Mungu anayo agenda, na usipojua agenda ya Mungu katika siku hizi za mwisho ni ngumu sana kuiona ile ng’ambo, Leo hii tunaishi maisha ya juu juu tu kwasababu hatujamjua YESU ni nani na tabia zake ni zipi kulingana na majira ya wakati.
Tunapenda kumjua tu katika ule upande wake mmoja, wa upole na unyenyekevu (Mathayo 11:29)..Lakini hatujui ule upande mwingine ambao anasema yeye ni MKEMEAJI, na MKANAJI, na MFUKUZAJI na MUUAJI WA WAOVU. Ikiwa leo hii hatutamwamini, halafu tukafa, au siku ile ya mwisho ikatukuta tupo katika njia zetu wenyewe, tujue kuwa tabia tutakazoziona kwake kipindi hicho zitatustaajabisha sana, tena sana.
Kanisa hili la mwisho tunaloishi linaloitwa Laodikia, ndio kanisa pekee kati ya yale saba, ambalo Bwana amelikemea vikali, kwa tabia zake, za kuwa vuguvugu.. Hii ikiwa na maana kuwa mimi na wewe kama tupo katika uvuguvugu huu uliopo sasa hivi duniani tujue kuwa tupo katika Hasira ya Kristo, ya kwenda kutapikwa.
Uvuguvugu wa kusema mimi nimeokoka, lakini maisha yako hayauhakisi wokovu ule wa kimaandiko, ndio tabia ya kanisa hili la mwisho ilivyo, mamilioni ya wakristo ndio hivyo walivyo leo hii. Jambo ambalo halikuwepo miaka ya zamani, ambayo watu hawakumchanganya Mungu na uovu, waliookoka walijulikana, waliokuwa waovu walijulikana. Hakukuwa na mtu aliyeshiriki meza ya Bwana na wakati huo huo ni mzinzi au mlevi, mtu anakwenda ibadani, halafu kesho pia anakwenda disco, hayakuwepo hayo. Waovu walijitenga, na watakatifu waliookolewa walijitenga, Lakini leo hii ni kawaida sana, kusikia hata mmiliki bar anasema ameokoka.
Ufunuo 3:15 “Nayajua matendo yako, ya kuwa hu baridi wala hu moto; ingekuwa heri kama ungekuwa baridi au moto.
3.16 Basi, kwa sababu una uvuguvugu, wala hu baridi wala moto, nitakutapika utoke katika kinywa changu.
17 Kwa kuwa wasema, Mimi ni tajiri, nimejitajirisha, wala sina haja ya kitu; nawe hujui ya kuwa wewe u mnyonge, na mwenye mashaka, na maskini, na kipofu, na uchi.
18 Nakupa shauri, ununue kwangu dhahabu iliyosafishwa kwa moto, upate kuwa tajiri, na mavazi meupe upate kuvaa, aibu ya uchi wako isionekane, na dawa ya macho ya kujipaka macho yako, upate kuona.
19 Wote niwapendao mimi NAWAKEMEA, na kuwarudi; basi uwe na bidii, ukatubu.
20 Tazama, nasimama mlangoni, nabisha; mtu akiisikia sauti yangu, na kuufungua mlango, nitaingia kwake, nami nitakula pamoja naye, na yeye pamoja nami”.
Lakini pia hakemei tu peke yake, kuna siku atasimama KUWAKANA na kuwaonea aibu watu wengi sana, mbele ya Baba yake, na mbele ya maelfu ya malaika zake huko mbinguni. Ikiwa leo hii unamwonea Kristo aibu unaogopa kuitwa mlokole, unaogopa kuvaa vizuri mavazi ya kujisitiri kisa utaitwa mshamba, unaona aibu kumtumikia Mungu wako, siku ile utakuonea aibu na wewe kweli kweli, hata hatapeleka jicho lake kukangalia.. wakati wengine akiwapongeza na kuwasifia.wewe utakuwa kama mtu baki tu.
Marko 8:38 “Maana kila mtu atakayenionea haya mimi, na maneno yangu, katika kizazi hiki cha uzinzi na dhambi, Mwana wa Adamu atamwonea haya mtu huyo, atakapokuja katika utukufu wa Baba yake pamoja na malaika watakatifu”.
Halikadhalika na kumkana vivyo hivyo, naye pia atakukana siku ile.
Kama hilo halitoshi Bwana Yesu pia anasema, atawafukuza watu wengi sana, siku ile, sio wachache, bali wengi sana. Na watakaofukuzwa sio watu wasiomjua Kristo bali, ni sisi sisi tuliopo kanisani, tunaolitumia jina lake kutenda miujiza lakini hatutaki kuishi maisha yampendezayo yeye. Tunapenda maisha ya uvuguvugu.
Mathayo 7:22 “Wengi wataniambia siku ile, Bwana, Bwana, hatukufanya unabii kwa jina lako, na kwa jina lako kutoa pepo, na kwa jina lako kufanya miujiza mingi?
23 Ndipo nitawaambia dhahiri, Sikuwajua ninyi kamwe; ondokeni kwangu, ninyi mtendao maovu”.
Biblia bado inatuonyesha siku ile atakapotokea mawinguni atawaua wanadamu wengi sana watakaokuwa wameipokea ile chapa ya mnyama na kufanya vita naye..
Ufunuo 19:13 “Naye amevikwa vazi lililochovywa katika damu, na jina lake aitwa, Neno la Mungu.
14 Na majeshi yaliyo mbinguni wakamfuata, wamepanda farasi weupe na kuvikwa kitani nzuri, nyeupe, safi.
15 Na upanga mkali hutoka kinywani mwake ili awapige mataifa kwa huo. Naye atawachunga kwa fimbo ya chuma, naye anakanyaga shinikizo la mvinyo ya ghadhabu ya hasira ya Mungu Mwenyezi.
16 Naye ana jina limeandikwa katika vazi lake na paja lake, MFALME WA WAFALME, NA Bwana WA MABwana”.
Unaweza kuona jinsi mwonekano wa Bwana utakavyokuwa wa tofauti sana wakati ule?. Ndio hapo utakapojua ni kwanini biblia inasema mataifa watamwombolezea, kwasababu hatakuja tena na sura ya upole kama wengi wetu tunavyodhani, bali atakuja na jina jipya la kifalme, la kuteka na kutawala, la kutiisha lenye nguvu nyingi. Sio tena la kuokoa mtu.
Lakini kwa upande wa pili, kwa wale waliomtii, waliokubali kutembea katika njia zake, anasema atawakiri, na kuona fahari kwa ajili yao mbele za Mungu na za malaika wake, vilevile atawapa mamlaka ya kutawala pamoja naye kama wafalme, Na atawafuta machozi watakatifu wake wote.
