Safari ya wana wa Israeli kutoka Misri, kuelekea Kaanani, ni ufunuo kamili wa safari yetu ya Kristo kutuokoa katika dhambi na kutuingiza katika Neema ya wokovu. Musa anafananishwa na Kristo.. Kama vile Musa alivyowaongoza wana wa Israeli kutoka Misri, kwa ishara na miujiza Mingi aliyokirimiwa na Mungu, ndivyo Kristo alivyodhihirishwa kwetu kutuokoa kutoka dhambini, kwa ishara na miujiza mikubwa kuliko ile ya Musa. Sasa ni kwa namna gani safari ile ya wana wa Israeli imefananishwa na safari yetu ya wokovu, unaweza kusoma binafsi kitabu cha 1Wakorintho 10:1-12.
Lakini kuna kipengele kimoja ningependa tukiangalie katika Wito huo wa kutolewa Misri kupelekwa Kaanani..na hicho tunakisoma katika mstari ufuatao..
Kutoka 8:1 “Bwana akamwambia Musa, Ingia kwa Farao, ukamwambie, Bwana asema hivi, Wape watu wangu ruhusa, ili WAPATE KUNITUMIKIA”
Tusome tena;
Kutoka 9:13 “Bwana akamwambia Musa, Ondoka asubuhi na mapema, ukasimame mbele ya Farao, umwambie, Bwana, Mungu wa Waebrania, asema, Wape watu wangu ruhusa WAENDE ILI WANITUMIKIE”.
Kupitia mistari hiyo nataka tuona sababu Nyingine ya Mungu kuwatoa wana wa Israeli kwenye utumwa wa Farao ni ipi.
Hapo tunasoma kwamba Bwana aliwatoa ili WAKAMTUMIKIE. Maana yake ni kwamba Wamefunguliwa kwenye utumwa mmoja na kupelekwa kwenye utumwa mwingine. Hawajafunguliwa na kisha kuwekwa huru tu, kutembea tembea huko la!. Bali walifunguliwa kutoka kumtumikia Farao na kupelekwa katika utumwa wa kumtumikia Mungu.
Pia tunasoma maneno hayo hayo katika…
Kutoka 10:3 “Basi Musa na Haruni wakaingia kwa Farao, na kumwambia, Bwana, Mungu wa Waebrania, asema hivi, Je! Utakataa hata lini kujinyenyekeza mbele zangu? Wape watu wangu ruhusa waende zao, ILI WANITUMIKIE”.
Ndugu, ni muhimu kulifahamu hili kwasababu pia lengo la Kristo kututoa dhambini ni hilo hilo la sisi kwenda kumtumikia yeye. Anatufungua ile nira ya Adui ambayo ni ngumu, na kutuvisha nira yake iliyo laini..
Ndio Bwana Yesu alisema katika Mathayo 11:28 kwamba “Njoni kwangu, ninyi nyote msumbukao na wenye kulemewa na mizigo, nami nitawapumzisha.
29 Jitieni nira yangu, mjifunze kwangu; kwa kuwa mimi ni mpole na mnyenyekevu wa moyo; nanyi mtapata raha nafsini mwenu”
SASA TUNAMTUMIKIA KWA NAMNA GANI?
Warumi 6:16 “Hamjui ya kuwa kwake yeye ambaye mnajitoa nafsi zenu kuwa watumwa wake katika kumtii, mmekuwa watumwa wake yule mnayemtii, kwamba ni utumishi wa dhambi uletao mauti, au kwamba ni utumishi wa utii uletao haki.
17 Lakini Mungu na ashukuriwe, kwa maana mlikuwa watumwa wa dhambi, lakini mliitii kwa mioyo yenu ile namna ya elimu ambayo mliwekwa chini yake;
18 na mlipokwisha kuwekwa huru mbali na dhambi, mkawa watumwa wa haki”
Unapowahubiria wengine Neno la Mungu, hapo tayari umefanyika kuwa mtumishi wa Mungu..Unakuwa unamtumikia Mungu, na Mungu atakuheshimu..Na kumtumikia Mungu sio tu kuwa mchungaji, au Mhubiri mkubwa, au Nabii au Mtume. Hapana…popote pale ambapo unaweza kufaa katika kulitangaza Neno..Katika nafasi hiyo, tayari unamtumikia Mungu. Hakunaga karama ya Mhubiri Mkubwa, au Nabii Mkuu, au Mchungaji mkuu, au Mwalimu mkuu…kama ni mhubiri ni mhubiri mbele za Kristo wote ni sawa, kama ni mwalimu ni mwalimu mbele za Kristo wote wanaheshimika sawa n.k. Aliye nabii mkuu ni Yesu mwenyewe, aliye Mwalimu Mkuu ni Yesu pekee, aliye Mtume Mkuu ni Yesu pekee..wengine wote haijalishi wingi wa wafuasi walionao…wote mbele ya Kristo wanafanana.
Hivyo kwa hitimisho ni muhimu kufahamu tumetolewa dhambini ili tukamtumikie Mungu na si tukajitumike wenyewe au tukautumikie ulimwengu. Ndio maana wana wa Israeli hatua ya kwanza baada ya kutolewa Misri, walipelekwa nyikani kupewa sheria na amri za Mungu..Na walipoingia kaanani Bwana aliwapa jukumu la kuwafundisha wana wao na vizazi vyao vilivyokuja juu ya sheria, amri na hukumu za Mungu. Na sisi wa sasa tunalo jukumu hilo hilo baada ya kuokoka.
Umeokoka, nenda kamtumikie Mungu..kwa kuwafundisha wengine uliyojifunza.
Mathayo 28:19 “Basi, enendeni, mkawafanye mataifa yote kuwa wanafunzi, mkiwabatiza kwa jina la Baba, na Mwana, na Roho Mtakatifu;
20 na kuwafundisha kuyashika yote niliyowaamuru ninyi; na tazama, mimi nipo pamoja nanyi siku zote, hata ukamilifu wa dahari”
Maran atha!
jiunge na channel yetu Kwa kubofya hapa >> WHATSAPP
Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema, na pia kama utapenda tuwe tunakutumia mafundisho ya Neno la Mungu ya mara kwa mara kwa njia ya email yako au Whatsapp basi tutumie ujumbe kwenye namba hii +255 789001312 / 0693036618
Mada Nyinginezo:
Bildi ni kitu cha kupimia kina cha maji,Mara nyingi huwa ni kamba ambayo wanaifungia kitu kizito kwenye moja ya ncha zake, kisha wanakishusha kitu hicho kwenye maji, aidha ya mto, au ya ziwa, au ya bahari. na moja kwa moja mpaka kwenye sakafu ya bahari. Kikishafika kule wanapima urefu wa kamba ile na hapo ndipo wanapojua bahari hiyo ina urefu wa kina gani.
Neno hilo utalipata, katika ile habari ya mtume Paulo alipokuwa akisafirishwa kama mfungwa kuelekea Rumi. Kama vile tunavyoijua habari, walipokuwa katikati ya safari yao bahari iliwachafukia sana, mpaka wakakata tamaa ya kuishi, wakakaa siku nyingi bila kuona jua wala nyota. Lakini kama baada ya siku 14 walifika mahali ambapo walihisi kama kuna nchi kavu mbele yao, hivyo ikabidi wajaribu habati yao kwa kupima kina cha maji sehemu mbili tofauti ili waone kama ni kweli kina ndio kinapungua au kinaongezeka..
