumapili ambayo yupo free. Matokeo yake anahudhuria kanisani mara moja kwa mwezi au miezi miwili. Hilo linaendelea mwaka mzima. Hajui kuwa mwili unafurahia kweli, lakini roho yake inadhoofika siku baada ya siku. Sasa baada ya kipindi kirefu hapo ndipo anashangaa haoni tofauti yake ni watu wa kidunia, kila jambo la ki-Mungu anaona ni mzigo kulifanya, yeye ambaye alikuwa anawaombea wengine anakuwa wa kuombewa, yeye ambaye alikuwa anawaokoa wengine, anafikiwa kuokolewa tena.Hana nguvu tena, ameshaleweshwa, shetani kamweka chini.

Sasa huyu ndio mfano wa Nuhu, Amelewesha na kazi yake. Na utumishi wake. Kwasababu hakujiwekea mipaka,.

Ndio maana maandiko yanatutaka tuwe na kiasi, katika huu ulimwengu.

1Wakorintho 7:31  Na wale wautumiao ulimwengu huu, kama hawautumii sana; kwa maana mambo ya ulimwengu huu yanapita.

Kuwa buzy kupita kiasi, si afya ya kiroho au kimaisha. Ni lazima upate nafasi ya kutosha kujijenga nafsi yako kwa Mungu. Ni vema utumie siku za tano, usiku na mchana kama ni hivyo kuwekeza na kupangilia ratiba yako, lakini upate pia nafasi nyingi ya kumwabudu na kumkaribia Mungu bila masumbufu. Umeajiriwa katika kazi ambayo siku zote saba za wiki, upo kazini, hupewi muda wa kupata ibada yako na Mungu, fahamu hiyo si kazi itokayo kwa Mungu. Fikiria kutafuta kazi nyingine.

Kama ubize, basi Mungu angekuwa buzy zaidi yetu sisi, kwasababu yeye ndio aliyeumba ulimwengu mzima, lakini alijipa pumziko Siku ya saba, akaiweka wakfu, akatuambia na sisi. Tufanye hivyo. Kumbuka hizi ni siku za mwisho, na wengi wataikosa mbingu kwa ubize usiokuwa na tija wa mambo ya ulimwengu huu, yanayopita.

Ni heri ukose vya dunia, lakini nafsi yako itajirike, kuliko kutajirika duniani na huku nafsi yako unaangamia. Uzima wako upo katika mambo ya rohoni, Jinsi unavyojitenga na Mungu ndivyo unavyojiua mwenyewe.

Kamwe usiyaige ya Nuhu mabaya ya ajira yake, bali yale mema aliyoyafanya kabla ya Gharika.

Shalom.

Washirikishe na wengine habari hizi njema kwa kushea

Ikiwa utapenda kupata msaada wa kumpokea Yesu maishani mwako bure, Basi wasiliana nasi kwa namba uzionazo chini ya makala hii.

Pia kwa kupokea mafundisho ya kila siku kwa njia ya WHATSAPP, jiunge na channel yetu kwa kupofya link hii >>https://whatsapp.com/channel/0029VaBVhuA3WHTbKoz8jx10

Kwa mawasiliano: +255789001312 au +255693036618

Bwana akubariki.

Mafundisho mengine:

KWANINI MTINI KATIKATI YA MIZABIBU?

UMUHIMU WA KUBATIZWA.(Opens in a new browser tab)

NUHU WA SASA.(Opens in a new browser tab)

(Opens in a new browser tab)KWANINI NI NUHU, AYUBU NA DANIELI?(Opens in a new browser tab)

Rudi Nyumbani

Print this post

Kuota unakemea mapepo/ unashindana na nguvu za giza.

Kunaweza maanisha namna tatu, ya kwanza, ni kwamba unapitia kweli vita vya kiroho, lakini ya pili ni unaonyeshwa na Mungu uhalisia wa vita vya kiroho, na tatu unaonyeshwa uwezo wa hali yako ya  kiroho.

Maandiko yanasema

Waefeso 6:12  Kwa maana kushindana kwetu sisi si juu ya damu na nyama; bali ni juu ya falme na mamlaka, juu ya wakuu wa giza hili, juu ya majeshi ya pepo wabaya katika ulimwengu wa roho.

13  Kwa sababu hiyo twaeni silaha zote za Mungu, mpate kuweza kushindana siku ya uovu, na mkiisha kuyatimiza yote, kusimama

Tukianza na maana ya kwanza,

Mara nyingine adui huanzisha mashambulizi kuanzia ndotoni, wakati mwingine utakuta mtu anaota ameumwa labda na nyoka kidoleni halafu  anapoamka, anashangaa kinauma kweli, na kama haiishii hapo, anaanza kuona kidole kinazidi kutengeneza kidonda, mpaka kuleta madhara mwili mzima, sasa hayo ni mashambulizi ya kipepo. Na hivyo ikiwa ndoto yoyote umeiota ambayo unaona uhalisia wake mpaka nje, unashindana na mapepo halafu linakukaba, unahangaika kitandani. Ujue ni mashambulizi ya adui, hapo unayo mamlaka ya kubatilisha, kwa jina la Yesu.

Lakini mara nyingine, utajikuta unaota tu unakemea mapepo, unashindana nayo. Si kwamba utakuwa unamashambulizi ya adui, lakini unaonyeshwa tu uhalisia wa vita vya kiroho, na hivyo vipo halisi, au vitakuja mbeleni katika safari yako ya maisha, na unapaswa uvishinde, kwa jina la YESU, kwa simama imara ndani yake..

Na mwisho ni Mungu anakuonyesha kiwango cha kiroho, ulichopo au unachopaswa uwe nacho. Mwingine atakuwa ameokoka, lakini anahofu ya kutoa pepo au kuombea watu, Mungu anakuonyesha uwezo wa kushindana na nguvu za giza unao, au unapaswa uanze kazi ya kuwaombea wengine wanaosumbuliwa na nguvu za giza. Lakini pia pale unapojiona umezidiwa nguvu zao, ni kuonyesha uongeze kiwango chako cha kiroho, kwa maombi, utakatifu, na Neno, ili uwe thabiti rohoni kuzipinga hila za adui.

Kwahiyo kwa vyoyote vile kuona unakemea mapepo, au unashindana na wachawi kwa jina la Yesu. Ni kuonyesha kuwa ni wakati wa kusimama  imara na Bwana. Kwasababu shetani ni adui wako, na adui za ndugu zako, na hivyo unapaswa umpinge sikuzote kwa kuwa thabiti rohoni kwa wewe ambaye umeokoka.

Lakini Ikiwa hujaokoka, basi ni vema ukafanya hivyo leo kwa kumkaribisha Yesu moyoni mwako, ukifahamu kuwa kamwe huwezi kumshinda adui kwa nguvu zako unamwita Kristo.

Ikiwa upo tayari  waweza kufungua hapa kwa mwongozo wa sala ya kuupokea wokovu. >>>> KUONGOZWA SALA YA TOBA

Washirikishe na wengine habari hizi njema kwa kushea

Ikiwa utapenda kupata msaada wa kumpokea Yesu maishani mwako bure, Basi wasiliana nasi kwa namba uzionazo chini ya makala hii.

Pia kwa kupokea mafundisho ya kila siku kwa njia ya WHATSAPP, jiunge na channel yetu kwa kupofya link hii >> https://whatsapp.com/channel/0029VaBVhuA3WHTbKoz8jx10

Kwa mawasiliano: +255789001312 au +255693036618

Bwana akubariki.

Mafundisho mengine:

UMEFUNGWA KATIKA GIZA NA UVULI WA MAUTI?(Opens in a new browser tab)

Je Mungu anaketi katika giza? (1Wafalme 8:12)

Uasherati wa Kiroho maana yake nini?(Opens in a new browser tab)(Opens in a new browser tab)

Rudi Nyumbani

Print this post