Hivyo ndugu, leo hii Kristo bado kaketi kama mwana-kondoo, aliyechinjwa, mpole, mnyenyekevu, aokoaye, anakuvuta kwa upole mwingi kwake, ili usiopote katika aungamivu wa ulimwengu. Angalia wakati huu umebakia mchache sana, kabla ya yeye kwenda kubadilisha ofisi yake. Kwanini usitubu umrudie muumba wako?
Damu yake bado ipo kukuokoa, na kukusamehe kabisa, mkaribishe leo kwenye moyo wako, akupe uwezo mpya wa kuushindwa huu ulimwengu. Pengine ulishamwamini au kumpokea lakini umekuwa mkristo vuguvugu mkristo jin, jambo ambalo ndio halitaki kabisa, amelikemea, hivyo toka kwenye huo uvuguvugu wako, toka katika udhehebu, mfuate Yesu kweli kweli, ondoa vizuizi vyote vinavyokufanya usiwe safi mbele za Mungu. Na yeye mwenyewe atakutengeneza na kukufanya uwe tayari kwa ajili ya kwenda kwenye unyakuo ambao upo karibuni kutokea.
Natumai sote tutaanzana kuuonyesha mabadiliko mapya. Kabla ya mabadiliko yake hayajajidhihirisha kwetu.
Bwana akubariki sana.
Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema,
Kwa maombezi/Ratiba za ibada/ Ushauri/ Maswali.
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312
pia kama utapenda uyapate mafundisho haya kwa njia ya Whatsapp au email basi tutumie ujumbe kwenye namba hizo hizo.
Mada Nyinginezo:
KARAMU YA MWANA-KONDOO.
UFUNUO: Mlango wa 2 part 3
UFUNUO: Mlango wa 14
ESTA: Mlango wa 8, 9 & 10. (SIKU KUU YA PURIMU)
UFUNUO: Mlango wa 19
Maganjo ni kitu kilichoharibiwa, kwa mfano jengo likiharibiwa labda tuseme kwa kombora, lile gofu linalobakia ndio maganjo. Au mji unapochomwa moto, yale masalia salia ya mji, ndio maganjo.
Mungu amekuwa akitumia Neno hili kuonyesha jinsi adhabu yake itakavyokuwa kwa wasiomcha yeye.
Hivi ni baadhi ya vifungu ambavyo utaweza kukutana na Neno hilo;
Walawi 26:30 “Nami nitapaharibu mahali penu palipoinuka, na kuziangusha sanamu zenu za jua, nami nitaitupa mizoga yenu juu ya mizoga ya sanamu zenu; na roho yangu itawachukia.
31 NAMI NITAIFANYA MIJI YENU IWE MAGANJO, na mahali penu patakatifu nitapatia ukiwa; wala sitasikia harufu ya manukato yenu yapendezayo.
32 Nami nitaitia hiyo nchi ukiwa; na adui zenu watakaokaa huko wataistaajabia”.
Ezekieli 6:14 “Nami nitanyosha mkono wangu juu yao, na kuifanya nchi kuwa MAGANJO, tena ukiwa mbaya kuliko jangwa upande wa Dibla, katika makao yao yote; nao watajua ya kuwa mimi ndimi Bwana”.
Yeremia 51:42 “Bahari imefika juu ya Babeli, Umefunikwa kwa wingi wa mawimbi yake.
43 Miji yake imekuwa MAGANJO; Nchi ya ukame, na jangwa; Nchi asimokaa mtu ye yote, Wala hapiti mwanadamu huko”.
Yeremia 4:7 “Simba ametoka katika kichaka chake, ndiye aangamizaye mataifa; ameanza kushika njia, ametoka katika mahali pake; ili aifanye nchi yako kuwa ukiwa, miji yako ifanywe MAGANJO, asibaki mwenyeji ndani yake. 8 Kwa sababu hiyo jifungeni nguo za magunia; ombolezeni na kulia kwa uchungu; kwa maana hasira kali ya Bwana haikugeuka na kutuacha”.
Som pia Ezekieli 12:20, 29:12, Amosi 9:14
Hata sasa, huu ulimwengu, utakwenda kufanywa maganjo kipindi si kirefu, haijalishi umejengwa vizuri kiasi gani, haijalishi umeshafikia hatua ya kuwa ustaarabu mzuri namna gani,..Bwana Yesu alisema kuwa hakuna jiwe litakalosalia juu ya jiwe. Kila kitu unachokiona leo hii kitateketezwa, siku ile ya Bwana itakapofika. Kila kitu kitafumuliwa, moto utaisafisha kweli kweli hii dunia, kama vile gharika ilivyoisafisha dunia ya kwanza wakati ule wa Nuhu.
Soma.
2Petro 3:10 “Lakini siku ya Bwana itakuja kama mwivi; katika siku hiyo mbingu zitatoweka kwa mshindo mkuu, na viumbe vya asili vitaunguzwa, na kufumuliwa, na nchi na kazi zilizomo ndani yake zitateketea.
11 Basi, kwa kuwa vitu hivi vyote vitafumuliwa hivyo, imewapasa ninyi kuwa watu wa tabia gani katika mwenendo mtakatifu na utauwa,
12 mkitazamia hata ije siku ile ya Mungu, na kuihimiza; ambayo katika hiyo mbingu zitafumuliwa zikiungua, na viumbe vya asili vitateketea na kuyeyuka”?
Swali ni je! Mimi na wewe tumeekeza wapi maisha yetu? Je ni duniani au mbinguni?..Kumbuka duniani ni tunapita, yapo maisha ya milele huko mbeleni yanatungojea.. Ni wajibu wetu kutambua lililo la muhimu kwanza, ambalo ni wokovu wetu, Lengo la Mungu kuifanya hii dunia kuwa maganjo si kwamba ni mbaya hapana, bali sisi ndio tumeifanya kuwa mbaya kwa dhambi zetu, na hivyo ni lazima iteketezwe tu.
Hivyo sisi sote tusiwe washirika wa hiyo ghadhabu ya Mungu. Kumbuka Unyakuo upo mlangoni. Na haya mambo hatutashangaa kuyaona yakitimia hata kwenye kizazi chetu.
Shalom.
Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema,
Kwa maombezi/Ratiba za ibada/ Ushauri/ Maswali.
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312
pia kama utapenda uyapate mafundisho haya kwa njia ya Whatsapp au email basi tutumie ujumbe kwenye namba hizo hizo.
Mada Nyinginezo:
Nakusalimu katika jina la Bwana na mwokozi wetu Yesu Kristo, ambaye yeye peke yake ndiye Mungu, aliyeshuka katika mwili wa kibinadamu kutukomboa sisi.
Yapo mambo ambayo hatuwezi kudhania kama Bwana Yesu angeyafanya alipokuwa hapa duniani.. Japo alikuja kweli kutuokoa, lakini hakuufanya wokovu kuwa mrahisi kiivyo kama wengi tunavyodhani.