Hapo ndipo wakatupa bildi hizo kwenye maji, walipotupa ya kwanza ikapima urefu wa “pima” 20, (Pima moja ni sawa na futi 6), hivyo urefu wa kwanza ulikuwa ni futi 120.
Wakaenda mbele kidogo wakatupa bildi nyingine tena, wakapata pima 15 ambazo ni sawasawa na futi 90. Hapo ndipo walipogundua kuwa kina cha bahari kinapungua na kwamba wapo karibu na nchi kavu. Ikawabidi watie nanga, wasisogee popote tena mpaka kukuche.
Matendo 27:27 “Hata usiku wa kumi na nne ulipofika, tulipokuwa tukichukuliwa huko na huko katika bahari ya Adria, kama usiku wa manane baharia wakadhani ya kuwa wanaikaribia nchi kavu.
28 Wakatupa bildi wakapata pima ishirini, wakaendelea kidogo wakatupa bildi tena, wakapata pima kumi na tano.
29 Wakachelea tusije tukapwelewa mahali penye miamba, wakatupa nanga nne za tezi, wakaomba kuche.”.
Hata sisi wakristo kila mmoja rohoni anapaswa awe na bildi ya kuipima safari yake akiwa hapa duniani.
Ni lazima tupime mienendo yetu, kila wakati, je namna ya maisha tunayoishi leo na jana tofauti yake ni nini?. Ikiwa hali ya maisha tunayoishi leo ndio inatufanya tuende mbali zaidi na Mungu, tupoe kiroho kuliko ilivyokuwa hapo jana..Hapo tunapaswa tuchukue maamuzi ya haraka sana ya kubadili mfumo wa maisha yetu, ili tusiendelee mbele kwenye madhara zaidi. Tukapotea moja kwa moja.
Lakini kama tutaishi maisha ambayo kila siku yanatutupa mbali na Mungu na bado tunaona ni sawa tu, tunaruhusu yaendelee hivyo hivyo , tujue kuwa mwisho wetu utakuwa ni mbaya sana.
Swali ni je mara ya mwisho kuishusha bildi yako ni lini?
jiunge na channel yetu Kwa kubofya hapa >> WHATSAPP
Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema, na pia kama utapenda tuwe tunakutumia mafundisho ya Neno la Mungu ya mara kwa mara kwa njia ya email yako au Whatsapp basi tutumie ujumbe kwenye namba hii +255 789001312 / 0693036618
Mada Nyinginezo:
Jina tukufu la Bwana wetu Yesu libarikiwe daima.
Karibu tuzidi kujifunza maneno ya uzima, kwasababu tupo katika nyakati za ukongoni kweli kweli, hivyo ni wajibu wetu kuzidi kujua mambo yahusuyo ukombozi wetu kwa umakini zaidi..
Neno letu la leo linatoka katika vifungu hivi;
Marko 9:30 “Wakatoka huko, WAKAPITA KATIKATI YA GALILAYA; NAYE HAKUTAKA MTU KUJUA.
31 KWA SABABU ALIKUWA AKIWAFUNDISHA WANAFUNZI WAKE, AKAWAAMBIA, Mwana wa Adamu yuaenda kutiwa katika mikono ya watu, nao watamwua; hata akiisha kuuawa, baada ya siku tatu atafufuka”.
Katika maneno hayo swali kuu unaweza ukajiuliza ni hili, ni kwanini Yesu hakutana watu wamwone , alipokuwa akipita Galilaya, ikumbukwe kuwa mji huo alishauendea mara nyingi na akafanya miujiza mingi kupita kiasi, lakini inafika wakati huu tena kwanini asijidhihirishe awahubirie na kuwaponya makutano kama kawaida badala yake, anaupita mji huo huo kimya kimya tena kwa siri kubwa.
Ukisoma hapo utaona biblia inatupa sababu ya yeye kufanya vile, inatuambia ni kwasababu alikuwa anataka kuwafundisha wanafunzi wake, hilo tu…Hiyo inatupa kuijua tabia nyingine ya Bwana Yesu ambayo pengine tulikuwa hatuijui. Hata sasa, wapo atakaowafundisha kwa wazi, na wapo atakaowafundisha akiwa sirini na mtu mwingine yeyote hatajua,.
Wakati wote makutano walifundishwa kwa wazi, lakini wale aliowaita, kisha baadaye wakawa wanafunzi wake, aliwavusha daraja lingine la rohoni, akawa anawafundisha mambo mengine tofauti kabisa na yale makutano aliyokuwa anawafundisha.
Na baadhi ya mambo yenyewe aliyowafundisha, kama tunavyosoma habari ni yale ambayo yatakwenda kutokea kipindi kifupi mbele yao, yaani juu ya kukamatwa kwa Yesu, mpaka kusulibiwa na kufufuka na kupaa. Walikuwa wanapewa siri za ukombozi wote wa mwanadamu kabla ya wakati wenyewe kufika..mambo ambayo makutano hawakuelezwa, wala kudokezewa hata kidogo.. Na waliambiwa mengine mengi zaidi ya hayo. Kwamfano hizi habari zote tunazozijua zihusuzo siku za mwisho, hawakuambiwa makutano, hapana bali hicho kilikuwa ni chakula walichopewa wanafunzi wake tu walipokuwa kule katika mlima wa mizeituni, (Mathayo 24, Marko 13, Luka 21:5).
Na ndio maana Bwana Yesu mahali pengine aliwaambia, niliyowaambia sirini, utafika wakati mtayasema hadharani, na ndio haya yanayotufaidia sisi..
Kwahiyo, hata sasa huu sio wakati wa kuzunguka huku na huko, kufurahia Yesu anaponya, Yesu anafufua, Yesu anabariki, hatupaswi kuwa kama makutano tu, waliomfuata Yesu, kwa ajili ya mikate na miujiza, na ishara, tunapaswa sasa tuingie gharama za kufanyika kuwa wanafunzi wake,(hicho ndicho anachokihitaji) kwasababu yapo mambo yahusuyo siri za Ufalme wa mbinguni, na Unyakuo tunapaswa tuyajue kwa wakati huu mfupi tuliobakiwa nao, na hatutayajua kama hatutakuwa wanafunzi kweli kweli wa Bwana Yesu.
Yesu ni yeye Yule jana na leo na hata milele, tusidhani alipojificha kwa wale, hawezi kujificha na kwetu pia..Hivyo tusipumbazwe na kitu chochote, kwa maana sisi tukizembea, wapo wengine wakati wetu huu huu wamekaa katika vyumba vya siri na Bwana Yesu wanafunuliwa mambo ambayo yanahusu wokovu wetu.
Tusikubali kuachwa nyuma na Yesu, tusikubali apite kwenye mitaa yetu, na kwenye makanisa yetu, na kwenye mikutano yetu kwa siri, Embu leo tujiachie na kufanyika kuwa wanafunzi wake kweli kweli.
Na tunafanya hivyo kwa kujitwika misalaba yetu, na kuuacha ulimwengu nyuma, na kumkaribisha ndani yetu, Na baada ya hapo, yeye mwenyewe atahusika, kutufundisha.
