DON’T BE AFRAID WHEN YOU GO DOWN.

HISIA YA MUNGU ILIYO MBAYA KULIKO ZOTE.

Tabia hizi zote tunazozionyesha zitokazo ndani yetu kwa mfano, furaha, amani, upendo, hasira, ghadhabu, wivu, uchungu, huruma, n.k. asili yake sio sisi bali ni Mungu, kwasababu sisi tumeumbwa kwa mfano wa Mungu kama maandiko yasemavyo, hivyo hizi ni baadhi tu ya tabia ambazo Mungu mwenyewe alikuwa nazo kabla hata ya ulimwengu kuwako.

Sababu ya Mungu kuviruhusu vitu kama hivi vitokee ndani yetu, ni kutufundisha sisi kwa vitendo ili tuyajue mapenzi yake ni nini. Pale tunapoweza kuuhisi upendo au kuutoa upendo kwa wengine, basi tunafahamu kuwa yupo ambaye anayeitwa Upendo mwenyewe, na hivyo hiyo inatufanya sisi kuilewa vizuri asili ya Mungu tofauti na kama tungekuwa tumehadithiwa tu kuwa Mungu anatupenda halafu hatujawahi kuhisi upendo wowote ndani yetu, au hatujui upendo ni kitu gani. Ni wazi kabisa kuwa tusingemwelewa Mungu vizuri, na vivyo hivyo katika mambo mengine mema kama vile huruma, furaha, amani, faraja,fadhili, upole, unyenyekevu n.k. Yote hayo tusingeweza kuyapokea kutoka kwa Mungu kama asingetuonjesha mambo hayo ndani yetu sisi wenyewe pale tunapohudumiana sisi kwa sisi.

Lakini pia upo upande wa pili wa hisia hizo, ambao huo sio mzuri sana, na kila mwanadamu amepewa, kwamfano hasira sio jambo jema, na hasira huja kwa kuudhiwa, na tunajua hakuna mtu hata mmoja anayependa kuudhiwa, lakini hasira hutokea yenyewe ndani pale mambo kama hayo yanapokuja, si kwamba mtu anaitengeneza hapana, bali ni jambo ambalo linatokea lenyewe pale vitu kama maudhi au makwazo vinapozuka kinyume na matarajio yake, kadhalika na mambo mengine kama ghadhabu, uchungu, huzuni, sononeko n.k.

Lakini lipo jambo ambalo linafunika vyote katika hisia mbaya, kama vile UPENDO unavyofunika hisia zote nzuri, kadhalika katika upande wa hisia mbaya lipo jambo linalofunika hisia zote kwa ubaya na hili si lingine zaidi ya WIVU. Wivu nao unaweza kuja kwa sababu nyingi lakini wivu ulio wa kiwango cha juu ni ule wivu unaokuja kwasababu ya mpenzi (mke au mume).

Kwasababu kiwango cha juu kabisa cha hisia nzuri (yaani upendo) huwa kinatoka kwa mpenzi, kadhalika na kiwango cha juu kabisa cha hisia mbaya (yaani wivu), huwa kinatoka kwa huyo huyo mpenzi. Hasira inaweza kuleta madhara ya hasira, ghadhabu inaweza kuletea madhara ya ghadhabu peke yake, uchungu unaweza kuleta madhara ya uchungu pekee yake,lakini kitu kinachoitwa WIVU ni mbali sana na hivi vingine hicho kinajumuisha vyote humo humo, ni kiwango cha juu kabisa cha hisia mbaya kwa mwanadamu, na ndivyo ilivyo hata kwa Mungu, na sababu kubwa ya wivu ni USALITI.

Leo hii ni wazi kabisa kuona watu wakijiua, watu wakiua wengine, watu wakisaliti hata wazazi wao ndugu zao,kwa ajili ya wivu wa mpenzi, watu wakimkosea Mungu wakienda hata kwa waganga, watu wakilipiza visasi vibaya kwa sababu ya jambo dogo tu la wivu wa mapenzi, watu wanapigana kila siku kwa ajili ya jambo hilo, wengine wanafanya uhalifu n.k. Kwa ufupi pale mtu anapofikia kiwango cha juu sana cha wivu basi mtu huyo huwa anaamua kufanya jambo lolote lile bila kujali ni madhara mangapi anaweza kuleta katika jamii yake au kwake mwenyewe kwa tukio hilo. Kwasababu ni jambo ambalo limechanganyikana na hasira humo humo, uchungu humo humo, ghadhabu humo humo, huzuni humo humo na kila kitu, Hivyo ili watu kuepuka na hilo mapema kabisa kabla hawajingia katika vifungo vya ndoa, huwa wanaingia kabisa katika mapatano kuwa huko mbele hawataumizana kwa kusalitiana.

Na ndio maana biblia inasema katika:

Mithali 27: 4 “Ghadhabu ni kali, na hasira ni gharika; LAKINI NI NANI AWEZAYE KUSIMAMA MBELE YA WIVU”.

Mungu ameziweka hizo hisia makusudi ndani ya wanadamu ili waweze nao kumwelewa pale anaposema jambo Fulani ni chukizo kwake, wajue alimaanisha linamchukiza kweli kweli , anaposema MIMI NI MUNGU MWENYE WIVU (Kutoka 20:5). Wajue kuwa kwa jinsi ile ile wivu unavyokula ndani yao ndivyo unavyokula ndani ya moyo wa Mungu, Na hivyo inawapasa wachukue sana tahadhari kujiepusha nayo, kwasababu wasipofanya hivyo basi wao wenyewe watakuwa wamejiweka katika hatari ya kupatwa na madhara makubwa sana yatokanayo na wivu wake.

Katika agano la kale Mungu alikuwa anatiwa wivu pale anapokuwa anaona watu wake wanaacha kumwabudu yeye, wanageukia masanamu na kuyafanya kuwa ndio miungu yao, jambo ambalo alishawaonya tangu zamani kwenye zile amri kuu 10 akisema:

Kutoka 20: 2 “Mimi ni Bwana, Mungu wako, niliyekutoa katika nchi ya Misri, katika nyumba ya utumwa.

3 Usiwe na miungu mingine ila mimi.

4 Usijifanyie sanamu ya kuchonga, wala mfano wa kitu cho chote kilicho juu mbinguni, wala kilicho chini

duniani, wala kilicho majini chini ya dunia.

5 Usivisujudie wala kuvitumikia; kwa kuwa mimi, Bwana, Mungu wako, NI MUNGU MWENYE WIVU; nawapatiliza wana maovu ya baba zao, hata kizazi cha tatu na cha nne cha wanichukiao”,.

Unaona lakini wengi wao hawakuijali hiyo hisia mbaya ya Mungu wakaendelea kufanya hivyo angali wanajua kabisa waliyokuwa wanayafanya sio sahihi. Matokeo yake ikawapelekea Mungu kuwapiga kwa mapigo ya kila namna, wanyama wakali, njaa, upanga,magonjwa ya kila namna, na mwisho wa siku wakaondolewa katika nchi ambayo Mungu aliwaambia itakuwa urithi wao milele, nchi ambayo Mungu aliwaapia itawazaliwa wenyewe, nchi ibubujikayo maziwa na asali. Lakini sasa imebalika na kuwa kinyume chake, kutokana na njia zao mbaya mbele zake.

Vivyo hivyo na katika agano jipya, kumbuka agano la kale ni kivuli cha agano jipya, mambo yale ambayo Mungu alikuwa anayachukia wakati ule ndiyo hayo hayo anaendelea kuyachukia hata wakati huu, na tena sasa hivi tunapaswa tuwe makini zaidi kwasababu Mungu ameuweka wivu wake kwa uwazi zaidi kuliko ilivyokuwa ameuweka katika agano la kale.

Kwani kipindi kile Wivu wale aliufunua tu katika mambo ya nje, kwenye ibada za sanamu za nje, lakini sasa sio tu zile za nje, bali pia na zile zinazotoka rohoni. Embu tuzitamaze kwa ufupi sanamu hizo.

1.SANAMU ZA NJE! ZA SASA.

1Wakorintho 10: 14 “Kwa ajili ya hayo, wapenzi wangu, ikimbieni ibada ya sanamu.

15 Nasema kama na watu wenye akili; lifikirini ninyi ninenalo.

16 Kikombe kile cha baraka tukibarikicho, je! Si ushirika wa damu ya Kristo? Mkate ule tuumegao, si ushirika wa mwili wa Kristo?

17Kwa kuwa mkate ni mmoja, sisi tulio wengi tu mwili mmoja; kwa maana sisi sote twapokea sehemu ya ule mkate mmoja.

18Waangalieni hao Waisraeli walivyokuwa kwa jinsi ya mwili; wale wazilao dhabihu, je! Hawana shirika na madhabahu?

19 Basi niseme nini? Ya kwamba kile kilichotolewa sadaka kwa sanamu ni kitu? Au ya kwamba sanamu ni kitu?

20 Sivyo, lakini vitu vile wavitoavyo sadaka wavitoa kwa mashetani, wala si kwa Mungu; nami sipendi ninyi kushirikiana na mashetani. Hamwezi kunywea kikombe cha Bwana na kikombe cha mashetani.

21 Hamwezi kushirikiana katika meza ya Bwana na katika meza ya mashetani.

22 AU TWAMTIA BWANA WIVU? Je! Tuna nguvu zaidi ya yeye?”.

Unaona hapo?, matambiko, na mila mtu asizozijua maana yake, unakuta mtu anakwenda kufanya huko kijijini kwake, hajui kuwa unafanya ushirika na mashetani badala ya Mungu, anakwenda kwenye ngoma na hivyo anamtia Mungu wivu kwa ibada hizo za masanamu anazozifanya, anakwenda kwa waganga, anakwenda kwa wasoma nyota. anaabudu sanamu za watakatifu waliokufa zamani (sanamu za bikira Maria, Mt Petro n.k), anafanya kazi katika makampuni ya pombe, au sigara, au ya biashara haramu au anauza hivyo vitu. Hizo zote ni ibada za sanamu na kibaya zaidi bado mtu huyo anajiita mkristo hujui kuwa anamtia Mungu wivu ambao huo hauzimwi kwa namna yoyote ile, isipokuwa mauti, biblia inasema ni NI NANI AWEZAJE KUSIMAMA MBELE YA WIVU?

2. SANAMU ZA NDANI.

Wakolosai 3:5-9

“5 Basi, vifisheni viungo vyenu vilivyo katika nchi, uasherati, uchafu, tamaa mbaya, mawazo mabaya, na kutamani, NDIYO IBADA YA SANAMU;

6 kwa ajili ya mambo hayo huja ghadhabu ya Mungu.

7 Katika hayo ninyi nanyi mlitembea zamani, mlipoishi katika hayo.

8 Lakini sasa yawekeni mbali nanyi haya yote, hasira, na ghadhabu, na uovu, na matukano, na matusi vinywani mwenu.

9 Msiambiane uongo, kwa kuwa mmevua kabisa utu wa kale, pamoja na matendo yake;”

Unaona hapo?, hata uasherati mtu anaoufanya ni ibada za sanamu, pornography ni ibada za sanamu, ushoga, usagaji, mustarbation, uasherati yote hayo ni ibada za sanamu mbele za Mungu, biblia inaendelea kusema matusi midomoni na lugha chafu, uovu, n.k. yote hayo ni ibada za sanamu na hivyo kwa hayo mtu anamtia wivu Mungu kila siku anavyozidi kuendelea kufanya. Na ghadhabu ya Mungu, inaujilia ulimwengu mzima kwasababu ya hayo.

Hivyo ndugu, tuikwepe ghadhabu ijayo kutokana na wivu wake, Kwasababu wivu huleta visasi hivyo tukae mbali na kisasi cha Mungu kila siku tuishi maisha ya kujitakasa ikiwa sisi ni wakristo.. Lakini kama upo nje ya ukristo (yaani hujampa Bwana maisha yako). Mungu pia hapendezwi na njia zako, ni heri ukageuka sasa, na kutubu angali muda upo, ukabatizwe katika ubatizo sahihi wa kuzamishwa na kwa jina la YESU upate ondoleo la dhambi zako, kisha Bwana atakupa Roho wake mtakatifu kukulinda na kukufundisha. Ni maombi yangu utafanya hivyo na Bwana akuangazie Nuru yake.

“Watoto wadogo, jilindeni nafsi zenu na sanamu.( 1Yohana 5:21)”

Ubarikiwe.

Print this post

HERI, WALE MUNGU ASIOWAHESABIA MAKOSA YAO.

Shalom! Mtu wa Mungu karibu tujifunze maandiko, kwa pamoja. Maandiko yanatuambia katika kitabu cha Zaburi 32:1-2 kwamba…

Zaburi 32:1 “Heri aliyesamehewa dhambi, Na kusitiriwa makosa yake.

Heri Bwana asiyemhesabia upotovu, Ambaye rohoni mwake hamna hila.”

Mstari huu pasipo ufunuo wa Roho ni mgumu kidogo kueleweka, unaweza ukajiuliza inakuwaje Mungu aliye mkamilifu na asiyechangamana na dhambi kuwa na kikundi cha watu Fulani ambao hata watendeje dhambi yeye hawahesabii makosa, na wakati huo huo pia anacho kikundi cha watu ambao kila dhambi wanayoitenda ina hesabiwa mbele zake. Ni mstari kidogo wenye utata na mgumu kuelewa.

Lakini ashukuriwe Mungu kwa kumpa Mtume Paulo ufunuo wa Neno hilo kwa uweza wa Roho, ambaye alielezea kwa undani kabisa maana ya mstari huu Mfalme Daudi aliouandika katika Zaburi 32. Alisema…

Warumi 4: 6 “Kama vile Daudi aunenavyo uheri wake mtu yule ambaye Mungu amhesabia kuwa na HAKI PASIPO MATENDO,

7 Heri waliosamehewa makosa yao, Na waliositiriwa dhambi zao.

8 HERI MTU YULE AMBAYE BWANA HAMHESABII DHAMBI.”

Unaona hapo! Paulo anaelezea vizuri kuwa uheri ni kwa wale ambao Mungu ANAWAHESABIA HAKI PASIPO MATENDO, yaani wale waliompokea Bwana Yesu Kristo na kuvua utu wa kale na kuvaa upya, hao ndio kundi la watu ambao Mungu hawahesabii makosa yao haleluya!.