Yesu havutiwi na wingi wa watu wanaokuja kumsikiliza, au wanaosema wanamfuata, hilo halimshawishi hata kidogo kutoa siri zake zote za wokovu. Wakati ule kulikuwa na umati mkubwa wa watu, ambao walikuwa wakimfuata kila mahali, wengine mpaka wanakanyagana, sasa unaweza kudhani Bwana angetumia fursa ile, kuwapa siri za Mungu wazi wazi.. Lakini biblia inatuambia hilo hakulifanya, badala yake alizungumza nao kwa mifano (yaani mafumbo). Na kama unavyojua mafumbo huwa hayampi tu majibu ya moja kwa moja, ikiwa na maana kuwa mtu anaweza akatoka hapo asipate jibu la wazo lako kama hatofikiria sana, au kutaka kuambiwa maana yake.. Unaweza kujiuliza kwanini afanye vile?
Bwana Yesu hataki kuwaokoa watu wasiomaanisha kweli kuutaka wokovu ndani ya mioyo yao. Haokoi wasikilizaji tu, bali watu wanaotaka kuelewa nini maana ya wokovu na wokovu huo unapatikanaje ndani ya mioyo yao. Na ndio maana alizungumza nao kwanza kwa mafumbo, na baadaye akawaambia wanafunzi wake kauli hii .”kwa wale walio nje, YOTE hufanywa kwa mifano”..Unaona? Hakusema “machache” hapana, bali YOTE.. Ikiwa na maana hakuna kufananuliwa chochote, ikiwa upo mbali na Kristo. Habari za Kristo zitakuwa mafumbo tu kwako, haijalishi wewe unamfuata kwenye mikutano yake, au unahudhuria semina zake nyingi kiasi gani.
Watu wengi waliomfuata Kristo walikuwa ni watembeleaji tu, wengine walimtafuta kwa ajili miujiza, wengine kama wapelelezi, wengine wasikilizaji tu wa kupoteza muda ili uende, wengine ni kuutazama mwonekano wake upoje, anavaaje,n.k…Hayo tu, hawana cha ziada..Wachache sana ndio waliokuwa wanatafuta kumjua yeye kwa kile alichokileta duniani, na ndio hao ambao baada ya mafundisho kuisha, walijiona nafsini mwao hakuna chochote walichokipata, zaidi ya stori stori tu, hakuna lolote lililowajengwa rohoni, ndipo wakamfuata akiwa peke yake, katika utulivu wakamwomba awafunulie siri za mifano ile… Hao ndio Yesu alikuwa amewakusudia wokovu.
Marko 4:10 “Naye alipokuwa peke yake, wale watu waliomzunguka, na wale Thenashara, walimwuliza habari za ile mifano.
11 Akawaambia, Ninyi mmejaliwa kuijua siri ya ufalme wa Mungu, BALI KWA WALE WALIO NJE YOTE HUFANYWA KWA MIFANO,
12 ili wakitazama watazame, wasione; Na wakisikia wasikie, wasielewe; Wasije wakaongoka, na kusamehewa”
Leo hii, upo umati mkubwa sana katika kanisa, upo umati mkubwa sana wanaosema wanamtafuta Mungu kila mahali,.Wakidhani Yesu anavutiwa na kumtembelea kwao.
Hilo halipo, ikiwa mtu mwenyewe binafsi hataki kumtafuta Kristo akiwa peke yake, amsaidie, hataki kuonyesha bidii yake kwa Kristo kujifunza na kumtafakari, kukitendea kazi kile alichokisikia, asahau kuupokea wokovu wake halisi wa kweli kweli.
Na ndio maana leo hii, utaona wokovu hauna nguvu yoyote ndani ya mioyo ya baadhi ya watu, mtu atasema ameokoka, lakini uzinzi unamshinda, ulevi unamshinda. Amekaa miaka mingi katika kanisa lakini hajui hata kama kuna jambo linaloitwa Unyakuo, hajui kama hili kanisa tunaloishi ndio kanisa la mwisho, lijulikanalo kama LAODIKIA kulingana na maandiko (Ufunuo 3), na kwamba hakutakuwa na kanisa lingine zaidi ya hili, hajui mpango wa Mungu kwa kanisa lake kwa wakati huu tunaoishi ni nini? Lakini atasema anamjua Kristo, na amemwona. Hajui kuwa hata watu wa kipindi kile walimwona Yesu, wakala naye, wakasikia sauti yake, wakaona miujiza yake mingi, lakini aliowafunulia siri za ufalme wa mbinguni ni wachache sana. Wale waliokwenda kutendea kazi kile walichokisikia.
Ndugu Bwana Yesu anawaokoa watu waliomaanisha kweli kweli, sio wasikilizaji tu, wasio na bidii yoyote, miaka nenda rudi, ni wasikilizaji tu wa mahubiri, makanisani, mitandaoni, n.k., huwajishughulishi kwa lolote kumtafuta Yesu binafsi, wakidhani kuwa Yesu amewafunulia tayari siri zake.
Huu wakati sio wa kuwa vuguvugu, ni wakati wa kujitwika msalaba wako na kumfuata YESU. Kumbuka alisema..
Mathayo 16:24 “Wakati huo Yesu aliwaambia wanafunzi wake, Mtu ye yote akitaka kunifuata, na ajikane mwenyewe, ajitwike msalaba wake, anifuate.
25 Kwa kuwa mtu atakaye kuiokoa nafsi yake, ataipoteza; na mtu atakayepoteza nafsi yake kwa ajili yangu, ataiona.
26 Kwani atafaidiwa nini mtu akiupata ulimwengu wote, na kupata hasara ya nafsi yake? Au mtu atatoa nini badala ya nafsi yake”?
Vinginevyo, tukiwa watu wasiomaanisha, kama wale makutano, tujue kuwa YOTE, ya Yesu, tutayasikia tu kama mifano.
Maran Atha.
Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema,
Kwa maombezi/Ratiba za ibada/ Ushauri/ Maswali.
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312
pia kama utapenda uyapate mafundisho haya kwa njia ya Whatsapp au email basi tutumie ujumbe kwenye namba hizo hizo.
Mada Nyinginezo:
Biblia ina maana gani inaposema akonyezaye kwa jicho huleta masikitiko?
JIBU: Tusome,
Mithali 10:10 “Akonyezaye kwa jicho huleta masikitiko; Bali mpumbavu mwenye maneno mengi ataanguka”.
Kukonyeza ni ishara inayojulikana kama ya undanganyifu au ya kupoteza uaminifu. Ni jambo la kawaida tumekuwa tukiliona hata katika maisha ya kawaida, kwa mfano, labda mteja, mmoja amekwenda kununua bidhaa Fulani kwa muuzaji sokoni, Sasa ikatokea, ghafla muuzaji mwingine akakatiza anauza bidhaa kama ile ile, Ni kawaida ya mnunuzi kutaka kuulizia bei halisi ya hiyo bidhaa kwa muuzaji mwingine, Sasa kama kweli yule muuzaji wa kwanza aliambiwa bei halali ,hatoonyesha chochote, lakini kama alitaka kumuuzia kwa bei ya juu Zaidi kuliko ilivyo kawaida, yule muuzaji wa kwanza atatumia ishara Fulani, aidha kumkonyeza muuzaji mwenzake, ili akae kimya..Asimwambie bei halali.