Tuzidi kukumbuka kuwa; Hii dunia ipo ukingoni sana, hatutashangaa hata unyakuo ukiwa ni usiku wa leo, kwasababu hakuna chochote ambacho hakijatimia, hivyo tukiyajua hayo hatutakuwa na muda tena wa kuichezea chezea neema ya wokovu. Yesu sio kama tunavyomfikiri, Sio kama tunavyomwaza vichwani mwetu, Yesu ni hekima ya Mungu na Nguvu ya Mungu yenyewe kama biblia inavyotuambia (1Wakorintho 1:24), tukifanyika kuwa wanafunzi wake kweli kweli, hatutabaki kama tulivyo.
Hivyo tuanze sasa kufanyika wanafunzi wa Bwana.
Maran Atha.
jiunge na channel yetu Kwa kubofya hapa >> WHATSAPP
Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema, na pia kama utapenda tuwe tunakutumia mafundisho ya Neno la Mungu ya mara kwa mara kwa njia ya email yako au Whatsapp basi tutumie ujumbe kwenye namba hii +255 789001312 / 0693036618
Mada Nyinginezo:
Ni vitu vipi hivyo viwili visivyoweza kubadilika? (Ebr 6:18)
Mlima Gerizimu na Ebali ni ipi, na umuhimu wao rohoni ni upi?
Zaburi 9:10 “Nao wakujuao jina lako wakutumaini Wewe, Maana Wewe, Bwana hukuwaacha wakutafutao”.
Shalom, tuzidi kujikumbusha kuwa..
Mungu anapenda sana watu wanaomtafuta, anapenda watu wanaoonyesha Nia ya dhati katika kumjua yeye, Mtu anayemtafuta Mungu kamwe Mungu hawezi kumuacha. Atakuwa naye bega kwa bega tu, mkono kwa mkono, mguu kwa mguu, kwasababu ni ahadi yake kuwa hawaachi wamtafutao.
Mungu si kama sisi wanadamu, sisi ni rahisi kumuacha mtu mwenzetu ghafla tu, hususani pale tunapoona hana msaada wowote kwetu, au katuudhi kwa mara moja, lakini kwa Mungu hilo halipo, haangalii ulimuudhi mara ngapi huko nyuma, wala haangalii madhaifu yako, haangalii uchanga wako, au ujuaji wako, hivyo vyote sio vinavyomshawishi, hivyo hilo hata usilifikirie unapokusudia kumgeukia yeye, ikiwa leo hii utageuka na kusema naanza tena upya na Baba..Saa hiyo hiyo na yeye anaonyesha nia ya kuanza kupiga hatua na wewe,kama kwamba hakuna chochote kibaya ulichowahi kumtendea huko nyuma.
Shetani atakuambia Mungu hawezi kukusikia mtu kama wewe, atajifunuaje kwako, kumbuka dhambi ile uliyofanya zamani, au dhambi hii unayotenda sasahivi unadhani atakusamehe? Ukiona hivyo yapinge hayo mawazo anafanya hivyo ili kukuvunja tu moyo usiendelee au usiwaze kumtafuta Mungu..Lakini ahadi ya Mungu ni ile ile kuwa kamwe hawaachi hao wamtafutao.
Yohana 6:37 “Wote anipao Baba watakuja kwangu; wala ye yote ajaye kwangu sitamtupa nje kamwe”.
Unaona? Mungu hawezi kuwaacha wale wote wanaomwendea yeye, hilo wazo halijawahi kuingia ndani yake, yaani kile kitendo tu cha kuamua na kusema namfuata Yesu, ujue ni tayari umeshapokelewa bila masharti yoyote, ni mlango ambao upo wazi wakati wote,kwa mtu yeyote haijalishi dini yake wala dhehebu lake, yaani ni jambo ambalo halina maswali maswali, au mashaka mashaka, ukimtafuta utajifunua kwako tu.
Sauti ya shetani inawadanganya wengi na kuwaambia, Mungu hawezi kujishughulisha na watu kama wao, bado huwajakidhi vigezo vya kusikiwa na Mungu, hawana upako wowote, wao ni takataka tu machoni pake, Ndugu hiyo sauti ikikuambia hivyo ijibu uiambie, ingekuwa mimi sina thamani yoyote machoni pake basi asingeniumba, lakini kama ameona vema kuniumba mimi mpaka nikawa hivi nilivyo mwanadamu kamili mwenye mfano wake na sura yake, na hakuniumba mende, au panya, au kononono basi mimi ni wa thamani nyingi machoni pake..
Hivyo ukishajipa moyo kwa namna hiyo halafu ukaanza kuutafuta uso wa Mungu wako, yeye mwenye atajifunua kwako, ni lazima afanye hivyo kwasababu anasema kamwe hawaachi wamtafutao, Mungu anafungwa na Neno lake, akisema hivi, amesema ni lazima atimize, sio kama sisi tulivyo.
Hivyo hatua ya kwanza kabisa inayothibitisha kuwa unamtafuta Mungu, ni kwa kutubu kwanza dhambi zako, kwa kumaanisha kabisa kuziacha, na pili kuwa tayari kwenda kubatizwa katika ubatizo sahihi wa kimaandiko wa kuzamishwa kwenye maji mengi na kwa jina la Bwana Yesu Kristo (Matendo 2:38) kama hukuwahi kubatizwa hapo kabla, na tatu ni kuanza kuzingatia kujifunza Neno la Mungu, na kuishi maisha yampendezayo Mungu na kufanya ushirika na kusali..
Ukizingatia hayo, nakutakia kila la heri katika kukutana na Mungu siku baada ya siku katika maisha yako yote hapa duniani, Kwasababu Bwana ni Mungu ambaye kamwe hawaachi wamtafutao.
Shalom.
jiunge na channel yetu Kwa kubofya hapa >> WHATSAPP
Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema, na pia kama utapenda tuwe tunakutumia mafundisho ya Neno la Mungu ya mara kwa mara kwa njia ya email yako au Whatsapp basi tutumie ujumbe kwenye namba hii +255 789001312 / 0693036618
Mada Nyinginezo:
Nini maana ya “Uchungu wa mauti ni dhambi, na nguvu za dhambi ni torati”
Ni vitu vipi hivyo viwili visivyoweza kubadilika? (Ebr 6:18)
SWALI: Nini maana ya “Uchungu wa mauti ni dhambi, na nguvu za dhambi ni torati” (1 Wakorinto:15:56)?.
JIBU: Pale Adamu alipoasi katika bustani ya Edeni, alipewa mapigo mawili makubwa…la kwanza Ardhi imelaaniwa kwa ajili yake, la pili ATAKUFA. Maana yake ni kwamba, Matokeo ya ardhi kulaaniwa ndio yale Bwana Mungu aliyoyataja pale kwamba atakula kwa jasho, maana yake ni kwamba ataishi lakini katika hali ya kuishi huko atakuwa katika mateso ya kuhangaika siku zote za Maisha yake, hatapumzika!.
Lakini pigo la pili aliloambiwa kwamba Atakufa, biblia haijataja matokeo yake…Maana yake ni kwamba nalo pia sio zuri, maana yake ni kwamba katika kufa huko pia sio kwamba atakwenda kustarehe na kupumzika. Hapana!.. Baada ya kufa atakwenda sehemu ya wafu nako huko sio sehemu ya kwenda kupumzika, bali pia kuna kutaabika baada ya kifo, kwasababu kifo ni pigo!.