Sasa swali lingine linakuja..Je! watu waliompokea Bwana Yesu na kupokea kipawa cha Roho Mtakatifu na kuzaliwa mara ya pili wanakuwa na makosa? Na wakati huo huo maandiko yanasema katika 1 Yohana 3: 9 “Kila mtu aliyezaliwa na Mungu hatendi dhambi, kwa sababu uzao wake wakaa ndani yake; wala hawezi kutenda dhambi kwa sababu amezaliwa kutokana na Mungu”.

Maadamu tunaishi katika huu mwili hatuwezi kuwa wakamilifu asilimia 100, tunayo madhaifu mengi na kuna makosa tunayoyafanya mengi pasipo kujua hata kama hatutayaona, hayo ndio makosa ambayo kwa mtu aliyezaliwa mara ya pili, Mungu hayahesabu, Na pia mtu aliyezaliwa mara ya pili hawezi kutenda dhambi kwa makusudi, hawezi kwenda kuzini, au kuiba, au kutukana, au kula rushwa..hizo ni dhambi za dhahiri kabisa na sio za madhaifu, yapo makosa ya udhaifu, kama hasira zinazomjia mtu pasipo kujijua, na ufahamu ukimrudi anajua kosa lake na haraka anakwenda kutubu na kujirekebisha, lakini sio hasira mpaka za kwenda kupiga mtu au kusababisha madhara yoyote. Na madhaifu mengine yote ambayo pengine ulimkosea Mungu au Mtu mwingine pasipo kujijua, mpaka siku alipokuja kukwambia kwamba pale ulinikosea, ndipo unapojua kosa lako. Hayo yote mbele za Mungu hayahesabu kwa wale waliompokea yeye.

Ili kuelewa vizuri maana ya mambo haya hebu tafakari mfano huu.

Mzazi (ambaye hamjui Mungu) ana mtoto wake anayempenda na hapo hapo ana mfanyakazi aliyemwajiri.

Na wote wawili wakafanya makosa kila mtu kwa sehemu yake, unadhani ni atakayepata adhabu kubwa zaidi kuliko mwingine, yupi atafukuzwa ndani ya nyumba na yupi ataachwa…ni wazi kuwa Yule mfanyakazi atafukuzwa kutoka ndani ya ile nyumba na mtoto kuachwa…. Kwahiyo hapo tunaweza kujifunza kuwa kwa namna Fulani makosa ya watoto yanafunikwa na wazazi kuliko makosa ya watu wasio watoto wao, huwezi kukuta mahali popote mzazi ambaye hamjui Mungu anamsema vibaya mwanae mbele ya watu..zaidi ya yote hapendi kusikia mwanawe anasemwa vibaya hata kama ni mwovu kiasi gani.

Na kwa Mungu wetu wa mbinguni ndio ivyo hivyo, watoto wake (yani wale waliomwamini mwanawe mpendwa Yesu Kristo), hawahesabii makosa, hata kama watakuwa na madhaifu mengi kiasi gani, yeye bado atabaki kuwa baba yao tu! Ndio maana biblia inasema WANA HERI HAO HAWAHESABIWI DHAMBI ZAO. Haleluya!.

Lakini kinyume chake ni OLE WAKE YULE AMBAYE BWANA ANAMHESABIA MAKOSA YAKE.

Sasa Mtu anahesabiwaje makosa yake?.

Kwa kutomwamini Yesu Kristo, na kutokuzaliwa mara ya pili, ni sawa na kuwa nje ya familia ya Mungu, hivyo mtu kama huyo akifanya uovu tu wowote ule uwe wa bahati mbaya uwe wa makusudi, kwasababu hana mtetezi juu yake,anakuwa kama yatima, basi huo uovu wake utahesabiwa

Hiyo ndiyo hasara aliyonayo mtu ambaye hajampokea Yesu Kristo katika ulimwengu huu tuliopo wa dhambi, anakuwa anaishi katika dunia ambayo hana kibali chochote mbele za Mungu, anakuwa anaishi katika dunia ambayo maombi yake yanakuwa hayasikilizwi na yanakuwa hayana thamani yoyote, anakuwa anatoa sadaka ambazo hazina thawabu kubwa mbele za Mungu, anakuwa anatenda wema ambao hauhesabiki au kama unahesabika unakuwa na thamani na heshima ndogo sana mbele za Mungu. Kamwe anakuwa hawezi kumpendeza Mungu. Siku zote anakuwa hana amani na maisha yake.

Ndio maana utasikia wengi leo hii wanakwambia “mimi kumfuata Yesu siwezi” lakini natenda mema halafu anaulizwa kwani nitahukumiwa??..Ndugu yangu wema wako nje ya familia ya MUNGU ni kupoteza Muda..Fanya hima uwe kwanza MWANA WA MUNGU ili wema wako uweze kuhesabiwa!. Hata wauzaji wa madawa ya kulevya wapo wakarimu, kuliko wewe, lakini Mungu hawatambui kwasababu sio wake,…Ni sawa na mfanyakazi anayejitahidi kumpendezesha bosi wake kwa kufanya kazi kwa bidii, na kuwa mwaminifu ili mwisho wa siku awe mrithi, hata atende wema mwingi kiasi gani URITHI atapewa Mtoto wa Yule Bosi hata kama Yule mtoto ni mpumbavu kiasi gani.

Na ndicho tunachopaswa kufanya sisi, sio kutafuta kutenda mema kwanza, hapana bali kutafuta kuwa WANA WA MUNGU. Kutafuta kuzaliwa mara ya pili kutoka katika kuwa WATUMWA WA DHAMBI(Wafanya kazi) na KUWA WANA WA MUNGU, Ndipo tutapata kibali mbele za Mungu katika hii dunia tunayoishi na katika ulimwengu ujao.

Kama hujampa Bwana maisha yako, huu ndio wakati, usisubiri kesho kwasababu biblia inasema “usijisifu kwa ajili ya kesho kwasababu hujua yatakayozaliwa katika siku moja”..Kesho huijui, mkabidhi Bwana leo maisha yako, unachotakiwa kufanya ni kutubu kabisa dhambi zako kwa kudhamiria kuziacha kuzifanya kuanzia leo na kuendelea, kisha baada ya hapo haraka sana nenda katafuta mahali wanapobatiza ubatizo sahihi wa maji mengi na kwa jina la YESU KRISTO kama hujabatizwa bado,(Zipo batizo nyingi, lakini unapaswa uujue ubatizo sahihi wa kimaandiko ni upi kwa ajili ya ondoleo la dhambi zako).

kisha baada ya kubatizwa Bwana Mwenyewe atafanya yaliyosalia,atakupa kipawa cha Roho wake Mtakatifu atakayekuwezesha kushinda dhambi na kukuongoza katika kuijua kweli yote ya Biblia. Na hapo utakuwa umeshazaliwa mara ya pili kulingana viwango vya Baba wa Mbinguni anavyovitaka yeye, lakini ukiendelea kudumu katika UTAKATIFU, basi utakuwa nawe ni mmoja wa wana wa Mungu, wasiohesabiwa makosa yao, na wanaopewa thawabu haraka hata kwa yale madogo wanayoyafanya, utakuwa miongoni mwa waliobarikiwa wazao wateule, ukuhani wa kifalme, watu wa Milki ya Mungu, warithi wa Utajiri wote wa Mungu.

Print this post

IELEWE SAUTI YA MUNGU.

Shalom Mwana wa Mungu, karibu tujifunze kwa pamoja Neno la Mungu, na Leo tutajifunza moja ya njia ya kuielewa sauti ya Mungu inapozungumza nasi.

Kwanza ni muhimu kufahamu kuwa Mungu ni Mkuu, Upeo wake na mawazo yake yapo mbali sana, mahali ambapo hatuwezi kuyafikia…Kwahiyo kwa ukuu wake namna hiyo tunajua kabisa hakuna mwanadamu yoyote atakayeweza kumwelewa kama akitaka kuzungumza na sisi katika ukuu wake wote.

Kwahiyo kwasababu yeye ni mkuu na katuumba sisi watu wake katika hali ya udogo, hawezi akazungumza na sisi kwa lugha zake, bali atazungumza na sisi kwa lugha nyepesi na inayoeleweka, ili tuweze kumwelewa. Hata na sisi pia huwa tunapokuwa na mifugo yetu, hatuwezi kuzungumza nayo kama tunavyozungumza na wanadamu wenzetu, kama tukifanya hivyo ni wazi kuwa mifugo haitatuelewa ni sharti tutumie vitendo au sauti watakazozielewa kama miluzi au kutumia ishara fulani.

Kwasababu hiyo basi Mungu naye anazungumza na sisi kwa lugha za kibinadamu, kwa sauti za kibinadamu, kwa lafudhi za kibinadamu..Kwasababu mfano akizungumza na sisi kwa lugha za malaika hatutamwelewa, kwa lafudhi za kimbinguni hatutamsikia. Na endapo angejishusha zaidi na kuzungumza na sisi kwa ngurumo na radi na umeme, ndio kabisa tusingemwelewa, tungeishia kumwogopa badala ya kumpenda n.k.

Na ndio maana tunasoma Katika kitabu cha 1Samweli 3, Bwana akizungumza na Samweli kwa sauti inayofanana na ya Eli. Tunaona hakumwita kwa sauti ya mawimbi au radi, bali kwa sauti kama ya Baba yake wa kiroho. Mpaka Samweli akadhani ni Eli ndiye anayemwita. Na tunaona hakuishia kumwita mara moja bali alimwita kwa sauti ile ile mara nne.

1 Samweli 3:1-8 “Basi, mtoto Samweli akamtumikia Bwana mbele ya Eli. Na neno la Bwana lilikuwa adimu siku zile; hapakuwa na mafunuo dhahiri.

2 Ikawa wakati huo, Eli alipokuwa amelala mahali pake (tena macho yake yalikuwa yameanza kupofuka, hata asiweze kuona),

3 na taa ya Mungu ilikuwa haijazimika bado, na Samweli alikuwa amelala katika hekalu la Bwana, palipokuwa na sanduku la Mungu;

4 basi, wakati huo Bwana akamwita Samweli; naye akasema, Mimi hapa.

5 Akamwendea Eli kwa haraka, akasema, Mimi hapa; kwa maana uliniita. Akasema, Sikukuita; kalale tena. Naye akaenda, akalala tena.

6 Bwana akaita mara ya pili, Samweli! Samweli! Akaondoka akamwendea Eli, akasema, Mimi hapa; kwa maana uliniita. Akajibu, Sikukuita, mwanangu; kalale tena.

7 Basi Samweli alikuwa hamjui Bwana bado, na neno la Bwana lilikuwa bado halijafunuliwa kwake.

8 Bwana akamwita Samweli mara ya tatu. Naye akaondoka akamwendea Eli, akasema, Mimi hapa; kwa maana uliniita. Ndipo Eli akatambua ya kuwa Bwana ndiye aliyemwita yule mtoto.”

Umeona hapo? Ni mara nyingi tumekuwa tukitafuta kuisikia sauti ya Mungu kwa namna nyingi, lakini ni muhimu kujua kwamba sauti ya Mungu haipo mbinguni, sauti ya Mungu ipo pamoja nawe pale ulipo. Ipo karibu sana na wewe, ipo hapo ulipo moyoni mwako au pembeni kidogo chumba cha pili kinachofuata cha jirani yako aliye mkristo.

Kumbukumbu 30: 11 “Kwa maana maagizo haya nikuagizayo leo, si mazito mno kwako, wala si mbali.

12 Si mbinguni, hata useme, Ni nani atakayetupandia mbinguni akatuletee, aje atuambie tusikie, tupate kuyafanya?

13 Wala si ng’ambo ya pili ya bahari, hata useme, Ni nani atakayetuvukia bahari, akatuletee, aje atuambie, tusikie, tupate kuyafanya?

14 Lakini neno li karibu nawe sana, li katika kinywa chako na moyo wako, upate kulifanya”.

Sauti ya Mungu haifanani na ya Malaika kwetu sisi, hapana sauti ya Mungu inafanana na sauti zetu sisi wanadamu, kiasi kwamba anapozungumza na sisi tusipokuwa makini tunaweza kudhani kuwa tunazungumza na wanadamu. Samweli pengine alifundishwa kuwa Mungu huwa anazungumza kutoka mbinguni, na akizungumza basi bahari na kuzimu, na mbingu na nchi zinatetemeka..Hiyo ni kweli, lakini hapa tunasoma sauti ya Mungu ilipoita ilisikika kama inatoka chumba kinachofuata, na ilifanana sana na sauti ya Baba yake wa kiroho aliyekuwa anamfundisha njia za wokovu.

Ndugu/Dada unayesoma ujumbe huu, mahali popote ulipo sauti ya Mungu ipo inazungumza na wewe, unaposikiliza Mahubiri au Mafundisho yanayohubiriwa na mtu fulani, yanayohusiana na wokovu wako, hiyo ni sauti ya Mungu inazungumza nawe..usijaribu hata kidogo kufikiri ni yule mtu ndiye anayezungumza na wewe la! Ni Mungu ndiye anayezungumza nawe, katika sauti ya Yule mtu.

Mahali popote usikiapo Mahubiri ya kutubu dhambi, ni sauti ya Mungu ikikukumbusha kile alichokiandika katika Neno lake (Biblia takatifu), kwamba wenye dhambi wote hawataurithi ufalme wa mbinguni, Mahali popote usikiapo habari za maonyo yahusuyo hukumu inayokuja hiyo ni sauti ya Mungu ikikukumbusha kile kilichoandikwa katika Biblia yake takatifu (juu ya hukumu itakayoijia ulimwengu mzima).

Kwahiyo usikiapo hiyo sauti usimkimbilie yule mtu anayekuhubiria na kudhani ni yeye ndiye anayezungumza na wewe kama Samweli alivyomkimbilia Eli, Kwasababu ukifanya hivyo basi anaacha kwanza kuzungumza na wewe, badala yake mkimbilie Mungu anayezungumza nawe moyoni mwako pale ulipo, Itii sauti yake na mgeukie yeye, Na kumwambia Bwana “ Zidi zungumza nami kwa kuwa mtumishi wako anakusikia, mwambie nibadilishe kwa kuwa mtumishi wako anakusikia” acha kuishi maisha ya dhambi kuanzi wakati huo na kuendelea, acha maisha ya ulevi, maisha ya uchawi, ya usengenyaji, ya uasherati,ya utazamaji pornography, ya ufanyaji masturbation, ya wizi,ya kamari, ya utukanaji, ya ulaji rushwa n.k n.K. Mtii Mungu na kuanza kuishi maisha yanayokubalika mbele zake, kwa kuacha kuvaa nguo zisizofaa; kama vimini, suruali,nguo zinazobana na upakaji wanja na lipstick..Jitenge na hivyo vyote kwasababu ndivyo vinavyowapeleka mamilioni ya watu kuzimu. Na sauti ya Bwana inakuonya leo uviache hivyo vyote.

Bwana Yesu alisema katika Yohana 3:3 “…Amin, amin, nakuambia, Mtu asipozaliwa mara ya pili, hawezi kuuona ufalme wa Mungu.”. Unazaliwa mara ya pili kwa kumwamini Yesu Kristo kwamba alitumwa na Mungu, akaishi duniani maisha matakatifu yanayokubalika na Mungu akampendeza Mungu, akakushuhudiwa kuwa ndiye pekee ampendezaye Mungu, akasulibiwa kwa ajili ya dhambi zetu, akafa, akazikwa na siku ya tatu akafufuka, akapaa mbinguni, naye amewekwa kuwa mpatanishi wa sisi na Mungu na hakuna mwingine, na atarudi tena kuja kulinyakua kanisa lake kwenda nalo mbinguni.

Baada ya kumwamini hivyo..Hatua inayofuata ni kukusudia na kudhamiria kuacha maisha ya dhambi uliyokuwa unaishi huko nyuma maisha yote ya usengenyaji, maisha yote ya ulevi na uvutaji sigara, maisha yote ya kikahaba na utoaji mimba, maisha yote ya ulaji rushwa, utapeli na uwizi, maisha yote ya uashetari na uvaaji mbaya..Unasema kuanzia leo na kuendelea mimi ni hayo maisha ndio basii..!!

Ukishakusudia kufanya hivyo kwa vitendo na sio kwa mdomo tu, moja kwa moja bila kukawia nenda katafute ubatizo sahihi, huo utakuwa ni kwa ajili ya ondoleo la dhambi zako,kulingana na Matendo 2:38, na kumbuka ubatizo sahihi sio wa kunyunyiziwa, bali ni wa maji mengi, wakuzamishwa mwili wote na ni kwa jina la Yesu Kristo.

Baada ya kufuata hatua hizo mbili rahisi, utakuwa umepiga hatua moja kubwa na ya muhimu katika maisha yako, ambayo hutajutia kamwe. Na baada ya hapo Bwana atayafanya yaliyosalia kwa kukupa kipawa cha Roho wake Mtakatifu atakayekuwezesha kuishi maisha matakatifu na kukutia katika kuijua na kuielewa kweli yote ya Neno lake (Yaani Biblia takatifu). Nawe utakuwa umezaliwa mara ya pili, Mrithi wa Baraka za Mungu.

Print this post

VITA BADO VINAENDELEA.

Shetani hapo nyuma alikuwa na mamlaka na hii dunia hata kufikia hatua ya kuweza kujiamulia kufanya jambo lolote na kufanikiwa, kiasi cha kuweza hata kuzuia majibu ya maombi ya watu yasiwafikie kwa wakati haijalishi mtu huyo atakuwa ni mcha Mungu kiasi gani, bado atayazuia tu, Tunaona mambo hayo yalitokea kwa Danieli, pale alipokuwa amefunga majuma matatu akiutafuta uso wa Mungu, Na kama tunavyosoma, biblia inasema mkuu wa ufalme wa Uajemi (Pepo la uajemi ), alimzuia malaika wa Bwana kwa muda wa wiki tatu ili tu asifikishe majibu ya maombi ya Danieli, Unaona hapo vita vya kiroho vilikuwa ni vikali sana wakati ule mpaka Danieli kufikia kusema, NI VITA VIKUBWA (Danieli 10:1) haikiwa ni kazi ndogo, aliiona taabu yake.

Zaidi ya hayo Shetani alikuwa na uwezo hata wa kuwaendea watakatifu wa Mungu waliokuwa wamelala, huko sehemu za wafu na kuzungumza nao, alifahamu mahali walipo na kwenda huko,kwani funguo za mauti na kuzimu zilikuwa bado mikononi mwake.

Hivyo Shetani aliendelea, kulitawala hili anga la kiroho kwa muda mrefu sana, vitu vyote vilikuwa mikononi mwake, na ndio maana alimwambia Bwana Yesu kule nyikani “Nitakupa wewe enzi hii yote, na fahari yake, kwa kuwa imo mikononi mwangu, nami humpa ye yote kama nipendavyo”.

Unaona? Wayahudi waliliona hilo tangu zamani, hivyo walikaa katika matumaini wakingojea siku ambazo ile Nuru kuu, nyota ya Alfajiri itakapozuka Israeli na kuangaza tena katikati yao na katika ulimwengu mzima, Walikuwa wanalisubiria hilo kwa hamu, siku ambazo Mungu atawarejeshea tena lile tumaini lao lililokuwa limepotea tangu Edeni..

Maneno haya yaliwatia faraja walipoyasoma:

Isaya 49: 6 “naam, asema hivi, Ni neno dogo sana wewe kuwa mtumishi wangu [Azungumza habari za YESU] ili kuziinua kabila za Yakobo, na kuwarejeza watu wa Israeli waliohifadhiwa; zaidi ya hayo nitakutoa uwe NURU YA MATAIFA, UPATE KUWA WOKOVU WANGU HATA MIISHO YA DUNIA”.

Isaya 9:2 “Watu wale waliokwenda katika giza WAMEONA NURU KUU; Wale waliokaa katika nchi ya uvuli wa mauti, Nuru imewaangaza.”

Nuru hiyo kuu, waliitazamia wakimwomba Mungu kila siku bila kukoma.

Na ndio hapo tunakuja kuona miaka 2000 iliyopita Nuru hiyo inakuja kutokea duniani, Nuru ambayo hata wanajimu waliuona utukufu wake kwa jinsi ilivyokuwa inang’aa sana gizani, Siku ambazo alizaliwa mwokozi duniani, ni wakati ambao shetani alipatwa na wakati mgumu sana, kuliko nyakati nyingine zote ambazo alishawahi kuwa nazo. Na tunaona siku ile Bwana alipokufa na kufufuka ndipo hali yake ilipozidi kuwa mbaya zaidi, akiona kuwa ameshanyang’anywa mamlaka yote na nguvu zote, na funguo zote za mauti na kuzimu alizokuwa nazo juu ya huu ulimwengu hapo kabla.

Tunayathibitisha hayo kwa maneno yaliyotoka katika kinywa cha Kristo mwenyewe akisema:

Mathayo 28: 18 “Yesu akaja kwao, akasema nao, akawaambia, Nimepewa mamlaka yote mbinguni na duniani.”

Unaona hapo? Kauli hiyo inaonyesha kuwa kumbe hapo kabla mamlaka hayakuwa kwake, bali yalikuwa mikononi mwa mtu mwingine, na huyu si mwingine zaidi ya shetani. Sasa kuanzia huu wakati, na kuendelea vitu vyote, mamlaka yote na chochote kile unachokifahamu kilianza kumilikiwa na YESU KRISTO, Bwana wetu.Haleluya!!…Vita alishavipigana na kushinda, kama kutupwa chini basi shetani alishatupwa chini tangu siku ile pale Kalvari, hana lake tena duniani.

Na kama ni hivyo basi, hapa juu yetu mkuu wa anga anapaswa awe YESU Kristo na si pepo tena, shetani hapaswi kuamua chochote juu ya miili yetu, hapaswi kuzuia maombi yetu, hapaswi kutuamulia mbaraka wetu kutoka kwa Mungu, yeye hana uwezo wa kututajirisha wala kutufukarisha, kwa ufupi hapaswi kuonekana katika dira ya maisha yetu popote pale, kwani alishashindwa vita na anayemiliki sasa ni mwingine, hivyo yeye hastahili kuwepo duniani, atafute sehemu yake nyingine ya kumiliki, lakini si katika dunia hii,

Lakini swali linakuja kama ni hivyo basi, ni kwanini, shetani bado anaendelea kuwatesa watu?, ni kwanini bado kuna vita, ni kwanini bado tunamwona shetani akizurura zurura katikati ya maisha yetu, ni kwanini bado anatuletea matatizo kana kwamba hakuna chochote kilichofanyika pale Kalvari, Na bado Biblia bado inatuambia maneno haya:

Waefeso 6:11-18 “Vaeni silaha zote za Mungu, mpate kuweza kuzipinga hila za Shetani.

12Kwa maana kushindana kwetusisi si juu ya damu na nyama; bali ni juu ya falme na mamlaka, juu ya wakuu wa giza hili, juu ya majeshi ya pepo wabaya katika ulimwengu wa roho.

13 Kwa sababu hiyo twaeni silaha zote za Mungu, mpate kuweza kushindana siku ya uovu, na mkiisha kuyatimiza yote, kusimama.

14 Basi simameni, hali mmejifunga kweli viunoni, na kuvaa dirii ya haki kifuani,

15 na kufungiwa miguu utayari tupatao kwa Injili ya amani;

16 zaidi ya yote mkiitwaa ngao ya imani, ambayo kwa hiyo mtaweza kuizima mishale yote yenye

moto ya yule mwovu.

17 Tena ipokeeni chapeo ya wokovu, na upanga wa Roho ambao ni neno la Mungu;

18 kwa sala zote na maombi mkisali kila wakati katika Roho, mkikesha kwa jambo hilo na kudumu katika kuwaombea watakatifu wote;

Ni kwanini haya yote?. Sasa Kama utakuwa ni mfuatiliaji mzuri wa habari zinazaoendelea duniani, utakuwa umeshawahi kusikia mara nyingi juu vita vinavyoendelea katikati ya mataifa Fulani, mfano jeshi la nchi la husika pamoja na vikosi vya umoja wa mataifa utasikia vimefanikiwa kudhibiti maficho yote, na maeneo yote yaliyokuwa yanamilikiwa na waasi na hivyo waasi wametawanywa na kukimbilia katika mataifa jirani, hivyo nchi sasa ipo katika amani. Lakini utaona taifa litadumu katika amani kwa kipindi kifupi tu, halafu ghafla utasikia mapambano yamezuka tena, waasi wamevamia kambi za wanajeshi na kuwaua, au sehemu nyingine utasikia waasi wamekivamia kijiji Fulani na kukichoma moto.

Na hali hiyo hiyo utaona itaendelea kwa muda mrefu sana, japo hiyo nchi ni kweli imefanikiwa kuwatokomeza waasi wote, lakini ile roho ya uasi bado ipo ndani ya nchi, na ndio hapo utaona leo kumetulia kesho mapambano, hivyo hivyo itaendelea kwa miaka na miaka . Na ndio hapo utaona majeshi yanalazimika kuweka makao ya kudumu katika nchi husika, muda wote yanakuwa macho, yanakesha kulinda usalama wa raia,na mali zao yanazunguka huku na huko, kuangalia kama upo usalama katikati ya vijiji vyake, na kuvuruga vikundi vyote wanavyovihisi vitakuwa vinahusika na shughuli za uasi.

Kwasababu wanajua mfano wakizembea tu, au wakipunguza nguvu kidogo, wanafahamu kabisa wale waasi bado wana hasira na serikali, japo wameshindwa lakini chini kwa chini bado wanaunda mbinu za kuupindua ufalme. Hivyo vile vikosi vya kulinda amani haviwezi kustarehe japo kweli vinaimiliki nchi yote.

Na ndivyo ilivyo kwetu sisi wakristo vita bado vinaendelea. Ni kweli ushindi tuliupata pale Kalvari, Tulifanikiwa kumnyang’anya shetani mamlaka yote kwa Damu ya Yesu Kristo iliyomwagika pale msalabani, shetani hana uwezo tena wa kuzuia maombi yetu, wala kufanya kitu chochote juu ya miili yetu au katika maisha yetu. Lakini kama na sisi hatutakuwa macho, kuilinda enzi yetu tukilala, tuwe na uhakika kuwa kama vile Bwana Yesu alivyosema katika

1Petro 5:8 “mshitaki wenu Ibilisi, kama simba angurumaye, huzunguka-zunguka, akitafuta mtu ammeze”. Basi tujue kuwa yale mambo aliyokuwa anaweza kuyafanya zamani bado ataendelea kuyafanya hata sasa hivi kama hatusimama.

Tusijifariji na kusema sisi ni wakristo maombi yetu hayawezi kuzuiwa kwasababu sisi tupo katika agano lililo bora zaidi ya lile agano la kale, na huku hatuzingatii kusimama kama wanajeshi wa Kristo, hatujajifunga kweli viunoni mwetu, Neno la Mungu hatulijui,halipo ndani yetu, chepeo ya wokovu ipo mbali nasi, habari za wokovu hatutaki kusikia, hatuna Roho ndani yetu, ambaye kwa huyo anatupa uhakika kuwa sisi ni watoto wa Mungu, na kutuongoza katika kweli yote. Dirii ya haki hatujaivaa yaani, mambo maovu ya rushwa, ulaguzi, biashara haramu vimekuwa ni sehemu ya maisha yetu na bado tunajiita wakristo. Hatuna muda wa kusali wala kudumu katika maombi kama biblia inavyotuagiza kila wakati tunawaza mambo ya ulimwengu huu, , unategemea vipi tutayakwepa majaribu ya Yule mwovu?.

Bwana mwenyewe alituambia tukeshe tuombe tusije tukaingia majaribuni, sasa kama sisi hatuna desturi hizo, unategemea vipi tutamkwepa Yule mwovu maishani mwetu? Yeye Bwana Yesu mwenyewe alifunga na kusali, sisi inatupasaje? Na ndio maana wakati mwingine tunaomba tunaona kama hatujibiwa, au majibu yanachukua muda kufika ni kwasababu Yule mkuu ya anga (Pepo) ambaye alishashindwa tangu siku nyingi, sisi tunamrudisha katika nafasi yake ya kale kwa mienendo yetu, na ndio maana matokeo yanakuwa ni hafifu au wakati mwingine kuchukua muda mrefu kujibiwa.

Vita bado vinaendelea. Kazi yako wewe ni kuilinda enzi uliyopewa na YESU, kila wakati kuhakikisha je! Zile silaha zote zinazozungumziwa katika Waefeso 6, umezivaa?. Kama umezivaa basi shetani atabakia kuwa mbali na wewe, na dunia yako itakuwa chini ya milki ya Bwana Yesu na vyote utakavyomwomba utapata, kwasababu shetani hatapata mlango wa kuzua mambo yake kwenye njia zako.

Mpaka siku itakapofika ambayo sasa, UASI wote utaondolewa duniani, Yaani siku ambayo shetani, pamoja na mapepo yake, pamoja na watu wake waovu watakapoondolewa duniani sasa siku hiyo ndiyo, hakutakuwa na haja ya kulinda enzi yoyote ile na siku hiyo haipo mbali ndugu, mwisho wa kila kitu umekaribia. Hakutakuwa na kukesha huko, hakutakuwa kusoma biblia, hakutakuwa na majaribu,ni wakati wa mambo mapya, ni wakati ambao mema yote Mungu aliyokuwa ameyakusudia watu wake kabla hata ya kuwekwa msingi ya ulimwengu ndipo yatakapofunuliwa, mambo ambayo jicho halijawahi kuona wala sikio kusikia. Tusitamani kukosa.

Lakini kwasasa hatuna budi kuyathibishwa mamlaka tuliyopewa, kwa kuzingatia kukesha, kuzivaa SILAHA ZOTE tulizopewa ili tuweze kuyafurahia matunda yote ya Bwana wetu Yesu aliyotushindia siku ile pale Kalvari.

Kama hujampa Bwana maisha yako, huu ndio wakati usingoje kesho, Mwamini kwamba yeye ni Mwana wa Mungu, na alikuja kwa ajili ya kukuosha dhambi zako, na kukupa uzima wa milele. Na kisha utubu dhambi zako zote naye ni mwaminifu atakusamehe na kukupa uzima wa milele.

Bwana akubariki sana.

Print this post

WACHUNGAJI WA BWANA MAKONDENI.

Japo Wayahudi walikuwa wanamtazamia masihi wao kwa muda mrefu na kwa shauku nyingi, lakini tunasoma siku za kuzaliwa mwokozi duniani ni kikundi cha watu wachache sana ndicho kilichojua, tena kwa kufunuliwa. Wengine wote waliosalia hawakuelewa chochote, walizidi kuendelea katika mambo yao, hawakujua kuwa wakati mwingine umeshafunguliwa. Na pia ukichunguza wale waliofunuliwa kuzaliwa kwa Bwana duniani utagundua wote ni watu waliokuwa wanaenenda katika haki na kuzishika amri zote za Mungu bila lawama, mfano tunamwona Zekaria, pamoja na mke wake Elizabeti, Tunamwona Simeoni, Tunamwona Yusufu, tunamwona, Ana, wote hawa kama tukitazama habari zao ni watu waliokuwa wamemaanisha kweli kweli kuutafuta uso wa Mungu,ni watu ambao macho yao siku zote yalikuwa yanaelekea mbinguni wakiutazamia wokovu ambao Mungu aliokuwa amewaahidia kupitia Masiya wao, na ndio maaana mwisho wa siku walikuja kufunuliwa ule wakati ulipofika.

Lakini pia kama tunavyosoma yapo makundi mengine mawili, ambayo hayo yalifunuliwa lakini haikuwa kwa njia kama za hawa wa kwanza, kundi la kwanza ni wale mamajusi kutoka mashariki na kundi la pili lilikuwa ni wale wachungaji wa makondeni. Na kama ukichunguza hawa nao hawakufunuliwa wakiwa mmoja mmoja bali walifunuliwa kimakundi. Hawa hawakuwa wanaichunguza torati, wala kuijua sana dini, wengine walitoka mbali kabisa nje ya Israeli. lakini ni kwanini na wao pia Neema hii ya kipekee iliwafikia ?. Mungu alikuwa anayosababu kuwachagua na wale, Lakini Leo tutawaangalia wale wachungaji waliokuwa wakilinda makundi yao kule kondeni.

Kama tunavyosoma habari:

Luka 2:8 “Na katika nchi ile ile walikuwako wachungaji wakikaa makondeni na kulinda kundi lao kwa zamu usiku.

9 Malaika wa Bwana akawatokea ghafula, utukufu wa Bwana ukawang’aria pande zote, wakaingiwa na hofu kuu.

10 Malaika akawaambia, Msiogope; kwa kuwa mimi ninawaletea habari njema ya furaha kuu itakayokuwa kwa watu wote;

11 maana leo katika mji wa Daudi amezaliwa, kwa ajili yenu, Mwokozi, ndiye Kristo Bwana.

12 Na hii ndiyo ishara kwenu; mtamkuta mtoto mchanga amevikwa nguo za kitoto, amelala katika hori ya kulia ng’ombe.

13 Mara walikuwapo pamoja na huyo malaika, wingi wa jeshi la mbinguni, wakimsifu Mungu, na kusema,

14 Atukuzwe Mungu juu mbinguni, Na duniani iwe amani kwa watu aliowaridhia.

15 Ikawa, malaika hao walipoondoka kwenda zao mbinguni, wale wachungaji waliambiana, Haya, na twendeni mpaka Bethlehemu, tukalione hilo lililofanyika, alilotujulisha Bwana.

16 Wakaenda kwa haraka wakamkuta Mariamu na Yusufu, na yule mtoto mchanga amelala horini.

17 Walipomwona wakatoa habari waliyoambiwa juu ya huyo mtoto.

18 Wote waliosikia wakastaajabu kwa hayo waliyoambiwa na wachungaji.

19 Lakini Mariamu akayaweka maneno hayo yote, akiyafikiri moyoni mwake.

20 Wale wachungaji wakarudi, huku wanamtukuza Mungu na kumsifu kwa mambo yote waliyosikia na kuyaona, kama walivyoambiwa.”

Tukianzia juu kidogo tunafahamu baada ya Yesu kuzaliwa biblia inatuambia Mariamu na Yusufu walikosa sehemu ya kukaa kwani vyumba vya wageni vilikuwa vimejaa hivyo wakalazimika usiku ule ule kutafuta mahali pa kumlazia mtoto, wakaona kuliko kulala kando kando ya njia ni heri wajitulize chini ya zizi la kulizishia ng’ombe huko kwa muda. Mungu aliruhusu iwe hivyo kwa makusudi ili kutimiza kusudi Fulani. Kwani huyo mtoto atakuja kufananishwa na mwanakondoo, Hivyo mwanakondoo hawezi kuishi katikati ya majumba ya kifalme bali ni sharti katika mazizi ya mifugo.

Na ndio hapo tunakuja kuona muda huo huo wale malaika wakawaendea wale wachungaji waliokuwa wamekaa kule makondeni kuwapasha habari za kuzaliwa kwa mwokozi. Swali linakuja Ni kwanini basi wawe wale wachungaji na si watu wengine kama wakulima, au watoza ushuru, au wahasibu, au matabibu, au maaskari?. Embu jaribu kufikiria lingekuwa ni kundi la watoza ushuru ndio waliopelekewa taarifa zile, kwanza usiku ule wangekuwa wapo kitandani wamelala katika majumba yao ya kifahari, pili hawajui mambo ya zizini yalivyo, pengine wangefika tu pale wangetapika kwa harufu za vinyesi na mikojo ya ile mifugo, na pengine wangekutana na ile mbolea iliyoganda pale chini kwa vinyesi vya mifugo wasingeweza kukanyagisha miguu yao waingie ndani ya zizi lile, ule ungekuwa ni mtihani mkubwa sana.

Pia Jaribu kufikiria kama Herode angepelekewa yeye taarifa za kuzaliwa kwa mfalme, unadhani angeweza kuingia ndani ya zizi lile lililochakaa la kale?. Ni wazi kuwa asingeweza, utunzaji wa mifugo ni jambo ambalo linahitaji moyo wa kujitolea na wa kipekee sana na wa uvumilivu. Ukiwa mfugaji huna budi kuweka mbali kinyaa, na kukubali kuchafuliwa na mazingira ya mifugo yaliyopo.

Na ndio maana utaona hata wale wachungaji waliokuwa na mifugo, wakati mwingine walikuwa tayari hata kwenda kulala huko makondeni, kwenye hatari nyingi, wakikaa siku nyingi, usiku na mchana kulihudumia kundi, lisije likafa kwa kukosa malisho. Ni kazi ambayo inahitaji moyo sana.

Hivyo siku ile ya kuzaliwa jicho la Bwana lilipozunguza Israeli yote na kutazama ni watu gani watakaoweza kustahimili kukutana na mwokozi katika mazingira yale magumu ya zizini, ndipo walipoonekana wale wachungaji waliokuwa wamekaa makondeni.

Wakati ule Yusufu na Mariamu wakiwa katika hali ya upweke wakiwaza ni nani atakayekuja kuwatazama mahali hapa pachafu, ni nani atakayekuja kusaidia kuweka mazingira safi na kuwafariji mahali pale pasipostahili kukaa mtu. Ndipo ghafla wakaona kundi kubwa la wachungaji linaingia katika zizi lile kwa furaha na kwa shangwe. Haleluya! mahali pale paligeuka kuwa kama Ikulu. Pengine hata watu waliokuwa wanaishi kando kando ya zizi lile walishangaa umati huo wa wachungaji wametoka wapi usiku ule, wakishangilia kwa furaha kuu na vigelegele, Na kwa jinsi walivyokuja kulakiwa kwa shangwe hata Mariamu na Yusufu hawakujali tena kama wapo katika zizi la kulishia ng’ombe, mahali pale palichangamka ghafla, Kwasababu wenyeji wao wamewasili, haraka moja kwa moja wakaanza kuzoa mavi ya kondoo na ng’ombe yaliyokuwa yapo karibu na wao,kwani hilo ni jambo la kawaida kwao, mambo ambayo mhasibu yeyote asingeweza kufanya, mambo ambayo mtoza ushuru yeyote asingeweza kufanya, askari yeyote asingeweza kufanya. 

Basi haraka haraka wakawaandalia wakawasaidia kufanya yale mambo ambayo hawakauweza kuyafanya peke yao, pengine uchafu ambao hawakuweza kuutoa,walisaidiwa na wale wachungaji na zizi lile likageuka kuwa mahali pa kukaa mtu. Na ndipo wakatoa habari zake, na kurudi makwao kwa furaha kuu na kwa shangwe. Ilikuwa ni furaha iliyokuja kwa kujua kuwa miongoni mwa wale wachache sana kati ya mamilioni ya waliokuwa Israeli, wao na walipata neema ile.

Lakini Mambo hayo kwa sasa yanafunua nini?, kama ilivyokuwa kuja kwa Bwana mara ya kwanza, ndivyo itakavyowa kuja kwa Bwana mara ya pili kulichukua kanisa lake. Kama kipindi kile Wayahudi wengi walikuwa wanamtazamia masihi wao siku moja aje kuwakomboa, ndivyo ilivyo kwa kanisa la sasa, Watu wote wanaojiita wakristo wanamtazamia Kristo kuja kulichukua kanisa lake.

Na kuja kwa sasa hivi sio kwa kuishi tena duniani kama alivyokuja mara ya kwanza, hapana bali ni kwa lengo la KUNYAKUA. Na yeye mwenyewe alituambia atakuja kwa siri kama mwivi ajavyo usiku, mfano tu wa jinsi alivyokuja kwa mara ya kwanza halikuwa ni jambo lililotangazwa mabarabarani kwa kila mtu aliyepita, bali walifunuliwa watu wachache sana, wale tu ambao muda wao wote walikuwa wanaenenda katika haki yote, na kuutazamiwa wokovu huo, mfano wa Ana na Simoni. Vivyo hivyo na leo hii watakaofunuliwa siku ile ni wale tu watu ambao macho yao na mawazo yao yote yanaelekea mbinguni, usiku na mchana wanatamani Bwana aje alichukue kanisa lake waende zao kwa Baba. Watu wa dizaini hiyo siku ile ikifika haitawajia kama mwivi bali watajua kwani ni Mungu mwenyewe atawafunulia.Watavuna walichokuwa wamekipanda kwa muda mrefu.

Lakini pia lipo kundi lingine, ambalo leo tutaliangalia, linalofananishwa na wale wachungaji waliokuwa kule makondeni. Kama tunavyofahamu Bwana akija hatakuja kwa ajili ya ulimwengu mzima, bali atakuja kwa ajili ya Kanisa lake. Hivyo siku ile atapita katika kanisa lake kwa siri kuwachukua walio wake na kuondoka. Na ndio maana tunaona hata Bwana kuja kwake kwa kwanza kulianzia katika HORI LA KULIA NG’OMBE, KATIKA ZIZI LA MIFUGO, mahali ambapo kondoo wapo, mahali ambapo kondoo wake wanalishiwa, wanapotengewa chakula ndipo alipokuja. Na kama tunavyojua kondoo wa Kristo wapo katika kanisa lake. Na ndiko huko huko Bwana atakapotulia. Hatakuja katikati ya taasisi Fulani ya serikali au chama Fulani cha kisiasa au jumuia Fulani ya kikabila, au katikati ya taifa fulani. Hapana bali katika kanisa lake teule,walipo kondoo wake.

Na hivyo kama vile UTUKUFU wa Bwana ulivyowaangazia kwanza wale wachungaji waliokuwa makondeni, vivyo hivyo Utukufu wa kurudi kwa pili kwa Bwana utawaangazia kwanza wachungaji wake wote waaminifu walio duniani wanaojitaabisha kwa ajili ya kulilisha kondoo, Usiku na mchana wanaokaa huko makondeni, wanaozunguka huku na kule, wanaotafuta hiki na kile kwa ajili ya kulilisha kundi lake, Na hivyo siku wasiyodhani utukufu wa Mungu utawaangazia wote kwa pamoja, wao ndio watakuwa wa kwanza kufahamu ujio wa Kristo, hata kama watakuwa hawana maarifa ya kutosha juu ya mafunuo ya Mungu, lakini siku hiyo ikifika fahamu tu ndio watakaokuwa wa kwanza kuuona utukufu wa Mungu. Hatabakia mchungaji yeyote aliye mwaminifu ambaye hata uona utukufu huo, hata awe mbali kiasi gani, atauona tu.

Wengi wanaona kulichunga kundi la Mungu, ni kazi ya kujichosha, isiyo na malipo kujitaabisha kwa ajili ya watoto wa Mungu, wanaona kama hakuna faida yoyote, wanaona ni kheri wakafanye shughuli zao nyingine, kuliko kuhangaika na vinyesi vya mifugo, ni kazi isiyopewa heshima yoyote. Lakini kumbuka kuwa Kristo hatakuja kwa waasibu, wala kwa wafanyabiashara, wala kwa wanasiasa, wala kwa madaktari, bali kwa kanisa lake, na hivyo ni sharti awaone kwanza wale walichungao kundi hilo kisha wafuate wengine. Atawatafuta kwanza wale watoa posho wake, aliowaweka katika kanisa lake, wawape watu wake posho kwa wakati.

Hivyo nataka kukutia moyo wewe ambaye utatoa muda wako kulitazaa kundi la Mungu, usikate tamaa, kwasababu ipo siku UTUKUFU MKUU wa Bwana utakuangazia na siku hizo si mbali. Zidi kulihurumia kundi la Bwana kwa jinsi Mungu anavyokupa neema, ikiwa ni usiku ikiwa ni mchana, endelea kuitenda kazi, fundisha, onya , karipia, Na wakati wa Bwana ukifika utakuwa wa kwanza kulipokea lile fungu la utukufu wake.

Ubarikiwe sana.

Tafadhali “share” ujumbe huu kwa wengine, Na Bwana atakubariki.


Mada Zinazoendana:

SIRI YA MUNGU.

UPUMBAVU WA MUNGU.

KWANINI YESU ALIMUITA BABA YAKE “ABA”?


Rudi Nyumbani

Print this post

UHARIBIFU WA MTU.

Mathayo 15.1 “Ndipo Mafarisayo na waandishi toka Yerusalemu walipomwendea Yesu wakisema,

2 Mbona wanafunzi wako huyahalifu MAPOKEO YA WAZEE, kwa maana hawanawi mikono walapo chakula.

3 Akajibu, akawaambia, Mbona ninyi nanyi huihalifu amri ya Mungu kwa ajili ya MAPOKEO YENU?

4 Kwa kuwa Mungu alisema, Mheshimu baba yako na mama yako, na Amtukanaye baba yake au mama yake kufa na afe.

5 Bali ninyi husema, Atakayemwambia babaye au mamaye, Cho chote kikupasacho kusaidiwa na mimi ni wakfu,

6 basi asimheshimu baba yake au mama yake. Mkalitangua neno la Mungu KWA AJILI YA MAPOKEO YENU.

7 Enyi wanafiki, ni vema alivyotabiri Isaya kwa habari zenu, akisema,

8 Watu hawa huniheshimu kwa midomo; Ila mioyo yao iko mbali nami.

9 Nao waniabudu bure, WAKIFUNDISHA MAFUNDISHO YALIYO MAAGIZOYA WANADAMU.

10 Akawaita makutano akawaambia

11 Sikilizeni, mfahamu; Sicho kiingiacho kinywani kimtiacho mtu unajisi; bali kitokacho kinywani ndicho kimtiacho mtu unajisi.

12 Ndipo wanafunzi wake walipomwendea, wakamwambia, Wajua ya kuwa Mafarisayo walipolisikia neno lile walichukizwa?

13 Akajibu, akasema, Kila pando asilolipanda Baba yangu wa mbinguni litang’olewa.

14 Waacheni; hao ni viongozi vipofu wa vipofu. Na kipofu akimwongoza kipofu mwenzake, watatumbukia shimoni wote wawili.

15 Basi Petro akajibu, akamwambia, Tueleze mfano huo.

16 Yesu akasema, Hata sasa ninyi nanyi mngali hamna akili?

17 Hamjafahamu bado ya kuwa kila kiingiacho kinywani hupita tumboni, kikatupwa chooni?

18 Bali vitokavyo kinywani vyatoka moyoni;

navyo ndivyo vimtiavyo mtu unajisi.

19 Kwa maana moyoni hutoka mawazo mabaya, uuaji, uzinzi, uasherati; wivi, ushuhuda wa

uongo, na matukano.

20 HAYO NDIYO YAMTIAYO MTU UNAJISI; LAKINI KULA KABLA HAJANAWA MIKONO HAKUMTII MTU UNAJISI”

Habari hiyo ni baada ya Mafarisayo kuwashutumu wanafunzi wa Bwana Yesu, Ni kwanini hawanawi mikono kabla ya kula chakula.

Sasa katika Torati hakuna mahali popote Bwana Mungu aliwaagiza wana wa Israeli wanawe mikono kabla ya kula chakula, hakuna mahali popote kwenye biblia (katika Agano la Kale) Mungu alitoa maagizo ya namna hiyo..Yalikuwa ni mapokeo yalitengenezwa na wazee wa kiyahudi, kwamba ni lazima watu wanawe kabla ya kula,ni mambo waliyojitungia wao wenyewe tu!, na si kutoka kwa Mungu…Na ndio maana utaona hapo mafarisayo wanawalaumu wanafunzi wa Yesu “kwanini wanayahalifu wapokeo ya wazee”..na sio mapokeo ya Mungu.

Kwa ufupi utaratibu wa kunawa mikono kabla ya kula “yalikuwa ni mafundisho ya wanadamu” na si mafundisho ya Mungu. Sasa kwa kawaida tendo lolote au pokeo lolote la kimwili sio baya, lakini linapochukua nafasi ya mapokeo ya ki-Mungu ndipo linapokuwa ni Baya na lenye madhara makubwa sana.

Kwa mfano pokeo hilo la desturi ya kunawa mikono kabla ya kula chakula sio baya, ni lizuri na linafaa sana,hata kwetu tunalo, kwanza kwa ajili ya usafi na kwaajili ya ustaarabu. Lakini shida inakuja ni pale linapotumika kama ndio sababu ya Mungu kumbarikia mtu au kumlaani mtu. Na kutafsiriwa isivyopasa kwamba ndio kitu cha Muhimu sana Mungu anachokiangalia kwa mtu, na kwamba akikihalifu hicho basi ni dhambi kubwa sana kwa huyo mtu, Jambo ambalo Mungu hajaliagiza mahali popote pale kwa watu wake.Ndio maana Bwana Yesu alizidi kuwaambia maneno yale.

“8 Watu hawa huniheshimu kwa midomo; Ila mioyo yao iko mbali nami.

9 Nao waniabudu bure, WAKIFUNDISHA MAFUNDISHO YALIYO MAAGIZOYA WANADAMU”.

Sasa tukirudi kwenye kiini cha Somo a kinachosema ni kitu gani kimtiacho Mtu unajisi??

Sasa ni vizuri tukafahamu maana ya neno “unajisi” kama lilivyotumika hapa lina maana gani…Kumbuka unajisi uliotumika kwa wanyama “najisi” sio sawa na lilivyotumika hapa “kwamba vimtokavyo mtu moyoni ndivyo vimtiavyo mtu unajisi”…unajisi uliotumika kwa wanyama una maanisha “wanyama wasio safi” kwa kiingereza “unclean animals”..kwahiyo unajisi hapo kwa wanyama umetumika kama “kitu kisicho-kisafi”

Lakini katika mstari huu wa Mathayo 15:19 Bwana aliozungumzia kitu kimtiacho Mtu unajisi..hakumaanisha kuwa ni “kitu kimfanyacho mtu kutokuwa safi” hapana bali unajisi kama ulivyotumika pale ni “kitu kinacho mharibu mtu”..kwa lugha ya kiingereza ni “Thing that defiles a man”..Kwahiyo neno unajisi hapo limetumika kama “Uharibifu”…na sio “kitu kisichosafi”

Kwahiyo hiyo sentensi kwa ufasaha zaidi tunaweza kuutafsiri hivi..

17 Hamjafahamu bado ya kuwa kila kiingiacho kinywani hupita tumboni, kikatupwa chooni?

18 Bali vitokavyo kinywani vyatoka moyoni;navyo ndivyo VIMHARIBUVYO MTU.

19 Kwa maana moyoni hutoka mawazo mabaya, uuaji, uzinzi, uasherati; wivi, ushuhuda wa uongo, na matukano.

20 hayo ndiyo YANAYOMHARIBU MTU; lakini kula kabla hajanawa mikono Hakumharibu mtu”

Kwa sentensi hiyo basi tunaweza tukaona ni mambo gani yanayomuharibu Mtu…Ni mambo gani yanayoweza kuiharibu nafsi ya mtu, ni mambo gani yanayoweza kumletea mtu dhiki, na mateso, na mauti, wakati mwingine hata magonjwa…Hayo sio mengine zaidi ya matendo yote ya giza, kama uasherati, utukanaji, wizi, uuaji, mawazo mabaya n.k

Vyakula au kwa ufupi riziki za ulimwengu huu, haziwezi kutufanya tupatikane au tusipatikane na madhara, vyakula havina ulinzi wowote katika maisha yetu..Mali hazina ulinzi wowote katika maisha yetu, Bali vitokavyo mioyoni mwetu ndivyo vyenye ulinzi..Kadhalika vile vitokavyo mioyoni mwetu ndivyo vyenye kuleta kuharibu pia.

Tunajijenga kwa vile vyema vitokavyo mioyoni mwetu, na tunajiharibu kwa vile vibaya vitokavyo mioyoni mwetu… Huoni mawazo mabaya ndiyo yanayompeleka mtu kuua, kuiba, kuafanya uasherati, kutukana, kupandikiza chuki na masengenyo haya yote ndiyo yanayomletea mtu uharibifu wake mwenyewe..

Ndugu yangu ni vizuri kushika mapokeo tuliyopokea kwa waalimu wetu wa dini, au wazazi wetu kwamba tuzingatie mlo kamili, tujitunze kwa kila namna, tuchemshe maji ya kunywa, tufanye check-up kila mara ili tuepukane na magonjwa hatarishi, na tuwe watanashati..hayo ni mazuri sana na yanatufaa lakini pamoja na hayo ongezea kufahamu kitu hichi kimoja tena… “kikuingiacho mwilini mwako hakikuharibu wewe, bali kikutokacho moyoni mwako ndicho kikuharibucho”..Moyo wako msafi ndio utakaokupa afya mifupani mwako na maisha marefu ya kuishi sio aina ya vyakula unavyobadilisha, wala checkup unazozifanya kila wiki.

Mithali 4: 20 “Mwanangu, sikiliza maneno yangu; Tega sikio lako, uzisikie kauli zangu.

21 Zisiondoke machoni pako; UZIHIFADHI NDANI YA MOYO WAKO.

22 MAANA NI UHAI KWA WALE WAZIPATAO, NA AFYA YA MWILI WAO WOTE.

23 LINDA MOYO WAKO KULIKO YOTE UYALINDAYO; Maana ndiko zitokako chemchemi za uzima.

24 Kinywa cha ukaidi ukitenge nawe, Na midomo ya upotovu uiweke mbali nawe.

25 Macho yako yatazame mbele, Na kope zako zitazame mbele yako sawasawa.

26 Ulisawazishe pito la mguu wako, Na njia zako zote zithibitike;

27 Usigeuke kwa kuume wala kwa kushoto; Ondoa mguu wako maovuni”

Neno la Mungu linatuambia tulinde mioyo yetu kuliko vyote tuwezavyo kulinda maana ndiko zitokazo chemchemi za Uzima.

Ni matumaini yangu kuwa Bwana amekujalia kuona na kujua kile alichotaka ukione siku ya Leo. Na kutafuta Ulinzi wa Moyo wako.

Kama hujampa Bwana Yesu maisha yako, hujachelewa ni kheri ufanye hivyo sasa hivi, maana nyakati tunazoishi ni nyakati za hatari, miaka imesogea sana na Kristo yupo mlangoni kurudi..Anza mwaka huu kwa kuanza kuishi maisha mapya katika Kristo, tubu kwa kumaanisha kuziacha dhambi zako, na kisha katafute mahali wanapobatiza ubatizo sahihi wa maji tele na kwa Jina la Yesu Kristo, ukabatizwe kwa ajili ya ondoleo la dhambi zako kulingana na Matendo 2:38, Na Bwana Yesu Mwenyewe atakupa kipawa cha Roho wake Mtakatifu atakayeweza kukusaidia kushinda dhambi na kukuongoza katika kuijua kweli yote ya Biblia..Na kwa kufanya hivyo utakuwa umeokoka! Na kuwa na tumaini la Uzima wa Milele, na kwenda mbinguni na Bwana atakapokuja kulichukua kanisa lake.

Print this post

FAHAMU ZA WATU HUWA ZINAONDOLEWA NA NINI?

Kama ukichunguza watu wote walioathiriwa na ulevi wa kupindukia huwa wanaonyesha tabia zinazofanana, moja ya tabia hizo ni kutokujali jambo lolote linaloweza kuja mbele yake, mtu akishalewa hata hajali tena thamani ya utu wake, anaweza akavua nguo mbele za watu, utakuta kabla hajanywa alikuwa ni mtu mwenye heshima lakini akishalewa tu, matusi yaanza kumtiririka mdomoni mwake, anakuwa sio mtu wa kujali, sio mtu wa kujizuia, sio mtu wa kuchukua tahadhari kwa kitu chochote kile kitakachokuja mbele yake, anaweza akasimama katikati ya barabara kuu sehemu ambayo magari yanapita na kuanza kujiongelea mwenyewe bila kujali kuwa anaweza kugongwa na gari akafa. Na ndio maana hata ajali nyingi zitokeazo zinasababishwa na madereva kuwa walevi..Ni kwasababu gani? Ni kwasababu FAHAMU ZAO zinakuwa zimeshawatoka kwa wakati huo na kama ufahamu umeshawatoka basi hata ule uwezo wa kufikiri, wa kujitawala na wa kuchukua tahadhari unakuwa umeondoka ndani yao.

Lakini mtu huyo huyo uje umwangalie baadaye zile pombe zimeshaisha kichwani mwake, na hapo ufahamu wake umeshamrudia atajishangaa ni kwanini amelala mtaroni, ni kwanini alikuwa anawavunjia watu wengine heshima, na ni kwanini alikuwa hathamini uhai wake kusimama katikati ya barabara n.k..

Na ndio maana Biblia inasema Hosea 4: 11 “UZINZI NA DIVAI na divai mpya huondoa fahamu za wanadamu”.

Unaona? kwa namna hiyo hiyo pombe inavyoweza kuondoa ufahamu wa watu ndivyo hivyo hivyo hata UZINZI unavyoondoa FAHAMU za watu biblia inatuambia hivyo. Maneno hayo alithibitishiwa Nabii Hosea pale alipopewa maagizo na Mungu akaoe mke kahaba, na azae naye watoto, mwanzoni alidhani pengine atakuwa kahaba tu halafu basi wala hakutakuwa na madhara mengine yoyote ya ndani, lakini kwa jinsi alivyokuwa anakaa nae na kuona mwenendo wake jinsi ulivyokuwa wa hatari sana, jinsi huyo mwanamke asivyokuwa mtu wa kujali mambo ya Mungu, jinsi huyo mwanamke alivyokuwa anapoteza mapenzi na Mungu wake siku baada ya siku, jinsi huyo mwanamke anavyozidi kuwa mbali sana na wanawake wengine kwa kila kitu, jinsi roho yake ilivyozidi kupotea pasipo hata yeye mwenyewe kujitambua kutokana na ukahaba wake, ndipo alipopata ufahamu huo kutoka kwa Mungu na kusema maneno haya.

“Uzinzi na divai na divai mpya huondoa fahamu za wanadamu.”. Ni kwanini leo hii mtu hajali juu ya hatma ya maisha yake ya milele baada ya kufa hata kama aambiwe moto wa Jehanum ni mkali mara elfu ya huu, bado hajali, Sababu sio kwamba yeye ni sugu hasikii, hapana sababu ni roho iliyo ndani yake ya UZINZI imeshamwondolea ufahamu wa kujali maisha yake bila hata yeye mwenyewe kujijua, na ndio hapo hata akielezwe habari za hukumu inayokuja utaona anaanza kufanyia mzaha, au anapuuzia, au anakufuru Ni kwasababu ule UFAHAMU aliopewa na Mungu wa kupambanua na kufikiri, na kuchukua tahadhari ulishamtoka siku nyingi.

Utakuta mtu kuongea matusi ni kitu cha kawaida kwake hasikii hata kuhukumiwa ndani ya moyo wake, unadhani alianza hivyo? Hapana zamani alikuwa anaogopa kutukana lakini kwasababu muda wote amekuwa akiishibisha nafsi yake kwa uasherati, na uzinzi na zinaa, na maneno ya uchafu, na huku biblia ilishakataza hata uasherati usitamkwe vinywani mwetu, basi bila kujua yeye anaendelea kufanya hivyo hajui kuwa kidogo kidogo anaupoteza ufahamu wake, ndipo hapo anajikuta kutukana ni sehemu ya maisha yake.

Kwa nje! Anaweza akajiona ni mwenye akili na mjanja, anaonyesha kuwa yeye naye ni kijana, lakini nyuma ya pazia hajui kuwa FAHAMU zinamtoka kidogo kidogo, na roho ya kutokujali inamvaa mpaka inafikia wakati hata aelezejwe habari za Mungu hawezi tena kugeuka, ndio inakuwa basi tena, anaishia kupinga Neno la Mungu na kuutukana msalaba. Zinaa ni mbaya kama ulivyo ulevi. Tuikimbie zinaa ndugu!!

Na ndio maana sehemu nyingine biblia inasema

Mithali 6: 32 “Mtu aziniye na mwanamke HANA AKILI KABISA; Afanya jambo litakalomwangamiza nafsi yake”.

Unaona, uasherati, uzinzi, ni mambo ambayo yanapoteza nafsi za watu kwa spidi kubwa kushinda hata mambo mengine yote. Na ndio maana shetani anapenda sana kuitumia hiyo kuwanasa watu, Anajua kabisa miili ya wanadamu ni mahekalu ya Roho Mtakatifu hivyo anafanya juu chini ayaharibu makao hayo ya Mungu ili Mungu akose mahali pa kutua, Na kama tunavyofahamu hata hii Dunia mfano kama Roho wa Mungu asingetua na kuanza kuipendezesha tena, basi ingeendelea kubakia katika hali ile ile ya utupu na ukiwa na giza milele, Sasa kama na sisi hatutaihifadhi miili yetu, na kumjengea Roho wa Mtakatifu mazingira ya kutua na kututengeneza unadhani tutapataje kupona au kuokoka?. Ni wazi kuwa tutaendelea kuwa katika giza mpaka siku ya hukumu na kuishia kutupwa katika ziwa la moto.

Ndugu/kaka kaa mbali na zinaa. Kaa mbali na vichochezi vyote vya zinaa, kaa mbali na mustarbation hivyo vyote vinaondoa ufahamu wako ndugu, unaweza ukajiona upo sawa lakini hujui ni jinsi gani nafsi yako inavyoharibika kwa spidi kubwa sana, kaa mbali na pornography na utazamaji wa picha za uchi mitandaoni, hivyo vinaondoa ufahamu wako kama vile pombe inavyoondoa ufahamu wa mtu. Weka mbali muvi na vitabu vinavyoonekana kuchochea zinaa ndani yako, hiyo ni kwa usalama wa roho yako ndugu kwa kizazi hichi Bwana anachokiona ni kizazi cha zinaa. Kaa mbali na watu au marafiki ambao muda wote mazungumzo yao ni habari za uasherati tu, disco na anasa..Hao watakupeleka kuzimu.

Usiruhusu roho ya kutokujali ikuingie, usikubali kupoteza ufahamu wako Mungu aliokupa, kwa Uzinzi. Mungu alikusudia wewe uwe mtakatifu kama yeye alivyo, hayo ndio mapenzi yake kwako 

1Petro 1: 15 “bali kama yeye aliyewaita alivyo mtakatifu, ninyi nanyi iweni watakatifu katika mwenendo wenu wote;

16 kwa maana imeandikwa, Mtakuwa watakatifu kwa kuwa mimi ni mtakatifu”.

Lakini ni kwanini ulikuwa ukisikia maneno hayo ya Mungu unapuuzia, na huku mwingine akiusikia anaogopa na kutetemeka, unadhani tatizo ni wewe? Hapana tatizo lipo kwenye ufahamu wako ambao umeshaliwa kwa roho za uasherati na uzinzi uliokuwa ndani yako. Lakini unayo sasa nafasi ya kugeuka, na kuacha mambo hayo ili Bwana ayatengeneze upya maisha yako. Embu tufuatilie pamoja maonyo haya mafupi Sulemani aliyotupa yahusianayo na mambo haya haya ya zinaa naamini yataongeza kitu katika mienendo yetu sote. Tusome:

MITHALI: MLANGO 7

1 Mwanangu, yashike maneno yangu, Na kuziweka amri zangu akiba kwako.

2 Uzishike amri zangu ukaishi, Na sheria yangu kama mboni ya jicho lako.

3 Zifunge katika vidole vyako; Ziandike juu ya kibao cha moyo wako.

4 Mwambie hekima, Wewe ndiwe umbu langu; MWITE UFAHAMU JAMAA YAKO MWANAMKE.

5 WAPATE KUKULINDA NA MALAYA, Na mgeni akubembelezaye kwa maneno yake.

6 Maana katika dirisha la nyumba yangu Nalichungulia katika shubaka yake;

7 Nikaona katikati ya WAJINGA, Nikamtambua miongoni mwa vijana, Kijana mmoja asiyekuwa na akili,

8 Akipita njiani karibu na pembe yake, Akiishika njia iendayo nyumbani kwake,

9 Wakati wa magharibi, wakati wa jioni, Usiku wa manane, gizani.

10 Na tazama, mwanamke akamkuta, Ana mavazi ya kikahaba, mwerevu wa moyo;

11 Ana kelele, na ukaidi; Miguu yake haikai nyumbani mwake.

12 Mara yu katika njia kuu, mara viwanjani, Naye huotea kwenye pembe za kila njia.

13 Basi akamshika, akambusu, Akamwambia kwa uso usio na haya,

14 Kwangu ziko sadaka za amani; Leo hivi nimeziondoa nadhiri zangu;

15 Ndiyo maana nikatoka nikulaki, Nikutafute uso wako kwa bidii, nami nimekuona.

16 Nimetandika kitanda changu, magodoro mazuri, Kwa matandiko ya Kimisri yenye mistari.

17 Nimetia kitanda changu manukato, Manemane na udi na mdalasini.

18 Haya, na tushibe upendo hata asubuhi, Tujifurahishe nafsi zetu kwa mahaba.

19 Maana mume wangu hayumo nyumbani, Amekwenda safari ya mbali;

20 Amechukua mfuko wa fedha mkononi; Atarudi wakati wa mwezi mpevu.

21 Kwa maneno yake mengi na ulaini akamshawishi, Kwa ubembelezi wa midomo yake akamshinda.

22 Huyo akafuatana naye mara hiyo, Kama vile ng’ombe aendavyo machinjoni; Au mpumbavu kuadhibiwa katika pingu;

23 Hata mshale umchome maini; Kama ndege aendaye haraka mtegoni; Wala hajui ya kuwa ni hasara ya nafsi yake.

24 Basi, wanangu, nisikilizeni sasa, Mkayaangalie maneno ya kinywa changu.

25 MOYO WAKO USIZIELEKEE NJIA ZAKE, WALA USIPOTEE KATIKA MAPITO YAKE.

26 Maana amewaangusha wengi waliojeruhi, NAAM, JUMLA YA WALIOUAWA NAYE NI JESHI KUBWA.

27 Nyumba yake ni njia ya kwenda kuzimu, Hushuka mpaka vyumba vya mauti”.

UZINZI NA DIVAI na divai mpya huondoa fahamu za wanadamu      

Unaona? Zinaa ni kama vile mtu apelekwaje machinjoni, wala hajui kuwa ni kwa hasara ya nafsi yake mwenyewe,Na biblia inatuambia walionaswa katika mtego huu si watu wawili au watatu, bali ni jeshi kubwa sana.. Hivyo mimi na wewe tusiwe miongoni mwa hilo jeshi kubwa, tuikimbie zinaa kama biblia inavyotuambia, tumpe Roho Mtakatifu nafasi ya kuyatengeneza upya maisha yetu. Ni dhambi mbaya ambayo mtume Paulo aliitaja inafanyika juu ya mwili wa mtu.

Ikiwa bado hujampa Bwana maisha yako bado hujachelewa muda ndio huu, unachopaswa kufanya ni kutubu mwenyewe kutoka ndani ya moyo wako, kukusudia kwa kumaanisha kabisa kuwa hutaki kurudia njia hizo mbovu za mauti, hutaki kuwa tena mlevi, hutaki kufanya zinaa tena, hutaki kufanya mustarbation(punyeto) tena, hutaki kutazama pornography tena, hutaki kuvaa “mavazi ya kikahaba” kama huyo mwanamke anayezungumziwa na Sulemani na mavazi ya kikahaba yanayozungumziwa kwa sasa ni vimini, suruali kwa wanawake, migongo wazi na vitop, na sketi zinazobana ambavyo ni vichocheo vikubwa vya uasherati n.k. hutaki tena kutazama picha za utupu na pornography na mengine yote. Ikiwa kweli umeonyesha nia hiyo mbele za Mungu ya kutaka kuacha basi Mungu naye kuanzia huo wakati atakupa NGUVU ya kuweza kuvishinda hivyo vyote.

Na mwisho wa siku utashangaa ni rahisi kuacha, hata mimi nilikuwa mzinzi, mlevi, mtazamaji wa pornography na kila kitu kiovu lakini siku ile Neema ya Bwana iliponifikia, nilipotubu kwa kumaanisha kuacha , Uwezo huo wa ajabu ulikuja ndani yangu, mpaka sasa dhambi ya zinaa si kitu kwangu. Na vivyo hivyo na wewe ukiamua kugeuka, Bwana atakupa Uwezo huo, Hivyo fanya maamuzi sasa angali nafasi unayo. Na mara baada ya kutubu kwako jambo linalofuata ni kubatizwa, kwa ajili ya ondoleo la dhambi zako,hivyo tafuta mahali popote wanapobatiza ubatizo sahihi wa kimaandiko, nao ni ule wa kuzamwishwa katika maji mengi na uwe kwa Jina la YESU KRISTO. Kama hujafahamu bado mahali pa kubatiziwa na unahitaji msaada wa kwa jambo hilo,unaweza kuwasiliana nami nitakuelekeza mahali karibu na wewe unaweza kupata hudumu hiyo ya kiroho.

Mwisho kabisa nikutakie mwanzo mema wa Mwaka huu, uwe wa mafanikio kwako ya kiroho na ya kimwili, na ya kukaa mbali na zinaa kwa jina la Bwana wetu YESU KRISTO.

Amen.

Print this post

SIKUKUU YA VIBANDA.

Moja ya sikuku saba ambazo Mungu aliwaagiza Wana wa Israeli wazishike ni SIKUKUU YA VIBANDA..Nyingne sita ni 1) Sikuku ya Pasaka,

2) Sikukuu ya Mikate isiyotiwa chachu,

3) Sikukuu ya Malimbuko ya Mavuno,

4) Sikukuu ya Majuma au Pentekoste

5) Sikukuu za kupiga Baragumu

6) Sikukuu ya siku ya Upatanisho na

7) Sikukuu ya Vibanda ndiyo ya Mwisho na ya saba.

Kila sikukuu ilikuwa na umuhimu wake na maana yake kubwa kimaandiko, Kwahiyo wana wa Israeli waliambiwa wazishike sikukuu hizi kwa faida zao wenyewe.Kumbuka sikukuu hizi hazikuwa kwa ajili ya kunywa na kula kama zinavyofanyika leo..Sikukuu hizi zilikuwa ni kwaajili ya kufanya sala na ibada tu! Na kukumbuka Mambo makuu ambayo Mungu aliwatendea walipotoka Misri na walipokuwa jangwani..na Mungu alionya siku hizo zifanywe kuwa takatifu daima.

Leo tutaitazama hii sikukuu ya mwisho inayojulikana kama sikukuu ya Vibanda na umuhimu wake kwa Wana wa Israeli na umuhimu wake kwetu sisi watu wa agano jipya.

Zamani wakati Mungu anawatoa Wana wa Israeli katika nchi ya utumwa Misri, aliwapitisha njia ya JANGWA ndefu ili kuwafundisha huko, kumbuka sio kwamba hapakuwa na njia ya mkato wa kufika nchi ya Ahadi, hapana ilikuwepo tena nzuri tu lakini Bwana aliamua kuwapitisha njia ya jangwa, iliyo ngumu, ili kuwanyeyekeza mioyo yao na kuwafundisha wamtegemee yeye kwa kila kitu, wamfahamu yeye kuwa sio Mungu tu wa mahali penye kijani bali pia ni Mungu wa jangwani, na kwamba mtu hataishi tu kwa vilimo, na katika milima mizuri yenye chemchemi, au katika fukwe nzuri zenye maji baridi, au katika nchi laini yenye udongo mzuri bali anaweza akaishi pia katika jangwa lisilokuwa na chakula, wala msimu wa mvua, wala maji wala upepo mwanana na bado akawa na afya nzuri, akawa na raha, na asichakae, asiugue endapo tu atatembea na Mungu..hilo ndilo somo Bwana alilokuwa anataka watoto wake wafahamu wakiwa kule jangwani.

Kumbukumbu 8: 1 “Amri hii ninayokuamuru leo mtaishika kuitenda, mpate kuishi na kuongezeka, na kuingia katika nchi ile ambayo Bwana aliwaapia baba zenu; nanyi mtaimiliki.

2 Nawe utaikumbuka njia ile yote Bwana, Mungu wako aliyokuongoza miaka hii arobaini katika jangwa, ili

akutweze, kukujaribu kuyajua yaliyo moyoni mwako, kwamba utashika amri zake, au sivyo.

3 Akakutweza, akakuacha uone njaa, akakulisha kwa mana, usiyoijua wewe wala baba zako hawakuijua;

APATE KUKUJULISHA YA KUWA MWANADAMU HAISHI KWA MKATE TU, BALI HUISHI KWA KILA LITOKALO KATIKA KINYWA CHA BWANA.

4 Mavazi yako hayakuchakaa, wala mguu wako haukuvimba, miaka hiyo arobaini.

5 Nawe fikiri moyoni mwakoya kuwa kama vile baba amrudivyo mwanawe, ndivyo Bwana, Mungu wako akurudivyo.

6 Nawe uzishike amri za Bwana, Mungu wako, upate kwenda katika njia zake, na kumcha”.

Sasa kule jangwani kama tunavyojua Jangwani hakuna misitu, wala makazi wala wafanya biashara wala chochote kile..walikuwa ni wao kama wao tu! hakukuwa na nyumba za kukaa hivyo suluhisho pekee la kutatua changamoto hiyo ilikuwa ni kwenda kutengeneza vibanda vidogo vidogo vitakavyowahifadhi wakiwa kule jangwani..vibanda hivyo walivitengeneza kiasi cha kwamba havikuwa vya kudumu..bali vya muda mfupi tu, kwasababu wao walikuwa ni watu wa kusafiri, leo wapo hapa kesho wapo kule..kwahiyo waliishi ndani ya hivyo vibanda kwa miaka 40, Na walipofika nchi ya Ahadi Bwana aliwaahidia hawatakaa tena katika vibanda kama walivyokuwa jangwani, wala hawatakula tena chakula cha aina moja (mana)..bali watakula vyakula vingi vya aina nyingi tofauti tofauti kwasababu hiyo nchi itawazalia yenyewe pindi watakapofika na pia watakaa kwenye majumba makubwa ambayo hata hawajayajenga wao, kadhalika mataifa yote yatawaogopa nao watakuwa watu wakufanikiwa sana.

Lakini kwasababu Bwana anaijua mioyo yao mbeleni, alijua watakapokula na kushiba watamsahau yeye, wataacha kuyashika maagizo yake, na kumsahau Mungu ambaye aliwapigania katika hali ngumu za jangwani, na kumsahau Mungu wao kuwa ndiye Mungu pekee aliyewasaidia wakati wa matatizo..Hivyo Bwana Mungu kwa kulifahamu hilo, aliwaagiza watakapoingia hiyo nchi ya ahadi kila mwaka wafanye sikukuu ya siku saba kuadhimisha jinsi Mungu alivyotembea nao jangwani.

Aliwaagiza kila mwisho wa Mwaka wa saba wa kalenda ya kiyahudi, watu wote watoke katika nyumba zao za kifahari wanazokaa…waende milimani wakachukua fito na matawi ya miti kila mtu akajenge kibanda kidogo pembezoni mwa nyumba yake kama vile walivyotengeneza walipokuwa kule jangwani..kila mtu au familia akalale ndani ya hicho kibanda ndani ya siku saba..wakumbuke Uweza wa Mungu na matendo yake aliyowatendea jangwani miaka 40, kwamba walikaa ndani ya vibanda na walikuwa wanalishwa na kunyweshwa ndani ya lile jangwa nene kimiujiza, na wala walikuwa hawaugui wala mavazi yao kuchakaa.

Kwahiyo sheria hiyo Mungu aliiagiza ifanyike kwa vizazi vyote..Kwamba kila mwaka mwezi wa saba ni lazima ishikwe..kumbuka haikuwa sherehe ya kula na kunywa, wala watu walikuwa hawaendi kwenye kumbi za starehe kusheherekea..ilikuwa ni sherehe ya kumwimbia Mungu,kumsifu na kukaa katika vyumba vya ndani katika uwepo wake na kutafakari kwa muda mrefu matendo yake makuu. Ulikuwa ni wakati wa kuisoma torati yote upya na kujikumbusha mambo yaliyoandikwa kule, na pia ulikuwa ni wakati wa kuwafundisha watoto wale waliozaliwa hivi karibuni sheria za Bwana na torati. Hiyo ndiyo tafsiri ya sikukuu mbele za Mungu. Tunasoma:

Kumbukumbu 31: 10 “Musa, akawaamuru, akasema, Mwisho wa kila mwaka wa saba, wakati wa maachilio, WAKATI ULIOAMRIWA WA SIKUKUU YA VIBANDA,

11 Israeli wote wafikapo ili kuonekana mbele za Bwana, Mungu wako, mahali pale atakapopachagua, uisome torati hii mbele ya Israeli wote masikioni mwao.

12 Wakusanye watu, wanaume na wanawake na watoto, na mgeni wako aliyemo malangoni mwako wapate kusikia na kujifunza, na kumcha Bwana, Mungu wenu, na kuangalia kutenda maneno yote ya torati hii;

13 na watoto wao wasiojua, wapate kusikia na kujifunza kumcha Bwana, Mungu wenu, siku zote mtakazokaa katika nchi mnayoivukia Yordani ili kuimiliki”.

Nehemia 8: 14 “Wakaona ya kuwa imeandikwa katika torati, jinsi Bwana alivyoamuru kwa mkono wa Musa, ya kwamba wana wa Israeli WAKAE KATIKA VIBANDA, katika sikukuu ya mwezi wa saba;

15 na ya kwamba wahubiri na kutangaza katika miji yao yote, na katika Yerusalemu, kusema, Enendeni mlimani, mkalete matawi ya mzeituni, na matawi ya mzeituni-mwitu, na matawi ya mihadasi, na matawi ya mitende, na matawi ya miti minene, ili kufanya vibanda, kama ilivyoandikwa.

16 Basi watu wote wakatoka, wakayaleta, wakajifanyizia vibanda, kila mtu juu ya dari ya nyumba yake, na katika nyua zao, na katika nyua za nyumba ya Mungu, na katika uwanja wa lango la maji, na katika uwanja wa lango la Efraimu.

17 Na mkutano wote wa watu, waliorudi kutoka nchi ya uhamisho wao, wakafanyiza vibanda, wakakaa katika vibanda hivyo; maana tokea siku za Yoshua, mwana wa Nuni, hata siku ile, wana wa Israeli hawakufanya hivyo. Pakawa na furaha kubwa sana.

18 Tena siku baada ya siku, tangu siku ya kwanza hata siku ya mwisho, akasoma katika kitabu cha torati ya Mungu. Wakafanya sikukuu muda wa siku saba; na siku ya nane palikuwa na kusanyiko la makini, kama ilivyoagizwa”.

Sasa mambo haya ni kivuli cha mambo yaliyopo sasahivi, kwasababu agano la kale ni kivuli cha agano jipya, mambo yaliyokuwa yanafanyika agano la kale kwa namna ya mwilini yanafanyika leo katika agano jipya kwa namna ya roho. Kama Bwana alivyowatoa wana wa Israeli kutoka nchi ya utumwa Misri, na sisi pia Bwana ametutoa katika nchi ya utumwa wa dhambi, na kama vile wana wa Israeli walivyobatizwa wote katika Bahari ya Shamu (1 Wakoritho 10:2) na kuwa huru na majeshi ya kimisri kikabisa kabisa na sisi pia kupitia ubatizo wa maji mengi kwa jina la Yesu tunawekwa huru mbali na dhambi kikabisa kabisa.

Na kama wana wa Israeli walivyofundishwa katika jangwa zito, na sisi pia Bwana ametupitisha katika majaribu mbali mbali kuijaribu imani yetu, na kama tutakuwa waaminifu Basi Bwana atatuingiza katika kaanani yake ya rohoni ambayo ni mbingu mpya na nchi mpya..Lakini kabla hajatuingiza katika hiyo Kaanani ya milele mahali pasipo kuwa na tabu wala shida..atatuingiza pia katika Kaanani ya miili yetu hii. Atatupa mara mia katika ulimwengu huu kama alivyoahidi katika Neno lake.

Na atakapokuingiza katika hiyo nchi, Ni wajibu wako kumfanyia Mungu sikukuu ndani ya moyo wako..Tenga siku, au wiki, au mwezi..funga yatafakari mambo yote makuu Mungu aliyokutendea wakati upo katika madarasa ya Mungu, Kipindi hauna chochote lakini Bwana anakupigania..kipindi unaumwa na huna msaada lakini Bwana anakuponya..kipindi ambacho ungestahili kufa kwenye lile jangwa la mateso lakini hukufa, kipindi ambacho ulipitia kila aina ya jaribu lakini Bwana hakukuacha..Zikumbuke hizo siku usizisahau, ibada ya kumbukumbu ya hizo siku ndiyo SIKUKUU INAYOMPENDEZA MUNGU.

Inayofananishwa na SIKU KUU YA VIBANDA, Unapozitafakari hizo siku, inakusaidia kutozisahau fadhili za Mungu alizokutendea nyuma, na hivyo siku zote unajikuta unaishi katika mstari wa Mungu…Kama wana wa Israeli ilikuwa ni amri kuishika sikukuu ya Bwana na sisi pia ni amri kukumbuka fadhili za Mungu na kuzitafakari siku zote za maisha yetu.

Kumbuka mema yote Mungu aliyokufanyia nyuma kwa kumfanyia ibada ya shukrani naye Mungu atakuangazia rehema zake daima.

Bwana akubariki sana, tafadhali “share” ujumbe huu kwa wengine.

   Jiunge na magroup yetu ya whatsapp kwa kubofya hapa > Group-whatsapp


Mada Zinazoendana:

SIKUKUU 7 ZA KIYAHUDI ZINAFUNUA NINI KWETU?

SIKU KUU YA PURIMU

PENTEKOSTE NI NINI?


Rudi Nyumbani

Print this post

USIISHIE KUTAZAMA JUU, ENDELEA MBELE.

Udhihirisho wa Bwana Yesu kabla ya kufufuka, ulikuwa ni tofauti na baada ya kufufuka..Kabla ya kusulibiwa Bwana Yesu alikuwa anaonekana kila mahali na sehemu nyingi, hata watu waliotaka kumwona na kumfahamu, walikuwa wakimtafuta kwa bidii wanampata mahali popote..Alifanya huduma yake kwa wazi sana..Lakini haikuwa hivyo tena baada ya kufufuka kwake. Baada ya kufufuka kutoka katika wafu, hakuwa anajidhihirisha kwa kila mtu, isipokuwa kwa watu wachache sana, tena,sana sana wale wanafunzi wake…Wengine wote waliosalia ambao walikuwa hawafuatani naye wala hawajishughulishi na mambo yake, walibakia kuamini uongo kwamba Bwana hajafufuka ameibiwa na wanafunzi wake usiku, na kuzusha kwamba amefufuka.

Kwahiyo waliokuwa wana uhakika kwamba Bwana Yesu kafufuka kweli kweli ni wale wanafunzi wake tu, na ndugu zake Bwana pamoja na kikundi cha watu wachache sana waliokuwa wanafuatana naye, mamilioni ya watu waliokuwa pale Yerusalemu hawakujua chochote..Na siku ya unyakuo itakuwa hivyo hivyo watakaomwona Kristo mawinguni watakuwa wachache sana kati ya mabilioni ya watu wanaoishi duniani.

Wakati hata ule mti ambao ulimsulibishia Bwana haujaoza, Tayari Bwana alikuwa anazungumza na wanafunzi wake katika vyumba vya ndani vya siri. Wakati ambao bado watu walikuwa wanamwombolezea tayari yeye ameshawatokea wengi na kuzungumza nao.

Wakati Pilato, Herode,mafarisayo, masadukayo pamoja na wayahudi wamestarehe wakisheherekea na kudhani Bwana sasa ni marehemu, kumbe maili kadhaa tu hapo,si mbali na wao Bwana anawaaga wanafunzi wake na kuchukuliwa juu mbinguni..

Matendo 1: 4 “Hata alipokuwa amekutana nao aliwaagiza wasitoke Yerusalemu, bali waingoje ahadi ya Baba, ambayo mlisikia habari zake kwangu;

5 ya kwamba Yohana alibatiza kwa maji, bali ninyi mtabatizwa katika Roho Mtakatifu baada ya siku hizi chache.

6 Basi walipokutanika, wakamwuliza, wakisema, Je! Bwana, wakati huu ndipo unapowarudishia Israeli ufalme?

7 Akawaambia, Si kazi yenu kujua nyakati wala majira, Baba aliyoyaweka katika mamlaka yake mwenyewe.

8 Lakini mtapokea nguvu, akiisha kuwajilia juu yenu Roho Mtakatifu; nanyi mtakuwa mashahidi wangu katika Yerusalemu, na katika Uyahudi wote, na Samaria, na hata mwisho wa nchi.

9 Akiisha kusema hayo, walipokuwa wakitazama, akainuliwa, wingu likampokea kutoka machoni pao.

10 Walipokuwa wakikaza macho mbinguni, yeye alipokuwa akienda zake, tazama, watu wawili wakasimama karibu nao, wenye nguo nyeupe,

11 wakasema, Enyi watu wa Galilaya, mbona mmesimama mkitazama mbinguni? Huyu Yesu aliyechukuliwa kutoka kwenu kwenda juu mbinguni, atakuja jinsi iyo hiyo mlivyomwona akienda zake mbinguni.

12 Kisha wakarudi kwenda Yerusalemu kutoka mlima ulioitwa wa Mizeituni, ulio karibu na Yerusalemu, wapata mwendo wa sabato”.

Kwahiyo tunaweza tukaona kujidhihirisha kwa Bwana baada ya kufufuka kulikuwa ni kwa siri sana, sio wote waliokuwa wanajua kinachoendelea wakati ule.

Lakini jambo la kipekee tunaloweza kujifunza ni kwamba, Wakati Bwana anachukuliwa juu katika wingu..wale wanafunzi walikuwa wanamtazama kwa macho yao jinsi alivyokuwa anaondoka hatua kwa hatua..jinsi wingu lilivyomchukua mpaka kupotelea mawinguni…Lakini tunaona baada ya kudumu kwa muda mrefu wakiangalia mawinguni malaika wawili waliwatokea katikati yao na kuwahamisha akili zao wasibaki kuangalia mbinguni, kwa maana Kwa jinsi hiyo hiyo aliyoondokea ndio atakayorudia..hivyo waache kuangalia juu, wakaendelee na mambo mengine yanayohusiana na kuutangaza ufalme wa mbinguni..Mpaka wakati wa Bwana kurudi, wakawe mashahidi wa Yesu Kristo, wakiutangaza ufalme wa mbinguni kwa watu wengine.

Kwa wakati huo ulikuwa ndio ule wakati Bwana Yesu aliowaambia mafarisayo kwamba utafika wakati Bwana arusi ataondolewa na ndipo wanafunzi wake watafunga na kuomboleza.

Mathayo 9: 14 “Wakati ule wanafunzi wake Yohana wakamwendea, wakasema, Kwa nini sisi na Mafarisayo twafunga, bali wanafunzi wako hawafungi?

15 Yesu akawaambia, Walioalikwa arusini wawezaje kuomboleza, muda bwana arusi akiwapo pamoja nao? Lakini siku zitakuja watakapoondolewa bwana arusi; ndipo watakapofunga”.

Siku zote upo wakati ambao Bwana atatembea na Mtu, kama mtu na rafiki yake au mpenzi wake, na upo wakati ambao Bwana atatembea na mtu kama mtu na mtumwa wake..wakati huo Bwana ataondoka juu, na kukutuma kama mfanya kazi katika shamba lake.

Utakuwa ni wakati wa Bwana kugeuza hisia zako, na kukusukuma kwenda kuzaa matunda zaidi badala ya kukaa mwenyewe mwenyewe tu!..

Nakumbuka kipindi cha kwanza kwanza nampa Bwana maisha yangu, nilikuwa sitamani kitu kingine chochote zaidi ya kuondoka kwenye hii dunia na kwenda kwa Baba..Nilikuwa natamani leo Kristo arudi niondoke..(sio kwamba hata sasa bado sikitamani,nakitamani hicho kitu sana) na nilikuwa namwona Bwana akinifariji kwa namna ya kipekee kwa njia hiyo, nilikuwa naona maono, na ishara baadhi kuthibitisha njia hiyo..Lakini ilifika wakati mambo yalibadilika ndani…

Nilianza kuhisi kuna majukumu Fulani nayakwepa, Nilianza kusikia msukumo mwingine tofauti na ule wa kwanza, badala ya kukaa peke yangu na kujifunza tu Neno, na kusikiliza tu mahubiri na kusoma vitabu..huku nikitamani siku yoyote parapanda ilie niondoke…Nilianza kuhisi kuna umuhimu wa kwenda kusambaza habari za Yesu Kristo kwa watu wengine..Jambo hilo lilikuja ndani kwa nguvu sana kwa muda mrefu kidogo..mpaka ikafika wakati siku ikipita pasipo kufanya chochote katika kuisambaza kazi ya Mungu, nakosa amani, hata nguvu za mwili naona zinapungua kabisa..Kwahiyo nikahama kutoka kutazama tu mbinguni na kuanza kazi nyingine ya kuhubiri, ndio angalau unafuu ndani ya nafsi ukarudi.

Kwahiyo ikawa nikiona tu ndani amani imetoweka najua sehemu ya kwenda kuirudisha.. “ni kwenda kuwahubiria wengine habari njema”..amani inarudi kama kawaida na siku yangu inaenda vizuri, tofauti na hapo kwanza ambapo hata nisipofanya hivyo..nikisoma tu Neno na kusikiliza mahubiri na kusali basi Napata amani.

Nimetoa ushuhuda huu mfupi tu wa mimi binafsi kuonyesha kwamba kuna nyakati na majira, kuna wakati wa kukaa na Bwana arusi (Yesu Kristo) na kuna wakati wa Bwana arusi kuondolewa.. Waliooa au walioolewa wanafahamu kuwa kuna wakati wa mume na mke kukaa pamoja kwa raha na furaha, wakiwa wawili tu..na kuna wakati wa majukumu, wakati ambao watoto wamezaliwa wanahitajika kutunzwa, wakati huo upendo lazima ugawanyike kidogo, sehemu Fulani lazima uelekee katika kuwatunza watoto. Upendo unahamia kwa watoto.

Na katika Ukristo nako ni hivyo hivyo, upo wakati wa kufurahi na Bwana, kipindi cha mwanzo cha wokovu lakini pia upo wakati wa kwenda kuzaa matunda, kipindi ambacho Bwana arusi ataondolewa..wakati ambao unalazimika kujihusisha na watoto wa kiroho zaidi, kuliko kitu kingine zaidi…Kama ilivyokuwa kwa wanafunzi, walikaa na Bwana miaka mitatu na nusu kwa raha…na siku Bwana anaondoka walidhani wataendelea kutembea naye na kula naye kama hapo kwanza..walimwuliza Bwana huu ndio wakati wa kurejeshewa ufalme (Yaani wakati wa kutawala na Bwana wao kwa raha na furaha pasipo usumbufu)..Lakini Bwana aliwaambia huo ni wakati wa kupokea nguvu kuwa mashuhuda wake, na kupeleka injili duniani kote na kuleta mazao mengi katika ufalme wa mbinguni…huo sio wakati wa kustarehe tena, ni wakati wa kufunga,na kuombeleza, ni wakati wa kupambana vita.

Kwa kupitia ujumbe huu mfupi, naamini utakuwa umeongeza kitu katika vile Bwana alivyokujalia kuvijua, ni maombi yangu kuwa Bwana atakusaidia Katika hilo, utapofikia katika hiyo hatua au kama upo katika hiyo hatua Bwana akufanikishe sana na azidi kukutia nguvu katika kuifanya kazi yake.

Kama hujampa Bwana maisha yako, nakushauri ufanye hivyo leo, kabla mlango wa Neema haujafungwa, kwa Kristo atakuja na wala hatudanganyi..Yeye anatupenda ndio maana amejitoa maisha yake kwa ajili yako na yangu.Hivyo mgeukie leo ukatubu dhambi zako zote kwa kumaanisha kuziacha, na yeye atakupokea kama alivyoahidi, na pia haraka tafuta mahali ukabatizwe ikiwa haukubatizwa ipasavyo, ili upate ondoleo la dhambi zako, na utakuwa na uhakika wa Uzima wa milele na kuiona Mbingu.

Print this post

MAMBO AMBAYO MALAIKA WANATAMANI KUYACHUNGULIA.

Siku hiyo itakuwa ni siku ya namna gani?, Siku hiyo ya watakatifu wote kunyakuliwa, siku hiyo ambayo itakuwa ni mwisho wa taabu zote kwa wana wa Mungu..Siku ambayo tutakutana na YESU uso kwa uso, siku ambayo Bwana atakapokwenda kuweka wazi mambo yake yote aliyokuwa ametuandalia tangu zamani , makao yetu ya milele, Biblia inasema ni mambo ambayo hata malaika watakatifu wanatamani kuyachulingulia wayaone yakoje..

Ni kama tu vile na sisi tulivyo na shauku ya kuona walau kwa uchache jinsi mbingu ilivyo, kwani tumekuwa tukiisikia uzuri wake usio wa kawaida tangu zamani jinsi ulivyo lakini tusiuone, Na kwa namna hiyo hiyo malaika nao sasa huko juu mbinguni, wanatamani kwa shauku kubwa walau waonjeshwe mambo walioandaliwa wateule wa Mungu na YESU KRISTO mwenyewe siku ile itakavyokuwa. Huko walipo Malaika watakatifu wanasikia tu! kuwa kuna utukufu mkubwa Bwana amewaandalia watakatifu wake, wanafahamu kuwa ni utukufu ulio mkuu sana usioneneka. lakini bado hawajauona ni wa namna gani, wanajua kuwa siku ya ukombozi wa watoto wa Mungu ni siku KUU sana, mambo yasiyoneneka wala kutamkika yatafunuliwa katika siku hizo, hivyo hiyo inawafanya wao nao waitamani siku hiyo ije kwa haraka wao nao wayashuhudie mambo hayo ya ajabu.

1Wakorintho 2:9 “Lakini, kama ilivyoandikwa, Mambo ambayo jicho halikuyaona wala sikio halikuyasikia, (Wala hayakuingia katika moyo wa mwanadamu,) Mambo ambayo Mungu aliwaandalia wampendao”.

Na Sio malaika tu peke yao, hata viumbe vingine vyote vinaitamani hiyo siku ifike, Mtume Paulo anasema ..

Warumi 8:18 “Kwa maana nayahesabu mateso ya wakati huu wa sasa kuwa si kitu kama UTUKUFU ULE UTAKAOFUNULIWA KWETU.

19 Kwa maana viumbe vyote pia vinatazamia KWA SHAUKU NYINGI kufunuliwa kwa wana wa Mungu.

20 Kwa maana viumbe vyote pia vilitiishwa chini ya ubatili; si kwa hiari yake, ila kwa sababu yake yeye atiyevitiisha katika tumaini;

21 kwa kuwa viumbe vyenyewe navyo vitawekwa huru na kutolewa katika utumwa wa uharibifu, hata viingie katika uhuru wa utukufu wa watoto wa Mungu”.

Kwasasa hatuwezi kusema mengi kwasababu bado hatujafunuliwa mambo yenyewe lakini tunafahamu sifa moja ya Mungu KUWA YEYE HUWA HASEMI UONGO, na kama alivyosema “ kama vile mbingu zilivyo juu sana kuliko nchi, kadhalika njia zangu zi juu sana kuliko njia zenu, na mawazo yangu kuliko mawazo yenu”..Alimaanisha kuwa tunaweza kuchukulia hivyo vitu kwa upeo wetu wa kibinadamu kiwepesi wepesi lakini siku tutakapokuja kuyaona hayo mambo ndipo tutakapojua kweli mawazo yake yalikuwa mbali sana na sisi tulivyokuwa kufikiri.

Siku hiyo sisi tutakapoondoka hapa duniani, haitakuwa heri kwetu tu sisi na viumbe vyote, bali itakuwa heri pia kwa Malaika wote walioko mbinguni. Kutakuwa na shangwe na furaha isiyoneneka.

Hivyo ndugu tukikaa na kuyatafakari hayo kwa utulivu, basi hatutajali ni mambo mangapi yatapita mbele yetu mabaya, sisi siku zote tutaelekeza macho yetu mbinguni, hatutajali ulimwengu unasemaje, sisi tutamtazama mwokozi wetu YESU KRISTO daima, huku tukingojea kwa saburi yale Mungu aliyoutandalia, tutaishi kama wapitaji na wasafiri tu hapa duniani.

1Petro 1:9-16

“9 KATIKA KUUPOKEA MWISHO WA IMANI YENU, YAANI, WOKOVU WA ROHO ZENU.

10 Katika habari ya wokovu huo manabii walitafuta-tafuta na kuchunguza-chunguza, ambao walitabiri habari za neema itakayowafikia ninyi.

11 Wakatafuta ni wakati upi, na wakati wa namna gani ulioonywa na Roho wa Kristo aliyekuwa ndani yao, ambaye alitangulia kuyashuhudia mateso yatakayompata Kristo, NA UTUKUFU UTAKAOKUWAKO BAADA YA HAYO.

12 Wakafunuliwa ya kuwa si kwa ajili yao wenyewe, bali kwa ajili yenu walihudumu katika mambo hayo, ambayo sasa yamehubiriwa kwenu na wale waliowahubiri ninyi Injili kwa Roho Mtakatifu aliyetumwa kutoka mbinguni. MAMBO HAYO MALAIKA WANATAMANI KUYACHUNGULIA.

13 Kwa hiyo vifungeni viuno vya nia zenu, na kuwa na kiasi; mkiitumainia kwa utimilifu ile neema mtakayoletewa katika ufunuo wake Yesu Kristo.

14 Kama watoto wa kutii msijifananishe na tamaa zenu za kwanza za ujinga wenu;

15 bali kama yeye aliyewaita alivyo mtakatifu, ninyi nanyi iweni watakatifu katika mwenendo wenu wote;

16 kwa maana imeandikwa, Mtakuwa watakatifu kwa kuwa mimi ni mtakatifu.”

Tukaze mwendo, ikiwa maisha yako sasa yapo mbali na Kristo, huu ni wakati wa kumrudia yeye maadamu mlango wa neema bado upo wazi, kumbuka siku ile ukijikuta umeachwa majuto hayatakuwa kwasababu unakwenda Jehanum, hapana majuto makubwa yatakujia kwasababu umekosa mambo mazuri ya umilele Mungu aliokuwa amewaandalia watoto wake tangu zamani.

Hivyo tubu kabisa kwa kudhamiria kuanza maisha mapya katika Bwana, na haraka bila kukawia nenda ukabatizwe katika ubatizo sahihi wa kuzamishwa kwenye maji tele, na kwa Jina la YESU KRISTO..Ili upate ondoleo la dhambi zao kulingana na Matendo 2:38., kisha Bwana mwenyewe atakupa kipawa cha Roho wake Mtakatifu kama alivyoahidi, na kuanzia hapo nawe utakuwa umeingizwa na kuwa mmojawapo wa waliostahili kuuona huo utukufu ambao utakuja kufunuliwa siku za hivi karibuni. Tunaishi katika siku za mwisho Zidi kudumu katika utakatifu, na ushirika na kusali daima.

Bwana akubariki.

Print this post