Sasa hiyo ni dalili ya kukosa uaminifu.
Mfano mwingine, utakuta labda mtu na familia yake wamealikwa kwenye sherehe fulani, na kule kwenye sherehe pengine baba wa familia hiyo akakutana na wanawake wengine wazuri, akawatamani, sasa njia ambayo anaweza kutumia kuwasiliana nao, kirahisi ili pengine baadaye wakutane, ni kwa kumkonyeza,..Huo ni mfano tu.
Umeona kitendo hicho kimetumika kama ishara ya udanganyifu.
Biblia inasema..
Mithali 6:12 “Mtu asiyefaa kitu, mtu wa uovu; Huenda njiani mwenye kinywa cha upotofu.
13 HUKONYEZA KWA MACHO, hunena kwa miguu, Huwaashiria watu kwa vidole vyake”
Na kukonyeza kwa siku hizi kumezidi hata kule kunakojulikana kwa kutumia jicho, zipo ishara nyingi za kukonyeza inategemea na mahali husika. Wakati mwingine hata lugha Fulani inaweza kutumika kukonyeza.
Sasa biblia inasema watu wa namna hiyo huleta masikitizo. Na masikitizo hayo huja kote kote, kwake, pamoja na kwa yule aliyemkonyeza. Ikiwa na maana mwisho wake hauwi mzuri sikuzote. Ni uchungu na majuto.
Biblia inatuonya tusiwe watu wa hila, za kutumia ishara za udanganyifu kuleta madhara, au uharibifu kwa wengine.
Hilo ni kosa.
Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema,
Kwa maombezi/Ratiba za ibada/ Ushauri/ Maswali.
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312
Jiunge na kundi letu la mafundisho ya Biblia whatsapp kwa kubofya hapa > Group-whatsapp
Mada Nyinginezo:
SWALI: tukisoma 2Mambo ya Nyakati 22:2.Inasema Hivi..
“Ahazia alikuwa na umri wa miaka AROBAINI NA MIWILI ALIPOANZA KUTAWALA; akatawala mwaka mmoja huko Yerusalemu; na jina la mamaye aliitwa Athalia binti Omri”.
NA tena Tukisoma 2Wafalme 8:26 inasema Hivi..
“;Ahazia alikuwa na umri wa miaka ISHIRINI NA MIWILI ALIPOANZA KUTAWALA; akatawala mwaka mmoja huko Yerusalemu. Na jina la mamaye aliitwa Athalia binti Omri mfalme wa Israeli”.
>>Hapa sijaelewa Kwenye Hizi Habari Kwa maana Kwenye 2Nyakati unasema Ahazia alianza kutawala akiwa na miaka 42 ila Kwenye 2Wafalme Inasema Ahazia alianza kutawala Akiwa na miaka 22..Naona Hii mistari Kama Inajipinga Yenyewe.
Umri hasaa wa Ahazia alipoanza kutawala ni upi?
JIBU: Vifungu hivyo vinaonekana kama vinajipinga, aidha kimojawapo kimekosewa au vyote, wengine wanasema ni hitilafu katika uchapishaji wa maandiko ya kale. Lakini kama ingekuwa ni hitilafu kwenye uchapishaji, ni wazi kuwa tangu zamani Wayahudi wangeshaliona hilo na kulirekebisha, kwasababu wale wapo makini sana katika uandishi wao, hususani katika mambo matukufu ya Mungu, lakini maandiko hayo yalikuwepo hivyo hivyo kwa maelfu ya miaka mbeleni. Na hawakuona hitilafu yoyote.
Lakini swali ni je, Ahazia alianza kutawala akiwa na umri wa miaka mingapi?
Ukweli ni kwamba alianza kutawala akiwa na miaka 22, kwasababu kama angekuwa ameanza kutawala akiwa na miaka 42, maandiko yangekuwa yamekosewa kwasababu utawala wa baba yake uliisha akiwa na umri wa miaka 40 (Soma 2Wafalme 8:17, 2Nyakati 21:20) . Hivyo, kama Ahazi angekuwa ameanza kutawala akiwa na umri wa miaka 42 basi angekuwa amemzidi baba yake kwa umri wa miaka 2 zaidi jambo ambalo haliwezekani kabisa.
Lakini ni kwanini, sehemu nyingine ionyeshe alianza kutawala akiwa na miaka 22, na sehemu nyingine miaka 42?
Zipo thathimini nyingi, lakini tukitazama historia fupi ya baba yake huyu Ahazia itatupa mwanga kidogo wa kuelekewa kwenye jibu letu. Baba yake huyu Ahazia aliitwa, Yehoramu. Yehoramu alikuwa ni mtawala mbaya sana mwenye uchu wa madaraka na ubinafsi, kwani hata Baba yake (Yehoshafati) alipokufa, licha ya kwamba aliwaachia mali nyingi yeye pamoja na ndugu zake, lakini pamoja na hayo alikwenda kuwaua wote, ili yeye avimiliki vyote.
Tendo hilo la kumwaga damu zisizokuwa na hatia za kuwaua ndugu zako, lilimuhuzunisha sana Mungu, ndipo Mungu akamlaani kwa kumpiga na ugonjwa huo usiokuwa na tiba wa kutokwa na utumbo.
Hivyo, hilo lilimfanya asiweze, kutawala vema katika hali ile ya kuugua..akawa kama mtu wa kukaa ndani tu aliyetengwa.
Sasa kumbuka na biblia haieleze kama alikufa kwanza ndipo mtoto wake, akachukua ufalme, hapana, inasema, alianza kutawala akiwa na miaka32, kisha akatawala miaka 8 tu. Lakini haisemi kwamba alikufa, hapana, kwahiyo pengine aliendelea kuishi, kwa kipindi kingine mbele akiwa kama mfalme asiyekuwa na kazi yoyote.
Hiyo ikapelekea wenyewe wa Yerusalemu kumfanya mwanawe kuwa mfalme, hivyo Ahazia akawa mfalme akiwa na umri wa miaka 22, lakini hakuwa mfalme kamili kabisa,kwasababu baba yake alikuwa bado hajafa. Ndipo alipokuja kufa huko mbeleni, Ahazia tayari alikuwa ameshafikisha umri wa miaka 42, ndipo wakamfanya kuwa mfalme kamili wa Yerusalemu. Akatawala miaka mmoja tu. Ambao ulianza kuhesabiwa katika umri wake wa 42
Hivyo biblia inaposema alianza kutawala akiwa na miaka 22 katika kitabu cha Wafalme, na miaka 42 katika kitabu cha Mambo ya Nyakati, biblia haijipingi, ni pengine tumekosa historia ya kutosha ya matukio yote ndani ya biblia ndio maana tunaona kama baadhi ya vifungu vimekosewa, lakini ukweli ni kwamba maandiko matakatifu hakuna mahali yalipokosewa..