Hivyo kabla ya Bwana Yesu mtu yeyote awe mkamilifu au mwovu baada ya kufa alikuwa anashuka sehemu ya wafu ambayo haikuwa salama sana, bado anaendelea kuitumikia laana, na shetani alikuwa anao uwezo wa kufika mahali wafu walipo, na baadhi yao kuwafanya anavyotaka..Sasa ili kuelewa vizuri kasome Habari za Samweli, jinsi shetani alivyomtaabisha kwa kumpandisha kutoka kwa wafu (kasome 1Samweli 28:15). Hivyo mauti ilikuwa ni sehemu chungu, kwasababu shetani alikuwa na mamlaka nako.
Mpaka Bwana Yesu alipokuja na kwenda kuzitwaa funguo za mauti na kuzimu, Ndipo ukatokea wokovu kwa wale watakaokufa katika haki, kwa kuhamishwa na kuwekwa sehemu salama inayoitwa Paradiso. Huko watapumzika bila kufikiwa na adui shetani, (kwasababu funguo anazo Kristo na si shetani tena, hivyo shetani hawezi kuwafikia wala hajui walipo), watakaa huko wakingoja ufufuo wa kwenda mbinguni, siku ile parapanda ya mwisho itakapolia, ambapo watafufuliwa na kuvaa miili yao ya asili kwanza, kisha ya utukufu itavikwa juu ya ile ya asili (ili ule unaoharibika uvae kutokuharibika, na mauti imezwe na uzima 1Wakorintho 15:54) na kisha wataungana na watakatifu walio hai, wote wakiwa na miili yao ya utukufu isiyoweza kuharibika wala kufa na kwa Pamoja watakwenda mbinguni.
Lakini wafu waliokufa katika dhambi (yaani ambao hawajamwamini Yesu), wanapokufa hawaendi paradiso bali kuzimu sehemu ya mateso ya muda, wakingojea kusimamishwa siku ile katika kiti cha hukumu na kuhukumiwa kulingana na matendo yao, na kutupwa katika lile ziwa la moto Pamoja na shetani na malaiika zake.
Hivyo Mauti ina UCHUNGU kwa wale waliokufa nje ya Kristo, na kwa wale watakaokufa wakiwa hawajampokea Kristo. Kwasababu hata baada ya kufa wataendelea kuteseka.. Na uchungu huo unakuja ni kwasababu ya Maisha ya Dhambi waliyokuwa wanayaishi, hivyo baada ya kufa, watapata uchungu, Lakini kama wangeishi Maisha ya utakatifu ambayo yanakuja kwa kumpokea Bwana Yesu na kujazwa Roho Mtakatifu, basi wasingepata uchungu baada ya kifo, badala yake baada ya kifo wangepumzishwa mahali pa raha panapoitwa peponi/paradiso…sawasawa na andiko hili ….
“Ufunuo 14:12 Hapa ndipo penye subira ya watakatifu, hao wazishikao amri za Mungu, na imani ya Yesu.
13 Nikasikia sauti kutoka mbinguni ikisema, Andika, HERI WAFU WAFAO KATIKA BWANA TANGU SASA. NAAM, ASEMA ROHO, WAPATE KUPUMZIKA BAADA YA TAABU ZAO; kwa kuwa matendo yao yafuatana nao”
Hiyo ndiyo sababu biblia inasema hapo katika 1Wakorintho 15:56 kuwa “UCHUNGU WA MAUTI NI DHAMBI”.. Maana yake tukifa katika dhambi, tutapata uchungu baada ya kifo.
Hapo ndipo utakapojua umuhimu wa Yesu Kristo upi?, na jinsi gani kama sio Baba kumleta ulimwenguni, shughuli yetu ilikuwa imekwisha!..tungekuwa hatuko salama hata baada ya kifo..Uchungu tungeendelea nao, baada ya kufa, na hiyo ingekuwa ni milele.
Kama utataka kujua mistari inayozungumzia Habari za Yesu kuzitwaa funguo za Mauti na kuzimu, na jinsi yeye mwenyewe alivyoshinda uchungu wa Mauti,.unaweza kusoma binafsi mistari ifuatayo.. (Matendo 2:23-27, Ufunuo 1:17-18, Warumi 14:8-9).
Sasa sehemu ya pili, inasema “NGUVU YA TORATI NI DHAMBI”..Maana yake ni Nini?
Ili tuelewe ni kwa namna gani, Torati au sheria ndiyo nguvu ya dhambi…Hebu tutafakari mifano ifuatayo..
Kama umewahi kuchunguza, mahali ambapo pamewekwa sheria kali, ndipo panapovuta umakini wa watu zaidi..Ukimwambia mtu usipite mahali hapa usiku, ndio kama umemtangazia apite..kwasababu kila siku atajiuliza kwanini yule anikataze nisipite pale usiku, kwani kuna nini…siku moja nitajaribu nipite kwa siri ili nijue ni nini kinaendelea pale. Umeona?..Hapo hiyo sheria uliyompa kwamba asipite mahali hapo usiku, tayari imemfungulia mlango wa kuivunja…Lakini kama usingemwambia hata asingehangaika kutafuta kupita mahali hapo usiku.
Vivyo hivyo, ukimwacha mtoto nyumbani na kumwambia ni marufuku kufungua kile chumba, ukikufungua ni utakuwa umefanya makosa!…Sasa kwa kumwambia vile ndio kama umemjulisha kuwa akatafute kukifungua hata kwa siri ili aangalie kuna nini ndani ambacho kinakatazwa kisiangaliwe, hivyo atajizuia siku ya kwanza, ya pili lakini siku moja atakuwa anajiuliza ni nini kipo kule, hivyo atatafuta hata kuchungulia tu.. “tayari kashaivunja ile sheria”.
Kadhalika sheria inaposema “Usizini” tayari imefungua mlango wa yule anayeambiwa usizini akazini…Ni hivyo hivyo na dhambi nyingine zozote..zinapata nguvu katika SHERIA au AMRI. Ndio maana Mtume Paulo kwa uongozo wa Roho alisema..
Warumi 7:8 “ Lakini dhambi ilipata nafasi kwa ile amri, ikafanya ndani yangu kila namna ya kutamani. KWA MAANA DHAMBI BILA SHERIA IMEKUFA.
9 Nami nalikuwa hai hapo kwanza bila sheria; ila ilipokuja ile amri, dhambi ilihuika, nami nikafa”.
Warumi 7: 5 “ Kwa maana tulipokuwa katika hali ya mwili, tamaa za dhambi, zilizokuwako kwa sababu ya torati, zilitenda kazi katika viungo vyetu hata mkaizalia mauti mazao”.
10 Nikaona ile amri iletayo uzima ya kuwa kwangu mimi ilileta mauti”.
Hiyo ndio sababu Neno la Mungu linasema hapo.. “Nguvu ya dhambi ni Torati”. Lakini Bwana Yesu alipokuja na kutoa uhai wake pale Kalvari, na kufufuka na kupaa mbinguni..alituachia ahadi ya Baba, ambayo ni Roho Mtakatifu.. Kwa huyo hatuishi kwa Sheria. Na hatuwi chini ya sheria..Huyo anatusaidia kushinda dhambi pasipo sheria…Maana yake ni kwamba sheria isema kwamba usizini, au isiseme bado Dhambi haina nguvu juu yetu. Hiyo ni nguvu ya kipekee sana na zawadi isiyoelezeka. Na hapa pia ndio utaona umuhimu wa Yesu Kristo. Kama sio kuja, ahadi hii tusingeipata…Ingekuwa kwa jinsi sheria zinavyoongezeka ndivyo na dhambi ingetulemea sana. Lakini wote waliompokea Kristo na kupokea Roho wake mtakatifu, wanapewa uwezo wa kipekee kushinda ndambi.
Hivyo kama hujampokea Kristo ndugu yangu..tumaini lako lipo kwa nani?..Unafikiri utaweza kushinda zinaa kwa nguvu zako?, unafikiri utaweza kuushinda ulevi? Au usengenyaji?..Hutaweza..na kwa jinsi utakavyozidi kujiwekea sheria kwamba sitafanya hivi au sitafanya vile, ndivyo unavyozidi kujimaliza..kwasababu nguvu ya dhambi ipo katika hizo sheria unazojiwekea…kwasababu utakapojiwekea sheria ya kwamba kesho sijakunywa pombe na humtaki Yesu, hiyo sheria uliyojiwekea utavumilia siku ya kwanza, pengine na ya pili.. lakini zitakapopita siku kadhaa utapata kiu ambayo hujawahi kuipata.. na utalewa mara mbili Zaidi ya ulivyokuwa unalewa. Kwasababu hiyo basi..mpokee Kristo leo, wokovu ni bure ili upate uwezo wa kushinda dhambi, na pia uepukane na UCHUNGU WA MAUTI.. ambao utawapata wale wote ambao hawajampokea Yesu baada ya kumaliza maisha haya. Baada ya kutubu, tafuta ubatizo sahihi ambao ni wa maji tele (Yohana 3:23) na kwa jina la Yesu Kristo, ambalo ndio jina la Baba, Mwana na Roho Mtakatifu (Matendo 2:38, Matendo 8:16). Na Roho Mtakatifu atakutia muhuri..
Bwana akubariki.
jiunge na channel yetu Kwa kubofya hapa >> WHATSAPP
Maran athan
Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema, na pia kama utapenda tuwe tunakutumia mafundisho ya Neno la Mungu ya mara kwa mara kwa njia ya email yako au Whatsapp basi tutumie ujumbe kwenye namba hii +255 789001312 / 0693036618
Mada Nyinginezo:
Moyo wake mwenye hekima upo upande wa kuume, maana yake nini?
Kama ni msomaji wa biblia utakuwa umekatana na hili neno sehemu nyingi..
Shokoa ni kiswahili cha zamani chenye maana ya “Vibarua”. Hususani wale waliotekwa na kulazimishwa kufanya kazi kwa nguvu.
Kwamfano katika biblia tunamwona Mfalme Sulemani, aliwachukua watu Shokoa..
2Nyakati 2: 7 “Basi kwa habari ya watu wote waliosalia wa Wahiti, na wa Waamori, na wa Waperizi, na wa Wahivi, na wa Wayebusi, wasiokuwa wa Israeli;
8 wa watoto wao waliosalia baada yao katika nchi, ambao wana wa Israeli hawakuwakomesha, katika hao Sulemani akawatumikisha SHOKOA HATA LEO”
Mistari mingine inayozungumzia juu ya shokoa ni 1Wafalme 5:13 , Yoshua 17:13, Waamuzi 1:28, Waamuzi 1:30 n.k
Na hata leo adui yetu shetani anawachukua watu Shokoa, kwa kuwateka na kuwatumikisha kwa nguvu. Anawatumikisha kwa dhambi, magonjwa, tabu na hofu.Wote aliowateka hawana raha, wala furaha, wala amani..Wamejawa na mashaka na kukata tamaa.. Yote hayo yanawapata kwasababu wamechukuliwa mateka (Shokoa) na adui shetani.
Lakini habari njema ni kwamba..Yupo mmoja ALIYETIWA MAFUTA NA MUNGU KUKOMESHA UTEKA. Huyo akikuweka huru umekuwa huru kweli kweli.. hofu yote itaondoka, hofu ya kifo, shida, tabu na magonjwa anaiondoa..na kisha anakupa raha nafsini mwako. Na huyo si mwingine zaidi ya YESU KRISTO.
Isaya 61: 1 “Roho ya Bwana MUNGU i juu yangu; kwa sababu Bwana amenitia mafuta niwahubiri wanyenyekevu habari njema; amenituma ili kuwaganga waliovunjika moyo, KUWATANGAZİA MATEKA UHURU WAO, NA HAO WALİOFUNGWA HABARİ ZA KUFUNGULİWA KWAO.
2 Kutangaza mwaka wa Bwana uliokubaliwa, na siku ya kisasi cha Mungu wetu; kuwafariji wote waliao”
Ukimpokea maishani mwako, Uteka shetani aliokuteka, itakuwa ni zamu yako kumteka yeye…atakaa chini ya miguu yako, na ukimwambia ondoka ataondoka kwa hofu nyingi.
Kama hujampokea na utamani kufanya hivyo fuatiliza sala hii ya mwongozo wa toba kwa kufungua hapa >>>KUONGOZWA SALA YA TOBA
jiunge na channel yetu Kwa kubofya hapa >> WHATSAPP
Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema, na pia kama utapenda tuwe tunakutumia mafundisho ya Neno la Mungu ya mara kwa mara kwa njia ya email yako au Whatsapp basi tutumie ujumbe kwenye namba hii +255 789001312 / 0693036618
Mada Nyinginezo:
Shalom.
Jina la Bwana wetu Yesu Kristo libarikiwe, karibu tujifunze maandiko. Yapo mambo kadhaa ya kujikumbusha pale tunapokuwa wakristo.
Ni lazima tujue kuwa Tunaposema tumeokoka, maana yake ni kuwa tunakuwa tumeingia katika maagano ya ndoa takatifu na Mungu wetu. Mungu anakuwa mume wetu (Yeremia 3:14), na sisi tunakuwa bibi-arusi wake katika roho. Sasa ipo tahadhari ambayo Mungu alishaitoa tangu zamani za kale kwa watu wake alioingia nao maagano, aliwaambia, Mimi ni Mungu mwenye WIVU. Soma Kutoka 20:4-6, utaliona hilo, na kwamba wivu wake ni mbaya na unaweza kwenda hata mpaka vizazi vine mbeleni, kama watu hawatamgeukia yeye. Na hiyo ni kwa kosa tu la kufanya ibada za sanamu.
Unaweza ukajiuliza Mungu muumba wa mbingu na nchi anakuwaje na wivu? Jibu ni kwamba wivu ni sehemu yake, kwasababu sisi wanadamu tuliumbwa kwa mfano wake, na sio yeye kwa mfano wetu, hivyo tabia ya kuwa na wivu katika mahusiano imetoka kwake na sio kwetu..
Na biblia inatuambia ukali wa wivu unazidi hata ule wa ghadhabu au hasira..Ni heri ukutane na mtu mwenye hasira umemuulia ndugu yake, kuliko kukutana na mtu mwenye wivu wa mpenzi wake.
Mithali 27:4 “Ghadhabu ni kali, na hasira ni gharika; Lakini ni nani awezaye kusimama mbele ya wivu”.
Na ndio maana tunapaswa tuliweke hilo akilini sisi wakristo, kwasababu wivu wa Mungu ulio juu yetu sisi wa agano jipya ni mkali kuliko ule uliokuwa kipindi cha agano la lake.
Unajua ni kwanini?
Ni kwasababu ya ROHO MTAKATIFU, basi. Ni heri wale waliomtia Mungu wivu jangwani kwa kutengeneza ndama wa dhahabu, na kumwabudu kuliko sisi tunaomtia wivu Roho Mtakatifu leo hii. Pale tunaposema tunapoiacha njia ya wokovu na kwenda kusujudia sanamu tunazozoziita za watakatifu, au tunapokwenda kuzini, au kufanya uasherati, ni ishara kamili kuwa tunamtia wivu Roho Mtakatifu aliye ndani yetu.
1Wakorintho 10: 21 “Hamwezi kushirikiana katika meza ya Bwana na katika meza ya mashetani. 22 Au twamtia Bwana wivu? Je! Tuna nguvu zaidi ya yeye?”
Biblia inasema hivi;
Yakobo 4:4 “Enyi wazinzi, hamjui ya kwamba kuwa rafiki wa dunia ni kuwa adui wa Mungu? Basi kila atakaye kuwa rafiki wa dunia hujifanya kuwa adui wa Mungu.
5 AU MWADHANI YA KWAMBA MAANDIKO YASEMA BURE? HUYO ROHO AKAAYE NDANI YETU HUTUTAMANI KIASI CHA KUONA WIVU?
Kama tunavyosoma katika maandiko hayo, kwa lugha rahisi ni kuwa pale Roho Mtakatifu anapoingia ndani yetu, anatupenda upeo, yaani anatupenda sana kiasi kwamba anatuonea wivu mkali pale tunapoyahalifu maagizo ya Mungu kwa makusudi.
Na wivu huo unaweza kumfanya achukue uamuzi wowote mbaya juu yetu; Baadhi yetu anaruhusu hata tupitie magonjwa, wengine hata vifo visivyokuwa vya wakati, na sio shetani bali ni Mungu mwenyewe kasababisha.
Waefeso 4:30 “Wala msimhuzunishe yule Roho Mtakatifu wa Mungu; ambaye kwa yeye mlitiwa muhuri hata siku ya ukombozi”.
Lakini Mungu wetu mara nyingi amekuwa ni wa rehema, anaipitishia ghadhabu yake mbali, akingojea mtu mmoja atubu amgeukie.
Hivyo kama wewe ni mmojawapo, ambaye ulikuwa umeokoka ukamuasi Mungu, ukamtia Roho Mtakatifu wivu mwingi kwa matendo yako, na kwamba ulistahili kuhukumiwa, lakini mpaka leo bado unaishi, ni kwa neema tu, hivyo kama upo tayari kugeuka kwa dhati, fahamu kuwa Mungu atakusamehe.
Kwahiyo unachopaswa kufanya ni wewe mwenyewe kufanya maamuzi ya kutubu, kwa kwenda sehemu yako ya siri, utubu mbele za Mungu, kisha, na baada ya hapo anza kuishi kama mkristo wa kweli, kwasababu Mungu ataanza kuyaangalia matendo yako kama kweli umebadilika, hivyo ukiwa umecha kweli kweli, basi ataiondoa hasira ya wivu wake juu yako, na kukuponya kama alikuwa tayari ameshaanza kukurarua.
Hivyo sikuzote kumbuka: Roho hututamani kiasi cha kutuonea wivu. Ni wajibu wetu kuishi kwa makini sana katika ukristo wetu.
Kama umeguswa kushare somo hili au mengine kama haya kwenye magroup ya whatsapp na penginepo, utafanya vyema kufanya hivyo, lakini tunaomba ufanye hivyo bila kubadilisha chochote wala kuondoa anwani ya wingulamashahidi na kuweka namba zako za simu ili kuzuia mkanganyiko. Kwasababu tumepokea malalamiko, kuna watu wasio kuwa na nia ya Kristo, kuchukua masomo na mwisho kuondoa namba au anwani yetu na kuweka namba zao, lengo lao ni kutaka sadaka kutoka kwa watu. (Wingu La Mashahidi hatujawahi kumpigia mtu simu na kumwomba sadaka). Hivyo chukua tahadhari!.
Bwana atubariki sote na kutuzidishia neema yake.
jiunge na channel yetu Kwa kubofya hapa >> WHATSAPP
Shalom.
Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema, na pia kama utapenda tuwe tunakutumia mafundisho ya Neno la Mungu ya mara kwa mara kwa njia ya email yako au Whatsapp basi tutumie ujumbe kwenye namba hii +255 789001312 / 0693036618
Mada Nyinginezo:
JIHADHARI NA DHAMBI YA WIVU/HUSUDA.
KWANINI NABII ISAYA ALIAGIZWA KUHUBIRI UCHI?
KWANINI MAISHA MAGUMU?
IFANYE KAZI YA MUNGU PASIPO HOFU!
IMANI NI KUWA NA UHAKIKA WA MAMBO YATARAJIWAYO.
Jina la Bwana wetu Yesu, libarikiwe.
Yapo mambo mengi ambayo yatawafanya wanadamu wengi wasiurithi uzima wa milele siku ile. Wakidhani wapo sawa na Mungu, na kwamba wanampendeza Mungu lakini itakuwa kama jambo la kuwashangaza kwamba wameukosa uzima wa milele. Na hilo si lingine zaidi ya kuukosa utakatifu, biblia inasema katika Waebrania 12:14 kuwa…“Tafuteni kwa bidii kuwa na amani na watu wote, na huo utakatifu, ambao hapana mtu atakayemwona Bwana asipokuwa nao”. Maana yake pasipo huo, haijalishi tunaona maono, haijalishi tunahubiri sana, haijalishi tunatoa sadaka sana, haijalishi tunatoa pepo wengi na kufanya miujiza…bado hatutamwona Mungu.
Fadhili za Mungu huwa zinawalewesha wengi.. Ndugu hata kama utalitukana jina la Mungu leo, hiyo haimfanyi Mungu kukunyima chakula au kutokukupa riziki, hata kama ukiwa mchawi haimfanyi Mungu kutokuangazia jua lake kwasababu fadhili zake ni za milele, na yeye hana upendeleo..anawanyeshea mvua waovu na wema, anawaangazia jua lake waovu na wema.. Hata yule mchawi mwovu kuliko wote anampa uzao, na tena hata katikati ya huo uzao wake wanaweza kutokea watumishi wa Mungu. Lakini pamoja na fadhili zote hizo za Mungu haimaanishi ndio tiketi ya kumwona Mungu siku ile..
Unapoumwa na kumwomba Mungu akuponye, na akakuponya hiyo haimaanishi kwamba ndio upo sawa na Mungu na kwamba hata ukifa leo utaingia mbinguni, Kama ni mtumishi unapomwombea mtu na akapona au unapotoa pepo na likatoka, huo sio uthibitisho kwamba Mungu anapendezwa na wewe…
Vile vile unapopitia shida na ukaona mkono wa Mungu umekuokoa katika hiyo shida…huo sio uthibitisho kwamba Mungu anafurahishwa na wewe ndio maana kakuokoa… anachokufanyia wewe ndicho anachowafanyia mamilioni ya watu duniani kote..na wengine hata sio wakristo anawaokoa kwa ushuhuda mkubwa. Kama unafikiri nakudanganya, tafuta mtu yeyote ambaye sio mkristo kabisa, mtu wa makamo mwulize ni tukio gani ambalo hutalisahau katika maisha yako, ambalo unaamini ni Mungu alikutendea..Utasikia shuhuda atakazokupa!…Hapo ndipo utakapojua kuwa Mungu hanaga upendeleo wa kuwapendelea watu wake tu!..
Hivyo fadhili za Mungu, zisitupumbaze na kujiachia katika dhambi, tukijitumainisha kuwa siku ile tutamwona Mungu…
Hebu yatafakari haya maneno ya Bwana..
Mathayo 7:21 “Si kila mtu aniambiaye, Bwana, Bwana, atakayeingia katika ufalme wa mbinguni; bali ni yeye afanyaye mapenzi ya Baba yangu aliye mbinguni.
22 Wengi wataniambia siku ile, Bwana, Bwana, hatukufanya unabii kwa jina lako, na kwa jina lako kutoa pepo, na kwa jina lako kufanya miujiza mingi?
23 Ndipo NITAWAAMBIA DHAHIRI, SIKUWAJUA NINYI KAMWE; ondokeni kwangu, ninyi mtendao maovu”
Hapo anasema atawaambia “DHAHIRI” yaani maana yake wazi pasipo vificho, kwamba siwajui.
Maana yake ni kwamba kama ukiwa mwasherati kwa siri au kwa wazi, haijalishi unaona malaika kila siku katika ndoto, hautaurithi uzima wa milele, kama unaabudu sanamu kama ni mchawi kama ni mlevi na mambo mengine yote yanayofanana na hayo, basi siku ile hautaurithi uzima wa milele.
Na Neno la Mungu ni upanga ukatao kuwili, hivyo linawahusu watu wote, hata mimi pia linanihusu, kama sitakuwa mtakatifu sitaurithi uzima wa milele, haijalishi nafanya nini sasa.
Ndio maana Mtume Paulo kwa uongozo wa Roho akasema mahali fulani maneno haya…
Wagalatia 5:19 “Basi matendo ya mwili ni dhahiri, ndiyo haya, uasherati, uchafu, ufisadi,
20 ibada ya sanamu, uchawi, uadui, ugomvi, wivu, hasira, fitina, faraka, uzushi,
21 husuda, ulevi, ulafi, na mambo yanayofanana na hayo, KATİKA HAYO NAWAAMBİA MAPEMA, kama nilivyokwisha kuwaambia, ya kwamba watu watendao mambo ya jinsi hiyo hawataurithi ufalme wa Mungu”.
Hapo mstari wa 21, anasema “ANATUAMBIA MAPEMA”..Maana yake ni kwamba siku ile tutakapojikuta tumekataliwa na Kristo kutokana na kuukataa utakatifu…tusije tukasema tulikuwa hatujui!…Ndio maana hapo anatuambia mapema kuwa waasherati, wagomvi, wanaoabudu sanamu n.k hawataurithi uzima wa Milele.
Na pia katika Waefeso ni jambo hilo hilo linajirudia…
Waefeso 5:5 “Maana neno hili mnalijua hakika, ya kwamba hakuna mwasherati wala mchafu wala mwenye tamaa, ndiye mwabudu sanamu, aliye na urithi katika ufalme wa Kristo na Mungu”.
Ndugu ni vizuri kuzifurahia fadhili za Mungu, tunapoumwa anatuponya, tunapokuwa katika mashaka anatupa faraja, tunapozungukwa na hatari anatuokoa..ni vizuri kuzifurahia hizo, kwasababu ndio uthibitisho kwamba tunaye Baba mbinguni, lakini hizo zisitupumbaze tukambweteka na kufikiri kuwa ndio tayari anapendezwa na sisi,.. ndio tayari tiketi za kutuingiza mbinguni…hapana! bado kuna jambo lingine la muhimu la kufanya, nalo ni utakatifu.
Hivyo ni lazima tuishi maisha masafi na ya utakatifu na ya toba kila siku. Ili tuwe na uhakika wa kumwona Baba siku ile.
Bwana atubariki.
jiunge na channel yetu Kwa kubofya hapa >> WHATSAPP
Kama hujaokoka, wokovu unapatikana bure.. Unachopaswa kufanya leo ni kutubu kwa kumaanisha kuacha dhambi, na Roho Mtakatifu atashuka juu yako, na kukusafisha kabisa na kukupa uwezo wa kushinda dhambi, jambo ambalo kwa nguvu zako mwenyewe huwezi!.Na utapata raha ya wokovu
Maran atha!
Tafadhali unapowashirikisha wengine ujumbe huu usipunguze wala kuongeza chochote, wala usiweke anwani au namba yoyote tofauti na hizi zilizopo hapa,
Na pia kama utapenda tuwe tunakutumia mafundisho ya Neno la Mungu ya mara kwa mara kwa njia ya email yako au Whatsapp basi tutumie ujumbe kwenye namba hii +255 789001312 / 0693036618
Mada Nyinginezo:
JINA LAKE KWA KIEBRANIA NI ABADONI, NA KWA KIYUNANI NI APOLIONI.
Kibiblia via ni viungo vya mwili wa mwanadamu au mnyama,, husasani mikono au miguu.
Hivi ni baadhi ya vifungu vinavyolitaja Neno hilo;
Ayubu 17: 7 “Jicho langu nalo limekuwa giza kwa sababu ya majonzi, Na via vyangu vyote vimekuwa kama kivuli”.
Ayubu 18:13 “Utakula via vya mwili wake, Naam, mzaliwa wa kwanza wa mauti atavila via vyake”.
Ayubu 41:12 “Sitanyamaa kusema habari za via vyake, Wala nguvu zake kuu, wala umbo lake zuri”.
Shalom.
jiunge na channel yetu Kwa kubofya hapa >> WHATSAPP
Tazama mana ya maneno mengine chini;
Je utapenda tuwe tunakutumia mafundisho ya Neno la Mungu ya mara kwa mara kwa njia ya email yako au Whatsapp? basi kama ni hivyo tutumie ujumbe kwenye namba hii +255 789001312 / 0693036618
Mada Nyinginezo:
Jina la Bwana wetu Yesu Kristo libarikiwe, nakukaribisha katika kuyatafakari maneno ya uzima, na leo tena kwa neema za Bwana tutajikumbusha juu ya mambo ya msingi ya kuzingatia siku hizi za mwisho
Tukisoma biblia tunaona Yakobo alikuwa na wana 12, na kila mmoja alikuwa na tabia yake ya kipekee, Yusufu alikuwa na ya kwake, Yuda alikuwa na ya kwake, Benyamini alikuwa na ya kwake, na wengine wote. Vivyo hivyo na uzao wao mbeleni nao pia ukaja kuwa na tabia zao za kipekee kujitofautisha na kabila lingine, kabila la Yuda lilikuwa na tabia yake, kabila la Lawi lilikuwa na ya kwake n.k.
Sasa leo hatutaangalia tabia za makabila yote, lakini tutaangalia tabia la kabila la Isakari, ni nini walikuwa nacho, Biblia inatuambia ilipofika wakati Mfalme Sauli amekufa, na anatafutwa mrithi wa ufalme wake pale Israeli, kulihitajika hekima katika kuchagua, ikumbukwe kuwa hapo kabla kulikuwa na mvutano Fulani wa makabila hayo hususani, lile la Benyamini ambalo mfalme Sauli alitokea huko, lenyewe lilikuwa linataka warithi waendelee kutokea katika uzao wa Sauli kwasababu Sauli alitokea kwenye kabila hilo, wakati makabila mengine yanamtaka Daudi ayamiliki.
Hivyo katika mazingira kama hayo, kulihitajika watu wenye akili ambao wanaweza kutambua majira na nyakati kwa wakati huo, kwamba ni nani anapaswa awe mfalme. Sasa kwa kuwa Israeli ilikuwa inajua wanapofikia saa kama hiyo wamtafute nani na nani, ndipo wote wakawaendea wana wa Isakari, na kuwasikiliza wanasema nini.
Sasa ili kufahamu habari yote, unaweza kwenda kusoma 1Nyakati 11-12 yote, hapa tutakiweka kile kifungu tu kinalielezea kabila hili la Isakari,
1Nyakati 12:32 “Na wa wana wa Isakari, watu wenye akili za kujua nyakati, kuyajua yawapasayo Israeli wayatende; vichwa vyao walikuwa watu mia mbili NA NDUGU ZAO WOTE WALIKUWA CHINI YA AMRI YAO”.
Unaona, Israeli kabla hawajafanya uamuzi wowote, waliwafuata kwanza hawa wana wa Isakari, ili kuuliza ni nini wanachopaswa wafanye kwa wakati huo, wasije baadaye kuingia matatizoni, walikuwa wapo tayari kujiweka chini ya amri yao, kama maandiko yanavyotuambia, haijalishi watakachoambiwa kitakuwa ni kinyume na matarajio yao..Na hiyo yote ni kwasababu waliwatambua kuwa Mungu aliwapa akili ya kujua nyakati na majira, kuijua torati, na kuisikia sauti ya Mungu inataka nini.
Ulipokuwa unafika wakati kama huo, makabila yote yaliondoa tofauti zao, wakasikilize ni nini Mungu anawaonya kupitia wana wa Isakari. Sio kwamba makabila mengine yalikuwa madhaifu hapana, biblia inasema kabila la Yuda lilishinda zaidi ya yote, na Nyumba ya Yusufu ilikuwa ni kuu. Lakini kuhusu hatma ya maisha yao, ya wakati ule na mbeleni, Isakari walihitajika sana. Na hiyo iliisababishia Israeli, ikae katika Nuru wakati wote.
Vivyo hivyo katika agano jipya, hatupaswi kuishi tu, ilimradi tunaishi, sio kusema nimeokoka tu, sio kusema Bwana atanibariki tu, sio kusema twende kanisani tutimize wajibu kama kawaida, hiyo peke yake haitoshi, tunapaswa tutafute ni nini Mungu anasema juu ya wakati huu na majira haya; Lakini cha kusikitisha ni kuwa Bwana Yesu alisema sisi ndio tulio nyuma kabisa katika kutambua majira tuliyo nayo, na kibaya zaidi, tunafanya hivyo kwa unafiki, na sio kwamba hatufahamu.
Luka 12:54 “Akawaambia makutano pia, Kila mwonapo wingu likizuka pande za magharibi mara husema, Mvua inakuja; ikawa hivyo.
55 Na kila ivumapo kaskazi, husema, Kutakuwa na joto; na ndivyo ilivyo.
56 Enyi wanafiki, mwajua kuutambua uso wa nchi na mbingu; imekuwaje, basi, kuwa hamjui kutambua majira haya”?
Unaona? Watu wa kipindi kile kwasababu waliipuuzia kujifunza juu ya nyakati zao na majira yao, walishindwa hata kujua kuwa wanatembea na Mungu mwenyewe duniani katika umbo la kibinadamu, mpaka sisi tunasema laiti tungekuwa kipindi chao tungelala na kutembea na Bwana Yesu wakati wote..
Lakini na wao pia huko walipo leo hii wanatuona sisi wa nyakati hizi za mwisho, ni jinsi gani tupo karibu sana na ule mwisho, wanasema laiti na wao wangekuwepo wakati wetu wangeishi maisha ya kama ya wapitaji tu hapa duniani, kwasababu muda tuliobakiwa nao ni mchache, Yesu yupo mlangoni kurudi na unyakuo ni wakati wowote…
Lakini ni kwanini tunaishi kama tunavyoishi leo hii, ni kwasababu, hatujui majira tuliyopo. Hatujui kuwa tangu kipindi cha Bwana Yesu hadi unyakuo kulitakiwa kupite kipindi cha makanisa saba, na kwamba sita ya kwanza yameshapita, na hili tunaloishi ndilo la mwisho la 7, lijulikanalo kama Laodikia sawasawa na Ufunuo 3:14 na hakutakuwa na kanisa lingine zaidi ya hili, sisi ndio tutakaoshuhudia tukio zima la Unyakuo. Kwamba lile juma la 70 la Danieli lipo karibuni kuanza kuhesabiwa.
Hatujui kuwa hii neema itakwenda kurudi Israeli siku za hivi karibuni, kama unabii wa biblia inavyotabiri, kwasababu tayari limeshakuwa taifa huru, na hivyo kinachosubiriwa ni unyakuo tu, Mungu akawarudie watu wake kama alivyowaahidi katika siku za mwisho.
Hatujui kuwa, roho ya mpinga-Kristo inafanya kazi tayari katikati ya madhehebu mengi, na kama hatuna macho ya rohoni, chapa tutaipokea tu pasipo hata sisi wenyewe kujua. Kwa ufupi hakuna dalili ambayo haijatimia inayozungumzia juu ya nyakati hizi za mwisho tukiachilia mbali kuibuka kwa wimbi la makristo na manabii wa uongo, biblia ilizungumzia Tauni(Corona), mafundisho potofu, na kuachiliwa kwa nguvu ya upotovu, ili watu waendelee kuamini uongo wapotee waende kuzimu n.k.
Embu tujitathimini maisha yetu tena, Je! bado tupo katika mstari au tunayumba yumba, Je! tunafahamu majira na nyakati kama wana wa Isakari?, au tupo tu, tunasubiria mambo hayo yatukute kwa ghafla tu,.tubakie kusema laiti tungejua..Bwana atusaidie tusifike huko wakati wa kujua ndio huu. Tunaishi katika saa ya kurudi kwa pili kwa Kristo, muda tuliopewa ni wa nyiongeza tu.
Shalom.
jiunge na channel yetu Kwa kubofya hapa >> WHATSAPP
Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema, na pia kama utapenda tuwe tunakutumia mafundisho ya Neno la Mungu ya mara kwa mara kwa njia ya email yako au Whatsapp basi tutumie ujumbe kwenye namba hii +255 789001312 / 0693036618
Mada Nyinginezo: