Category Archive Home

SIFA TATU ZA MUNGU.

Tukisoma katika biblia mahali pengine Bwana alijitambulisha kama  ALFA na OMEGA.

Ufunuo 22: 12 “Tazama, naja upesi, na ujira wangu u pamoja nami, kumlipa kila mtu kama kazi yake ilivyo.13 Mimi ni Alfa na Omega, mwanzo na mwisho, wa kwanza na wa mwisho”.

Hapo kuna vitu vitatu…1) Yeye ni Alfa na Omega…2) Yeye ni mwanzo na mwisho….3) Yeye ni wa kwanza na wa mwisho.

Hizo ni sentensi tatu zinazoelezea maumbile ya Mungu. Hebu tuzitame kwa ufupi moja baada ya nyingine.

ALFA NA OMEGA:

Tafsiri ya Alfa na Omega sio mwanzo na mwisho, kama inavyofahamika na wengi…ingekuwa ndiyo tafsiri yake hiyo, visingetenganishwa vitu vitatu hapo juu…Sasa Afla ni herufi ya kwanza kwenye alfabeti za Kingiriki..yenye alama hii (α) Na Omega ni herufi ya mwisho ya kwenye alfabeti za lugha ya kigiriki yenye alama hii (ω)…Kwenye alfabeti zetu sisi herufi ya kwanza ni (A) na ya mwisho ni (Z)….kwa kigiriki ya kwanza ndiyo hiyo alfa na ya mwisho ni omega.

Kwahiyo katika mstari huo aliposema yeye ni alfa na omega, alikuwa anajitambulisha uungu wake katika umbo la NENO. (Kumbuka hapo mwanzo kulikuwako Neno….naye Neno alikuwako kwa Mungu, naye Neno alikuwa ni Mungu,…Vitu vyote vilifanyika kwa huyo wala pasipo yeye hakuna chochote kilichofanyika Yohana 1:1).

Kwahiyo akiwa katika Neno, yeye ndiye Neno la Kwanza na ndiye Neno la Mwisho, kwahiyo ili lijitambulishe lazima litumie Herufi kujitambulisha, (herufi ya kwanza na ya mwisho, alfa na Omega)… Kwanini hakutumia herufi ya A na Z?..ni kwasababu lugha zinazotumia alfabeti hizi kama vile kiingereza zilikuwa hazijazaliwa bado, na hata kama zingekuwa zimeshazaliwa bado zilikuwa ni lugha changa, kwani wakati Yohana anapewa haya maono lugha iliyokuwa kuu na uliyozungumzwa sehemu kubwa ya dunia ilikuwa ni kigiriki, hata lugha iliyotumika kuandika vitabu vingi vya agano jipya ni lugha hii, ndio maana yakatumika maneno ya kigiriki.

Yeye ni MWANZO NA MWISHO:

Sifa ya pili, Hapa Mungu anajitambulisha kwa umbo la MUDA….

Kama alivyosema mahali Fulani yeye ni UPENDO, na sio yeye ana upendo…kadhalika hapa, anajitambulisha kuwa yeye ni MWANZO  na sio yeye ana mwanzo!..halikadhalika yeye ndiye MWISHO, na sio yeye mwenye mwisho…yeye hana mwanzo na wala hana mwisho, kwasababu yeye ndio mwanzo wenyewe na ndio mwisho wenyewe.

Ili uelewe vizuri hebu tafakari jambo hili: umewahi kuchunguza mwanzo wa magharibi ni upi? Au mwisho wa magharibi ni upi?…au mwanzo wa mashariki ni upi na mwisho wake ni upi?..utakuja kugundua kuwa mashariki haina mwanzo wake wala mwisho wake, vivyo hivyo na magharibi haina mwanzo wala haina mwisho, kwasababu mahali ulipo tayari panaweza kuwa ni mashariki ya mbali sana kwa sehemu nyingine halikadhalika panaweza kuwa ni magharibi ya mbali sana kutoka sehemu nyingine…kwahiyo hapo ulipo tayari ni mwanzo na mwisho wa magharibi na mashariki. Kuna mstari wanaouita kitaalamu IDL huo ndio wanasema umetenganisha mashariki na magharibi lakini kiuhalisia hakuna mstari pale…Wamebuni tu, ili kuwarahisishia kutimiza matakwa yao ya kijeografia, lakini hakuna mwanzo wa mashariki wala magharibi, ingawa kuna mashariki na magharibi..

Na ndio Mungu yupo hivyo hivyo, ingawa kuna kitu kinaitwa MWANZO na Mwisho, lakini yeye hana mwanzo, wala hana mwisho……kwasababu yeye pale alipo ndio mwanzo na ndio mwisho….Na kama vile tunavyozidi kuelekea sana mwisho wa mashariki ndivyo tunavyojikuta tunatokea mwanzo wa mashariki hiyo hiyo…kadhalika na Mungu…tunapodhani tunamjua sana na hivyo tumefika karibia na mwisho wa kumjua yeye…kumbe ndio tupo mwanzo wa kumjua yeye….Na pale tunapodhani yupo mbali sana na sisi kumbe ndio yupo karibu sana na sisi, na pale tudhaniapo kuwa tumemkaribia sana, kumbe bado sana tumfikie..Kwasababu yeye ndio mwanzo na ndio mwisho, akili zake hazichunguziki, wala hakuna mtu anayeweza kumwelezea asilimia mia na kusema sasa nimemjua Mungu.

Isaya 40:28 “Je! Wewe hukujua? Hukusikia? Yeye Mungu wa milele, Bwana, Muumba miisho ya dunia, hazimii, wala hachoki; akili zake hazichunguziki.”

Yeye ni WA KWANZA NA WA MWISHO:

Sifa ya tatu na ya mwisho, Hapa Mungu anajifunua na kujitambulisha katika umbo la mtu…Lile Neno lililojitambulisha kwa herufi alfa na Omega, sasa linavaa mwili na kujitambulisha kama Mtu, na kusema Yeye ni wa Kwanza na wa Mwisho.

Hapa anaelezea Uungu wake kabla ya vitu vyote..Yeye alikuwepo kabla ya kiumbe chochote kile…kabla ya Malaika na kitu kingine chochote…ndiye wa Kwanza, akaitoa sehemu ya roho yake akatuumba sisi wanadamu na malaika…Na hivyo sisi wote tumetoka kwake…Na mwisho wa siku tutarudi kwake..kwasababu yote yametoka kwake..

Mungu wetu hakuna linalomshinda, wala hakuna asilolijua, utasemaje leo hakujui, wala hajui unayopitia?..huyu mwanzo na mwisho utasemaje kakusahau?..hajakusahau alisema “hata nywele za vichwa vyetu zimehesabiwa zote (Luka 12:7)”….kama anajishughulisha na mambo madogo sana ya nywele zetu atashindwaje kujishughulisha na mambo makubwa ya Maisha yetu, Hivyo kuna baraka nyingi sana katika kumwamini huyu Mungu.

Lakini pia huyu Mungu ni alfa na Omega, maneno yake ndio mwanzo na mwisho, akisema Neno lake ni lazima litimie, na halirekebishwi wala halina marekebisho…limehakikiwa na limejitosheleza, akisema roho itendayo dhambi itakufa…ni kweli itakufa, akisema mtu asipozaliwa mara ya pili hawezi kuurithi ufalme wa mbinguni…maneno yake hayo ni alfa na Omega..yatatimia kama yalivyo, akisema atakuja ni kweli atakuja..

Hivyo mpaka sasa bado anawaalika watu karamuni, je! Wewe ni mmoja wao wa walioalikwa?..kama bado unasubiri nini, usigeuke leo na kutubu? Siku ile utakuwa mgeni wa nani utakapojikuta upo kuzimu?..kumbuka hakuna nafasi ya pili kwa mtu yeyote atakayekufa katika dhambi leo,..wengi wanajifariji kuwa mbele ya kiti cha hukumu watakuwa na hoja za kujitetea, nataka nikuambie siku ile kutakuwa hakuna kujitetea…Kwasababu hakuna yeyote awezaye kumtega wala kumkamata Mungu kwa maneno.

Bwana akubariki sana.

Pia kwa Mawasiliano, Ushauri au Ratiba za Ibada Wasiliana nasi kwa +225693036618/ +225789001312

Pia unaweza ukapata mafundisho haya Kwa njia ya Whatsapp yako, jiunge na channel yetu Kwa kubofya hapa >> WHATSAPP


Mada Zinazoendana:

KWANINI YESU KRISTO ALIKUJA DUNIANI?

BADO KITAMBO KIDOGO HAMNIONI

UNAMCHUKULIA YESU KWAKO KAMA NANI?


Rudi Nyumbani

Print this post

UTAJI ULIOKUWA JUU YA USO WA MUSA.

Kutoka 34:29 “Hata ikawa, Musa aliposhuka katika mlima Sinai, na zile mbao mbili za ushuhuda zilikuwa mkononi mwa Musa, hapo aliposhuka katika mlima, Musa hakujua ya kuwa ngozi ya uso wake iling’aa kwa sababu amesema naye.

30 Basi Haruni na wana wote wa Israeli walipomwona Musa, tazama, ngozi ya uso wake iling’aa; nao wakaogopa kumkaribia.

31 Musa akawaita; Haruni na wakuu wote wa kusanyiko wakarudi kwake; Musa akasema nao.

32 Baadaye wana wa Israeli wote wakakaribia; akawausia maneno yote ambayo Bwana amemwambia katika mlima Sinai.

33 Na Musa alipokuwa amekwisha kusema nao, akatia utaji juu ya uso wake.

34 Lakini desturi ya Musa ilikuwa alipoingia mbele za Bwana kusema naye, kuuvua huo utaji mpaka atoke; akatoka akawaambia wana wa Israeli maneno yote aliyoambiwa.

35 Wana wa Israeli wakauona uso wa Musa ya kuwa ngozi ya uso wake Musa iling’aa; naye Musa akautia utaji juu ya uso wake tena, hata alipoingia kusema naye.”.

Itakuwa hata wewe ulishawahi kugundua kitu hichi mfano ukikaa karibu na mtu ambaye amejipulizia marashi makali kwa muda mrefu, halafu ukaondoka utagundua kuwa vimelea vya yale marashi kwa sehemu Fulani vimebaki kwenye mwili wako,..Na ndivyo ilivyokuwa kuwa kwa Musa, baada ya kukaa uweponi mwa Mungu kwa muda wa siku nyingi, siku zaidi ya 80, ukijumlisha na zile 40 za Kwanza, alizokwenda kupewa amri na hukumu na zile mbao 2 za mawe, kwa wakati huo wote alipokuwa uweponi mwa Mungu kumbe kidogo kidogo utukufu wa Mungu ulikuwa unajiambukiza ndani yake pasipo yeye kujijua..Hadi siku aliposhuka chini na kuona watu wanamwogopa ndipo alipogundua kuwa Uso wake uling’aa sana kwa kule kumtazama Mungu.

Japo biblia haituambii ulikuwa unang’aa kwa namna gani hadi watu kumwogopa, lakini tunajua uling’aa kwa utukufu wa Mungu, pengine ulikuwa unameta meta kama almasi, mpaka watu wakaona huyu anaweza akawa asiwe mtu wa kawaida, pengine tukimgusa tunaweza tukafa..Ndipo Musa alipoona hivyo, akachukua utaji akaufunika uso wake, kupunguza makali ya utukufu ule, ili aweze kusimama mbele ya watu na kungumza nao.

Lakini japo uso wake uling’aa sana kwa namna ile, bado utukufu ule ulikuwa sio wa kudumu, kwasababu ulikuwa na wa kuhakisi tu, na sio kitu kilichotoka ndani yake, hivyo alipoondoka katika uwepo wa Mungu, kidogo kidogo ulikuwa unapungua hadi mwishowe ukatoweka kabisa…Japo biblia haituambii ni kwa kipindi gani utukufu huo ulidumu kwenye uso wake, pengine ulichukua siku, au wiki, au mwezi, au miezi, hatujui, lakini tunachojua ni kuwa ulikuwa ni utukufu usiodumu…Ulihitaji kuu-chaji, Na ndio maana ukisoma hapo juu utaona kila wakati Musa alipotoka kuzungumza na Mungu aliuvaa utaji ule, kwasababu utukufu wa Mungu ulijiakisi kwenye uso wake tena kwa wakati huo.

Hivyo ule utaji uliwazuia wana wa Israeli kuona hatma ya ule utukufu jinsi unavyokwisha, kwasababu Musa alikuwa anavaa utaji muda wote, Na ndio maana mtume Paulo, aliandika katika 2Wakorintho 3:13-16, kuwa hata leo hii wana wa Israeli utaji huo upo mbele yao, kwamba hawawezi kuona jinsi utukufu wake Torati ya Musa usivyokuwa wa kudumu..

“13 nasi si kama Musa alivyotia utaji juu ya uso wake, ili kwamba Waisraeli wasitazame sana mwisho wa ile iliyokuwa ikibatilika;

14 ila fikira zao zilitiwa uzito. Kwa maana hata leo hivi, wakati lisomwapo Agano la Kale, utaji uo huo wakaa; yaani, haikufunuliwa kwamba huondolewa katika Kristo; 

15 ila hata leo, torati ya Musa isomwapo, utaji huikalia mioyo yao.

16 Lakini wakati wo wote watakapomgeukia Bwana, ule utaji huondolewa.”

Swali linakuja je! mwanadamu afanye nini ili awe na utukufu usio batilika kutoka kwa Mungu? Apate Utukufu unaodumu wakati wote?.

Jibu lipo pale pale juu, tunapaswa tusiuakisi utukufu wa Mungu, bali tugeuzwe tuwe kama yeye. Hiyo ndio dawa pekee. Kwa kuelewa zaidi angalia mfano wa mwezi na nyota, utagundua kuwa nyota siku zote zinaangaza tu, huwezi kuta zinaonekana nusu, lakini mwezi, leo utauona unaonekana wote, kesho nusu, kesho kutwa theluthi, ni kwasababu gani?, ni kwasababu wenyewe unategemea mwanga wa jua kuangaza, unalihakisi jua, lakini nyota hazihakishi chochote kutoka katika jua kwani watafiti wanasema Nyota ni ma-jua mengine, isipokuwa tu yapo mbali na dunia na ndio maana kuangaza kwa nyota hakubadiliki badiliki.

Vivyo hivyo, ili sisi tuangaze utukufu kamili wa Mungu, tunapaswa tuguezwe tuwe miungu duniani, na anayeweza kufanya hii kazi si mwingine zaidi ya YESU KRISTO mwenyewe.

Pale tunapoiamini injili kweli kweli kwa kudhamiria kumwishia Mungu, na kubatizwa katika ubatizo sahihi, tunapotubu dhambi zetu, kuanzia hapo Kristo anachofanya ni kutubadilisha asili zetu, na kuwa kama Mungu,..kuanzia huo wakati utukufu wa Mungu unakuwa unamulika ndani yetu milele NON-STOP..Kazi yako itakuwa ni kujiweka mbele zake katika hali ya utakatifu na usafi zaidi, na kulitii Neno lake, ili uzidi kuangaza kwa utukufu mwingi zaidi, hapo ndipo unapokuwa kutoka utukufu hadi utukufu, kwasababu kumbuka hata nyota zinatofautiana utukufu(1Wakorintho 15:41)..Isipokuwa tu utukufu wa zote hauwezi kuisha kabisa kama mwezi, kwasababu tayari ndani yao kuna Nuru ya jua, lakini ni wajibu wa kila mwaminio, atoke utukufu hadi utukufu.

2 Wakorintho 3:7 “Basi, ikiwa huduma ya mauti, iliyoandikwa na kuchorwa katika mawe, ilikuja katika utukufu, hata Waisraeli hawakuweza kuukazia macho uso wa Musa, kwa sababu ya utukufu wa uso wake; nao ni utukufu uliokuwa ukibatilika;

8 je! Huduma ya roho haitazidi kuwa katika utukufu?

9 Kwa maana ikiwa huduma ya adhabu ina utukufu, siuze huduma ya haki ina utukufu unaozidi.

10 Maana hata ile iliyotukuzwa haikuwa na utukufu hivi, kwa sababu ya utukufu uzidio sana.

11 Kwa maana, ikiwa ile inayobatilika ilikuwa na utukufu, zaidi sana ile ikaayo ina utukufu.

12 Basi, kwa kuwa mna taraja la namna hii, twatumia ujasiri mwingi;

13 nasi si kama Musa alivyotia utaji juu ya uso wake, ili kwamba Waisraeli wasitazame sana mwisho wa ile iliyokuwa ikibatilika;

14 ila fikira zao zilitiwa uzito. Kwa maana hata leo hivi, wakati lisomwapo Agano la Kale, utaji uo huo wakaa; yaani, haikufunuliwa kwamba huondolewa katika Kristo; 

15 ila hata leo, torati ya Musa isomwapo, utaji huikalia mioyo yao.

16 Lakini wakati wo wote watakapomgeukia Bwana, ule utaji huondolewa.

17 Basi <Bwana> ndiye Roho; walakini alipo Roho wa Bwana, hapo ndipo penye uhuru.

18 Lakini sisi sote, kwa uso usiotiwa utaji, tukiurudisha utukufu wa Bwana, kama vile katika kioo, TUNABADILISHWA TUFANANE NA MFANO UO HUO, TOKA UTUKUFU HATA UTUKUFU, kama vile kwa utukufu utokao kwa Bwana, aliye Roho”.

Unaona ni faida gani, mtu aliyonayo aliyedhamiria kweli kumwamini Kristo, na sio kigeugeu,? Mtu wa namna hii hata katika ulimwengu wa roho mashetani na mapepo wanachokiona ni miale ya moto tu inapita, uchawi utampatae mtu kama huyo? Au LAANA?. Na ndio maana Shetani anachofanya sasa katika hichi kipindi cha mwisho ni kupofusha tu fikra za watu wapuuzie mambo haya ya msingi:

2Wakorintho 4:3 “Lakini ikiwa injili yetu imesitirika, imesitirika kwa hao wanaopotea;

4 ambao ndani yao mungu wa dunia hii amepofusha fikira zao wasioamini, ISIWAZUKIE NURU YA INJILI YA UTUKUFU WAKE KRISTO ALIYE SURA YAKE MUNGU.”

Mfikirie Kristo kwa jicho lingine, Yule huwa akimbadilisha mtu, anambadilisha kweli kweli, hasemi uongo kama sisi wanadamu tulivyo, Hakuja kufanya kazi ya kubahatisha duniani, kazi yake ni thabiti kabisa.

Bwana akubariki sana. 

Kwa Maombezi, Ushauri au Ratiba za Ibada Wasiliana nasi kwa namba

+225693036618/ +255789001312

Pia unaweza ukapata mafundisho haya Kwa njia ya Whatsapp yako, jiunge na channel yetu Kwa kubofya hapa >> WHATSAPP


Mada Zinazoendana:

DHAMBI ZINAZOTANGULIA NA ZINAZOFUATA.

MADHAIFU

WATU WASIOJIZUIA.

UNAFANYA NINI HAPO?


Rudi Nyumbani

Print this post

VITABU VYA BIBLIA: Sehemu ya 5

Karibu katika mwendelezo wa vitabu vya Biblia, leo tutaendele na vitabu 4 vya mbele, yaani Wafalme wa kwanza (1Wafalme), na Wafalme wa Pili (2Wafalme), Mambo ya nyakati wa kwanza (1Nyakati) na Mambo ya nyakati wa pili(2 Nyakati).. Tumekwisha pitia vitabu 10 vya kwanza, hivyo ni vizuri kama hujapitia maelezo ya vitabu vilivyopita, ukavipitia kwanza ili tuende pamoja katika hivi vitabu vinavyofuata.

Kitabu cha Wafalme wa kwanza na Wafalme wa Pili, kilikuwa ni kitabu kimoja, isipokuwa kiligawanywa katika sehemu mbili…Na mwandishi wa kitabu hichi alikuwa ni Nabii Yeremia. Ingawa Nabii Yeremia alizaliwa mwishoni kabisa mwa enzi za Wafalme lakini aliweza kukusanya rekodi zote za habari za Wafalme, kwani habari za kila mfalme na matendo yake zilikuwa zinarekodiwa na kuhifadhiwa kwenye vitabu maalumu vinavyojulikana kama vitabu vya Tarehe.

Lakini kwa ufupi Kitabu hivi viwili vya wafalme kama jina lake lilivyo, vinazungumzia Utawala wa wafalme wa Israeli, Na vitabu viwili vinavyofuata vya (1 Nyakati na 2 Nyakati) Ni marudio ya habari hizo hizo za Wafalme isipokuwa yana habari chache chache sana ambazo hazikurekodiwa katika kitabu cha wafalme…Ni sawa na injili iliyoandikwa na Mathayo na Luka ni vitabu viwili vilivyoandikwa na waandishi wawili tofauti lakini vyote vinazungumzia habari moja..ndivyo ilivyo kitabu cha Wafalme na Mambo ya nyakati, vyote vinaelezea habari moja za Wafalme wa Israeli…isipokuwa hichi cha mambo ya nyakati kimeanzia nyuma kidogo, kwa mfalme Daudi. Na mwandishi wa kitabu cha Mambo ya Nyakati alikuwa ni EZRA..ambaye ndiye aliyekiandika kitabu cha Ezra pia..Huyu alikuwa ni mwandishi..ambaye habari zake tutakuja kuziona tutakapofika katika kitabu cha Ezra..

Sasa tukirudi katika habari za Wafalme..kumbuka haukuwa mpango wa Mungu, Israeli wawe na Mfalme juu yao tangu mwanzo, lakini kwasababu ndio ilikuwa nia yao kukataa uongozi wa Mungu, usiohusisha mwanadamu, Mungu akawapa haja ya mioyo yao, lakini pamoja na hayo hakuwaacha…tofauti na sisi wanadamu, mtu asipofanya tunavyotaka tunamtupa moja kwa moja, hatutaki hata kumsikia tena, lakini kwa Mungu haipo hivyo, hakuwatupa Israeli watu wake moja kwa moja ingawa walimuasi…Hivyo Mungu akatengeneza njia ya kuwaokoa kwa kupitia hao hao wafalme waliowataka…

Kwahiyo kitabu cha Wafalme wa Kwanza, kinaanza na Mfalme Sulemani, ambaye alikuwa ni mfalme wa tatu wa Israeli akitanguliwa na Sauli na Daudi ambao habari zao utazipata katika vitabu vya Samweli. Sulemani alikuwa ni mwana wa Daudi, na mama yake alikuwa ni yule mke wa Uria, ambaye Daudi aliyemtamani..Hivyo baadaye Mungu alikuja kumfanyia wema mwanamke yule na kumfanya mwanawe kuwa mfalme juu ya Israeli, Sulemani alitawala miaka 40 katika Israeli, alianza vizuri lakini hakumaliza vizuri, kwani pamoja na Hekima yote na ufahari wote aliopewa na Mungu alikuja kukengeuka dakika za mwisho, na kwenda kuoa wanawake wa kigeni, ambao Mungu alimkataza asioe, (Nehemia 13:25-26 )na hao wanawake wakamgeuza moyo akaenda kutengenezea maashera hiyo miungu migeni, ambayo ni machafuko makubwa sana mbele za Mungu, Ingawa alikuja kutubu dakika za mwisho, na Bwana alimsamehe lakini tayari alikuwa ameshaisababishia Israeli madhara makubwa sana..

Sasa kabla ya kwenda kwenye madhara aliyoisababishia Israeli, tutazame jambo moja jema na kuu alilolifanya.; Tunaona baada ya kufa baba yake, yeye ndiye aliyekuwa na dhamana ya kumtengenezea Mungu nyumba, biblia inasema Mungu hakai kwenye nyumba zilizotengenezwa na mikono, lakini pamoja na Daudi kulifahamu hilo bado alilazimisha kumjengea Mungu nyumba hivyo hivyo, na Mungu akaliona hilo akapendezwa naye na kumbariki, na kuuchagua mji wake na kabila lake kuwa makao makuu ya kuweka jina lake, japo Mungu alimzuia Daudi asimjengee kwasababu alimwaga damu nyingi, hivyo mwanawe ambaye ni Sulemani ndiye atakayejenga HEKALU kwa niaba yake. Na wakati ulipowadia Sulemani alimjengea Mungu hekalu, alitumia akili nyingi, na hekima nyingi kuijenga ile nyumba…

Alikwenda kutafuta miti maalum na ya thamani kutoka nchi za mbali, na vito maalumu kutoka kila kona ya dunia, na kuileta Israeli, Zaidi alikwenda kutafuta watu wenye akili nyingi, kutoka mataifa mengine kusaidia kuongeza ujuzi katika ujenzi, kwahiyo Hekalu lilijengwa kwa gharama kubwa na kwa ujuzi wa hali ya juu, kulikuwa hakuna mfano wake duniani kote. Na lilitengenezwa Yerusalemu, katika mji wa kabila la Yuda, hakukusikika kelele yoyote wakati wa ujenzi, hivyo ilipunguza hata kasi ya maadui, kuvamia kwasababu hakuna mtu aliyekuwa anaelewa kitu kinachoendelea ndani..wengi walidhani kazi imesimama tu!..lakini ilikuwa inaendelea ndani kwa ndani…ghafla wanakuja kushangaa nyumba hii hapa imekamilika!..Sasa inawekwa wakfu kwa Mungu.

Mungu akalibariki Taifa la Israeli na Mfalme, kwa jambo hilo, na kukawa na amani kwa Zaidi ya miaka 40, lakini Sulemani alipokuwa mzee akakengeuka, na hivyo Mungu hakupendezwa naye tena, hakumwua lakini alimnyang’anya sehemu ya Ufalme wake, kwani hapo kwanza alikuwa anatawala makabila yote 12, kama Sauli na Daudi walivyokuwa wanatawala, lakini matokeo yake akapokonywa 10 akabakiwa na mawili tu, yaani kabila la Benyamini pamoja na kabila lake mwenyewe Yuda…lakini hakunyakang’anywa kwenye utawala wake bali wa mwanae.

1 Wafalme 11:1 “Mfalme Sulemani akawapenda wanawake wengi wageni, pamoja na binti yake Farao, wanawake wa Wamoabi, na wa Waamoni, na wa Waedomi, na wa Wasidoni, na wa Wahiti,

2 na wa mataifa Bwana aliyowaambia wana wa Israeli, Msiingie kwao, wala wasiingie kwenu; kwa kuwa hakika wataigeuza mioyo yenu kuifuata miungu yao. Sulemani akaambatana nao kwa kuwapenda.

3 Akawa na wake mia saba binti za kifalme, na masuria mia tatu; nao wakeze wakamgeuza moyo.

4 Maana ikawa, Sulemani alipokuwa mzee, wake zake wakamgeuza moyo wake, afuate miungu mingine, wala moyo wake haukuwa mkamilifu kwa Bwana, Mungu wake, kama moyo wa Daudi baba yake.

5 Kwa kuwa Sulemani akamfuata Ashtorethi, mungu mke wa Wasidoni na Milkomu, chukizo la Waamoni. 6 Sulemani akafanya yaliyo mabaya machoni pa Bwana, wala hakumfuata Bwana kwa utimilifu, kama Daudi baba yake.

7 Sulemani akamjengea Kemoshi, chukizo la Wamoabi, mahali pa juu, katika mlima uliokabili Yerusalemu, na Moleki, chukizo la wana wa Amoni.

8 Na kadhalika ndivyo alivyowafanyia wake zake wa nchi za kigeni, waliofukiza uvumba, wakawatolea miungu yao dhabihu.

9 Basi Bwana akamghadhibikia Sulemani kwa sababu moyo wake umegeuka, naye amemwacha Bwana, Mungu wa Israeli, aliyemtokea mara mbili,

10 akamwamuru katika habari ya jambo lilo hilo asifuate miungu mingine; lakini yeye hakuyashika aliyoyaamuru Bwana.

11 Kwa hiyo Bwana akamwambia Sulemani, Kwa kuwa umefanya hayo, wala hukuyashika maagano yangu, na sheria zangu nilizokuamuru, hakika nitaurarua ufalme usiwe wako, nami nitampa mtumishi wako.

12 Walakini katika siku zako sitafanya haya, kwa ajili ya Daudi baba yako; nitaurarua utoke katika mkono wa mwana wako.

13 Lakini sitauondoa ufalme wote pia; nitampa mwana wako kabila moja, kwa ajili ya Daudi mtumishi wangu, na kwa ajili ya Yerusalemu niliouchagua”

Hivyo hayo yote yalitokea wakati wa utawala wa mtoto wake Rehoboamu, na kuanzia huo wakati Israeli ikagawanyika sehemu mbili, kaskazini na kusini, upande wa kusini ndio huo uliokuwa na makabila mawaili (yaani Yuda na Benyamini) na upande wa kaskazini (makabila 10 yaliyosalia). Hivyo kaskazini wakawa na mfalme wao na Kusini wakawa na Mfalme wao…

Kaskazini PAKAITWA ISRAELI na kusini PAKAITWA YUDA. Hivyo Israeli ambayo hapo kwanza ilikuwa ni taifa moja ikagawanyika na kuwa mataifa mawili ndani ya Taifa moja…kutokana na dhambi ya Sulemani.

Hayo ndio madhara ya dhambi aliyoyaleta Sulemani, na ndio madhara ya dhambi, unaweza ukasema nikitenda dhambi fulani itaniathiri mimi peke yangu, haitawahusu wengine, nataka nikuambie ndugu, ukiwa mwamini ukifanya dhambi yoyote ya makusudi haitakuathiri wewe peke yako bali itaathiri na wengine na Zaidi ya yote itaathiri kazi ya Mungu, kwasababu jina la Mungu litatukanwa kwa ajili yako.

Baada tu ya Israeli kugawanyika katika sehemu hizo mbili, hapo ndio ikawa sehemu nyingine ya chanzo cha machafuko, watu waliokuwa wanakaa kaskazini (yaani yale makabila 10) yakaacha kabisa kumcha Mungu wa Israeli kama hapo kwanza kwasababu mfalme wao wa kwanza anayeitwa Yeroboamu aliwatengenezea sanamu ya ndama, waiabudu kama Mungu wao badala ya Mungu wa Israeli..hivyo ikawa ni machafuko makubwa zaidi, wakawa hawana tofauti na watu wa Mataifa.

Na yale makabila mawili yaliyosalia ambayo yalikuwa kusini angalau kidogo watu waliokuwa wanakaa kule walikuwa wanamwogopa Mungu ingawa si sana, na walikuwa wanamcha Mungu kwasababu tu Hekalu la Mungu lilikuwa huko nchini kwao Yuda, hiyo kidogo ikawafanya wawe na hofu ya Mungu. Lakini na wao pia wakaja kukengeuka baadaye…Hivyo mataifa haya mawili ndani Taifa moja yakawa na kila moja na mfalme wake, na itikadi zake, ingawa walikuwa wanatambuana kama ndugu, na hakukuwa na Mfalme mmoja kwa mataifa yote mawili, hapana kila moja lilikuwa na mfalme wake kuanzia huo wakati na kuendelea.

Walipita Wafalme karibia 20 katika Israeli ( yaani upande wa kaskazini)…lakini wote walifanya machukizo mbele za Mungu, kila aliyekuja alikuwa anafanya mabaya kuliko aliyemtangulia…Na miongoni mwa wafalme waliofanya mabaya sana ni Mfalme Ahabu ambaye alikuwa na mke wake aliyemtoa nchi za mataifa, ambaye alikuwa ni mchawi, aliyeitwa Yezebeli, hawa waliichafua Israelli kwa kiwango cha juu sana…Mpaka ikafika kipindi Bwana akaileta huduma ya Eliya duniani, na lengo la huduma ya Eliya ilikuwa ni KUWAREJESHA WANA WA ISRAELI WAMRUDIE MUNGU WAO. Mungu alitumia ishara nyingi katika huduma ya Eliya ili kuwarejesha wamgeukie yeye…(kwa maelezo marefu juu ya huduma hii ya Eliya tutumie ujumbe inbox tukutumie )…wachache wakawa wanatii na kugeuka lakini wengi wakawa hawatii..

Na katika Yuda pia walikuwa wanatumiwa manabii wengi, lakini angalau Yuda kidogo watu walikuwa si wagumu kama Israeli..Kwani kulikuwa kuna Wafalme katika Yuda ambao walikuwa wanamtii Mungu na kumheshimu kama alivyofanya Daudi, mfano wa wafalme hao alikuwepo mfalme Hezekia, na Mfalme Yosia hawa walikwenda katika njia za Mungu katika ukamilifu wote, hivyo katika vipindi vya utawala wao Mungu aliwabariki na kuwaepushia madhara,… Manabii wote tunaowasoma katika Biblia, kuanzia Eliya, Elisha, Habakuki, Isaya, Hosea, Nahumu, Yona, Amosi, Yeremia, Obadia, Habakuki, Mika n.k wote hawa walitokea kipindi hichi cha Wafalme kasoro nabii Danieli, Hegai, zekaria pamoja na Malaki hawa walitokea baada ya Isreali kutawanyishwa…

lakini hao wengine Walikuwa wanatumwa kuwaonya wana wa Israeli na wana wa Yuda pamoja na wafalme wao wamgeukie Mungu…Unapopitia kitabu hichi ili upate picha vizuri, ni vyema ukapitia pia vitabu vya manabii, uone Bwana alivyokuwa anawaonya Israeli kwa nguvu, na jinsi gani alivyokuwa anawatabiria kuwa watakwenda utumwani Babeli wasipotubu..Kwa muda wako soma kitabu cha Yeremia, Hosea, Nahumu, Isaya utayaona mambo hayo kwa urefu, …

Kwa miaka mingi Zaidi ya 400, walikuwa wanatumiwa manabii wa kuwarejesha lakini ni wachache tu ndio waliokuwa wanatii na kugeuka, hivyo uvumilivu wa Mungu ukafika kikomo, kukawa hakuna tena msamaha, Mungu akaamua kuwatoa Waisraeli wote kutoka katika nchi yao waliyopewa na Mungu, waliokuwa wanakaa upande wa kaskazini, yaani Israeli (yale makabila 10)..yalichukuliwa utumwani kwenda nchi inayoitwa ASHURU, na wale waliokuwa wanakaa kusini (yaani Yuda) baada ya miaka 125 mbeleni nao pia walichukuliwa na kupelekwa utumwani BABELI,..wao hawakuchukuliwa kipindi kimoja na Israeli kwasababu angalau kwao kulikuwa na hofu ya Mungu kuliko Israeli, lakini baadaye nao pia wakakengeuka kama Israeli na kuchukuliwa mpaka Babeli…Nchi ya Ahadi ikabaki nyeupe!! Wakaletwa makafiri wakaishi huko kwa niaba yao, nchi ya Israeli ikakaliwa na makafiri. Yuda Wakapelekwa utumwani miaka 70..

2 Nyakati 36:14 “Na zaidi ya hayo wakuu wote wa makuhani, na watu, wakakosa mno sawasawa na machukizo yote ya mataifa; wakainajisi nyumba ya Bwana aliyoitakasa katika Yerusalemu.

15 Naye Bwana, Mungu wa baba zao, akatuma kwao kwa mikono ya wajumbe wake, akiondoka mapema, na kutuma; kwa sababu ALIWAHURUMIA WATU WAKE, NA MAKAO YAKE;

16 lakini waliwadhihaki wajumbe wa Mungu, na kuyadharau maneno yake, na kuwacheka manabii wake, HATA ILIPOZIDI GHADHABU YA BWANA JUU YA WATU WAKE, HATA KUSIWE NA KUPONYA.

17 Kwa hiyo akaleta juu yao mfalme wa Wakaldayo, aliyewaua vijana wao kwa upanga nyumbani mwa patakatifu pao, asiwahurumie kijana wala mwanamwali, mzee wala mkongwe; akawatia wote mkononi mwake.

18 Na vyombo vyote vya nyumba ya Mungu, vikubwa kwa vidogo, na hazina za nyumba ya Bwana, na hazina za mfalme, na za wakuu wake; vyote pia akavileta Babeli.

19 Wakaiteketeza nyumba ya Mungu, wakaubomoa ukuta wa Yerusalemu, wakayateketeza kwa moto majumba yake yote, wakaviharibu vyombo vyake vyote vya thamani.

20 Na wale waliookoka na upanga akawachukua mpaka Babeli; wakamtumikia yeye na wanawe hata kulipoingia milki ya Uajemi;

21 ili kulitimiza neno la Bwana kwa kinywa cha Yeremia, hata nchi itakapofurahia sabato zake; kwa maana siku zote ilipokaa ukiwa ilishika sabato, kutimiza miaka sabini.”

Mstari wa 16, unasema “lakini waliwadhihaki wajumbe wa Mungu, na kuyadharau maneno yake, na kuwacheka manabii wake, HATA ILIPOZIDI GHADHABU YA BWANA JUU YA WATU WAKE, HATA KUSIWE NA KUPONYA”.

Ndugu katika vitabu hivi tunajifunza kuwa..kuna wakati unafika ghadhabu ya Mungu, itajaa hata kusiwe na kuponya, wewe unayesema Mungu anakawia, wewe unayedharau na kuidhihaki na kuicheka injili leo, na kuwacheka na kuwafanyia mizaha watu wa Mungu, siku inakuja ambapo utalia na kutakuwa hakuna msaada, siku ya ghadhabu ya Mungu inakuja! Usidanganywe na watu wanaosema kuwa Mungu hawezi kuangamiza dunia, au hakuna mwisho wa dunia, ndugu watu wa kipindi cha Nuhu ndio walikuwa wanasema hivyo hivyo…lakini ghafla tu walishangaa siku moja mbingu zimefunga, zimekuwa nyuesi……Jiepushe na ghadhabu ya Mungu, Uvumilivu wa Mungu ni kukufanya wewe utubu, umgeukie Mungu, tubia uasherati wako, rushwa zako, utukanaji wako, usengenyaji wako, na kutokusamehe kwako…Wema wa Mungu unakuvuta leo kwasababu hataki upotee soma tena mstari wa 15 unasema…

“15 Naye Bwana, Mungu wa baba zao, akatuma kwao kwa mikono ya wajumbe wake, akiondoka mapema, na kutuma; kwa sababu ALIWAHURUMIA WATU WAKE, NA MAKAO YAKE; ”

Ni mara ngapi asubuhi na mapema umekutana na mahubiri, kwenye redio, kwenye Tv, mitandaoni, mitaani au hata sehemu zako za kazi?..Usipuuze unaposikia injili unayopewa bure pasipo hata kulipia hata sh. Moja..siku ile utakosa cha kujitetea..

Kuna wakati mlango wa rehema utafungwa, ambapo utatamani kutubu utashindwa: Wana wa Israeli walilia na kuomboleza, siku ile wanapochukuliwa mateka, lakini Mungu hakusikia chochote. Ndivyo itakavyokuwa kwa wale wanaochezea neema sasa.

Luka 13:24 “Jitahidini kuingia katika mlango ulio mwembamba, kwa maana nawaambia ya kwamba wengi watataka kuingia, wasiweze.

25 Wakati mwenye nyumba atakaposimama na kuufunga mlango, nanyi mkaanza kusimama nje na kuubisha mlango, mkisema, Ee Bwana, tufungulie; yeye atajibu na kuwaambia, Siwajui mtokako;

26 ndipo mtakapoanza kusema, Tulikula na kunywa mbele yako, nawe ulifundisha katika njia zetu.

27 Naye atasema, Nawaambia, Siwajui mtokako; ondokeni kwangu ninyi nyote mlio wafanyaji wa udhalimu.

28 Ndipo kutakapokuwa na kilio na kusaga meno,

mtakapomwona Ibrahimu na Isaka na Yakobo na manabii wote katika ufalme wa Mungu, nanyi wenyewe mmetupwa nje.”

Hivyo unachopaswa kufanya ni kutubu hapo ulipo kwa kudhamiria kuacha dhambi zako, na kwenda kutafuta ubatizo sahihi kwa ajili ya ondoleo la dhambi zako, ubatizo sahihi ni wa kuzamishwa mwili wote na kwa jina la Yesu Kristo kulingana na Matendo 2:38, na Bwana mwenyewe atakupa kipawa cha Roho wake Mtakatifu.

Hakikisha unakisoma vitabu hivi mwenyewe, usiache kipengele hata kimoja, kwasababu ni habari zinazoeleweka na zimewekwa katika mfumo mrahisi wa kueleweka, haihitaji ufafanuzi sana kukielewa. Hapa tunajaribu kukupa picha tu, ili kukusaidia wewe mwenyewe kuvisoma vitabu hivyo kiurahisi, Hivyo tumia muda wako mwingi kuvisoma peke yako, Na Mungu atakufunulia mengi zaidi…

Usikose mwendelezo, na Pia washirikishe wengine habari njema..

Bwana akubariki.

Kwa mwendelezo >>> VITABU VYA BIBLIA: Sehemu ya 6

Kwa maombezi/ Ushauri/ Ratiba za Ibada/Maswali/ Whatsapp/ Piga namba hizi: +255693036618/ +255789001312

Pia unaweza ukapata mafundisho haya Kwa njia ya Whatsapp yako, jiunge na channel yetu Kwa kubofya hapa >> WHATSAPP


Mada Nyinginezo:

BIDII YA MFALME YOSIA.

KITABU CHA YASHARI KINACHOZUNGUMZIWA KATIKA 2SAMWELI 1:17-18, NI KITABU GANI?

NABII ELISHA ALIKUWA ANA MAANA GANI KULIA NA KUSEMA”GARI LA ISRAELI NA WAPANDA FARASI WAKE”?

ROHO YA ELIYA KATIKA AGANO JIPYA INATENDAJE KAZI?

SAUTI NYUMA YA ISHARA.

KANUNI JUU YA KANUNI.


Rudi Nyumbani:

Print this post

JINSI WATU WANAVYOZAMA KATIKA USHIRIKINA NA UCHAWI.

Uchawi katika Biblia.

Mambo yote ambayo biblia imeyataja kama vile, kutazama bao(utambuzi), kubashiri, kuloga kwa kupiga mafundo. Kupandisha pepo/kupunga pepo, kuomba kwa wafu, kusihiri n.k. Yote haya kwa ufupi tunaweza kuyaweka katika kundi moja linalojulikana kama uchawi.

Na kazi hii imehasisiwa na shetani mwenyewe, baada ya kuona kuna upungufu wa taarifa Fulani za muhimu zimuhusuzo mwanadamu. na huku wanadamu wanao kiu ya kuzijua. ndipo hapo akabuni kitu kinachoitwa uchawi. Ni sawa na leo hii uone kisima kinachimbwa kijijini kwenu. Moja kwa moja utagundua kuwa ni kwasababu ya ukosefu au upungufu wa maji na ndio maana kisima kimekuja kuchimbwa.

Vivyo hivyo na Shetani naye, aliuleta uchawi baada ya kuona kuna taarifa Fulani zimuhusuzo mwanadamu zimekosekana au zimefichwa. Na aliyezificha ni Mungu mwenyewe kwa makusudi yake maalumu. ili wanadamu na viumbe vyake vyote viishi kwa kumtegemea yeye. Na si kwa kutegemea nguvu zao au akili zao.

Jambo hili lilimkasirisha shetani tangu mwanzo, na ndio maana aliasi ili ajitawale mwenyewe. Lakini alipoona ameshindwa kujua hata chanzo na mwisho wa maisha yake mwenyewe akaamua mawazo yake maovu ayalete kwa wanadamu kwa njia hiyo ya uchawi.

Uchawi ulianzi wapi?

Hivyo uchawi wa kwanza aliouleta, ulianzia pale Edeni, Mungu alipomweka Adamu na Hawa. Akawaagiza na kuwaambia wale matunda ya kila mti lakini matunda ya mti wa ujuzi wa mema na mabaya wasile. kwasababu siku watakapokula, watakufa. Lakini tunamwona shetani akitokea ndani ya nyoka, Na kuanza kumwambia Hawa, Hakika hamtakufa…”Hilo Neno Hakika hamtakufa” Ndio Mwanzo wa siri za uongo, na vitu kama hivyo mwanadamu sikuzote anapenda kusikia,.akaendelea na kusema, kwasababu Mungu anajua siku mtakapokula mtafumbuliwa macho na kuwa kama Mungu: Mkijua mema na mabaya..

Unaona Yaani hapo shetani alikuwa anawafunulia siri kuu sana, kama tunavyojua mtu aliyefikia hatua ya kutambua mema na mabaya ni mtu aliyepevuka akili anaweza kujiongoza mwenyewe. na kujiamulia mambo yake mwenyewe,..Hivyo shetani hapo alikuwa anawaaminisha kuwa watakapoasi na kula tunda, basi watakuwa na uwezo wa kupanga na kuchagua juu ya maisha yao, bila msaada wowote wa Mungu. vile vile wanaweza kuamua lolote wajisikialo, huyu Mungu wa nini tena?..hawezi kuwaambia chochote kwani yeye ni nani?…Hivyo Hawa akavutiwa sana na taarifa hizo mpaka akadhubutu kufanya kile kitendo kiovu . Ambacho matokeo yake ndio tunayaona hadi sasa.

Na jambo hilo hilo shetani aliendelea kulileta ndani ya watu, kwa vizazi na vizazi watu wakiwa na tama ile ile kujua hatma za maisha yao zitakuwaje na huku hawataki kumwangalia Mungu. Shetani anapata nafasi ya kuwadanganya kwa elimu zake za uongo, za utazamaji nyota.

Anawadanganya watu kuwa nyota zinazoonekana mbinguni zimebeba hatma ya maisha yao.

Anawadanganya kuwa kuwa alama za mikono zimebeba siri za maisha yao, anawadanganya miti Fulani au majani, ukiyapaka, au ukiyachanganya na vitu Fulani wataona mafanikio ya maisha yao. Na mambo chungu nzima,..huku anafahamu kabisa anayejua hatma ya maisha ya mwanadamu na mambo yake yote si mwingine zaidi ya Mungu lakini kwasababu watu hawamtaki Mungu. hivyo yeye anafanya hivyo kwa lengo moja tu, kuzidi kuwafanya watu wazidi kupoteza uelekeo wao kwa Mungu, ili awavute kwake, na wakishakita mizizi kwake, basi awaangamize waishie jehanum.

Sasa unaweza ukauliza lakini mbona kweli mganga Fulani, aliniambia kila ikifika mwezi wa 6 niwe ninavaa gauni jekundu. Kwasababu nyota yangu ya mafanikio ipo hapo, inaniagiza hivyo? na kweli nimekuwa nikivaa na kuona mafanikio makubwa katika huo mwezi.

Nataka nikuambie shetani ni mjanja sana. Hakuna cha nyota yako hapo, wala hakuna chochote alichogundua juu ya maisha yako, kama tulivyosema lengo lake ni kukuvuta kwake.

sasa wewe unapokwenda pale kwa mara ya kwanza, au unapomsikiliza kwenye TV. Na kutii maagizo yake, kuvaa hilo gauni jekundu alilokuambia huo mwezi. Anachofanya ni anaagiza tu mapepo yake, kukufanyia wewe kazi unapofika huo mwezi wa 6. Na ndio hapo unaweza kuona kama ni wateja wako wanaongezeka, au kitu Fulani kinafanikiwa kirahisi katika huo mwezi..Lakini huo ni mtego wa awali anafanya hivyo kwako kwa mara ya kwanza ili umwamini yeye.

Na kwa namna ya kawaida mtu akishaona kafanikiwa atarudi tena kwa Yule mganga au msoma nyota aliyempa yale maagizo. Ashuhudie aombe msaada zaidi,.ndipo atapewa tena masharti mengi ya ziada. kwa kuahidiwa kuwa ili nyota yake ifanye kazi kiufasaha zaidi, anapaswa akapigiwe ramli nyumbani kwake, au alale chooni hicho kipindi. Na mambo ya ajabu ajabu mengi, na yeye atafanya. kwasababu alishaona mafanikio hapo mwanzo, baada ya muda tena aturudi kupewa maagizo mengine. Ataambiwa sasa atoe kafara ya mtoto wake ili kusafisha nyota, asipofanya hivyo wazee wa nyota yake watakasirika na hivyo atakufa, ataenda kufanya kwa woga.

Hivyo hivyo kesho kutwa tena ataambiwa tena, apae na ungo waende Jupita kuitembelea nyota yake, atapaa na ungo. siku moja atakasirishwa na jirani yake na ataenda kutafuta msaada na atapewa uwezo wa kumdhuru mtu (kuloga). mpaka mwisho wa siku anajikuta amekuwa mchawi mashuhuri. Na yeye anakuwa mganga wa kuwafundisha wengine mambo hayo. Na mtu huwa akishafikia hatua kama hizo kurudi tena ni Neema ya Kristo. Wengi wanafia huko, ninaweza kusema asilimia 99 wanafia kwenye uchawi… na kuishia motoni.

Hivyo ndivyo watu wanavyozama kidogo kidogo kwenye ushirikina na uchawi pasipo wao kujijua.

Leo hii utaona katika magazeti vipengele wanavyoviita NYOTA ZETU. kaa mbali na hayo mambo wala usisome, ni mtego wa ibilisi, anataka ukakijaribu kile kilichoandikwa pale, wala usidhubutu,kwasababu kweli anaweza kukuletea majibu chanya kutokana na kile ulichokisoma pale, lakini kumbe unaelekea shimoni.

UKWELI WA MAISHA YETU UPO WAPI?

Ndugu Ukweli wa maisha yetu upo mikononi mwa Mungu peke yake. Ikiwa utapenda kufahamu chochote kuhusu maisha yako ni heri ukapiga magoti na kumwomba akufunulie. Akikufunulia ni sawa asipokufunulia ni sawa vile vile ishi maisha ya amani ukijua kabisa wote waliomtumaini yeye watakuwa salama mikononi mwake…Pia hatima yetu imeandikwa kwenye Neno lake. Ukilisoma vizuri na kulielewa basi utakuwa umejua hatima ya Maisha yako. Njia za haraka haraka na za mkato kujua kesho yako itakuwaje, au za kutaka kujua ni nini kinaendelea kukuzunguka. Au za kutafuta mali za ghafla ziogope! Shetani kaweka mitego kila mahali.

Mungu aliwaonya sana wana wa Israeli juu ya jambo hili watakapofika nchi ya Kaanani.

Wasidhubutu mambo hayo, kwasababu hayo ndiyo yaliyomkasirisha Mungu mpaka wakaondolewa wale wenyeji wa Kaanani..

Kumbukumbu 18:10 “Asionekane kwako mtu ampitishaye mwanawe au binti yake kati ya moto, wala asionekane mtu atazamaye bao, wala mtu atazamaye nyakati mbaya, wala mwenye kubashiri, wala msihiri.

11 wala mtu alogaye kwa kupiga mafundo, wala mtu apandishaye pepo, wala mchawi, wala mtu awaombaye wafu.

12 Kwa maana mtu atendaye hayo ni chukizo kwa Bwana; kisha ni kwa sababu ya hayo Bwana, Mungu wako, anawafukuza mbele yako.

13 Uwe mkamilifu kwa Bwana, Mungu wako.

14 Maana mataifa haya utakaowamiliki huwasikiliza wanaoshika nyakati mbaya na kutazama bao; bali wewe, Bwana, Mungu wako, hakukupa ruhusa kutenda hayo.’’

Ndugu kama ulishawahi kujaribu mambo yoyote katika hayo. Tubu sasa, uombe rehema Mungu atakusamehe na uanze sasa kumfanya Mungu kuwa tumaini lako. Na yeye mwenyewe ndiye atakayekuongoza katika njia salama. Kwasababu hukumu ya Mungu ipo juu ya watu wote wanaojaribu kusikiliza mafundisho ya mashetani.

Malaki 3:5 “Nami nitawakaribieni ili kuhukumu; nami nitakuwa shahidi mwepesi juu ya wachawi,”

Ufunuo 21:8 “Bali waoga, na wasioamini, na wachukizao, na wauaji, na wazinzi, na wachawi. na hao waabuduo sanamu, na waongo wote, sehemu yao ni katika lile ziwa liwakalo moto na kiberiti. Hii ndiyo mauti ya pili.”

Ubarikiwe sana.

Pia kwa Maombezi, Ushauri, Maswali au Ratiba za Ibada Wasiliana nasi kwa namba

+225693036618/ +225789001312

Pia unaweza ukapata mafundisho haya Kwa njia ya Whatsapp yako, jiunge na channel yetu Kwa kubofya hapa >> WHATSAPP


Mada Zinazoendana:

HADITHI ZA KIZEE.

MAFUNDISHO YA MASHETANI

JE!MUNGU ANAWEZA KULETA MAJIBU KUPITIA NGUVU ZA GIZA KAMA TUNAVYOSOMA NABII SAMWELI KUPATA MAJIBU KWA MWANAMKE MCHAWI?


Rudi Nyumbani

Print this post

FIMBO YA HARUNI!

Shalom! Karibu tujifunze Biblia..

Haruni alikuwa ni kaka yake Musa, waliozaliwa tumbo moja…isipokuwa Haruni alikuwa ni Mkubwa kwa Musa kwa miaka 3, Lakini Bwana alimchagua Musa kubeba kusudi lake la kuwatoa wana wa Israeli kutoka nchi ya Misri kuelekea Kaanani…Na biblia inasema Mungu alimchagua Haruni kaka yake Musa kuwa kama Nabii wa Musa…Na pia walikuwa na dada yao aliyeitwa Miriamu ambaye naye pia alikuwa ni Nabii (Kutoka 7:1).

Lakini haikuishia hapo, Mungu alilifanya kabila la Musa kuwa kabila la kikuhani,(Kabila la LAWI) na alimchagua Haruni kaka yake Musa, baadaye kama Kuhani Mkuu wa kwanza katika Israeli’’.

Na wote wawili hawa, Musa na Haruni Mungu alikuwa anatembea nao kwa namna ya kipekee sana, na wote walipewa mamlaka Fulani na Mungu. Lakini kama ukijifunza Biblia kwa makini utaona, Mungu alitembea na Musa sana kwa kutumia ile fimbo aliyokuwa nayo kule nyikani aliyokuwa anaitumia kuchungia kondoo za Mkwe wake (aliyeitwa Yethro) baada ya kumkimbia Farao zamani..Fimbo ambayo alikuwa anatumia kuchungia mifugo ilikugeuka baadaye kuwa fimbo ya kuwachunga wana wa Israeli, na fimbo ya adhabu kwa Farao.

Sasa hii fimbo mara ya kwanza ilikuwa ni ya Musa, na ilikuwa ni ya kwake tangu akiwa kwa Yethro, lakini baada ya Musa, kutomwamini Mungu na kuanza kujitetea kwamba yeye si msemaji, ndipo Mungu akamfanya Haruni awe anazungumzaji kwa niaba yake, …na ile fimbo akapewa Haruni kwasababu yeye ndiye atakayekwenda kufanya zile ishara zote mbele ya Farao kwa niaba ya Musa, kwahiyo ile fimbo ikaitwa FIMBO YA HARUNI. Ndio ile ile fimbo iliyogeuka nyoka mbele ya Farao, na kuwameza wale nyoka wa Farao, na ndio ile ile fimbo iliyogeuza maji yote ya Misri kuwa Damu.(Kutoka 7:19),na ndiyo ile ile iliyogeuza mavumbi kuwa chawa, na ndio iliyoigawanya bahari ya Shamu ili wana wa Israeli wapite na ndiyo iliyoifunga bahari ya Shamu ili Jeshi la Farao liangamie n.k

Sasa ilikuwa ni fimbo ya hukumu na mamlaka…Kama mchungaji, kazi ya fimbo ya mchungaji ni kuwaweka kondoo kwenye mstari na pia kuwapiga maadui wanaotaka kuwadhuru kondoo.

Sasa wakiwa jangwani katika safari ya kwenda Kaanani kuna baadhi ya watu walinyanyuka kinyume cha Musa na Haruni, na kusema inatosha sasa nyie kujifanya wakubwa juu yetu…Hivyo wakataka wao ndio wawe viongozi wa lile kundi lote…Mungu hakupendezwa na kile kitendo hivyo akawaua wote walijaribu kutekeleza hilo zoezi..Unaweza kusoma hayo katika kitabu cha Hesabu mlango wa 16.

Watu hao pamoja na kuona miujiza yote bado walikuwa wanadhani ni Musa na Haruni kwa akili zao ndio walioamua kuwatoa Misri, hawakujua kuwa ni Mkono wa Mungu, kwa ile fimbo ya kichungaji ndiyo iliyowatoa Misri…hivyo badala ya kumwangalia Mungu na uweza wake wakaanza kuwashambulia Musa na Haruni kana kwamba wao ndio waliowatoa Misri, waliwachoka hivyo wakataka kujichagulia watu wengine wa kuongoza.

Lakini Mungu kuthibitisha kuwa si mwanadamu anayeokoa bali ni Mungu, na kuwathibitishia kuwa hapangiwi mtu wa kulibeba kusudi lake..aliwaambia wakuu wote wa makabila kila mmoja alete fimbo yake mbele ya agano la ushuhuda, kwahiyo zikaletwa fimbo 12, Na hizi fimbo hazikutwaliwa tu kutoka kwa watu wa kawaida, hapana bali zilitwaliwa kutoka kwa Wakuu wa kila kabila la Israeli..Wakuu wa makabila walikuwa ni watu wa Mungu, na walioheshimika na kila kabila lilikuwa na mkuu mmoja, na kila mkuu alikuwa na fimbo yake kama vile Musa alivyokuwa na fimbo…Na hao Mungu aliwajalia hekima katika kuongoza, na pia fimbo zao zilikuwa na miujiza Fulani, hazikuwa fimbo za kawaida..

Kwahiyo fimbo zao zikakusanywa zote, na kila fimbo ikaandikwa jina la mhusika…. na katika kabila la Lawi wakaichagua ile fimbo ya Haruni, kwahiyo zikapelekwa mbele ya hema ya kukutania.

Hesabu 17:1 “Kisha Bwana akanena na Musa, akamwambia,

2 Nena na wana wa Israeli, kisha upokee kwao fimbo, fimbo moja kwa ajili ya nyumba ya kila baba, katika wakuu wao wote, kama nyumba za baba zao zilivyo, fimbo kumi na mbili; kisha andika jina la kila mtu katika fimbo yake.

3 Na katika fimbo ya Lawi utaliandika jina la Haruni; maana, itakuwa fimbo moja kwa kila kichwa cha nyumba za baba zao.

4 Nawe utaziweka katika hema ya kukutania mbele ya huo ushahidi, hapo nikutanapo pamoja nanyi.

5 Kisha itakuwa, mtu huyo nitakayemchagua, fimbo yake itachipuka; nami nitayakomesha kwangu manung’uniko ya wana wa Israeli, wanung’unikiayo juu yenu.

6 Basi Musa akawaambia wana wa Israeli, ndipo wakuu wao wote wakampa fimbo, fimbo moja kwa kila mkuu, kama nyumba za baba zao zilivyokuwa, fimbo kumi na mbili; na fimbo ya Haruni ilikuwa kati ya fimbo zao.

7 Kisha Musa akaziweka hizo fimbo mbele za Bwana katika hema ya kukutania”.

Kesho yake walipoingia ndani ya Hema… wakaikuta ile fimbo ya Haruni imechipuka na kuzaa matunda, na zile nyingine hazijachipuka…Ndipo wana wa Israeli wakajua kuwa ni Mungu ndiye aliyekuwa pamoja na Musa na Haruni, Na Mungu amewachagua hao kubeba kusudi lake.

“8 Ilikuwa siku ya pili yake, Musa akaingia ndani ya hema ya ushahidi; na tazama, ile fimbo ya Haruni iliyokuwa kwa nyumba ya Lawi ilikuwa imechipuka, imetoa michipukizi, na kuchanua maua; na kuzaa malozi mabivu.

9 Kisha Musa akazileta nje hizo fimbo zote kutoka hapo mbele za Bwana na kuziweka mbele ya wana wa Israeli wote; nao wakaangalia, na kila mtu akaitwaa fimbo yake. 

10 Kisha Bwana akamwambia Musa, Irudishe fimbo ya Haruni mbele ya ushahidi, ili itunzwe iwe ishara juu ya hawa wana wa maasi; ili uyakomeshe manung’uniko yao waliyoninung’unikia, ili wasife.

11 Basi Musa akafanya vivyo; kama Bwana alivyomwagiza, ndivyo alivyofanya ”.

Malozi ni matunda Fulani yanayojulikana kama matipisi, au sehemu nyingine yanajulikana kama mapindigesi au mapichi. Ni matunda ambayo yakiiva yanakuwa matamu sana na yana mbegu ngumu sana ndani, na pia maua yake ni mazuri sana kupita kiasi..Sasa tabia ya mti wa Mlozi au mtipisi ni kwamba hautoi matunda msimu mmoja na maua, msimu wa maua huwezi kukuta tunda hata moja unakuta mti wote ni maua tu, na maua yake ni mazuri sana, ni mchanganyiko wa rangi ya pink na nyeupe..kadhalika msimu wa matunda huwezi ukakuta ua hata moja, mti wote unakuwa ni kijani tu, na umejaa matunda..lakini hapa kwenye hii fimbo ya Haruni unaona mwujiza matunda na maua yamechipuka kwa wakati mmoja…

Tabia yake nyingine ya kipekee ya mti wa Mlozi (mtipisi)..ni kwamba unachukua muda mrefu sana mpaka ukomae na kufikia kiwango cha kuzaa matunda, sio mti mkubwa sana ni kama mchungwa tu! Lakini unaweza kuchukua hata miaka 12 mpaka ufikie hatua ya kuzaa matunda…Lakini hapa katika hii fimbo ya haruni unaona imechukua usiku mmoja tu kuzaa, ina maana kubwa sana ambayo tutakuja kuona hapo mbeleni.

Na mti wa Mtipisi, ni mti ambao unahitaji mizizi mirefu ili iweze kukua, mizizi ya mti huu inakadiriwa kuwa na urefu mara mbili ya mti wenyewe…kwahiyo unaweza kuona ni mti unaohitaji sana mizizi ili ukue..lakini hapa kwenye fimbo ya Haruni kulikuwa hakuna mizizi.

Kwahiyo ile fimbo ya Haruni ilikuwa inawakilisha Mkono wa Mungu juu ya wana wa Israeli, kwamba anawachunga wana wa Israeli kwa miujiza, kwa fimbo ya kimiujiza, kwamba Bwana anatoa chakula mahali ambapo hakuna chanzo cha chakula, ndio maana umeona ile fimbo imechipua na haina mizizi, Wana wa Israeli walikula mana na nyama jangwani mahali ambapo hakuna mashamba wala mvua… pia Bwana anaweza kuumba jambo leo leo kwa jambo ambalo lingeweza kuchukua miaka mingi kufanyika ndio maana unaona ile fimbo imechipuka kwa usiku mmoja tu na kuzaa matunda mengi.

Pia Bwana ana uwezo wa kuikusanya misimu miwili au zaidi na kuileta pamoja, kwa Bwana inawezekana kuzaa na kuchanua kwa wakati mmoja ndio maana unaona ile fimbo ilizaa matunda na kuzaa maua kwa wakati mmoja.

Kadhalika Kristo ndiye Kiongozi wetu sasa, yeye ndiye aliyepokea mamlaka yote ya Mbinguni na Duniani kutoka kwa Baba kama vile Haruni alivyopokea uongozi kutoka kwa Musa na fimbo ya kichungaji, na sisi leo tukimpokea Kristo na kumwamini, basi tutakuwa chini ya FIMBO YA KICHUNGAJI YA BWANA YESU KRISTO, ambayo hiyo haina msimu maalumu wa kutupa mema, hiyo tukiumwa haihitaji mamia ya miaka ndipo tupone, ni papo kwa hapo…hiyo haihitaji kuhofia tutakula nini wala tutakunywa nini?…inatoa chakula mahali pasipo na chakula na kutoa maji mahali pasipo na maji, kama fimbo ya Haruni ilivyotoa maji mwambani kule jangwani… na inatengeneza njia mahali pasipokuwa na njia..

Lakini sharti kwanza lazima ukubali kuwa kondoo wake, ndipo uchungwe na unakuwa kondoo wake kwa kumwamini na kwa kutubu dhambi kwa kumaanisha kuziacha na kisha kwenda kubatizwa katika ubatizo sahihi wa maji mengi na kwa jina la Yesu, na kupokea kipawa cha Roho Mtakatifu, hapo utakuwa kondoo wake, na utashiriki Baraka zote za uchungaji wake..

Fimbo za wengine hazina nguvu ya kiungu, haziwezi kufanya lolote haziwezi kuchipuka zinahitaji mizizi, zinahitaji muda mrefu kukupatia msaada, vile vile haziwezi kukutetea, wakati wa maadui, fimbo ya Haruni iligeuka pia kuwa nyoka kwa Farao pale ilipopasa…Si zaidi fimbo ya BWANA wetu YESU KRISTO?.

Zaburi 23:1 “Bwana ndiye mchungaji wangu, Sitapungukiwa na kitu.

2 Katika malisho ya majani mabichi hunilaza, Kando ya maji ya utulivu huniongoza.

3 Hunihuisha nafsi yangu; na kuniongoza Katika njia za haki kwa ajili ya jina lake.

4 Naam, nijapopita kati ya bonde la uvuli wa mauti, Sitaogopa mabaya; Kwa maana Wewe upo pamoja nami, GONGO LAKO NA FIMBO YAKO VYANIFARIJI”.

Ubarikiwe.

Pia kwa Maombezi, Ushauri, Maswali au Ratiba za Ibada Wasiliana nasi kwa namba

+225693036618/ +225789001312

Pia unaweza ukapata mafundisho haya Kwa njia ya Whatsapp yako, jiunge na channel yetu Kwa kubofya hapa >> WHATSAPP


Mada Zinazoendana:

NABII MUSA NI NANI?

HARUNI ALIKUWA NI NANI?

VITABU VYA BIBLIA: Sehemu ya 1

NI KWASABABU YA YESU KRISTO.


Rudi Nyumbani

Print this post

MUNGU WANGU,MBONA UMENIACHA?.

Bwana wetu Yesu Kristo japo alikuwa ni Mungu mwenyewe katika mwili lakini hakuwa mnafiki kutokuonyesha hisia zote wanadamu wanazopitia wakiwa hapa duniani, Kama wengine walivyotazamia kuwa Mungu akiuvaa mwili, basi yeye atakuwa ni kama malaika duniani, Na ndio maana Waebrania 2:16-18 inasema:

16 Maana ni hakika, hatwai asili ya malaika, ila atwaa asili ya mzao wa Ibrahimu.

17 Hivyo ilimpasa kufananishwa na ndugu zake katika mambo yote, apate kuwa kuhani mkuu mwenye rehema, mwaminifu katika mambo ya Mungu, ili afanye suluhu kwa dhambi za watu wake.

18 Na kwa kuwa mwenyewe aliteswa alipojaribiwa, aweza kuwasaidia wao wanaojaribiwa.

Unaona? Bwana alilia palipopaswa kulia, sehemu nyingine aliomba Mungu amwepushe, na kikombe cha mateso ikiwa ni sawa sawa na mapenzi ya Baba yake, kwa namna ya kawaida tunaweza kusema hofu ya kibinadamu ya kuuawa ilimwingia.

Vile vile Japo siku zote alifahamu Baba yake yupo pamoja naye, hawezi kumwacha, na alishamweleza kitu kuhusu maisha yake, na mwisho wake utakavyokuwa, na yatakayotokea baada ya hapo, lakini kuna saa huzuni ilikuwa inamwingia….Halikadhalika Bwana akiwa pale msalabani alijua kabisa siku zisizodi tatu atakuwa utukufuni, akijua kabisa safari yake imeshakwisha kikamilifu, amebakisha dakika chache tu aondoke duniani lakini katika hatua ile ile ya mwisho, tunaona anamwambia baba yake maneno haya:

Mathayo 27:46 “Na kama saa tisa, Yesu akapaza sauti yake kwa nguvu akisema, Eloi, Eloi, lama sabakthani? Yaani, Mungu wangu, Mungu wangu, mbona umeniacha?”

Fahamu kuwa alikuwa hazungumzi maneno haya ili kujifanya, ni kweli kabisa ndani ya moyo wake, hakuwa anaona uwepo wowote wa ki-Mungu, ndani yake hakukuwa na chochote, alikuwa hana tofauti na wale wezi aliosulibiwa nao, ni kama vile kaachwa Solemba, alikuwa kama mtu ambaye Mungu hajawahi kuzungumza naye kabisa, ndivyo alivyojiona ndani yake..

Tukitafsiri kwa lugha ya leo tunaweza kusema, Ee! Mungu mbona katika siku za raha ulikuwa pamoja nami, ulikuwa unatembea nami, wala hakukuwa na shida yoyote, iweje leo katika shida zangu, umejitenga mbali nami?. Mungu wangu, Mungu wangu, upo wapi mbona umeniacha?.

Hali kama hii hii ilimkuta Daudi wakati anakimbizwa na Sauli, wakati anapitia shida nyingi mapangoni, wakati yupo katika kukataliwa, na dhiki, akaona kama vile Mungu hajihusishi tena, kamwacha peke yake, tunasoma:

Zaburi 10:1 “Ee Bwana, kwa nini wasimama mbali? Kwani kujificha nyakati za shida?”.

Zaburi 13: 1 Ee Bwana, hata lini utanisahau, hata milele? Hata lini utanificha uso wako?

2 Hata lini nifanye mashauri nafsini mwangu, Nikihuzunika moyoni mchana kutwa? Hata lini adui yangu atukuke juu yangu?

3 Ee Bwana, Mungu wangu, uangalie, uniitikie; Uyatie nuru macho yangu, Nisije nikalala usingizi wa mauti.

Nawe pia Wakati mwingine unaweza ukawa unapitia hali ngumu, magonjwa ya kutisha ambayo madaktari wamekuambia hakuna matumaini hapa, watu wanakutisha na kukupa shuhuda za waliokufa kwa magonjwa ya namna hiyo, unaumwa Kansa, unaumwa Ukimwi, Presha, Kisukari na magonjwa yote ya ajabu yaliyo duniani siku hizi. Umeombewa sana, ila hali bado ipo vilevile.

Na kweli ndani ya moyo wako unajua kabisa Mungu wako hawezi kukuacha, lakini bado unahisi kama vile hakuoni katika hali unayopitia sasa, unahisi kama vile, amekaa kimya, hachukui hatua yoyote kwa hilo tatizo ulilonalo kwa muda mrefu..

Nataka nikutie moyo, Biblia inasema Mungu hakuwahi kulidharau teso la mteswa. Na maneno hayo yafaraja tunayapata katika Kitabu cha Zaburi, kitabu kile kile ambacho Bwana YESU alikinukuu akiwa pale msalabani, ndicho hicho hicho Mungu alimpa majibu ya maneno yake…

Tusome:

ZABURI 22

1 Mungu wangu, Mungu wangu, Mbona umeniacha? Mbona U mbali na wokovu wangu, Na maneno ya kuugua kwangu?

2 Ee Mungu wangu, nalia mchana lakini hujibu Na wakati wa usiku lakini sipati raha.

3 Na Wewe U Mtakatifu, Uketiye juu ya sifa za Israeli.

4 Baba zetu walikutumaini Wewe, Walitumaini, na Wewe ukawaokoa.

5 Walikulilia Wewe wakaokoka, Walikutumaini wasiaibike.

6 Lakini mimi ni mdudu wala si mtu, Laumu ya wanadamu na mzaha wa watu.

7 Wote wanionao hunicheka sana, Hunifyonya, wakitikisa vichwa vyao;

8 Husema, Umtegemee Bwana; na amponye; Na amwokoe sasa, maana apendezwa naye.

9 Naam, Wewe ndiwe uliyenitoa tumboni, Ulinitumainisha matitini mwa mama yangu.

10 Kwako nalitupwa tangu tumboni, Toka tumboni mwa mamangu ndiwe Mungu wangu.

11 Usiwe mbali nami maana taabu i karibu, Kwa maana hakuna msaidizi.

12 Mafahali wengi wamenizunguka, Walio hodari wa Bashani wamenisonga;

13 Wananifumbulia vinywa vyao, Kama simba apapuraye na kunguruma.

14 Nimemwagika kama maji, Mifupa yangu yote imeteguka, Moyo wangu umekuwa kama nta, Na kuyeyuka ndani ya mtima wangu.

15 Nguvu zangu zimekauka kama gae, Ulimi wangu waambatana na taya zangu; Unaniweka katika mavumbi ya mauti

16 Kwa maana mbwa wamenizunguka; Kusanyiko la waovu wamenisonga; Wamenizua mikono na miguu.

17 Naweza kuihesabu mifupa yangu yote; Wao wananitazama na kunikodolea macho.

18 Wanagawanya nguo zangu, Na vazi langu wanalipigia kura.

19 Nawe, Bwana, usiwe mbali, Ee Nguvu zangu, fanya haraka kunisaidia.

20 Uniponye nafsi yangu na upanga, Mpenzi wangu na nguvu za mbwa.

21 Kinywani mwa simba uniokoe; Naam, toka pembe za nyati umenijibu.

22 Nitalihubiri jina lako kwa ndugu zangu, Katikati ya kusanyiko nitakusifu.

23 Ninyi mnaomcha Bwana, msifuni, Enyi nyote mlio wazao wa Yakobo, mtukuzeni, Mcheni, enyi nyote mlio wazao wa Israeli.

24 MAANA HAKULIDHARAU TESO LA MTESWA, WALA HAKUCHUKIZWA NALO; WALA HAKUMFICHA USO WAKE, BALI ALIPOMLILIA AKAMSIKIA.

25 Kwako zinatoka sifa zangu Katika kusanyiko kubwa. Nitaziondoa nadhiri zangu Mbele yao wamchao.

26 Wapole watakula na kushiba, Wamtafutao Bwana watamsifu; Mioyo yenu na iishi milele.

27 Miisho yote ya dunia itakumbuka, Na watu watamrejea Bwana; Jamaa zote za mataifa watamsujudia.

28 Maana ufalme una Bwana, Naye ndiye awatawalaye mataifa.

29 Wakwasi wote wa dunia watakula na kusujudu, Humwinamia wote washukao mavumbini; Naam, yeye asiyeweza kujihuisha nafsi yake,

30 Wazao wake watamtumikia. Zitasimuliwa habari za Bwana, Kwa kizazi kitakachokuja,

31 Nao watawahubiri watakaozaliwa haki yake, Ya kwamba ndiye aliyeyafanya.


Ukisoma ule mstari wa 24, anasema: 24 MAANA HAKULIDHARAU TESO LA MTESWA, WALA HAKUCHUKIZWA NALO; WALA HAKUMFICHA USO WAKE, BALI ALIPOMLILIA AKAMSIKIA.

Na wewe vile vile ambaye umeokoka, umepitia hali ya shida kwa muda mrefu, bila kuona dalili yoyote ya kuponywa au kutoka katika mahali ulipo, fahamu kuwa Mungu hajalidharau teso lako, wala hachukizwi nawe, wala hajauficha uso wake kwako, bali siku ile ya kwanza ulipomlilia alishakusikia, hivyo hutakufa. Kwahiyo kaa katika matumaini ya kuipokea muujiza wako, wakati aliokuandalia utaufurahia wema wake, ulio mwingi. Ilikuwa ni lazima Mungu aruhusu Bwana Yesu ayapitie yale ili alete faida kubwa zaidi katika ufalme wa mbinguni ndio maana Mungu alikaa kimya kwa wakati ule, lakini alipomaliza kazi yake, mateso yale yamekuwa sababu ya mimi na wewe kuupata wokovu. Vivyo hivyo na wewe usitishwe na kitu chochote, maadamu yupo pamoja na wewe sikuzote. Atakupigania.

Songa mbele na Bwana Yesu Kristo atakuonekania.

Ubarikiwe sana. Tafadhali “Share” Ujumbe huu na kwa wengine. Na Mungu atakubariki.

Pia kwa Maombezi, Ushauri, Maswali au Ratiba za Ibada Wasiliana nasi kwa namba

+225693036618/ +225789001312

Pia unaweza ukapata mafundisho haya Kwa njia ya Whatsapp yako, jiunge na channel yetu Kwa kubofya hapa >> WHATSAPP


Mada Zinazoendana:

BASI MUNGU AKAMUADHIMISHA SANA..

MNGOJEE BWANA

MAISHA ULIYOPITIA NYUMA NI USHUHUDA TOSHA WA WEWE KUMTUMIKIA MUNGU:

USIISHIE KUTAZAMA JUU, ENDELEA MBELE.


Rudi Nyumbani

 

Print this post

USIWE SABABU YA WATU KUMKUFURU MUNGU.

2 Samweli 12:9 “Kwa nini umelidharau neno la Bwana, na kufanya yaliyo mabaya machoni pake? Umempiga Uria, Mhiti, kwa upanga, nawe umemtwaa mkewe awe mke wako, nawe umemwua huyo kwa upanga wa wana wa Amoni.

10 Basi, sasa upanga hautaondoka nyumbani mwako, kwa sababu umenidharau, ukamtwaa mkewe Uria, Mhiti, kuwa mke wako.

11 Bwana asema hivi, Angalia, nitakuondokeshea uovu katika nyumba yako, nami nitawatwaa wake zako mbele ya macho yako, na kumpa jirani yako, naye atalala na wake zako mbele ya jua hili.

12 Maana wewe ulifanya jambo lile kwa siri; bali mimi nitalifanya jambo hili mbele ya Israeli wote na mbele ya jua.

13 Daudi akamwambia Nathani, Nimemfanyia Bwana dhambi. Nathani akamwambia Daudi, Bwana naye ameiondoa dhambi yako; hutakufa.

14 Lakini, KWA KUWA KWA TENDO HILI UMEWAPA ADUI ZA BWANA NAFASI KUBWA YA KUKUFURU, MTOTO ATAKAYEZALIWA KWAKO HAKIKA YAKE ATAKUFA”.

Shalom! Jina la Bwana Yesu Kristo libarikiwe.

Leo tutajifunza, madhara ya kuruhusu dhambi katika maisha yetu!..Tukijifunza kwa Daudi, ambaye Mungu alimpaka mafuta awe Mfalme juu ya Israeli, kama wengi wetu tunavyojua, alikwenda katika njia za Mungu kwa ukamilifu wote isipokuwa katika habari za Mke wa Uria.

1 Wafalme 15:5 “kwa sababu Daudi alifanya yaliyo mema machoni pa Bwana, wala hakukosa katika yote aliyomwamuru, siku zote za maisha yake, isipokuwa katika habari ya Uria, Mhiti”.

Kosa la Daudi kumchukua mke wa Uria na kumwua Uria mwenyewe, ndio lililotia doa haki yake…Lilikuwa ni machukizo makubwa sana mbele za Mungu, mpaka Daudi alikuwa hatiani kufa…kwasababu alistahili kufa…Lakini kwasababu pia alikuwa ni mwepesi wa kujirudi na kukimbilia kutubu, Bwana alimhurumia na akaghairi kumwua, lakini hakumwacha bila adhabu.

Unajua wengi wetu tunadhani madhara ya dhambi ni kumwudhi Mungu tu basi..si zaidi ya hapo…lakini kiuhalisia madhara ya dhambi ni marefu sana, hayaishii tu kumwudhi Mungu bali yanakwenda mpaka kuathiri kazi ya Mungu.

Unaweza ukatenda sasahivi jambo, wewe ukaliona ni dogo tu! Lakini hilo jambo ulilolifanya likaenda kusababisha madhara mengine makubwa huko, ya jina la Mungu likatukanwa..kwahiyo ikawa umemletea mazao mengi shetani. Ndio maana kuna umuhimu mkubwa sana wa kujiepusha na dhambi za makusudi.

Tukirudi kwa Daudi tunaona alifanya nayeye dhambi kama hiyo ya makusudi, yeye alifanya kwa siri, akijua ni dhambi ndogo, lakini mbele ya jicho la Mungu ilikuwa ni dhambi yenye kuleta madhara makubwa katika Israeli..Kwa maana kwa kitendo kile Daudi alichokifanya, watu wote ambao walikuwa wanamsifia Daudi kuwa ni Mtumishi wa Mungu mkamilifu, waliposikia kamwua mtu asiye na hatia na kumwibia mke wake, walimdharau Mungu wake,…Hayo ndiyo madhara ambayo Mungu yanamchukiza zaidi.

Ndio maana Bwana alimwambia katika ule mstari wa 14 maneno yafuatayo.. “14 Lakini, KWA KUWA KWA TENDO HILI UMEWAPA ADUI ZA BWANA NAFASI KUBWA YA KUKUFURU, MTOTO ATAKAYEZALIWA KWAKO HAKIKA YAKE ATAKUFA”.

Mtoto Yule Mungu alimwua sio kwasababu ya makosa ya huyo mtoto, ni kwasababu ya Daudi, na aliadhibiwa hivyo kwasababu ALIWAPA ADUI ZA BWANA NAFASI YA KUKUFURU.

Hivyo na sisi tunajifunza hapo, tusipime kimo cha dhambi kwa jicho la juu juu tu! Kwamba nitatenda dhambi na kutubu! Tambua kuwa dhambi za makusudi zina madhara makubwa sana, sio kwako tu bali pia katika kuidhoofisha kazi ya ufalme wa mbinguni. Kwasababu zinasababisha jina la Mungu linatukanwa.

Warumi 2:21 “basi wewe umfundishaye mwingine, je! Hujifundishi mwenyewe? Wewe uhubiriye kwamba mtu asiibe, waiba mwenyewe?

22 Wewe usemaye kwamba mtu asizini, wazini mwenyewe? Wewe uchukiaye sanamu, wateka mahekalu? 

23 Wewe ujisifuye katika torati, wamvunjia Mungu heshima kwa kuiasi torati?.

24 KWA MAANA JINA LA MUNGU LATUKANWA KATIKA MATAIFA KWA AJILI YENU, kama ilivyoandikwa”.

Hatupaswi kufanya watu wamkufuru Mungu wetu kwa tabia zetu za ubishi, mashindano, wizi, kwa uasherati, uzinzi, wizi na utukanaji na mambo mengine yote machafu, Ni heri useme wewe sio mkristo kuliko useme ni mkristo halafu mtu asiyeamini akukute unafanya hayo mambo, utakuwa umemfanya aamini kuwa Ukristo ni unafki na uongo, jambo ambalo si kweli. Utakuwa unamsulibisha Kristo mara ya pili.

Daudi alimsababishia Yule mke wa Uria uchungu mwingi, kwa kumwulia mumewe na pamoja na huyo mtoto aliyemzaa Bwana alimwua… lakini Bwana alimfariji baadaye, Mama yake Sulemani alikuwa ni huyu mke wa Uria, ingawa Daudi alikuwa na wake wengi wenye watoto wengi lakini wana wao hawakuketi mahali pa Daudi isipokuwa mwana wa huyu mke wa Uria ambaye alikuwa ni Sulemani, mfalme mkuu.

Kwahiyo tunaonywa tujichunguze mienendo yetu, na tuyajue madhara ya dhambi kuwa hayaishii tu kutuletea sisi madhara, bali pia yanaathiri kazi za Mungu za kuwavuta watu kwake.

Ubarikiwe.

Pia kwa Maombezi, Ushauri, Maswali, au Ratiba za Ibada Wasiliana nasi kwa namba

+225693036618/ +225789001312

Pia unaweza ukapata mafundisho haya Kwa njia ya Whatsapp yako, jiunge na channel yetu Kwa kubofya hapa >> WHATSAPP


Mada Zinazoendana:

MSHAHARA WA DHAMBI:

DHAMBI ZINAZOTANGULIA NA ZINAZOFUATA.

SWALI: JE! KUNA DHAMBI KUBWA NA NDOGO, NA KAMA HAKUNA JE! MTU ALIYEUA NA ALIYETUKANA JE WATAPATA ADHABU SAWA?


Rudi Nyumbani

Print this post

LAANA YA YERIKO.

Shalom mtu wa Mungu, karibu tujifunze maneno ya uzima. Wana wa Israeli walipokuwa wanavuka Yordani kuingia Kaanani kama tunavyosoma habari walikutana na kizuizi kikubwa sana, nacho si kingine zaidi ya Mji wa Yeriko pamoja na watu wake ambao walikuwa hodari sana, majitu makubwa yenye nguvu, hayo ndiyo yaliyowasababishia mpaka Mungu achukizwe nao, kwa vile walivyojiona mbele zao kama mapanzi na hivyo Mungu akakasirishwa nao na kuwafanya wazunguke jangwani kwa muda wa miaka 40.

Hivyo mji huu wenye kuta kubwa, ulikuwa ni kama kikwazo kikubwa cha wana wa Israeli kumiliki nchi yao tangu zamani, hata hakukuwa na mji uliokuwa mkubwa zaidi ya ule, mfano Yeriko usingekuwepo, wana wa Israeli tangu zamani wangeshakuwa wamewasili katika nchi yao ya Kaanani Mungu aliyowaahidia.

Sasa ndio baadaye tunaona Yoshua baada ya kupewa maagizo ya kuushambulia ule mji, kwa kuuzunguka mara 7, kisha waingie ndani waue kila kitu, na walipomaliza vita, na kuuchoma mji tunaona Yoshua anasimama na kuzungumza maneno haya ya Laana:

Yoshua 6:26 “Naye Yoshua akawaapisha kiapo wakati ule, akasema, Na alaaniwe mbele za Bwana mtu yule atakayeinuka na kuujenga tena mji huu wa Yeriko; ataweka msingi wake kwa kufiliwa na mzaliwa wa kwanza wake, tena atayasimamisha malango yake kwa kufiliwa na mtoto wake mwanamume aliye mdogo.

27 Basi Bwana alikuwa pamoja na Yoshua; sifa zake zikaenea katika nchi ile yote”.

Tunaona Laana hii Yoshua aliitamka tu kwa mji huu, wa Yeriko hakutamka maneno kama hayo kwenye miji mingine ya Kaanani waliyoishambulia, ni kwasababu gani? Ni kwasababu Yeriko ndio mji pekee uliowatesa, na ndio uliowagharimu muda mwingi kuuweka chini. Yoshua ndio anayejua vizuri shida waliyoipata wakati ule walipokuwa na wale wapepelezi wenzake miaka 40 iliyopita jinsi mji huo ulivyokuwa kikwazo kikubwa kwao mbele za Mungu, Mpaka Yoshua akaona kujengwa tena mji huo ni sawa na kukumbushwa machungu yote ya kule jangwani..Ndio maana akazungumza Laana ile.

Hivyo wale watu waliokuwa na Yoshua, waliyashika maneno yale, hata wakati wamemaliza kuiteka miji yote na kuanza kujenga na kupanda, kama Bwana alivyowaagiza kuwa watakapoingia nchi ya ahadi wajenge na kupanda maana atawabikia kwa vingi…lakini ule mji wa Yeriko ulibakia vile vile bila kuguswa kama makumbusho ya Taifa, hakuna aliyedhubutu kwenda kuuendeleza kwa namna yoyote ile, na hiyo iliendelea kwa miaka mingi mbeleni.

Lakini baada ya miaka kama 530 hivi kupita, wakati wa utawala wa mfalme Ahabu, alitokea mtu mmoja, aliyeitwa Hieli mbetheli, yeye kwa kutokujua, au kwa kupuuzia, au kwa uzembe wake wa kutofuatilia msingi ipoje, na torati inasema nini juu ya mji huo, hakujiuliza ni kwanini mji huo umeachwa ukiwa muda mwingi angali mingine inaendelezwa yeye akanyanyuka na kwenda kuanza kuujenga Yeriko,..Na Laana ile ikampata sawasawa na maneno ya Yoshua.

1Wafalme16:34 “Katika siku zake, Hieli Mbetheli akajenga Yeriko; akatia misingi yake kwa kufiwa na Abiramu mzaliwa wake wa kwanza, na kuyaweka malango yake kwa kufiwa na mwana wake mdogo Segubu; sawasawa na neno la Bwana alilolinena kwa Yoshua mwana wa Nuni.”

Hii inatufundisha nini?, …kutokujua sheria hakukufanyi wewe usihukumiwe kwa sheria..Mungu akitamka laana zake halikadhalika na Baraka zake haijalishi unafahamu au haufahamu zitakupata tu. Hapa tunaona jambo hili lilitimia miaka 530 baadaye, nataka nikuambie hata na Leo eneo la Israeli ambalo mji wa Yeriko ulikuwepo, mtu aliyehusika au atakayehusika kuliendeleza eneo hilo jambo hili lilimpata au litampata haijalishi anafahamu au afahamu.

Sasa hiyo ni laana inayowahusu waisraeli, na agano la Kale, lakini vilevile katika agano jipya ipo laana ya namna hiyo hiyo imetolewa na Mtume Paulo..Tena hii ndio mbaya zaidi kwasababu inahusisha na mambo ya rohoni moja kwa moja.

Wakati ule, Mitume walipokuwa wanateseka, kuuhubiri injili ya ufalme wa mbinguni unaopatikana kwa Imani ya YESU KRISTO tu, wakiwa wanazunguka huku na huko, wakipitia hatari nyingi za kupigwa, na kufungwa na kuuawa, Na mwisho wa siku wanafanikiwa kuifikisha injili duniani kote..Mataifa yanaokoka, watu wanamtazama Yesu Kristo, wanaufurahia wokovu wake, wamestarehe.

Lakini huku nyuma kukaanza kutokea jopo lingine la wayahudi wa uongo, mitume wa uongo, waalimu wa uongo na manabii wa uongo, wakaanza kuwafundisha wale watu ambao walishamwamini Kristo injili ya namna nyingine ambayo mitume hawakuipeleka kwao. Jambo hili liliwahuzunisha sana mitume mpaka ikafikia hatua mtume Paulo anatoa laana hii kwa uweza wa Roho:

Wagalatia1:6 “Nastaajabu kwa kuwa mnamwacha upesi hivi yeye aliyewaita katika neema ya Kristo, na kugeukia INJILI YA NAMNA NYINGINE.

7 Wala si nyingine; lakini wapo watu wawataabishao na kutaka kuigeuza injili ya Kristo.

8 Lakini ijapokuwa sisi au malaika wa mbinguni atawahubiri ninyi injili yo yote isipokuwa hiyo tuliyowahubiri, NA ALAANIWE.

9 Kama tulivyotangulia kusema, na sasa, nasema tena, mtu awaye yote akiwahubiri ninyi injili yo yote isipokuwa hiyo mliyoipokea, NA ALAANIWE.

10 Maana, sasa je! Ni wanadamu ninaowashawishi, au Mungu? Au nataka kuwapendeza wanadamu? Kama ningekuwa hata sasa nawapendeza wanadamu, singekuwa mtumwa wa Kristo.”

Umeona, laana hii ilitoka karibia miaka 2000 iliyopita, na inayo nguvu ile ile hadi sasa, kama kipindi kile kulikuwa kumeshaanza kuonekana mitume wa uongo, sasahivi tusemeje.Hakuna mtu asiyejua hilo, Kila mahali tunasikia injili ambazo ukizilinganisha na injili za mitume hazina uhalisia wowote.. Na hatujui kuwa laana hii inaendelea kufanya kazi hadi sasa. Tusijidanganye na kusema hatujui, ni vizuri kabla ya kutaka kuwa waalimu, au wahubiri wa Neno la Mungu, tufahamu biblia inatufundisha nini au inataka nini. Vinginevyo tunaweza kujikuta tunadondokea katika laana mbaya ya Mungu pasipo hata sisi kujua.

Bwana Yesu alifunga vitabu vya agano jipya kwa maneno haya:

Ufunuo 22:17 “Na Roho na Bibi-arusi wasema, Njoo! Naye asikiaye na aseme, Njoo! Naye mwenye kiu na aje; na yeye atakaye, na ayatwae maji ya uzima bure.

18 Namshuhudia kila mtu ayasikiaye maneno ya unabii wa kitabu hiki, Mtu ye yote akiyaongeza, Mungu atamwongezea hayo mapigo yaliyoandikwa katika kitabu hiki.

19 Na mtu ye yote akiondoa lo lote katika maneno ya unabii wa kitabu hiki, Mungu atamwondolea sehemu yake katika ule mti wa uzima, na katika ule mji mtakatifu, ambao habari zake zimeandikwa katika kitabu hiki.”

Tufundishe Injili ya mitume ili tuwe katika Upande salama. Bwana atusaidie katika hilo.

Pia kwa Maombezi, Ushauri, Maswali au Ratiba za Ibada Wasiliana nasi kwa namba

+225693036618/ +225789001312

Pia unaweza ukapata mafundisho haya Kwa njia ya Whatsapp yako, jiunge na channel yetu Kwa kubofya hapa >> WHATSAPP


Mada Zinazoendana:

MADHARA YA KUTAFUTA ISHARA.

MWAMUZI WA KWELI

TUMEPEWA, SI KUMWAMINI TU KRISTO, ILA NA KUTESWA KWA AJILI YAKE;

NJIA YA MSALABA


Rudi Nyumbani

Print this post

VITABU VYA BIBLIA: Sehemu ya 4

Shalom! Karibu tujifunze Biblia, bado tupo katika mwendelezo wa kujifunza vitabu vya Biblia, tukiwa tayari tumeshavitazama vitabu tisa vya kwanza, na leo tutaendelea na kitabu kimoja kinachofuata kijulikanacho kama Samweli wa Pili,

Kumbuka huu ni uchambuzi tu! Ambao umechukua tu baadhi ya sehemu, sio ukamilifu wote, na biblia haina tafsiri moja maalumu, hapana! Mstari mmoja unaweza kuwa na mafunuo au mafunzo zaidi hata ya milioni moja, kwa jinsi tu Roho atakavyopenda kumfunulia mtu na mtu.

Kwahiyo ikiwa wewe ni mkristo mwenye Roho Mtakatifu ndani yako ni vizuri pia kuutumia muda wako binafsi kuisoma biblia yako, ukiwa peke yako, kwani Roho anaweza kukufunulia jambo ambalo haujawahi kulisikia likihubiriwa kwa mtu yoyote au mtumishi yoyote. Kwasababu Roho ya Mungu sio ya mwanadamu. Yeye hagawanywi kwa vipimo, hivyo mtu yoyote akiwa na NIA ya kujua, Roho Mtakatifu atamfunulia yote kama alivyoahidi katika neno lake.(Yohana 16:13)

Katika kitabu kilichopita cha Samweli wa kwanza (1Samweli), tulishaona kuwa kitabu hichi kiliandikwa na Nabii Samweli mwenyewe, isipokuwa katika sehemu za mwishoni mwa kitabu hicho, ambazo ziliandikwa na Nabii Nathani na Nabii Gadi, kwasababu Samweli asingeweza kuandika habari za kufa kwake mwenyewe katika kitabu hicho, hivyo ni wazi kuwa kuna wengine ndio waliondika sehemu hizo za mwisho..kama hujapitia bado hichi kitabu basi ni vizuri ukapitia kwanza uchambuzi wa vitabu vya mwanzo ili tuende pamoja huku mbeleni. BOFYA HAPA⏩ Vitabu vya biblia:Sehemu ya 3

Kitabu cha Samweli wa Pili, kiliandikwa na Nabii Nathani na sehemu baadhi kiliandikwa na Nabii Gadi..Nabii Nathani alikuwa ni Nabii wa Mungu, Wafalme hawakuwa manabii, ilikuwa ni ngumu wao kusikia Neno la moja kwa moja kutoka kwa Mungu, hivyo walihitaji watu maalumu waliopewa hiyo karama (ambao ndio manabii) kwahiyo kila mfalme alikuwa na manabii kadhaa ambao ndio walikuwa washauri wake wa karibu na ndio waliokuwa wanawaambia mambo yote Mungu aliyozungumza kuwahusu wao na ufalme wao. Kwahiyo Nathani alikuwa ni Nabii wa Mfalme Daudi, chochote Bwana alichokuwa anataka kuzungumza alikuwa anamwambia Nathani na kisha Nathani anakwenda kumwambia Daudi..kwahiyo Nathani kwasababu muda wote ndio alikuwa anakaa na Daudi yeye ndiye aliyekuwa anarekodi matukio yote ya utawala wake kwa kuongozwa na Mungu.

Sasa kitabu hichi kinaelezea maisha ya Daudi katika Ufalme wake, Kumbuka baada ya kufa mfalme wa Kwanza wa Israeli (yaani Sauli), Daudi ndio aliuchukua utawala mahali pake, kwasababu aliahidiwa na Mungu kuwa atatawala juu ya Israeli. Kwahiyo kitabu hichi kinamhusu Daudi mwanzo mwisho.

Unaweza kuipata historia ya Daudi kwa kusoma mwenyewe kitabu cha Samweli wa kwanza, lakini kwa ufupi ni kwamba Daudi hakuupata ufalme kama Sauli alivyoupata..Ukielewa vizuri jambo hili litakusaidia kujua kuwa wakati mwingine njia za Mungu si kama za mwanadamu,…utajifunza pia kutokujilinganisha na mtu mwingine na kumshukuru Mungu kwa kila kitu, katika mahali ulipowekwa… kwasababu njia hazifanani…Umewahi kusikia watu ambao Mungu kawabariki kwa mali za urithi na wale ambao Mungu kawabariki kwa kuhangaika kwao wenyewe?…Makundi yote haya mawili yanaweza yakawa yamepewa thawabu hiyo moja na Mungu mwenyewe isipokuwa katika njia mbili tofauti, mmoja kwa kurithi pasipo kuhangaika na mwingine kwa kuhangaika..Lakini kila moja ina faida zake na hasara zake.

Na kwa Daudi ilikuwa ni hivyo hivyo, Mfalme wa Kwanza Sauli, aliupata ufalme pasipo hata kuhangaika, baada ya kutiwa tu mafuta na Samweli, Bwana akamtengenezea njia akawa mfalme ndani ya usiku mmoja pasipo hata kuhangaika, lakini ilipofika zamu ya Daudi kuwa mfalme juu ya Israeli, shughuli ilikuwa ni nzito kidogo…hakuupata kama Sauli alivyoupata…Na hiyo ni kwasababu ilimpendeza Mungu iwe hivyo, ndio maana unaona Daudi alimpendeza Mungu zaidi ya Sauli.

Daudi baada ya kupakwa mafuta na nabii Samweli alidhani itakuwa ni rahisi tu kuingia kwenye ile enzi kama ilivyokuwa kwa Sauli, alijua utafika wakati tu, Israeli wote watautii unabii wa Samweli juu ya yeye kuwa mfalme na hivyo watakusanyika na kwenda kumwomba awe mfalme kwasababu amechaguliwa na Mungu, kama ilivyokuwa kwa Sauli hakutakuwa na upinzani wowote…lakini ukisoma biblia ndio utajua mambo Daudi aliyoyapitia mpaka alipokuja kuwa mfalme…Aliteseka nyikani kutwa kuchwa kuwindwa kama ndege kwa muda wa si chini ya miaka 15, baada tu ya kupakwa mafuta, aliongeza idadi ya maadui kwa kasi kubwa, mpaka mfalme alikuwa adui yake…Jaribu kujenga picha sasahivi unakuwa adui wa Raisi?..utakimbia wapi asijue? Maana anao wapelelezi wake kila kona, hata kitongoji wa kijiji atakuwa adui yako kwasababu akikuona ni kama kapata deal la fedha, au “kick” kwa mfalme…Inahitaji mkono wa Mungu tu! Kuepukana naye…ndio Daudi naye alikuwa hivyo hivyo, ilihitajika mkono wa Mungu tu kuepuka na mkono wa Mfalme Sauli aliyekuwa anamwinda usiku kucha.

Ilifika kipindi akawa hakai mjini tena, anakaa maporini na kwenye mapango kwa miaka ya kutosha, kwasababu akitokeza mjini tu, waandishi wa habari wapo wa kumpelekea mfalme taarifa, chakula kilikuwa ni cha kwenda kuomba! Omba! Unakula leo hujui kesho itakuwaje!..kuna wakati alikuwa anapungukiwa kabisa anapitia njaa kali pamoja na wale watu wachache aliokuwa nao…na mbaya zaidi alipata maadui ambao walikuwa wanamchochea kwa mfalme mambo ya uongo…

Ilifika kipindi wale mafilisti ambao alikuwa anawaita wamelaaniwa na wasiotahiriwa, wale ambao aliwaulia jemedari wao Goliathi, alikimbilia nchini kwao kuomba msaada (kuungana nao) [1Samweli 27:1], joto lilikuwa kali Israeli mpaka akaona akiendelea kukaa Israeli ana muda mchache sana wa kuishi…maana alikuwa anatafutwa kila kona, alikuwa na kesi za kutengenezewa si haba!.kiasi kwamba alikuwa anajua akishikwa tu na mfalme ni anakwenda kuchunwa ngozi mzima mzima. Ilifika kipindi hofu ya Mfalme ilikuwa kubwa hata kwa Israeli kiasi kwamba ukimwona Daudi halafu hujatoa taarifa na ikajulikana ulimwona hujatoa taarifa, ilikuwa ni KIFO!.

Sijui kama ulishawahi kupitia hali kama hivyo? Daudi hakuna chochote alichokuwa anafanya cha kujiendeleza kwa miaka zaidi ya 15.Wala alikuwa haishi maisha ya raha, Ni pori na yeye yeye na pori, Sio wewe unapitia kusemwa kidogo unasema una maadui!! Unapitia kutukanwa kidogo unasema unamaadui!..unatengwa kidogo unalalamika na kunung’unika unasema una maadui na bado unakula vizuri na unakunywa, na kesho unao uhakika wa kuishi… Daudi mpaka alihamia nchi jirani, kwenda kwa watu wasiotahiriwa ambao aliwatukana hapo kabla, angalau apate unafuu, kwa makubaliano kuwa hata ikitokea vita dhidi ya ndugu zake yupo tayari kuungana na wafilisti kwenda kunyume nao…

Taifa zima lilimgeuka, hata kama kulikuwa na wachache waliomkubali lakini itasaidia nini, kama Serikali nzima iko kinyume chako?..Wewe sasahivi Raisi atoe agizo la kukutafuta ili uuawe, ukizingatia kwenu ni wakulima na wafugaji, huna chochote…si utasema ni heri usingezaliwa…tena afadhali siku hizi mfumo wetu ni wa Uraisi ,zamani ilikuwa ni Ufalme, Mfalme alikuwa yupo juu ya sheria, tofauti na sasahivi ambapo Raisi hayupo juu ya sheria, na Mfalme alikuwa anatawala mpaka afe sio sasahivi baada ya miaka 10 tu amebadilika ameingia mwingine..

Kwahiyo hayo ndio mambo Daudi aliyokuwa anayapitia …Wengi wetu hatujui Kitabu cha Zaburi kiliandikwaje andikwaje! Sehemu kubwa ya kitabu cha Zaburi Daudi alikiandika akiwa nyikani, alipokuwa anawindwa…wakati anapitia shida! Ndipo akawa anasema….

Zaburi 13:1 “Ee Bwana, hata lini utanisahau, hata milele? Hata lini utanificha uso wako?

2 Hata lini nifanye mashauri nafsini mwangu, Nikihuzunika moyoni mchana kutwa? Hata lini adui yangu atukuke juu yangu?

3 Ee Bwana, Mungu wangu, uangalie, uniitikie; Uyatie nuru macho yangu, Nisije nikalala usingizi wa mauti.

4 Adui yangu asije akasema, Nimemshinda; Watesi wangu wasifurahi ninapoondoshwa.

5 Nami nimezitumainia fadhili zako; Moyo wangu na uufurahie wokovu wako.

6 Naam, nimwimbie Bwana, Kwa kuwa amenitendea kwa ukarimu”.

Huo ni mfano wa Maombi ya Daudi akiwa katika tabu ya kuwindwa na majeshi ya Mfalme Sauli..na hakuomba leo yakajibiwa leo leo…yalichukua miaka ya kutosha…Kwahiyo hizo Zaburi hazikuandikwa na mtu aliyekuwa hajui nini anazungumza, hakumwandikia mtu hizo, alijiandikia yeye…kila maombi aliyokuwa anaomba alikuwa anayaandika…ndio sisi tunayasoma leo kama ZABURI.

Kila hatua aliyokuwa anapitia alipokuwa anatafutwa, alikuwa anamwomba Mungu na kumshukuru na kumwimbia..na kila nyimbo kila sala na kila shukrani alikuwa anaiiandika, siku baada ya siku..Kuna wakati Daudi alikuwa hatiani kufa kwa kushikwa na Sauli, alikuwa ameshazingirwa pande zote, lakini Bwana akamwokoa na mkono wa Sauli, hivyo akamwimbia Mungu nyimbo za kumshukuru na akaziandika zote…

Sehemu chache sana za Zaburi Daudi aliziandika akiwa tayari kashakuwa mfalme…na nyingi ya hizo aliziandika kwa lengo la kumshukuru Mungu jinsi alivyomwokoa na maadui zake alipokuwa taabuni…Sasa utauliza ni wapi penye uthibitisho kuwa Zaburi iliandikwa na Daudi wakati yupo matesoni au wakati yupo kwenye ufalme?…Ukisoma kitabu cha Zaburi 18:1-7 biblia inasema “

1 Wewe, Bwana, nguvu zangu, nakupenda sana;

2 Bwana ni jabali langu, na boma langu, na mwokozi wangu, Mungu wangu, mwamba wangu ninayemkimbilia, Ngao yangu, na pembe ya wokovu wangu, na ngome yangu.

3 Nitamwita Bwana astahiliye kusifiwa, Hivyo nitaokoka na adui zangu.

4 Kamba za mauti zilinizunguka, Mafuriko ya uovu yakanitia hofu.

5 Kamba za kuzimu zilinizunguka, Mitego ya mauti ikanikabili.

6 Katika shida yangu nalimwita Bwana, Na kumlalamikia Mungu wangu. Akaisikia sauti yangu hekaluni mwake, Kilio changu kikaingia masikioni mwake.

7 Ndipo nchi iliyotikisika na kutetemeka, Misingi ya milima ikasuka-suka; Ikatikisika kwa sababu alikuwa na ghadhabu……”

Ukisoma mistari hiyo ya mlango wa 18 wa Zaburi, unaweza usielewe mwandishi kwanini aliandika hivyo au ni nini kilichomsukuma mpaka akaandika hivyo…alikuwa katika mazingira gani?…sasa jibu la swali hilo tunalipata katika kitabu cha 2 Samweli 22…

2 Samweli 22:1 BASI DAUDI AKAMWAMBIA BWANA MANENO YA WIMBO HUU, SIKU ILE BWANA ALIPOMWOKOA MIKONONI MWA ADUI ZAKE ZOTE, NA MKONONI MWA SAULI;

2 akasema, Bwana ndiye jabali langu, na ngome yangu, na mwokozi wangu, naam, wangu;

3 Mungu wa mwamba wangu, nitamwamini yeye; Ngao yangu, na pembe ya wokovu wangu, mnara wangu, na makimbilio yangu; Mwokozi wangu, waniokoa na jeuri.

4 Nitamwita Bwana astahiliye kusifiwa; Hivyo nitaokoka na adui zangu.

5 Maana mawimbi ya mauti yalinizunguka, Mafuriko ya uovu yakanitia hofu.

6 Kamba za kuzimu zilinizunguka; Mitego ya mauti ikanikabili.

7 Katika shida yangu nalimwita Bwana, Naam, nikamlalamikia Mungu wangu;

8 Ndipo nchi ilipotikisika na kutetemeka, Misingi ya mbinguni ikasuka-suka Na kutikisika, kwa sababu alikuwa na ghadhabu…”.

Umeona sababu za Daudi kuandika Zaburi?… Hivyo kitabu cha Samweli wa pili kinatufundisha jinsi Mungu anavyotenda kazi juu ya mtu na mtu…njia atakayotumia kukupa wewe, sio sawa na atakavyotumia kumpa mwingine, ni vizuri zaidi kupenda kupitishwa njia ngumu kwasababu hizo ndio zinazotufanya mara nyingi tuwe wakamilifu kuliko zile njia rahisi. Njia rahisi za kupata kitu zinatufanya tusikithamini kile kitu chenyewe,…kama Mfalme Sauli alipata ufalme kwa njia rahisi ndio maana hakuuthamini ufalme wake, akawa anafanya mambo ambayo Mungu hakumuagiza,…

lakini Daudi kwa miaka zaidi ya 15 alijaribiwa kwa mateso na hatari za vifo na kwa kurudia rudia kuomba pasipo majibu ya papo kwa hapo…..ndipo tunaona alipokuja kuupata ufalme aliuthamini sana, na aliishi kulingana na mapenzi ya Mungu..siku zote za ufalme wake, mpaka Mungu akamwahidia uzao wake utamtoa MASIHI (BWANA YESU KRISTO) ambaye sasa ndiye mkombozi wetu MWANA WA DAUDI. Katika ufalme wake alijifunza kunyenyekea na kuwathamini na kuwafariji pia walioko kwenye tabu..maana na yeye alishayapitia hayo..alikuwa hawaonei watu maana anajua uchungu wa kuonewa na kukimbizwa..

Pia kitabu hichi kinatufundisha njia kamili ya Mungu ni kutupa kidogo kidogo, mpaka kinakuwa kingi (Mithali 13:11)…usipende njia za haraka haraka, nyingi ya hizo sio mpango wa Mungu, utaona pamoja na Daudi kupitia taabu zote hizo hata ufalme hakupewa wote ndani ya siku moja…ukisoma biblia utakuja kuona kuwa alipewa na Mungu kwanza utawala juu ya Kabila moja kwa miaka 7, na baadaye ndipo akapewa utawala wa Israeli yote kwa miaka 33..Na aliishi kwa kumpendeza Mungu maisha yake yote, isipokuwa kwa kasoro ndogo ndogo alizokuwa nazo, lakini kwa ujumla alimpendeza Mungu sana..hiyo ni kutokana na kunolewa vyema kabla ya kuipokea ahadi aliyopewa na Mungu.

Na pia tunajifunza katika kitabu hichi kutokukata tamaa…Daudi alipitia tabu, mpaka dakika ya mwisho aliyokuwa amekata tamaa ndio kipindi hicho hicho Mungu alimpa ufalme, kipindi ambacho yupo nchi nyingine..kipindi ambacho asingetarajia, wala kulikuwa hakuna dalili yoyote ya yeye kumiliki ufalme ndio kipindi alichopokea ufalme tofauti na mategemeo yake, pengine alidhani wakati anamuua mfilisti wakati Israeli wote wanamshangalia ndio angeupata ufalme lakini badala yake, mahali ambapo yupo katika shida nchi ya ugenini ndipo Mungu anamnyanyua..kadhalika, njia za Mungu hazichunguziki, kipindi ambacho mtu anaweza kusema hapa haiwezekani tena, afadhali ingekuwa jana au juzi au mwaka juzi, lakini hajui kuwa kumbe huo ndio wakati uliofaa wa Mungu, kwahiyo ni kujifunza kuishi maisha ya kutokukata tamaa na kutokunung’unika siku zote na kumwamini Mungu.

Na mwisho maisha ya Daudi yamebeba siri ya Maisha ya Yesu Kristo, jinsi alivyopitia na kuishi ni Ufunuo wa Yesu Kristo jinsi alivyoishi hapa duniani..Naye pia alikuwa ni mfalme aliyekataliwa kama Daudi, na hata zaidi ya Daudi..tangu kuzaliwa kwake. Biblia inatuambia hivyo katika..

Isaya 53:1 Ni nani aliyesadiki habari tuliyoileta? Na mkono wa Bwana amefunuliwa nani?

2 Maana alikua mbele zake kama mche mwororo, Na kama mzizi katika nchi kavu; Yeye hana umbo wala uzuri; Na tumwonapo hana uzuri hata tumtamani.

3 Alidharauliwa na kukataliwa na watu; Mtu wa huzuni nyingi, ajuaye sikitiko; Na kama mtu ambaye watu humficha nyuso zao, Alidharauliwa wala hatukumhesabu kuwa kitu.

4 Hakika ameyachukua masikitiko yetu, Amejitwika huzuni zetu; Lakini tulimdhania ya kuwa amepigwa, Amepigwa na Mungu, na kuteswa.

Tunaona Herode alitamani kumwua, hata Israeli hawakumwamini ingawa yeye ndiye aliyeteuliwa na kupakwa mafuta na Mungu kuwa mfalme juu ya Israeli..lakini alipofika miaka 30 kama Daudi ndipo ulimwengu kidogo kidogo ukaanza kumsikia, ile ahadi ya ufalme ikaanza kutimia…akaanza kuutangaza mwaka wa Bwana uliokubaliwa…Na alipokuja na kufufuka ikatimia, sasahivi hatumtambui tu kama mfalme bali ni MFALME MKUU,MUNGU MWENYE NGUVU..Tutakuja kuulewa vizuri ufalme wake wakati wa Utawala wa miaka 1000 hapa duniani, sasahivi bado.

Hivyo kama hujayakabidhi maisha yako kwake ni vyema ukafanya hivyo leo usikawie kawie kwasababu haya maisha hatujapewa guarantee ya kufika kesho, na hakuna mwingine utakayeweza kupata tumaini kwake kama sio KRISTO…Yeye ndiye mpakwa mafuta pekee wa Mungu, tubu leo kwa kudhamiria kabisa kuacha dhambi, kama hujafanya hivyo…ukabatizwe katika ubatizo sahihi kwa jina lake upate ondoleo la dhambi zako, na kisha upokee kipawa cha Roho wake Mtakatifu, kabla mlango wa Neema haujafungwa.

Bwana akubariki sana

Kwa maombezi/ Ushauri/ Ratiba za Ibada/Maswali/ Whatsapp/ Piga namba hizi: +255693036618/ +255789001312

Pia unaweza ukapata mafundisho haya Kwa njia ya Whatsapp yako, jiunge na channel yetu Kwa kubofya hapa >> WHATSAPP

Kwa mwendelezo >>>VITABU VYA BIBLIA: Sehemu ya 5


Mada Nyinginezo:

ALIYE MKUU KATIKA UFALME WA MBINGUNI.

TABIA YAKO NI YA MNYAMA GANI?

MANABII WALISEMA “NENO LA MUNGU LIKANIJIA” ..MAANA YA HILI NENO NI NINI?.

MSTARI HUU UNA MAANA GANI? “TUPA CHAKULA CHAKO USONI PA MAJI; MAANA UTAKIONA BAADA YA SIKU NYINGI”. (MHUBIRI 11:1)

JE! VITABU VYA BIBLIA VILIWEZAJE KUKUSANYWA PAMOJA?


Rudi Nyumbani:

Print this post

PEPETO LA MUNGU.

Siku moja nilipokuwa nakula wali na choroko, nilikutana na zile choroko ngumu ambazo tunajua hata ukizipika vipi huwa haziivi, nilishazoea kukutana nazo mara kwa mara, lakini sikuhiyo nilikutana nazo nyingi kiasi cha kushindwa kula chakula, hapo ndipo nilipotamani kujua hasaa huwa zinaondolewaje kwenye choroko nzuri, kwasababu wakati zinachambuliwa huwa hazionekana, ni rahisi kweli kutoa uchafu wote, na makapi yote lakini zile haziondoki zina sura ile ile kama choroko nyingine..

Ndipo nikafuatilia na kuuliza, nikagundua kuwa kumbe choroko hazichambuliwi kama maharage, maharage utatoa uchafu unaouna na kwenda kuosha na kubandika kazi imeisha, lakini choroko huwa inaenda hatua nyingine ya ziada,..Na ndio maana ukila chakula kwenye hoteli nzuri inayothamini huduma zake, chakula kama hichi huwezi kukutana na hizo choroko-mawe mdomoni, niziite hivyo, je! wanafanya nini?.

Wao wakishamaliza kutoa ule uchafu unaoonekana katika hatua ya awali, na kuziosha vizuri choroko zao, hatua inayofuata huwa wanachukua maji ya moto, kisha wanaziweka choroko ndani yake, na kuziacha hapo kwa muda wa kama dakika 5 hivi, kisha warudi kuyamwaga yale maji yote, halafu wanazimwaga kwenye sinia au ungo, wanaanza kuchambua tena, Sasa zile choroko-mawe ambazo hata uzipike na makaa ya mawe haziivi, zinajionyesha zenyewe.Kwasababu katika hatua ya awali zile nyingine zinapoanza kubadilika rangi na kuwa kama jani lililokauka hivi, zenyewe huwa zinabakia na ukijani wake hivyo hivyo kama vile vimetolewa jana shambani,..Hivyo ni rahisi kuziona na kuzitoa moja moja na kuzitupa..baadaye zile zilizobakia nzuri, wanazirudisha jikoni, na kuzipika mpaka mwisho ziive, Na hapo hata ule sufuria nzima la choroko huwezi kukutana na choroko-mawe hata moja mdomoni..

Ndivyo ilivyo hata katika kanisa la Kristo, Mungu naye huwa anachambua watu wake, katika hatua za awali, anawaita wengi sana kwake, na wengi wanamwamini na kusema mimi ni mkristo, nimeokoka, kiasi kwamba ni ngumu kutofautisha mkristo wa kweli ni yupi na Yule feki ni yupi, wote wamebatizwa, wote ni waaminio, wote ni washirika, ni sawa tu na zile choroko zinazooshwa katika maji, haijalishi ndani yao kuna nini..Lakini sasa ili lile andiko litimie linalosema “walioitwa ni wengi, lakini wateule ni wachache”, kutenganisha magugu, na ngano ni lazima kutokee..

Hapo ndipo maji ya moyo ambayo ndio (Neno la Mungu kama upanga linapopita juu ya watu)..kuangalia ni wapi watatii, na ni wapi watakuwa sugu..Hiyo ndio hatua ambayo Kristo anatupima kwa kile tulichokisikia na kufundishwa kutoka katika Neno lake na jinsi tunavyokitendea kazi,..Ikiwa wewe unajiita mkristo halafu umehubiriwa Neno miaka mingi, na ndani yako hakuonekani mabadiliko yoyote, bado ni mzinzi, mtukanaji, mvaaji vibaya, mtazamaji pornography, msengenyaji, mwendaji Disco n.k..na huku nyuma umebatizwa, ni mshirika mzuri wa Kanisani, mwimbaji kwaya,..wewe ni zile choroko-mawe ambazo hazisikii joto la maji, na siku si nyingi utaingia katika pepeteo la pili na la mwisho. Ambalo hilo ni pepeto la milele, hakuna kurudiwa tena. Hili andiko ndipo linapotimia.

1Yohana 2:19 “Walitoka kwetu, lakini hawakuwa wa kwetu. Maana kama wangalikuwa wa kwetu, wangalikaa pamoja nasi. Lakini walitoka ili wafunuliwe kwamba si wote walio wa kwetu.

Wakati wengine Mungu anawavukisha madarasa mengine ya kiroho, wanapikwa vizuri, kwa ajili ya kuurithi ufalme wa mbinguni, wewe kumbe siku nyingi ulishatupwa nje, unakuwa msindikizaji tu pasipo hata wewe kujijua, na dalili mojawapo itakayokuonyesha kuwa siku nyingi Mungu alishakuacha ni wewe kuzidi kuwa vuguvugu wa ajabu, na wenzako maisha yao ya rohoni kuimarika.

Mungu huwa anasema na watu katika viwango tofauti, ikiwa katika hatua awali, mafundisho ya msingi hayakurekebishi, mafundisho gani mengine utafundishwa yakugeuze. Choroko-mawe hata zikiachwa mpaka hatua ya mwisho bado zitabakia vile vile tu.

Ndugu tunaishi katika kanisa la 7 na la mwisho linalojulikana kama LAODIKIA, naamini utakuwa unalifahamu hilo, ni kanisa ambalo linasifika kwa tabia ya kuwa vuguvugu kuliko makanisa yote yaliyotangulia huko nyuma. (soma Ufu3:14). Na kumbuka pia SIRI ya Mungu ipo kwa bibi-arusi wa Kristo tu, na sio pamoja na Masuria..Masuria ndio wale wanawali wapumbavu ambao tunasoma walikuwa wanamngojea Bwana wao, aje lakini hawakuwa na mafuta ya ziada katika TAA ZAO (Mathayo 25)..Mbaya sana na Huo ndio uvuguvugu unaozungumziwa, nusu kwa Bwana, nusu, kwa shetani..nusu choroko, nusu uchafu…na hivyo unakuwa umekidhi vigezo vyote vya kuwa CHOROKO-MAWE. Na kustahili kutapikwa.

Wakati unao sasa wa kutengeneza mambo yako sawa, kabla mlango wa rehema hujafungwa, Mungu ni mwaminifu ukitubu atakupokea na kukuhifadhi kwake..

2Petro 1:10 “Kwa hiyo ndugu, jitahidini zaidi kufanya imara kuitwa kwenu na uteule wenu; maana mkitenda hayo hamtajikwaa kamwe.

11 Maana hivi mtaruzukiwa kwa ukarimu kuingia katika ufalme wa milele wa Bwana wetu, Mwokozi wetu Yesu Kristo”.

Ubarikiwe. Tafadhali “Share” Ujumbe huu na wengine. Na Bwana atakubariki.

Pia kwa Maombezi, Ushauri, Maswali au Ratiba za Ibada Wasiliana nasi kwa namba

+225693036618/ +225789001312

Pia unaweza ukapata mafundisho haya Kwa njia ya Whatsapp yako, jiunge na channel yetu Kwa kubofya hapa >> WHATSAPP


Mada Zinazoendana:

WALIOITWA NI WENGI, ILA WATEULE NI WACHACHE.

TABIA YA KIPEKEE USIYOIJUA KUHUSU NENO LA MUNGU.

HATUA ZA ROHO MTAKATIFU KATIKA KUTUONGOZA.

TUKAZE MWENDO KWA TULIYOANDALIWA.


Rudi Nyumbani

Print this post