Bwana akubariki.
Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema,
Kwa maombezi/Ratiba za ibada/ Ushauri/ Maswali.
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312
pia kama utapenda uyapate mafundisho haya kwa njia ya Whatsapp au email basi tutumie ujumbe kwenye namba hizo hizo.
Mada Nyinginezo:
Je! Ni ipi tarehe sahihi Evil-merodaki alimtoa Yekonia gerezani?
Biblia ilimaanisha nini iliposema “Mwanamke atamlinda mwanamume” Yeremia 31:22?
JIBU: Tusome,
Yeremia 31:22 “Hata lini utatanga-tanga, Ee binti mwenye kuasi? Kwa maana Bwana ameumba jambo jipya duniani; mwanamke atamlinda mwanamume”.
Katika biblia hususani agano la kale utaona sehemu nyingi, Mungu akilifananisha Taifa la Israeli na mwanamke aliyeolewa, na Bwana Mungu mwenyewe akijifananisha kama Mume wa Taifa hilo, Ndio maana mwanzo kabisa katika zile amri kumi alizozitoa Mungu, alianza na kusema yeye ni Mungu mwenye “Wivu”, wivu unaozungumziwa hapo ni wivu wa mwanaume kwa mke wake.
Kwahiyo popote pale Israeli ilipoasi na kumwacha Mungu na kwenda kuabudu miungu mingine, katika roho ilitafsirika kama ni mwanamke aliyemwacha mumewe na kwenda kufanya uzinzi nje ya ndoa. Kwahiyo Taifa la Israeli lilifananishwa na mwanamke aliyeolewa, au binti aliyeposwa.. unaweza kusoma hayo binafsi katika mistari ifuatayo. (Isaya 54:5, Yeremia 3:1-14, Yeremia 13:27, 1Nyakati 5:25, Hosea 3:1-5, Zaburi 106: 33-41, Ezekieli 23:21-29).
Kwa msingi huo, tunaweza kurudi kusoma Yeremia 31:22 “Hata lini utatanga-tanga, Ee binti mwenye kuasi? Kwa maana Bwana ameumba jambo jipya duniani; mwanamke atamlinda mwanamume”.
Hapo mwanamke anayezungumziwa ni Israeli (Yaani Taifa la Mungu), Huyo ndiye binti mwenye kuasi, kwanini ametajwa kama binti mwenye kuasi, ni kwasababu alikuwa amemwacha Mungu ambaye ndiye mume wake na kwenda kutanga-tanga kuabudu miungu mingine.
Sasa hapo anasema Bwana ameumba jambo jipya.. “mwanamke atamlinda mwanamume”..maana yake hapo kale ni “mwanamume ndiye aliyekuwa anamlinda mwanamke”. Sasa kulinda kunapozungumziwa hapo sio ulinzi dhidi ya maadui, La!. Bali ulinzi wa kimapenzi. Maana yake katika jambo hilo jipya, Mwanamke atakuwa na wivu mwingi juu ya mume wake, Maana yake atakapoona mumewe kamwacha, atajisikia vibaya na wala hataruhusu hilo jambo, wakati wote atatamani awe karibu na mume wake kuliko kawaida, hatoruhusu mahusiano yake yaharibike kwa vyovyote vile. Tofauti na hapo kwanza ambapo Mwanamume ndiye aliyekuwa anatia bidii kumlinda mkewe.
Sasa tafsiri yake katika roho ni kwamba wakati utafika ambapo Taifa la Mungu ambalo linafananishwa na mwanamke, litakuwa linampenda Mungu sana, na kumtafuta, na kumwonea Mungu wivu lenyewe..Maana yake Mungu ataweka kitu ndani ya watu wake ambacho kitawafanya wao wenyewe watafute kumpenda Mungu sana na kwa bidii. Ndio maana mbele kidogo katika hiyo hiyo sura ya 31, ya kitabu hicho hicho, utaona Bwana Mungu analiweka hilo sawa, kwamba itakuwaje.
Tusome..
Yeremia 31:31 “Angalia, siku zinakuja, asema Bwana, nitakapofanya agano jipya na nyumba ya Israeli, na nyumba ya Yuda.
32 Si kwa mfano wa agano lile nililolifanya na baba zao, katika siku ile nilipowashika mkono, ili kuwatoa katika nchi ya Misri; ambalo agano langu hilo walilivunja, ingawa nalikuwa MUME KWAO, asema Bwana.
33 Bali agano hili ndilo nitakalofanya na nyumba ya Israeli, baada ya siku zile, asema Bwana; Nitatia sheria yangu ndani yao, na katika mioyo yao nitaiandika; nami nitakuwa Mungu wao, nao watakuwa watu wangu.
34 Wala hawatamfundisha kila mtu jirani yake, na kila mtu ndugu yake, wakisema, Mjue Bwana; kwa maana watanijua wote, tangu mtu aliye mdogo miongoni mwao hata aliye mkubwa miongoni mwao, asema Bwana; maana nitausamehe uovu wao, wala dhambi yao sitaikumbuka tena”.
Umeona hapo?..Mstari wa 32 anasema “ingawa nalikuwa mume kwao”. Lakini agano lake walilivunja…Lakini katika agano hilo jipya, wao wenyewe watamtafuta Mungu, hawatahitaji tena kusukumwa sukumwa. Kuna kitu kitaingia ndani yao ambacho kitawafanya waulinde upendo kwa Mungu wao.
Na agano hili jipya, au “jambo jipya” lilianza siku ile ya Pentekoste ambapo Roho Mtakatifu alishuka katikati ya watu wake, siku hii, ndipo wakati ambapo Mungu alianza kutia sheria ndani ya mioyo ya watu, kiasi kwamba kwa yeyote ambaye atapokea Roho Mtakatifu, hatahitaji tena kusukumwa sukumwa katika kumtafuta Mungu, kuna kiu Fulani ya kipekee itaingia ndani yake, hiyo itampeleka mwenyewe kumtafuta Mungu, atajikuta tu anatafuta kuulinda uhusiano wake na Mungu usipotee (Hapo anamlinda mwanamume wake yaani Yesu), hatahitaji kuambiwa na Mungu hapaswi kujichubua, hapaswi kuiba, hapaswi kubeti, hapaswi kuvaa nguo nusu utupu, kwani ndani yake tayari ipo sheria, iliyoingia, ambayo inamshuhudia kabisa kwamba anapovaa mavazi yasiyompasa anafukuza uwepo wa Mungu ndani yake.
Kwahiyo kwa mtu aliyepokea Roho Mtakatifu, tayari jambo jipya limeumbika ndani yake. Na biblia inasema wote wasio na Roho Mtakatifu hao sio wake (Warumi 8:9). Na habari nzuri ni kwamba Roho Mtakatifu sio wa watu baadhi tu Fulani. La!.. Bali ni zawadi kwa wote ambao wanamkimbilia Bwana.
Matendo 2:39 “Kwa kuwa ahadi hii ni kwa ajili yenu, na kwa watoto wenu, na kwa watu wote walio mbali, na kwa wote watakaoitwa na Bwana Mungu wetu wamjie”.
Kwahiyo tunaishi katika siku ambazo ili kumpendeza Mungu ni lazima tuwe na Roho Mtakatifu. Swali ni je! Jambo jipya limeumbika moyoni mwako?..Je kuna nguvu inayokusukuma kwa Mungu? Je kuna hofu ya Mungu ndani yako ambayo inakufanya uhakikishe unaulinda wokovu wako?..Kama ndiyo basi usimzimishe huyo Roho aliyeko ndani yako, kwasababu huyo ndio Muhuri wa Mungu kwetu (Waefeso 4:30). Lakini kama hiyo nguvu haipo ndani yako, basi unaihitaji leo kwasababu pasipo Roho kamwe hatuwezi kumkaribia Mungu.
Hivyo kama unataka kumpokea Roho Mtakatifu maishani mwako, ni sharti kwanza umwamini Yesu maishani mwako, kwamba alikuja kufa kwaajili ya dhambi zako, na pia akafufuka, na sasa anaishi. Na baada ya hapo, tubu dhambi zako zote kwa kumaanisha kuziacha, hakikisha unaziacha kwa vitendo, maana yake kama ulikuwa unaiba unaacha kuiba,kama ulikuwa mzinzi unaacha uzinzi, kama ulikuwa unaufuata ulimwengu huu, unaacha. Na baada ya hapo Roho Mtakatifu ataanza kukupa amani, ambayo itakamilika baada ya wewe kwenda kubatizwa ubatizo sahihi, kama bado hujabatizwa. Ubatizo sahihi ni ule wa kuzama kwenye maji tele na kwa jina la Yesu Kristo (Matendo 2:38, 8:16, 10:48, 19:10).
Bwana akubariki.
Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema,
Kwa maombezi/Ratiba za ibada/ Ushauri/ Maswali.
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312
pia kama utapenda uyapate mafundisho haya kwa njia ya Whatsapp au email basi tutumie ujumbe kwenye namba hizo hizo.
Mada Nyinginezo:
Shubaka ni dirisha, lililojengwa kwa kupishanisha vipande vya mbao au chuma au kitu kingine chochote, kama pazia, katikati ya dirisha hilo. Tazama picha.
Ujenzi wa madirisha mengi ya kisasa, Haupo kwa muundo huo. Madirisha ya kisasa, yapo wazi sana, nikiwa na maana huwezi kuona kitu chochote kimekatiza katikati,pengine utakuta ni kioo tupu eneo lote, lakini kwa zamani madirisha ya shubaka yalikuwa ni kawaida kuyakuta karibu katika nyumba zote.
Neno hilo kwenye biblia utalipata katika habari hii;
Mithali 7:4 “Mwambie hekima, Wewe ndiwe umbu langu; Mwite ufahamu jamaa yako mwanamke.
5 Wapate kukulinda na malaya, Na mgeni akubembelezaye kwa maneno yake.
6 Maana katika dirisha la nyumba yangu Nalichungulia katika SHUBAKA YAKE;
7 Nikaona katikati ya wajinga, Nikamtambua miongoni mwa vijana, Kijana mmoja asiyekuwa na akili,
8 Akipita njiani karibu na pembe yake, Akiishika njia iendayo nyumbani kwake, 9 Wakati wa magharibi, wakati wa jioni, Usiku wa manane, gizani.
10 Na tazama, mwanamke akamkuta, Ana mavazi ya kikahaba, mwerevu wa moyo;
11 Ana kelele, na ukaidi; Miguu yake haikai nyumbani mwake.
12 Mara yu katika njia kuu, mara viwanjani, Naye huotea kwenye pembe za kila njia.
13 Basi akamshika, akambusu, Akamwambia kwa uso usio na haya,
14 Kwangu ziko sadaka za amani; Leo hivi nimeziondoa nadhiri zangu;
15 Ndiyo maana nikatoka nikulaki, Nikutafute uso wako kwa bidii, nami nimekuona.
16 Nimetandika kitanda changu, magodoro mazuri, Kwa matandiko ya Kimisri yenye mistari.
17 Nimetia kitanda changu manukato, Manemane na udi na mdalasini.
18 Haya, na tushibe upendo hata asubuhi, Tujifurahishe nafsi zetu kwa mahaba. 19 Maana mume wangu hayumo nyumbani, Amekwenda safari ya mbali;
20 Amechukua mfuko wa fedha mkononi; Atarudi wakati wa mwezi mpevu.
21 Kwa maneno yake mengi na ulaini akamshawishi, Kwa ubembelezi wa midomo yake akamshinda.
22 Huyo akafuatana naye mara hiyo, Kama vile ng’ombe aendavyo machinjoni; Au mpumbavu kuadhibiwa katika pingu;
23 Hata mshale umchome maini; Kama ndege aendaye haraka mtegoni; Wala hajui ya kuwa ni hasara ya nafsi yake.
24 Basi, wanangu, nisikilizeni sasa, Mkayaangalie maneno ya kinywa changu.
25 Moyo wako usizielekee njia zake, Wala usipotee katika mapito yake.
26 Maana amewaangusha wengi waliojeruhi, Naam, jumla ya waliouawa naye ni jeshi kubwa.
27 Nyumba yake ni njia ya kwenda kuzimu, Hushuka mpaka vyumba vya mauti”.
Hiyo ni kutukumbusha kuwa, Mungu pia, anatutazama kutoka juu mbinguni akiyaangalia matendo yetu, na mienendo yetu katika madirisha na shubaka zake mbinguni, yeye ndiye anayechunguza na kujua siri zote za mioyo ya watu, na mwisho wake utakuwaje. Hivyo ni wajibu wetu tusiwe wajinga kama yule kijana, bali tuikwepe mitego ya ibilisi kwa kuzishika amri za Mungu na kuziishi.
Shalom.
Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema,
Kwa maombezi/Ratiba za ibada/ Ushauri/ Maswali.
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312
Jiunge na kundi letu la mafundisho ya Biblia whatsapp kwa kubofya hapa > Group-whatsapp
Mada Nyinginezo:
SWALI: Naomba kuuliza watumishi wa Mungu katika Mwanzo 17:20 anaposema kwa habari ya Ishmaeli atazaa maseyidi 12, hao ndio akina nani kwa Sasa?
2) Pia katika 1samweli 3:3 anasema kipindi Samweli anaitwa na Mungu taa ilikua haijazimika bado Nia taa gani hiyo? Asante Sana Ni hayo.
JIBU:
Mwanzo 17:18 “Ibrahimu akamwambia Mungu, Lau kwamba Ishmaeli angeishi mbele yako.
19 Mungu akasema, Sivyo, lakini Sara mkeo atakuzalia mwana wa kiume, nawe utamwita jina lake Isaka. Nami nitafanya agano langu imara kwake kuwa agano la milele kwa ajili ya uzao wake baada yake.
20 Na kwa habari za Ishmaeli nimekusikia, nimembariki, nitamzidisha, nami nitamwongeza sana sana. Atazaa maseyidi kumi na wawili, nami nitamfanya awe taifa kuu”.
Neno Seyidi linamaanisha mtawala, hivyo hapo biblia ilimaanisha kuwa Ishmaeli atazaa watawala 12.. ambao utaona wakitajwa kwa majina katika Mwanzo 25:13
Mwanzo 25:13 “Na haya ndiyo majina ya wana wa Ishmaeli, kwa majina yao, na kwa vizazi vyao. Mzaliwa wa kwanza wa Ishmaeli, ni Nebayothi, na Kedari, na Abdeeli, na Mibsamu,
14 na Mishma, na Duma, na Masa,
15 na Hadadi, na Tema, na Yeturi, na Nafishi, na Kedema.
16 Hao ndio wana wa Ishmaeli, na hayo ni majina yao, katika miji yao, na katika vituo vyao, maseyidi kumi na wawili kwa kufuata jamaa zao.
Katika historia wana hawa wa Ishmaeli walikuwa watu wakuu sana, na ndio chimbuko la mataifa ya kiharabu tunayoyaona sasahivi kule mashariki ya kati.
2) Je ni Taa ipi hiyo inayozungumizwa katika 1Samweli 3:1?,
Tusome.
1 Samweli 3:1 “Basi, mtoto Samweli akamtumikia Bwana mbele ya Eli. Na neno la Bwana lilikuwa adimu siku zile; hapakuwa na mafunuo dhahiri.
2 Ikawa wakati huo, Eli alipokuwa amelala mahali pake (tena macho yake yalikuwa yameanza kupofuka, hata asiweze kuona),
3 na taa ya Mungu ilikuwa haijazimika bado, na Samweli alikuwa amelala katika hekalu la Bwana, palipokuwa na sanduku la Mungu;
Inadhaniwa kuwa hiyo ni ile taa ya hekaluni, lakini ukitafakari kwa ukaribu, utaona kuwa biblia haikumaanisha ile taa ya hekaluni au ile ya kwenye hema ya kukutania, bali ilimaanisha pumzi au uhai wa Eli, ukikumbuka kuwa habari iliyokuwa inazungumziwa hapo juu ni kuhusu uzee wa Eli, ambapo inasema umri wake ulikuwa umeshaenda sana mpaka macho yake yalikuwa yameshaanza kupofuka.
Biblia inasema..
Mithali 20:27 “Pumzi ya mwanadamu ni taa ya Bwana; Hupeleleza yote yaliyomo ndani yake”.
Unaona? Hivyo hapo ilimaanisha kuwa Pumzi ya uhai wa Eli ilikuwa bado haijamuacha.
Hiyo ni kutukumbusha pia, kuwa upo wakati na sisi Taa ya Mungu itazima ndani yetu. Na kama tunavyojua taa ikizimika huwa kunakuwa na giza na sikuzote gizani hakuna shughuli yoyote inayoendelea. Vivyo hivyo na siku ambayo kila mmoja wetu atakufa, huko atakapoenda hakuna jambo lolote la kimaendeleo atakalolifanya, Hatakuwa na nafasi ya pili ya kutubu ikiwa alikufa katika dhambi, hatakuwa na nafasi ya pili ya kufanya marekebisho ikiwa alizembea zembea katika masuala ya wokovu wake akiwa hapa duniani. Atakachokuwa anasubiria huko ni hukumu tu.
Mhubiri 9:5 “kwa sababu walio hai wanajua ya kwamba watakufa; lakini wafu hawajui neno lo lote, wala hawana ijara tena; maana kumbukumbu lao limesahauliwa”.
Hivyo tunapaswa tujithamini maisha yetu tunamalizaje mwendo tukiwa hapa duniani? . Kwasababu huko ng’ambo hakuna nafasi ya pili.
Bwana akubariki.
Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema,
Kwa maombezi/Ratiba za ibada/ Ushauri/ Maswali.
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312
Jiunge na kundi letu la mafundisho ya Biblia whatsapp kwa kubofya hapa > Group-whatsapp
Mada Nyinginezo:
SWALI: Biblia inamaanisha nini iliposema “wakidhania kuwa ulevi wakati wa mchana ni anasa;?
JIBU: Tusome vifungu vyenyewe..
2Petro 2:12 “Lakini hao kama wanyama wasio na akili, ambao walizaliwa kama wanyama tu wa kukamatwa na kupotezwa, wakikufuru katika mambo wasiyoyajua, wataangamizwa katika maangamizo yao;
13 Wakipatikana na madhara, ambayo ni ujira wa udhalimu wao, WAKIDHANIA KUWA ULEVI WAKATI WA MCHANA NI ANASA; wamekuwa ni mawaa na aibu wakifuata anasa zisizo kiasi katika karamu zao za upendo, wafanyapo karamu pamoja nanyi”;
Hapa Mtume Petro, alikuwa anaeleza jinsi watu waovu wanavyoenenda katika tamaa za mwili, ukisoma tokea juu utaona akiwafananisha na watu wa Sodoma na Gomora..Na moja ya tabia zao ndio hiyo aliyosema “Wakidhania kuwa ulevi wakati wa mchana ni anasa” akiwa na maana kuwa, wamefikia hatua ambayo kwao anasa zao kama ulevi hawazifanyi tena usiku, bali hata mchana.
Ikumbukwe kuwa anasa zote huwa zinajulikana kuwa zinafanyika usiku.. Na ndio maana wakati ule wa Pentekoste, Roho aliposhuka, wale watu waliwashutumu mitume kuwa wamelewa kwa mvinyo, Lakini Petro aliwaaambia, hakuna aliyelewa, kwasababu sasa hivi ni saa tatu ya mchana (akiwa na maana ni saa 9 alasiri), hakuna mtu anayelewa muda huo.
Matendo 2:13 “Wengine walidhihaki, wakisema, wamelewa kwa mvinyo mpya.
14 Lakini Petro akasimama pamoja na wale kumi na mmoja, akapaza sauti yake, akawaambia, Enyi watu wa Uyahudi, na ninyi nyote mkaao Yerusalemu, lijueni jambo hili, mkasikilize maneno yangu.
15 Sivyo mnavyodhani; watu hawa hawakulewa, kwa maana ni saa tatu ya mchana”;
Soma pia..
1Wathesalonike 5:7 “Maana walalao usingizi hulala usiku, pia na walewao hulewa usiku”.
Umeona, hivyo mpaka mtu imetokea anafanya anasa kama ulevi wakati wa mchana,. Ni mtu aliyevuka mipaka, haoni tena shida kufanya mambo yake maovu hadharani amewazidi hata wenye dhambi wengine wafanyao mambo kama hayo.Ndivyo walivyofanya watu wa Sodoma na Gomora, walivuka mipaka waliuanika ushoga wao hadharani, bila aibu yoyote.
Ni kama vile tu leo hii, hakuna staha tena duniani, mambo ya giza yanafanyika wazi kwenye matamasha, kwenye TV, yanatumwa Whatsapp, yanaonekana Youtube na kwenye mitaa yetu.
Hii ni kuonyesha kuwa tunaishi katika majira ya kurudi kwa pili kwake Yesu Kristo. Wakati huu ni wa kuilinda mioyo yetu isilemewe na mambo ya kidunia, kama alivyofanya Lutu alivyokuwa Sodoma. Kwasababu ulimwengu huu utakwenda kuangamizwa kwa moto muda si mrefu, kama mtume Petro alivyomalizia kusoma katika waraka huo.
2Petro 3:10 “Lakini siku ya Bwana itakuja kama mwivi; katika siku hiyo mbingu zitatoweka kwa mshindo mkuu, na viumbe vya asili vitaunguzwa, na kufumuliwa, na nchi na kazi zilizomo ndani yake zitateketea.
11 Basi, kwa kuwa vitu hivi vyote vitafumuliwa hivyo, imewapasa ninyi kuwa watu wa tabia gani katika mwenendo mtakatifu na utauwa,
12 mkitazamia hata ije siku ile ya Mungu, na kuihimiza; ambayo katika hiyo mbingu zitafumuliwa zikiungua, na viumbe vya asili vitateketea na kuyeyuka?”
Je umeokoka? Je parapanda ikilia leo unaouhakika wa kwenda mbinguni?. Majibu sote tunayo.
Maran Atha.
Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema,
Kwa maombezi/Ratiba za ibada/ Ushauri/ Maswali.
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312
Jiunge na kundi letu la mafundisho ya Biblia whatsapp kwa kubofya hapa > Group-whatsapp
Mada Nyinginezo:
Isaya 10:22 “Maana watu wako, Ee Israeli, wajapokuwa wengi kama mchanga wa pwani, ni mabaki tu watakaorudi; kuangamiza kumekusudiwa, kunakofurika kwa haki”.
Wana wa Israeli walidhani, kuchukuliwa tena utumwani na kurudishwa (Babeli na Misri) kungekuwa ni kurahisi kama ilivyokuwa wakati ule walipotolewa Misri. Walidhani Mungu atakuja kuwatoa tena kama taifa kwa mkono hodari wa nabii kama Musa, na wote watarudi nchi yao.
Lakini mambo hayakuwa hivyo, Mungu aliwaonya mapema akiwaambia hilo jambo halitakuwepo, na ndio maana alitumia muda mrefu sana kuwasihi, watubu waache njia zao mbaya, lakini hawakusikia badala yake wakawa wanawapiga manabii wake na wengine kuwaua,
Lakini siku ya siku ilipofika, yale mataifa 10 yalichukuliwa utumwani Ashuru, na biblia inatuonyesha hakuna hata mmoja aliyerudi hadi wakati huu wa sasa.. watu wote waliendelea kubaki kule kule, hata na lile taifa moja la Yuda, ambalo lilikuja kuchukuliwa nalo baadaye Babeli na Nebukadreza, japokuwa nalo lilikuwa na watu wengi sana, lakini ni kikundi kidogo sana, yaani watu wachache sana ndio Mungu aliwarudisha, na hiyo ilikuwa tu ni kuwatunzia uzao vinginevyo wangefananishwa na Sodoma na Gomora, kwa jinsi ambavyo wangepotea wote.
Warumi 9:27 “Isaya naye atoa sauti yake juu ya Israeli, kusema, Hesabu ya wana wa Israeli,ijapokuwa ni kama mchanga wa bahari,ni mabaki yao tu watakaookolewa.
28 Kwa maana Bwana atalitekeleza neno lake juu ya nchi, akilimaliza na kulikata.
29 Tena kama Isaya alivyotangulia kunena, Kama Bwana wa majeshi asingalituachia uzao, Tungalikuwa kama Sodoma, tungalifananishwa na Gomora”.
Sasa biblia inasema mambo hayo yaliandikwa kwa mifano ili kututahadharisha na sisi tulio katika nyakati hizi za hatari (1Wakorintho 10:11). Kwasababu kanisa la Israeli la mwilini lilikuwa linawakilisha kanisa la Kristo la rohoni sasa hivi. Kumbuka mara baada ya Israeli kuingiliwa na ukengeufu, pale walipoanza kuabudu miungu mingine, hapo ndipo Mungu alipokusudia kuwaangamiza wote, mikononi mwa maadui zao.
Vivyo hivyo na katika Kanisa la Kristo leo hii, Bwana alishatabiri kuwa kuwa kuna majira litaingiliwa na ukengeufu..ndio yale magugu yaliyopandwa na ibilisi ndani ya kanisa (Mathayo 13:24-30).. Sasa ukengeufu huu, ndio unaowafanya wakristo wengi wawe vuguvugu kupita kiasi, Hatushangai kuona idadi ya watu wanaojiita wakristo duniani ikizidi kuongezeka, sasa hivi ni Zaidi ya bilioni tatu.. Ni kama mchanga wa bahari tu, hata zaidi ya walivyokuwa Israeli.
Lakini hiyo sio tija kwamba wote tutaokolewa siku ile. Ni mabaki tu ndio yatakayookoka, ambayo Yesu aliyafananisha na ‘kundi dogo’
Luka 12:32 “Msiogope, enyi kundi dogo; kwa kuwa Baba yenu ameona vema kuwapa ule ufalme”.
Na ndio maana Bwana Yesu alisema. Walioitwa ni wengi lakini wateule ni wachache. Hichi ni kipindi cha kurekebisha mienendo yetu kama wakristo, kwasababu kurudi Yerusalemu kwa sasa ni kugumu sio kama kule kwa kwanza. Nguvu ya kukuvuta umgeukie Mungu sasa sio kama ile ya kwanza ulipoanza kuamini.
Ni wachache tu ndio watakaorejea, na sisi tuwe miongoni mwa hao. Mungu anatuita kuache dhambi, tumgeukie yeye, tusiungalie ulimwengu, kwani unapoteza sana.. Kwasababu hizi ni nyakati za mwisho na Kristo yupo mlangoni, wakati huu ni ule wa kumalizia, siku yoyote, wakati wowote, tunaweza kushuhudia tendo hilo kuu la unyakuo. Ambapo kwa upande mmoja utakuwa ni furaha na shangwe, lakini kwa upande mwingine kilio na kusaga meno na majuto makubwa.
Bwana atusaidie.
Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema,
Kwa maombezi/Ratiba za ibada/ Ushauri/ Maswali.
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312
pia kama utapenda uyapate mafundisho haya kwa njia ya Whatsapp au email basi tutumie ujumbe kwenye namba hizo hizo.
Mada Nyinginezo: